Horace Kolimba hafanyiwagi kumbukumbu?

Nini kilichotokea kati ya Kolimba na Nyerere?

Godfrey Dilunga

Toleo la 223
25 Jan 2012













HORACE Kolimba ni miongoni mwa viongozi waandamizi nchini ambaye Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, alitofautiana naye na baadhi ya wenzake kuhusu masuala ya msingi katika uongozi na mwelekeo wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Lakini mbali na Mwalimu, Kolimba alitofautiana na chama chake (CCM), angali Katibu Mkuu, akiweka bayana chama hicho kimepoteza dira.
Kwa ujumla, hakuna ubishi kwamba Mwalimu Nyerere alikuwa akifahamu mifumo yote ya uongozi wa nchi kwa sababu ameshiriki kuibuni n kuiridhia, akiwa kiongozi mkuu.
Bila shaka, alielewa wapi apate taarifa ipi na kuhusu nani au nini. Kubwa zaidi, watoa taarifa katika vyombo nyeti nchini walijitolea kumdokeza kwa kadiri ilivyowezekana wakiamini ndiye mtu wa uhakika asiye na hila kwa nchi yake. Asiye na mikono michafu dhidi ya nchi.
Lakini pia hakuna ubishi Mwalimu huyo huyo, alifahamu tabia na mienendo ya viongozi karibu wote waandamizi nchini. Ikumbukwe, asilimia kubwa ya viongozi ‘aliwalea’ baada ya kuwaingiza katika mfumo wa uongozi.
Kwa hiyo, ni sahihi kusema Mwalimu alitambua uhodari na udhaifu wao na alijenga mazingira ya kuingilia majukumu yao kwa kadiri mambo yanavyoanza kwenda kombo katika ofisi alizowakabidhi chini ya kauli mbiu; “cheo ni dhamana.”
Na pengine tatizo lililokuwapo ni kwamba wakati mwingine; ‘ndoto’ nzuri alizokuwanazo Mwalimu kuhusu Tanzania bora isiyotegemea wahisani kujiendesha na isiyoongozwa na mchanganyiko wa viongozi wezi na waadilifu wanaovumiliana na hata kuwa genge moja dhidi ya umma, hazikusambaa vizuri kwa baadhi ya viongozi wenzake.
Na kwa hiyo basi, pengine alikuwa akihisi wenzake wanavuruga ‘ndoto’ yake bila kujua kwamba ndoto hiyo haieleweki kwao au inaeleweka lakini kwao haina ‘mashiko’. Kwamba wakati yeye akiwa ameridhia hata mshahara wake upunguzwe ili kukabili hoja za mgomo wa wanafunzi wa Chuo Kikuu Dar es Salaam (UDSM) bila kulalamika maisha yake yatakuwa magumu (Msasani sio Dodoma kama sasa), wenzake wengi walitamani mshahara mkubwa zaidi.
Na kwa mantiki hiyo kutokana na baadhi ya hatua alizokuwa akichukua kama kiongozi wa nchi na hata baada ya kustaafu, wengi wanaamini ilikuwa vigumu kwa viongozi wengi waandamizi kubishana hadharani na Mwalimu Nyerere.
Ni kama vile uadilifu wa Mwalimu ulikuwa kikwazo au silaha kwa baadhi kumshambulia hadharani, ingawa kwa nadra ilijitokeza wachache kufanya hivyo huku wengine wakiishia kulalamika pembeni (mitaani).
Kati ya ambao miongoni mwao hawakuridhiki na walitumia mbinu nyingine za kumjibu Mwalimu ni pamoja na Horace Kolimba, kama tutakavyoona katika mfululizo wa makala hizi.
Kimsingi, inawezekana viongozi wengi waandamizi waliamini kwamba mbele ya umma, nguvu za Nyerere ni kubwa zaidi hasa kwa kigezo cha uadilifu na kwa hiyo, si rahisi kumpinga katika hali ya kumdhalilisha na ukabaki salama.
Imani hii ya uadilifu wa Nyerere ndiyo bila shaka, iligeuzwa na Watanzania kuwa dhamana kwa Benjamin Mkapa asiyekuwa ‘mwenyeji’ kwao, na wakampigia kura za urais 1995.
