Hadithi: Mwendawazimu Aliyefufuka

Hadithi: Mwendawazimu Aliyefufuka

Kanungila Karim

JF-Expert Member
Joined
Apr 29, 2016
Posts
20,746
Reaction score
25,662
MWENDAWAZIMU2.jpg


MWANDISHI: ALLY AYUBU KATALAMBULA


GIZA nene na mvua kubwa iliyoambatana na upepo, haikumzuia wala kumpa rapsha kiumbe mmoja, mwanadamu, aliyekuwa amelala kifudifudi, ametulia tuli kwenye tawi la mti mkubwa ulio katikati ya miti mingi ndani ya msitu wa Goma nchini Kongo.



Kifuani mwa kiumbe huyo alikuwa amekumbatia bunduki aina ya ‘sniper rifle SVU’ ya masafa marefu. Jicho lake moja alikuwa amelifumba wakati jingine likichungulia kwa makini katika darubini yenye nguvu ya kuona mbali iliyokuwa katika bunduki hiyo kutoka nchi ya Urusi.



Mwanaume huyo wa miraba minne, alijituliza kwenye mtutu wa bunduki yake pasina kutikisika wala kupepesa kope la jicho lake. Kidole chake cha mkono wa kuume kilishika kifyatulio cha risasi, kidole hicho kikiwa tayari kufyatua muda wowote pale kitakapo agizwa kufanya hivyo.



Ingawa kulikuwa na giza nene na mvua kubwa ya upepo, hata hivyo kiona mbali cha bunduki ya ‘rifle SVU’ kiliweza kumwonesha mmiliki wake picha nzuri ya kung’aa, mahali popote alipotaka.

Jamaa huyo, alikuwa amevaa mavazi ya kiraia. Alikuwa kwenye shati kubwa jeusi na jinsi ya kaki iliyotapakaa tope, miguuni mwa kiumbe huyo alivaa viatu, ‘katambunga’ za Kimasai.



Alikuwa ni mpiganaji, askari wa msituni, Muasi, mwenye shani ya udunguaji. Apiganaye dhidi ya serikali yake, serikali aliyoamini imewasaliti wanyonge na kuwadhulumu wenye haki, waliamini keki yao ya nchi. Ilikimbizwa mlango wa nyuma na kuliwa na wajanja wachache.



Yeye na kundi lake (wapiganaji wenziye) walijitolea maisha yao, ikiwezekana hata kufa, lakini rais aliyekuwa madarakani ang’oke na serikali yake yote halafu wao waunde serikali yao, ambayo waliamini itakuwa ni serikali yenye siasa safi, haki na usawa kwa watu wote, masikini na matajiri. Watoto kwa wakubwa, wake kwa waume.



Lakini hadi kufika huko, mwanaume huyu na wenziye, waliamini ilikuwa ni lazima wajitoe kwa ajili ya kizazi chao. Ndio! Pamoja na wasiwasi juu ya mauti aliyonayo binadamu, lakini kwa mwanaume huyu, hawakuona njia nyingine ya kuikomboa jamii yao zaidi ya kuziweka rehani roho zao.

Akiwa pale katika tawi la mti, mdunguaji huyo alikuwa akiwaza kwamba:



Hatua za kulifikia kaburi lake zipo karibu mno, nukta yoyote anaweza kuwa maiti na mwili wake kuliwa na fisi kama inavyotokea kwa wenziye waliokwisha kufa.

Walikuwa wakiuawa kila siku dhidi ya Majeshi ya Serikali na yale ya Umoja wa Mataifa. Jeshi lao lilikuwa likipungua kwa kasi, hata hivyo, fikra za kurudi nyuma hazikuwepo kichwani mwao, walikuwa tayari kupambana hadi tone la mwisho la damu.



Sababu za kupigana zilikuwa ni nzito na zenye maana kubwa nafsini mwao. Aliamini akifa kwa ajili ya kizazi chake ni kifo cha heshima kuliko kufa kwa Malaria kitandani.

Kufa akiwa anapigania maslahi ya taifa lake ilikuwa ni jambo alilolipa nafasi kubwa kuliko uhai wake. Alifundishwa somo hilo tangu akiwa mdogo na somo likamwingia.



Uzalendo ulikuwa umetamalaki kifuani mwake, chuki dhidi ya wanajeshi wateteao serikali ya rais aliye madarakani kwa kivuli cha ‘walinda amani’ ilimuudhi mno moyoni.

Aliapa kumuua yeyote atakayeonekana kwenye ardhi ya Kongo akijitia kulinda amani.

“Nitaua” alinong’ona kimoyomoyo.

Matone ya mvua yalikuwa yakidondoka kwa nguvu na kujipigiza ardhini. Muanguko wa matone hayo alikuwa ameyaweka akilini kadiri mvua ilivyokuwa ikinyesha.

Katikati ya utulivu aliojitengenezea, ghafla aligutuka baada ya kusikia utofauti wa muanguko wa matone ya mvua. Akatega sikio na kujipa utulivu zaidi.



Naam! Akaisikia chakarachakara ijongeayo kwa kunyata. Mnyato huo ndio uliokuwa unaharibu mwenendo wa muanguko wa matone ya mvua chini ya mti ule.

Aliongeza umakini. Akatizama kila upande kupitia darubini iliyokuwa kwenye bunduki yake ya kijeshi. Lakini wapi! Hakufanikiwa kuona chochote. Mwanaume akachakarika. Mjongeo wa chakarachakara unatokea wapi?

Akageuza bunduki yake, upande wa nyuma. Hatimaye akafanikiwa kuona kitu. Ni mita kama mia moja, kulikuwa na kichaka kidogo kinacho tembea!.



“Lakini!!… lakini!!..lakini!!.. ni mbali, minyato hii iko karibu” Jamaa alinong’ona. Uso wake ulikuwa umesawijika kwa mashaka na wasiwasi.

Ni kweli. Umbali mdogo kulikuwa na kichaka kinachotembea. Yamkini alikuwa ni moja ya maadui zao, ambao wamekuwa wakiwindana kwenye misitu hiyo kila siku.

Hata hivyo, adui huyo alikuwa mbali. Minyato yake isingeweza kusikika kutokea pale alipo. Mtu aliyekuwa akimnyatia hakuwa mbali naye, alikuwa jirani mno. Huyu ni hatari zaidi. Yuko wapi?

Akahaha huku na kule kuangalia kupitia bunduki ya rifle SVU. Lakini wapi!



Sauti moja kichwani ikamwambia: Tizama chini ya mti huu. Akatupa jicho kule chini.

Lahaulaaa!! Hakuamini alichokiona.

Kulikuwa na mwanamke, ama binti mmoja aliyekuwa amebana nyuma ya mti huku akijisuka kujibanza kwenye mti huo. Alionekana ni kama anayekimbia maadui fulani. Uso wake ulijawa na hofu.

Mdunguaji wa juu ya mti, akiwa katika taharuki ya kuangalia kioja hicho chini ya mti aliokuwa amebana juu yake. Nukta ile ile, mara kitu kigumu kilichimba sentimita chache kutoka kichwani mwake na kuparaza gome la mti ule.



“Nimeonekana… Nashambuliwa!!!!” alibweka kama jibwa koko, lakini sauti ilimezwa na sauti ya matone ya mvua iliyoongeza kasi ya kunyesha.

Kwa wepesi, akajirusha kwenye tawi jingine. Almanusra aanguke kwa utelezi, lakini kwa umakini aliokuwa nao, akawa ameng’ang’ania tawi hilo kama nyani. Bunduki yake ya sniper rifle SVU ikining’inia kifuani kwake.



Harakaharaka akailaza mbele ya tawi lile tayari ili kuangalia anashambuliwa kutokea upande upi ili ajibu mashambulizi. Ila kabla hajafanikiwa mara akasikia yowe la uchungu likitoka kwa mtu aliyemwona chini ya mti ule.

“She was attacked!!!!..” alibweka tena kwa sauti akishuhudia yule mrembo akigaa gaa chini kwa maumivu huku damu ikimchuruzika.

Akaona kuendelea kupoteza sekunde za kumwangalia binti yule ni kupoteza muda dhidi ya adui. Akarudisha umakini kwenye bunduki yake. Hata hivyo alikwishachelewa. Alichelewa muda mrefu sana!!!!!!!

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 02


ALIPOISHIA…

“She was attaked!!!!..” alibweka tena kwa fadhaa akishuhudia yule mrembo akigaa gaa chini kwa maumivu huku damu ikimchuruzika.

Akaona kuendelea kupoteza sekunde za kumwangalia binti yule ni kupoteza muda dhidi ya adui. Akarudisha umakini kwenye bunduki yake. Hata hivyo alikwisha chelewa. Alichelewa muda mrefu sana!!!!!!!



ENDELEA NAYO…

RISASI
moja ilichimba pembeni kidogo ya bega lake la kulia. Alipiga yowe moja la uchungu halafu akapiga kimya cha ghafla, akabakia akiugulia ndani kwa ndani. Maumivu makali yakasambaa mwili mzima. Almanusra aanguke chini ya mti huo, kwa bahati alibaki amelikumbatia tawi la mti.

Ile bunduki yake ya masafa marefu nayo ilibaki ikining’inia chini. Ilikuwa ni kama bahati tu kwa ni mkanda wa bunduki hiyo uliuvaa kifuani.



Alibaki amejikunyata pale tawini, ametulia tuli. Kwa sekunde hapakuwa na mashambulizi yeyote, hakuna kilichosikika zaidi ya yowe la mwanamke chini ya mti sambamba na matone ya mvua.

Giza lilikuwa ni zito ndani ya msitu huo wa Goma. Kama hutumii darubini zenye uwezo mkubwa, basi kwa macho ya kawaida kamwe yasingeweza kuona japo umbali wa sentimita 120.

Mara chache miale ya radi ilipowaka, ndipo nuru ya mwanga iliangaza sehemu kubwa ya msitu, ungeweza kuona namna matawi ya miti na majani yanavyosukwa sukwa na upepo uliokuwa unavuma kwa nguvu.



Mpiganaji yule aliyekuwa amebana kwenye tawi la mti ule mkubwa, akiwa tayari amekwisha jeruhiwa, kupitia uzoefu wake kwenye medali za kivita, aling’amua adui anayemshambulia ni ‘sniper’ yaani mdunguaji ambaye anashambulia kwa hesabu kali.

Hakujua adui huyo anatokea upande upi. Alijiuliza: Je, ni kile kichaka alichokiona kupitia darubini ya kwenye bunduki yake kikiwa kinanyata?



Lakini hapana! Mtu yule aliyejivika majani na magome ya mti kiasi cha kumtengenezea taswira kama ya kichaka, alikuwa mbali na mazingira ya eneo alilokuwepo, kamwe isingekuwa rahisi kuonekana.

Swali kuu likaendelea kubaki kuwa, adui anayemshambulia yuko wapi? Na vipi mwanamke anayebweka kwa maumivu hapo chini ya mti?

Mwanamke ambaye usiku huo ingembidi awe anahudumia mumewe haki yake ya ndoa. Anafanya nini ndani ya uwanja wa vita. Ni nani huyu mwanamke na kwa nini anashambuliwa? Je, adui yetu ni mmoja? Yeye amewakosea nini maadui zetu?



Jamaa alijiuliza. Akili yake ilimzunguka kwa kasi sana, alimini ipo sababu inayojibu kwa nini binti yule anashambuliwa na maadui zake. Hakujua na hakuona njia ya kupata majibu ya maswali hayo zaidi ya kuikoa roho yake.

Aliamini kama akizubaa, uwezekano wa kufa kizembe ni mkubwa. Wakati huohuo, yule mwanamke kule chini aliendelea kupiga kelele za maumivu makali. Ajabu mdunguaji hakummalizia.

“Hii ina maana gani?” alinong’ona. Alihisi uwepo wa mtego. Alikuwa makini sana. Kosa moja lingempeleka akhera.



Akiwa amekumbatia tawi lile la mti, maumivu yakiendelea kutambaa kwa kasi mwilini mwake. Mwanaume akajikaza kisabuni, akawa anaivuta bunduki yake iliyokuwa inaning’inia.

Lilikuwa ni kosa kubwa.

“PaAAA!.. PaaAAA..! KbbBUUM!!… Chwaaarr!!!”

“Yalaa!!”



Mlio wa vyuma vikigonga ile bunduki na vingine vikiparaza gome la mti vilisikika! Mpiganaji yule kwa mara nyingine, alipiga yowe la uchungu. Risasi nyingine ilikuwa imembamiza mkononi mwake.

Na katika hali asiyo iratajia bunduki yake ilianguka chini kabisa ya mti ule.

Alikuwa amejeruhiwa vibaya sana. Risasi ilikuwa imechimba kwenye kiganja cha mkono wake na kutoboa tundu baya lililo tiririsha damu kama bomba la maji lililofunguliwa koki.

“Blood Coward, nakufa, sina ujanja” Jamaa alibweka. Na kweli alikuwa hana ujanja. Siku hiyo ilikuwa ni Arobaini yake. Adui alikuwa amemdhibiti karibu kona zote. Kifo chake kilikuwa sentimita chache mbele yake.

**



KARIAKOO – TANZANIA

Edna Manyanga, mwandishi wa habari wa kujitegemea. Alizipiga hatua za harakaharaka huku moyoni akiwa na hofu na mashaka makubwa. Alitembea akiupita mtaa wa Gerezani, akavuka barabara na kukifuata Kituo cha Daladala cha Agrey.

Alikuwa anatembea huku akiwa ameshikilia mkoba wake kwa makini sana. Umakini na mkoba huo sio dhidi ya vibaka waliotapakaa kila kona mjini Kariakoo. Laa! Bali thamani ya vitu vilivyokuwa ndani ya mzigo huo.



Ndani ya mkoba kulikuwa na kamera, kamera ya siri mfano wa miwani ya macho, ambayo alikuwa akiitumia kwenye kazi zake mbalimbali za kichunguzi.

Siku hiyo, ndani ya memori kadi ya kamera hiyo ilikuwa imebeba jambo zito tena la kutisha na kwa kweli kama jambo hilo mwandishi huyo ataliweka hadharani basi nchi ingesimama kwa muda. Ilikuwa ni siri ya kuogopesha sana.

Mwandishi huyo aliyebobea kwenye habari za kichunguzi, alikuwa na miaka takribani saba kwenye taaluma hiyo. Pamoja na umahiri wake wa kuibua habari mbalimbali za kichunguzi, hakuwahi kupata habari kubwa na ya kusisimumua kama ambayo alikuwa amepata siku hiyo.



Alikuwa ametembea kwa mguu akitokea mtaa wa Lindi, ambako alishuka kwenye bodaboda ambayo aliikodi akitokea Oysterbay, ambako huko ndiko alikopata tukio lililokuwa ndani ya mkoba wake.

Ilikuwa ni habari iliyobeba skendo chafu ya kiongozi mkubwa wa nchi. Tena ambaye yupo katika idara nyeti ya usalama wa nchi.

Edna Manyanga, alikuwa na hofu, alitembea kuliendea gari lililokuwa likipakia abiria. Tangu aliposhuka kwenye bodaboda kule mtaa wa Lindi, nyuma yake kulikuwa na mwanaume aliyekuwa amevalia kofia ya pama, ambaye alikuwa akimfuata kwa karibu sana.



Mtu huyo ndiye alikuwa akimtia wasiwasi. Hakujua alianza kumfutilia kuanzia wapi, Edna Manyanga alibaini kufuatiliwa muda mchache baada ya kushuka kwenye bodaboda ni baada ya yeye mwenyewe kufutulia nyendo za watu waliokuwa nyuma yake. Ndipo mtu mwenye kofia ya pama alipogundulika.

Alipogeuka nyuma, akamwona jamaa anahangaika kuvuka barabara, wakati huo yeye tayari alikuwa amekwisha likabili daladala lililokuwa tayari kwa kuondoka. Upesi akatumia nafasi hiyo kuingia ndani ya daladala. Dereva akaliondoa gari.

Wakati anaketi kwenye kiti, mara jamaa mwenye kofia ya pama naye akawa amekwisha da ndia basi hilo la Buguruni.

Itaendelea
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom