HADITHI: Damu, mabusu na machozi

HADITHI: Damu, mabusu na machozi

SEHEMU YA 25
Saa nzima baadae Nancy alitolewa chumba cha upasuaji akiwa amenyolewa nywele zote kichwani na kushonwa nyuzi kumi na nne sehemu aliyopasuka, badala ya kuruhusiwa kwenda nyumbani ilibidi apewe kitanda kwa sababu mwili wake ulionekana kuwa dhaifu! Wote walikubaliana na Danny akaamua kubaki na mgonjwa wote wakaondoka, mzee Katobe alirejea tena saa kumi mbili jioni akiongozana na wazazi wa Danny na mama Nancy akiwa na watoto wake! Hakuna aliongelea suala la ndoa tena,wote walijifanya hawakumbuki yaliyotokea mchana ingawa ni kweli yalikuwemo vichwani mwao.
“Vipi hali ya mgonjwa?”Baba yake Danny aliuliza.
“Anaendelea vizuri ila hana kumbukumbu kabisa! Sijui itakuwaje?”
“Hivyo ndivyo ilivyo! Si umechagua mwenyewe bwana ukikoroga ni lazima ulinywe!” Baba yake alimwambia akitabasamu.
Hawakukaa sana wodini, masaa mawili baadae waliaga na kuondoka kurejea nyumbani kwa mzee Katobe ambako pia wazazi wa Danny walifika, hapakuwa na maongezi sana,baada tu ya chakula cha usiku kilichopikwa na mama Nancy akiwa nyumbani kwake tena, waliingia chumbani kulala,mzee Katobe na mke wake walitumia usiku huo kuongea juu ya kilichotokea, mama Nancy alieleza kila kitu akifafanua vizuri juu ya watoto aliokuwa nao! Mzee Katobe hakuweza kuyazuiya machozi, badala ya kuchukia alilia kama mtoto mdogo huku mke wake akimbembeleza.
“Nimekusamehe mke wangu, najua usingeweza kufanya jambo hili kwa makusudi naelewa ni kiasi gani unanipenda na kiasi gani wewe ni mwaminifu!Ulikuwa mateka na ndio maana ukajamiiana na mtu mwingine hatimaye kupata watoto hawa! Hawana hatia yoyote,sina sababu ya kuwachukia!” aliongea mzee Katobe.
Hawakulala mpaka saa kumi na mbili asubuhi waliponyanyuka na kujiandaa kwenda hospitali, mama na Nancy alitayarisha kifungua kinywa na ilipotimia saa moja na nusu ya asubuhi mzee Katobe aliondoka na wageni wao hadi hospitali ambako walikuta hali ya mgonjwa ni ile ile, hapakuwa na mabadiliko yoyote upande wa akili ingawa kidonda chake kinandelea vizuri na kulikuwa na dalili kuwa siku hiyo angeruhusiwa na kuondoka.
Lakini hivyo sivyo ilivyotokea kwani wakati wa raundi madaktari walishauri Nancy ahamishiwe wodi ya wagonjwa wa vichaa na haikuwa katika hospitali hiyo, ilibidi ahamishwe na kupelekwa katika hospitali ya wilaya ambako kulikuwa na wodi ya aina hiyo! Nancy akawa maewekwa kwenye madawa makali ya akili, Danny hakurusiwa kukaa wodini ingawa aliomba jambo hilo lifanyike, alisikitika wakati akiondoka hospitali kurudi nyumbani! Hakuwa na kumbukumbu tena juu ya Agness na hakuelewa hata mahali alipokuwa kipindi hicho.
Siku chache baadaye wazazi wa Danny waliondoka kurejea Canada wakiwa wamesikitishwa na kitendo kilichofanywa na mtoto wao. Nancy aliendelea kulazwa wodini karibu mwezi mzima akipatiwa matibabu ya vichaa lakini hayakumsaidia chochote bado aliendelea na hali yake ya wendawazimu mzee Katobe akashauriwa na marafiki zake kumwondoa hospitali na kumpeleka kwa wataalam wa tiba za jadi.
Kwa sababu alitaka mtoto wake apone, mzee Katobe hakuwa na chaguo lingine, alikubali kila kitu alichoambiwa na kumsafirisha mwanawe akiwa na Danny aliyesitisha masomo yake kwa mara nyingine hadi sehemu za Lushoto mkoani Tanga ambako alitibiwa na mganga wa kienyeji kwa muda wa miezi mitatu bila mafanikio na kuhamishwa tena kwenda kwa mganga mwingine, walizunguka nae sehemu nyingi sana mkoani humo bila mafanikio! Si Danny wala mzee Katobe aliyekuwa tayari kukata tamaa.
“Huyu mpaka mkutane na mganga yule yule aliyemrisha yamini! Vinginevyo hatafunguka, hatokufa mwendawazimu, kwani yuko wapi huyo mganga?”Mganga mmoja maarufu mjini Tanga aliwauliza walipokwenda kwake na kumsimulia historia ya mgonjwa.
“Alikuwa Bagamoyo huko Pwani lakini baadae alihamia Zaire!”
“Nakushauri uende kumtafuta huyo mganga kwanza! Ni kazi ndogo sana akipatikana, yeye anafahamu ni kitabu gani alisoma na akikisoma tena kwa lengo la kumfungua atafunguka! Vinginevyo mtapoteza fedha nyingi na bado mtoto wenu hatapona!”
Maneno hayo yaliwaingia sana akilini na kufikia uamuzi wa Danny kuondoka kwenda Zaire kumtafuta mzeeMwinyimkuu, alirudi Bagamoyo na kupata maelezo ya kutosha kutoka kwa mama yake Nancy juu ya mahali mzee huyo alipoishi nchini Zaire.
“Kabla hajapata tatizo alilonalo, Nancy aliwahi kunitajia kuwa sehemu aliyoishi mzee Mwinyimkuu ni Kalemi!Hivyo ukifika hapo anza kumuulizia”.
“Sawa mama!Nitajaribu kumtafuta kwa nguvu zangu zote.”