Urais ambao baadhi ya machapisho yanabainisha kuwa Kolimba naye alikwishaonesha nia mapema zaidi, takriban miezi 10 kabla (mwishoni mwa mwaka 1994).
Lakini hata hivyo, ni dhahiri kuwa nyuma ya nguvu hizi za Mwalimu Nyerere katika jamii aliyoshiriki kusaka uhuru wake dhidi ya watawala wa kigeni, kulikuwa pia na nguvu za dola zilizokuwa na jukumu la kusukuma na kusimamia hoja zake za kitaifa.
Wengi mtakumbuka jinsi Mwalimu alivyotofautiana dhahiri na aliyekuwa Waziri Mkuu, John Malecela, achilia mbali Katibu Mkuu wa CCM (chama tawala), Horace Kolimba.
Na kwa namna ya kipekee, Mwalimu pia alitofautiana kuhusu namna Mzee Ali Hassan Mwinyi alivyokuwa akiongoza nchi katika baadhi ya masuala ya msingi, ingawa wakati mwingine alimtetea kuwa anashauriwa vibaya.
Nini hasa kilitokea?
Kutokana na tofauti hizo na hasa kwa kuangalia viongozi hao watatu, Kolimba, Malecela na Mwinyi, itakumbukwa Mwalimu aliandika kitabu; Uongozi wetu na Hatima ya Tanzania.
Sijui kwa sababu zipi hasa ambazo pengine Mzee Ali Hassan Mwinyi na Mzee John Malecela wanaweza kuzieleza kwamba hawakutaka kujibishana na Mwalimu Nyerere, tofauti na alivyofanya Horace Kolimba.
Hata hivyo, Kolimba naye hakufanya majibizano na Mwalimu moja kwa moja hadharani, anadaiwa kutumia vyombo vya habari vya Chama cha Mapinduzi (magazeti ya Uhuru na Mzalendo) akiwa Katibu Mkuu, kumjibu Nyerere.
Inaaminika katika hali inayothibitisha nia ya Kolimba kuwania urais mwaka unaofuatia (1995), mwaka 1994 mwanasiasa huyo alijipanga kwanza kujinasua na mashambulizi ya Mwalimu Nyerere kwake na hata kwa wenzake (Mwinyi na Malecela ambao walikaa kimya). Mashambulizi hayo yamo kwenye kitabu cha Nyerere; Uongozi wetu na hatima ya Tanzania.
Maswali zaidi yanajitokeza katika mkakati huo wa Kolimba kama ambavyo pia tutazidi kubaini katika mufululizo wa makala hizi.
Kwa mfano, wakati Kolimba akidaiwa kutumia vyombo vya chama kumjibu Nyerere katika ‘staili’ ya kipekee ambayo ilifichuliwa na magazeti mengine nchini, Mzee Mwinyi akiwa Mwenyekiti wa chama, alikaa kimya.
Kupitia magazeti ya Uhuru na Mzalendo, Kolimba anadaiwa kuwatumia waandishi ambao inadaiwa pia walikuwa wakitumia majina tofauti, kama ilivyopata kufichuliwa na gazeti jingine la binafsi baadaye.
Baadhi ya makala hizo ni zile zilizotolewa katika gazeti la Uhuru la Novemba 8, mwaka 1994 ukurasa wa saba na Novemba 18, mwaka huo huo, pia ukurasa wa saba. Makala hizi inaelezwa ziliandikwa na Kolimba lakini kwa jina la mwandishi aliyejiita Alex Kowe.
Makala hizi (ambazo nitazichambua siku zijazo) ziliandikwa katika wakati ambao kwanza ni mwaka mmoja kuelekea Uchaguzi Mkuu huku Kolimba akidaiwa kutaka kuwania urais.
Lakini pia ni yeye ambaye kuelekea uchaguzi huo huo wa 1995, aliweka bayana chama anachokiongoza kimepoteza dira, ikielezwa angegombea kwa chama kingine.
Na kwa namna ya kipekee katika kile kinachoelezwa ni kujibu mapigo ya Mwalimu Nyerere kwa kitabu chake cha “Uongozi wetu na Hatima ya Tanzania” Novemba 4, mwaka 1994, Kolimba alijigamba mbele ya waandishi kuwa; hajioni kuwa na kasoro kama Mtendaji Mkuu wa CCM na kwamba uamuzi ni wa wananchi.
Kauli yake kwamba; “uamuzi ni wa wananchi” ilizua maswali mengi kwa baadhi ya watu na hasa waliopata kuhisi au kuelezwa kuwa Kolimba anataka kuwania urais mwaka 1995. Kwamba alitaka awe Amiri Jeshi Mkuu wa tatu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama.
