Hadithi ya mashimo ya mfalme Sulemani

blackstarline

JF-Expert Member
Sep 19, 2016
3,092
7,468
UTANGULIZI
Hadithi hii ilipigwa chapa kwa lugha ya Kiingereza katika mwaka 1885. Katika mwaka 1905 Bwana H. Rider Haggard aliandika maneno haya: 'Sasa katika mwaka 1905 naweza kuzidisha maneno yangu kwa kusema ya kuwa nimefurahishwa sana kuona hadithi yangu inadumu kuwapendeza wasomaji wengi. Hayo yaliyobuniwa yamedhibitishwa kuwa ni kweli: Mashimo ya Malme Sulemani niliyokuwa nikiyafikiri sasa yamegunduliwa nayo sasa yanatoa dhahabu tena, na kwa habari zilizotoka hivi karibuni hata almasi pia hutoka.'

MASHIMO YA MFALME SULEIMAN​

SURA YA KWANZA​

Kukutana na Bwana Henry Curtis​

Ni ajabu sana kwa mtu aliyefika umri wangu, yaani miaka hamsini na tano, kushika kalamu na kuanza kuandika kitabu, kama hivi ‘nifanyavyo mimi sasa. Sijui habari hizi zitakuwaje nikiisha kuzitunga, yaani nikijaliwa kufika mwisho wa safari yangu salama, maana ingawa nimefanya mambo mengi katika maisha yangu, lakini sijawahi kujaribu kuandika kitabu. Tokea utoto wangu nimeshughulika na kazi ya biashara na kuwinda, kupigana na kuchimba dhahabu, na tangu kupata utajiri huu nilionao ni miezi minane tu.



Sasa nina mali nyingi sana, hata jumla yake siijui, lakini nadhani nisingekubali kuvumilia tena hayo yote niliyoyavumilia katika miezi kumi na tano iliyopita hata kama ningejua kwa hakika kuwa nitatoka salama pamoja na mali nyingi pia. Mimi ni mtu mtaratibu, sipendi ghasia, na tena nimechoka kabisa kusafirisafiri na kupambana na mambo ya ajabu. Sijui kwa nini naandika kitabu hiki, maana uandishi si kazi yangu. Mimi si mwana chuoni ingawa napenda sana kusoma vitabu. Hebu kwanza nijaribu kuandika sababu zangu za kutunga kitabu hiki, ili muone kama kweli ninazo sababu.

Sababu ya kwanza ni kuwa Bwana Henry Curtis na Bwana Good wameniomba nikitunge. Sababu ya pili ni kuwa nimebaki hapa Durban kwa kuwa mguu wangu wa kushoto waniuma sana. Tangu nilipoumwa na simba ninapata maumivu, na hasa siku hizi yanazidi, hata siwezi kwenda vizuri. Nadhani haikosi meno ya simba yana sumu na kama sivyo majeraha yangeisha pona kabisa na yasinge rudi tena, na hasa ajabu ni kuwa yanarejea mwezi ule ule niliyong’atwa. Ni ajabu sana kuwa baada ya kuua simba sitini na tano na labda zaidi, Yule wa sitini na sita aliniuma mguu. Jambo hili limeharibu mipango yangu ya desturi yote, na kwa kuwa mimi ni mtu wa kufuata taratibu na mipango naona dhiki kabisa. Lakini hayo hayamo katika habari za kitabu hiki.

Sababu ya tatu ni kuwa nataka mwanangu Harry anaesoma katika chuo cha utabibu, awe na mazungumzo ya kumfurahisha na kumpendeza. Asifanye upumbavu. Kusomea utabibu si kazi rahisi, na kazi ya kuvumbua habari za mwili vile vile inachosha. Habari zilizomo katika kitabu hiki si kama zile zinazotokea kila siku, kwa hivyo labda zitamfurahisha kwa muda kidogo.

Sababu ya nne na ilivyo ya mwisho ni kuwa nataka kusimulia hadithi ya ajabu kupita zote ninazozijua. Labda itakuwa ajabu kweli kwa kuwa hapana mwanamke aliyetajwa katika hadithi hii, ila Foulata. Lakini ngoja kwanza! Nilitaka kumsahau Gagula, lakini sina hakika kama alikuwa mwanamke au shetani. Lakini kwa umri wake ulizidi miaka mia moja na kwa kuwa: haoleki, basi simhesabu kuwa mwanamke. Basi afadhali nijifunge kibwebwe. Kazi ni ngumu nami naona kama nimekwisha yavulia nguo maji. Lakini kama wasemavyo wajuzi, ‘Pole pole ndio mwendo,’ Basi sasa naanza.

‘Mimi Alan Quatermain, mzaliwa wa Durban, Natal, naapa na kusema …’Hii ndiyo namna nilivyoanza kusema mbele ya kadhi nilipokuwa natoa habari za kufa kwa Khiva na Ventvogel, lakini naona kuwa hii siyo namna ya kuanza kutunga kitabu. Basi, je, mimi ni muungwana? Muungwana ni nini? Sijui hakika. Maisha yangu yote nilikuwa nikifanya kazi ya biashara na kuwinda tu. Nimejaribu daima kuwa muungwana, basi wewe usomaye utanihukumu. Mungu ajua kuwa nimejaribu. Ama kweli katika maisha yangu nimeua watu wengi, lakini sikuu mtu bure wala sikuua mtu asiye na hatia, ila kwa kujilinda mwenyewe tu. Mwenyezi Mungu alitupa maisha, nadhani nia yake ni kwamba tujilinde, nami siku zote nimeshikilia hivyo ; natumaini kwamba hayo hayatanitia hatiani siku ya kuhukumiwa itakapowadia.

Lakini dunia ina ukali na maovu, na ingawa mimi ni mtu taratibu na mwoga kidogo nimeona mauaji mengi. Lakini naweza kusema kuwa sijaiba, ingawa mara moja nilimdanganya mtu mmoja nikachukua kundi la ng’ombe wake. Lakini yeye alikuwa amenifanyia mambo mabaya kabisa na hata hivyo, tangu siku ile ninajuta kwa vitendo vyangu nilivyovifanya.

Toka nilipokutana na Bwana Henry Curtis na Bwana Good mara ya kwanza, imepita miezi kumi na nane, na namna tulivyokutana ilikuwa hivi: Nilikwenda kupita Bamangwato ili kuwinda ndovu. Nikawa na bahati mbaya sana katika safari hiyo, na juu ya hayo nilishikwa na homa kali. Nilipopona nikasafiri mpaka kunakochimbwa almasi, nikauza pembe zangu zote nilizokuwa nazo pamoja na gari la ng’ombe, nikawapa ruhusa wawindaji wangu, na mimi mwenyewe nikapanda gari niende Captown. Baada ya kukaa Captown kwa muda wa jumaa moja niliona kuwa gharama za hoteli zinazidi sana, tena nilikuwa nimekwisha ona yote niliyoyataka kuyaona, basi nikanuia kurudi Natal kwa meli iitwayo Edinburg Castle inayotoka Ulaya.

Basi nikaenda kukata tiketi nikaingia melini, na jioni ile ile meli ikang’oa nanga tukasafiri. Katika abiria walioingia melini niliona wawili niliowatazama sana. Mmoja alikuwa mtu mwenye umri kadiri ya miaka thelathini, kifua kipana na mikono mirefu kushinda watu wote niliowahi kuwaona. Nywele zake zilikuwa za rangi ya kimanjano na alikuwa na ndevu nyingi za rangi ile ile, na macho yake yalikuwa ya rangi ya kijivujivu tena yameingia ndani. Wala nilikuwa sikupata kuona mtu mzuri kumpita yeye. Halafu nikajua kuwa huyu ni Bwana Henry Curtis. Yule mtu mwingine aliyekuwa akiongea na Bwana Henry alikuwa mfupi tena mnene, kisha mweusi kidogo, na sura yake ilikuwa haikufanana hata kidogo na ile ya Bwana Henry. Halafu nikajua kuwa anaitwa Bwana Good.

Basi jioni nilipokuwako sitahani nilisikia sauti, mara nikageuka kuangalia, nikaona kuwa ni Yule Bwana Good. Hata tulipokwenda chini kula chakula tulimkuta Bwana Henry amekwisha kaa mezani, na mara tukaanza kuongea habari za kuwinda na mambo mengineyo. Akaniuliza maswali mengineyo. Akaniuliza maswali mengi sana, nami nikamjibu kadiri nilivyoweza. Halafu yake tukaanza kuongea habari za ndovu, na mtu mmoja aliyekuwa karibu yetu akasema, ‘Ee bwana, kama ukitaka mtu hasa anayeweza kukwambia kweli habari za ndovu, ni mwindaji Quatermain.’ Bwana Henry Curtis aliposikia hivi, akashtuka na akasema kwa sauti ya upole, ‘Niwie radhi bwana, jina lako wewe ni Allan Quatermain?’ Nikamwambia, ‘Ndiye mimi.’

Tulipokwisha kula, tukawa tunatoka mezani, na Bwana Henry akanijia kunikaribisha niende chumbani kwake tukavute tumbako, nami nikakubali. Mradi tulikuwa watu watatu, na mara Bwana Henry Curtis akasema, ‘Bwana Quatermain, nadhani miaka miwili iliyopita ulipata kuwako mahali panapoitwa Bamangwato katika nchi ya Transvaal,sivyo? Kusikia hivyo nikaona ajabu sana yeye kujua habari za safari zangu. Nikamwambia, ‘Ndiyo nilikuwako’, Bwana Good akauliza, ‘Ulikuwa ukifanya biashara sivyo?’ Nikajibu, ‘Ndiyo, nilichukua gari la bidhaa nikapiga kambi nje ya mji, nikakaa huko mpaka nilipokwisha kuuza zote .’ Bwana Henry aliyekuwa amekaa katika kiti kukabili kiti changu, akaniuliza, ‘Ulipata kukutana na mtu mmoja jina lake Neville?’ Nikajibu, ‘Ndiyo, tulipiga kambi zetu karibu kwa muda wa siku kumi na nne, na baada ya miezi michache nikapokea barua kutoka kwa Mwana Sheria ya kuniuliza habari zake kama namjua alipo, nami nikapeleka majibu kueleza habari zake kama nilivyoweza.’

Bwana Henry akasema, ‘Najua, maana barua yako ililetwa kwangu. Ulisema kwamba mtu aitwaye Neville alitoka Bamangwato mwanzo wa mwezi wa Mei akasafiri kwa gari pamoja na watu wake na mwindaji mtu mweusi mmoja jina lake Jim, naye alisema kuwa anakwenda mpaka Inyati ambao ndio mji wa mwisho katika nchi ya Mtabele ; akifika hapo atauza gari lake aende kwa miguu. Kisha ulisema kuwa kweli aliuza gari lake kwa sababu uliliona tena baada ya miezi sita, na mtu uliyemwona nalo alikuwa ni Mreno mfanya biashara aliyekwambia kuwa amelinunua Inyati kwa mtu mweupe mmoja, ambaye jina lake amelisahau ila anafikiri kuwa yeye pamoja na boi wake amekwenda mwituni kuwinda.’ Nikajibu, ‘Hayo ni kweli.’ Basi tukanyamaza kidogo, kisha, Bwana Henry Curtis akasema, ‘Naona ya kuwa hujui vema habari hizo. Huwezi kukisia sababu zake za kusafiri kwenda kaskazini na mahali gani alipokwenda?’ Nikamjibu, ‘Nilisikia kidogo.’

Na kwa kuwa sikutaka kusema naye zaidi juu ya habari hizi nikanyamaza kimya. Bwana Henry na Bwana Good wakatazamana, kisha Bwana Good akatikisa kichwa kwa kumfanyia ishara Bwana Henry, akasema, ‘Bwana Quatermain nitakusimulia hadithi yangu, halafu unipe shauri na msaada wako. Yule wakili wangu aliyeniletea barua yako aliniambia kuwa wewe ni mtu wa heshima sana na watu wote wanakustahi, na kwa hiyo naweza kukuamini. Basi nikainamisha kichwa kwa haya kwa vile nilivyosifiwa na Bwana Henry akaendelea kusema, ‘Huyo Bwana Neville ni ndugu yangu.’ Niliposikia hivi nikastuka sana, maana sasa nalifahamu sababu ya kumtazama sana nilimwona mara ya kwanza, kwa kuwa wamefanana sana.

Basi Bwana Henry akaendelea kusema, ‘Yeye ni mdogo wangu, na mpaka miaka mitano iliopita nadhani hatukupata kuachana hata kwamuda wa mwezi mmoja. Lakini katika mwaka ule wa mwisho tulioonana tulipatwa na msiba kama wanavyopatwa watu wote mara kwa mara. Maana tuligombana sana hata nilimtenda mambo yasiyo ya haki kwa ajili ya hasira zangu. Haikosi unajua kuwa mtu akifa na kama mali yake ni mashamba tu, wala naye hakuacha wosia wowote, kwa sheria ya Uingereza mrithi huwa ni Yule mtoto mwanaume mkubwa, yaani aliyezaliwa kwanza, ndiye anayechukua mali yote. Basi hivyo ndivyo ilivyokuwa. Na wakati ule tulipokuwa tukigombana baba yetu alifariki naye hakuwahi kuandika wosia. Basi kwa hivyo ilionekana kuwa mdogo wangu hakuwa na urithi.

Kusema kweli ilikuwa ni wajibu wangu kumsaidia na kumtunza, lakini kwa ule uchungu wa ugomvi jinsi ulivyokuwa mwingi sana, hata sasa naona aibu kukiri kuwa sikufanya jambo. Sikuwa na nia ya kumnyima haki yake, ila nilitaka yeye aje kwangu’ kuomba suluhu, naye hakuja. Nasikitika sana kukuudhi kwa habari hizi zangu, lakini naona sina budi kukueleza waziwazi mambo yote, sivyo Bwana Good?’ Bwana Good akajibu, ‘Ndivyo, nami najua kwa hakika kuwa Bwana Quatermain atayasitiri yote moyoni mwake.’ Nikajibu, ‘Vema,’ Maana mimi natafakari sana kuwa si mtu wa kupayuka.

Halafu Bwana Henry akasema, ‘Mdogo wangu alikuwa na fedha kidogo na bila kunishauri alitoa fedha zote alizokuwa nazo katika banki, na kuchukua jina lingine la Neville, akafunga safari kwenda kuchuma Afrika ya Kusini. Nikakaa kwa muda wa miaka mitatu bila kupata habari zake wala salamu zake, ingawa mimi nilimwandikia barua nyingi. Labda zilikuwa hazimfikii. Lakini baadaye nikaanza kuwa na wasiwasi, maana mtu haachi kumpenda ndugu yake.’
Nikasema, ‘Hayo ni ya kweli. ‘Maana nilikuwa nikimkumbuka mtoto wangu. Bwana Henry akawa anaendelea kusema, ‘Nikahisi kuwa hata nusu ya mali yangu yote nitatoa ili nipate kujua yaliyompata mdogo wangu, maana ni mmoja tu aliyebaki katika ukoo wangu. Basi siku zilipozidi kupita nami nikazidi kuwa na wasiwasi, nikatamani sana kupata habari zake. Ndipo nikaanza kuulizauliza, hata nikapata ile barua. Basi mpaka sasa habari ni nzuri, maana zaonyesha kuwa yu hai mpaka sasa. Na nilitia nia kwenda mwenyewe kumtafuta, na Bwana Good amenifurahisha sana kwa kufuatana nami.’ Basi Bwana Good akasema, ‘Ndiyo na sasa Bwana, labda utatwambia habari zote ujuazo za Yule mtu aitwaye Neville.’

SURA YA PILI

Basi kabla sijaanza kumjibu Bwana Good, nilitia tumbako katika kiko changu, na Bwana Henry akauliza, ‘ Ulisikia habari gani juu ya safari ya ndugu yangu ulipokuwako Bamangwato?’ Nikamjibu, ‘Nalisikia hivi, ya kuwa anakwenda kutafuta Mashimo ya Sulemani. Na tangu siku hiyo hata hivi leo, sijamwambia mtu habari hizo.’ Wote wawili wakauliza pamoja, ‘Mashimo ya Sulemani! Yapo wapi?’ Nikajibu, ‘Mimi sijui, lakini najua mahali ambapo watu husema kuwa yapo. Siku moja niliona vilele vya milima inayopakana nayo, lakini baina ya mahali hapo nilipokuwa mimi na milima hiyo palikuwa na jangwa la upana wa maili mia moja na thelathini, nami sijapata kusikia kuwa Mzungu yeyote amepata kuvuka jangwa hilo, isipokuwa mtu mmoja tu.



Lakini nadhani itakuwa vizuri zaidi nikisimulia habari hizo, yaani kama nilivyopokea kutoka kwa wenyeji, za Mashimo ya Sulemani kwa kadiri ninavyojua, ikiwa mtaahidi kuwa mtazisitiri mioyoni mwenu na kutomwambia mtu yeyote bila ya idhini yangu. Je, mtakubali sharti hilo?’ Bwana Henry akainamisha kichwa, na Bwana Good akaitikia, ‘Naam, naam.’ Basi, nikaanza kutoa hadithi yangu: ‘Kwa kawaida mwajua kuwa wawindaji wa ndovu ni watu wasiotamani anasa za dunia, wala hawashughuliki na mambo ila ya kweli ya dunia. Lakini pengine mwaweza kumkuta mtu mmoja mmoja anajitia katika mambo ya kuandika hadithi na kujaribu kutunga habari za zamani za watu wa kale. aliyeniambia maneno haya alikuwa ni mtu wa namna hiyo, na tangu aliponiambia maneno haya umepita muda wa miaka thelathini. Ilikuwa hivi: katika safari yangu ya kwanza nilikwenda kuwinda ndovukatika nchi ya Matabele. Mtu mmoja aliyeitwa Evans ndiye aliyeniambia maneno hayo, naye masikini aliuawana nyati mwaka wa pili yake, akazikwa mahali palipokuwa karibu na maporomoko ya maji yam to wa Zambezi. Nami nakumbuka sana kuwa siku moja nilikuwa nikizungumzia habari za kulungu na pofu katika mtaa mmoja wa Transvaal.’

Evans akasema, ‘Ndiyo, lakini mimi nitakutolea hadithi iliyo ya ajabu zaidi kupita habari za wanyama.’ Akaendelea kuhadithia jinsi alivyopata kuvumbua magofu ya mji wa zamani sana ambao aliamini kuwa ni mji ule uliokuwa ukiitwa Ophir uliotajwa katika Agano la Kale,na tangu siku hizo, watu wengi wenye maarifa kuliko yeye marehemu Evans wamesema hivyohivyo. Mimi nikakaa kusikiliza sana, maana wakati ule mimi nilikuwa bado kijana, na hadithi zile za kale zilinipendeza sana, na mara akasema, ‘je, mwanangu, umepata kusikia habari za milima ya Sulemani iliyo upande wa kaskazini wa nchi ya Mashukulumbwe?’’ , Nikamwambia, ‘Sijapata kusikia .’Akasema, ‘Basi, haidhuru, hapo ndipo mashimo ya Sulemani yalipo, yaani mashimo ya almasi.’ Nikamuuliza, ‘Je, wewe umejuaje?’ Akajibu, ‘Najuaje! Najua kwa jina lake lilivyo, na tena niliambiwa na mwanamke mmoja mchawi wa kabila la Isanusi katika nchi ya Manika. Alisema kwamba watu wanaokaa upande wa pili wa milima ile ni wa ukoo wa Amazulu, wanasema lugha inayofanana na Kizulu, ila wao ni wakubwa, tena wazuri zaidi ya Amazulu. Lakini kuna wachawi wenye nguvu nyingi wanaokaa humo na walikuwa na siri ya shimo la ajabu lenye mawe yale yanayong’aa.’ Nilicheka sana niliposikia hadithi hii, nikaipuuza, lakini ilinipendeza sana, maana wakati ule mashimo ya almasi yalikuwa bado hayajavumbuliwa. Lakini Yule marehemu Evans aliuawa, nami nikakaa muda wa miaka ishirini bila kufikiri tena jambo hili.