Danny hakuwa na chaguo lingine zaidi ya kupewa fedha na kuiacha Bagamoyo hadi Dar es Salaam ambako alipanda treni iliyomfikisha Kigoma baada ya siku tatu na kuvuka ziwa Tanganyika kwa meli hadi upande wa pili nchini Zaire, kazi yake ilikuwa moja tu kumtafuta mtu aliyekuwa na siri ya tatizo la Nancy! Alisafiri hadi Kalemi lakini hakufanikiwa kumpata mzee Mwinyimkuu, watu walimfahamu sana katika eneo hilo lakini walimpa taarifa kuwa alihamia Kinshasa miezi michache kabla.
“Anatumia jina tu?”
“Ndivyo!Na ni mganga maarufu sana utampata tu,anafanya kazi zake sehemu ya stendi kuu ya Kinshasa! Wala usihangaike kuwauliza sana, ofisini kwake kuna bango kubwa lililoandikwa Africana Medicine”
“Ahsante sana”
Danny hakutaka kupumzika asingeweza kufanya hivyo kabla ya kumpata mzee Mwinyimkuu, siku hiyo hiyo alisafiri hadi Kinshasa kwa ndege, bahati mbaya aliingia usiku hakuweza kamtafuta lakini hata muhudumu wa hoteli aliyofikia alilitambua jina la mzee Mwinyimkuu aliyesifika sana kwa dawa za biashara na kuzindika nyumba za watu, alidaiwa kuwa mganga kutoka Tanzania.
Furaha aliyolala nayo siku hiyo ilikuwa kubwa mno na asubuhi kitu cha kwanza kilikuwa ni kwenda stendi ya mabasi alikoelekezwa, bango la Africana Medicine lilionekana wazi juu nyumba kubwa iliyotazamana na stendi, Danny akajua mwisho wa safari yakea ulikuwa umefika, kumpata mzee Mwinyimkuu kulimaanisha kupona kwa Nancy na hatimaye ndoa yake na mwanamke aliyempenda kufanyika.
Aliingia ndani ya nyumba hiyo na kushangazwa na uzuri uliokuwepo, ilikuwa nyumba nzuri iliyopambwa kwa tarazo za kung’aa na kila kitu ndani kilikuwa vioo! Haikuwa rahisi kuamini eti hiyo ilikuwa ofisi ya mganga wa jadi! Msichana mrembo alikaaa nyuma ya kompyuta akichapa vitu fulani fulani, kichwani mwake Danny alihisi maelezo aliyopewa hayakuwa sahihi.
“Habari za leo dada?”
“Nzuri tu kaka nikusaidie?”
“Ndio!Mimi ni mgeni wa mzee Mwinyimkuu sijui hapa ndio ofisisni kwake?”
“Ni hapa ndio!”
“Nimemkuta?”
“Hapana!”
“Yupo wapi?”
“Bahati mbaya sana juzi alipatwa na ajali wakati akitoka hapa kwenda nyumbani kwake, hivi sasa ninavyoongea na wewe yupo chumba cha wagonjwa mahututi cha hospitali ya Mulubwanzi!Hali yake ni mbaya mno,hana fahamu na hawezi kuongea lolote!”
“Unasema kweli?”
“Ndio kaka!”
”Mungu wangu! Nitafanya nini mimi?”
“Kwani kuna nini kaka?”
Danny alisimulia kila kitu kilichotea na kilichofanya yeye kusafiri hadi Zaire, msichana huyo alisikitika sana na kuendelea kusisitiza kuwa jambo ambalo Danny lifanyike lisingewezekana bila mzee Mwinyimkuu kurejewa na fahamu zake kwani hapakuwa na mtu mwingine kwenye kitu hicho aliyekuwa na uwezo wa kusoma vitabu vyake vya uganga.
“Sasa nitafanya nini?”
“Kwa kweli sijui inabidi mimi na wewe tumuombe Mungu amnusuru mzee Mwinyimkuu na kifo!Tofauti na hapo hakuna kinachoweza kufanyika mchumba wako aweze kupona lakini ungemkuta ninakuhakikishia lazima angekuwa tayari kukusaidia”.
“Unaweza kunipeleka hospitalini nikamwone?”
“Hakuna tatizo!”
Msichana huyo ambaye katika mazungumzo yao Danny alifanikiwa kumfahamu kwa jina la Aminata, alikubali kufunga ofisi na wote kwa kutumia gari lake waliongozana hadi hospitali ya Mulubwanzi kumwona mzee Mwinyimkuu, ni kweli alikuwa chumba cha wagonjwa mahututi! Kichwa chake kikiwa kimefungwa bendeji nyingi, huku mashine za oksjeni zikiwa mdomoni mwake, kwa hali aliyokuwa nayo hapakuwa na matumaini ya kupona.
“Jamani kwa nini mimi nina bahati mbaya? Kwa nini nimempata mzee Mwinyimkuu akiwa katika hali hii? Aliwaza Danny huku machozi yakimlengalenga.

Je nini kitaendelea?
Je wataweza kumuona mzee Mwinyimkuu?
Je ataweza kumrudisha Nancy katika hali yake?
 
SEHEMU YA 26
Ni mtu mmoja tu aliyehitajika kuokoa maisha ya Nancy, huyo hakuwa mwingine bali mzee Mwinyimkuu, ni yeye ndiye aliyemlisha Nancy Yamini! juhudi za mwanzo kumpata zilizofanywa na Nancy na mama yake zilishindikana lakini Danny alifanikiwa kufika hadi Kinshasa, kuiona zahanati ya tiba za jadi iliyomilikiwa na mzee huyo aliyekuwa maarufu sana katika jiji hilo.
Dany alilia machozi ya uchungu baada ya kupewa taarifa juu ya ajali mbaya iliyompata mzee Mwinyimkuu, kwake ulikuwa ni mkosi na balaa kubwa! Alishindwa kuelewa ni kwanini ajali ilitokea wakati huo na siku nyingi kabla!
“Ng’ombe wa masikini hazai!” Aliwaza Danny akimwangalia mzee Mwinyimkuu aliyelala kitandani kichwa chake kikiwa kimefungwa na bendeji nyingi.
