Hadithi: siku za mwisho za uhai wangu

Hadithi: siku za mwisho za uhai wangu

SEHEMU YA 16

Mike alikuwa hoi kitandani, nyumbani kwake, akiamini kabisa kuwa angekufa baada ya siku si nyingi. Alikuwa katikati ya mateso makali na mawazo mengi na alimhurumia sana mke wake kwa sababu mateso aliyokuwa akiyapata hata mkewe pia yalikuwa yakimsubiri.
Ndani ya nafsi yake alijilaumu ni kwa nini alikubali kuacha matumizi ya kondomu kama walivyokuwa wamepanga.
"Mke wangu, UKIMWI si mchezo. Nakuhurumia sana nisingependa mateso haya yakupate lakini hakuna la kufanya, itabidi tu uyapitie haya yote. Mimi najua nitakufa lakini mali yote nitakuachia wewe na ninaagiza kuwa uitumie pesa hiyo kujali afya yako na kuwatunza wagonjwa wengine wa UKIMWI na hata yatima."
"Usiwe na wasiwasi, utapona tu Mike," Beatrice alimpa moyo.
"Mke wangu hali yangu si nzuri, naomba uende mjini haraka iwezekanavyo ukamwite Rwezaura nije nikuandikie hati ya urithi usije ukasumbuliwa baada ya mimi kuondoka."
"Mike lakini unajuaje kama unakufa? Tumwachie Mungu mume wangu!"
"Mimi najua tu Beatrice, ninaomba ufanye hivyo."
Beatrice alizidi kusimama pale bila kujua la kufanya, jambo lililomkera Mike ambaye aliangaza macho yake huku na kule na kumwona dada yake mdogo Violeth aliyeishi naye nyumbani.
"Violeth!" Mike aliita akiwa kakasirika. Violeth alikuja mbio chumbani.
"Nenda kwa Rwezaura upesi mwambie aje na mihuri yake yote nina kitu nataka kuandika sawa?”
Violeth aliitikia na kutoka hadi nje ambako aliondoka na gari la Mike, dakika kumi baadaye alirejea na wakili Rwezaura. Hali ya Mike ilikuwa dhaifu mno. Wakili aliandika hati ya urithi kuwa baada ya kifo cha Mike mali yote irithiwe na Beatrice na Beatrice akifa mali yote irithiwe na Violeth au watoto yatima.
Wakili aliondoka na nakala moja ya hati ya urithi kama kumbukumbu na nakala halisi alibaki nayo Beatrice.
"Mke wangu, najua nikifa wanaume wengi watakufuata na kutaka kukuoa sababu ya mali. Naomba usikubali, si kwamba sitaki mali yangu itumiwe na mtu mwingine, ila sitaki uue mtu mwingine tena; acha tufe wenyewe!" Mike alimwambia mkewe baada ya wakili kuondoka.
Baadaye Mike alimwomba Beatrice amsaidie kuandika barua kwa Chancellor Edmund kumjulisha juu ya hali mbaya aliyokuwa nayo kwani hapakuwa na mawasiliano yoyote kati yao. Beatrice hakutaka kufanya mzaha tena kwani hali ilishamtisha.
"Iweke hiyo barua kwenye bahasha kesho ukaitume Uingereza, pia hiyo hati iweke kwenye bahasha uitunze vizuri maana familia zetu za Kiafrika zina matatizo. Mara nyingi wake wa marehemu hunyanyaswa sana baada ya waume zao kufa!"
Beatrice alifanya kama alivyoambiwa, bahasha iliyokuwa na hati aliiweka katikati ya Biblia na kuifungia ndani ya kabati.
***
Mlango uligongwa, Beatrice akaufungua, alikuwa daktari Kalegeya kutoka kitengo cha kupambana na UKIMWI, pamoja na sista Fortunata aliyekuwa mhamasishaji wa mapambano dhidi ya UKIMWI kutoka Kanisa Katoliki jimbo la Mwanza.
"Ah! Karibuni sana dokta."
"Ahsante, tumekuja kumwona Mike maana siku nyingi sana zimepita bila kumtia machoni, anaendeleaje?"
"Yupo ndani, anaendelea hivyohivyo, tafadhali ingieni tu muongee naye."
Daktari Kalegeya na sista Fortunata waliingia ndani.
"Karibuni sana," Mike alimkabisha Dkt. Kalegeya.
Baada ya maongezi marefu na kupeana pole, daktari Kalegeya alikuwa na jambo.
“Kesho ni Siku ya UKIMWI Duniani, tungependa sana tuwakaribishe mshirikiane nasi katika kuadhimisha siku hiyo.”
"Zitafanyika wapi?" Mike aliuliza.
"Uwanja wa mpira wa Nyamagana."
"Nitapenda sana kuwepo...nina jambo la kuwaeleza vijana ambao bado wanauona UKIMWI kama kitu kidogo, ninataka wapate nafasi ya kuona labda itasaidia kidogo kuibadilisha jamii."
***
Maelfu ya watu walifurika katika Uwanja wa Nyamagana Barabara ya Posta mjini Mwanza, wakisikiliza hotuba za viongozi mbalimbali akiwemo Mkuu wa Mkoa juu ya ugonjwa wa UKIMWI.
Kila mtu alionekana kuwa na huzuni, yalikuwa ni maadhimisho mengine ambayo hufanyika katika viwanja hivyo. Kila kilichoongelewa kilionekana kuwagusa kwa uzito wote waliokuwepo uwanjani.
"Hivi sasa ni wakati wa kumkaribisha Mike Martin, kijana mwathirika wa UKIMWI ambaye ameamua kuongea nanyi siku ya leo ili mpate kuuona mfano hai wa mtu anayekufa kwa UKIMWI.
"Karibu Mike!" Mshereheshaji alimkaribisha.
Mike alinyanyuka kwa msaada wa mkewe na kusimama wima huku akiyumba, ilibidi Beatrice amshikilie vizuri. Uwanja wote ulikuwa kimya kabisa. Watu walipomwona jinsi alivyokuwa amekonda walisikitishwa sana.
"Jamani mnanionaaaa!" Mike alisema kwa sauti, umati wote wa watu ukaitikia.
"Ndiyoooooo!"
"Basi mimi ni mfano halisi wa mtu aneyekufa kwa UKIMWI, ndugu zangu! Leo hii nimeamua kujitokeza hadharani ili muelewe ugonjwa huu unatesa kiasi gani, mpate kubadilisha tabia zenu.”
Alisita kidogo, baadaye aliendelea: "Ndugu zangu ugonjwa huu ni mbaya nikisema mbaya, naomba nieleweke una mateso mengi mno na nisingependa mateso haya yampate mtu mwingine yoyote!
Ningependa mimi ndiye niwe mtu wa mwisho kufa kwa ugonjwa huu. Ndio maana nimesimama mbele yenu kuwaelezeni ninayoyasema.
Nimesikia vijana wengi wakisema UKIMWI ni kama mafua, UKIMWI ni kama malaria, UKIMWI ni kama taifodi lakini maneno hayo mnayasema kabla hamjaupata ugonjwa huu na kuyashuhudia mateso yake.
Ukishaupata utaomba atokee mtu autoe mwilini mwako lakini haitawezekana tena. Ni hapo ndipo utakapoanza kujuta na kuteseka."
Aliendelea, "Kama UKIMWI ungekuwa unaondolewa mwilini kwa pesa mimi ningepona, kwani nilibahatika kupata pesa nikiwa katika umri mdogo sana lakini pesa zangu zimeshindwa kunisaidia! Nimeshakwenda Kenya na Zaire nikatumia mamilioni ya fedha kwa dawa za Kemron na MMI bila mafanikio.
“Nimekwishakwenda Marekani kubadilisha damu mara mbili bila mafanikio, leo hii ninakufa pamoja na fedha nilizo nazo, naziacha pesa zangu!
"UKIMWI si jambo la kufanyia mzaha ndugu zangu..." Wakati Mike akitoa hotuba hii karibu nusu ya watu uwanjani hapo walikuwa wakilia.
"Msilie, chukueni tahadhari kabla mambo hayajawafika..." Alipofika hapo ghafla Mike alianguka chini na kugeuza macho, akaanza kutupa mikono.
Beatrice alianza kulia akimtingisha.
ANGELINA MOSHA 1962-1999 (2)
Mzee Martin, baba yake Mike, alizaliwa katika familia ya Mtemi Mchenya wa huko Dutwa, Bariadi. Alizaliwa akiitwa Longa na alikuwa mtoto wa mwisho katika familia yao iliyokuwa na watoto wengine saba waliotangulia. Ndugu zake wengine wote hawakujaliwa kwenda shule, walibaki nyumbani kumsaidia baba yao kazi na utawala wa ufugaji wa ng'ombe.
Longa akiwa na umri wa miaka mitano, baada ya kiongozi wa kikoloni DC William kumwona na kumpenda, alimwomba Mtemi Mchenya kumruhusu amchukue na kwenda kuishi naye Ikulu ili awe akicheza na mtoto wake aliyeitwa Smith mwenye umri sawa na Longa.
Kwa sababu aliombwa na DC, Mtemi Mchenya hakuwa na pingamizi, alikubali mtoto wake achukuliwe, Longa akawa amejiunga na familia ya DC Smith, Shinyanga mjini. Muda mfupi baadaye alibatizwa na kuitwa Martin Longa Mchenya.
Martin na Smith, kwa pamoja walifundishwa na mwalimu Mwingereza na katika muda mfupi Martin alijikuta akibadilika na kuwa kama Mwingereza. Ilikuwa sio rahisi kuamini alizaliwa katika familia ya Mtemi Mchenya, mara chache sana alikwenda nyumbani kwao Bariadi. Muda mwingi wa maisha yake alikuwa uzunguni, Shinyanga.
Martin akiwa na umri wa miaka kumi na mitano, DC William alitakiwa arudi nyumbani kwao Uingereza, kwa jinsi familia nzima ya DC huyo ilivyokuwa imemzoea Martin, ilishindwa kumuacha Tanganyika.
DC alimfuata Mtemi Longa kuomba ruhusa ili waondoke naye, lakini Mtemi alikataa na kusema mtoto wake asingeweza kuishi mbali na wazazi wake kiasi hicho. Alitaka Martin arudishwe nyumbani mara moja.
Hata hivyo, baadaye Martin alikwenda Bariadi kumbembeleza baba yake ambaye hatimaye alikubali na kutoa ruhusa mtoto wake aondoke na familia ya DC William kwenda Uingereza.
Martin hakurudi nchini mpaka mwaka 1961, ambapo alikuta utaratibu wa Utemi umefutwa lakini kwa elimu aliyokuwa nayo alipata kazi ya Ualimu katika shule ya msingi Mwika, huko Marangu, Kilimanjaro.
Ni shuleni hapo ndipo alipokutana na msichana wa Kichaga aliyeitwa Veridiana Mosha, yeye pia alikuwa mwalimu katika shule hiyo, na kujenga naye urafiki wa kimapenzi.
Matokeo ya urafiki wao yalisababisha ujauzito lakini mimba hiyo ikiwa na miezi sita mwalimu Martin aliomba uhamisho kwenda Mwanza ambako miaka mitatu baadaye alimwoa Cecilia Ndaki, mwanamke wa Kisukuma na miaka mitano baadaye mama huyo akawa mjamzito na kuzaa mtoto wao wa kwanza wa kiume ambaye walimwita jina la Mike!
Mike alikuwa ni mtoto mzuri mno, kila mtu alimpenda. Mama yake kila alipopanda basi na kusimama abiria walimgombania kumbeba mtoto huyo.
Je nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 17


