Akizungumza Februari 25, 2026 jijini Dodoma katika Kikao cha Mwaka cha Majaji Wafawidhi, Jaji Mkuu Masaju amesema viongozi wa Mahakama wanapaswa kutambua wajibu wao bila kusubiri kusukumwa na maelekezo kutoka juu.
“Hatuwezi kuishi kwa maelekezo. Sisi ni binadamu tuna akili na tunatambua wajibu wetu. Sisi ni viongozi wenye dhamana kubwa katika taifa hili, tunapaswa kuwajibika ipasavyo,” amesema.
Ameonya kuwa utamaduni wa kusubiri maagizo kabla ya kutekeleza majukumu unaweza kuharibu mahusiano ya kikazi na kushusha hadhi ya taasisi hiyo muhimu.
Aidha, Jaji Mkuu huyo amesema Mahakama inapaswa kuwa mfano wa uwajibikaji kwa taasisi nyingine, akisisitiza kuwa ndiyo kimbilio la wananchi wanapotafuta haki.
“Hii tabia ya kuzungumza kwenye vikao halafu wanaotakiwa kutekeleza wanasubiri kikao kingine, hatutakuwa na utamaduni wa namna hiyo,” amesema.
Ameongeza kuwa tangu aingie madarakani amekuwa akisisitiza suala la kujituma katika utendaji kazi, akieleza kuwa si sharti lake binafsi bali ni wajibu unaotokana na Katiba.