Baada ya miaka ishirini, na huo ni muda mrefu sana, maana mwindaji wa ndovu ana shida kuishi miaka ishirini katika kazi yake, nikasikia habari zaidi juu ya milima ya Sulemani na nchi iliyo upande wa pili yake. Hapo mimi nilikuwa katika nchi ya Manika, mahali paitwapo KwaSitanda, napo ni mahali pabaya sana, maana sikuweza kupata chakula wala wanyama hakuna. Nilishikwa na homa kali mno hata hali yangu ikawa dhaifu sana, na siku moja akafika Mreno mmoja pamoja na mwenziwe mmoja suriama. Tukaongea kidogo pamoja, maana yeye aliweza kusema Kiingereza kidogo, nami pia nilijua kusema Kireno kidogo, akaniambia kuwa jina lake ni Jose Silvestre, na tena ana shamba karibu na Delagoa Bay. Lakini siku ya pili yake aliondoka pamoja na mwenziwe. Katika kuniaga akasema ‘Bwana, tukionana tena natumai mimi nitakuwa tajiri kuliko watu wote duniani, nami nitakukumbuka.’ Nikacheka kidogo, maana nilikuwa mnyonge kwa homa na kwa hivyo sikuweza kucheka sana; nikamwona akienda kuvuka lile jangwa kwenda upande wa magharibi. Nikadhani kuwa ana wazimu, kwani anakwenda kutafuta nini huko? Baada ya juma moja, nikapona, na jioni nilipokuwa nimekaa nje ya hema langu dogo, nikitafuna paja la kuku wa mwisho niliyemnunua kwa mtu mmoja kwa bei ya kitambaa kimoja kilichonipatia kuku ishirini, nikitazama jua jinsi lilivyokuwa jekundu linavyoshuka nyuma ya jangwa hilo, mara nikaona kitu kama mzungu amevaa koti akiteremka mteremko uliokuwako kiasi hatua mia sita, mbele yangu.

Kwanza mtu huyo alitambaa kwa magoti na mikono, kisha akasimama na kupepesuka hatua chache mbele, tena akaanguka na kutambaa. Mradi nikaona kuwa ni mtu aliye taabani. Nikapeleka mmoja wa wawindaji wangu kwenda kumsaidia, na baadae kidogo akaja nae. Je, wadhani alikuwa ni nani? Alikuwa ni Yule Jose Silvetre, kwa kweli, mifupa yake ilikuwa dhaifu, tena alikuwa amekonda kabisa. Uso wake ulikuwa manjano, uking’aa kwa homa aliyokuwa nayo, nayale macho yake meusi makubwa yalionekana kama yaliyotokeza nje, maana alikuwa hana nyama kabisa .. Ngozi yake ilikuwa imekauka, na nywele zake zilikuwa zimegeuka rangi zikawa nyeupe, na mifupa imemtoka. Akawa anaugua huku akisema, ‘Nipeni maji! Jamani.

Nikaona kuwa midomo yake imepasuka na ulimi ulikuwa mweusi tena umevimba. Nikampa maji yaliyochanganyika na maziwa kidogo, akayabugia. Nikamzuia kusudi asinywe zaidi. Na mara homa ilimshika tena na kuanza kupayuka na kusema habari za milima ya Sulemani, na almasi na jangwa. Nikamchukua na kumweka hemani mwangu nikamtunza kama nilivyoweza; lakini nilijua kuwa atakufa. Kama saa tano ya usiku akatulia kidogo, nami ndipo nilipopata usingizi kidogo, nikalala. Kulipopambazuka nikaamka, nikamwona namna alivyokuwa amekonda sana amekaa na kulikodolea jangwa macho. Baadae kile kianga cha kwanza chajua kilionekana mawinguni, kikaangaza jangwa mpaka kufika kilele kirefu katika milima ya Sulemani, masafa ya maili mia moja na zaidi. Mara Yule mgonjwa akanyosha mkono wake mwembamba kuelekeza kileleni na huku akisema kwa Kireno, ‘Ndipo, ndipo papo hapo, lakini mimi sitawahi kupafikia kamwe. Wala hapana atakayepafikia kwamwe!’ Mara akakaa kimya kidogo kama mtu anayewaza jambo moyoni, halafu akanigeukia akasema, ‘Rafiki bado ungalipo? Ama sasa naona macho yangu yanaingia giza,’ Nikajibu, ‘Ndiyo, nipo hapa hapa.

Lakini sasa afadhali ulale upumzike.’ Akasema, ‘Ndiyo nitapumzika sasa hivi; tena nitakuwa na wasaa mwingi wa kupumzika, hata milele. Nisikilize, ninakufa! Wewe umenitendea mema. Nitakupa hati. Labda utaweza kupafikia ikiwa utaishi na kuvuka jangwa ambalo limemuua mtumishi wangu na mimi!’

Akapapasapapasa katika mfuko wake akatoa kitu nilichokidhania kuwa kikoba cha kuwekea tumbako kilichofanywa kwa ngozi ya mnyama. Kikoba hicho kilifungwa kwa uzi wa ngozi naye alijaribu kukifungua asiweze. Akanipa akisema, ‘Fungua.’Nikakifungua nikatoa kipande cha kitambaa kikuukuu cha katani kilichokuwa kimeandikwa maneno, na ndani ya kitambaa hicho mlikuwamo karatasi. Kisha akasema kwa sauti ya kufifia, maana alizidi kudhofu, akanena, ‘Juu ya hiyo karatasi kumeandikwa yote yaliyoshindikwa juu ya kitambaa na hivyo ilinibidi kufanya kazi miaka hata kuweza kuisoma. Sikiliza: Babu yangu ambaye ilimlazimu kuutoka mji wa Lisbon alikuwa katika Wareno hao wa kwanza waliofika katika nchi hii.

Aliandika maneno hayo wakati alipokuwa akifa katika milima ile ambayo hapana hata Mzungu mmoja aliyepata kuikanyaga kwa miguu yake mpaka hivi leo. Jina lake lilikuwa Jose da Silvestre, naye aliishi miaka mia tatu, nyuma. Mtumishi wake aliyekuwa akimngojea upande huu wa milima aliona kuwa amekwisha kufa, nae ndiye aliyeleta maandishi haya mpaka Delagoa. Na tokea wakati huo yametunzwa na warithi wake, lakini hapana aliyetaka kuyasoma, mpaka mimi nilipofaulu. Nami nimepoteza maisha yangu kwa ajili yake, lakini labda mtu mwingine ataweza kufaulu na kuwa tajiri kupita watu wote duniani. Lakini usimpe mtu mwingine bwana, wewe nenda mwenyewe!’ Akaanza kuugua tena, na baada ya saa moja akafa. Mungu amrehemu. Nilimzika katika kaburi la kwenda chini sana, nikaweka na mawe makubwa juu ili kusudi asifukuliwe na fisi. Kisha nikaondoka pale.

Bwana Henry akauliza, na sauti yake ilionyesha jinsi alivyokuwa akisikiliza maneno yangu, ‘Ehe, lakini hiyo hati iko wapi? Naye Bwana Good akaongeza, ‘Hati hiyo iko wapi sasa, iliandikwa habari gani?’ Nikasema, ‘Mkitaka nitawasimulia habari zake. Nami sijamwonyesha hata mtu mmoja ila Mreno mmoja mfanya biashara aliyekuwa amelewa wakati alipoitafsiri, tena hakosi’ kuwa alikuwa amekwisha sahau habari zake ulevi ulipomtoka. Hicho kitambaa chenyewe nimekiweka kwangu Durban pamoja na hiyo karatasi aliyoifasiri marehemu Jose, lakini hapa ninayo tafsiri ya Kiingereza na nakala ya ramani iliyokuwamo, nayo ni hii:’

Mimi Jose da Silvestre nipo hapa ninakufa kwa njaa ndani, ya pango dogo katika upande wa kaskazini mwa titi la mlima ulio upande wa kusini wa milima miwili ambayo nimeipa jina la Maziwa ya Sheba. Naandika haya kwa kipande cha mfupa na wino wa damu yangu mwenyewe katika mwaka 1590. Ikiwa mtumishi wangu atakuja na kuiona na kuichukua mpaka Delagoa, nataka rafiki yangu (Na hapo katika hati, jina lake limefutika.) ampashe habari mfalme ili alete jeshi la askari watakaoweza kuvuka jangwa hili na kuwashinda hawa Wakukuana walio majabali sana na wenye uchawi mwingi. Lakini kwa sababu ya hila na udanganyifu wa Mchawi Gagula sikuweza kuleta kitu cha ushahidi, tena hata maisha yangu nayo nimeyaokoa kwa shida nyingi. Na huyu atakayekuja na afuate ramani, apande theluji ya ziwa la kushoto la Sheba mpaka afike penye titi, ambapo kwa upande huo wa kaskazini pana njia kuu iliyotengenezwa na Sulemani. Kutoka hapo ni mwendo wa siku tatu kufikia jumba la Mlalme. Basi na amwue Gagula. Nawe niombe dua.

Kwaheri. Jose da Silvestre.

Nilipokwisha soma barua na kuonyesha ile nakala ya ramani iliyoandikwa na Yule mzee kwa damu ya mkono wake, wakanyamaza kimya kwa ajili ya kustaajabu kwao. Baadae Bwana Good akasema, ‘Lo! Nimezunguka dunia mara mbili, tena nimefika bandari nyingi lakini sijapata kusikia hadithi kama hii hata vitabuni.’ Bwana Henry akasema, ‘Ni hadithi ya ajabu Bwana Quatermain. Natumai unajaribu kutuhadaa! Najua kwamba watu hudhani kuwa si vibaya kumhadaa mjinga.’ Niliposikia hivi nikaudhika, nikatwaa karatasi nikaiweka mfukoni, maana sikupenda kudhaniwa kuwa ni mmoja wa wale wapendao kusimulia uwongo na kuwahadithia wageni habari za kuwinda na mambo mengine ambayo hayakutokea kamwe. Basi nikajibu, ‘Kama unafikiri hivyo basi mambo yaishe hapa hapa. Nikasimama nikataka kwenda zangu. Bwana Henry akaniwekea mkono wake begani pangu akasema, ‘ Kaa, Bwana Quatermain, niwie radhi, usiudhike; kwani naona kuwa hupendi kutuhadaa, lakini hadithi yenyewe ni ya ajabu mno hata kwanza niliona vigumu kuisadiki.’

Basi ndipo nilipoanza kutulia kidogo, maana nilipofikiri niliona kuwa si ajabu kuwa yeye hawezi kusadiki hadithi, nikamwambia, Tutakapojaliwa kufika Durban utaona ramani ya asili na maandishi yake. Lakini bado sijakwambia habari za ndugu yako. Nilimjua Yule Jim aliyekuwa pamoja naye. Yeye ni Mbechuana, mwindaji hodari, tena na mtu mwenye busara. Siku hiyo Bwana Neville alipoanza safari yake nilimwona Jim amesimama karibu na gari langu akisokota tumbako yake, nikasema, ‘Jim, safari hii unakwenda wapi? Kuwinda ndovu?’ Akajibu ‘La! Tunakwenda kutafuta kitu kinachotafutwa sana zaidi ya pembe za ndovu.’ Mimi nikazidi kumdadisi, nikamuuliza, ‘Je, kitu hicho chaweza kuwa nini? Ni dhahabu? Akacheka akajibu, ‘siyo Bwana, ni kitu kinachotakiwa zaidi ya dhahabu.’

Basi sikumuuliza neno tena, maana sikupenda kuonekana kuwa ni mdaku. Baada ya Jim kuisha kusokota tumbako yake, akasema ‘Bwana, sisi tunakwenda kutafuta almasi.’ Nikasema, ‘Almasi! Lakini mbona unafuata njia ambayo si njia ya kwendea huko; kwa nini hufuati njia inayoendelea kwenye mashimo?’ Akajibu, ‘ Bwana, umepata kusikia habari za mlima wa Sulemani?’ Nikamjibu, ‘Ndiyo.’ Akaniuliza, ‘Umesikia habari za almasi zilizoko huko?’ Nikwamwambia, ‘Ni upuuzi tu.’ Akanena, ‘Si upuuzi,? Wana maana, namjua mwanamke aliyetoka huko, naye alifika Natal pamoja na mtoto wake, akaniambia; lakiniamekufa sasa.’

Nikamjibu, ‘Wewe na bwana wako mkijaribu kufika nchi ya Sulemani, hamkosi mtaliwa na tai.’ Akacheka, akasema, ‘Labda, bwana . Mtu amezaliwa naye atakufa; nami ningependa kutembea katika nchi ngeni; maana ndovu wanakwisha katika nchi hii.’ Nikasema, ‘Haya, tutaona.’ Baada ya nusu saa nikaona gari la Neville likitoka. Na baadae kidogo Jim akarudi mbio akasema, ‘Kwaheri bwana, kwani sikupenda kuanza safari bila kuagana nawe. Ninaona labda umesema kweli ya kuwa hatutasafiri kwenda kusini tena.’ Nikamuuliza, ‘Je, Jim, wasema kweli? Bwana wako amesema kuwa anakwenda mlima wa Sulemani, au sivyo?’ Akasema, ‘Ni kweli bwana maana aliniambia kuwa imempasa ajaribu kuchuma mali kwa njia yoyote; basi ni afadhali ajaribu kutafuta hiyo almasi.’ Nikasema, ‘Vema Jim, lakini ngoja kwanza, nataka uchukue barua hii, lakini lazima uahidi kuwa hutampa mpaka nifike Inyati.’ Kufika Inyati ilikuwa ni mwendo wa maili kama mia. Basi akaahidi. Nami nikachukua karatasi nikaandika maneno haya: ‘Kwa huyo atakayekuja ..apande theluji ya ziwa la kushoto la Sheba mpaka afike penye titi, ambapo kwa upande huo wa kaskazini pana njia kuu iliyotengenezwa na Sulemani.’

Basi nikampa, kisha nikamwambia, ‘Sasa utakapompa bwana wako barua hii, mwambie afuate sana shauri lililomo. Wala usimpe sasa barua hii kwa sababu sipendi arudi kuja kuniuliza maswali mengi ambayo sitaweza kuyajibu. Haya nenda.’ Basi Jim akaitwaa barua akaenda zake. Na hayo ndiyo yote ninayoyajua juu ya ndugu yako, Bwana Henry; lakini nachelea sana ya kuwa.. ‘Bwana Henry akasema, ‘Tazama, Bwana Quatermain, mimi ninakwenda kumtafuta ndugu yangu; nitamtafuta hata mlima wa Sulemani, hata nitaupita ikiwa ni lazima, mpaka hapo nitakapomwona au mpaka hapo nitakapo hakikisha ya kuwa amekufa; je, utafuatana nami?’

Nimekwisha sema kuwa mimi ni mtu wa taratibu , kweli na pengine ni mwoga kidogo, na haya yalinitia hofu. Maana safari kama hiyo iliyokusudiwa nilibaini kuwa ni kufa tu. Na tena juu ya hivyo nina mtoto anaenitegemea mimi kwa hivi sipendi nife. Basi nilijibu, ‘Hapana bwana, ahsante sana lakini naona ni afadhali nisiende. Sasa mimi ni mzee siwezi kusafiri safari ya kubahatisha hivyo, na tena naona mwisho wetu utakuwa kama ule wa rafiki yetu Silvestre. Mtoto wangu ananitegemea mimi, basi kwa hivyo sina haki ya kujitia katika hatari.’

Basi hapo wote wawili, yaani Bwana Henry na Bwana Good wakahuzunika sana, na Bwana Henry alisema, ‘Bwana Quatermain, mimi ni tajiri sana, nami nimenuia kusafiri ili nimtafute ndugu yangu, na kadhalika waweza kutaja mshahara wowote uutakao nami nitakupa kabla ya kuanza safari. Tena nitausia kuwa tukipatikana na ajali, mtoto wako atazamwe. Mradi sasa naona kwa maneno hayo utaweza kutambua jinsi tunavyo kuhitaji wewe ufuatane pamoja nasi. Tena ikiwa kwa bahati tutavumbua mahali pale palipo na almasi, basi hizo zitakuwa shirika wewe na Bwana Good, mimi sizitaki. Vile vile ikiwa tutapata pembe za ndovu. Waweza kutoa shauri na kufanya mapatano yoyote yanayokupendeza, na tena gharama zote za safari ni juu yangu mwenyewe.’ Nikajibu, ‘Bwana Henry, maneno yako ni mema kweli kweli, lakini lazima niyafikiri kwanza, maana mimi sina mali nyingi, pili kwa sababu najua kuwa ni kazi kubwa sana, basi nipe nafasi nipate kuyafikiri zaidi. Nitakupa jibu kabla hatujafika Durban.’ Bwana Henry akasema, ‘Vema.’ Nikamwambia kwa heri, nikaenda kulala, na nilipolala nilimwota Yule marehemu Silvestre na almasi!

Itaendelea...
 
UTANGULIZI
Hadithi hii ilipigwa chapa kwa lugha ya Kiingereza katika mwaka 1885. Katika mwaka 1905 Bwana H. Rider Haggard aliandika maneno haya: 'Sasa katika mwaka 1905 naweza kuzidisha maneno yangu kwa kusema ya kuwa nimefurahishwa sana kuona hadithi yangu inadumu kuwapendeza wasomaji wengi. Hayo yaliyobuniwa yamedhibitishwa kuwa ni kweli: Mashimo ya Malme Sulemani niliyokuwa nikiyafikiri sasa yamegunduliwa nayo sasa yanatoa dhahabu tena, na kwa habari zilizotoka hivi karibuni hata almasi pia hutoka.'

MASHIMO YA MFALME SULEIMAN​

SURA YA KWANZA​

Kukutana na Bwana Henry Curtis​

Ni ajabu sana kwa mtu aliyefika umri wangu, yaani miaka hamsini na tano, kushika kalamu na kuanza kuandika kitabu, kama hivi ‘nifanyavyo mimi sasa. Sijui habari hizi zitakuwaje nikiisha kuzitunga, yaani nikijaliwa kufika mwisho wa safari yangu salama, maana ingawa nimefanya mambo mengi katika maisha yangu, lakini sijawahi kujaribu kuandika kitabu. Tokea utoto wangu nimeshughulika na kazi ya biashara na kuwinda, kupigana na kuchimba dhahabu, na tangu kupata utajiri huu nilionao ni miezi minane tu.



Sasa nina mali nyingi sana, hata jumla yake siijui, lakini nadhani nisingekubali kuvumilia tena hayo yote niliyoyavumilia katika miezi kumi na tano iliyopita hata kama ningejua kwa hakika kuwa nitatoka salama pamoja na mali nyingi pia. Mimi ni mtu mtaratibu, sipendi ghasia, na tena nimechoka kabisa kusafirisafiri na kupambana na mambo ya ajabu. Sijui kwa nini naandika kitabu hiki, maana uandishi si kazi yangu. Mimi si mwana chuoni ingawa napenda sana kusoma vitabu. Hebu kwanza nijaribu kuandika sababu zangu za kutunga kitabu hiki, ili muone kama kweli ninazo sababu.

Sababu ya kwanza ni kuwa Bwana Henry Curtis na Bwana Good wameniomba nikitunge. Sababu ya pili ni kuwa nimebaki hapa Durban kwa kuwa mguu wangu wa kushoto waniuma sana. Tangu nilipoumwa na simba ninapata maumivu, na hasa siku hizi yanazidi, hata siwezi kwenda vizuri. Nadhani haikosi meno ya simba yana sumu na kama sivyo majeraha yangeisha pona kabisa na yasinge rudi tena, na hasa ajabu ni kuwa yanarejea mwezi ule ule niliyong’atwa. Ni ajabu sana kuwa baada ya kuua simba sitini na tano na labda zaidi, Yule wa sitini na sita aliniuma mguu. Jambo hili limeharibu mipango yangu ya desturi yote, na kwa kuwa mimi ni mtu wa kufuata taratibu na mipango naona dhiki kabisa. Lakini hayo hayamo katika habari za kitabu hiki.