Kitendo cha Martin kuhama Moshi kwenda Mwanza na kuoa, kilimuudhi sana Veridiana na kumfanya aamue kukata mawasiliano kabisa na Martin. Alijifungua mtoto wa kike aliyemwita Angelina, aliendelea kumtunza peke yake bila msaada wa baba mtoto wake.
Akiwa na umri wa miaka kumi, Angelina alionekana wazi kuwa mtoto mtukutu kupita kiasi na utukutu huo uliendelea. Akiwa kidato cha pili katika Shule ya Sekondari Ashira alimpiga mwalimu wake kwa jiwe jichoni na kulipasua kabisa jicho lake na kulifanya ling'olewe. Mwalimu akawa chongo.
Kwa kosa hilo Angelina alishitakiwa na kufungwa mwaka mmoja na nusu gereza la watoto lililoko Upanga jijini Dar es Salaam! Alipomaliza kifungo, hakuendelea tena na masomo ya sekondari kwani jina lake lilishafutwa katika shule aliyokuwa akisoma.
Mama yake alimtafutia nafasi katika shule ya sekondari ya Kibosho ambako hata huko hakumaliza kidato cha pili akatoroka na kurudi tena mjini Dar es Salaam ambako alijiunga na watoto wa mitaani. Akawa analala kwenye mabaraza ya maduka ya Wahindi. Baadaye alijiingiza katika biashara ya ukahaba, akiwa na umri wa miaka kumi na sita tu.
Akiwa katika biashara hiyo alikutana na mtalii wa Kiitaliano aliyeitwa Mariano Covre ambaye alimpenda na kuamua kumtoroshea Milano, huko Italia.
Wakiwa huko walifanya biashara ya madawa ya kulevya kutoka Pakstani na kuyaingiza nchini humo ambapo walijipatia mamilioni ya dola za Kimarekani na kutajirika!
Maisha yao yalibadilika na kuwa ya kifahari. Siku zote waliishi hotelini na kila mumewe alipotaka wanunue angalau nyumba Angelina alikataa.
Mumewe alipotaka pesa walizopata waziweke angalau benki pia Angelina alikataa! Hivyo, mamilioni yote ya dola waliyoyapata yalirundikwa ndani ya chumba chao kwenye sanduku kubwa! Lengo la Angelina lilikuwa ni kumdhulumu mwanaume huyo pesa zote.
Hivyo ndivyo ilivyokuja kuwa, kwani miaka ishirini baadaye Angelina alimuua Mariano Corve kwa kumnywesha madawa ya kulevya aina ya Morphine! Alikufa akiwa usingizini na Angelina akatoroka na pesa zote kuja Dar es Salaam ambako alianzisha kiwanda cha kutengeneza vyombo vya Plastiki alichokiita Longa Plastics Ltd.
Hii ni kwa kulienzi jina la baba yake ambaye hakuwahi kumwona hata mara moja! Hakuna mtu aliyeijua siri ya utajiri wa Angelina na iliaminika ndiye alikuwa mwanamke wa kwanza kumiliki kiwanda nchini Tanzania.
Akiwa katika shughuli zake za biashara, Angelina alianza kusikia habari za mfanyabiashara Mike Martin Longa wa Mwanza. Jina hilo lilimfanya ahisi kuwa kijana huyo angekuwa ni mtoto wa baba yake! Hakuwahi hata siku moja kusafiri kwenda Mwanza kuwaona Mike wala baba yake Martin.
Aliendelea na maisha yake, alimjengea mama yake nyumba ya kifahari huko Marangu na maisha yao yaliendelea vizuri.
***
Baada ya Mike kuanguka mbele ya watu waliofurika uwanjani wakisikiliza hotuba yake, Beatrice alimwangukia palepale na kuanza kumkumbatia huku akilia.
"Mike please dont die, please live for me Mike, I love you so much. Please don't go, don't leave me!" (Mike tafadhali usife, tafadhali ishi kwa ajili yangu, nakupenda mno Mike, usiende usiniache Mike).
Mkutano ulivunjika palepale na harakaharaka Mike alibebwa na kuingizwa ndani ya gari la WAMAU lililokuwa uwanjani na kukimbizwa moja kwa moja hadi hospitali ya Rufaa ya Bugando. Alipofikishwa aliingizwa katika chumba cha daktari ambaye baada ya kumpima palepale aliwatangazia waliomleta kuwa Mike hakuwa duniani tena.
Alikuwa amefariki dunia baada ya mateso ya muda mrefu!
Beatrice alianza kulia, haikuwa rahisi kwake kuamini kuwa ule ndio ulikuwa mwisho wa mume wake. Palepale taswira ilimrudisha toka siku ya kwanza kabisa walivyokutana shuleni Nsumba. Aliikumbuka barua ya kwanza ambayo alimwandikia Mike kumtaka urafiki.
"Hapana, daktari umekosea, huu hauwezi kuwa mwisho wa Mike, tafadhali rudia tena kupima!" Beatrice alisema kwa sauti, baadaye alianguka chini na kupoteza fahamu. Alipozinduka baadaye alikuwa wodini akiwa na dripu mkononi.
"Masikini Mike mume wangu umekufa kweli? Kwa nini umeniacha peke yangu darling?" Beatrice aliendelea kulia huku ndugu na jamaa wakimfariji.
Baadaye usiku, kama majira ya saa nne hivi, hali ya Beatrice ilipoonekana kuwa nzuri aliruhusiwa kwenda nyumbani. Watu wengi walikusanyika wakiomboleza kifo cha mume wake.
Mama yake marehemu Mike alianguka chini na kupoteza fahamu mara tu baada ya kumtia machoni Beatrice na palepale alichukuliwa na kupelekwa hospitali ya Mkoa ya Sekou Toure kwa matibabu zaidi.
Ilikuwa siku ya huzuni mno. Nguzo ya familia ilikuwa imeondoka! Mama yake aliona giza nene mbele, hakujua maisha yangeendeleaje baada ya hapo maana waliishi kwa kumtegemea mtoto wao.
Kufuatia kifo cha Mike, kijana aliyekuwa kipenzi cha watu, mji wa Mwanza ulikuwa kimya, kitendo cha kufa akitoa hotuba juu ya UKIMWI kilimfanya Mike aonekane shujaa kupita kiasi. Maneno ya hotuba aliyotoa siku hiyo uwanja wa Nyamagana juu ya UKIMWI ndio yalitumika kukitangaza kifo chake redioni, ambapo WAMAU ndio waliolipa gharama zote za matangazo ya kifo chake.
****
Ilikuwa ni jioni, Angelina alikuwa nyumbani kwake akisikiliza redio, ghafla akasikia tangazo la kifo lililotanguliwa na hotuba juu ya UKIMWI.
"Alikuwa mpiganaji hodari dhidi ya gonjwa hatari la UKIMWI, hakuificha hali yake, alitaka watu wote wajue kuwa UKIMWI ni hatari!
“Mike Martin Longa, mfanyabiashara maarufu mjini Mwanza aliyekuwa akiteseka kwa UKIMWI amefariki dunia leo wakati akihutubia uwanjani Nyamagana... Maziko yatafanyika mara baada ya kufika kwa ndugu wa marehemu. Shujaa ameondoka."
Taarifa ile ilimshtua sana Angelina, akaamua kumpigia simu mama yake kule Moshi. Mama Angelina alidai kuzisikia pia taarifa zile za redioni. Wote walikuwa na imani kuwa aliyefariki alikuwa ni Mike mtoto wa mzee Martin.
"Hivyo mama mimi kesho nitakwenda huko Mwanza nikahakikishe kama kweli aliyefariki ni kaka yangu."
"Huyo baba yako mwenyewe hamjawahi kukutana hata siku moja atakufahamu kweli?" Mama Angelina alimuuliza mwanaye.
"Nitajitambulisha kwake," alijibu.
***
Watu walikuwa wengi mno msibani, wengi walilia na kuomboleza, wengine walizimia, kwaya mbalimbali zilikuwepo msibani hapo kuwafariji wafiwa.
Mpaka saa sita mchana Beatrice alikuwa amekwishazimia mara saba. Kila alipozinduka aliendelea kulia huku akiwa na picha ya marehemu mumewe mkononi. Watu walijaribu kumpa kila aina ya faraja lakini haikuwezekana.
Hadi majira ya saa saba mchana watu bado walikuwa wakivutana kuhusu kwenda makaburini kuzika. Tangu Mike afariki na mama yake kuzimia na kupelekwa hospitalini mvutano ulitokea kama Mike azikwe au hadi mama yake atoke hospitalini.
Wakati haya yakiendelea, ghafla helikopta moja ilitokea na kutua mbele ya nyumba. Iliposimama ardhini mwanamke mmoja aliteremka akiwa amevaa nguo nyeusi zilizoashiria kuwa alikuwa akihudhuria mazishi, akifuatiwa na kijana mmoja nyuma yake.
"Dada ni hapa."
"Asante sana, wewe chukua hii shilingi elfu tano uchukue teksi urudi uwanja wa ndege sawa?" Angelina alimwambia yule kijana aliyemchukua uwanja wa ndege wa Mwanza ili ampeleke kwenye mazishi ya Mike. Alikuwa rubani wa ndege za Wazungu wa kampuni ya madini ya Tanzania Mines.
Baada ya kuachana na kijana huyo huku watu wote wakimshangaa, Angelina alitembea taratibu hadi karibu kabisa na kundi kubwa la vijana waliokusanyika wakionekana wenye huzuni.
"Habari zenu jamani na poleni kwa matatizo."
"Nzuri shikamoo," walijibu karibu wote kwa pamoja.
"Marahaba, ninaweza kuonyeshwa mahali alipokaa mzee Martin?"
Kijana mmoja alijitokeza na kumpeleka hadi ndani ambako alimkuta mzee Martin pamoja na wazee wengine wamekaa wakiongea.
"Shikamooni wazee, poleni sana kwa matatizo yaliyowapata."
"Asante sana mwanetu ni mambo ya dunia."
"Ninaitwa Angelina, ninaomba niongee na mzee Martin kama yupo hapa kati yetu," Angelina alisema.
Mzee Martin aligeuka na kumwangalia mwanamke huyo lakini hakumtambua. Hilo halikuwa tatizo kwake, alinyanyuka wakaondoka kwenda kukaa kando.
"Mzee, mimi naitwa Angelina Martin. Nafikiri utakuwa unamkumbuka mama yangu mzazi anaitwa Veridiana Mosha uliyemwacha akiwa mjamzito huko Kilimanjaro! Mimi ndiye mtoto niliyezaliwa kutokana na ujauzito huo."
"Kwa hiyo wewe ndiye mwanangu?"
"Ndiyo baba."
"Aah, karibu mwanangu, tupo katikati ya msiba wa kaka yako Mike, alifariki dunia jana bahati mbaya hamkuwahi kuonana."
"Pole sana baba, nilisikia taarifa hizo redioni jana ndiyo maana nimekuja nihudhurie mazishi ya ndugu yangu."
"Ulitoka lini Moshi?"
"Nimetoka Dar es Salaam leo hii kwa helikopta ya kukodi."
"Helikopta ya kukodi?"
"Ndiyo baba."
Baada ya salamu hizo mzee Martin alimwongoza Angelina hadi chumba walichokuwa wanawake ambako pia alikaa Beatrice na Violeth, dada yake Mike.
"Samahani jamani huyu ni dada yake marehemu anaitwa Angelina, kafika sasa hivi kutoka Dar es Salaam naomba mkae naye tuomboleze pamoja," Mzee Martin alisema.
Beatrice alinyanyua uso wake kumwangalia Angelina. Hakukumbuka kama aliwahi kuona sura kama ile maishani mwake. Angelina hakuwa amefanana kabisa na marehemu mume wake.
Je nini kitaendelea?
Je Beatrice ataweza kumkumbuka Angelina?
 
SEHEMU YA 18

Siku iliyofuata baada ya mama yake Mike kuruhusiwa kutoka hospitalini na ndugu wote kufika, mipango ya mazishi ilikamilika, heshima za mwisho zikatolewa, baadaye mwili wa marehemu Mike ulibebwa mpaka kanisani eneo la Buzuruga kwa ajili ya ibada.
Ilikuwa ni siku ya huzuni mno kwa Beatrice, alitembea akiwa ameshikwa na watu kila upande, akiwemo dada yake Maggie, wifi yake Violeth, mama yake mzazi na marafiki wengine wa familia.
Baada ya ibada ya Kikatoliki, mwili wa marehemu ulibebwa hadi makaburini karibu tu na kanisa ambako uliingizwa kaburini na kufukiwa. Baadaye zege ilimwagwa juu yake! Beatrice hakuamini kama ule ndio ulikuwa mwisho wa Mike, mume wake.
Siku zote alizoea kupita eneo hilo akienda kwa shangazi yake aliyeishi jirani na makaburi hayo lakini hata siku moja hakuwahi kufikiria kuwa pale ndio mume wake angelala mauti!
***
Baada ya maziko kila mtu alianza kuondoka kurejea nyumbani. Akiwa hatua kama ishirini kutoka kwenye kaburi, Beatrice aligueka kuangalia nyuma. Ukweli ulikuwa dhihiri kuwa mume wake aliyempenda sana alikuwa amemwacha peke yake duniani, hakuelewa maisha yangekuwaje bila Mike.
Ilikuwa ni sawa na mshumaa bila sehemu ya kuusimamisha, ni lazima angeanguka.
Kitendo cha kuondoka na kumwacha mume wake makaburini alikiona kama usaliti na ghafla alijichomoka kutoka mikononi mwa watu waliomshikilia na kuanza kukimbia akirudi makaburini! Alipolifikia kaburi la mume wake alilala juu yake huku akilia.
"Tafadhali Mike rudi, tafadhali Mike rudi siwezi kuishi bila wewe."
Akinamama waliokuwa naye, akiwemo mama yake mzazi, walifika kaburini wakikimbia na kuanza kumbembeleza anyanyuke ili waondoke lakini alikataa katakata na kuendelea kugalagala kwenye kaburi la mumewe akiliita jina lake!
Baada ya kuombwa na kubembelezwa sana hatimaye Beatrice alikubali na kunyanyuka wakaanza kuondoka kurudi nyumbani ambako bado aliendelea na kilio chake!
Siku hiyo hakupata usingizi hata kidogo, kwani sura ya mumewe iliendelea kumjia kichwani mwake, alishindwa kuelewa nini kingefuata baada ya pale maishani mwake bila Mike.
Ni kweli kulikuwa na mali nyingi zilizoachwa lakini kwake hazikuwa na maana bila mume wake.
***
Mzee Rugakingira na mkewe walikuwa ni miongoni mwa watu waliohudhuria msiba huo, moyoni mwake mzee Rugakingira alijiuliza maswali mengi kama kweli Beatrice na marehemu walipima UKIMWI au walidanganya!
Katika siku zote za ugonjwa wa Mike mzee Rugakingira alipokuja Mwanza kuwajulia hali hakuwahi kuliuliza swali hilo ingawa dalili za ugonjwa wa Mike zilifanana kabisa na za wagonjwa wa UKIMWI.
"Kama kweli walipima kuna mmoja wao alikuwa si mwaminifu katika ndoa! Lakini ni nani? Je, ni Beatrice au ni Mike?" Kwa jinsi mzee Rukakingira alivyowafahamu vizuri watoto wake hapakuwa na mtu mwenye tabia ya umalaya kati yao. Alishindwa kuelewa ugonjwa huo uliingiaje katika familia yao.
Mzee Rugakingira alikuwa ni mzazi mwenye busara, pamoja na kuelewa wazi kilichomuua Mike lakini alizidi kumfariji na kumtia moyo ili asimame imara katika wakati huo mgumu. Alijua muda si mrefu pia mwanaye, Beatrice, angekufa kwa ugonjwa huohuo na hilo lilimuumiza sana moyoni mwake. Hakuwa na njia yoyote ya kulikwepa zaidi ya kuukubali ukweli uliokuwepo!
Kilichomshangaza zaidi Beatrice ni Angelina, aliyedaiwa kuwa ni dada wa marehemu mumewe. Angelina hakuonekana kuwa na majonzi hata kidogo na zaidi ya yote hayo, jicho alilomwangalia halikuwa la kawaida! Lilikuwa jicho la chuki.
***
Siku tatu baada ya maziko ya Mike wazazi wa pande zote mbili, ndugu na marafiki wa karibu na familia ya mzee Martin walikuwa wamekaa barazani baada ya maombi ya usiku kabla ya kwenda kulala. Angelina alionekana mwenye mawazo mengi.
"Baba!" Angelina alimwita mzee Martin huku wote wakisikiliza.
"Naam mwanangu."
"Mimi kesho nitaondoka kurudi Dar es Salaam lakini kuna kitu nilitaka tukiongelee kabla sijaondoka!"
"Kitu gani mwanangu?"
"Ni juu ya mali za marehemu..."
Watu wote walipigwa na butwaa hawakutegemea jambo kama hilo ikiwa ni siku tatu tu tangu Mike afariki.
"Mali za marehemu?" Mzee Martin aliuliza, naye pia kwa mshangao.
"Ndiyo! Huyu mwanamke nilichoambiwa ni kwamba hakuzaa na marehemu kaka yangu hata kitoto kimoja, hivyo ni vyema aondoke kurudi kwao na hizo mali tubaki nazo sisi, hana haki ya kupata kitu chochote hapa!"
"Mwanangu unauliza swali gani hilo tena katikati ya majonzi kiasi hiki?"
"Nina haki ya kuuliza kwani aliyefariki ni kaka yangu kabisa."
Watu wote walionekeana kuchukizwa vibaya na jambo hilo.
"Wewe unauliza kama nani katika familia hii maana mimi ndiyo kwanza nimekuoa na sijui hata huyo marehemu kama unamfahamu kwa sura," Violeth aliuliza kwa hasira.
"Mimi dada wa marehemu Mike."
"Kutoka wapi? Eti baba huyu naye nani?" Violeth alijifanya kuuliza.
"Ni nduguyo, nilimzaa huko Moshi miaka mingi iliyopita!"
"Muda wote huo alikuwa wapi mpaka aje leo kuulizia mali ya Mike baada ya kifo chake?" Violeth aliendelea kuuliza akionyesha hasira ya waziwazi, Beatrice alijifunika kwa kanga usoni na kuendelea kulia.
"Nimekwishasema ninayo haki ya kuuliza kama dada na si vinginevyo!" Angelina alijibu kwa ukali.
"Jamani yaani mimi bado namlilia mume wangu leo siku ya tatu tu nyie mnaanza mzozo wa mali? Niacheni nisahau jamani na mali zote nitawaachia kwangu kilichokuwa cha muhimu ni Mike wala si mali, baba naomba mnielewe!" Beatrice alianza kulia tena.
Mzozo huo uliwaudhi sana mzee Rukakingira na mkewe, wakanyanyuka na kutoka nje ambako mzee Martin aliwafuata.
"Mzazi mwenzangu vipi tena hali hii?" mzee Rugakingira aliuliza.
"Bwana hata mimi nashangaa huyu mtoto ndiyo ni mtoto wangu kweli, nilikuwa sijamtia machoni kwa miaka karibu thelathini, ndio kwanza kaja hapa kwangu juzi, leo hii anaulizia mambo yasiyomhusu hata mimi nimeshtuka sana ndugu zangu!"
"Kama ndivyo mlivyopanga basi acha sisi tuondoke na mtoto wetu," mama yake Beatrice alisema.
"Mkifanya hivyo mtakuwa mnafanya makosa makubwa sana na mtatuhukumu kwa kosa lisilo letu, tafadhali hebu mvute subira kidogo nijaribu kulishughulikia suala hili," Mzee Martin alisema.
Baadaye aliingia ndani na kuwakuta watu wote wakilia lakini Angelina alikuwa akisoma gazeti, kitu kilichoashiria kweli alikuwa na roho ya kinyama!
"Binti yangu nakuomba tuongee kidogo nje,” mzee Martin aliingia na kumwambia Angelina ambaye akawa mzito kutoka nje. Hivyo mzee Martin akabidi ayaseme aliyokuwa nayo moyoni palepale.
“Uliyoyafanya yamenifedhehesha sana. Unaona hali uliyoisababisha hapa nyumbani? Sababu mimi nina masikitiko makubwa ya kufiwa na mwanangu, badala ya kuhuzunika wewe unafikiria mali. Nakuomba uondoke hapa kwangu mara moja na nisikuone tena maishani mwangu, sina haja ya kuwa na mtoto kama wewe!"
"Sawa lakini ukweli utabaki palepale kuwa huyu mwanamke ni lazima arudi kwao na mali zibaki kwetu, kwanza ndiye aliyemwambukiza Mike ugonjwa wa UKIMWI," maneno yale yalimhuzunisha kila mtu hata Beatrice mwenyewe alipoyasikia aliangua kilio upya!
"Sawa naondoka lakini nitarudi mpaka nihakikishe mwanamke huyu hapati kitu!" Alisonya, akapanda helikopta na kuondoka zake.
Je nini kitaendelea?
Je Beatrice ataweza kubaki na mali za mumewe?
 
