Uongo kwani?
Hali ya uchumi ya watu wetu ni mbaya sana
Hali hiyo inawiana na takwimu zote za kinchi zinazoonyesha kuwa maisha ya WATU wetu yamekuwa mabaya zaidi ndani ya miaka hii miwili ya Serikali ya awamu ya 5, mifano michache ifuatayo inaonyesha hali hiyo:
1. UFUKARA: Kwa mujibu wa utafiti wa Afrobarometer wa REPOA, 76% ya Watanzania wana ufukara wa kipato kwa sasa, kulinganisha na 64% ya mwaka 2014. Hivyo basi, ndani ya miaka hii miwili ya utawala huu, mafukara wameongezeka kwa 12%. Hivyo kwa sasa zaidi ya robo 3 ya Watanzania ni mafukara zaidi. Hawa hawana uwezo kabisa wa kulipia huduma za afya, kununua mbegu bora, kunua mbolea, kula mlo bora nk.
2. NJAA: Kwa mujibu wa utafiti huo wa REPOA, 27% ya Watanzania wanalala na njaa sasa kulinganisha na chini ya robo ya Watanzania wanaolala na njaa mwaka 2014.
3. UDUMAVU: Tatizo hilo la njaa linaonekana zaidi kwa kuongeza kwa hali ya udumavu nchini. Mwaka 2011 42% ya watoto wa Tanzania walikuwa wamedumaa, Idadi hiyo ya waliodumaa ilishuka mpaka 34.4% mwaka 2015, kwa sasa imepanda na kufikia 34.7 %. Katika kila watoto 10 nchini walio chini ya miaka mitano, basi watoto wanne (4) wamedumaa kwa sababu ya Lishe duni. Watoto wenye udumavu huu hawanufaiki kabisa na elimu bure inayotolewa.
4. VIFO VYA UZAZI: Kwa mujibu wa ripoti ya Tume ya Takwimu ya Taifa, NBS iliyotoka wiki 2 zilizopita, Vifo vitokanavyo na UZAZI vimepanda kutoka 438/ 100,000 (kwa vizazi salama) hadi 556/100,000. Likiwa ni ongezeko la vifo 118 zaidi. Hali hii inatisha.
5. AJIRA: Utafiti wa REPOA umeonyesha hali ya ajira ni mbaya sana, 31% tu ya Watanzania ndio wanaona Serikali inazalisha ajira kwa sasa, tofauti na 43% walioona hivyo mwaka 2014. Na hili ni kielelezo cha biashara nyingi zilizofungwa tangu utawala wa awamu ya 5 uingie madarakani, kiasi zaidi ya 69% ya Watanzania wanaona Serikali haina uwezo wa kuzalisha ajira na wamekatishwa tamaa. Wengi wa hawa ni vijana, waliomaliza vyuo mbalimbali bila kuajiriwa, tunazalisha bomu litakalotulipukia.
6. MAJI: Kwa mujibu wa Utafiti wa REPOA, Watanzania wanaona upatikanaji wa Maji ni tatizo zaidi sasa kuliko zamani, 42% wanaona maji ni tatizo kubwa ukilinganisha 34% ya mwaka 2014. Ukosefu huu wa maji safi na salama unachagiza maradhi, unapunguza muda wa uzalishaji wa Wananchi, na unavunja ndoa.
7. UFUKARA WA MAJI VIJIJINI: Wastani wa Pato la Taifa la Mtanzania ni shilingi milioni 2.1. Mwananchi wa Kata ya Gehandu, Manyara ananunua maji pipa moja la lita 200 kwa 7000/-, familia yenye watu 6 inahitaji angalau pipa moja kwa siku kwa matumizi ya kujibana kabisa ya maji. Kwa hiyo, familia hii itahitaji takribani shilingi 2.5 milioni kwa mwaka kwa ajili ya Maji tu, hivyo basi, wastani wa 16% ya kipato cha kila mwanafamilia (hata mtoto mdogo wa siku 1) hutumika kununua Maji. Miji mingi nchini kwetu hupata maji kutoka mamlaka za Maji safi na salama. Wastani wa bei ya maji kwa pipa la lita 200 kwa mamlaka za maji nchini ni shilingi 300 tu. Mwananchi wa Uzunguni jijini Arusha au Mikocheni jijini Dar es Salaam au Shanty Town Manispaa ya Moshi au Capri Point jijini Mwanza hutumia wastani wa shilingi 108,000 kwa mwaka kama gharama za Maji kwa familia yake. Familia ya watu 6 ya mjini inatumia chini ya 1% ya wastani wa kipato cha familia kununua maji.
