HADITHI: KIZUIZI
SEHEMU YA SITA
Macho ya Lameck yakajaa huba kuliko yale ya James. Emmy akaligundua hilo, bila kutarajia akajikuta anamsogelea Lameck. Lameck upesi upesi akajikumbusha mazoezi ya kubeba vitu vizito jeshini. Akambeba Emmy mzegamzega hadi chumbani. Kitanda kikawatazama
kwa namna ya kuwahitaji sana, mashuka meupe yakawavutia wote.
Emmy akiwa kama aliyepoteza fahamu akajikuta uchi wa mnyama juu ya kitanda kile. Baadaye……………
Baada ya saa zima fahamu zikamrejea, shuka hazikuwa nyeupe tena bali kuna nakshi nyekundu zilikuwa zimejichora.
Emmy hakuwa akiweza kutembea upesi. Alikuwa mfano wa mwanaume aliyefanyiwa tohara.
Hakuna aliyemwangalia mwenzake usoni!!!!
****
ENDELEA.........
Usiku wa mang'amung'amu ulimkumba Jose, alitamani asubuhi ifike upesi ili aweze kutimiza azma yake aliyoipanga ya kumwongezea kipato.
Japo alichelewa sana kuupata usingizi lakini hatimaye usingizi ulimpitia na asubuhi aliyoihitaji ikafika.
Aliwahi kuamka kabla ya wote pale nyumbani. Akafagia uwanja. Akajisafisha mwili na kisha akachomoa kwa tahadhari kubwa noti nyekundu nyekundu sita akaziweka katika pochi yake. Akaondoka.
Saa mbili asubuhi akiwa na rafiki yake aliyempeleka mahali alipokuwa anaishi Bibiana, kauli mbiu ya ‘biashara asubuhi jioni mahesabu' ndio chanzo cha kuwahi sana.
Eneo lilikuwa na watu wengi sana, ni kama aidha ilikuwa harusi ama msiba. Jose akajipenyeza kimyakimya katika umati wa watu matusi aliyotukanwa kwa sababu ya kuleta usumbufu wa kusukuma sukuma watu hakuyajali sana alichokuwanacho makini ni pochi yake mfukoni.
Hatimaye alifika mbele kabisa. Akakutana na askari wakamzuia asiendelee zaidi.
Maneno maneno ya watu yakamshtua. Kuna jambo la kushangaza lilikuwa limetokea pale nyumbani kwa akina Bibiana, kulikuwa kuna tukio la mauaji.
Dakika kadhaa baadaye mwili ukatolewa ndani. Kwa kuwa Jose B alikuwa mbele aliitambua sura ya Bibiana.
Mapigo ya moyo yakaenda kasi zaidi aliposikia kuwa ameuwawa kwa kupigwa risasi. Hofu ikatawala akatokomea eneo lile bila kukumbuka kuwa hakuwa amekuja peke yake pale.
Jose alikuwa amekumbwa na taharuki kubwa sana. amani ikatoweka.
Mtu wa kwanza kumuhusisha katika mauaji haya alikuwa ni James. Jose alizifikiria zile milioni mbili alizopewa kama malipo kwenye biashara ya kuuziana siri, siri ya kizuizi. Katika mawazo haya Jose akaisaliti ile dhana yake ya kwanza kwamba zile pesa zilikuwa chache sasa aliziona kuwa zilikuwa nyingi sana kwa ajili ya kununua habari ile.
Tena alipokumbuka kuwa bei ya habari hiyo ilikuwa ni milioni sita, akajipa uhakika kuwa pana kitu hapo!!!! Milioni sita kwa ajili ya kununua habari???
James ameua!!!! Alijiuliza Jose akiwa njiani kuelekea alipopajua yeye mwenyewe. Swali hilo likamfanya atetereke kimawazo. Maana jibu lake lilikaribiana na ndio!!
Akajihisi yupo hatarini. Hatari ya kuuwawa. Kuuwawa kwa kuijua siri. Siri ya kizuizi!!! Na sasa siri ya mauaji.
Kivipi Bibiana afe!!! Kivipi mh!! Hapana kuna kitu. Kizuizi kimemuua Bibiana" Jose alizidi kujiuliza kisha akaamua kujipatia jibu mwenyewe.
Wakati akijipa uhakika kuwa huenda ni kizuizi kimemuua Bibiana, alijiaminisha kuwa kizuizi hichohicho kinaweza kumtia yeye matatani.