SEHEMU YA 19

BEATRICE RUGAKINGIRA 1962-2002 (3)
MPAKA miezi mitatu baadaye Beatrice alikuwa bado hajapona kidonda cha kuondokewa na mume wake moyoni. Kila siku alilia hasa alipopita makaburini akienda kanisani! Alipoliona kaburi la Mike alilia mfululizo na kuna wakati alishinda kaburini kwa mume wake akiimba na kusali! Alifanya hayo yote kumuombea mume wake mpendwa.
Jumatatu ya kwanza ya mwezi wa nne tangu mume wake afariki alipokea wito wa kuitwa mahakama ya wilaya ya Mwanza. Alipoisoma barua ile ilikuwa ni ya kuitwa kwenye kesi ya mirathi!
Aliyeileta kwake alikuwa balozi, mdai alikuwa Angelina Martin Longa, aliyetajwa kama dada wa marehemu na mdaiwa alikuwa Beatrice Rugakingira mke wa marehemu.
Taarifa hiyo ilimshtua karibu kila mtu na mzee Martin alizidi kuchanganyikiwa. Kila alipojiuliza Angelina alikuwa akitafuta nini hasa kutoka katika familia yake, alikosa jibu. Alimchukia kupita kiasi.
Mahakamani Angelina aliwakilishwa na wakili wake Johnson Rutashobya, kutoka Dar es Salaam na Beatrice alisimama mwenyewe kizimbani kwa sababu alikuwa hajajiandaa vya kutosha.
Cha kushangaza na kilichowafanya Beatrice na ndugu wengine waamini kuwa Angelina alikuwa ametembeza pesa, kesi hiyo ilianza kusikilizwa siku hiyohiyo! Jambo ambalo kisheria lilikuwa nje ya utaratibu.
Angelina alikabidhi hati ya urithi aliyodai iliandikwa na marehemu Mike kabla ya kifo chake kuwa mali zote za marehemu azirithi yeye! Nakala ya hati ile Beatrice alipoipata alishangaa na kukuta kweli ilikuwa na saini ya marehemu mumewe.
Alishindwa kuelewa iliandikwa lini mpaka ikamfikia Angelina wakati marehemu Mike alifia mikononi mwake?" Beatrice alimwaga machozi mahakamani.
"Ndiyo, Mheshimiwa, ninayo nakala aliyoandika marehemu mume wangu ikiwa imesainiwa na wakili wetu."
"Basi unaombwa uiwasilishe mahakamani kama utetezi wako, saa tatu asubuhi wiki mbili zijazo, kesi hii inaahirishwa mpaka tarehe hiyo," hakimu alitangaza.
Angelina aliondoka mahakamani kwa gari la kifahari aina ya Nissan Patrol bila hata kusalimiana na mzee Martin! Watu wote walishangaa na kugundua kweli alichotaka ni dhuluma.
"Achana naye huyo mwehu, mama umesema unayo nakala siyo?"
"Ndiyo baba."
"Basi kaitayarishe tutapambana naye yeye si anajifanya ana pesa?"
****
Kumbukumbu alizokuwa nazo Beatrice ni kwamba hati ya urithi aliitunza ndani ya Biblia, hivyo alipofika nyumbani alikwenda moja kwa moja hadi chumbani, na kufungua kabati akaitoa Biblia na kuanza kuangalia katikati ya karatasi zake.
Ingawa hakuwa na uhakika sana lakini alipoiona bahasha aliiweka Biblia pembeni na kuanza kuifungua. Alichokikuta humo kilimfanya atokwe na machozi! Haikuwa hati ya urithi bali barua ambayo Mike alimwandikia Chancellor Edmund kumbe wakati wa kuzitunza alizichanganya!
Hati ya urithi aliiweka ndani ya bahasha ya Chancellor Edmund na kuituma Uingereza na barua yake ndiyo akaiweka ndani ya bahasha ya hati na kuitunza katikati ya Biblia akifikiri katunza hati ya mirathi!
Beatrice aliishiwa nguvu na akahisi kukata tamaa, alijua tayari jambazi Angelina lilikwishamdhulumu mali zote alizoachiwa na mumewe! Alishindwa kuelewa maisha angeyaandesha vipi wakati akisubiri kifo chake.
Akiwa katikati ya mawazo hayo alikumbuka kuwa mwanasheria wao alichukua nakala moja ya hati hiyo! Bila kupoteza muda alitoka akiwa na furaha ya ajabu kuelekea barabara ya Posta ilipokuwa ofisi ya Rwezaura and Co. Advocates.
Aliegesha gari na kuingia ndani moja kwa moja lakini alishangaa kukuta ndani ya ofisi aliyoijua kama ya wakili wao kuna nguo nyingi za kike zimetundikwa.
"Dada habari yako?"
"Nzuri, karibu uchague nguo dada kuna magauni mapya kabisa yameingiza juzi tu kutoka Uingereza!" Dada aliyekuwa akiuza nguo dukani mle alijibu.
"Samahani naomba nikuulize."
"Uliza tu dada yangu."
"Ofisi iliyokuwa hapa ilihamishiwa wapi?"
"Ah, wale mawakili?"
"Ndiyo."
"Walifunga ofisi yao wakaenda masomoni Uingereza, tena wameondoka mwezi mmoja tu uliopita."
Beatrice alihisi kuchanganyikiwa, akaanza kulia mbele ya msichana aliyemkuta ndani ya duka hilo.
"Vipi mbona unalia dada?"
Beatrice hakujibu kitu bali aliondoka bila kuaga, baada ya kutoka dukani hakwenda nyumbani kwake ila alinyoosha moja kwa moja kwenda Nyakato kwa wazazi wa marehemu Mike.
Kwa kasi ya ajabu, Beatrice aliendesha gari hadi Nyakato kwa mzee Martin, akaliegesha, akateremka na kuingia ndani.
"Vipi mwanangu mbona unahema kasi kiasi hiki kimetokea nini?" Mzee Martin aliuliza.
"Baba ni matatizo makubwa sana inavyoonyesha huyu mwanamke ni lazima atatudhulumu mali zote."
"Kwa nini unasema hivyo?"
"Kwa sababu nimeikosa ile hati aliyoandika marehemu kuturithisha mali mimi na Violeth."
Mzee Martin alikaa kimya habari ile ilikuwa nzito kwake.
"Unasema nini mwanangu?" Aliuliza kwa huzuni.
"Ile hati baba nimeikosa!" Beatrice alijibu.
"Imeibiwa au ndio ile aliyoiwasilisha yule mwendawazimu kule mahakamani?"
"Hapana baba, ukweli ni kuwa nilizichanganya," baada ya kusema hayo Beatrice aliinama na kuanza kulia.
Mama yake Mike aliyekuwa jikoni alisikia sauti ya Beatrice akilia. Alitoka mbio kukimbilia sebuleni.
"Vipi tena jamani?" Aliuliza.
"Kuna tatizo kidogo, lakini si kubwa sana," mzee Martin alimpoza mkewe sababu alikuwa ni mgonjwa wa BP!
"Tatizo gani hilo? Hebu niambie upesi maana wengine roho zetu zina mushkeli."
"Mtoto kapoteza ile hati ya mirathi aliyoandikiwa na marehemu mwanao."
"Ni kweli Beatrice?"
Beatrice alieleza jinsi alivyozichanganya barua na hati.
"Sasa tutafanya nini?" Mama aliuliza.
"Cha muhimu nafikiri Beatrice aende nyumbani ajaribu kutafuta angalau namba ya simu itakayowezesha kuwasiliana na Chancellor Edmund, tumwombe atutumie ile hati. Nina imani ni lazima atakuwa bado ameitunza," mzee Martin alisema.
Ghafla mzee Martin alikumbuka kitu.
"Nakumbuka Violeth aliwahi kuniambia kuwa nakala ya hati mliipeleka kwa wakili au siyo mama?"
"Ndiyo baba lakini bahati mbaya wakili hayupo, amekwenda Uingereza kimasomo, ilipokuwa ofisi yao siku hizi kuna duka."
"Basi kajitahidi sana kutafuta namba ya simu au njia yoyote ya mawasiliano ili tuwasiliane na Chancellor Edmund."
"Nitajitahidi kuitafuta namba nikifika nyumbani kasoro pekee ni kuwa baada ya marehemu mume wangu kufariki vitu vingi nilivichoma moto kwa sababu viliendelea kunikumbusha maisha yetu ya nyuma! Lakini nitajitahidi kutafuta..."
***
Mpaka siku moja kabla ya kesi, Beatrice alikuwa bado hajaipata hati ya mirathi aliyoandikiwa na mumewe! Walishauriana na mzee Martin kuwa watafute wakili awawakilishe mahakamani na kuomba wapewe muda zaidi wa kuitafuta hati hiyo muhimu katika kesi yao kwani ilionekna bila hati hiyo haikuwa rahisi kushinda kesi.
Siku ya kesi Beatrice na Angela waliwakilishwa mahakamani na mawakili wao. Wakili wa Beatrice aliiomba mahakama itoe muda wa miezi miwili zaidi ili upande wa utetezi uandae vizuri ushahidi wake.
Hakimu hakukataa ombi hilo alikubaliana nalo na badala ya miezi miwili alitoa miezi mitatu lakini alisisitiza umuhimu wa kupelekwa vielelezo hivyo kwani kulikuwa na uwezekano wa mahakama siku hiyo kutoa hukumu.
Je nini kitaendelea?
Je Beatrice ataweza kushinda kesi hiyo ngumu?
 