Maswali ni mengi na miongoni mwa hoja zilizoibuka ni kwanza; Kolimba ambaye si kiongozi wa kuchaguliwa (mteule) ni kwa vipi aseme wananchi wawe waamuzi wakati hawakuwahi kumchagua?
Je, alitaka kwenda kujipima kwa wananchi kwa njia ya kupigiwa kura baada ya kuachana na wadhifa wa kuteuliwa? Na je, kupigiwa kura katika nafasi ipi ya uongozi? Je, ni urais?
Swali kubwa zaidi ni; je, kwa kauli hiyo kama Kolimba angekwenda kugombea urais, asingeungwa mkono na Mwalimu Nyerere? Kama jibu ni hapana, je, angeungwa mkono na Mwinyi pamoja na viongozi wengine waliotofautiana na Mwalimu kuhusu uongozi wa nchi na hususan kuelekea Uchaguzi Mkuu wa mwaka 1995?
Lakini katikati ya kile kinachoelezwa kuwa ni majibu ya Kolimba kwa Nyerere kupitia vyombo vya habari vya chama, wapo waandishi wa habari waliodokezwa kuhusu mipango ya Kolimba na ‘wakachochewa’ ili kwenda kumuuliza Mwalimu.
Wamuulize kwanza; kama amesoma mfululizo wa makala kwenye magazeti ya chama ambazo ingawa zimeandikwa na ‘waandishi’ (kwa majina mengine si Kolimba) lakini zinamjibu na hata kumshambulia.
Pili, nini majibu yake. Tatu, anadhani Kolimba anapata wapi ‘ujasiri’ huo wa kutumia hata vyombo vya chama kwa maslahi yake kisiasa? Yalikuwa maswali ya kumchokoza Mwalimu na hata kupima upeo wake wa busara.
Majibu ya Mwalimu Nyerere ambayo pia yamenukuliwa katika baadhi ya machapisho nchini yanaeleza kwa kifupi lakini katika hali ya upeo mkubwa wa busara, pengine kinyume cha hata matarajio ya wanahabari hao kwamba Mwalimu angehamaki.
Mwalimu Nyerere ananukuliwa kuwajibu waandishi waliomfuata katika hali ya utulivu akitamka maneno sita tu. Akawajibu akisema; mwacheni aendelee, tutajibizana hoja kwa hoja.”
Majibu haya ya Mwalimu bila shaka hayakukidhi matarajio ya waandishi wa habari waliokuwa wakifuatilia sakata hilo kwa kina, na hapa bila shaka, Katibu Mkuu wa Baraza la Habari Tanzania (MCT) kwa sasa, Kajubi Mukajanga, anafahamu hili kwa namna fulani, wakati huo akiwa Mhariri wa gazeti la kila wiki la WAKATI ni HUU.
Lakini pia maneno hayo sita tu ya Mwalimu katika suala pana la mgogoro wa kiuongozi, yalithibitisha Mwalimu alikuwa na taarifa za Kolimba kutumia vyombo vya chama kumjibu, kisichojulikana dhahiri ni je, ‘wakubwa’ gani walikuwa kambi ya Kolimba dhidi ya Nyerere?
Kwa kuzingatia mazingira hayo, wanahabari walizidi kuhoji kwa mfano; pamoja na kwamba Rais Ali Hassan Mwinyi, ni Mwenyekiti wa CCM na ameelezwa kuhusu ‘matatizo’ hayo ya Kolimba kutumia vyombo vya chama kwa kadiri anavyotaka, kwa nini hafanyi lolote?
Maswali hayo na mengine yaliongeza joto na kwa kipekee, ukali wa joto uliongezwa na majibu ya Nyerere; mwacheni tutapambana kwa hoja. Hatimaye, kutokana na joto hilo Mzee Mwinyi akapewa tafsiri kuwa alikuwa akimuunga mkono Kolimba na hasa ikieleweka kuwa naye ni majeruhi katika kitabu cha Uongozi wetu na Hatima ya Tanzania.
Wiki ijayo tutaangalia hoja za Kolimba katika kujibu mapigo ya Mwalimu Julius Nyerere, akitumia magazeti ya chama angali akiwa Katibu Mkuu, huku kimya cha Mwenyekiti wa chama, Ali Hasssan Mwinyi kikizidi kubeba tafsiri ya kumuunga mkono Kolimba.
 