Nyuma ya Danny alikuwepo Aminata, msichana aliyefanya kazi katika zahanati ya mzee Mwinyimkuu yeye pia uso wake ulijawa na huzuni kubwa! Alikuwa haamini kilichokuwa mbele yake, alimhitaji sana mzee Mwinyimkuu katika shughuli zake kama yeye angekufa basi hata zanahati yao ingekuwa imefikia mwisho na maisha ya Aminata yangekuwa magumu kupita kiasi tangu siku hiyo.
Daktari alipoingia alimkuta Dany akijifuta machozi na hivyo ndivyo alivyofanya Aminata! Daktari aliwahurumia sana kiasi kwamba alipomaliza tu kumpima mzee Mwinyimkuu akaanza kuongea nao juu ya hali ya mgonjwa.
“Hali ya mgonjwa sio nzuri! Ajali aliyoipata imeharibu ubongo wake, kichwa chake kilijipigiza kwenye chuma, damu imevuja chini ya kichwa! Tunategemea kumfanyia upasuaji baada ya mapigo yake ya moyo yakikaa vizuri ili kujaribu kuondoa damu iliyoganda!”Daktari aliongea akiwaangalia Danny na Aminata usoni.
“Atapona?”
“Siwezi kusema sana kwani hali yake haileti matumaini makubwa, lakini hata kama atapona kuna uwezekano mkubwa sana wa kupoteza kumbukumbu zake zote za nyuma na sehemu yake ya mwili kupooza!’
Jibu la daktari lilimshtua sana Danny pengine kuliko lilivyofanya kwa Aminata, hakuna kitu alichohitaji kutokwa ka mzee Mwinyimkuu kama kumkumbuka Nancy na mambo aliyomfanyia, kwake haikuwa na maana yoyote kama mzee huyo angepona lakini asiweze kukumbuka yaliyotokea nyuma yake.
“Daktari hakuna njia yoyote unayoweza kufanya ili apone na kumbukumbu zake ziwe kawaida!’
“Sidhani! Ubongo wake umeharibika sana!’
“Mungu wangu hizo kumbukumbu zake ndizo ninazohitaji zaidi!”
“Sio uhai wake?”
“Vyote pamoja!”
“Lakini kwanini kumbukumbu zaidi?”Daktari aliuliza na Danny akalazimika kumsimulia stori nzima juu ya yaliyotokea Tanzania na kwanini alikwenda nchini Zaire kumfuata mzee Mwinyimkuu, daktari alibaki mdomo wazi akionekana kutoamini kama mambo ya kula Yamini yalikuwa na uwezo wa kuharibu akili ya mtu.
“Haya mambo huwa nayasikia lakini hata siku moja sikuwahi kuamini kama kweli yanaweza kufanya lolote kumdhuru mtu!”
“Hicho ndicho kilitokea! Ndio maana namhitaji sana huyu mzee, kurejewa kwake na fahamu pamoja na kumbukumbu kutaamanisha maisha ya mtu mwingine nchini Tanzania, tafadhali daktari nisaidie!”
“Lakini hilo liko nje ya uwezo wangu ni suala la mwili wenyewe kupona, ninachotegemea mimi atapoteza fahamu lakini hawezi kujua asili inaweza kutenda kazi yake kusiwe na mambo yote ninayosema!”
“Jitahidi daktari!”
“Nitafanya kadri niwezavyo!’
Danny aliwasiliana na Tanzania na kuwajulisha mambo yote aliyoyafikia nchini Zaire, wote walisikitika kusikia kwamba alimpata mzee Mwinyimkuu lakini akiwa katika hali mbaya! Hakuweza tena kuondoka ikabidi abaki Kinshasa akisubiri mzee Mwinyimkuu apate nafuu lakini haikuwa hivyo mpaka mwezi mmoja baadaye alikuwa bado hajaweza kuongea ingawa aliweza kufumbua macho! Mambo yote yaliyosemwa na daktari ndiyo yaliyojitokeza, upande mmoja wa mwili wake ulikuwa umepooza.
Danny alikataa tamaa kabisa na kuamua kurudi Tanzania akiwa amechukua namba ya simu ya Aminata ili aendelee kuwasiliana naye juu ya maendeleo ya mgonjwa, hilo ndilo lililofanyika, lakini mpaka miezi mitatu baadaye Nancy akizidi kuwa mwendawazimu, hali ya mzee Mwinyimkuu ilikuwa bado mbaya.
“Anaweza kunyanyuka kitandani lakini bado hawezi kusema chochote!”
“Daktari anasemaje?”
“Anadai kuna maendeleo kidogo na ana matumaini fahamu zitamrejea baada ya muda!”
“Kweli?”
“Ndiyo!’
“Kwa hiyo nije?”
“Hapana, subiri tu hukohuko Tanzania kwa sababu tunaweza kuwasiliana kwa simu nitakujulisha kila kitu kinachoendelea!”
“Ahsante sana Aminata!’
Furaha aliyokuwa nayo Danny siku hiyo ilikuwa kubwa mno, alipowataarifu mzee Katobe na mkewe juu ya hali ya mzee Mwinyimkuu nao walifurahi kupita kiasi, maisha yao yalikuwa mazuri na yenye furaha kama vile hakikutokea kitu! Walishasameheana mambo yote yaliyotokea ili mradi hayakufanyika kwa mapenzi yao, mzee Katobe aliwapenda na kuwakubali watoto Catherine na David! Kwake walikuwa ni kama watoto wa kuzaa.
Mwezi mmoja baadaye ikiwa ni siku ya Jumapili baada tu ya kutoka kanisani simu ya mkononi ya Danny ililia, kabla ya kuipokea alitupa macho yake kwenye kioo cha simu na kugundua ilikuwa simu ya Aminata, moyo wake ulienda kasi kwani alikuwa na muda mrefu tangu apokee simu kutoka Zaire alishindwa kuelewa ni nini kilikuwa kimetokea.
“Hallo habari yako?”
“Safi! Nipe habari ya huko!”
“Leo nina habari mzuri!”