SEHEMU YA 20


Miezi mitatu iliyotolewa na mahakama ilipita, Beatrice alikuwa bado hajafanikiwa kupata anwani wala namba ya simu ya Chancellor Edmund, walipokwenda mahakamani wakili wake aliiomba mahakama iongeze tena muda wa wiki moja ili akamilishe utetezi wake.
Walipotoka mahakamani Beatrice na wakili wake walipata muda wa kukaa na kuongea.
"Nafikiri kitu pekee unachoweza kufanya kwa hivi sasa Beatrice ili kuziokoa mali zote ulizoachiwa na mumeo ni kwenda huko Uingereza na kumtafuta huyo Chancellor nani vile?"
"Edmund."
"Yes, kisheria bila kuipata hiyo hati utapoteza kila kitu."
Beatrice alikaa kimya akimsikiliza wakili wake akitoa maelezo.
"Nina hakika katika muda wa wiki moja utampata na akishakupa hiyo hati rudi hapa mara moja!" Wakili wa Beatrice aliendelea kushauri, baada ya kufikiri kwa dakika tano Beatrice aliibuka na jibu.
"Hamna tatizo, nafikiri itanibidi nijiandae tu na safari. Lakini inawezekana kupata viza hapa Mwanza ya kuniruhusu kuingia Uingereza kweli? Tuliposafiri na marehemu mume wangu kwenda Marekani tulichukua viza Dar es Salaam sasa sijui kama na hapa Mwanza huduma hiyo ipo?"
"Hapa, hakuna, itabidi usafiri hadi Dar es Salaam au Nairobi ambako kuna balozi za Uingereza huko utafanya maombi ya viza, ukishapata viza utakata tiketi na kuondoka, wala usiwe na wasiwasi, ni kitu rahisi tu."
"Sio kazi ngumu kupata viza kweli?" Beatrice aliuliza kwa wasiwasi.
"Sio kazi ngumu kama una vitu vyote vinavyohitajika. Je, pasipoti unayo?"
"Ninayo!"
"Basi hakuna tatizo," wakili alimtoa hofu.
***
Siku mbili baadaye alikuwa safarini kwenda Nyakato kumuaga mzee Martin na familia nzima. Alitegemea kusafiri siku iliyofuata hadi Nairobi ambako angepata viza na kupanda ndege kwenda Uingereza kumsaka Chancellor Edmund.
Kama kawaida, Beatrice aliendesha gari lake kwa kasi kubwa sana. Alipofika maeneo ya sokoni Nyakato karibu na Msikiti, kabla hajakata kona ya mkono wa kushoto kuelekea mtaa wa Mecco ambako ndipo yalipo makazi ya wazazi wa marehemu mumewe, aliona basi la kiwanda cha nguo cha Mwatex likiwa limeegeshwa pembeni mwa barabara, tairi lake la kulia likiwa limefunguliwa. Lilionekana kuwa na pancha.
“Haya magari ya Mwatex bwana! Tangu marehemu aache kazi kila siku yamekuwa mabovu, sijui kwa nini?” Beatrice alishangaa.
Akiwa katika mawazo hayo alimwona mtu mmoja aliyeonekana kama utingo wa basi akimwonyesha ishara ya kusimamisha.
“Haya mashirika ya umma bwana. Sijui watakuwa wanataka spana! Ah! Bwana mimi sisimami mwisho nitamkuta mzee Martin amekwenda kanisani bure!” Beatrice alijisemea moyoni wakati akilipita basi lile na kuendelea na safari yake.
Mtu yule hakusita, alizidi kupunga mkono wake juu huku akikimbia kulifuata gari la Beatrice. Mbele kidogo Beatrice alipoangalia kwenye kioo cha pembeni alimwona yule kijana akiendelea kulifuata gari lake kwa nyuma. Mwisho aliamua kusimama na kuanza kurudi kinyumenyume, alipomfikia kijana yule alisimamisha gari.
"Shikamoo mama!" yule kijana alimwamkia Beatrice huku akihema kwa taabu, kifua kilimbana kwa sababu ya kukimbia.
"Marahaba, hujambo? Vipi gari limeharibika nini? Si basi la Mwatex hilo au siyo?" Beatrice aliuliza.
"Ndiyo mama, tuna pancha kidogo."
"Haya nieleze niwasaidie nini?"
"Hapana mama, wenzangu wamepeleka tairi mjini kuzibwa, ila mimi nina barua yako ambayo nilipewa na Ofisa Usafirishaji miezi minne iliyopita, lakini kwa bahati mbaya nikaisahau kwenye kisanduku cha huduma ya kwanza ndani ya basi. Naomba unisamehe sana mama, naomba tafadhali mama usimwambie bosi atanifukuza kazi."
"Barua yenyewe iko wapi?" Beatrice aliuliza.
"Ngoja niilete mama!" yule kijana aliondoka mbio kuelekea kwenye basi na dakika moja tu baadaye alirejea akiwa na bahasha mkononi na kumkabidhi Beatrice na kupiga magoti.
"Mama naomba sana usimwambie bosi wangu juu ya jambo hili!"
Beatrice aliipokea barua ile na alishangaa kuona juu yake kuna stempu za Uingereza, moyo wake ukadunda kwa kasi na akatokwa na kijasho cha shauku.
Kwa kasi ya umeme, Beatrice aliifungua bahasha ile na kutoa barua iliyokuwa ndani. Juu kabisa ya barua aliona jina Edmund! Moyo wake ukaingia hamu ya kutaka kujua kilichoandikwa ndani ya barua ile. Beatrice hakumkumbuka tena kijana aliyepiga magoti chini na kuendelea kuisoma barua hiyo.
Dear Mike,
At the moment the weather here in the United Kingdom is very cool, people are as busy as bees. How is Tanzania at the moment? And how is your beautiful wife, Beatrice, your dad and mom as well?
Your letter landed in a month ago, I couldn't respond immediately because I wasn't in the UK at the time. I was in Philadelphia on my study tour. Now I', back, that is why you have my letter in your hands!
I was tremendously puzzled when I found a WILL in your letter. That really troubled my mind, and to be frank what I have in my mind right now is that you're not fine Mike! It shows me that you are very sick! I wish I was there to give you my support or could come to Tanzania and help you out of the agony you're facing! But I can't come to Tanzania because I have a very tight programme.
However, I have sent you two British Airways tickets for both of you so that you may come to the UK. As soon as you receive the tickets please come and meet the best doctors in the world. I will be right here waiting for you and ready to pay all the medical costs!
I have also sent back the original copy of your WILL and retained its copy. I did so because there is a long distance between the UK and Tanzania. For that reason, I saw you had the need to stay with the original copy in case anything happens!
I'm looking foward to seeing you in a week!
Thanks.
It is me,
Chancellor Edmund
Get well soon!
Mpendwa Mike,
Kwa sasa hivi hali ya hewa Uingereza ni tulivu ingawa watu wanafanya kazi kwa nguvu kama ilivyo kawaida yao. Vipi Tanzania? Je, mkeo mzuri, Beatrice, hajambo na baba na mama yako nao hawajambo?
Barua yako ilifika hapa mwezi mmoja uliopita lakini sikuweza kuijibu haraka kwa sababu sikuwa Uingereza wakati huo. Nilikuwa Philadelphia huko Marekani katika ziara zangu za kimasomo. Hivi sasa nimerudi ndio maana unayo barua yangu mikononi mwako.
Nilishtushwa sana kukuta hati ya mirathi katika barua yako, suala hilo limenivuruga sana akili na kusema ukweli ninachoamini hivi sasa ni kuwa una matatizo na afya yako si nzuri!
Ningependa sana niwe huko kukupa moyo na kukusaidia kukutoa katika masaibu uliyonayo lakini inaonekana kama siwezi kufanya hivyo kwa sababu hivi ssa nimebanwa na mambo mengi sana hapa Uingereza.
Ila nilichofanya ni kukutumia tiketi mbili za ndege ili wewe na mkeo muweze kusafiri kuja hapa Uingereza kutibiwa na daktari bora kuliko wote duniani na niko tayari kuwalipia gharama zote! Nawategemea hapa katika muda wa wiki moja!
Pia narudisha nakala halisi ya hati ya mirathi uliyonitumia kwa sababu Uingereza na Tanzania ni mbali sana, hivyo ni vyema ukawa nayo HATI halisi ili ikusaidie litakapotokea tatizo lolote.
Mungu akusaidie upone upesi, nategemea kukuona wewe na mkeo katika muda wa wiki moja.
Asante.
Ni mimi Chancellor Edmund.
Ugua pole!
Beatrice alisikitika sana kugundua kuwa kumbe Chancellor Edmund alikuwa hajui kuwa Mike alikwishafariki dunia! Alijisikia vibaya ni kwa nini hakukumbuka kumwarifu.
Pamoja na huzuni hiyo lakini alipoigeuza barua kwa nyuma na kuitia machoni hati aliyokuwa asafiri kuifuata Uingereza alipiga kigelegele cha furaha na kushangilia, akamshtua yule kijana aliyekuwa amepiga magoti ardhini ambaye wakati wote Beatrice alipokuwa akisoma barua alikuwa amezama katika mawazo, akawa kama amezinduka usingizini.
Naye akataka kumsemesha Beatrice ili amhakikishie usalama wake.
"Sasa mama..." yule kijana alianza.
"Hee kijana kumbe upo? Nakushukuru sana na Mungu akubariki," Beatrice alisema akiwa katika hali ya furaha kupita kiasi.
Hakuamini kama muujiza ule ulikuwa umetokea! Shukurani aliyompa yule kijana aliona haitoshi akachukua mkoba wake na kuufungua, akatoa shilingi elfu hamsini na kumkabidhi yule kijana. Kijana yule hakujua ni kwa nini barua ile ilimfurahisha Beatrice kiasi kile lakini alishindwa kuuliza.
"Unaitwa nani, kijana?"
"Mimi?" Yule kijana aliuliza kisha akajibu, “ninaitwa Hollywood..”
"Umenisaidia sana, kijana, matatizo haya yakiisha, njoo ofisini kwangu nitakupa kazi."
"Matatizo gani mama?"
"Siwezi kukuambia sasa hivi."
"Ofisini ni palepale zilipokuwa ofisi za mzee au sio?"
"Ndiyo, njoo baada ya wiki mbili sawa?"
"Sawa mama."
Waliagana.
Bila kuchelewa Beatrice alitia gari moto na kuendelea na safari yake moyoni akiwa amejawa na furaha, alihisi ushindi mkubwa mno dhidi ya Angelina.
"Nimeipata hii haki, yule jambazi sasa amekwisha. He! He! He!" Beatrice alisema na kucheka kicheko cha ushindi.
Alipofika nyumbani kwa mzee Martin aliwasimulia jinsi Mungu alivyo wa ajabu, walisikitika kugundua kuwa Chancellor Edmund hakuwa na taarifa juu ya kifo cha rafiki yake.
"Bwana ashukuriwe sana, mwanangu ulitaka kudhulumiwa kila kitu na Angelina," mzee Martin alisema huku akimshika mkono Beatrice.
Alipotoka pale Beatrice aliipeleka hati ile kwa wakili wake, hata yeye hakuamini muujiza ulioileta hati ile.
"Sasa ushindi ni wako mama na mimi nitahakikisha yule shangingi anakwenda gerezani kwa kosa la kughushi," Revocatus Magesa, wakili wa kujitegemea kutoka Magesa and Co Advocates, alisema.
 