Sababu ya tatu ni kuwa nataka mwanangu Harry anaesoma katika chuo cha utabibu, awe na mazungumzo ya kumfurahisha na kumpendeza. Asifanye upumbavu. Kusomea utabibu si kazi rahisi, na kazi ya kuvumbua habari za mwili vile vile inachosha. Habari zilizomo katika kitabu hiki si kama zile zinazotokea kila siku, kwa hivyo labda zitamfurahisha kwa muda kidogo.

Sababu ya nne na ilivyo ya mwisho ni kuwa nataka kusimulia hadithi ya ajabu kupita zote ninazozijua. Labda itakuwa ajabu kweli kwa kuwa hapana mwanamke aliyetajwa katika hadithi hii, ila Foulata. Lakini ngoja kwanza! Nilitaka kumsahau Gagula, lakini sina hakika kama alikuwa mwanamke au shetani. Lakini kwa umri wake ulizidi miaka mia moja na kwa kuwa: haoleki, basi simhesabu kuwa mwanamke. Basi afadhali nijifunge kibwebwe. Kazi ni ngumu nami naona kama nimekwisha yavulia nguo maji. Lakini kama wasemavyo wajuzi, ‘Pole pole ndio mwendo,’ Basi sasa naanza.

‘Mimi Alan Quatermain, mzaliwa wa Durban, Natal, naapa na kusema …’Hii ndiyo namna nilivyoanza kusema mbele ya kadhi nilipokuwa natoa habari za kufa kwa Khiva na Ventvogel, lakini naona kuwa hii siyo namna ya kuanza kutunga kitabu. Basi, je, mimi ni muungwana? Muungwana ni nini? Sijui hakika. Maisha yangu yote nilikuwa nikifanya kazi ya biashara na kuwinda tu. Nimejaribu daima kuwa muungwana, basi wewe usomaye utanihukumu. Mungu ajua kuwa nimejaribu. Ama kweli katika maisha yangu nimeua watu wengi, lakini sikuu mtu bure wala sikuua mtu asiye na hatia, ila kwa kujilinda mwenyewe tu. Mwenyezi Mungu alitupa maisha, nadhani nia yake ni kwamba tujilinde, nami siku zote nimeshikilia hivyo ; natumaini kwamba hayo hayatanitia hatiani siku ya kuhukumiwa itakapowadia.

Lakini dunia ina ukali na maovu, na ingawa mimi ni mtu taratibu na mwoga kidogo nimeona mauaji mengi. Lakini naweza kusema kuwa sijaiba, ingawa mara moja nilimdanganya mtu mmoja nikachukua kundi la ng’ombe wake. Lakini yeye alikuwa amenifanyia mambo mabaya kabisa na hata hivyo, tangu siku ile ninajuta kwa vitendo vyangu nilivyovifanya.

Toka nilipokutana na Bwana Henry Curtis na Bwana Good mara ya kwanza, imepita miezi kumi na nane, na namna tulivyokutana ilikuwa hivi: Nilikwenda kupita Bamangwato ili kuwinda ndovu. Nikawa na bahati mbaya sana katika safari hiyo, na juu ya hayo nilishikwa na homa kali. Nilipopona nikasafiri mpaka kunakochimbwa almasi, nikauza pembe zangu zote nilizokuwa nazo pamoja na gari la ng’ombe, nikawapa ruhusa wawindaji wangu, na mimi mwenyewe nikapanda gari niende Captown. Baada ya kukaa Captown kwa muda wa jumaa moja niliona kuwa gharama za hoteli zinazidi sana, tena nilikuwa nimekwisha ona yote niliyoyataka kuyaona, basi nikanuia kurudi Natal kwa meli iitwayo Edinburg Castle inayotoka Ulaya.

Basi nikaenda kukata tiketi nikaingia melini, na jioni ile ile meli ikang’oa nanga tukasafiri. Katika abiria walioingia melini niliona wawili niliowatazama sana. Mmoja alikuwa mtu mwenye umri kadiri ya miaka thelathini, kifua kipana na mikono mirefu kushinda watu wote niliowahi kuwaona. Nywele zake zilikuwa za rangi ya kimanjano na alikuwa na ndevu nyingi za rangi ile ile, na macho yake yalikuwa ya rangi ya kijivujivu tena yameingia ndani. Wala nilikuwa sikupata kuona mtu mzuri kumpita yeye. Halafu nikajua kuwa huyu ni Bwana Henry Curtis. Yule mtu mwingine aliyekuwa akiongea na Bwana Henry alikuwa mfupi tena mnene, kisha mweusi kidogo, na sura yake ilikuwa haikufanana hata kidogo na ile ya Bwana Henry. Halafu nikajua kuwa anaitwa Bwana Good.

Basi jioni nilipokuwako sitahani nilisikia sauti, mara nikageuka kuangalia, nikaona kuwa ni Yule Bwana Good. Hata tulipokwenda chini kula chakula tulimkuta Bwana Henry amekwisha kaa mezani, na mara tukaanza kuongea habari za kuwinda na mambo mengineyo. Akaniuliza maswali mengineyo. Akaniuliza maswali mengi sana, nami nikamjibu kadiri nilivyoweza. Halafu yake tukaanza kuongea habari za ndovu, na mtu mmoja aliyekuwa karibu yetu akasema, ‘Ee bwana, kama ukitaka mtu hasa anayeweza kukwambia kweli habari za ndovu, ni mwindaji Quatermain.’ Bwana Henry Curtis aliposikia hivi, akashtuka na akasema kwa sauti ya upole, ‘Niwie radhi bwana, jina lako wewe ni Allan Quatermain?’ Nikamwambia, ‘Ndiye mimi.’

Tulipokwisha kula, tukawa tunatoka mezani, na Bwana Henry akanijia kunikaribisha niende chumbani kwake tukavute tumbako, nami nikakubali. Mradi tulikuwa watu watatu, na mara Bwana Henry Curtis akasema, ‘Bwana Quatermain, nadhani miaka miwili iliyopita ulipata kuwako mahali panapoitwa Bamangwato katika nchi ya Transvaal,sivyo? Kusikia hivyo nikaona ajabu sana yeye kujua habari za safari zangu. Nikamwambia, ‘Ndiyo nilikuwako’, Bwana Good akauliza, ‘Ulikuwa ukifanya biashara sivyo?’ Nikajibu, ‘Ndiyo, nilichukua gari la bidhaa nikapiga kambi nje ya mji, nikakaa huko mpaka nilipokwisha kuuza zote .’ Bwana Henry aliyekuwa amekaa katika kiti kukabili kiti changu, akaniuliza, ‘Ulipata kukutana na mtu mmoja jina lake Neville?’ Nikajibu, ‘Ndiyo, tulipiga kambi zetu karibu kwa muda wa siku kumi na nne, na baada ya miezi michache nikapokea barua kutoka kwa Mwana Sheria ya kuniuliza habari zake kama namjua alipo, nami nikapeleka majibu kueleza habari zake kama nilivyoweza.’

Bwana Henry akasema, ‘Najua, maana barua yako ililetwa kwangu. Ulisema kwamba mtu aitwaye Neville alitoka Bamangwato mwanzo wa mwezi wa Mei akasafiri kwa gari pamoja na watu wake na mwindaji mtu mweusi mmoja jina lake Jim, naye alisema kuwa anakwenda mpaka Inyati ambao ndio mji wa mwisho katika nchi ya Mtabele ; akifika hapo atauza gari lake aende kwa miguu. Kisha ulisema kuwa kweli aliuza gari lake kwa sababu uliliona tena baada ya miezi sita, na mtu uliyemwona nalo alikuwa ni Mreno mfanya biashara aliyekwambia kuwa amelinunua Inyati kwa mtu mweupe mmoja, ambaye jina lake amelisahau ila anafikiri kuwa yeye pamoja na boi wake amekwenda mwituni kuwinda.’ Nikajibu, ‘Hayo ni kweli.’ Basi tukanyamaza kidogo, kisha, Bwana Henry Curtis akasema, ‘Naona ya kuwa hujui vema habari hizo. Huwezi kukisia sababu zake za kusafiri kwenda kaskazini na mahali gani alipokwenda?’ Nikamjibu, ‘Nilisikia kidogo.’

Na kwa kuwa sikutaka kusema naye zaidi juu ya habari hizi nikanyamaza kimya. Bwana Henry na Bwana Good wakatazamana, kisha Bwana Good akatikisa kichwa kwa kumfanyia ishara Bwana Henry, akasema, ‘Bwana Quatermain nitakusimulia hadithi yangu, halafu unipe shauri na msaada wako. Yule wakili wangu aliyeniletea barua yako aliniambia kuwa wewe ni mtu wa heshima sana na watu wote wanakustahi, na kwa hiyo naweza kukuamini. Basi nikainamisha kichwa kwa haya kwa vile nilivyosifiwa na Bwana Henry akaendelea kusema, ‘Huyo Bwana Neville ni ndugu yangu.’ Niliposikia hivi nikastuka sana, maana sasa nalifahamu sababu ya kumtazama sana nilimwona mara ya kwanza, kwa kuwa wamefanana sana.

Basi Bwana Henry akaendelea kusema, ‘Yeye ni mdogo wangu, na mpaka miaka mitano iliopita nadhani hatukupata kuachana hata kwamuda wa mwezi mmoja. Lakini katika mwaka ule wa mwisho tulioonana tulipatwa na msiba kama wanavyopatwa watu wote mara kwa mara. Maana tuligombana sana hata nilimtenda mambo yasiyo ya haki kwa ajili ya hasira zangu. Haikosi unajua kuwa mtu akifa na kama mali yake ni mashamba tu, wala naye hakuacha wosia wowote, kwa sheria ya Uingereza mrithi huwa ni Yule mtoto mwanaume mkubwa, yaani aliyezaliwa kwanza, ndiye anayechukua mali yote. Basi hivyo ndivyo ilivyokuwa. Na wakati ule tulipokuwa tukigombana baba yetu alifariki naye hakuwahi kuandika wosia. Basi kwa hivyo ilionekana kuwa mdogo wangu hakuwa na urithi.

Kusema kweli ilikuwa ni wajibu wangu kumsaidia na kumtunza, lakini kwa ule uchungu wa ugomvi jinsi ulivyokuwa mwingi sana, hata sasa naona aibu kukiri kuwa sikufanya jambo. Sikuwa na nia ya kumnyima haki yake, ila nilitaka yeye aje kwangu’ kuomba suluhu, naye hakuja. Nasikitika sana kukuudhi kwa habari hizi zangu, lakini naona sina budi kukueleza waziwazi mambo yote, sivyo Bwana Good?’ Bwana Good akajibu, ‘Ndivyo, nami najua kwa hakika kuwa Bwana Quatermain atayasitiri yote moyoni mwake.’ Nikajibu, ‘Vema,’ Maana mimi natafakari sana kuwa si mtu wa kupayuka.

Halafu Bwana Henry akasema, ‘Mdogo wangu alikuwa na fedha kidogo na bila kunishauri alitoa fedha zote alizokuwa nazo katika banki, na kuchukua jina lingine la Neville, akafunga safari kwenda kuchuma Afrika ya Kusini. Nikakaa kwa muda wa miaka mitatu bila kupata habari zake wala salamu zake, ingawa mimi nilimwandikia barua nyingi. Labda zilikuwa hazimfikii. Lakini baadaye nikaanza kuwa na wasiwasi, maana mtu haachi kumpenda ndugu yake.’
Nikasema, ‘Hayo ni ya kweli. ‘Maana nilikuwa nikimkumbuka mtoto wangu. Bwana Henry akawa anaendelea kusema, ‘Nikahisi kuwa hata nusu ya mali yangu yote nitatoa ili nipate kujua yaliyompata mdogo wangu, maana ni mmoja tu aliyebaki katika ukoo wangu. Basi siku zilipozidi kupita nami nikazidi kuwa na wasiwasi, nikatamani sana kupata habari zake. Ndipo nikaanza kuulizauliza, hata nikapata ile barua. Basi mpaka sasa habari ni nzuri, maana zaonyesha kuwa yu hai mpaka sasa. Na nilitia nia kwenda mwenyewe kumtafuta, na Bwana Good amenifurahisha sana kwa kufuatana nami.’ Basi Bwana Good akasema, ‘Ndiyo na sasa Bwana, labda utatwambia habari zote ujuazo za Yule mtu aitwaye Neville.’

SURA YA PILI

Basi kabla sijaanza kumjibu Bwana Good, nilitia tumbako katika kiko changu, na Bwana Henry akauliza, ‘ Ulisikia habari gani juu ya safari ya ndugu yangu ulipokuwako Bamangwato?’ Nikamjibu, ‘Nalisikia hivi, ya kuwa anakwenda kutafuta Mashimo ya Sulemani. Na tangu siku hiyo hata hivi leo, sijamwambia mtu habari hizo.’ Wote wawili wakauliza pamoja, ‘Mashimo ya Sulemani! Yapo wapi?’ Nikajibu, ‘Mimi sijui, lakini najua mahali ambapo watu husema kuwa yapo. Siku moja niliona vilele vya milima inayopakana nayo, lakini baina ya mahali hapo nilipokuwa mimi na milima hiyo palikuwa na jangwa la upana wa maili mia moja na thelathini, nami sijapata kusikia kuwa Mzungu yeyote amepata kuvuka jangwa hilo, isipokuwa mtu mmoja tu.



Lakini nadhani itakuwa vizuri zaidi nikisimulia habari hizo, yaani kama nilivyopokea kutoka kwa wenyeji, za Mashimo ya Sulemani kwa kadiri ninavyojua, ikiwa mtaahidi kuwa mtazisitiri mioyoni mwenu na kutomwambia mtu yeyote bila ya idhini yangu. Je, mtakubali sharti hilo?’ Bwana Henry akainamisha kichwa, na Bwana Good akaitikia, ‘Naam, naam.’ Basi, nikaanza kutoa hadithi yangu: ‘Kwa kawaida mwajua kuwa wawindaji wa ndovu ni watu wasiotamani anasa za dunia, wala hawashughuliki na mambo ila ya kweli ya dunia. Lakini pengine mwaweza kumkuta mtu mmoja mmoja anajitia katika mambo ya kuandika hadithi na kujaribu kutunga habari za zamani za watu wa kale. aliyeniambia maneno haya alikuwa ni mtu wa namna hiyo, na tangu aliponiambia maneno haya umepita muda wa miaka thelathini. Ilikuwa hivi: katika safari yangu ya kwanza nilikwenda kuwinda ndovukatika nchi ya Matabele. Mtu mmoja aliyeitwa Evans ndiye aliyeniambia maneno hayo, naye masikini aliuawana nyati mwaka wa pili yake, akazikwa mahali palipokuwa karibu na maporomoko ya maji yam to wa Zambezi. Nami nakumbuka sana kuwa siku moja nilikuwa nikizungumzia habari za kulungu na pofu katika mtaa mmoja wa Transvaal.’

Evans akasema, ‘Ndiyo, lakini mimi nitakutolea hadithi iliyo ya ajabu zaidi kupita habari za wanyama.’ Akaendelea kuhadithia jinsi alivyopata kuvumbua magofu ya mji wa zamani sana ambao aliamini kuwa ni mji ule uliokuwa ukiitwa Ophir uliotajwa katika Agano la Kale,na tangu siku hizo, watu wengi wenye maarifa kuliko yeye marehemu Evans wamesema hivyohivyo. Mimi nikakaa kusikiliza sana, maana wakati ule mimi nilikuwa bado kijana, na hadithi zile za kale zilinipendeza sana, na mara akasema, ‘je, mwanangu, umepata kusikia habari za milima ya Sulemani iliyo upande wa kaskazini wa nchi ya Mashukulumbwe?’’ , Nikamwambia, ‘Sijapata kusikia .’Akasema, ‘Basi, haidhuru, hapo ndipo mashimo ya Sulemani yalipo, yaani mashimo ya almasi.’ Nikamuuliza, ‘Je, wewe umejuaje?’ Akajibu, ‘Najuaje! Najua kwa jina lake lilivyo, na tena niliambiwa na mwanamke mmoja mchawi wa kabila la Isanusi katika nchi ya Manika. Alisema kwamba watu wanaokaa upande wa pili wa milima ile ni wa ukoo wa Amazulu, wanasema lugha inayofanana na Kizulu, ila wao ni wakubwa, tena wazuri zaidi ya Amazulu. Lakini kuna wachawi wenye nguvu nyingi wanaokaa humo na walikuwa na siri ya shimo la ajabu lenye mawe yale yanayong’aa.’ Nilicheka sana niliposikia hadithi hii, nikaipuuza, lakini ilinipendeza sana, maana wakati ule mashimo ya almasi yalikuwa bado hayajavumbuliwa. Lakini Yule marehemu Evans aliuawa, nami nikakaa muda wa miaka ishirini bila kufikiri tena jambo hili.

Baada ya miaka ishirini, na huo ni muda mrefu sana, maana mwindaji wa ndovu ana shida kuishi miaka ishirini katika kazi yake, nikasikia habari zaidi juu ya milima ya Sulemani na nchi iliyo upande wa pili yake. Hapo mimi nilikuwa katika nchi ya Manika, mahali paitwapo KwaSitanda, napo ni mahali pabaya sana, maana sikuweza kupata chakula wala wanyama hakuna. Nilishikwa na homa kali mno hata hali yangu ikawa dhaifu sana, na siku moja akafika Mreno mmoja pamoja na mwenziwe mmoja suriama. Tukaongea kidogo pamoja, maana yeye aliweza kusema Kiingereza kidogo, nami pia nilijua kusema Kireno kidogo, akaniambia kuwa jina lake ni Jose Silvestre, na tena ana shamba karibu na Delagoa Bay. Lakini siku ya pili yake aliondoka pamoja na mwenziwe. Katika kuniaga akasema ‘Bwana, tukionana tena natumai mimi nitakuwa tajiri kuliko watu wote duniani, nami nitakukumbuka.’ Nikacheka kidogo, maana nilikuwa mnyonge kwa homa na kwa hivyo sikuweza kucheka sana; nikamwona akienda kuvuka lile jangwa kwenda upande wa magharibi. Nikadhani kuwa ana wazimu, kwani anakwenda kutafuta nini huko? Baada ya juma moja, nikapona, na jioni nilipokuwa nimekaa nje ya hema langu dogo, nikitafuna paja la kuku wa mwisho niliyemnunua kwa mtu mmoja kwa bei ya kitambaa kimoja kilichonipatia kuku ishirini, nikitazama jua jinsi lilivyokuwa jekundu linavyoshuka nyuma ya jangwa hilo, mara nikaona kitu kama mzungu amevaa koti akiteremka mteremko uliokuwako kiasi hatua mia sita, mbele yangu.

Kwanza mtu huyo alitambaa kwa magoti na mikono, kisha akasimama na kupepesuka hatua chache mbele, tena akaanguka na kutambaa. Mradi nikaona kuwa ni mtu aliye taabani. Nikapeleka mmoja wa wawindaji wangu kwenda kumsaidia, na baadae kidogo akaja nae. Je, wadhani alikuwa ni nani? Alikuwa ni Yule Jose Silvetre, kwa kweli, mifupa yake ilikuwa dhaifu, tena alikuwa amekonda kabisa. Uso wake ulikuwa manjano, uking’aa kwa homa aliyokuwa nayo, nayale macho yake meusi makubwa yalionekana kama yaliyotokeza nje, maana alikuwa hana nyama kabisa .. Ngozi yake ilikuwa imekauka, na nywele zake zilikuwa zimegeuka rangi zikawa nyeupe, na mifupa imemtoka. Akawa anaugua huku akisema, ‘Nipeni maji! Jamani.

Nikaona kuwa midomo yake imepasuka na ulimi ulikuwa mweusi tena umevimba. Nikampa maji yaliyochanganyika na maziwa kidogo, akayabugia. Nikamzuia kusudi asinywe zaidi. Na mara homa ilimshika tena na kuanza kupayuka na kusema habari za milima ya Sulemani, na almasi na jangwa. Nikamchukua na kumweka hemani mwangu nikamtunza kama nilivyoweza; lakini nilijua kuwa atakufa. Kama saa tano ya usiku akatulia kidogo, nami ndipo nilipopata usingizi kidogo, nikalala. Kulipopambazuka nikaamka, nikamwona namna alivyokuwa amekonda sana amekaa na kulikodolea jangwa macho. Baadae kile kianga cha kwanza chajua kilionekana mawinguni, kikaangaza jangwa mpaka kufika kilele kirefu katika milima ya Sulemani, masafa ya maili mia moja na zaidi. Mara Yule mgonjwa akanyosha mkono wake mwembamba kuelekeza kileleni na huku akisema kwa Kireno, ‘Ndipo, ndipo papo hapo, lakini mimi sitawahi kupafikia kamwe. Wala hapana atakayepafikia kwamwe!’ Mara akakaa kimya kidogo kama mtu anayewaza jambo moyoni, halafu akanigeukia akasema, ‘Rafiki bado ungalipo? Ama sasa naona macho yangu yanaingia giza,’ Nikajibu, ‘Ndiyo, nipo hapa hapa.

Lakini sasa afadhali ulale upumzike.’ Akasema, ‘Ndiyo nitapumzika sasa hivi; tena nitakuwa na wasaa mwingi wa kupumzika, hata milele. Nisikilize, ninakufa! Wewe umenitendea mema. Nitakupa hati. Labda utaweza kupafikia ikiwa utaishi na kuvuka jangwa ambalo limemuua mtumishi wangu na mimi!’

Akapapasapapasa katika mfuko wake akatoa kitu nilichokidhania kuwa kikoba cha kuwekea tumbako kilichofanywa kwa ngozi ya mnyama. Kikoba hicho kilifungwa kwa uzi wa ngozi naye alijaribu kukifungua asiweze. Akanipa akisema, ‘Fungua.’Nikakifungua nikatoa kipande cha kitambaa kikuukuu cha katani kilichokuwa kimeandikwa maneno, na ndani ya kitambaa hicho mlikuwamo karatasi. Kisha akasema kwa sauti ya kufifia, maana alizidi kudhofu, akanena, ‘Juu ya hiyo karatasi kumeandikwa yote yaliyoshindikwa juu ya kitambaa na hivyo ilinibidi kufanya kazi miaka hata kuweza kuisoma. Sikiliza: Babu yangu ambaye ilimlazimu kuutoka mji wa Lisbon alikuwa katika Wareno hao wa kwanza waliofika katika nchi hii.

Aliandika maneno hayo wakati alipokuwa akifa katika milima ile ambayo hapana hata Mzungu mmoja aliyepata kuikanyaga kwa miguu yake mpaka hivi leo. Jina lake lilikuwa Jose da Silvestre, naye aliishi miaka mia tatu, nyuma. Mtumishi wake aliyekuwa akimngojea upande huu wa milima aliona kuwa amekwisha kufa, nae ndiye aliyeleta maandishi haya mpaka Delagoa. Na tokea wakati huo yametunzwa na warithi wake, lakini hapana aliyetaka kuyasoma, mpaka mimi nilipofaulu. Nami nimepoteza maisha yangu kwa ajili yake, lakini labda mtu mwingine ataweza kufaulu na kuwa tajiri kupita watu wote duniani. Lakini usimpe mtu mwingine bwana, wewe nenda mwenyewe!’ Akaanza kuugua tena, na baada ya saa moja akafa. Mungu amrehemu. Nilimzika katika kaburi la kwenda chini sana, nikaweka na mawe makubwa juu ili kusudi asifukuliwe na fisi. Kisha nikaondoka pale.

Bwana Henry akauliza, na sauti yake ilionyesha jinsi alivyokuwa akisikiliza maneno yangu, ‘Ehe, lakini hiyo hati iko wapi? Naye Bwana Good akaongeza, ‘Hati hiyo iko wapi sasa, iliandikwa habari gani?’ Nikasema, ‘Mkitaka nitawasimulia habari zake. Nami sijamwonyesha hata mtu mmoja ila Mreno mmoja mfanya biashara aliyekuwa amelewa wakati alipoitafsiri, tena hakosi’ kuwa alikuwa amekwisha sahau habari zake ulevi ulipomtoka. Hicho kitambaa chenyewe nimekiweka kwangu Durban pamoja na hiyo karatasi aliyoifasiri marehemu Jose, lakini hapa ninayo tafsiri ya Kiingereza na nakala ya ramani iliyokuwamo, nayo ni hii:’

Mimi Jose da Silvestre nipo hapa ninakufa kwa njaa ndani, ya pango dogo katika upande wa kaskazini mwa titi la mlima ulio upande wa kusini wa milima miwili ambayo nimeipa jina la Maziwa ya Sheba. Naandika haya kwa kipande cha mfupa na wino wa damu yangu mwenyewe katika mwaka 1590. Ikiwa mtumishi wangu atakuja na kuiona na kuichukua mpaka Delagoa, nataka rafiki yangu (Na hapo katika hati, jina lake limefutika.) ampashe habari mfalme ili alete jeshi la askari watakaoweza kuvuka jangwa hili na kuwashinda hawa Wakukuana walio majabali sana na wenye uchawi mwingi. Lakini kwa sababu ya hila na udanganyifu wa Mchawi Gagula sikuweza kuleta kitu cha ushahidi, tena hata maisha yangu nayo nimeyaokoa kwa shida nyingi. Na huyu atakayekuja na afuate ramani, apande theluji ya ziwa la kushoto la Sheba mpaka afike penye titi, ambapo kwa upande huo wa kaskazini pana njia kuu iliyotengenezwa na Sulemani. Kutoka hapo ni mwendo wa siku tatu kufikia jumba la Mlalme. Basi na amwue Gagula. Nawe niombe dua.

Kwaheri. Jose da Silvestre.

Nilipokwisha soma barua na kuonyesha ile nakala ya ramani iliyoandikwa na Yule mzee kwa damu ya mkono wake, wakanyamaza kimya kwa ajili ya kustaajabu kwao. Baadae Bwana Good akasema, ‘Lo! Nimezunguka dunia mara mbili, tena nimefika bandari nyingi lakini sijapata kusikia hadithi kama hii hata vitabuni.’ Bwana Henry akasema, ‘Ni hadithi ya ajabu Bwana Quatermain. Natumai unajaribu kutuhadaa! Najua kwamba watu hudhani kuwa si vibaya kumhadaa mjinga.’ Niliposikia hivi nikaudhika, nikatwaa karatasi nikaiweka mfukoni, maana sikupenda kudhaniwa kuwa ni mmoja wa wale wapendao kusimulia uwongo na kuwahadithia wageni habari za kuwinda na mambo mengine ambayo hayakutokea kamwe. Basi nikajibu, ‘Kama unafikiri hivyo basi mambo yaishe hapa hapa. Nikasimama nikataka kwenda zangu. Bwana Henry akaniwekea mkono wake begani pangu akasema, ‘ Kaa, Bwana Quatermain, niwie radhi, usiudhike; kwani naona kuwa hupendi kutuhadaa, lakini hadithi yenyewe ni ya ajabu mno hata kwanza niliona vigumu kuisadiki.’

Basi ndipo nilipoanza kutulia kidogo, maana nilipofikiri niliona kuwa si ajabu kuwa yeye hawezi kusadiki hadithi, nikamwambia, Tutakapojaliwa kufika Durban utaona ramani ya asili na maandishi yake. Lakini bado sijakwambia habari za ndugu yako. Nilimjua Yule Jim aliyekuwa pamoja naye. Yeye ni Mbechuana, mwindaji hodari, tena na mtu mwenye busara. Siku hiyo Bwana Neville alipoanza safari yake nilimwona Jim amesimama karibu na gari langu akisokota tumbako yake, nikasema, ‘Jim, safari hii unakwenda wapi? Kuwinda ndovu?’ Akajibu ‘La! Tunakwenda kutafuta kitu kinachotafutwa sana zaidi ya pembe za ndovu.’ Mimi nikazidi kumdadisi, nikamuuliza, ‘Je, kitu hicho chaweza kuwa nini? Ni dhahabu? Akacheka akajibu, ‘siyo Bwana, ni kitu kinachotakiwa zaidi ya dhahabu.’

Basi sikumuuliza neno tena, maana sikupenda kuonekana kuwa ni mdaku. Baada ya Jim kuisha kusokota tumbako yake, akasema ‘Bwana, sisi tunakwenda kutafuta almasi.’ Nikasema, ‘Almasi! Lakini mbona unafuata njia ambayo si njia ya kwendea huko; kwa nini hufuati njia inayoendelea kwenye mashimo?’ Akajibu, ‘ Bwana, umepata kusikia habari za mlima wa Sulemani?’ Nikamjibu, ‘Ndiyo.’ Akaniuliza, ‘Umesikia habari za almasi zilizoko huko?’ Nikwamwambia, ‘Ni upuuzi tu.’ Akanena, ‘Si upuuzi,? Wana maana, namjua mwanamke aliyetoka huko, naye alifika Natal pamoja na mtoto wake, akaniambia; lakiniamekufa sasa.’

Nikamjibu, ‘Wewe na bwana wako mkijaribu kufika nchi ya Sulemani, hamkosi mtaliwa na tai.’ Akacheka, akasema, ‘Labda, bwana . Mtu amezaliwa naye atakufa; nami ningependa kutembea katika nchi ngeni; maana ndovu wanakwisha katika nchi hii.’ Nikasema, ‘Haya, tutaona.’ Baada ya nusu saa nikaona gari la Neville likitoka. Na baadae kidogo Jim akarudi mbio akasema, ‘Kwaheri bwana, kwani sikupenda kuanza safari bila kuagana nawe. Ninaona labda umesema kweli ya kuwa hatutasafiri kwenda kusini tena.’ Nikamuuliza, ‘Je, Jim, wasema kweli? Bwana wako amesema kuwa anakwenda mlima wa Sulemani, au sivyo?’ Akasema, ‘Ni kweli bwana maana aliniambia kuwa imempasa ajaribu kuchuma mali kwa njia yoyote; basi ni afadhali ajaribu kutafuta hiyo almasi.’ Nikasema, ‘Vema Jim, lakini ngoja kwanza, nataka uchukue barua hii, lakini lazima uahidi kuwa hutampa mpaka nifike Inyati.’ Kufika Inyati ilikuwa ni mwendo wa maili kama mia. Basi akaahidi. Nami nikachukua karatasi nikaandika maneno haya: ‘Kwa huyo atakayekuja ..apande theluji ya ziwa la kushoto la Sheba mpaka afike penye titi, ambapo kwa upande huo wa kaskazini pana njia kuu iliyotengenezwa na Sulemani.’

Basi nikampa, kisha nikamwambia, ‘Sasa utakapompa bwana wako barua hii, mwambie afuate sana shauri lililomo. Wala usimpe sasa barua hii kwa sababu sipendi arudi kuja kuniuliza maswali mengi ambayo sitaweza kuyajibu. Haya nenda.’ Basi Jim akaitwaa barua akaenda zake. Na hayo ndiyo yote ninayoyajua juu ya ndugu yako, Bwana Henry; lakini nachelea sana ya kuwa.. ‘Bwana Henry akasema, ‘Tazama, Bwana Quatermain, mimi ninakwenda kumtafuta ndugu yangu; nitamtafuta hata mlima wa Sulemani, hata nitaupita ikiwa ni lazima, mpaka hapo nitakapomwona au mpaka hapo nitakapo hakikisha ya kuwa amekufa; je, utafuatana nami?’

Nimekwisha sema kuwa mimi ni mtu wa taratibu , kweli na pengine ni mwoga kidogo, na haya yalinitia hofu. Maana safari kama hiyo iliyokusudiwa nilibaini kuwa ni kufa tu. Na tena juu ya hivyo nina mtoto anaenitegemea mimi kwa hivi sipendi nife. Basi nilijibu, ‘Hapana bwana, ahsante sana lakini naona ni afadhali nisiende. Sasa mimi ni mzee siwezi kusafiri safari ya kubahatisha hivyo, na tena naona mwisho wetu utakuwa kama ule wa rafiki yetu Silvestre. Mtoto wangu ananitegemea mimi, basi kwa hivyo sina haki ya kujitia katika hatari.’

Basi hapo wote wawili, yaani Bwana Henry na Bwana Good wakahuzunika sana, na Bwana Henry alisema, ‘Bwana Quatermain, mimi ni tajiri sana, nami nimenuia kusafiri ili nimtafute ndugu yangu, na kadhalika waweza kutaja mshahara wowote uutakao nami nitakupa kabla ya kuanza safari. Tena nitausia kuwa tukipatikana na ajali, mtoto wako atazamwe. Mradi sasa naona kwa maneno hayo utaweza kutambua jinsi tunavyo kuhitaji wewe ufuatane pamoja nasi. Tena ikiwa kwa bahati tutavumbua mahali pale palipo na almasi, basi hizo zitakuwa shirika wewe na Bwana Good, mimi sizitaki. Vile vile ikiwa tutapata pembe za ndovu. Waweza kutoa shauri na kufanya mapatano yoyote yanayokupendeza, na tena gharama zote za safari ni juu yangu mwenyewe.’ Nikajibu, ‘Bwana Henry, maneno yako ni mema kweli kweli, lakini lazima niyafikiri kwanza, maana mimi sina mali nyingi, pili kwa sababu najua kuwa ni kazi kubwa sana, basi nipe nafasi nipate kuyafikiri zaidi. Nitakupa jibu kabla hatujafika Durban.’ Bwana Henry akasema, ‘Vema.’ Nikamwambia kwa heri, nikaenda kulala, na nilipolala nilimwota Yule marehemu Silvestre na almasi!

Itaendelea...
UTANGULIZI
Hadithi hii ilipigwa chapa kwa lugha ya Kiingereza katika mwaka 1885. Katika mwaka 1905 Bwana H. Rider Haggard aliandika maneno haya: 'Sasa katika mwaka 1905 naweza kuzidisha maneno yangu kwa kusema ya kuwa nimefurahishwa sana kuona hadithi yangu inadumu kuwapendeza wasomaji wengi. Hayo yaliyobuniwa yamedhibitishwa kuwa ni kweli: Mashimo ya Malme Sulemani niliyokuwa nikiyafikiri sasa yamegunduliwa nayo sasa yanatoa dhahabu tena, na kwa habari zilizotoka hivi karibuni hata almasi pia hutoka.'

MASHIMO YA MFALME SULEIMAN​

SURA YA KWANZA​

Kukutana na Bwana Henry Curtis​

Ni ajabu sana kwa mtu aliyefika umri wangu, yaani miaka hamsini na tano, kushika kalamu na kuanza kuandika kitabu, kama hivi ‘nifanyavyo mimi sasa. Sijui habari hizi zitakuwaje nikiisha kuzitunga, yaani nikijaliwa kufika mwisho wa safari yangu salama, maana ingawa nimefanya mambo mengi katika maisha yangu, lakini sijawahi kujaribu kuandika kitabu. Tokea utoto wangu nimeshughulika na kazi ya biashara na kuwinda, kupigana na kuchimba dhahabu, na tangu kupata utajiri huu nilionao ni miezi minane tu.



Sasa nina mali nyingi sana, hata jumla yake siijui, lakini nadhani nisingekubali kuvumilia tena hayo yote niliyoyavumilia katika miezi kumi na tano iliyopita hata kama ningejua kwa hakika kuwa nitatoka salama pamoja na mali nyingi pia. Mimi ni mtu mtaratibu, sipendi ghasia, na tena nimechoka kabisa kusafirisafiri na kupambana na mambo ya ajabu. Sijui kwa nini naandika kitabu hiki, maana uandishi si kazi yangu. Mimi si mwana chuoni ingawa napenda sana kusoma vitabu. Hebu kwanza nijaribu kuandika sababu zangu za kutunga kitabu hiki, ili muone kama kweli ninazo sababu.

Sababu ya kwanza ni kuwa Bwana Henry Curtis na Bwana Good wameniomba nikitunge. Sababu ya pili ni kuwa nimebaki hapa Durban kwa kuwa mguu wangu wa kushoto waniuma sana. Tangu nilipoumwa na simba ninapata maumivu, na hasa siku hizi yanazidi, hata siwezi kwenda vizuri. Nadhani haikosi meno ya simba yana sumu na kama sivyo majeraha yangeisha pona kabisa na yasinge rudi tena, na hasa ajabu ni kuwa yanarejea mwezi ule ule niliyong’atwa. Ni ajabu sana kuwa baada ya kuua simba sitini na tano na labda zaidi, Yule wa sitini na sita aliniuma mguu. Jambo hili limeharibu mipango yangu ya desturi yote, na kwa kuwa mimi ni mtu wa kufuata taratibu na mipango naona dhiki kabisa. Lakini hayo hayamo katika habari za kitabu hiki.

Sababu ya tatu ni kuwa nataka mwanangu Harry anaesoma katika chuo cha utabibu, awe na mazungumzo ya kumfurahisha na kumpendeza. Asifanye upumbavu. Kusomea utabibu si kazi rahisi, na kazi ya kuvumbua habari za mwili vile vile inachosha. Habari zilizomo katika kitabu hiki si kama zile zinazotokea kila siku, kwa hivyo labda zitamfurahisha kwa muda kidogo.

Sababu ya nne na ilivyo ya mwisho ni kuwa nataka kusimulia hadithi ya ajabu kupita zote ninazozijua. Labda itakuwa ajabu kweli kwa kuwa hapana mwanamke aliyetajwa katika hadithi hii, ila Foulata. Lakini ngoja kwanza! Nilitaka kumsahau Gagula, lakini sina hakika kama alikuwa mwanamke au shetani. Lakini kwa umri wake ulizidi miaka mia moja na kwa kuwa: haoleki, basi simhesabu kuwa mwanamke. Basi afadhali nijifunge kibwebwe. Kazi ni ngumu nami naona kama nimekwisha yavulia nguo maji. Lakini kama wasemavyo wajuzi, ‘Pole pole ndio mwendo,’ Basi sasa naanza.

‘Mimi Alan Quatermain, mzaliwa wa Durban, Natal, naapa na kusema …’Hii ndiyo namna nilivyoanza kusema mbele ya kadhi nilipokuwa natoa habari za kufa kwa Khiva na Ventvogel, lakini naona kuwa hii siyo namna ya kuanza kutunga kitabu. Basi, je, mimi ni muungwana? Muungwana ni nini? Sijui hakika. Maisha yangu yote nilikuwa nikifanya kazi ya biashara na kuwinda tu. Nimejaribu daima kuwa muungwana, basi wewe usomaye utanihukumu. Mungu ajua kuwa nimejaribu. Ama kweli katika maisha yangu nimeua watu wengi, lakini sikuu mtu bure wala sikuua mtu asiye na hatia, ila kwa kujilinda mwenyewe tu. Mwenyezi Mungu alitupa maisha, nadhani nia yake ni kwamba tujilinde, nami siku zote nimeshikilia hivyo ; natumaini kwamba hayo hayatanitia hatiani siku ya kuhukumiwa itakapowadia.

Lakini dunia ina ukali na maovu, na ingawa mimi ni mtu taratibu na mwoga kidogo nimeona mauaji mengi. Lakini naweza kusema kuwa sijaiba, ingawa mara moja nilimdanganya mtu mmoja nikachukua kundi la ng’ombe wake. Lakini yeye alikuwa amenifanyia mambo mabaya kabisa na hata hivyo, tangu siku ile ninajuta kwa vitendo vyangu nilivyovifanya.