dilunga_1.jpg



Nini kilichotokea kati ya Kolimba na Nyerere? II










Godfrey Dilunga

Toleo la 224
1 Feb 2012













WIKI iliyopita katika sehemu ya kwanza ya mfululizo wa makala hizi, nilieleza katika hali ya kudadisi zaidi ni kwa nini viongozi wengi hawakuwa tayari kumkosoa Mwalimu Julius Nyerere hadharani na kama baadhi walithubutu, basi, walikuwa wachache mno na ukosoaji ulikuwa wa nadra.
Nilieleza kuwa wengi hawakuwa katika ‘mizani' sawa na Mwalimu kwa kigezo cha uadilifu mbele ya umma na hata wale waadilifu, ilitokea wakiiga njia ya uadilifu wa Mwalimu Nyerere. Lakini pia nilieleza licha ya nguvu hizo za kiuadilifu, Mwalimu alikuwa na ushawishi mkubwa katika mifumo ya kidola nchini.
Mifumo ya kidola ambayo alishiriki kuibuni na kuiridhia, akiwa Mkuu wa Nchi wa kwanza baada ya Uhuru wa iliyokuwa Tanganyika na hata Tanzania (baada ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar).
Nilieleza ni Mwalimu Nyerere ambaye ujasiri wake wa kumkosoa yeyote hadharani, ulivunja mipaka na hadi kumgusa Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama, Rais aliyekuwa madarakani, Ali Hassan Mwinyi.
Ukosoaji huo pia uliwagusa bila woga, aliyekuwa Waziri Mkuu, John Malecela na aliyepata kuwa Katibu Mkuu wa chama tawala (CCM), Horace Kolimba. Hawa wote aliwakosoa kupitia kitabu chake cha Uongozi wetu na Hatima ya Tanzania.
Makala ilieleza kuwa ni Kolimba pekee kati ya viongozi hao watatu ndiye aliyejitokeza kujibu mapigo dhidi ya Mwalimu kupitia makala maalumu katika magazeti ya chama (CCM), akiwa Katibu Mkuu, huku Mwinyi na Malecela wakibaki kimya.
Nikaeleza, Mwalimu alijua hilo hasa pale alipoulizwa wanahabari na kujibu akitamka maneno sita tu; mwacheni nitajibizana naye hoja kwa hoja. Hata hivyo, katika makala hiyo ya kwanza katika mfululizo wa makala hizi, kulikuwa na makosa.
Nilieleza Kolimba alitamka CCM kupoteza dira akiwa angali Katibu Mkuu wa chama hicho, ukweli ni kwamba alitamka hivyo lakini wakati akiwa tayari ameondoka kwenye nafasi hiyo.
Leo tunaendelea na sehemu hii ya pili ya mfululizo wa makala hizi. Katika sehemu hii ya pili, naanza kuchambua hoja za Kolimba katika kujibu mapigo dhidi ya Mwalimu Nyerere.
Kolimba ambaye kama tulivyoona katika sehemu ya kwanza ya mfululizo wa makala hizi, tayari alikuwa na nia ya kugombea urais katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 1995. Inawezekana ukosoaji wa Mwalimu dhidi yake aliutafsiri kama kikwazo na kwamba Mwalimu ameingilia nia yake hiyo (lugha ya siku hizi kumchafua-sio kumkosoa).
Inadaiwa kuwa Kolimba kupitia kwa mwandishi aliyetambulishwa kwa jina la Alex Kowe, aliandika makala katika gazeti la Uhuru, Novemba 8, 1994, takriban miezi 10 kabla ya Uchaguzi Mkuu wa 1995.
Miongoni mwa hoja zake katika makala husika ni malalamiko dhidi ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere. Anamlalamikia Nyerere kwa kile anachokieleza kuwa ni hatua yake ya kumlazimisha Rais Ali Hassan Mwinyi, asipokee ushauri wake (Kolimba).
Ni Nyerere pekee angeweza kufafanua hili ingawa pia inawezekana alimuonya Mwinyi kutopokea ushauri wa Kolimba pengine baada ya kubaini ni aina ya kiongozi asiyeaminika kwa kiwango cha kuridhisha katika baadhi ya masuala ya kiuongozi.
Ni kutokana na maelezo ya Nyerere kwa Mwinyi kwamba ushauri wa Kolimba ni wa shaka, Kolimba mwenyewe anapinga hilo akisema haikuwa sahihi kwa sababu anaamini si wakati wote angekuwa na ushauri mbaya au ushauri wenye nia mbaya kwa Rais Mwinyi.
Ni katika mazingira hayo ya kumuonya Mzee Ali Hassan Mwnyi kutoamini moja kwa moja ushauri wa Kolimba, kuna maelezo pia yanayodai kwamba Nyerere alikuwa akimwona Rais Mwinyi kuwa ni kiongozi aliyezongwa na udhaifu wa kiuongozi.
Udhaifu aliouona Nyerere kwa Mzee Mwinyi unadaiwa ni kuhusu namna ya kuchuja (kupima) ushauri kutoka kwa viongozi wengine wanaomsaidia na hapa, izingatiwe kuwa, ushauri mbovu ni msingi wa uamuzi mbovu.
Kwa hiyo, Kolimba kupitia makala hiyo ambayo inadaiwa kuandikwa naye ingawa ilipewa jina (by-line) la Alex Kowe, anapingana na Nyerere kuhusu hoja ya udhaifu wa Mwinyi kiuongozi. Katika kupinga, Kolimba anadai kwamba udhaifu wa Mwinyi si kushindwa kuchuja (kupima) ushauri bali ni uungwana wake kupita kiasi.
Anasema Mwinyi ni muungwana kupita kiasi. Kwa mujibu wa Kolimba, msingi wa uungwana huo wa Mwinyi uliovuka mipaka ni mwelekeo wake wa kuchelea kumuudhi (kutompinga) Baba wa Taifa na hivyo kumpa mwanya wa kumyumbisha.
Kwa lugha nyingine, wakati Nyerere anaamini Mzee Mwinyi ni dhaifu katika baadhi ya masuala ya kiuongozi na hasa kupima ushauri anaopewa na wasaidizi wake, Kolimba aliamini huo si udhaifu kwa tafsiri halisi ya udhaifu, bali ni uungwana uliopita kiasi ambao Nyerere ‘aliutumia' kumyumbisha Mwinyi kiuongozi.
Kolimba anamgeukia Nyerere akijibu mapigo kutoka kitabu cha Uongozi wetu na Hatima ya Tanzania dhidi yao (Kolimba na wenzake Mwinyi, Malecela) akimwelezea (Nyerere) kuwa ni mtu ambaye haambiliki na ni king'ang'anizi.
Katika mashambulizi yake kwa Nyerere ambaye tayari katika makala iliyopita tuliona alifuatwa na waandishi wa habari na wakamuuliza kuhusu mashambulizi dhidi yake kutoka kwa Kolimba naye akawajibu; mwacheni aendelee nitajibishana naye hoja kwa hoja, Kolimba anasema Nyerere akishikilia jambo lake huwa hashauriki kwa urahisi na wala hashawishiki.
Katika sentensi fupi akimwelezea Nyerere, Kolimba kupitia makala anayodaiwa kuiandika na kubandika jina la Alex Kowe, anamtafsiri akisema kwake (Nyerere); "msimamo kwanza na maslahi baadaye."
Kolimba anatetea tafsiri yake hiyo dhidi ya Nyerere (msimamo kwanza na maslahi baadaye) akiorodhesha mambo ambayo anaamini Nyerere aliyasimamia kwa kutanguliza msimamo badala ya maslahi ya nchi na hivyo, hayakuwa na mafanikio mazuri kwa nchi.
Mambo hayo ambayo Kolimba anaamini yalitekelezwa kwa msimamo usioridhia ushauri ni kwanza; Azimio la Arusha. Pili, operesheni vijiji. Tatu, kuvunjika kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki iliyokuwa ikiundwa na nchi tatu- Tanzania, Kenya na Uganda (mwaka 1977).
Nne, mapambano yake (Nyerere) ya muda mrefu dhidi ya sera za Shirika la Fedha duniani (IMF), kwa wakati huo Mwalimu akikerwa mno na masharti ya shirika hilo kwa nchi masikini akifikia hatua kutamka IMF si Wizara ya Fedha ya Dunia.
Kolimba katika makala hiyo anayodaiwa kuiandika yeye, anamkabili Mwalimu akisema mambo hayo manne ni mifano na vielelezo vya misimamo mikali ya kisiasa ya Mwalimu Nyerere, ambayo haikutanguliza mbele maslahi ya taifa na watu wake. Hii ni sehemu ya pili ya mfululizo wa makala hizi kuhusu nini kilichotokea kati ya Kolimba na Mwalimu Nyerere?
Wiki ijayo tutachambua namna wakati fulani Kolimba alipofurahia ‘kusita' kwa Mzee Mwinyi kukidhi haja za shinikizo la Mwalimu Nyerere, kutaka yeye (Kolimba) na Malecela waondolewe madarakani. Tutaangalia je, Kolimba alichukuliaje uamuzi huo wa Mwinyi ambao hata hivyo, baadaye waliondolewa madarakani.
Kwake yeye Kolimba, kitendo cha Rais Mwinyi kukataa shinikizo la Mwalimu Nyerere kutaka Malecela na yeye waondolewe madarakani (jambo kuchelewa kutekeleza shinikizo hilo) ni kitendo cha ujasiri na wala si kielelezo cha udhaifu kama ambavyo Nyerere angetaka Watanzania waamini.
 