SEHEMU YA 21

Kesi ya Beatrice na Angelina ilikuwa na mashabiki wengi sana mjini Mwanza, siku hiyo mamia ya watu walifurika katika mahakama ya wilaya ya Mwanza ili kujua hatima ya ndugu yao na rafiki yao, Beatrice ingekuwa nini.
"Haya upande wa utetezi una vielelezo kuthibitisha kweli nyie ni warithi halali wa mali za marehemu Mike?"
"Ndiyo Mheshimiwa na ninawasilisha mbele ya mahakama hii tukufu hati halali ya urithi iliyoandikwa na marehemu siku chache kabla ya kifo chake na ninaomba mahakama hii tukufu isiitambue hati iliyotolewa awali na upande wa mdai kwani hati hiyo ni batili na ya kughushi."
Wakili Magesa alisonga mbele na kumkabidhi hakimu hati ile. Baada ya kuipokea hati ile hakimu alionyesha mshangao wa wazi.
"Naomba niletewe haki iliyotolewa awali na upande wa mdai," hakimu aliagiza.
Zilipoletwa, hakimu aliziangalia na palepale akagonga meza kuashiria kuwa mahakama ilikuwa inapumzika kwa muda. "Mahakama itapumzika kwa muda wa dakika tano, ninaomba nionane na mawakili wa pande zote mbili chemba," hakimu alinyanyuka na kuondoka kuelekea ndani akifuatiwa na mawakili wa mdai na mdaiwa.
Mahakama ilikuwa kimya, Angelina alianza kuona mambo yakimwendea kombo. Mwelekeo wa ile kesi hakuutazamia hata kidogo, katu hakutegemea kuwa Beatrice angeweza kuleta uthibitisho wa kurithishwa mali za Mike. Jasho likamtoka.
Dakika tano baadaye mawakili wote wawili walirejea na punde hakimu naye aliingia na akatoa hukumu yake.
"Mrithi halali wa mali za marehemu Mike Martin ni Beatrice Rugakingira, kama lolote litatokea kwamba Beatrice anashindwa kuziendesha mali za marehemu basi, dada wa marehemu, Violeth Martin, ndiye ataziendeleza," hakimu alitoa hukumu na huo ukawa mwisho wa kesi na watu wote wakatoka nje ya mahakama.
Nje ya mahakama ilikuwa furaha tupu, watu wakimpa mkono wa hongera Beatrice, Violeth na mzee Martin! Angelina akiwa amevimbiana alimfuata Beatrice mbele ya mzee Martin na ndugu wengine bila hata ya salamu na kuanza kumtukana.
"We malaya unajiona bingwa sio? Mali hii itakutokea puani, nakwenda Dar es Salaam lakini yatakayokukuta nyuma utajuta!"
"Lakini wee mwanamke mbona unashupalia kiasi hiki mali ya kaka yangu?" Violeth aliuliza.
"Na wewe funga do..." kabla hajamaliza Angelina alikamatwa na polisi kurudishwa tena mahakamani ambako alitakiwa kujibu shitaka la kugushi hati. Hakuwa na la kujitetea, hivyo alihukumiwa kifungo cha miaka miwili jela.
"Nitarudi tu kutoka jela na mapambano bado yanaendelea!" Angelina alisema wakati anapandishwa kwenye karandinga kupelekwa gereza la Butimba.
***
Baada ya kesi hiyo kwisha Beatrice alimwandikia Chancellor Edmund kumtaarifu juu ya kifo cha mumewe! Haukupita muda mrefu Chancellor Edmund alikuja nchini kuhani na kuzuru kaburi la rafiki yake mpendwa, Mike.
Kutokana na uzoefu wa kufanya biashara wakati wa uhai wa mume wake, Beatrice hakupata matatizo kuendesha biashara yao. Biashara iliendelea vizuri na katika muda wa miaka mitatu tayari mali iliongezeka mara tatu, kwani aliendesha kampuni ya ujenzi kwa ubia na raia wawili wa Uingereza aliotafutiwa na Chancellor Edmund, hisa zake katika kampuni hiyo zilikuwa asilimia sabini.
Beatrice alichaguliwa kuwa mwenyekiti wa Chama cha Walio katika Mapambano dhidi ya UKIMWI. Alituma pesa nyingi kusaidia kituo hicho na siku zote hakuyasahau maneno ya mumewe kuwa awakumbuke yatima wa UKIMWI na hatawatupa wengine walioteseka na ugonjwa huo, na hivyo ndivyo siku zote alivyofanya. Alifanya yote hayo huku akitambua kuwa huo ndio ungekuwa mwisho wake.
***
Kutokana na utajiri aliokuwa nao Beatrice, vijana wengi hawakuacha kumtaka kimapenzi lakini siku zote jibu lake lilikuwa moja tena la wazi: "Nina virusi vya UKIMWI."
Hata hivyo, pamoja na kuwaeleza hayo bado wanaume waliendelea kumbembeleza wakidai kifo ni kifo.
Siku zote Beatrice aliyafuata maneno ya mume wake: "Tufe peke yetu, Beatrice, usimuue mtu mwingine ni dhambi."
Hakutaka kufanya jambo tofauti na alivyoagizwa na mume wake.
KUMBUKUMBU ZANGU ZIKO WAPI ?
"Sista, hivi mimi naitwa nani?"
"Wewe, unaitwa Beatrice."
"Beatrice? Beatrice nani?"
"Beatrice Rugakingira."
"Na hapa kwenu nilifika vipi na nilikuwa naishi wapi kabla ya kuja hapa?"
"Wewe, ulikuwa ukiishi hapahapa Mwanza."
"Mwanza? Ndiyo wapi?"
"Hujui Mwanza?"
"Sijui! Lakini nilikuwa nafanya shughuli gani kabla?"
Beatrice hakuwa na kumbukumbu yoyote juu ya maisha yake ya nyuma! Hakuwa na kumbukumbu hata juu ya utajiri wote aliokuwa nao! Alikuwa akiishi katika jumba la masista nje tu ya hospitali ya Bugando!
Alikuwa na jeraha kubwa la panga kichwani lililodaiwa kuukaka ubongo wake kiasi cha kumsababishia ugonjwa wa kupoteza kabisa kumbukumbu zake, yaani Amnesia. Wakati Beatrice anapelekwa hospitali ya Bugando miezi sita kabla ya kuhamishiwa kwa masista hakuna mtu aliyetegemea kuwa angepona kwa jinsi mwili wake ulivyokuwa umesambatarishwa kwa mapanga!
***
Ilikuwa ni siku ya Ijumaa, mawingu mazito yalitanda angani na dalili zote za mvua zilionekana. Siku hiyo Beatrice alikuwa na furaha mno kwani ilikuwa ndiyo siku aliyosaini mkataba wa ujenzi wa barabara ya Mwanza hadi Biharamulo kwa niaba ya kampuni yake ya ujenzi iliyoitwa Beatrice & Mike Construction Limited na kukabidhiwa hundi ya dola za Kimarekani milioni hamsini.
Siku hiyo wifi yake, Violeth, hakuwepo nyumbani, alikuwa amekwenda Nyakato kumwona mama yake aliyekuwa na homa ya malaria.
Beatrice alimteremsha sekretari wake, Linda, nyumbani kwao, hatua chache kutoka nyumbani kwake na kunyoosha moja kwa moja hadi ndani ya ngome ya nyumbani kwake ambako aliegesha gari lake.
Saa nzima baadaye alipomaliza kuoga alichukua kinanda chake na kuanza kuimba mapambio huku akijirekodi kwenye redio yake kubwa iliyokuwa sebuleni. Siku zote alifurahia sana kumwimbia Bwana, ilionekana kuwa siku ya furaha kwake, kidonda cha kufiwa na mume wake kilishapona.
Majira ya saa nne hivi usiku, huku mvua kubwa ilikuwa ikinyesha, Beatrice alisikia mlio wa risasi nje ya nyumba yake. Hofu kubwa ilimjaa akaacha kupiga kinanda na kukimbilia chumbani.
Akiwa huko, aliusikia mlango wa mbele ya nyumba yake ukivunjwa na baadaye akasikia vishindo vya watu wakitembea kuelekea chumbani kwake ambako pia waliuvunja mlango na kuingia ndani.
Beatrice alijificha ndani ya kabati kubwa la nguo huku akiendelea kumwomba Mungu aepushe balaa lililokuwa likija mbele yake, alijua kilichokuwa mbele yake ni tabu.
"Baba ikiwezekana kikombe hiki kinipishe lakini mapenzi yako yatimizwe!" Alisema Beatrice akiyakumbuka maneno ya Mwokozi Yesu Kristo, matumaini yake yote alishahamishia kwa Mungu.
"Yuko wapi?"
"Hata mimi sijui."
"Au kapitia dirishani nini?"
"Haiwezekani nondo zote hizi? Ingekuwa ni Uswahilini angeweza!"
Majambazi yalimsaka huku na kule chumbani bila kumwona, Beatrice alikuwa ndani ya kabati akihema polepole kwa kuhofia kugundulika.
"Yuko wapi?" Yaliendelea kuulizana.
"Labda humo ndani ya kabati."
Beatrice alijikuta mkojo ukimtoka kwa hofu!
"Yaani leo ndio mwisho wangu kweli?" Beatrice alijiuliza.
Ndipo kwa bahati mbaya kwa Beatrice na nzuri kwa majambazi, mmoja wao alifungua mlango wa kabati la nguo, alimkuta Beatrice akitetemeka kwa hofu, akamvuta na kumtoa nje.
"Njoo huku wewe kunguni, watu tumeshakula pesa nusu halafu unataka kuleta kiwingu?" Jambazi mmoja alisema.
Beatrice alipowaangalia watu wale aliogopa sana, walivaa vitamba vyeusi usoni na kuacha matundu ya macho peke yake. Walikuwa na sauti nzito zilizokwaruza.
"Jamani msiniue semeni chochote mnachotaka nitawapa!" Alisema Beatrice akilia, alijua watu hao walitumwa na alijua walitumwa na mtu mmoja tu: Angelina.
"Hatutaki pesa yako ila tunakuuliza swali moja. Je, unamfahamu Angelina?" Swali hilo lilifanya mawazo yake kuwa kweli.
"Ndiyo namfahamu! Kwani anahusiana nini na suala hili?"
"Tutakayokufanyia yote ni vema ukamuulize yeye, sisi hatuna kosa lolote ni watekelezaji tu!"
"Lakini jamani nawaomba msiniue! Hebu nisikilizeni kwanza."
"Hapana ni lazima ufe."
Mmoja kati ya majambazi yale lilimwangalia Beatrice kwa huruma na kujikuta likisema maneno ambayo wenzake hawakuyategemea.
"Jamani kwa nini tumuue mwanamke mzuri kama huyu?" Aliwauliza wenzake.
Ghafla jambazi mmoja lilitoka nyuma likiwa na panga, liliwapita wenzake wote na kwenda mpaka mahali alipokaa Beatrice na kuanza kumkatakata na panga bila huruma!
Beatrice alilia akilibembeleza lile jambazi lisiendelee kumtendea unyama lakini jambazi wala halikusikia, liliendelea kufanya hivyo mpaka Beatrice akapoteza fahamu!
"Twendeni bwana! Mnachelewesha kazi wakati pesa zinatusubiri," aliyaambia majambazi mengine na majambazi yote yakatoka nje na kuondoka zao yakijua kazi ya kumuua Beatrice imekamilika. Kilichofuatia kilikuwa kwenda kuchukua mabaki yao.
Je nini kitaendelea?
Je Beatrice amekufa?
 