Toka nilipokutana na Bwana Henry Curtis na Bwana Good mara ya kwanza, imepita miezi kumi na nane, na namna tulivyokutana ilikuwa hivi: Nilikwenda kupita Bamangwato ili kuwinda ndovu. Nikawa na bahati mbaya sana katika safari hiyo, na juu ya hayo nilishikwa na homa kali. Nilipopona nikasafiri mpaka kunakochimbwa almasi, nikauza pembe zangu zote nilizokuwa nazo pamoja na gari la ng’ombe, nikawapa ruhusa wawindaji wangu, na mimi mwenyewe nikapanda gari niende Captown. Baada ya kukaa Captown kwa muda wa jumaa moja niliona kuwa gharama za hoteli zinazidi sana, tena nilikuwa nimekwisha ona yote niliyoyataka kuyaona, basi nikanuia kurudi Natal kwa meli iitwayo Edinburg Castle inayotoka Ulaya.

Basi nikaenda kukata tiketi nikaingia melini, na jioni ile ile meli ikang’oa nanga tukasafiri. Katika abiria walioingia melini niliona wawili niliowatazama sana. Mmoja alikuwa mtu mwenye umri kadiri ya miaka thelathini, kifua kipana na mikono mirefu kushinda watu wote niliowahi kuwaona. Nywele zake zilikuwa za rangi ya kimanjano na alikuwa na ndevu nyingi za rangi ile ile, na macho yake yalikuwa ya rangi ya kijivujivu tena yameingia ndani. Wala nilikuwa sikupata kuona mtu mzuri kumpita yeye. Halafu nikajua kuwa huyu ni Bwana Henry Curtis. Yule mtu mwingine aliyekuwa akiongea na Bwana Henry alikuwa mfupi tena mnene, kisha mweusi kidogo, na sura yake ilikuwa haikufanana hata kidogo na ile ya Bwana Henry. Halafu nikajua kuwa anaitwa Bwana Good.

Basi jioni nilipokuwako sitahani nilisikia sauti, mara nikageuka kuangalia, nikaona kuwa ni Yule Bwana Good. Hata tulipokwenda chini kula chakula tulimkuta Bwana Henry amekwisha kaa mezani, na mara tukaanza kuongea habari za kuwinda na mambo mengineyo. Akaniuliza maswali mengineyo. Akaniuliza maswali mengi sana, nami nikamjibu kadiri nilivyoweza. Halafu yake tukaanza kuongea habari za ndovu, na mtu mmoja aliyekuwa karibu yetu akasema, ‘Ee bwana, kama ukitaka mtu hasa anayeweza kukwambia kweli habari za ndovu, ni mwindaji Quatermain.’ Bwana Henry Curtis aliposikia hivi, akashtuka na akasema kwa sauti ya upole, ‘Niwie radhi bwana, jina lako wewe ni Allan Quatermain?’ Nikamwambia, ‘Ndiye mimi.’

Tulipokwisha kula, tukawa tunatoka mezani, na Bwana Henry akanijia kunikaribisha niende chumbani kwake tukavute tumbako, nami nikakubali. Mradi tulikuwa watu watatu, na mara Bwana Henry Curtis akasema, ‘Bwana Quatermain, nadhani miaka miwili iliyopita ulipata kuwako mahali panapoitwa Bamangwato katika nchi ya Transvaal,sivyo? Kusikia hivyo nikaona ajabu sana yeye kujua habari za safari zangu. Nikamwambia, ‘Ndiyo nilikuwako’, Bwana Good akauliza, ‘Ulikuwa ukifanya biashara sivyo?’ Nikajibu, ‘Ndiyo, nilichukua gari la bidhaa nikapiga kambi nje ya mji, nikakaa huko mpaka nilipokwisha kuuza zote .’ Bwana Henry aliyekuwa amekaa katika kiti kukabili kiti changu, akaniuliza, ‘Ulipata kukutana na mtu mmoja jina lake Neville?’ Nikajibu, ‘Ndiyo, tulipiga kambi zetu karibu kwa muda wa siku kumi na nne, na baada ya miezi michache nikapokea barua kutoka kwa Mwana Sheria ya kuniuliza habari zake kama namjua alipo, nami nikapeleka majibu kueleza habari zake kama nilivyoweza.’

Bwana Henry akasema, ‘Najua, maana barua yako ililetwa kwangu. Ulisema kwamba mtu aitwaye Neville alitoka Bamangwato mwanzo wa mwezi wa Mei akasafiri kwa gari pamoja na watu wake na mwindaji mtu mweusi mmoja jina lake Jim, naye alisema kuwa anakwenda mpaka Inyati ambao ndio mji wa mwisho katika nchi ya Mtabele ; akifika hapo atauza gari lake aende kwa miguu. Kisha ulisema kuwa kweli aliuza gari lake kwa sababu uliliona tena baada ya miezi sita, na mtu uliyemwona nalo alikuwa ni Mreno mfanya biashara aliyekwambia kuwa amelinunua Inyati kwa mtu mweupe mmoja, ambaye jina lake amelisahau ila anafikiri kuwa yeye pamoja na boi wake amekwenda mwituni kuwinda.’ Nikajibu, ‘Hayo ni kweli.’ Basi tukanyamaza kidogo, kisha, Bwana Henry Curtis akasema, ‘Naona ya kuwa hujui vema habari hizo. Huwezi kukisia sababu zake za kusafiri kwenda kaskazini na mahali gani alipokwenda?’ Nikamjibu, ‘Nilisikia kidogo.’

Na kwa kuwa sikutaka kusema naye zaidi juu ya habari hizi nikanyamaza kimya. Bwana Henry na Bwana Good wakatazamana, kisha Bwana Good akatikisa kichwa kwa kumfanyia ishara Bwana Henry, akasema, ‘Bwana Quatermain nitakusimulia hadithi yangu, halafu unipe shauri na msaada wako. Yule wakili wangu aliyeniletea barua yako aliniambia kuwa wewe ni mtu wa heshima sana na watu wote wanakustahi, na kwa hiyo naweza kukuamini. Basi nikainamisha kichwa kwa haya kwa vile nilivyosifiwa na Bwana Henry akaendelea kusema, ‘Huyo Bwana Neville ni ndugu yangu.’ Niliposikia hivi nikastuka sana, maana sasa nalifahamu sababu ya kumtazama sana nilimwona mara ya kwanza, kwa kuwa wamefanana sana.

Basi Bwana Henry akaendelea kusema, ‘Yeye ni mdogo wangu, na mpaka miaka mitano iliopita nadhani hatukupata kuachana hata kwamuda wa mwezi mmoja. Lakini katika mwaka ule wa mwisho tulioonana tulipatwa na msiba kama wanavyopatwa watu wote mara kwa mara. Maana tuligombana sana hata nilimtenda mambo yasiyo ya haki kwa ajili ya hasira zangu. Haikosi unajua kuwa mtu akifa na kama mali yake ni mashamba tu, wala naye hakuacha wosia wowote, kwa sheria ya Uingereza mrithi huwa ni Yule mtoto mwanaume mkubwa, yaani aliyezaliwa kwanza, ndiye anayechukua mali yote. Basi hivyo ndivyo ilivyokuwa. Na wakati ule tulipokuwa tukigombana baba yetu alifariki naye hakuwahi kuandika wosia. Basi kwa hivyo ilionekana kuwa mdogo wangu hakuwa na urithi.

Kusema kweli ilikuwa ni wajibu wangu kumsaidia na kumtunza, lakini kwa ule uchungu wa ugomvi jinsi ulivyokuwa mwingi sana, hata sasa naona aibu kukiri kuwa sikufanya jambo. Sikuwa na nia ya kumnyima haki yake, ila nilitaka yeye aje kwangu’ kuomba suluhu, naye hakuja. Nasikitika sana kukuudhi kwa habari hizi zangu, lakini naona sina budi kukueleza waziwazi mambo yote, sivyo Bwana Good?’ Bwana Good akajibu, ‘Ndivyo, nami najua kwa hakika kuwa Bwana Quatermain atayasitiri yote moyoni mwake.’ Nikajibu, ‘Vema,’ Maana mimi natafakari sana kuwa si mtu wa kupayuka.

Halafu Bwana Henry akasema, ‘Mdogo wangu alikuwa na fedha kidogo na bila kunishauri alitoa fedha zote alizokuwa nazo katika banki, na kuchukua jina lingine la Neville, akafunga safari kwenda kuchuma Afrika ya Kusini. Nikakaa kwa muda wa miaka mitatu bila kupata habari zake wala salamu zake, ingawa mimi nilimwandikia barua nyingi. Labda zilikuwa hazimfikii. Lakini baadaye nikaanza kuwa na wasiwasi, maana mtu haachi kumpenda ndugu yake.’
Nikasema, ‘Hayo ni ya kweli. ‘Maana nilikuwa nikimkumbuka mtoto wangu. Bwana Henry akawa anaendelea kusema, ‘Nikahisi kuwa hata nusu ya mali yangu yote nitatoa ili nipate kujua yaliyompata mdogo wangu, maana ni mmoja tu aliyebaki katika ukoo wangu. Basi siku zilipozidi kupita nami nikazidi kuwa na wasiwasi, nikatamani sana kupata habari zake. Ndipo nikaanza kuulizauliza, hata nikapata ile barua. Basi mpaka sasa habari ni nzuri, maana zaonyesha kuwa yu hai mpaka sasa. Na nilitia nia kwenda mwenyewe kumtafuta, na Bwana Good amenifurahisha sana kwa kufuatana nami.’ Basi Bwana Good akasema, ‘Ndiyo na sasa Bwana, labda utatwambia habari zote ujuazo za Yule mtu aitwaye Neville.’

SURA YA PILI

Basi kabla sijaanza kumjibu Bwana Good, nilitia tumbako katika kiko changu, na Bwana Henry akauliza, ‘ Ulisikia habari gani juu ya safari ya ndugu yangu ulipokuwako Bamangwato?’ Nikamjibu, ‘Nalisikia hivi, ya kuwa anakwenda kutafuta Mashimo ya Sulemani. Na tangu siku hiyo hata hivi leo, sijamwambia mtu habari hizo.’ Wote wawili wakauliza pamoja, ‘Mashimo ya Sulemani! Yapo wapi?’ Nikajibu, ‘Mimi sijui, lakini najua mahali ambapo watu husema kuwa yapo. Siku moja niliona vilele vya milima inayopakana nayo, lakini baina ya mahali hapo nilipokuwa mimi na milima hiyo palikuwa na jangwa la upana wa maili mia moja na thelathini, nami sijapata kusikia kuwa Mzungu yeyote amepata kuvuka jangwa hilo, isipokuwa mtu mmoja tu.



Lakini nadhani itakuwa vizuri zaidi nikisimulia habari hizo, yaani kama nilivyopokea kutoka kwa wenyeji, za Mashimo ya Sulemani kwa kadiri ninavyojua, ikiwa mtaahidi kuwa mtazisitiri mioyoni mwenu na kutomwambia mtu yeyote bila ya idhini yangu. Je, mtakubali sharti hilo?’ Bwana Henry akainamisha kichwa, na Bwana Good akaitikia, ‘Naam, naam.’ Basi, nikaanza kutoa hadithi yangu: ‘Kwa kawaida mwajua kuwa wawindaji wa ndovu ni watu wasiotamani anasa za dunia, wala hawashughuliki na mambo ila ya kweli ya dunia. Lakini pengine mwaweza kumkuta mtu mmoja mmoja anajitia katika mambo ya kuandika hadithi na kujaribu kutunga habari za zamani za watu wa kale. aliyeniambia maneno haya alikuwa ni mtu wa namna hiyo, na tangu aliponiambia maneno haya umepita muda wa miaka thelathini. Ilikuwa hivi: katika safari yangu ya kwanza nilikwenda kuwinda ndovukatika nchi ya Matabele. Mtu mmoja aliyeitwa Evans ndiye aliyeniambia maneno hayo, naye masikini aliuawana nyati mwaka wa pili yake, akazikwa mahali palipokuwa karibu na maporomoko ya maji yam to wa Zambezi. Nami nakumbuka sana kuwa siku moja nilikuwa nikizungumzia habari za kulungu na pofu katika mtaa mmoja wa Transvaal.’

Evans akasema, ‘Ndiyo, lakini mimi nitakutolea hadithi iliyo ya ajabu zaidi kupita habari za wanyama.’ Akaendelea kuhadithia jinsi alivyopata kuvumbua magofu ya mji wa zamani sana ambao aliamini kuwa ni mji ule uliokuwa ukiitwa Ophir uliotajwa katika Agano la Kale,na tangu siku hizo, watu wengi wenye maarifa kuliko yeye marehemu Evans wamesema hivyohivyo. Mimi nikakaa kusikiliza sana, maana wakati ule mimi nilikuwa bado kijana, na hadithi zile za kale zilinipendeza sana, na mara akasema, ‘je, mwanangu, umepata kusikia habari za milima ya Sulemani iliyo upande wa kaskazini wa nchi ya Mashukulumbwe?’’ , Nikamwambia, ‘Sijapata kusikia .’Akasema, ‘Basi, haidhuru, hapo ndipo mashimo ya Sulemani yalipo, yaani mashimo ya almasi.’ Nikamuuliza, ‘Je, wewe umejuaje?’ Akajibu, ‘Najuaje! Najua kwa jina lake lilivyo, na tena niliambiwa na mwanamke mmoja mchawi wa kabila la Isanusi katika nchi ya Manika. Alisema kwamba watu wanaokaa upande wa pili wa milima ile ni wa ukoo wa Amazulu, wanasema lugha inayofanana na Kizulu, ila wao ni wakubwa, tena wazuri zaidi ya Amazulu. Lakini kuna wachawi wenye nguvu nyingi wanaokaa humo na walikuwa na siri ya shimo la ajabu lenye mawe yale yanayong’aa.’ Nilicheka sana niliposikia hadithi hii, nikaipuuza, lakini ilinipendeza sana, maana wakati ule mashimo ya almasi yalikuwa bado hayajavumbuliwa. Lakini Yule marehemu Evans aliuawa, nami nikakaa muda wa miaka ishirini bila kufikiri tena jambo hili.

Baada ya miaka ishirini, na huo ni muda mrefu sana, maana mwindaji wa ndovu ana shida kuishi miaka ishirini katika kazi yake, nikasikia habari zaidi juu ya milima ya Sulemani na nchi iliyo upande wa pili yake. Hapo mimi nilikuwa katika nchi ya Manika, mahali paitwapo KwaSitanda, napo ni mahali pabaya sana, maana sikuweza kupata chakula wala wanyama hakuna. Nilishikwa na homa kali mno hata hali yangu ikawa dhaifu sana, na siku moja akafika Mreno mmoja pamoja na mwenziwe mmoja suriama. Tukaongea kidogo pamoja, maana yeye aliweza kusema Kiingereza kidogo, nami pia nilijua kusema Kireno kidogo, akaniambia kuwa jina lake ni Jose Silvestre, na tena ana shamba karibu na Delagoa Bay. Lakini siku ya pili yake aliondoka pamoja na mwenziwe. Katika kuniaga akasema ‘Bwana, tukionana tena natumai mimi nitakuwa tajiri kuliko watu wote duniani, nami nitakukumbuka.’ Nikacheka kidogo, maana nilikuwa mnyonge kwa homa na kwa hivyo sikuweza kucheka sana; nikamwona akienda kuvuka lile jangwa kwenda upande wa magharibi. Nikadhani kuwa ana wazimu, kwani anakwenda kutafuta nini huko? Baada ya juma moja, nikapona, na jioni nilipokuwa nimekaa nje ya hema langu dogo, nikitafuna paja la kuku wa mwisho niliyemnunua kwa mtu mmoja kwa bei ya kitambaa kimoja kilichonipatia kuku ishirini, nikitazama jua jinsi lilivyokuwa jekundu linavyoshuka nyuma ya jangwa hilo, mara nikaona kitu kama mzungu amevaa koti akiteremka mteremko uliokuwako kiasi hatua mia sita, mbele yangu.

Kwanza mtu huyo alitambaa kwa magoti na mikono, kisha akasimama na kupepesuka hatua chache mbele, tena akaanguka na kutambaa. Mradi nikaona kuwa ni mtu aliye taabani. Nikapeleka mmoja wa wawindaji wangu kwenda kumsaidia, na baadae kidogo akaja nae. Je, wadhani alikuwa ni nani? Alikuwa ni Yule Jose Silvetre, kwa kweli, mifupa yake ilikuwa dhaifu, tena alikuwa amekonda kabisa. Uso wake ulikuwa manjano, uking’aa kwa homa aliyokuwa nayo, nayale macho yake meusi makubwa yalionekana kama yaliyotokeza nje, maana alikuwa hana nyama kabisa .. Ngozi yake ilikuwa imekauka, na nywele zake zilikuwa zimegeuka rangi zikawa nyeupe, na mifupa imemtoka. Akawa anaugua huku akisema, ‘Nipeni maji! Jamani.

Nikaona kuwa midomo yake imepasuka na ulimi ulikuwa mweusi tena umevimba. Nikampa maji yaliyochanganyika na maziwa kidogo, akayabugia. Nikamzuia kusudi asinywe zaidi. Na mara homa ilimshika tena na kuanza kupayuka na kusema habari za milima ya Sulemani, na almasi na jangwa. Nikamchukua na kumweka hemani mwangu nikamtunza kama nilivyoweza; lakini nilijua kuwa atakufa. Kama saa tano ya usiku akatulia kidogo, nami ndipo nilipopata usingizi kidogo, nikalala. Kulipopambazuka nikaamka, nikamwona namna alivyokuwa amekonda sana amekaa na kulikodolea jangwa macho. Baadae kile kianga cha kwanza chajua kilionekana mawinguni, kikaangaza jangwa mpaka kufika kilele kirefu katika milima ya Sulemani, masafa ya maili mia moja na zaidi. Mara Yule mgonjwa akanyosha mkono wake mwembamba kuelekeza kileleni na huku akisema kwa Kireno, ‘Ndipo, ndipo papo hapo, lakini mimi sitawahi kupafikia kamwe. Wala hapana atakayepafikia kwamwe!’ Mara akakaa kimya kidogo kama mtu anayewaza jambo moyoni, halafu akanigeukia akasema, ‘Rafiki bado ungalipo? Ama sasa naona macho yangu yanaingia giza,’ Nikajibu, ‘Ndiyo, nipo hapa hapa.

Lakini sasa afadhali ulale upumzike.’ Akasema, ‘Ndiyo nitapumzika sasa hivi; tena nitakuwa na wasaa mwingi wa kupumzika, hata milele. Nisikilize, ninakufa! Wewe umenitendea mema. Nitakupa hati. Labda utaweza kupafikia ikiwa utaishi na kuvuka jangwa ambalo limemuua mtumishi wangu na mimi!’

Akapapasapapasa katika mfuko wake akatoa kitu nilichokidhania kuwa kikoba cha kuwekea tumbako kilichofanywa kwa ngozi ya mnyama. Kikoba hicho kilifungwa kwa uzi wa ngozi naye alijaribu kukifungua asiweze. Akanipa akisema, ‘Fungua.’Nikakifungua nikatoa kipande cha kitambaa kikuukuu cha katani kilichokuwa kimeandikwa maneno, na ndani ya kitambaa hicho mlikuwamo karatasi. Kisha akasema kwa sauti ya kufifia, maana alizidi kudhofu, akanena, ‘Juu ya hiyo karatasi kumeandikwa yote yaliyoshindikwa juu ya kitambaa na hivyo ilinibidi kufanya kazi miaka hata kuweza kuisoma. Sikiliza: Babu yangu ambaye ilimlazimu kuutoka mji wa Lisbon alikuwa katika Wareno hao wa kwanza waliofika katika nchi hii.