Hatia ya kuwa mbinafsi na kutomshirikisha yeyote tangu mchezo huu unaanza ikaanza kumtafuna, alitamani japo angekuwa amewahi kumshirikisha mama yake, lakini haikuwa hivyo. Sasa mambo yanaanza kuwa magumu. Majuto yanachukua nafasi.
Ile pesa ikaanza kuwa chungu hata kabla haijatumika kufikia nusu. Mipango ya kumtafuta huyo mke mtarajiwa ikaonekana kuwa batili. Hatia ikatambaa vyema na kujikita katika moyo wa kijana huyu mwembamba, mrefu wa wastani mwenye macho makavu ya mviringo, kichwa chenye nywele chache lakini kikiwa na siri lukuki na mdomo mdogo lakini wenye maneno mengi. Jose B waukweli.
Mara akawaza juu ya kuukimbia mji.
Wazo hili akalifutilia mbali mara moja na kujiona kuwa anatawaliwa na uoga usiokuwa na mantiki yoyote. Kwanza huyo James hafahamu ni wapi anapoishi. Pili .......akazima simu yake kisha akamalizia.
Pili sipatikani kwenye simu.
Atanipataje?
****
James aliamka mapema sana lakini hakubanduka kitandani. Jose B, bado alikuwa hapatikani kwenye simu.
James aliamini kuwa Jose ameingiwa kiwewe kwa kuzipata pesa nyingi kiasi kile kwa pamoja, kwa mtazamo wa waziwazi alimwona Jose kuwa alitetemeka sana baada ya kupokea pesa zile za malipo.
James akaamini kuwa Jose atakuwa amejichimbia katika vilabu mbalimbali vya pombe akifaidi maisha ya kipekee ambayo kamwe hajawahi kuyapitia. James akampuuzia Jose B na kufikiria kwamba hana athari zozote katika mpango wake wa kufunga ndoa.
James akazihesabia zile pesa alizompatia Jose, kwa maisha yake ya kimasikini hakika ingemchukua muda mrefu sana kuweza kuzimaliza. Mwanzo wa kuzimaliza zile pesa ndio ungekuwa mwanzo wa kutafuta mbinu za kupata pesa nyingine. Wakati huo ukifika tayari tangazo la tatu litakuwa limepita, na hapo James atakuwa amefunga goli la kisigino!!!!
James akampuuzia Jose. Akajichukulia pointi zote upesi upesi na kujichukulia kuwa yeye ni mjanja kuliko Jose.
"Kesho narejea Dar!!!" akajihakikishia James, kisha akaitwaa simu yake na kumpigia Emmy. Simu iliita mara ya kwanza haikupokelewa, mara ya pili hali ikawa ileile.
"Katakuwa kanaoga ka-Emmy kangu!!!" alijisemea huku akiinuka kitandani.
Naye akaelekea maliwatoni kukidhi haja zake.
****
Almanusura hisia za James ziwe sahihi juu ya mchumba na mke wake mtarajiwa. Alihisi kwamba yu bafuni anaoga lakini hakuwa anaoga bali alikuwa anaugulia maumivu makali baada ya kuruhusu bikra yake itolewe na mwanajeshi sasa alikuwa anajikanda ili kupunguza adhabu ile ya kuchechemea huku akisingizia kuwa alikuwa ufukweni anaogelea mawimbi yakamchukua vibaya na kumrusha juu, akatua juu ya kitu kigumu.
Aliporejea kutoka bafuni alikuta simu yake inawakawaka ishara ya simu iliyokosa majibu. Alipotazama kidogo aitupe chini, aliogopa alichokiona, lilikuwa jina la James ambalo alikuwa amelihifadhi kwa jina la kubuni la ‘Sweet husband' jina hili lilikuwa likimfanya atabasamu siku chache nyuma sasa likaanza kumkosesha amani.
Kile alichomuahidi James hakikuwepo tena. Aibu kuu.
Sasa Emmy anaitazama ile simu kama mdudu wa kutisha ambaye akiguswa analeta madhara makubwa.
Akatamani ampigie lakini hakuwa tayari kusikia jibu la mume mtarajiwa kuwa yupo njiani anakuja Dar es salaam.
Wakati huo lilisalia tangazo moja tu ndoa iweze kuthibitishwa na kanisa.