Ingependeza kama mtu mmoja anayeijua vizuri historia ya Kolimba ataiweka humu kwa mapana na marefu kwa sababu wengi wetu hatufahamu kwe undani historia ya mtu huyu.
Horace Kolimba alikua mbnge wa Ludewa kipindi hicho ludewa mkoa wa Iringa ,pia alijua katibu mkuu wa chama cha siasa ccm aliongoza kipindi cha mkapa ana watoto wa 5 ,mkewe yupo kwembe Dsm .Kwa kifupu.
 
Labda ungetuambia kalifanyia nini Taifa hadi akumbukwe. Vinginevyo sasa kila mtu atakumbukwa.
 
Kuna mtu wa kusini anakumbukwa, watu wa kusini ni toilet paper wanatumiwa kwenye uchaguzi , na kutupwa mbali
 
Uzi umenikumbusha ile hadithi ya yule nyoka kutoka kaskazini. Alinyoosha mikono juu lakini wazee wa kazi wakampelekea shaba.

Mfumo ni dudu fulani hivi lina sura mbaya, muda wowote ule mtu anageukwa tena pasipo kufahamu.
 
Horace Kolimba alikua mbnge wa Ludewa kipindi hicho ludewa mkoa wa Iringa ,pia alijua katibu mkuu wa chama cha siasa ccm aliongoza kipindi cha mkapa ana watoto wa 5 ,mkewe yupo kwembe Dsm .Kwa kifupu.
nakumbuka niliona picha ya huyu mama analia sana kwenye gazeti la Dar Leo kama sijakosea kipindi hicho ilikua huzuni sana

kitochi
 
"CCM haina dira wala mwelekeo" haya yataishi milele, RIP Katibu wetu Mkuu.
 
Back
Top Bottom