Aliandika maneno hayo wakati alipokuwa akifa katika milima ile ambayo hapana hata Mzungu mmoja aliyepata kuikanyaga kwa miguu yake mpaka hivi leo. Jina lake lilikuwa Jose da Silvestre, naye aliishi miaka mia tatu, nyuma. Mtumishi wake aliyekuwa akimngojea upande huu wa milima aliona kuwa amekwisha kufa, nae ndiye aliyeleta maandishi haya mpaka Delagoa. Na tokea wakati huo yametunzwa na warithi wake, lakini hapana aliyetaka kuyasoma, mpaka mimi nilipofaulu. Nami nimepoteza maisha yangu kwa ajili yake, lakini labda mtu mwingine ataweza kufaulu na kuwa tajiri kupita watu wote duniani. Lakini usimpe mtu mwingine bwana, wewe nenda mwenyewe!’ Akaanza kuugua tena, na baada ya saa moja akafa. Mungu amrehemu. Nilimzika katika kaburi la kwenda chini sana, nikaweka na mawe makubwa juu ili kusudi asifukuliwe na fisi. Kisha nikaondoka pale.

Bwana Henry akauliza, na sauti yake ilionyesha jinsi alivyokuwa akisikiliza maneno yangu, ‘Ehe, lakini hiyo hati iko wapi? Naye Bwana Good akaongeza, ‘Hati hiyo iko wapi sasa, iliandikwa habari gani?’ Nikasema, ‘Mkitaka nitawasimulia habari zake. Nami sijamwonyesha hata mtu mmoja ila Mreno mmoja mfanya biashara aliyekuwa amelewa wakati alipoitafsiri, tena hakosi’ kuwa alikuwa amekwisha sahau habari zake ulevi ulipomtoka. Hicho kitambaa chenyewe nimekiweka kwangu Durban pamoja na hiyo karatasi aliyoifasiri marehemu Jose, lakini hapa ninayo tafsiri ya Kiingereza na nakala ya ramani iliyokuwamo, nayo ni hii:’

Mimi Jose da Silvestre nipo hapa ninakufa kwa njaa ndani, ya pango dogo katika upande wa kaskazini mwa titi la mlima ulio upande wa kusini wa milima miwili ambayo nimeipa jina la Maziwa ya Sheba. Naandika haya kwa kipande cha mfupa na wino wa damu yangu mwenyewe katika mwaka 1590. Ikiwa mtumishi wangu atakuja na kuiona na kuichukua mpaka Delagoa, nataka rafiki yangu (Na hapo katika hati, jina lake limefutika.) ampashe habari mfalme ili alete jeshi la askari watakaoweza kuvuka jangwa hili na kuwashinda hawa Wakukuana walio majabali sana na wenye uchawi mwingi. Lakini kwa sababu ya hila na udanganyifu wa Mchawi Gagula sikuweza kuleta kitu cha ushahidi, tena hata maisha yangu nayo nimeyaokoa kwa shida nyingi. Na huyu atakayekuja na afuate ramani, apande theluji ya ziwa la kushoto la Sheba mpaka afike penye titi, ambapo kwa upande huo wa kaskazini pana njia kuu iliyotengenezwa na Sulemani. Kutoka hapo ni mwendo wa siku tatu kufikia jumba la Mlalme. Basi na amwue Gagula. Nawe niombe dua.

Kwaheri. Jose da Silvestre.

Nilipokwisha soma barua na kuonyesha ile nakala ya ramani iliyoandikwa na Yule mzee kwa damu ya mkono wake, wakanyamaza kimya kwa ajili ya kustaajabu kwao. Baadae Bwana Good akasema, ‘Lo! Nimezunguka dunia mara mbili, tena nimefika bandari nyingi lakini sijapata kusikia hadithi kama hii hata vitabuni.’ Bwana Henry akasema, ‘Ni hadithi ya ajabu Bwana Quatermain. Natumai unajaribu kutuhadaa! Najua kwamba watu hudhani kuwa si vibaya kumhadaa mjinga.’ Niliposikia hivi nikaudhika, nikatwaa karatasi nikaiweka mfukoni, maana sikupenda kudhaniwa kuwa ni mmoja wa wale wapendao kusimulia uwongo na kuwahadithia wageni habari za kuwinda na mambo mengine ambayo hayakutokea kamwe. Basi nikajibu, ‘Kama unafikiri hivyo basi mambo yaishe hapa hapa. Nikasimama nikataka kwenda zangu. Bwana Henry akaniwekea mkono wake begani pangu akasema, ‘ Kaa, Bwana Quatermain, niwie radhi, usiudhike; kwani naona kuwa hupendi kutuhadaa, lakini hadithi yenyewe ni ya ajabu mno hata kwanza niliona vigumu kuisadiki.’

Basi ndipo nilipoanza kutulia kidogo, maana nilipofikiri niliona kuwa si ajabu kuwa yeye hawezi kusadiki hadithi, nikamwambia, Tutakapojaliwa kufika Durban utaona ramani ya asili na maandishi yake. Lakini bado sijakwambia habari za ndugu yako. Nilimjua Yule Jim aliyekuwa pamoja naye. Yeye ni Mbechuana, mwindaji hodari, tena na mtu mwenye busara. Siku hiyo Bwana Neville alipoanza safari yake nilimwona Jim amesimama karibu na gari langu akisokota tumbako yake, nikasema, ‘Jim, safari hii unakwenda wapi? Kuwinda ndovu?’ Akajibu ‘La! Tunakwenda kutafuta kitu kinachotafutwa sana zaidi ya pembe za ndovu.’ Mimi nikazidi kumdadisi, nikamuuliza, ‘Je, kitu hicho chaweza kuwa nini? Ni dhahabu? Akacheka akajibu, ‘siyo Bwana, ni kitu kinachotakiwa zaidi ya dhahabu.’

Basi sikumuuliza neno tena, maana sikupenda kuonekana kuwa ni mdaku. Baada ya Jim kuisha kusokota tumbako yake, akasema ‘Bwana, sisi tunakwenda kutafuta almasi.’ Nikasema, ‘Almasi! Lakini mbona unafuata njia ambayo si njia ya kwendea huko; kwa nini hufuati njia inayoendelea kwenye mashimo?’ Akajibu, ‘ Bwana, umepata kusikia habari za mlima wa Sulemani?’ Nikamjibu, ‘Ndiyo.’ Akaniuliza, ‘Umesikia habari za almasi zilizoko huko?’ Nikwamwambia, ‘Ni upuuzi tu.’ Akanena, ‘Si upuuzi,? Wana maana, namjua mwanamke aliyetoka huko, naye alifika Natal pamoja na mtoto wake, akaniambia; lakiniamekufa sasa.’

Nikamjibu, ‘Wewe na bwana wako mkijaribu kufika nchi ya Sulemani, hamkosi mtaliwa na tai.’ Akacheka, akasema, ‘Labda, bwana . Mtu amezaliwa naye atakufa; nami ningependa kutembea katika nchi ngeni; maana ndovu wanakwisha katika nchi hii.’ Nikasema, ‘Haya, tutaona.’ Baada ya nusu saa nikaona gari la Neville likitoka. Na baadae kidogo Jim akarudi mbio akasema, ‘Kwaheri bwana, kwani sikupenda kuanza safari bila kuagana nawe. Ninaona labda umesema kweli ya kuwa hatutasafiri kwenda kusini tena.’ Nikamuuliza, ‘Je, Jim, wasema kweli? Bwana wako amesema kuwa anakwenda mlima wa Sulemani, au sivyo?’ Akasema, ‘Ni kweli bwana maana aliniambia kuwa imempasa ajaribu kuchuma mali kwa njia yoyote; basi ni afadhali ajaribu kutafuta hiyo almasi.’ Nikasema, ‘Vema Jim, lakini ngoja kwanza, nataka uchukue barua hii, lakini lazima uahidi kuwa hutampa mpaka nifike Inyati.’ Kufika Inyati ilikuwa ni mwendo wa maili kama mia. Basi akaahidi. Nami nikachukua karatasi nikaandika maneno haya: ‘Kwa huyo atakayekuja ..apande theluji ya ziwa la kushoto la Sheba mpaka afike penye titi, ambapo kwa upande huo wa kaskazini pana njia kuu iliyotengenezwa na Sulemani.’

Basi nikampa, kisha nikamwambia, ‘Sasa utakapompa bwana wako barua hii, mwambie afuate sana shauri lililomo. Wala usimpe sasa barua hii kwa sababu sipendi arudi kuja kuniuliza maswali mengi ambayo sitaweza kuyajibu. Haya nenda.’ Basi Jim akaitwaa barua akaenda zake. Na hayo ndiyo yote ninayoyajua juu ya ndugu yako, Bwana Henry; lakini nachelea sana ya kuwa.. ‘Bwana Henry akasema, ‘Tazama, Bwana Quatermain, mimi ninakwenda kumtafuta ndugu yangu; nitamtafuta hata mlima wa Sulemani, hata nitaupita ikiwa ni lazima, mpaka hapo nitakapomwona au mpaka hapo nitakapo hakikisha ya kuwa amekufa; je, utafuatana nami?’

Nimekwisha sema kuwa mimi ni mtu wa taratibu , kweli na pengine ni mwoga kidogo, na haya yalinitia hofu. Maana safari kama hiyo iliyokusudiwa nilibaini kuwa ni kufa tu. Na tena juu ya hivyo nina mtoto anaenitegemea mimi kwa hivi sipendi nife. Basi nilijibu, ‘Hapana bwana, ahsante sana lakini naona ni afadhali nisiende. Sasa mimi ni mzee siwezi kusafiri safari ya kubahatisha hivyo, na tena naona mwisho wetu utakuwa kama ule wa rafiki yetu Silvestre. Mtoto wangu ananitegemea mimi, basi kwa hivyo sina haki ya kujitia katika hatari.’

Basi hapo wote wawili, yaani Bwana Henry na Bwana Good wakahuzunika sana, na Bwana Henry alisema, ‘Bwana Quatermain, mimi ni tajiri sana, nami nimenuia kusafiri ili nimtafute ndugu yangu, na kadhalika waweza kutaja mshahara wowote uutakao nami nitakupa kabla ya kuanza safari. Tena nitausia kuwa tukipatikana na ajali, mtoto wako atazamwe. Mradi sasa naona kwa maneno hayo utaweza kutambua jinsi tunavyo kuhitaji wewe ufuatane pamoja nasi. Tena ikiwa kwa bahati tutavumbua mahali pale palipo na almasi, basi hizo zitakuwa shirika wewe na Bwana Good, mimi sizitaki. Vile vile ikiwa tutapata pembe za ndovu. Waweza kutoa shauri na kufanya mapatano yoyote yanayokupendeza, na tena gharama zote za safari ni juu yangu mwenyewe.’ Nikajibu, ‘Bwana Henry, maneno yako ni mema kweli kweli, lakini lazima niyafikiri kwanza, maana mimi sina mali nyingi, pili kwa sababu najua kuwa ni kazi kubwa sana, basi nipe nafasi nipate kuyafikiri zaidi. Nitakupa jibu kabla hatujafika Durban.’ Bwana Henry akasema, ‘Vema.’ Nikamwambia kwa heri, nikaenda kulala, na nilipolala nilimwota Yule marehemu Silvestre na almasi!

Itaendelea...
 
SURA YA TATU UMBOPA AMEINGIA KAZINI

Kutoka Capetown mpaka Durban ni mwendo wa siku nne au tano kwa kadiri ya mwendo wa meli ulivyo, na hali ya baharini na upepo ilivyo. Pengine meli inacheleweshwa East London muda wa saa ishirini na nne ikiwa mawimbi ni makubwa na bahari imechafuka. Lakini safari hii hatukuwekwa kwa sababu mawimbi yalikuwa si makubwa ila ya kadiri tu, na matishari yaliletwa mara moja kuja kuteremsha shehena. Basi kwa muda huo wote tuliokuwa tukisafiri kwenda Natal nilikuwa nikifikiri sana maneno ya Bwana Henry. Hatukupata kuongea juu ya safari muda wa siku mbili tatu, ingawa nilimsimulia visa vingi vya safari zangu za kuwinda, na hivyo vyote vilikuwa vya kweli kabisa.

Basi siku moja jioni katika mwezi wa January, tulipita bara ya Natal, tukitarajia kuingia bandari ya Durban kabla ya kuchwa. Lakini tulikuwa hatukupima wakati vizuri, maana jua lilikuwa limeshuka kabisa wakati tulipotia nanga nje ya rasi, tukasikia mzinga wa kuonya watu wa Durban kuwa meli ya Kiingereza imekwishafika. Tulichelewa kuingia bandarini usiku ule, kwa hivi baada ya kuteremsha mifuko ya barua katika mashua, tulikaa mezani tukala kwa raha bila ghasia. Tulipopanda tena juu sitahani, mwezi ulikuwa umetoka na kung’aa vizuri juu ya bahari kadiri ya kufanya taa ya mnara kama si kitu. Kutoka pwani upepo ulileta, harufu nzuri ya matunda iliyonitia hamu ya kuimba nyimbo za dini kwa jinsi zilivyokuwa nzuri, na huko katika madirisha ya nyumba za pwani, taa kwa mamia zilitoa mwangaza.

Tukasikia sauti za mabaharia waliokuwa katika meli nyingine wakijitayarisha kung’oa nanga ili wawe tayari kushika majira yao. Sisi watatu, yaani Bwana Henry Curtis na Bwana Good na mimi tulikwenda karibu na usukani tukakaa kimya kwa muda, Na badae kidogo, bwana Henry akasema, ‘Je, Bwana Quatermain umekwisha yafikiri maneno yangu?’ Na Bwana Good akasema, ‘Ndiyo, waonaje Bwana Quatermain? Natumai kuwa utapenda kusafiri pamoja nasi mpaka Mashimo ya Sulemani, au popote alipofika Yule mtu jina lake Neville.

Nikaondoka nikagonga kiko changu ili kukikongoa tumbako. Nalikuwa bado sijakata shauri, mradi nikataka nafasi ya dakika moja nipate kukata shauri kabisa. Basi dakika ile ilinitosha, nikakaa tena nikasema, ‘Vema nitakwenda, na kama mkinipa ruhusa nitawaambia sababu zangu za kwenda, na vile vile nitawaambia kwa mapatano gani. Kwanza mapatano ni haya:
Utalipa gharama zote, na pembe za ndovu zozote na vitu vya thamani vyovyote vingine tutakavyo pata vitakuwa shirika kati ya Bwana Good na mimi, Yapili, unipe pauni mia tano mshahara wangu kabla ya kuanza safari, nami nitaahidi kukutumikiavema mpaka siku utakapoazimu kuacha safari, au mpaka tutakapofaulu, au mpaka tutakapofikwa na ajali.

Ya tatu, kabla ya kuanza safari utaandika hati ya kuahidi kumpa mtoto wangu anaeelimishwa katika hospitali ya London, pauni mia mbili mwaka kwa muda wa miaka mitano, wakati huo ndipo atakapoweza kufanya kazi mwenyewe, akiwa ana akili zake timamu. Basi ni haya tu, na labda utaona ninataka mengi.’
Bwana Henry akajibu, ‘Sidhani kuwa unataka mengi, nami nakubali kwa furaha hayo yote. Mimi nimekaza nia kwenda safari hiyo, nami nilikuwa tayari kukulipa zaidi, ili nipate msaada wako, maana maarifa uliyonayo wewe si ya kawaida, watu wengine hawana.’basi nikasema, ‘Wanifanya kusikitika kwa kuwa sikutaka zaidi! Lakini haidhuru, mimi siwezi kuvunja ahadi yangu.

Na sasa tumekwisha patana, nitakwambia kwa nini nimekubali kwenda. Kwanza, siku hizi zilizopita nilikuwa nikiwatizama sana nyinyi watu wawili, na ikiwa hamtaudhika, nitasema kuwa ninawapenda na tena nadhani kuwa tutapatana vema pamoja. Tena kupatana huku si jambo dogo katika safari ya siku nyingi kama hii tunayokusudia kufanya.

Na sasa kuhusu safari yenyewe, nasema waziwazi kuwa naona hatutarudi salama, yaani, kama tukijaribu kuvuka milima ya Sulemani. Kumbukeni yaliyompata mzee Silvestre miaka mia tatu nyuma, tena yaliyompata Yule mtu mmoja wa ukoo wake miaka ishirini iliyopita! Na sasa yapi yaliyompata ndugu yako? Nitakwambieni waziwazi kuwa mimi nadhani ajali yao itakuwa ndiyo yetu.’

Kisha nikawatazama kuona nini watakayoyafikiri wakisikia maneno yangu. Bwana Good akageuka uso kidogo, lakini Bwana Henry akawa imara kabisa, akasema, ‘Liwalo na liwe, lazima tubahatishe.’Mimi nikaendelea kusema, ‘ Labda utaona ajabu ya kuwa mimi ingawa nimesema maneno hayo, lakini nimekubali kwenda safari hii? Lakini nina sababu mbili. Kwanza, mimi ninaamini ya kuwa mwanadamu hana hiari, yalioandikwa yameandikwa. Ikiwa ajali yangu imefika itakuwa tu bila shaka. Ikiwa nilazima niende safari ya milima ya Sulemani na kuuawa, basi nitakwenda na kuuawa. Haikosi, Mungu mwenyewe anajua nia yake juu yangu, nami sina haja ya kushughulika juu yake.

Na sababu ya pili, ni kuwa mimi si tajiri. Yapata miaka arubaini nimefanya biashara na kuwinda bila kupata kitu isipokuwa riziki tu. Nyinyi mnajua ya kuwa watu huhesabu maisha ya mwindaji ndovu kuwa miaka minne, au mitano tu. Hivyo nimeishi vizazi saba vya watu wanaoshika kazi ninayofanya, nami naona kuwa wakati wangu wa kufariki hauwezi kuwa mbali sasa. Na sasa namna ninavyoishi, ikiwa nitapatwa na ajali yoyote, sina kitu chochote cha kumwachia mwanangu arithi. Lakini tokea sasa atatazamwa kwa muda wa miaka mitano. Basi hizo ndizo sababu zinazonivuta niende.’

Bwana Henry alisikiliza sana maneno yangu, kisha akajibu, ‘Bwana Quatermain, zile sababu ‘ulizotaja za kukubali safari hii, ingawa unafikiri kuwa mwisho wake ni kufa, zaonyesha kuwa wewe ni mtu thabiti kabisa. Kama yale unayoyafikiri yatatokea kuwa kweli itaonekana baadae. Lakini ikiwa yatatokea kuwa kweli au si kweli, mimi nimenuia kuendelea mpaka nione mwisho wake, ukiwa mtamu au ukiwa uchungu. Ikiwa ndiyo tutakufa, basi mimi naona ni afadhali na tupate furaha ya kuwinda kwanza, sivyo Bwana Good? Bwana Good akajibu, ‘Ndivyo, ndivyo. Sisi sote watu watatu tumezoea tangu zamani kuingia katika hatari za namna nyingi na kustahamili mashaka makuu.’

Basi tukashuka chini tukalala. Siku ya pili tulishuka kwenda pwani nikamchukua Bwana Henry na Bwana Good mpaka nyumba yangu ndogo niliyokuwa nimejenga huko Durban zamani. Yule mtu aliyekuwa akitunza nyumba na bustani ni mtumishi aitwae Jack. Alikuwa mtu wangu wa zamani. Aliwahi kuvunjwa paja na nyati katika nchi ya Sikukuni tulipokwenda kuwinda, nae hawezi kuwinda tena. Lakini anaweza kufanya kazi kidogo kidogo katika bustani.