SEHEMU YA 22


Asubuhi ya siku ya Jumamosi Linda aliamka mapema na kujiandaa kwa ajili ya kwenda kazini. Kama ilivyokuwa kawaida yake. Alitembea kwa miguu kutoka nyumbani kwake kuelekea nyumbani kwa Beatrice ambako siku zote alipewa lifti na bosi wake hadi kazini.
Tayari jua lilishatoka, ilikuwa ni siku isiyo na mawingu kabisa. Mwanga ulitawala kila mahali, dalili kuwa mvua isingenyesha.
Kabla hajaingia ndani alishangaa kuona damu nyingi sakafuni ambayo ilionekana kutiririka kutoka ndani. Mlango wa nyumba ya Beatrice ulikuwa wazi! Moyo wake ukaruka, akajua ni lazima kuna tatizo lililokuwa limempata Beatrice.
Aliingia hadi sebuleni ambako alikuta damu imetapakaa kila mahali! Hakumwona Beatrice mahali pale na kuamua kwenda chumbani ambako pia hakumkuta! Ndipo alipoamua kurudi sebuleni akiita jina la Beatrice bila kuitikiwa.
"Beatrice! Beatrice! Uko wapi?" Linda aliuliza lakini bado nyumba nzima ilikuwa kimya, akaanza kuita jina la Violeth lakini bado kuliendelea kuwa kimya! Alirudi sebuleni na kuanza kuangaza kila mahali bila kumwona Beatrice wala Violeth. Ndipo alipoamua kuufuata mchirizi wa damu iliyoganda ulioelekea nyuma ya kochi kubwa lililokuwa hapo sebuleni, kule nyuma ya kochi hakuamini alichokiona na kujikuta akipiga kelele kwa sauti ya juu.
"Beatrice what has happened to you!" (Beatrice kimekupata nini?).
Beatrice alikuwa pale amelala chini mwili ukiwa umetapakaa damu! Alikuwa amekatwakatwa mwili mzima, damu ilikuwa haimtoki tena ila mabonge ya damu yalikuwa yameganda pembeni ya mwili wake. Linda alimwangukia na kuanza kumtingisha lakini hakushtuka, alionekana tayari amekwishakufa! Alilia kwa sauti ya juu.
Linda aliikimbilia simu iliyokuwa hapo sebuleni na kuinyanyua ili apige polisi kuwataarifu juu ya kilichotokea. Alishangaa kukuta simu haina mawasiliano yoyote, na alipochunguza vizuri kwa juu aligundua kuwa waya ulikuwa umekatwa.
Hakutaka kupoteza muda, alitoka mbio kuelekea nyumbani kwao ambako aliwasimulia wazazi wake kilichotokea na akapiga simu polisi.
"Ni nyumba namba 150, kitalu namba FFF/555 karibu na Hoteli ya Kamazimas, njooni haraka nafikiri amekufa."
"Kimetokea nini?"
"Mtu kakatwakatwa na mapanga."
"Hiyo nyumba unayoisema sio ya Beatrice?"
"Ndio yenyewe na ni yeye aliyekatwakatwa."
"Mama yangu! Tunakuja sasa hivi!"
Linda alibaki pale akipiga kelele kuita majirani wengine zaidi, kilio chake kilisikika na watu wengi walikusanyika. Kila mmoja wao alikiri kusikia milio ya risasi jana yake lakini hawakuelewa ni nani aliyevamiwa sababu baadaye hali ilikuwa shwari tu.
"Risasi tulizisikia lakini baadaye ikawa kimya hivyo hatukujali sana!"
Dakika kumi baadaye gari la polisi lilifika na kuuchukua mwili wa Beatrice kwenda hospitali ya Bugando kwa uchunguzi. Kila aliyeuona mwili huo ulivyokatwakatwa alijua alikuwa mfu tayari, lakini madaktari walipompima waligundua moyo ulikuwa bado unapiga kwa mbali.
Hali ya Beatrice ilikuwa mbaya kiasi kwamba hata madaktari walikuwa na wasiwasi. Hata hivyo, madaktari waliamua kujaribu kuyanusuru maisha yake.
Bila kuchelewa, zilichukuliwa chupa tano za damu kutoka benki ya damu na Beatrice alishonwa majeraha yake yote huku akiongezwa damu kwa kasi ili kufidia damu iliyopotea.
"Nafikiri atapona ila...!" Mmoja wa madaktari alisema.
"Ila nini?"
"Atakuwa na majeraha sana, hawa watu waliomvamia wanaonekana ni makatili sana, sasa pua yake waliiondoa ya nini?"
"Atahitaji ushauri nasaha ili aweze kuishi vinginevyo hataishi," daktari mwingine aliongezea wakati operesheni ikiendelea.
Habari za kuvamiwa na kukatwakatwa kwa Beatrice zilitapakaa kila mahali. Zilipowafikia wazazi wake huko Bukoba ilibidi wasafiri hadi Mwanza.
Violeth alilia na kuzimia kwa uchungu! Kila mtu alimwomba Mungu muujiza utokee ili Beatrice apone. Ibada na misa vilifanyika katika vituo mbalimbali vya kulelea watoto yatima, ambavyo Beatrice alivifadhili, ili kumwombea apone.
***
Beatrice alilala kitandani kwa mwezi mzima bila kujitambua. Manesi walimsafisha vidonda vyake bila yeye kusikia maumivu ingawa vidonda vyake vilikuwa vikubwa mno. Alikuwa ni kama mfu ingawa alikuwa bado akipumua, mapigo yake ya moyo na shinikizo yalikuwa sawa.
Ndugu na marafiki walishapoteza matumaini, walikaa kusubiri siku ambayo Beatrice angekata roho na kuzikwa!
Siku ya tatu ya mwezi wa pili tangu Beatrice apatwe na mkasa huo, alifumbua macho, kila mtu hakuamini kumwona Beatrice akiangalia tena.
"Linda lete faili la Invoice zote za Rwanda haraka!" Beatrice alisema baada ya kuzinduka akidhani alikuwa ofisini.
Mzee Rugakingira aliyekuwa jirani alimshika na kumtuliza kitandani alipotaka kunyanyuka ili akae.
"...Wewe mtoto tulia Mungu amekusaidia," alimwambia mwanaye. Watu wote waliokuwepo pembeni mwa kitanda walipiga magoti na kusali wakimshukuru Mungu, kwani hakuna aliyetegemea kuwa Beatrice angeweza kufumbua macho tena. Kila mtu alishakata tamaa.
Pamoja na Beatrice kuamka hakuwa na kumbukumbu yoyote juu ya yaliyompata, wala hakukumbuka alikuwa nani! Hakuwakumbuka hata baba na mama yake, sekretari wake, Linda na hata Violeth wifi yake, watu waliokuwa karibu naye sana katika maisha.
Jambo hili liliwashangaza wote ikabidi wamuombe mzee Rugakingira amuulize daktari.
"Mzee, kilichompata Beatrice ni mshtuko mkubwa wa ubongo kutokana na majeraha makubwa aliyoyapata kichwani ambayo yalisababisha vituo vya kumbukumbu kutikisika na kufuta kumbukumbu zote! Hivyo, tunategemea Beatrice atakuwa katika hali hii kwa muda mrefu lakini ipo siku kumbukumbu zake zote zitarejea."
"Kweli?"
"Ndiyo baba, ingawa itachukua muda kidogo! Cha kushukuru Beatrice yuko hai tena."
Kila siku mamia ya watu waliompenda Beatrice walimiminika kwenda kumwona hospitali ya Bugando, wengine walimpelekea chakula, kadi na vinywaji. Kwa sababu ya chanzo cha tatizo la Beatrice, ilibidi chakula na vinywaji vyote alivyoletewa vipimwe kabla hajapewa ili kuhakikisha usalama wake.
***
Ilikuwa ni asubuhi na mapema siku ya Jumatatu zikiwa ni siku kumi na tano tu tangu Beatrice arejewe na fahamu zake. Wauguzi walikuwa wakisafisha wodi, ghafla mmoja wao aliona kikaratasi kidogo chini ya kitanda cha Beatrice.
Alijikuta akitamani kukiokota ili akisome. Kiliandikwa kwa wino mwekundu, maandishi yaliyokuwa katika kikaratasi hicho yalimtisha sana na kumfanya awaite wauguzi wenzake waje mbio karibu na kitanda cha Beatrice.
"Vipi?"
"Jamani huu ujumbe ni nani ameuweka hapa chini ya kitanda cha Beatrice?"
"Sijui kwani unasemaje ujumbe wenyewe?"
"Aisee unatisha!"
"Kwani unasemaje?"
Wote walisogeleana na kuanza kuisoma kwa pamoja kila mmoja wao akitetemeka na kushindwa kuelewa uliandikwa na kuletwa wodini na nani?
“Pamoja na kuwa umepona sijakata tamaa ni lazima ufe tu. Nimedhamiria kukuua na ni lazima utakufa hata kama ungefanya kitu gani kujilinda.
Ni mimi adui yako.”
Yalikuwa maneno machache lakini ya kuogofya. Wauguzi walikipeleka kikaratasi hicho ofisini kwa muuguzi mkuu na tangu siku hiyo watu wa ajabuajabu walianza kuonekana kumtembelea Beatrice katika muda wa kuwaona wagonjwa. Madaktari na masista walipokaa na ndugu wa Beatrice waliamua kwa kauli moja kumhamisha Beatrice wodini kumpeleka mahali kulikokuwa na usalama zaidi.
Usiku wa manane siku iliyofuata, chini ya ulinzi mkali, masista walimbeba Beatrice kumpeleka kwenye nyumba yao ya utawa ambako walimpa chumba maalumu alikoendelea kulala na kupata matibabu yake.
Ni yeye tu aliyeishi katika nyumba hiyo asiye mtawa, hakuna mtu aliyejua Beatrice alikuwa wapi, hata ndugu na marafiki pia hawakuelewa jambo hilo.
Kwa pesa za Beatrice, nyumbani kwa masista, palilindwa usiku na mchana.
"Lakini kwa nini wanataka kumuua msichana huyu?"
"Hata mimi nashindwa kuelewa!"
"Yaani pamoja na kumjeruhi na pia kuiharibu sura yake kiasi hiki bado wanataka kumuua tu?"
"Lakini kwa hapa kwetu kidogo kuna usalama kulinganisha na ulinzi ambao ndugu zake wameweka hapa nje!"
Yalikuwa ni maongezi kati ya sista Florentina na Agnes waliokuwa watawa viongozi wa nyumba hiyo, kila mmoja alionekana kumuonea huruma sana Beatrice.
Je nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 23

Mpaka miezi sita baadaye Beatrice alikuwa bado akiishi katika nyumba ya masista. Hali yake haikuwa mbaya, kilichomsumbua ni kidonda kilichokuwa puani kwake, hicho kiligoma kabisa kupona lakini pamoja na hayo yote Beatrice alikuwa na uwezo wa kufanya hata kazi ndogondogo.
Kila siku asubuhi alifanya kazi ya kumwagilia bustani ya maua ya jumba la masista, alipazoea sana mahali hapo na kuona ndipo palikuwa nyumbani kwao! Hakukumbuka kitu kingine chochote katika maisha yake, hakuelewa alikotoka na hakukumbuka hata alikuwa nani.
Kwa jinsi alivyovalishwa na masista, ilikuwa si rahisi kumtofautisha nao kwani alifungwa kilemba cheupe kichwani na kuvalishwa gauni kubwa jeupe na miwani mikubwa iliyofanana na miwani ya macho ingawa haikuwa hivyo.
Yote hayo yalifanyika ili kufanya isijulikane kuwa Beatrice alikuwa ndani ya nyumba ya masista. Ilikuwa ni siri kubwa hata wageni waliotembelea jumba hilo hawakuelewa kuwa Beatrice alikuwa pale.
Lilikuwa ni jambo la ajabu sana binadamu kupoteza kumbukumbu zake lakini huo ndio ulikuwa ukweli. Beatrice hakuwa na kumbukumbu yoyote ile juu ya yaliyotokea maishani mwake.
Mapanga aliyokatwakatwa kichwani yaliziharibu kumbukumbu zake zote kichwani. Kumbukumbu zake zote za nyuma zilipotea, kila alipoangalia mwili wake uliojaa makovu alishindwa kuelewa ni kitu gani hasa kilifanya awe hivyo.
Aligundua wazi hakuwa kawaida lakini hakuelewa tofauti hiyo ilitokana na nini. Kila siku masista walijaribu kuzipima kumbukumbu zake ili kuona kama angeweza kukumbuka lakini mabadiliko hayakuwepo.
"Mimi naitwa sista Floretina, wewe mwenzangu jina lako nani?" Hilo ndilo lilikuwa swali la mtego ambalo masista walimuuliza Beatrice kila siku asubuhi kuona kama kumbukumu zake zilikuwa zimerudi.
"Mimi? Jina languuuuuu! Sijui nani vile?" Hakuwa na kumbukumbu ya jina lake, si hilo tu bali hata utajiri aliokuwa nao! Alimtia huruma kila mtu aliyemwona, sura yake ilibadilika mno.
Beatrice hakuwa mzuri kama alivyokuwa awali, uso wake ulijaa makovu makubwa na hakuwa na masikio wala pua! Vyote vilikatwa na majambazi waliomvamia nyumbani kwake.
Vidonda vyote mwilini mwake vilipona kasoro kidonda kimoja kilichokuwa puani, hicho ndicho kilimpa mateso kila siku! Nacho pia hakuweza kuelewa kilitokana na nini.
"Sista hivi kwa nini kidonda changu hakiponi? Na nilikuwaje? Mbona mimi sikumbuki kuanguka?" Mara kwa mara Beatrice alimsumbua sista Florentina kwa swali hilo.
"Kilitokea tu na kitapona hivi karibuni, usiwe na wasiwasi! Niambie kwanza jina lako nani?"
"Jina langu?"
"Ndiyo!"
"Mmmmmh! Naitw.aa.aaa...B!" Alisema huku akijikuna kichwani, kichwa chake kilionekana kuwa tupu kabisa, ilikuwa ni kama kompyuta mbovu inayowaka na kuzimika yenyewe!
***
Taarifa kuwa Beatrice hakufa baada ya uvamizi wa majambazi aliowatuma zilimtia hasira kali sana Angelina na kulazimika kupanga mauaji mengine. Alilazimika kuwatafuta vijana wake wa kazi na kuwaahidi pesa nyingi zaidi ili wamuue akiwa wodini!
Kwa miezi miwili majaribio kadhaa ya kumuua yalifanyika bila mafanikio, na hatimaye taarifa za mpango huo zilivuja baada ya mmoja wa majambazi aliyemwonea huruma Beatrice kutoa taarifa hizo kwa uongozi wa hospitali. Siku chache baada ya kipande cha karatasi kiliokotwa chini ya kitanda cha Beatrice kilichoandikwa maneno ya kutisha kumuua.
Ndipo masista walipoamua kumhamisha Beatrice kwa siri kutoka wodini kumpeleka katika jumba lao lililokuwa jirani tu na hospitali.
Lilikuwa ni jengo la masista wa Roho Mtakatifu wa Bwana, ambao hawakutakiwa kutoka nje wala kuonana na watu maishani mwao. Walikuwa ni wana maombi na sala kila siku, waliiombea dunia ipate msamaha kwa Mungu!
Usiku na mchana waliishi ndani ya vyumba wakisali. Ni masista wawili tu walioruhusiwa kutoka nje ya jengo hilo, hao walikuwa viongozi wao, sista Florentina na sista Agnes.
Majambazi walimtafuta kwa muda mrefu bila kujua mahali alikofichwa. Hakuna hata mmoja kati yao aliyehisi Beatrice angeweza kuwa ndani ya jengo la masista.
Walifanya kila aina ya upelelezi ili waweze kujua alipo bila mafanikio yoyote. Waliamini wazazi wake walimtorosha na kumpeleka Bukoba lakini upelelezi wao mjini Bukoba na mkoa mzima wa Kagera haukuonyesha hivyo! Walizidi kuchanganyikiwa.
"Nitamuua tu ni lazima afe! Hata kama watamficha wapi?" hayo ndiyo yalikuwa maneno ya Angelina kila siku.
Upande mmoja wa Angelina ulikuwa ni wa ukatili, na huu aliutumia kwa siri kubwa. Upande wake wa pili baada ya kutoka gerezani, aliutumia kujifanya mwanamke msamaria mwema na muungwana, aliyekuwa tayari kuutumia utajiri wake wote kusaidia wenye shida.
Kila mwaka alitumia kiasi kikubwa sana cha fedha kusaidia watu wenye matatizo. Hilo lilimpa heshima kubwa sana katika jamii kiasi kwamba ilikuwa si rahisi kwa mtu yeyote kuamini kuwa Angelina alikuwa muuaji.
Alikuwa miongoni mwa watu waliolisaidia sana jumba la masista kwa chakula na mambo mengine mengi. Alitenga kiasi kikubwa cha pesa kuwasaidia masista wa Roho Mtakatifu na walimheshimu kutokana na msaada wake, bila kuelewa alikuwa ni mtu mnyama kuliko Hltler. Laiti wangejua wasingeipokea misaada yake.
***
Jiji la Dar es Salaam lilikuwa na joto kali sana siku hiyo. Ilikuwa ni siku ya Jumapili jioni, watu walikuwa katika hekaheka za mwisho wa wiki.
Angelina alikuwa nyumbani kwake akiwa amepumzika, kichwa chake kilijaa mawazo alifikiria ni kwa njia gani angeweza kumuua Beatrice. Ilikuwa ni lazima Beatrice afe kwa sababu kuu mbili.
Ya kwanza ikiwa ni kulipiza kisasi baada ya kushindwa kudhulumu mali zilizoachwa na marehemu kaka yake, ya pili ilikuwa ni kuficha siri ya majambazi aliowatuma kwenda kumuua!
Alijua wazi kama Beatrice angepona na kurejewa na fahamu zake vizuri angetoboa siri na kumtia Angelina matatani, kitu ambacho hakutaka kabisa kitokee kwa sababu aliheshimiwa mno na jamii.
Akiwa katika mawazo hayo ghafla simu yake iliita.
"Hallow!" Ilikuwa ni sauti ya sista Florentina akiongea kutoka Mwanza.
"Tumsifu Yesu Kristu sista?" Angelina alimsalimia sista kama alivyozoea siku zote.
"Milele amina!" Sista alijibu salamu hiyo.
"Ndiyo…ndiyo...sista unasemaje leo? Kuna matatizo yoyote?"
"Hakuna matatizo yoyote ila kuna jambo nataka kukueleza, kifupi tunahitaji ushauri wako."
"Jambo gani sista?"
"Kuna msichana ambaye alivamiwa na majambazi kama miezi saba iliyopita na kulazwa hospitali ya Bugando, majambazi walimkatakata vibaya mno na kumtoa hata baadhi ya viungo vyake lakini kwa uwezo wa Mungu amepona!
“Cha kushangaza hao majambazi bado wanataka kumuua na wameshamtumia kikaratasi cha kutishia kufanya hivyo, tulichofanya ni kumtorosha na kuja kumficha hapa kwenye jumba letu."
"Mnaye?" Aiuliza Angelina kwa mshangao.
"Ndiyo tunaye."
"Kweli?"
"Kwa nini nikudanganye?"
Angelina hakuyaamini masikio yake kuwa aliyoyasikia yalikuwa sahihi lakini sista Florentina alizidi kusisitiza jambo hilo na kumwomba Angelina afanye kila awezalo kuwasaidia masista kumhamisha msichana huyo kwa siri kumpeleka Dar es Salaam.
"Nitakupigia kesho sista juu ya mpango nitakaokuwa nimeuandaa! Usiwe na wasiwasi nitawasaidia tu," alisema Angelina na kukata simu.
Bila kuchelewa alinyanyua simu haraka na kuwapigia vijana wake waliokuwa Mwanza kutekeleza mpango wa mauaji, aliwataarifu juu ya mahali alikofichwa Beatrice.
"Yuko kwenye jumba la masista."
"Lipi?"
"La masista wa Roho Mtakatifu."
"Wale wasioonana na watu?"
"Ndiyo!"
"Tutaingiaje huko ndani?"
"Hiyo mimi sio kazi yangu, ninachojua ni kupatikana kwa Beatrice na sitaki mmuulie hapo Mwanza, nataka atekwe na muondoke naye hadi Nairobi ambako nitakuwa nimeshamtaarifu mfanyabiashara mwenzangu aitwaye Njoroge. Huyo atawasaidia kila kitu!
Mtamuua, na hakuna hata mtu mmoja atakayefahamu na wala mfupa wake hautaonekana.
"Sawa mama, basi tupe muda tupange na wenzangu jinsi ya kufanya."
"Muda gani niwape?"
"Saa mbili"
"Oke, nitapiga baada ya muda huo lakini nataka utekaji ufanyike leo hiihii."
Dakika mbili baadaye Angelina alikuwa kwenye simu akiongea na William Njoroge, mfanyabiashara maarufu mjini Nairobi na kumweleza mpango wote aliokuwa nao. Alihakikishiwa kila aina ya msaada na kufurahi sana. Aliwapigia tena vijana wake mjini Mwanza akitaka kujua ni wapi walikuwa wamefikia.
"Mama usiwe na wasiwasi kazi itafanyika! Tayari tumeshapanga mkakati wa kazi, hivi sasa mafundi wanashona mavazi kama ya masista."
"Ya nini?"
"Tutavaa tufanane nao, kisha tutakwenda kwenye jumba lao kama wageni, tukishaingia ndani ya jengo lao risasi zitaanza kulia na tutawaamuru masista wote walale chini, ni hapo ndipo tutakapomteka Beatrice na kuondoka naye.”
"Mtafanya usiku, sio?"
"Hapana, hii inafanyika saa tisa mchana! Tukifanya usiku watatushtukia!"
"Sawa lakini msije mkaua sista yeyote, hiyo ni dhambi kubwa sana."
Je nini kitaendelea?
Je Beatrice ataweza kutekwa?
Tukutane siku ya Ijumaa mahali hapa.
 