“Habari gani hiyo?”
“Mzee alitoka ku-hospitali jana!”
“Unasema?”
“Mzee alitoka mu-hospitali jana!”
“Unasema kweli? Ina maana amepona?”
“Huwezi amini!Amepona kabisa ingawa bado pande moja ya mwili ina matatizo!”
“Kumbukumbu zake je?”
“Iko safi! Na nimemweleza juu ya stori yote uliyoniambia na amemkumbuka Nancy vizuri, amesikitika sana na amesema mtu yeyote anaweza kuja kumchukua baada ya mwezi moja!”
“Unasema kweli?”
“Kabisa!”
Danny alirukaruka juu akilia kwa furaha, haikuwa rahisi kuamini alichokuwa amekisikia! Hata masikio yake mwenyewe aliona yamemdanganya hivyo kuendelea kuuuliza mara kadhaa akitaka kufahamu kama kilichosemwa ni kweli au Aminata aliendelea kumsisitiza kuwa mzee Mwinyimkuu alikuwa na afya nje kabisa na tayari alikuwa akisafiri kuja Tanzania kumrekebisha Nancy!
“Ahsante sana! Nashukuru sana! Msalimie sana Mwambie tunampenda sana, inawezekana baada ya mwezi mmoja nitakuja mwenyewe kumchukua!”
Simu ilipokatika Danny alikwenda moja kwa moja hadi nyumbani kwa mzee Katobe na kuwapa taarifa juu ya simu aliyoongea nayo kutoka Kinshasa familia nzima ilifurahi, mama aliruka juu na kushangilia kwa furaha.
“Itakuwa vyema! Ili mwanangu arejewe na akili zake!”
“Nafikiri tutaweza hata kufunga ndoa!”
“Unastahili hili Danny umemvumilia sana mwenzi wako!”
“Hakuna matatizo mama! Ulikuwa ni wajibu wangu!”
SIku hiyo hiyo ilifanyika sherehe, wala Nancy hakuwa na habari juu ya kilichoendelea muda wote, alikuwa akiongea peke yake na kucheka! Jina Tonny halikukosekana katika maongezi yake jambo lililoonyesha kuwa pamoja na kuchanganyikiwa alikuwa bado akimkumbuka, mara chache sna alimtaja Danny.
Danny alibaki akisubiri mwezi mmoja ufike na ulipotimia alipewa nauli na mzee Katobe na kusafiri hadi Dar es Salaam ambako alipanda ndege iliyomfikisha Kinshasa siku hiyo hiyo.
*****
Maisha hayakuwa kama yalivyotegemewa kwa Tonny ni kweli baada ya kumaliza Chuo Kikuu cha Beijing yeye na Mimi walihamia Marekani ambako baba yake Mimi, mfanyabiashara maarufu nchini marekani alimkubali Tonny awe mume wa mtoto wake na ndoa kubwa ya kifahari ikafungwa!
Walipewa nyumba kubwa ya kifahari katika Jiji la New York ambako Tonny na Mimi waliishi pamoja wakifurahia maisha. Tonny alimhamisha mama yake kutoka Tanzania na kumpeleka Marekani! Hakuwa na kumbukumbu hata kidogo juu ya Nancy na hata aliposikia kuwa msichana huyo alishikwa na wendawazimu alicheka ingawa alielewa kabisa ni yeye ndiye aliyesababisha yote hayo.
“Shauri yake kwanini hakuweza kuvumilia! Au kurudi kwa mganga amwondolee?” alijiuliza Tonny.
Maisha yalikuwa na kila dalili yangeendelea vizuri katika familia ya Tonny! Hakuamini kama siku moja angerudi tena Tanzania, alijihesabu Mmarekani mweusi na hakutaka watu wafahamu alitokea Afrika Mashariki katika nchi ya ulimwengu wa tatu.
Aliaminiwa na baba mkwe wake na kupewa nafasi kubwa katika kampuni! Kichwa chake kikavimba na kujiona yeye ndiye kila kitu katika kampuni hiyo ya kutengeneza matairi ya TrenTyre, wafanyakazi wote walimheshimu kwani alikuwa mtu wa karibu sana na tajiri yao.
Miaka mitano baadaye mambo yalibadilika ghafla, wazazi wa Mimi pamoja na Mimi mwenyewe walifariji katika ajali mbaya ya gari wakisafiri kutoka Miami walikokuwa wamekwenda kwa mapumziko ya Pasaka kurudi New York, Tonny alikuwa nchini Canada kushughulikia masoko ya matairi! Alipopata taarifa za msiba huo alirudi haraka na kukuta mambo yamebadilika.
Nyumba yake ilikuwa imefungwa mama yake akiwa nje, hakuruhusiwa kufika kwenye msiba kwani familia ilidai hakutambuliwa! Kiburi alichokipata kufuatia madaraka aliyopewa kilimgombanisha na wana ukoo! SIku hiyo hiyo mipango ilifanywa uhamiaji akawa amepewa masaa ishirini na nne aondoke nchini Marekani.
Uchungu mkubwa ulimshika ni hapo ndipo alimpomkumbuka mwanamke wake wa zamani, Nancy! Alitamani kuwa naye tena akiamini huyo ndiye mwanamke aliyepangiwa na Mungu, alimweleza mama yake kuhusu jambo hilo na alimshauri wakirudi nyumbani amtafute, Tonny hakuwa na ubishi alikubaliana na mama yake moja kwa moja.
Walisafirishwa kutoka Marekani hadi Tanzania chini ya uangalizi maalum, waliposhushwa uwanja wa ndege wa Dar es Salaam waliachwa waende zao na wakiwa hawana hata mzigo walipanda teksi iliyowapeleka moja kwa moja hadi Bagamoyo, watu walipomwona Tonny walishangaa sana.
Kitu cha kwanza alichokifanya Tonny baada ya kufika Bagamoyo akiwa haamini kama kweli alikuwa amerudi ni kumuulizia Nancy, alipewa taarifa zote na kusikitika lakini alikuwa tayari kuwa naye hivyo hivyo alivyokuwa! Alihisi bado anampenda na alihitaji sana kumwomba msamaha kwa makosa aliyomfanyia.