Bwana Henry na Bwana Good walilala katika hema katika bustani yangu kwa sababu hapakuwa na nafasi ndaniya nyumba. Lakini lazima niendelee kusimulia hadithi yangu usije ukachoka. Mara niliponuia kwenda safari hiyo nilianza kutengeneza kila kitu tayari. Kwanza niliandikisha hati ile ya mapatano ili mwanangu apate haki yake ikiwa nitapatwa na ajali. Kisha nikapata zile pauni mia tano. Kisha nikafanya hivi, nikanunua gari na ng’ombe wa kulivuta. Gari lilikuwa refu sana, lina namna ya hema iliyofunika nusu ile ya gari iliyo nyuma, na mbele nafasi ilikuwapo ya kuwekea mizigo yetu. Katika hema ile palikuwa na kitanda kikubwa likichotosha watu wawili, na tena mahali pa kuwekea bunduki na vitu vingine. Kisha nilinunua ng’ombe wa Kizulu ishirini waliokwisha zoea magonjwa ya humo. Kwa kawaida kumi na sita wanatosha, lakini nilichukua wane zaidi kwa tahadhari ikiwa wengine wata kufa.

Kisha kufanya hivi ilikuwa kazi ya kufikiri namna ya chakula na dawa za kuchukua katika safari. Kwa bahati Bwana Good alikuwa amekwisha elimishwa kidogo katika elimu ya utabibu, nae alikuwa na kasha lake la dawa za kila namna. Kisha, tulitengeneza mipango ya bunduki na risasi za kufaa safarini, tukazichagua kwa uangalifu sana, maana kila mwindaji anajua kuwa bunduki na risasi ni jambo muhimu sana. Sasa tukaanza kuchagua watu watakaofuatana nasi katika safari yetu, na baada ya mashauri mengi tukachagua watano, mtu mmoja wa kuchunga ng’ombe, kiongozi mmoja, na watumishi watatu. Yule mchungaji na kiongozi tukawapata upesi, walikuwa Wazulu wawili, na majina yao yalikuwa Goza na Tom; lakini kupata watumishi ilikuwa taabu kidogo. Ilikuwa lazima kuwachagua watu waaminifu na hodari, maana pengine labda maisha yetu yatategemea walivyo.

Mwisho tulichagua wawili, mmoja alikuwa kabila la Hottentot jina lake Ventvogel, maana yake ‘Ndege wa upepo,’ na Yule wa pili alikuwa Mzulu mdogo aliyeitwa Khiva, naye alijua Kiingereza sana. Nilimjua Ventvogel, tangu zamani, alikuwa mtu hodari wa kusaka wanyama, akiweza kufuata nyayo zao kwa namna ya ajabu kabisa, tena alikuwa hachoki kabisa. Sasa tulikuwa tumekwisha chagua wawili, lakini wa tatu hatukuweza kumpata, tukanuia kuanza safari yetu na kujaribu kutafuta mwingine njiani.

Lakini siku moja kabla ya kuondoka, wakati wa jioni, Yule Mzulu Khiva aliniambia kuwa yupo mtu mmoja anataka kuonana nami. Basi tulipokwisha kula, nilimwambia Khiva amlete. Baadae kidogo mtu jamili mwenye umri wa kama miaka thelathini aliingia. Alikuwa mwekundu kuliko Wazulu walivyo. Aliingia akaniamkia kwa kuinua rungu lake, akakaa kitako katika pembe ya chumba.

Niliona ya kuwa alikuwa mtu mwenye cheo, maana kichwani alivaa methali ya taji iliyong’aa, ambayo inavaliwa na Wazulu wakiisha kupata umri fulani, au cheo Fulani. Tena nikaona kama ninamtambua sura yake. Baada ya kitambo, nilimuuliza, ‘Je, jina lako nani? Akajibu, ‘Umbopa.’ Na sauti yake ilikuwa nene na alitamka polepole. Nikasema, ‘Nadhani tumekwisha onana mahali zamani.’ Akajibu, ‘Ndiyo, umeniona katika mahali paitwapo ‘Isandhlwana’ (maana yake ni ‘Mkono mdogo’) siku ile iliyotangulia vita.’
Ndipo nilipomkumbuka.

Mimi nilikuwa mmoja wa viongozi wa Jemedari mmoja katika vita vya Wazulu, na yeye alikuwa mkubwa katika kikosi kidogo cha wenyeji, na siku moja aliniambia ya kuwa alifikiri kuwa kambi letu lina hatari. Mimi nikaona uchungu kidogo, nikamwambia afadhali na uwaachie mashauri kama hayo wakubwa wenye akili kupita zake; lakini baadae niliona kuwa maneno yake yalikuwa ya kweli. Basi nilimwambia, ‘Ndiyo, sasa nakukumbuka. Je, unataka nini?’ Akajibu, ‘Ni hivi Makumazahn (hilo ndilo jina walilonipa wenyeji, na maana yake ni ‘ Akeshaye usiku’. Nasikia ya kuwa unasafiri kaskazini pamoja na mabwana hawa waliotoka Ulaya. Je, ni kweli?’ Nikamwambia, ‘Ni kweli.’ Akasema, ‘Nimesikia ya kuwa utapita mto wa Lukanga ulio safari ya mwezi mmoja kupita nchi ya Manika. Ni kweli, Makumazahn?’
Nikaona ajabu, maana habari za safari yetu tulifanya kuwa ni siri, nikamuuliza, ‘Kwa nini unauliza habari za safari yetu?’ Akajibu, ‘Kwa sababu hata na mimi nataka kufuatana nanyi.

Jina langu ni Umbopa. Mimi ni Mzulu lakini si Mzulu. Ukoo wangu unatoka katika nchi ya kaskazini kabisa. Wametoka huko zamani, miaka elfu nyuma. Wazulu walipokuja hapa, zamani sana kabla ya kutawala Chaka. Mimi sina nyumba. Nimetembeatembea kwa muda wa miaka mingi. Nilikuwa mtu wa Setewayo katika kikosi cha Nkomabakosi, nilikuwa chini ya Umslopogaas (maana yake, ‘Mwenye shoka’) naye ndiye aliyenifundisha kupigana. Baadae nilikimbia kutoka nchi ya Wazulu kwa sababu nilitaka kuona mambo ya watu weupe. Kisha nilimpigania Setewayo katika vita. Na tangu wakati ule nimefanya kazi katika Natal na sasa nimechoka, nataka kurudi kaskazini tena. Hapa si kwangu. Sitaki mshahara , lakini mimi ni mtu hodari nami nadhani ninastahili kupewa nafasi katika safari yako.’ Kwa namna alivyosema nilitambua kuwa anasema kweli. Lakini nilikuwa na shaka kidogo kwa kuwa alitaka kuja bila ya kupata mshahara. Basi nikawaeleza Bwana Henry na Bwana Good, nikawataka wakate shauri.

Bwana Henry akamwambia asimame. Umbopa akasimama akavua koti kubwa alilokuwa kavaa, akasimama amevaa ngozi kiunoni tu na makucha ya simba shingoni. Hakika alikuwa mtu aliyeumbika kabisa wala sijaona mtu aliyependeza kupita yeye. Urefu wake ulikuwa futi sita na inchi tatu, nae alikuwa mpana kwa kadiri ya urefu wake. Alikuwa mwekundu wala si mweusi sana, isipokuwa alikuwa na makovu ya majeraha aliyopata katika vita. Bwana Henry akasimama karibu nae akamtazama usoni, akasema kwa Kiingereza, ‘Napenda watu walio kama wewe Umbopa, utakuwa mtumishi wangu.’ Umbopa akafahamu maneno yale, akasema, ‘Vema.’ Akamtazama namna alivyokuwa mkubwa na mpana, akasema, ‘Sisi ni wanaume, wewe na mimi.’
 
SURA YA NNE
Si nia yangu kueleza habari zote za safari yetu mpaka kufika mji wa Sitanda ulio karibu na mahali inapoungana mto Lukanga na mto Kalukwe. Maana ni safari ya zaidi ya maili elfu moja kutoka Durban, na sehemu ya mwisho wa safari, yaani mwendo wa maili mia tatu hivi tulikwenda kwa miguu kwa kuwa chafuo wengi wapo na ng’ombe wakiumwa nao hufa.

Tulitoka Durban mwisho wa mwezi wa Januari, na tulipofika Sitanda na kupiga kambi yetu, ilikuwa katikati ya mwezi wa Mei. Mambo yaliotokea ni kama yale yanayotokea katika kila safari katika nchi hii ya Afrika, ila jambo moja, na hilo nitaeleza baadaye. Tulipofika Inyati, ulio mji wa mwisho wa biashara katika nchi ya Matabele inayotawaliwa na Lobengula, tuliacha gari letu bila ya kutaka. Katika wale ng’ombe ishirini tulionunua, kumi na mbili tu walibaki. Mmoja aliumwa na nyoka, watatu walikufa kwa njaa na kiu: mmoja alitembeatembea akapotea, na watatu wengine walikufa kwa kula majani yenye sumu. Watano wengine waliugua kwa kula majani hayo hayo lakini tuliweza kuwaponya.

Basi tuliacha gari letu katika mikono ya Goza na Tom, yaani mchungaji na kiongozi, tukamwomba mtu wa Mission aliyekaa karibu aende kuwaangalia mara kwa mara, tukaanza safari yetu ya hatari pamoja na Umbopa, na Khiva, na Ventvogel na wapagazi sita tuliowaandika pale pale. Nakumbuka ya kuwa sote tulikuwa kimya kabisa tulipoanza safari hiyo. Nadhani sote tulikuwa tukifikiri labda hatutaliona gari lile tena; na mimi kwa hakika sikutumai kuliona tena. Kwa muda kidogo tulitembea kimya kabisa mpaka Umbopa aliyekuwa katangulia kidogo alianza kuimba wimbo wa Kizulu kuhusu watu hodari waliokuwa wamechoka kukaa hivi hivi tu, wakaanza safari ili watafute mambo mapya. Na kumbe, walipokuwa wamesafiri mbali sana katika jangwa waliona kuwa si jangwa ila ni mahali pazuri mno penye wanawali wazuri na ng’ombe walionona , na wanyama wa kuwinda porini, na adui wa kupigana nao. Basi sote tulianza kucheka tukaifanya kuwa ni njozi njema.

Umbopa alikuwa mcheshi na wakati mwingine alikaa akijisemea tu mwenyewe, nae aliweza kutuchangamsha sana kwa fikira zake. Sote tulimpenda sana. Na sasa lazima nisimulie habari za jambo nililotaja. Baada ya kupita juma mbili kutoka Inyati tulifika mahali pazuri katika mwitu. Miti mingi ya namna nyingi ilikuwa ikiota juu ya vilima, na miti mingi ilikuwa ikizaa matunda wanayopenda sana ndovu. Tukaona alama ya kuwa kweli wapo ndovu, maana wengine wameng’oa kabisa miti wapate kula matunda yake ndovu ni mlaji mharibifu sana.

Jioni moja, baada ya kufanya safari ndefu, tulitokea mahali pazuri chini ya kilima penye mto wa maji matamu kabisa. Mara tulipoingia katika mto tukaona kundi la twiga wakitoka: mbio’ kwa mwendo wao wa kuchekesha, na mikia yao imeinuka juu. Walikuwa mbali, hatua mia nne hivi na kwa hivyo ilikuwa mbali kuweza kuwapiga bunduki, lakini Bwana Good aliyekuwa katangulia hakuweza kujizuia, akaona lazima ajaribu kuwapiga.

Akaelekeza bunduki yake na kwa bahati alimpiga mmoja aliyekuwa nyuma kidogo. Risasi ikampiga shingoni akaanguka kichwa chini, kama sungura tu. Basi ustadi wa Bwana Good ulihakikishwa tokea siku ile, lakini kwa kweli alikuwa hana shabaha hata kidogo. Ikawa baadae kila mara alipomkosa mnyama, tulimsamehe kwa sababu ya kumpiga Yule twiga. Basi tukawatuma wapagazi watengeneze riyama ya Yule twiga, nasi tukaanza kutengeneza kambi yetu. Kambi yenyewe ilikuwa boma la miiba, na katikati tulitandaza majani makavu ya kulalia, tukakoka moto mwingi wa kuzunguka kambi.

Basi tulipokuwa tumekwisha tengeneza kambi, mwezi ukatoka na chakula chetu cha nyama ya twiga na mafuta ya mifupa yake kilikuwa tayari. Tulifurahi sana kula mafuta yale ya twiga, lakini ilikuwa kazi kuivunja jinsi ilivyokuwa migumu. Nadhani hapana chakula kitamu kama mafuta ya mifupa ya twiga, ila labda moyo wa ndovu.

Tulikula chakula chetu kwa mwangaza wa mbalamwezi, na mara kwa mara tulimsifu Bwana Good kwa shabaha yake; kisha tukakaa tukavuta tumbako na kusimuliana hadithi. Ungalituona ungalistaajabu tulivyokaa. Mimi nywele zangu zaanza kuwa na mvi, na Bwana Henry zake zilizo na rangi ya kimanjano zaanza kuwa ndefu na hatukufanana hata kidogo. Maana yeye ni mrefu, mweupe mpana, na mzito; lakini mimi ni mfupi, mweusi, mwembamba na mwepesi. Lakini labda aliyekuwa mcheshi zaidi ni Bwana Good. Alikaa juu ya mfuko wa ngozi kama ndiyo kwanza amerudi kutoka safari ya kuwinda kwao Ulaya, maana alikuwa maridadi sana, safi kabisa; nae amevaa vizuri. Alikuwa amevaa nguo za kizungu, na kofia vile vile iliyopatana na nguo zake, tena amenyoa vizuri na amevaa miwani yake ya jicho moja.

Basi tulikaa sisi watatu tukizungumza huku tukiwatazama watu wetu waliokuwa wamekaa karibu wakivuta tumbako yao, hata wakaanza mmoja mmoja kujifunika blanketi na kulala penye moto, ila Umbopa aliyekaa mbali kidogo peke yake kashika tama anafikiri. Niliona kuwa hachanganyiki kabisa na wenzake. Baadae kidogo kwa nyuma yetu tulisikia sauti, ‘Woof, Woof!’ Nikasema kuwa huyu ni simba, tukakaa tunasikiliza na mara kutoka mahali penye mto tulisikia sauti ya ndovu. ‘Unkungunklovo! Ndovu!’ Kikasisikia watu wetu wakinong’ozana, ‘Ndovu! Na baadae kidogo tukamwona wameandamana kama vivuli vikubwa wakitoka penye maji wanakwenda mwituni. Mara moja Bwana Good aliruka akataka kuwafuata. Nadhani labda alifikiri kuwa kumpiga ndovu ni sawasawa na kupiga twiga, lakini nilimshika mkono nikamwambia, ‘Waache waende zao.’ Basi Bwana Henry akasema, ‘Naona ni pahali pazuri hapa pa kuwinda wanyama, ni afadhali na tukae siku mbili tatu tuwinde.’ Nikasema, ‘ Vema, nadhani tunataka kujiburudisha kidogo, lakini sasa na tulale tuamke asubuhi na mapema na labda tutawaona wale ndovu kabla hawajaenda mbali.’

Tukajifunika na mablanketi yetu, tukalala. Mara nilisikia kishindo, nikashtuka na sote tuliruka na kutazama kwenye moto. Tukasikia kelele nyingi na mingurumo mingi sana kama nyama wanavutana. Tulijua kuwa hapana ila simba anayeweza kunguruma hivyo, tukazidi kutazama. Macho yalipozoea giza, mara tuliona mchanganyiko wa vivuli vyeusi na vya kimanjano vinatujia. Tukashika bunduki zetu tukavaa viatu vyetu tukatoka kambini kutazama kunanini. Sasa mchanganyiko wa vivuli ulianguka chini ukagalagala na tulipofika pale ulilala kimya.

Sasa tuliweza kuona ni kitu gani. Pale chini tuliona kulungu amekufa kabisa, na juu ya pembe zake amechomeka simba dume mkubwa naye vile vile amekwisha kufa. Nadhani yaliyotokea ni hivi: Yule kulungu alikuja kunywa maji, na Yule simba alikuwa pale akimvizia, akamrukia na akanaswa na pembe zake. Sasa Yule simba hakuweza kujitoa, lakini akageuka na kumuuma Yule kulungu mgongoni na shingoni, naye kulungu alikimbia mbio mpaka akaanguka na kufa.

Tulipokwisha tazama, tuliwaita watu wetu wawavute wanyama wale mpaka kambini, tukalala tena mpaka asubuhi. Kulipopambazuka tu! Tuliondoka tukafunga safari kwenda kuwinda. Tulichukua bunduki kubwa tatu na risasi nyingi, tukaweka chai baridi katika viriba vyetu vya maji. Baada ya kufungua kinywa kwa haraka, tuliondoka tukafuatana na Umbopa na Khiva na Ventvogel.

Tuliwaacha watu wengine kambini kuchuna ngozi ya Yule simba na kukatakata nyama ya Yule kulungu. Hatukuona shida kufuata nyayo za ndovu, na Ventvogel alikisia kuwa walikuwa ndovu ishirini au thelathini katika kundi lile, na wengi ni dume wakubwa. Tulikwenda mbali sana, na ilipopata karibu na saa tatu tulikuwa tumelowa jasho, lakini tulijua kuwa sasa hawako mbali. Tulifahamu hivyo kwa sababu ya miti iliyovunjika na kwa sababu mavi yao yalikuwa bado moto.

Baadae tukaliona kundi, tukaona kuwa kweli wapo ishirini au thelathini, nao wamesimama katika bonde wamekwisha kula, wanapunga masikio yao makubwa. Ilikuwa shani kubwa kuwaona, maana walikuwa karibu, kadiri ya hatua mia mbili na hamsini tu. Nikainama nikatwaa majani makavu kidogo nikayatupa juu hewani ili nipate kujua upepo unatoka upande upi; maana nilijua kuwa wakisikia harufu yetu watakimbia nasi hatutapata nafasi kuwapiga.

Basi nikaona kuwa upepo unatoka kwao, tukatambaa chini na kwa kuwa majani yalikuwa marefu tuliweza kuwakaribia mpaka kufika kiasi hatua hamsini hivi. Pale mbele yetu ndovu wakubwa dume wenye pembe kubwa sana walikuwa wamesimama. Nikanong’ona kumwambia Bwana Henry amlenge ‘yule wa upande wa kushoto, na Bwana Good achague Yule wa upande wa kulia, na mimi nikamlenga Yule wa katikati.

Nikasema , ‘Piga.’ Na mara bunduki zote tatu zikalia pamoja, na ndovu wa Bwana Henry alianguka amekufa, risasi imempenya moyo. Ndovu wangu aliangukia magoti, nikafikiria kama anakufa, lakini mara akasimama tena akaja mbio akanipita kabisa, lakini alipokuwa akinipita, nilimpiga risasi ya mbavu akaanguka. Basi nilimkaribia nikampiga ya kichwa kummaliza kabisa na kukomesha maumivu yake. Kisha niligeuka nimtazame Bwana Good, maana nilipokuwa nikimpiga ndovu wangu nilisikia ndovu akilia kwa hasira na maumivu. Nilipomfikia Bwana Good nilimwona ameingiwa na wasi wasi kabisa. Ikaonekana kuwa mara alipopiga ndovu wake ndovu huyo akaja mbio kumtafuta, nae Bwana Good alikuwa na shida ya kujiokoa. Kisha ndovu alikwenda mbio akifuata njia ya kwendea kambi yetu. Huku nyuma kundi zima lilikimbilia porini.

Kwa muda kidogo tulifikiri, tufuate kundi au tumfuate Yule aliyejeruhiwa, ndipo tulipokata shauri kufuata kundi, tukafikiri kuwa hatutamwona tena Yule ndovu mkubwa. Na toka siku ile ninatamani laiti kwamba tusingalimwona tena. Ilikuwa kazi nyepesi kufuata kundi, maana njia walimopita ilikuwa wazi kabisa kwa jinsi walivyokimbia.

Lakini kuwafikia tena ilikuwa kazi, tukafanya kazi ngumu kwa muda wa saa mbili kabla ya kuwafikia tena. Wote walikuwa wamesimama pamoja ila dume mmoja, nao kwa namna walivyoinua mikonga yao mara kwa mara kunusa nikajua kuwa wamefahamu kuwa hatari ipo karibu. Yule dume alikuwa amesimama yapata hatua hamsini kutoka kundi na hatua sitini kutoka sisi tulipo, akawa amesimama kama analinda zamu.