SEHEMU YA 24

Masista walikuwa wameketi sebuleni ndani ya jengo lao baada ya chakula cha mchana. Ilikuwa tayari imetimu saa 8:30 mchana, Beatrice alikuwa miongoni mwao na akicheka pamoja nao! Alifanana kabisa na masista kwa kila kitu, kumbukumbu zilikuwa bado ni tatizo kwake, bado hakuelewa kitu chochote kuhusu maisha yake.
Masista walimsikitikia na kumwonea huruma, walijua alikuwa msichana tajiri kiasi gani ambaye kwa hakika wakati huo alitakiwa awe kwenye shughuli zake za biashara akiendesha makampuni yake. Alikuwa ni mwanamke tajiri pengine kuliko mwanamke mwingine yeyote katika Afrika Mashariki.
"Hivi tutafanya kitu gani ili huyu binti arejewe na kumbukumbu zake? Maana sasa karibu miezi minane tangu apatwe na matatizo yake."
"Daktari alisema ipo siku kumbukumbu zake zitarejea ingawa inaweza kuchukua muda mrefu kidogo."
Waliendelea kuongea mambo mengi pamoja na baadaye ilipotimu saa 9:00 alasiri waliingia katika chumba cha maombi na kuanza kusali.
Dakika mbili tu tangu waanze sala hizo, gari aina ya Range Rover jeusi liliegesha mbele ya jengo la masista, liliendeshwa na kijana mweusi mrefu aliyevaa suti ya rangi ya kijivu.
Katika kiti cha nyuma cha gari hilo, walikaa watu watatu wakiwa wamejifunika nyuso zao kwa vitambaa vyeupe, kichwani walikuwa na vilemba vyeupe na walivalia magauni makubwa ya rangi hiyohiyo.
Maaskari waliolinda jengo la masista walilizunguka gari hilo na kuanza kumhoji dereva maswali mbalimbali ya kiusalama.
"Vipi mzee?"
"Hakuna tatizo nimewaleta hawa masista."
"Masista gani?"
"Masista wa Mtakatifu Marietha kutoka Nakuru Kenya, wapo safarini kuelekea Rwanda na wamependa kupita hapa kuwasalimia masista wenzao!"
"Hakuna tatizo," alijibu askari mwenye bunduki mkononi, na hilo ndilo kosa pekee kubwa alilofanya. Alitakiwa kumuuliza kwanza sista Florentina juu ya ujio wa wageni hao lakini hakufanya hivyo badala yake alifungua lango na gari likaingia moja kwa moja hadi uani mwa jengo la masista.
Sista Florentina na wenzake wakati huo walikuwa katikati ya maombi.
"Wako wapi masista?" Dereva alimuuliza mlinzi.
"Wako kwenye maombi."
"Masista wanauliza chumba gani ili waungane nao?"
"Wapo kwenye hicho chumba kilichoandikwa 26D."
"Sawa, basi wewe unaweza kuendelea na shughuli zako sisi tutawasubiri."
"Sawa!" Alijibu mlinzi na kutoka hadi nje ambako yeye na wenzake waliendelea na kazi ya kuhakikisha kuna usalama kwenye jumba la masista.
Alipoondoka tu majambazi wakiwa ndani ya mavazi ya kitawa walishuka garini na kwenda moja kwa moja hadi kwenye chumba walichoelekezwa. Ndani ya mavazi yao kila mmoja alikuwa na bunduki aina ya SMG tayari kwa kazi.
Waliusukuma mlango na kuingia hadi ndani na kukuta masista wamesujudu wakisali.
"Wote mko chini ya ulinzi, atakayefanya fujo au kupiga kelele atauawa ingawa tumekatazwa kuwaua!" Alisema mmoja wa majambazi kwa sauti ya tahadhari lakini masista hawakuonyesha kushtuka wala kukatisha maombi yao.
Waliendelea kusali mpaka wakamaliza sala yao. Walikuwa masista zaidi ya ishirini, na wote wakawa chini ya mtutu wa bunduki. Walifungwa kamba na kujazwa matambara mdomoni kisha majambazi wakamchagua Beatrice peke yake na kuanza kumvuta kutoka naye nje akiwa amefunikwa mdomo kwa kiganja ili asipige kelele.
Walimtambua kwa alama walizopewa hasa kidonda kilichokuwa puani. Nje walimpakia kwenye gari na taratibu walianza kuondoka na kuwaacha masista wakiwa wamefungwa kamba ndani ya chumba cha maombi.
Walinzi walifungua lango na majambazi waliwapungia mkono na kuondoka kwa kasi. Hakuna mlinzi hata mmoja aliyeelewa kilichotokea.
Walikuja kugundua saa nne baadaye, mpishi alipoivisha chakula cha usiku na kwenda vyumbani kwa masista kuwapa taarifa.
Alishangaa kutomkuta hata sista mmoja chumbani lakini alipoingia katika chumba cha maombi aliwakuta masista wote wamelala chini wakiwa wamefungwa kamba na kujazwa matambara mdomoni.
Alipiga kelele akiwaita walinzi na walipokuja waliamini waliowakaribisha hawakuwa masista bali majambazi. Hawakutaka kupoteza muda waliwafungua masista kamba na haraka waliwakimbiza hospitali ya Bugando ambako walipewa matibabu.
Taarifa zilitolewa polisi lakini zilichelewa kwani wakati huo tayari majambazi walikuwa wakivuka mpaka kuingia Esbania nchini Kenya.
Beatrice alikuwa amefungiwa nyuma ya gari na majambazi walikaa viti vya mbele. Nia yao ilikuwa ni kufika Nairobi siku hiyohiyo na kukamilisha mauaji hayo.
Walipotoka mpakani gari liliendeshwa kwa mwendo wa kasi ya kilometa 250 kwa saa! Ulikuwa ni mwendo wa kasi mno ukizingatia usiku ulishaingia lakini dereva hakujali na wote walifurahia kuikamilisha kazi hiyo kwani walijua malipo yao yalikuwa makubwa mno wakirejea Dar es Salaam baada ya kumuua Beatrice.
Hilo ndilo jambo pekee lililokuwa limebaki.
Kilometa kama tano hivi baada ya kuiacha Esbania, ghafla bila kutegemea dereva aliliona lori kubwa likiwa limeegeshwa katikati ya barabara. Lilikuwa mita kama 50 kutoka mahali gari lao lilipokuwa!
Kwa kasi waliyokuwa nayo, dereva alijua wazi hiyo ilikuwa ni ajali. Alijaribu kukanyaga breki ili lisimame lakini haikuwezekana. Lilijivuta na kwenda moja kwa moja na kuligonga lori kwa nyuma, sehemu ya mbele ya gari lao ilijikunja na kurudi ndani ikiwakandamiza majambazi wote na kuwaua palepale!
Kumfungia Beatrice ndani ya gari kulisaidia sana kuokoa maisha yake! Hakuuumia wala kuchubuka mahali popote zaidi ya mtikisiko mkubwa uliompata. Alifungua mlango kwa haraka na kutoka nje na kuanza kukimbia kuelekea porini ambako alitafuta mahali pazuri chini ya mti na kulala.
Kulipokucha asubuhi alitembea na kuelekea hadi kijijini ambako alikuta watu wakiongelea sana ajali iliyotokea.
"Ajali gani hiyo?" Alijiuliza Beatrice, tayari alishapoteza kumbukumbu juu ya yaliyotokea. Huo ulikuwa utaratibu wa ubongo wake tangu akatwekatwe mapanga, haukutunza kumbukumbu kwa muda mrefu.
Siku hiyohiyo alitembea kwa miguu kurudi hadi mpakani Esbania ambako aliendelea kuishi akirandaranda mitaani. Alionekana kama mwendawazimu na hakuna mtu aliyefahamu ni wapi alikotokea.
Baadhi ya watu walihisi alikuwa ni mkimbizi wa Rwanda aliyenusurika katika vita vya kikabila na kukimbilia nchini Kenya. Walifikiria hivyo sababu ya majeraha aliyokuwa nayo usoni! Hata hivyo, walipokisikia Kiswahili chake waliyafuta mawazo hayo na kugundua alikuwa Mtanzania.
Kwa muda mrefu aliendelea kuishi hapo mpakani kama mwendawazimu. Ndugu zake pamoja na masista walishamtafuta kwa muda mrefu bila mafanikio. Hatimaye wakaamua kupitisha kuwa Beatrice alikuwa marehemu, wakakaa matanga ya siku tatu wakimlilia mtoto wao.
Kupotea kwa Beatrice kulikuwa ni pigo kubwa pia kwa familia ya marehemu mume wake, Mike! Alikuwa tegemeo lao kwa vitu vingi hasa uendeshaji wa miradi iliyoachwa na marehemu mtoto wao.
Je nini kitaendelea?
Je Beatrice ataweza kupatikana?
 
SEHEMU YA 25

Miezi mitatu baadaye, siku moja akiwa Esbania akitoka msituni kukusanya kuni kwa ajili ya kubadilishana na chakula hotelini -- kazi aliyokuwa anaifanya ili aweze kuishi kwa sababu hakuwa na pesa -- ghafla aliliona lori kubwa lenye tela likiwa limeegeshwa kandokando ya barabara ya kuelekea Nairobi. Alipolisoma ubavuni aligundua lilikuwa limeandikwa maandishi makubwa ya MIKE TRANSPORTERS LTD!
‘Mmh! Hili jina mbona kama nalifahamu? Hiki ni kitu ninachokifahamu kabisa, ni nini hiki?’ Alijiuliza Beatrice na kuutupa mzigo wake wa kuni na kuanza kukimbia kwenda kwenye mlango wa dereva wa gari hilo.
"Aaah! Mama!" alipiga kelele dereva wa gari hilo na kuruka hadi chini ambako alimkumbatia Beatrice na kuanguka naye hadi chini. Badala ya kufurahi, Beatrice alionyesha mshangao! Hakumkumbuka kijana huyo.
"Malik! Malik! Malik! Njoo umwone Beatrice huyo hapa bado yuko hai!" Dereva alipiga kelele akimwita utingo wake.
"Ndiy...ndiy...ndiyo! Nimekumbuka jina langu naitwa Beatrice! Ndiyo Beatrice Rugakingira, lakini mbona simwelewi anachokisema mtu huyu!" Aliwaza Beatrice.
Kitendo cha kumkumbatia kiliwafanya watu wengi washtuke na kwenda hadi eneo alilosimama Beatrice, dereva pamoja na utingo wake na kutaka kujua kilichotokea.
Walieleza kila kitu na watu wote walishangaa! Beatrice aliyasikia maneno yote na kumbukumbu zake zilianza kurejea polepole, hatua kwa hatua.
"Sasa mtafanya nini?" Aliuliza mama mmoja miongoni mwa watu waliokusanyika.
"Hatuna la kufanya zaidi ya kumrudisha nyumbani, itabidi tuondoke naye kwa sababu hata sisi tunakwenda Mwanza. Watu watashangaa sana kumwona Beatrice akiwa hai tena," alisema dereva.
Siku hiyohiyo walimpakia Beatrice ndani ya gari lao na kuondoka naye. Iliwachukua saa nne kuingia mjini Mwanza!
Njiani walijaribu kumuuliza Beatrice mambo mengi juu ya mahali alikokuwa lakini hakutoa ushirikiano mzuri ambapo waligundua kwamba hakuwa na kumbukumbu vizuri na hata hakukumbuka kuwa ni yeye aliyewapa ajira. Hawakutaka kwenda moja kwa moja nyumbani kwake, badala yake walinyoosha kuelekea ofisini kwake mtaa wa Nkrumah.
Kwenye makutano ya Barabara ya Kenyatta na Posta walikata kulia na kuingia Barabara ya Posta kuelekea Barabara ya Nyerere.
Ghafla alishtuka na kukaza macho yake na kuangalia pembeni.
‘Mh! Hapa napafahamu mara nyingi nilikuja hapa kuongea na rafiki zangu,’ aliendelea kuwaza Beatrice alipoliona jengo la Hoteli ya Mwanza.
“Hapa ni Mwanza, aisee hivi kumbe nipo Mwanza?!” Beatrice alimwambia dereva.
Baadaye waliingia Barabara ya Nkrumah, mbele kidogo Beatrice alipiga kelele akimwomba dereva asimamishe gari.
"Hallo! Hallo! Hebu simama! Kuna kitu nimekiona hapo!"
Dereva alielewa, alisimamisha gari na Beatrice akafungua mlango na kushuka kwa haraka na kuanguka chini! Alikuwa ameona jengo lililoandikwa MIKE TRANSPOTERS LTD, ilikuwa ni kampuni yake mwenyewe.
"Nilishawahi kuingia katika jengo hili mara nyingi," alisema Beatrice baada ya kunyanyuka chini. Tayari watu walishajaa na hawakuamini kuwa msichana waliyemwona alikuwa Beatrice. Wengi walijua alishakufa, walimwonea huruma kwa jinsi alivyokuwa amebadilika sura yake.
"Masikini Beatrice ndio amekuwa hivi?" Alisema dada mmoja na Beatrice aliyasikia maneno hayo.
Dereva na utingo walimshika Beatrice mkono na kuanza kuvuka naye barabara kwenda kwenye ofisi ya MIKE TRANSPORTERS LTD huku kundi kubwa la watu likiwafuata nyuma! Alipoingia tu ndani, macho yake yalitua usoni kwa Linda.
"Ah! Jamani Linda!" Alipiga kelele Beatrice baada ya kumwona sektretari wake wa siku nyingi.
"Ah! bosi karibu sana!"
“Hivi mimi ni bosi? Bosi wa nani?” Aliwaza Beatrice na ghafla kumbukumbu zote zilimrejea akaanza kulia na kupiga kelele akitaka kukimbia kwenda nje.
"Haooooo! Haooooo! Wananiua! Hao wanataka kunikatakata, hao, wametumwa na wifi yangu Angelina, jamani majambazi hao nisaidieni!"
Kumbukumbu za tukio la usiku alipokatwakatwa kwa mapanga zilimiminika kama filamu kichwani mwake. Beatrice alianguka chini na kuzimia, ikabidi yaletwe maji amwagiwe na baadaye daktari alipigiwa simu na kufika katika muda wa dakika kumi na kukuta Beatrice ameshazinduka.
"Amezinduka?"
"Ndiyo!" alijibu Linda.
"Basi mwacheni apumzike."
"Sawa."
Aliachwa kwa saa nzima lakini muda wote huo alilia na kutetemeka kwa hofu. Picha iliyokuwa ikija kichwani mwake ilimtisha sana! Kutajwa kwa Angelina kuwa ndiye aliyewatuma majambazi kuja kumkatakata mapanga, kuliwafanya wakazi wa mji wa Mwanza kutoa taarifa polisi na maaskari wa upelelezi walikuja haraka hadi ofisini kwa Beatrice.
"Beatrice!" Daktari alimwita.
"Bee!"
"Hawa ni maaskari, wanataka uwaeleze ukweli juu ya jambo lililotokea."
"Sawa nitawaeleza."
Watu wote walikaa kimya kumsikiliza Beatrice akieleza kilichotokea mpaka kukatwakatwa mapanga kiasi hicho. Maaskari walikuwa wakichukua maelezo na waandishi wa habari pia walikuwepo wakirekodi kila kitu alichokisema.
Kilikuwa ni kitu cha kushangaza sana kwa mtu aliyeaminika kuwa mfu kuonekana tena! Watu wengi hasa wanawake walisikika wakilia nje ya ofisi sababu ya kumhurumia Beatrice.
"Jana nilikuwa nyumbani baada ya kutoka kanisani," alianza Beatrice akifikiri labda tukio hilo lilitokea siku moja kabla wakati ilishapita miezi mingi tangu tukio hilo litokee.
Alieleza kila kitu kilichotokea, jinsi majambazi walivyoingia na walivyomweleza kuwa walitumwa na Angelina ili wamuue.
"Niliwauliza wamepewa shilingi ngapi ili niwape zaidi lakini walikataa na kuanza kunikatakata kwa mapanga bila huruma mpaka nikapoteza fahamu kabisa!" alimaliza Beatrice na kuanza kulia.
Baada ya maongezi askari waliondoka hadi kituoni wakiwa na hasira kali dhidi ya Angelina na siku hiyohiyo mawasiliano yalifanyika kati ya Mwanza na Dar es Salaam.
Angelina alikamatwa na kupewa mateso makali kupita kiasi, alishindwa kuvumilia na kuwataja majambazi wote alioshirikiana nao kufanya unyama huo ambapo nao walitiwa mbaroni siku hiyohiyo jijini Dar es Salaam.
Walipofikishwa mahakamani ushahidi wa kutosha ulikuwepo na hawakuwa na jinsi ya kuruka, wote pamoja na Angelina mwenyewe walikiri kosa na kuhukumiwa kunyongwa.
***
Miezi mitatu baada ya hukumu ya Angelina na wenzake, hali ya Beatrice iliendelea vizuri, kumbukumbu zake zilikuwa sawa na aliendelea na kazi zake kama kawaida. Kilichomsikitisha kilikuwa ni sura yake!
Kwani kila alipojianglia katika kioo, roho ilimuuma sana, muda mwingi alilia kila alipoiangalia picha yake ya zamani aliyoibandika ofisini mwake na kuona tofauti iliyokuwepo kabla na baada ya kuvamiwa na majambazi.
Alipatwa na simanzi kubwa sana moyoni mwake, kwani vitu vingi vilimuumiza. Hakuweza tena kujiangalia kwenye kioo! Alikiogopa na alikiona ni adui yake, kila alikopita watu walimshangaa na kuonyeshana kwa vidole na alikuwa gumzo la kitu mtu mjini Mwanza na Tanzania nzima kwa ujumla.
Kasoro pekee iliyokuwepo katika mwili wake ni kidonda cha puani, hicho hakikukubali kabisa kupona! Kilizidi kuchimba kwenda ndani zaidi, hatimaye alijikuta amerudishwa tena hospitali na kulazwa. Alipewa matibabu kwa muda mrefu lakini kidonda hakikupona na hali yake ilizidi kudhoofika.
Hatimaye Beatrice alikufa kwa mateso makali lakini kabla ya kifo chake aligawa mali zake kama ifuatavyo: Asilimia 25 alitoa kwa wazazi wa Mike, asilimia 10 kwa sektretari wake Linda, asilimia 15 kwa wifi yake Violeth na asilimia 50 kwa watoto yatima wa UKIMWI na pia aliacha ujumbe kwa vijana wote duniani akisema kilichomponza yeye ni mapenzi na kutofikiria maisha ya baadaye.
“Nilimpenda Mike lakini sikutakiwa hata kidogo kumlazimisha alipokataa kunioa! Sikutakiwa kumlazimisha kwa sababu alishagundua kuwa ana virusi na mimi sikuwa navyo na simlaumu Mike kwa kitu chochote kilichotokea maishani mwangu.
Nawaonea huruma sana watu waliobaki duniani, wakubwa kwa wadogo, kwani ugonjwa huu si wa kuchezea. Ni vyema watu wakachukua hatua madhubuti kubadilika, dunia nzima ni lazima iungane katika vita hivi.
Kama hapatakuwa na ushirikiano hakuna atakayebaki hai si Mwingereza, Mmarekani, Muasia, Mwafrika au mtu yeyote yule. Ni lazima watu wote duniani waelewe kuwa wapo ndani ya mtumbwi mmoja unaopita katika bahari iliyochafuka!
Kama ukizama hakuna atakayedai yupo salama...” ilisema sehemu ya barua hiyo na Beatrice akawa amepumzika kwa amani!
MWISHO.
 
Nifah Divine... glory to yhwh BansenBurner Alisen Papushikashi Magazine Fire miss chagga SANCTUS ANACLETUS mngony Excel Mussolin5 Jimena Inferiority Complex gwijimimi wambura marwa Hoshea shareef conscious wambeke The Boss Deejay nasmile gkileo Juma chief Mangi flani hivi Ngongo makaveli10 KENZY kadada wa pili Root aretasludovick jonnie_vincy Clkey KAFA.cOm mbewe makedonia Afande Nyati peterchoka Leonard Robert Nchi Kavu STUNTER Chrizo jully Van persie Khalidoun Tetramelyz punje haradari Mazigazi @Alybaba babu na mjukuu platozoom jimmyfoxxgongo Nicodemas Tambo Mwikozi @Ls man Heaven Sent sifongo Infantry Soldier haa mym 20acres MTS MarkHilary compos Tembo2 Erick the future nancy1983 Bulah binsaad @Fazzaly the wolf everhurt Melvine Mgibeon kijana wa leo samsun Coolant Jagood pacesetter apologize payton George Betram kisengeli Kiranga Jiwe Linaloishi Madame B jay john Guasa Amboni Dinazarde Analyse Diva Beyonce snowhite Mmanu Expected Value onechromosome Missy rose Innocenthezron Immortal_MH Ficus sunola Robot la Matope mamaafacebook II JEKI likikima Compact scorpio me G'taxi YNWA adna yuzo ntamaholo Otorong'ong'o naan ngik-kundie kandukamo1 AFRICA101 mwalidebe Kobe Blaki Womani kalendi savius The Great Emanuel r2ga Ntaluke.N. Transcend Msemachochote Mchumiajuone mwampepec MTOTO WA KUKU Fukara proto cute kawombe zinginary MLALUKO JR Vupu barafu BlackPanther Ntuzu Matola impongo ntamaholo Mkoroshokigoli Deadbody KING easy mahoza Msolo kkenzki deborah1 KIDUDU buffalo44 winlicious riziki Allys MUHUNZI Moses2015 nacktary Liuumi dochivele Renzo @barbers hmjamii mbere TATIANA famicho LUCKDUBE mwanadome Straton memphis ghazar Graph Theory Honey Faith Shunie Slave ddcmanesto zinginary pacesetter Nkanaga KOMUGISHA mikatabafeki johnsonmgaya lee empire wigo MJINI CHAI Asprin mtzmweusi Erasto kalinga Chrizo kichakaa man LULU bike FORTALEZA poleni shibumi ZE DONE umande Edger Sr sir joshua sammoo Roram Password Bavaria hambiliki mwanangu Asili100 Evarist Massawe nice1 Jumong S Rogie 1babake nasreen uberito baest dustless Kilemachocho Tumosa mtembea kwa miguu debbs Joe scorpnose musacha shibumi seeker of knowledge Simuchi Veni Vidi Vici TUJITEGEMEE abuu garcia Hon Nkundwe Festo Festo marion09 mike2k The dream bro kay vandelintz kirikou1 POINT LOAD lusaka city Dirham Rodcones bato MANCNOO @multiphill90 GEORGE Dalali mwanamalundi90 MwaFreeca Roram Ta-kibombo troublemaker mambo KOMUGISHA calabocatz Papaa Azonto Msemachochote Mdomo bakuli tizo1 option dikembe iL Buono fakalava ABDUL KAREEM @Gobe Justine Marack Goodluck Mchika MR UNINFORMED darcity nkasoukumu nG'aMBu thatonegAl kabanga MPARE KIBOGOYO Edward Sambai Rassa mnonje srinavas last king of uscoch proto cute Kennedy krava Rais2020 kbosho Mzee wa BsN sam2000 fuma 999 Bableee dawa yenu The Certified DON SINYORI mij adden
bwii ONTARIO Kobe The Vein @Mondray jaxonjaxon successor mzee wa liver sawariya SITAKI ukuda Domhome Mpatanishi MKANDAHARI mtugani wa wapi huyo wealthier cluecell Toyota escudo mgumu2 troublemaker Linamo @shedede kamtu33 SteveMollel Ngushi DONALD stewart Mshuza2 Glycel mnonje Ochuanilove SingleFather Santi DEOD 360 Ngushi anatory antony ukhuty chris van chicha auxillius Goma Son Hubeb pes KING DUBU VILLAIN mwayena donbeny Aleppo JipuKubwa shoo61 BOMBAY John mungo Nyakageni bato Dogo 1 sufra chamlungu painscott wegman Bravo Engliash MOSELBAY wa stendi FaizaFoxy bigmind cadabraa Internal Kelvin mwalukas mnonje Kelvin X Somoche Wgr30 Miiku Poise Jabman kalamuyamwalimu BOMBAY the say juxhb witnessj Gide MK Mmanyema mgogoone Mnongane Mandingo koncho77 afsa ngaboru Paradoxer Heavy Metal KIMBURU 06 Raaj kichekoh ngumba njeche kikale DullahTza Goodluck Mshana julius Darcy Denis Kasekenya mashonga kitalembwa Khaleed Shaban middle east SirChief jiwe jeusi Mkambarani mansakankanmusa gambada ynwa ney kush
 
@owledge @Simuchi @Veni Vidi Vici @TUJITEGEMEE @abuu garcia @Hon Nkundwe @Festo Festo @marion09 @mike2k @The dream @bro kay @vandelintz @kirikou1 @POINT LOAD @lusaka city @Dirham @Rodcones @bato @MANCNOO @multiphill90 @GEORGE @Dalali @mwanamalundi90 @M
 
Back
Top Bottom