Mchana wa siku iliyofuata alisindikizwa na mama yake kwenda nyumbani kwa mzee Katobe, walipokelewa vizuri si mzee Katobe wala mkewe walioonyesha chuki! Tonny alipiga magoti chini na kuomba msamaha lakini wazazi wa Nancy walimwambia wazi hawakuwa tayari kumpa msamaha kwa sababu alisababisha mtoto wao tatizo kubwa! Tonny alilia kama mtoto mdogo na baadaye kumfuata Nancy mahali alipokaa akiongea peke yake kwa kupiga magoti akimwomba msamaha pia, kama kawaida ya wendawazimu Nancy alicheka bila kuelewa alichokuwa akifanya.
Muda mfupi baadaye akiwa bado amepiga magoti mlango ulifunguliwa, Danny akaingia akiongozana na mzee aliyetembea akichechemea, alikuwa mzee Mwinyimkuu! Danny aliwasalimia watu wote waliokuwepo ndani ya nyumba na baadaye kutambulishwa kwa Tonny na mama yake.
“Huyu kijana tuliishi naye hapa, aliwahi kuwa mchumba wa Nancy! Kifupi ni yeye ndiye aliyemharibia maisha mtoto wetu, anaitwa Tonny! Ana bahati siku hizi sina silaha ningemmaliza!” Mzee Katobe aliongea.
Danny alimwangalia Tonny na kucheka, hakutaka kuonyesha chuki ingawa ni kweli alimchukia sana! Alimsogelea na kumpa mkono na wakasalimia bila kinyongo. Mzee mwinyimkuu alisalimiana familia nzima kisha kupewa pole na baada ya hapo akaeleza nia ya safari yake na kuomba nafasi afanye kazi yake ili kumrejesha Nancy katika hali ya kawaida.
Aliletewa begi lake akatoa vitabu viwili na kuanza kusoma Nancy akiwa ameketishwa mbele yake, alisoma cha kwanza mpaka akamaliza kisha akachukua cha pili kilichokuwa na rangi nyeupe na kuanza kukisoma, alipofika katikati yake tu Nancy alianza kutoa macho kisha kuanguka chini na kuanza kutoa mapovu mdomoni kama mtu mwenye kifafa, walipotaka kumwangia maji aliwazuia na kuendelea kusoma hadi mwisho wa kitabu.
Wakati huo Nancy alikuwa usingizini fofofo, Danny na Tonny walikuwepo wakishuhudia! Nusu saa baadaye alizinduka akiwa mwenye akili timamu mbele yake aliwaona wanaume wawili, Danny na Tonny.
“Tonny......Danny!” Aliita Nancy kwa wakati moja huku akizungusha macho yake kutoka kwa mtu mmoja kwenda kwa mwingine! Alionekana kutoamini kilichokuwa mbele yake, baada ya hapo aliendelea kuita jina la Tonny mara nyingi zaidi kuliko Danny!

Je nini kitaendelea mahali hapo?
Je Nancy atamchagua nani?
 
SEHEMU YA 27
Watu wote ndani ya nyumba walikuwa kimya, mzee Katobe na mkewe walibaki midomo wazi bila kuelewa nini kingetokea! Ilikuwa ni kama ndoto, hawakuamini macho yao kama kweli Nancy alikuwa amerejewa na fahamu zilizopotea kwa muda mrefu, walizidi kumshangaa mzee Mwinyimkuu na walizidi kumshukuru Danny kwa juhudi alizozifanya kwani bila yeye Nancy asingekuwa binadamu wa kawaida tena.
Pamoja na shukrani hizo hawakuwa na uhakika nini kingetokea ndani ya nyumba yao, ilikuwa ni lazima Nancy achague mwanaume mmoja kati ya wawili waliosimama mbele yao hakika ulikuwa mtihani mgumu! Ingekuwa ni wao waliotakiwa kuchagua basi wangemchagua Danny, walilidhishwa na tabia yake na walimpenda kwa namna walivyoishi nae vizuri na kusaidiana katika mambo mengi.
Lakini hawakuwa na uhakika kama chaguo la Nancy lingekuwa lao kwani katika mapenzi kila mtu na kitu akipendacho, kwa hali iliyokuwa imeonekana na jinsi ambavyo Nancy alilitaja jina la Tonny mara nyingi dalili nyingi ziliashiria yeye ndiye angeibuka mshindi jambo ambalo hata mzee Katobe na mkewe hawakulifurahia hata kidogo.
“Haiwezekani!” Mama yake Nancy alimnong’oneza mzee Katobe.
“Haiwezekani nini?”Mzee Katobe aliuliza.
“Mwanangu hawezi kurudiana naTommy tena!”
“Hilo hata mimi nakubaliana nalo lakini tutafanya nini? Inavyoonekana huyu mtoto bado anamkumbuka Tonny na pia anampenda tutafanya nini?” Mzee Katobe aliuliza.
“Lazima uzuie!”
“Wacha kidogo tuone kitakachotokea pengine ni wasiwasi wetu!”
Wakati wakiongea maneno hayo kwa sauti ya chini Nancy alikuwa bado amesimama wima mikono yake ikiwa kichwani na alikuwa akilia kwa uchungu huku akizidi kuwaangalia wanaume waliokuwa mbele yake, kichwa chake kilionekana kuwa na kumbukumbu kidogo na juu ya yaliyotokea maishani mwake akiwa mwendawazimu! Alipogeuza kichwa upande wa pili aliwaona baba na mama yake wakiwa wamesimama, akatabasamu.
“Mama huyu ni Tonny kweli au?”
“Ni yeye!”
“Amekuja lini?”
“Tumemwona leo!”
Baada ya kuongea na mama yake bila hata kuongea kitu chochote na mzee Katobe, Nancy aligeuka upande wa mwanzo na kuwaangalia wanaume wawili wakiwa wamesimama kama askari, uso wa Danny ulionyesha kujawa na huzuni na kwa mbali alikuwa akitokwa na machozi! Mambo machache yaliokuwa yamejitokeza ndani ya nyumba hiyo baada ya Nancy kurejewa na fahamu zake yalitosha kumwonyesha juhudi zake zisingezaa matunda.