Nikadhani labda tukikaribia zaidi atasikia harufu yetu,. Basi nikawaambia wenzangu afadhali sote tumpige pamoja. Tukapiga na mara moja akaanguka amekwisha kufa. Basi lile kundi likashtuka likakimbia, lakini walifuata njia iliyowaongoza katika bonde, na mwinuko wa upande wa pili ulikuwa umekwenda juu sana. Basi tulipofika karibu tukawakuta wameshangaa kabisa na kusukumana na kupigana na kupiga kelele wakitafuta njia ya kuokoka.

Basi sasa tulipata wasaa; tukawapiga tukawaua watano. Kisha wakatoka kwa njia nyingine nasi kwa kuwa tumekwisha choka hatukuwafuata tena, maana ndovu wanane kwa siku moja walitosha kabisa. Baada ya kupumzika kidogo, watu wetu waliwakata ndovu wawili wakachukua mioyo yao kuwa chakula cha jioni, tukarudi kambini tukifurahiya kazi za mchana, na tukakusudia kupeleka watu kutoa pembe zote asubuhi. Tulipopita mahali pale tulipopiga wale ndovu wa kwanza, tuliona kundi la wanyama wengine, lakini hatukuwapiga, maana nyama tuliyokuwa nayo ilitosha kabisa. Lakini Bwana Good alitaka kuwakaribia ili awatazame vizuri maana alikuwa bado hajaona namana yao, akampa Umbopa bunduki yake, naye alifuatana na Khiva akaingia mwituni na sisi tulikaa tukiwangoja.

Jua lilikuwa linaanza kutua, likawa jekundu kabisa na Bwana Henry na mimi tukakaa tukitazama uzuri wake, na mara tulisikia ndovu analia, tukamwona anakuja mbio kabisa, mkonga na mkia juu hewani. Tena tukaona jambo jingine, tukaona Bwana Good na Khiva wanakuja mbio na Yule ndovu anawafuata. Tukaona kumbe ni Yule mkubwa aliyejeruhiwa na Bwana Good.

Kwa muda tulishangaa, maana hatukuweza kupiga bunduki kwa kuogopa kuwapiga Bwana Good na Khiva. Hapo jambo la kutisha sana likatokea, Bwana Good aliteleza akaanguka pale pale mbele ya miguu ya Yule ndovu.
Roho zilikuwa si zetu kwa hofu, tukamkimbilia tulivyoweza. Katika muda wa nukta tatu, mambo yangalikuwa yamekwisha, lakini hayakutokea kama tulivyodhania. Maana, Khiva mara alipoona kuwa Bwana Good ameanguka akageuka akatupa mkuki wake usoni pa ndovu, ukampiga mkonga.

Yule ndovu akalia kwa maumivu, akamshika Khiva akamtupa chini, akaweka mguu mmoja juu yake, akamzungushia mkonga wake akamvunja sehemu mbili. Sisi tulishikwa kama na wazimu kwa chuki, Yule ndovu tukampiga bunduki tena na tena, na mwishowe akamwangukia Yule mtu aliye muua. Bwana Good akaondoka akatikisa mikono yake juu ya Yule mtu hodari aliyemwokoa kwa kujitolea maisha yake, na hata mimi niliyezoea sana mambo ya hatari niliona kwikwi ikinipanda kooni. Umbopa akasimama akatazama maiti ya ndovu mkubwa na vipande vya maiti ya maskini Khiva, na baadae kidogo akasema, ‘Amekufa, lakini amekufa kiume!’
 
SURA YA NNE
Si nia yangu kueleza habari zote za safari yetu mpaka kufika mji wa Sitanda ulio karibu na mahali inapoungana mto Lukanga na mto Kalukwe. Maana ni safari ya zaidi ya maili elfu moja kutoka Durban, na sehemu ya mwisho wa safari, yaani mwendo wa maili mia tatu hivi tulikwenda kwa miguu kwa kuwa chafuo wengi wapo na ng’ombe wakiumwa nao hufa.

Tulitoka Durban mwisho wa mwezi wa Januari, na tulipofika Sitanda na kupiga kambi yetu, ilikuwa katikati ya mwezi wa Mei. Mambo yaliotokea ni kama yale yanayotokea katika kila safari katika nchi hii ya Afrika, ila jambo moja, na hilo nitaeleza baadaye. Tulipofika Inyati, ulio mji wa mwisho wa biashara katika nchi ya Matabele inayotawaliwa na Lobengula, tuliacha gari letu bila ya kutaka. Katika wale ng’ombe ishirini tulionunua, kumi na mbili tu walibaki. Mmoja aliumwa na nyoka, watatu walikufa kwa njaa na kiu: mmoja alitembeatembea akapotea, na watatu wengine walikufa kwa kula majani yenye sumu. Watano wengine waliugua kwa kula majani hayo hayo lakini tuliweza kuwaponya.

Basi tuliacha gari letu katika mikono ya Goza na Tom, yaani mchungaji na kiongozi, tukamwomba mtu wa Mission aliyekaa karibu aende kuwaangalia mara kwa mara, tukaanza safari yetu ya hatari pamoja na Umbopa, na Khiva, na Ventvogel na wapagazi sita tuliowaandika pale pale. Nakumbuka ya kuwa sote tulikuwa kimya kabisa tulipoanza safari hiyo. Nadhani sote tulikuwa tukifikiri labda hatutaliona gari lile tena; na mimi kwa hakika sikutumai kuliona tena. Kwa muda kidogo tulitembea kimya kabisa mpaka Umbopa aliyekuwa katangulia kidogo alianza kuimba wimbo wa Kizulu kuhusu watu hodari waliokuwa wamechoka kukaa hivi hivi tu, wakaanza safari ili watafute mambo mapya. Na kumbe, walipokuwa wamesafiri mbali sana katika jangwa waliona kuwa si jangwa ila ni mahali pazuri mno penye wanawali wazuri na ng’ombe walionona , na wanyama wa kuwinda porini, na adui wa kupigana nao. Basi sote tulianza kucheka tukaifanya kuwa ni njozi njema.

Umbopa alikuwa mcheshi na wakati mwingine alikaa akijisemea tu mwenyewe, nae aliweza kutuchangamsha sana kwa fikira zake. Sote tulimpenda sana. Na sasa lazima nisimulie habari za jambo nililotaja. Baada ya kupita juma mbili kutoka Inyati tulifika mahali pazuri katika mwitu. Miti mingi ya namna nyingi ilikuwa ikiota juu ya vilima, na miti mingi ilikuwa ikizaa matunda wanayopenda sana ndovu. Tukaona alama ya kuwa kweli wapo ndovu, maana wengine wameng’oa kabisa miti wapate kula matunda yake ndovu ni mlaji mharibifu sana.

Jioni moja, baada ya kufanya safari ndefu, tulitokea mahali pazuri chini ya kilima penye mto wa maji matamu kabisa. Mara tulipoingia katika mto tukaona kundi la twiga wakitoka: mbio’ kwa mwendo wao wa kuchekesha, na mikia yao imeinuka juu. Walikuwa mbali, hatua mia nne hivi na kwa hivyo ilikuwa mbali kuweza kuwapiga bunduki, lakini Bwana Good aliyekuwa katangulia hakuweza kujizuia, akaona lazima ajaribu kuwapiga.

Akaelekeza bunduki yake na kwa bahati alimpiga mmoja aliyekuwa nyuma kidogo. Risasi ikampiga shingoni akaanguka kichwa chini, kama sungura tu. Basi ustadi wa Bwana Good ulihakikishwa tokea siku ile, lakini kwa kweli alikuwa hana shabaha hata kidogo. Ikawa baadae kila mara alipomkosa mnyama, tulimsamehe kwa sababu ya kumpiga Yule twiga. Basi tukawatuma wapagazi watengeneze riyama ya Yule twiga, nasi tukaanza kutengeneza kambi yetu. Kambi yenyewe ilikuwa boma la miiba, na katikati tulitandaza majani makavu ya kulalia, tukakoka moto mwingi wa kuzunguka kambi.

Basi tulipokuwa tumekwisha tengeneza kambi, mwezi ukatoka na chakula chetu cha nyama ya twiga na mafuta ya mifupa yake kilikuwa tayari. Tulifurahi sana kula mafuta yale ya twiga, lakini ilikuwa kazi kuivunja jinsi ilivyokuwa migumu. Nadhani hapana chakula kitamu kama mafuta ya mifupa ya twiga, ila labda moyo wa ndovu.

Tulikula chakula chetu kwa mwangaza wa mbalamwezi, na mara kwa mara tulimsifu Bwana Good kwa shabaha yake; kisha tukakaa tukavuta tumbako na kusimuliana hadithi. Ungalituona ungalistaajabu tulivyokaa. Mimi nywele zangu zaanza kuwa na mvi, na Bwana Henry zake zilizo na rangi ya kimanjano zaanza kuwa ndefu na hatukufanana hata kidogo. Maana yeye ni mrefu, mweupe mpana, na mzito; lakini mimi ni mfupi, mweusi, mwembamba na mwepesi. Lakini labda aliyekuwa mcheshi zaidi ni Bwana Good. Alikaa juu ya mfuko wa ngozi kama ndiyo kwanza amerudi kutoka safari ya kuwinda kwao Ulaya, maana alikuwa maridadi sana, safi kabisa; nae amevaa vizuri. Alikuwa amevaa nguo za kizungu, na kofia vile vile iliyopatana na nguo zake, tena amenyoa vizuri na amevaa miwani yake ya jicho moja.

Basi tulikaa sisi watatu tukizungumza huku tukiwatazama watu wetu waliokuwa wamekaa karibu wakivuta tumbako yao, hata wakaanza mmoja mmoja kujifunika blanketi na kulala penye moto, ila Umbopa aliyekaa mbali kidogo peke yake kashika tama anafikiri. Niliona kuwa hachanganyiki kabisa na wenzake. Baadae kidogo kwa nyuma yetu tulisikia sauti, ‘Woof, Woof!’ Nikasema kuwa huyu ni simba, tukakaa tunasikiliza na mara kutoka mahali penye mto tulisikia sauti ya ndovu. ‘Unkungunklovo! Ndovu!’ Kikasisikia watu wetu wakinong’ozana, ‘Ndovu! Na baadae kidogo tukamwona wameandamana kama vivuli vikubwa wakitoka penye maji wanakwenda mwituni. Mara moja Bwana Good aliruka akataka kuwafuata. Nadhani labda alifikiri kuwa kumpiga ndovu ni sawasawa na kupiga twiga, lakini nilimshika mkono nikamwambia, ‘Waache waende zao.’ Basi Bwana Henry akasema, ‘Naona ni pahali pazuri hapa pa kuwinda wanyama, ni afadhali na tukae siku mbili tatu tuwinde.’ Nikasema, ‘ Vema, nadhani tunataka kujiburudisha kidogo, lakini sasa na tulale tuamke asubuhi na mapema na labda tutawaona wale ndovu kabla hawajaenda mbali.’

Tukajifunika na mablanketi yetu, tukalala. Mara nilisikia kishindo, nikashtuka na sote tuliruka na kutazama kwenye moto. Tukasikia kelele nyingi na mingurumo mingi sana kama nyama wanavutana. Tulijua kuwa hapana ila simba anayeweza kunguruma hivyo, tukazidi kutazama. Macho yalipozoea giza, mara tuliona mchanganyiko wa vivuli vyeusi na vya kimanjano vinatujia. Tukashika bunduki zetu tukavaa viatu vyetu tukatoka kambini kutazama kunanini. Sasa mchanganyiko wa vivuli ulianguka chini ukagalagala na tulipofika pale ulilala kimya.

Sasa tuliweza kuona ni kitu gani. Pale chini tuliona kulungu amekufa kabisa, na juu ya pembe zake amechomeka simba dume mkubwa naye vile vile amekwisha kufa. Nadhani yaliyotokea ni hivi: Yule kulungu alikuja kunywa maji, na Yule simba alikuwa pale akimvizia, akamrukia na akanaswa na pembe zake. Sasa Yule simba hakuweza kujitoa, lakini akageuka na kumuuma Yule kulungu mgongoni na shingoni, naye kulungu alikimbia mbio mpaka akaanguka na kufa.

Tulipokwisha tazama, tuliwaita watu wetu wawavute wanyama wale mpaka kambini, tukalala tena mpaka asubuhi. Kulipopambazuka tu! Tuliondoka tukafunga safari kwenda kuwinda. Tulichukua bunduki kubwa tatu na risasi nyingi, tukaweka chai baridi katika viriba vyetu vya maji. Baada ya kufungua kinywa kwa haraka, tuliondoka tukafuatana na Umbopa na Khiva na Ventvogel.

Tuliwaacha watu wengine kambini kuchuna ngozi ya Yule simba na kukatakata nyama ya Yule kulungu. Hatukuona shida kufuata nyayo za ndovu, na Ventvogel alikisia kuwa walikuwa ndovu ishirini au thelathini katika kundi lile, na wengi ni dume wakubwa. Tulikwenda mbali sana, na ilipopata karibu na saa tatu tulikuwa tumelowa jasho, lakini tulijua kuwa sasa hawako mbali. Tulifahamu hivyo kwa sababu ya miti iliyovunjika na kwa sababu mavi yao yalikuwa bado moto.

Baadae tukaliona kundi, tukaona kuwa kweli wapo ishirini au thelathini, nao wamesimama katika bonde wamekwisha kula, wanapunga masikio yao makubwa. Ilikuwa shani kubwa kuwaona, maana walikuwa karibu, kadiri ya hatua mia mbili na hamsini tu. Nikainama nikatwaa majani makavu kidogo nikayatupa juu hewani ili nipate kujua upepo unatoka upande upi; maana nilijua kuwa wakisikia harufu yetu watakimbia nasi hatutapata nafasi kuwapiga.

Basi nikaona kuwa upepo unatoka kwao, tukatambaa chini na kwa kuwa majani yalikuwa marefu tuliweza kuwakaribia mpaka kufika kiasi hatua hamsini hivi. Pale mbele yetu ndovu wakubwa dume wenye pembe kubwa sana walikuwa wamesimama. Nikanong’ona kumwambia Bwana Henry amlenge ‘yule wa upande wa kushoto, na Bwana Good achague Yule wa upande wa kulia, na mimi nikamlenga Yule wa katikati.

Nikasema , ‘Piga.’ Na mara bunduki zote tatu zikalia pamoja, na ndovu wa Bwana Henry alianguka amekufa, risasi imempenya moyo. Ndovu wangu aliangukia magoti, nikafikiria kama anakufa, lakini mara akasimama tena akaja mbio akanipita kabisa, lakini alipokuwa akinipita, nilimpiga risasi ya mbavu akaanguka. Basi nilimkaribia nikampiga ya kichwa kummaliza kabisa na kukomesha maumivu yake. Kisha niligeuka nimtazame Bwana Good, maana nilipokuwa nikimpiga ndovu wangu nilisikia ndovu akilia kwa hasira na maumivu. Nilipomfikia Bwana Good nilimwona ameingiwa na wasi wasi kabisa. Ikaonekana kuwa mara alipopiga ndovu wake ndovu huyo akaja mbio kumtafuta, nae Bwana Good alikuwa na shida ya kujiokoa. Kisha ndovu alikwenda mbio akifuata njia ya kwendea kambi yetu. Huku nyuma kundi zima lilikimbilia porini.

Kwa muda kidogo tulifikiri, tufuate kundi au tumfuate Yule aliyejeruhiwa, ndipo tulipokata shauri kufuata kundi, tukafikiri kuwa hatutamwona tena Yule ndovu mkubwa. Na toka siku ile ninatamani laiti kwamba tusingalimwona tena. Ilikuwa kazi nyepesi kufuata kundi, maana njia walimopita ilikuwa wazi kabisa kwa jinsi walivyokimbia.

Lakini kuwafikia tena ilikuwa kazi, tukafanya kazi ngumu kwa muda wa saa mbili kabla ya kuwafikia tena. Wote walikuwa wamesimama pamoja ila dume mmoja, nao kwa namna walivyoinua mikonga yao mara kwa mara kunusa nikajua kuwa wamefahamu kuwa hatari ipo karibu. Yule dume alikuwa amesimama yapata hatua hamsini kutoka kundi na hatua sitini kutoka sisi tulipo, akawa amesimama kama analinda zamu.

Nikadhani labda tukikaribia zaidi atasikia harufu yetu,. Basi nikawaambia wenzangu afadhali sote tumpige pamoja. Tukapiga na mara moja akaanguka amekwisha kufa. Basi lile kundi likashtuka likakimbia, lakini walifuata njia iliyowaongoza katika bonde, na mwinuko wa upande wa pili ulikuwa umekwenda juu sana. Basi tulipofika karibu tukawakuta wameshangaa kabisa na kusukumana na kupigana na kupiga kelele wakitafuta njia ya kuokoka.

Basi sasa tulipata wasaa; tukawapiga tukawaua watano. Kisha wakatoka kwa njia nyingine nasi kwa kuwa tumekwisha choka hatukuwafuata tena, maana ndovu wanane kwa siku moja walitosha kabisa. Baada ya kupumzika kidogo, watu wetu waliwakata ndovu wawili wakachukua mioyo yao kuwa chakula cha jioni, tukarudi kambini tukifurahiya kazi za mchana, na tukakusudia kupeleka watu kutoa pembe zote asubuhi. Tulipopita mahali pale tulipopiga wale ndovu wa kwanza, tuliona kundi la wanyama wengine, lakini hatukuwapiga, maana nyama tuliyokuwa nayo ilitosha kabisa. Lakini Bwana Good alitaka kuwakaribia ili awatazame vizuri maana alikuwa bado hajaona namana yao, akampa Umbopa bunduki yake, naye alifuatana na Khiva akaingia mwituni na sisi tulikaa tukiwangoja.

Jua lilikuwa linaanza kutua, likawa jekundu kabisa na Bwana Henry na mimi tukakaa tukitazama uzuri wake, na mara tulisikia ndovu analia, tukamwona anakuja mbio kabisa, mkonga na mkia juu hewani. Tena tukaona jambo jingine, tukaona Bwana Good na Khiva wanakuja mbio na Yule ndovu anawafuata. Tukaona kumbe ni Yule mkubwa aliyejeruhiwa na Bwana Good.

Kwa muda tulishangaa, maana hatukuweza kupiga bunduki kwa kuogopa kuwapiga Bwana Good na Khiva. Hapo jambo la kutisha sana likatokea, Bwana Good aliteleza akaanguka pale pale mbele ya miguu ya Yule ndovu.
Roho zilikuwa si zetu kwa hofu, tukamkimbilia tulivyoweza. Katika muda wa nukta tatu, mambo yangalikuwa yamekwisha, lakini hayakutokea kama tulivyodhania. Maana, Khiva mara alipoona kuwa Bwana Good ameanguka akageuka akatupa mkuki wake usoni pa ndovu, ukampiga mkonga.

Yule ndovu akalia kwa maumivu, akamshika Khiva akamtupa chini, akaweka mguu mmoja juu yake, akamzungushia mkonga wake akamvunja sehemu mbili. Sisi tulishikwa kama na wazimu kwa chuki, Yule ndovu tukampiga bunduki tena na tena, na mwishowe akamwangukia Yule mtu aliye muua. Bwana Good akaondoka akatikisa mikono yake juu ya Yule mtu hodari aliyemwokoa kwa kujitolea maisha yake, na hata mimi niliyezoea sana mambo ya hatari niliona kwikwi ikinipanda kooni. Umbopa akasimama akatazama maiti ya ndovu mkubwa na vipande vya maiti ya maskini Khiva, na baadae kidogo akasema, ‘Amekufa, lakini amekufa kiume!’
Hii kitu ni kali sana aisee, nimesoma hadi nikasisimka

Big up mkuu blackstarline



Sent using Jamii Forums mobile app
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom