Katika mjadala unaoendelea kumekuwa na malumbano na mabishano kati ya wasemaji, wafuasi na wapigadebe wa ama serikali tatu au serikali mbili. Wachambuzi, kama wapo, ni wachache sana na hata hao wachache hawasemi au hawasikiki. Rai yangu kwenu ni kwamba sisi kama wanazuoni tusijidandie kundi lolote kati ya makundi hayo matatu.
Jukumu na wajibu wetu ni tofauti kabisa. Wajibu wetu ni kuchambua hali halisi bila jazba; na kutokana na uchambuzi wetu kuonesha uzuri na ubaya wa mambo. Sisi wanazuoni nafasi yetu ni kuwa kioo cha jamii, kuonesha jamii uzuri na ubaya wake na kwa vipi na kwa njia gani uzuri unaweza kuimarishwa na ubaya kupunguzwa.