“Tonny bado unanipenda?”Nancy aliuliza.
“Hakika ndio maana nimerudi, bado nakupenda sana na ninataka kuwa na wewe tena maishani, nisamehe kwa yote niliyokukosea!”
“Mimi yuko wapi?”
“Alifariki dunia! Nisamehe sana Nancy kwa yaliyotokea na tusiongee tena mambo ya siku za nyuma, yote hayo yalipita hebu tugange yajayo!” Maongezi kati ya Tonny na Nancy yaliendelea kama dakika mbili watu wengine wakiwa kimya.
Kila mtu aliyemwangalia Danny alimwonea huruma hata mzee Mwinyimkuu kwani ni kweli alikuwa ametumia juhudi nyingi sana kuokoa maisha ya Nancy na alistahili kuwa mume wake. Danny alisimama kwa unyonge mikono yake ikiwa imekunjwa kifuani! Machozi yakiendelea kumtoka, hakuwa tayari kukubali Nancy aondolewe mikononi mwake wakati alishapoteza muda mwingi kumshughulikia.
“Tonny!”Danny aliita.
“Yes!”Tonny aliitikia kwa mkato huku macho yake yakimpandisha Danny juu na kumshusha chini kwa dharau.
“Lakini mshikaji si wewe ulimwacha? Sasa kwa nini usiniachie tu mimi niliyemuhangaikia?”
“Nini?”
“Usiniachie mimi, kwa nini tugombane!”
Danny aliongea kwa unyonge akimgeukia Tonny na kupiga magoti chini akimbembeleza ili amwachie Nancy.
“Najua una uwezo wa kumchukua na anakupenda kuliko anavyonipenda mimi nakusihi ndugu yangu uniachie huyu mwanamke, nimehangaika sana! Sitaweza kuishi tena kama Nancy akiondoka maishani mwangu, itakuwa aibu kubwa mno ambayo sitaweza kuivumilia!”
Aliongea Danny kwa sauti ya kutia huruma.
Wazazi wa Nancy walishuhudia kitendo hicho na kuumia moyoni mwao, yalikuwa ni matendo ya kusikitisha na waliamini Danny hakustahili kutendewa hivyo kwa sababu alikuwa mwema sana kwa mtoto wao.
“Ni Danny huyuhuyu aliyepigwa risasi na mzee Katobe lakini akaficha siri kitendo kilichofanya mume wangu aepuke kifungo gerezani, ni Danny huyuhuyu aliyehairisha masomo chuo kikuu mara ya kwanza na sasa mara ya pili ili amtafute Nancy, ni Danny huyuhuyu ndiye aliyemtafuta mzee Mwiyimkuu hatimaye kupatikana na sasa Nancy amerejewa na fahamu zake! Haiwezekani, Nancy hawezi hata siku moja kurejea kwa Tonny, lazima tumsaidie!” Mama Nancy aliunganisha mambo kichwani mwake.
“Toka hapa! Haya mambo ya kutafuta ya kumuhangaikia unayajua mwenyewe hapa ni kura tu?Ukishinda kuchukua mtoto, nikishinda ondoka zako!” aliongea Tonny kisha kumsukuma Danny na kumfanya anguke chali sakafuni.
Nancy alishuhudia kila kitu kilichotokea badala ya kusikitika alichekelea na kisha kutembea kwenda mbele mahali alipokuwa amesimama Tonny akitamka maneno na kuonyesha ni jinsi gani alimpenda na alikuwa amesahau yote yalitokea.
“ Nancy! Kwa nini unanifanyia hivi? Umesahau nilijitoa kwa ajili yako? Nifikirie, utayafupisha maisha yangu”Aliongea Danny lakini Nancy hakujali wala kumsikiliza alichokifanya ni kusonga mbele hadi kumfikia Tonny na kumkumbatia, mama yake Tonny alikuwa ameketi kwenye kiti pembeni alinyanyuka na kuanza kushangilia huku akipiga vigelegele kwake ulikuwa ushindi.
“We mama hamnazo nini?” Unashangilia kitu gani gani? Hapa kuna jambo la kushangilia, tena kaa kimya vinginevyo uondoke hapa nyumbani kwangu!” Mama yake Nancy alifoka akitembea kwa haraka kuelekea mahali Nancy na Tonny waliposimama wakiwa wamekumbatiana.
Kwa nguvu zake zote alimkamata Nancy na kuanza kumvuta hatimaye kufanikiwa kumwondoa mikononi mwa Tonny akaanza kumvuta kuelekea chumbani ambako alimwingiza na kufunga mlango nyuma yake, Nancy alilalamikia kitendo hicho lakini mama yake alielewa wazi akili yake ilikuwa haijatulia au alikuwa hafahamu mambo yaliyotokea mpaka kufikia siku hiyo.
“Niachie mama! Niachie niende kwa Tonny! Nampenda kwa moyo wangu wote, ndiye mtu niliyemchagua maishani lakini alichukuliwa kutoka kwangu na Mimi lakini sasa Mungu amemrudisha! Niacheni nimchague nimpendaye ni mimi wa kuchagua, siwezi kuchaguliwa! Simpendi Danny hata kidogo nilionyesha mapenzi kwake kwa sababu nilitaka kumwokoa baba yangu na jela!”
Aliongea Nancy kwa uchungu huku akilia, kwa jinsi maneno yalivyomtoka kulikuwa na kila dalili ya kumaanisha alichokisema.
“Sikiliza mwanangu Nancy!Najua unampenda Tonny lakini pia kuna vitu kama natakiwa kukueleza baada ya hapo utakuwa na uamuzi wa kuchukua, nina uhakika huna kumbukumbu juu ya nini kilikutokea, laiti ungefahamu usingediriki kumwacha Danny! Hebu kwanza jiangalie, nenda simama kwenye kile kioo uangalie mwili wake pamoja na nywele zako ya hapo nitakueleza kila kitu!”