8. VIWANDA NA SEKTA BINAFSI: Ripoti za BoT zinaonyesha Uzalishaji wa bidhaa za Viwandani umeshuka kwa zaidi ya nusu, hata mauzo ya bidhaa za viwandani yameshuka, kutoka trilioni 1.5 mpaka bilioni 700. Mbaya zaidi, tangu mwaka huu uanze viwanda kadhaa vimefunga/kusitisha uzalishaji kutokana na kukosekana kwa sukari ya viwandani pamoja na kutolipwa kwa Ritani zao la Kodi zitokanazo na hiyo Sukari ya Viwandani (pamoja na Ritani za VAT). Viwanda vikubwa viwili vya Saruji vikiwa navyo vimesitisha uzalishaji, na kufanya gharama za bidhaa hiyo kupaa zaidi. Hivyo kuua ndoto nzima ya uchumi wa Viwanda.
9. BEI - NAFAKA: Bei ya mazao ya Wakulima imeshuka mno. Mwaka 2017, Mkulima wa Kata ya Tomondo, Mikese, Morogoro alipata mifuko 10 ya Saruji (cement) kwa kuuza gunia 1 tu la Mahindi (Gunia ilikuwa ni shilingi 120,000 na Mfuko mmoja wa Saruji wa kilo 50 ulikuwa ni shilingi 12,000). Kwa sasa Mkulima huyo anapata mifuko ya Saruji 3.5 akiuza Gunia lake 1 la Mahindi (Gunia sasa ni shilingi 50,000 na Saruji sasa ni shilingi 14,000). Mwaka 2017 Mkulima wa Maharagwe wa Kata ya Msambara, Kasulu, Kigoma aliuza kilo 7.5 za maharagwe na kupata fedha za kununua mfuko mmoja wa Saruji (kilo ya Maharagwe ilikuwa shilingi 2000 na Mfuko wa Saruji ulikuwa shilingi 15,000). Kwa sasa, Mkulima huyo atapaswa kuuza kilo 14.6 za Maharagwe ili kupata mfuko 1 wa Saruji (Maharagwe 1kg ni shilingi 1300 na Saruji ni shilingi 19,000).
10. BEI - MIFUGO: Mwaka 2017 Mfugaji wa Kata ya Sumbugu, Misungwi, Mwanza, aliuza Ng’ombe 1 ili kununua mifuko 27 ya Saruji (Ng’omne mmoja ilikuwa ni shilingi 400,000/- na mfuko mmoja wa Saruji ulikuwa ni shilingi 15,000/-). Kwa sasa, Mfugaji huyo anapata mifuko 9 tu kwa kuuza ng’ombe mmoja (Ng’ombe mmoja ni shilingi 150,000/- na mfuko mmoja wa Saruji ni shilingi 17,000/-).
11. BEI - MAZAO YA BIASHARA: Utafiti wa Mwezi Januari, 2018 uliofanywa na taasisi za Tanzania Pulses Network na East Africa Grain Council unaonyesha kuwa hasara iliyopatikana kutokana na mbaazi zilizokosa soko hapa nchini ni zaidi ya shilingi Bilioni 100. Hasara hii ni kubwa mno kwa wakulima wa mikoa ya Kusini na Pwani. Hasara hii pia iko kwa wakulima wa Giligilani na Pareto katika mkoa wa Manyara ambao bei ya mazao yao imeshuka kwa zaidi ya nusu. Hasara hiyo pia ipo kwa Wakulima wa Tumbaku wa Tabora ambao tumbaku yao imekosa soko kabisa na kudumbukizwa kwenye ufukara.
12. MBOLEA IMEPANDA BEI: Pamoja na matatizo yote hayo ya kupungua kwa tija kwenye Kilimo (kukosekana kwa soko na kushuka kwa bei kwa mazao), Serikali imeamua KUWANYONGA zaidi wakulima, kwa kupandisha bei ya mbolea. Bei elekezi mpya ya Mbolea ya Serikali imepanda kutoka kati ya 41,00/- na 54,000/- mpaka kati ya 47,000/- na 57,000/- kwa mfuko wa 50kg. Jambo hili litawaumiza zaidi wakulima wetu na kuzidisha Ufukara wao. Tangu hapo kuna unyonyaji kwenye sekta ya mbolea, mfano mbolea ambayo bei elekezi ni shilingi 41,000 - 54,000, inauzwa mtaani kwa wastani wa shilingi 60,000 - 85,0000. Sasa badala ya Serikali kuhakikisha inakesha huu unyonyaji, nayo imeamua kuwanyonga zaidi wakulima.