Ile subira aliyokuwanayo na matamanio makubwa ya kufunga ndoa yakaanza kuyeyuka. Akauona uchungu mkubwa ukimkabili baada ya kuifunga ndoa.
"Au nisingizie kuwa ilitoka katika ajali ya wimbi la bahari?? Lameck ameniponza Lameck." Alitafakari.
Akiwa bado ametulia bila kujua ni dakika ngapi zimepotea akiwa hajafanya maamuzi, simu yake iliita.
Alikuwa Lameck. Hofu nyingine tena.
Kwanza aliona aibu kwa kitendo alichofanya na baba yake huyo, kisha akajivunja mshipa wa aibu akapokea.
"Unaendeleaje kipenzi." Sauti nzito ya Lameck ilimnong'oneza Emmy.
"Lameck...acha kuniita mimi jina hilo tafadhali."
"Nimeongea na mama amenambia upo chumbani peke yako na James bado hajarudi, kuna ubaya gani kwani mamii." Lameck alibembeleza. Emmy akapagawa na mauzauza ya huyu bwana.
"Lakini ninakaribia kufunga ndoa. Lameck please hebu tufanye kama hakuna kilichotokea ndugu yangu."
Emmy alisihi huku akijaribu kuizuia hasira yake.
"Mimi sio muigizaji mamii, siwezi kabisa kujifanya sijui kilichotokea...Emmy si unajua nilikupenda nawe ulinipenda hapo kabla na hadi sasa..."
"Ndio nakupenda Lameck lakini umeniharibia ujue..."
"Kivipi?"
"Jamaa anajua kuwa mimi ni bikra. Sa itakuwaje?"
"Hayo ndo maneno sasa, kumbe hasira zote hizo ni hilo tu...njoo kesho home kwangu"
"Kufanyaje sasa."
"Njoo utafurahi."
Walimaliza maongezi baada ya makubaliano. Emmy alikubali lakini kwa shingo upande. Majuto yalikuwa yamemzidi nguvu.
Akiwa bado anatafakari kidogo juu ya wito wa kwenda kwa baba yake mdogo, simu ikaita tena, sasa alikuwa James. Mume mtarajiwa.
Hofu mpya ikajengeka. Lakini hakuwa na budi, akalainisha koo kwa kukohoa kisha akapokea simu akiulazimisha uchangamfu.
"Vipi mpenzi umelala...." Sauti nzito ya James iliuliza.
"Wala sema nilikuwa nawatch kideo sikuisikia simu yako..."
Lile neno kideo likamshambulia ghafla James aliyekuwa ameketi kitandani, hakushtuka kwa sababu tu mpenzi wake alikuwa amejikita katika kutazama luninga, lakini lile neno kideo liliambatana na jambo jingine la muhimu sana. Jina Deo.
Mdomo ukawa mzito, Emmy aliendelea kukazana kuita ‘halo..halo..' lakini hapakuwa na majibu. Mara simu ikakatwa.
Emmy hakufanya jitihada zozote za kupiga simu, kwanza ilikuwa faraja kukwepa kuzungumza na James.
Akajirusha kitandani aweze kufanya mtihani wa kuwaza na kuwazua.
Wakati akijirusha kitandani, James alikiacha kitanda akasimama wima akakumbuka kuna tatizo kubwa anakaribia kuliacha jijini Mwanza. Deo.
Huyu kijana na yeye alikuwa bega kwa bega kumfitini asiweze kufunga ndoa na Emmy John. Kuondoka huku akiiacha roho hii ikifurahia hali ya hewa ya jiji la Mwanza lilikuwa kosa ambalo mwisho wa siku litamfanya aaibike hadharani na kukosa nafasi ya kipekee ya kuwa mwanaume wa kwanza kushirikiana na Emmy.
Safari aliyotaka kuiandaa kwa ajili ya siku iliyofuata akalazimika kughairi. Alikiri kuwa anafanya haya yote kwa ajili ya mtu anayempenda kwa dhati, tena muaminifu kwake.
Laiti kama angejua ukauzu aliofanyiwa na Emmy, huenda angeubadili uelekeo.
James akakiri tena kuwa alikuwa akimuhitaji sana Jose B waukweli ili aweze kumfanikishia mipango ya kuonana na Deo.
Atampata wapi? hilo likawa swali.
Katika simu ya mkononi hakuwa anapatikana.
James akaulazimisha usingizi. Hatimaye akapitiwa.
Usingizi ukapaa majira ya saa kumi alfajiri na kuelekea kwa wengine, ukawa umemtupa mkono James.
Akabaki kugaagaa kitandani akijiuliza ni namna gani anaweza kukabiliana na Deo pamoja na Jose B kimya kimya bila kuwa hata na mawasiliano nao??
Akakosa jibu. Akasimama akaliendea begi lake dogo akatwaa tembe mbili za dawa akameza. Zilikuwa za kutuliza maumivu ya kichwa.
Hakika James alikuwa amezidiwa.
Akiwa katika kufikiri zaidi akakumbuka kuwa ameuwa watu wawili tayari, na wala hawakumuumiza kichwa na wala hakujuta.
Kifo cha bwana mpenda kujua yasiyomuhusu kule ziwani hakikuwa na uzito sana. Lakini kifo cha Bibiana hiki kilikuwa cha kipekee, aliamini kitawavuta watu wengi sana, akakiri kuwa Deo kama patna wa marehemu Bibiana lao likiwa moja lazima atahudhuria mapema sana katika msiba huo na huenda hatabanduka hadi maiti ifukiwe kaburini na kama hiyo haitoshi hata matanga atayangoja.
Pata potea. James akarusha karata kuwa huenda anaweza kupata hisia juu ya Deo katika msiba huo ambao utashangaza zaidi ya kuhuzunisha.
Akaamua kuwahi mapema kabisa, miwani yake nyeusi machoni, kofia kubwa kichwani na ile hali ya hewa ya ubaridi akajificha ndani ya koti kubwa jeusi. Ilikuwa ngumu kumfahamu.
****
Jose B akiwa katika nyumba ya kulala wageni ambayo alijihisi ni salama zaidi ya nyumbani kwao alikuwa katika kizungumkuti cha namna yake, alikuwa anahangaika kuamini iwapo ni kweli James ndiye muuaji ama ni hisia zake potofu? Alitamani awashe simu na kumpigia amuulize lakini akasita akagundua swali lile ni gumu sana na pia ni zito.
Na kabla ya kuuliza akaamua kufanya ubashiri, iwapo Jose ndiye muuaji kweli kisha akasikia swali hili. kwanamna yoyote ile lazima atamsaka kwa udi na uvumba aweze kumteketeza asiweze kuisambaza siri hii zaidi.
Kizuizi.
Jose alipofikiria kuhusu kufa akapatwa mshtuko, hakuwa tayari kufa.
Asubuhi alidamka na wazo la kijasiri, akaamua kwenda msibani huku kauli mbiu ya ‘Penye wengi pana mengi' ikimuongoza na kujiaminisha kuwa lazima atagundua kitu cha ziada.
Jose B akasahau kuhusu hatari inayomkabiri, akatawaliwa na tabia yake ya kujua mengi hata yasiyomuhusu akaamua kufuata kiguu na njia kuelekea katika msiba wa Bibiana.
Hakujua kama James naye alikuwa katika msafara huohuo.
Laiti angejua...............
****
EMMY JOHN alimuaga mama yake mzazi kuwa anaelekea ufukweni kupunga upepo kwani hawezi kuishi kipweke bila uwepo wa James.
Mama alimsikitikia mwanaye, akamruhusu huku akimtia moyo kuwa muda si mrefu mume wake atarejea.
Aliyoyazungumza mama yalipenya kama upepo wa kawaida tu usiokuwa na maana. Emmy hakuwa akimuwaza James hata kidogo.
Mawazoni mwake Lameck alijikita, kwa kuwa alimuahidi jambo jema. Kumsaidia kuificha aibu.
Emmy akatoweka, safari ya kuelekea nyumbani kwa Lameck.
**JOSE B na JAMES wote bila kutaarifiana wanaamua kwenda msibani....nini kitatokea?? Je huu utakuwa mwisho wa Jose B??
**DEO anasakwa bila kujua kama anasakwa...vp atapatikana na kuhukumiwa kwa kukifahamu KIZUIZI??
**EMMY si bikra tena lakini mtaalam LAMECK anamwambia kwake hilo ni jambo dogo??
Je atamsaidia kabla tangazo la tatu la ndoa halijatangazwa???
ITAENDELEA