Mama yake aliongea kwa huzuni, alifahamu wazi Nancy hakuelewa kitu chichote juu ya wendawazimu uliomtesa na alitaka hilo lifahamike kwanza ndipo aanze kumsimulia.
“Mama nilikuwaje?”
“Ni habari ndefu! Unawakumbuka mzee Kiwembe na Babu Ayoub?”
Nancy aliinamisha kichwa chake chini na kuzama katika fikra nzito akijaribu kuyazungusha majina ubongoni mwake ili kuona kwamba kumbukumbu zake zilikuwepo,muda mfupi baadae alinyanyua kichwa chake na kumuangalia mama yake.
“Ndiyo mama, nayakumbuka majina hayo, tulikuwa kisiwani, baba na Danny hawakuwepo! Nashangaa leo wapo na ameongezeka Tonny, walikuja lini? Nakumbuka babu Ayoub ndiye alinifanyia kitendo kibaya ambacho nilizuiliwa kukifanya na mtu yoyote isipokuwa Tonny!T ena aliyenizuia yupo hapa ndani! Wamekujaje watu wote hawa hapa kisiwani Galu?”
“Hapa hatupo Galu mwanangu tupo Bagamoyo? Na sijui kama unakumbuka kilichotokea baada ya babu Ayoub kukufanyia kitendo cha ukatili”.
“Sikumbuki mama!”
“Kwa sababu ni wajibu wangu kukuambia basi nitakueleza ukweli!”
Alipoongea mama Nancy alijiweka vizuri kitandani.
Wakati maongezi yakiendelea kati ya mama na mtoto kelele nyingi zilisikika sebuleni, kulikuwa na kila dalili kuwa watu walikuwa wakigombana!
Sauti ya mzee Katobe ilisikika ikiita jina la Danny na kumzuia asifanye kitendo alichotaka kukifanya.
“Danny! Danny! Usifanye hivyo mwanangu, acha kabisa utaua halafu utakwenda jela!”
“Sijali kitu ni bora nimuue kabisa huyu mshenzi halafu na mimi nife! Hawezi kunionyesha dharau kiasi hiki!”
“Baba nakuomba uniachie!” ilikuwa sauti ya Danny na muda mfupi baadae Tonny alisikika akilia kwa sauti ya juu kuomba msaada akidai amechomwa kisu mbavuni mama Nancy aliposikia maneno hayo alikatisha maongezi na kuondoka chumbani mbio kwenda sebuleni, hakuamini alipokuta damu imetapakaa sakafuni! Tonny alilala sakafuni akijitupa huku na kule damu ikizidi kumwagika.

Je nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 28
Lilikuwa tukio la kutisha na kusikitisha sana, moyo wa kila mtu aliyekuwepo sebuleni kwa mzee Katobe ulikuwa ukidunda kwa nguvu! Nancy alikuwa bado amelala sakafuni uso wake ukiwa umechimbiwa katikati ya viganja mikono yake yote miwili, pamoja na kusikia wazazi wake wakiongea bado hakuamini kama majambazi walikuwa wameondoka.
“Kwa hiyo wamemteka?”Mzee Mwinyimkuu aliuliza.
“Ndivyo inavyoonekana!”
“Unahisi watakuwa ni akinanani?”
“Hakuna mtu mwingine wa kufanya kitendo hiki isipokuwa Tonny!”
“Inawezekana! Basi pigeni simu polisi tuwataarifu pia jambo hili”
“Sawa!”
Wakati mzee Katobe anaisogelea simu ili apige kituo cha polisi, Nancy alinyanyuka sakafuni na kusimama wima! Maongezi kati ya baba yake na mzee Mwinyimkuu ndiyo yaliyomshtua, alitaka kuelewa ni nani aliyekuwa ametekwa, kichwani mwake aliwafikiria watu wawili tu, kama si mama yake basi alikuwa Danny maana kabla majambazi hayajaingia sebuleni walipokuwa wameketi wakijiandaa kwenda kanisani kulikuwa na watu watano peke yake, watoto Catherine na David walikuwa chumbani.
“Nani ametekwa?”Aliuliza Nancy.
“Danny!” Mzee Katobe alijibu.
“Haiwezekani! Yumo humuhumu ndani labda amejificha mahali fulani!”
“Hapana! Lazima tuukubali ukweli kuwa hawa watu wameondoka na Danny! Si unakumbuka walivyoingia walisema wamekuja kumtafuta mtu mmoja, sasa kukosekana kwa Danny hapa ndani kunamaanisha nini Nancy?”Mzee Katobe aliuliza.
“Inawezekana kweli katekwa, tutafanyaje sasa kumpata?”
“Nataka kupiga simu polisi niwataarifu juu ya tukio hili!”
“Baba subiri kwanza, naelewa aliyefanya kitendo hiki si mwingine bali ni Tonny! Acha nikazungumze naye, nina uhakika atamrudisha!” Aliongea Nancy akijaribu kumshawishi mzee Katobe asitoe taarifa polisi kwanza.
Baada ya maongezi ya karibu dakika kumi mama yake Nancy akipinga wazo lililotolewa na binti yake akidai hapakuwa na sababu ya kusubiri, wote walikubaliana na Nancy akatoka mbio hadi nje akipitia ufunguo wa gari ya baba yake juu ya kabati, aliingia ndani na kuwasha kisha kugeuza na kuondoka kwa kasi ya ajabu akitimua vumbi nyuma yake hadi nyumbani kwao na Tonny!
Aliegesha gari mbele ya nyumba ndogo ya matope, akashuka na kutembea hadi mlangoni ambako alianza kugonga, hakuna mtu aliyemwitikia na hapakuwa na dalili za watu kuwemo ndani ya nyumba hiyo! Aliendelea kugonga karibu dakika tano huku watu wakipita njiani na kumshangaa, hakuelewa ni kwanini.
“Nyumba hiyo haina watu dada walishahama muda mrefu!” Mpitanjia mmoja alimwambia.
“Wako wapi?”
“Miaka mingi hawakuwepo ila nasikia walirudi kutoka Marekani na kufikia hapa lakini baadaye wakahamia kwenye hoteli moja huko ufukweni inaitwa Badeco!”
“Ahsante sana!” Nancy aliitikia na kurudi hadi kwenye gari na kuondoka zake kuelekea kwenye hoteli aliyoelekezwa, aliifahamu vizuri sana Badeco Hoteli, ndio hoteli pekee ya kitalii iliyotisha kwa uzuri mjini Bagamoyo kipindi hicho. Kutoka nyumbani kwa akina Tonny hadi hotelini ilichukua muda wa dakika kumi lakini Nancy alitumia dakika tano, tayari akawa anaegesha gari lake mbele ya hoteli na kushuka.
“Habari yako dada?” Nancy alimsalimia msichana aliyemkuta mapokezi.
“Nzuri! Nikusaidie?”
“Ndiyo, namuulizia kaka mmoja anaitwa Tonny amepanga hapa?”
“Kweli yupo lakini hivi sasa amepumzika kidogo!”
“Mpigie simu mwambie mimi Nancy niko hapa!”
“Sawa! Karibu ukae kwenye kiti wakati nikikushughulikia!”
Nancy alilisogelea kochi lililokuwa jirani na kuketi bila kusema kitu, moyo wake ulikuwa ukienda kasi na hasira ilizidi kumpanda ingawa hakutaka kumwonyesha msichana wa mapokezi hasira zake. Akiwa kwenye kochi aliendelea kumshuhudia msichana akiongea na simu na alipoiweka chini alimwonyesha ishara kwamba amsogelee.
“Nifuate!” Alisema msichana wa mapokezi.
Nancy alimfuata msichana huyo nyuma bila kusema chochote na wote wakatembea pamoja hadi pembeni kabisa mwa hoteli kulikokuwa na nyumba nzuri iliyoezekwa kwa makuti msichana wa mapokezi alibonyeza kengele iliyokuwa juu pembeni mwa mlango, sekunde chache baadaye mlango ulifunguliwa, Tonny akatokeza uso wake haukuonekana kuwa na mshangao mkubwa sana, alikuwa kama mtu aliyemtegemea Nancy afike chumbani kwake muda huo.
“Karibu sana!”
“A...h..s..an..te!”Aliitikia Nancy kwikwi za kulia zikiwa zimemkaba kooni, hasira yake iliongezeka maradufu alipouona uso wa Tonny! Alimchukia sana kijana na hakuwa na mapenzi naye tena kufuatia kitendo cha kikatili alichomfanyia Danny.
“Tonny kwanini umenifanyia hivi?” Alianza kuongea kabla hata ya salamu.
“Vipi?”
“Kwanini umetuma watu kuja kumteka Danny?”
“Nini? Nani kakuambia nimefanya hivyo?” Aliuliza Tonny uso wake ukionyesha mshtuko ambao akili ya Nancy iliutafsiri kama maigizo.
“Usinifanyie maigizo Tonny, nipo siriasi kabisa! Hicho ndicho kitu ulichoahidi kukifanya wakati unaondoka nyumbani tafadhali naomba umrudishe Danny kwangu, usininyanganye mtu ambaye kwa sasa ninampenda huo ni ukatili Tonny, nitatoa taarifa polisi!” Aliongea Nancy akionyesha hasira.
“Sijafanya hivyo Nancy! Siku ile niliposema ilikuwa ni hasira tu, kamwe siwezi kumteka mtu!”
“Siangalii unachokisema sasa hivi, maneno yako ya siku ile ndiyo yaliyonifanya nikufikirie wewe! Tafadhali naomba umrudishe Danny kwangu! Vinginevyo nakwenda polisi”
“Ukienda polisi ujue ndio utakuwa umenichokoza, hapo ndipo nitalazimika kulipa kisasi!”
“Nakwenda, fanya lolote utakalo!”
“Huo ni uamuzi wako lakini yatakayotokea baada ya hapo usinilaumu!”
Nancy aliubamiza mlango wakati akitoka nje na dakika moja baadaye muungurumo wa gari likiondoka kwa kasi ulisikika kulikuwa na kila dalili kuwa kilichotoka mdomoni kwa Nancy hakikuwa utani, alimaanisha alichokisema na tayari kulikuwa na vita kali kati ya Nancy na Tonny ambayo mwisho wake usingekuwa rahisi kufikiri.
“Kama anakwenda polisi basi mimi pia nawasiliana na mzee Katapila! Tuone nani ni mjanja kati yangu mimi na yeye!” aliongea Tonny akiisogelea simu iliyokuwa pembeni mwa kitanda chake, kabla hajabonyeza namba yoyote mama yake aliyekuwa akiishi naye hotelini aliingia akitaka kufahamu nini kilikuwa kimetokea.
“Nancy, amekuja hapa anadai nimemteka Danny!”
“Umemteka Danny?” Mama yake aliuliza kwa mshangao.
“Ndiyo!”
“Ni kweli?”
“Hapana mama siwezi kufanya hivyo!”
“Sasa?”
“Kwa sababu ameamua kunipa jina la utekaji basi nimeamua kufanya kweli!” Tonny aliongea uso wake ukiwa umefura kwa hasira, mara nyingi akiwa katika hali hiyo hata mama yake alimwogopa. Kwa harakaharaka alibonyeza namba kadhaa kwenye simu kisha kuanza kuongea na mtu ambaye mama yake hakumfahamu.
“Naongea na mzee Katapila?...Sawasawa....sasa hebu sikiliza, ninachotaka ufanye ni kuhakikisha wote wanatekwa na utawapeleka hukohuko Tindiga ulikosema, wafiche huko kwa muda mrefu lakini usiwaue mpaka nitakapoona nao na ninaomba uje haraka hapa hotelini nikukabidhi hundi yako ili uchukue pesa benki......tafadhali wahi maana ukichelewa nitakuwa nimeshakamatwa na polisi....ndiyo ....Nancy amekwenda kushtaki!....najua watanichukua lakini wataniachia, ukishawakamata kaa nao siku nikitoka nitaamua nini cha kufanya juu ya watu hao! Nataka Nancy aelewe mimi si mtu wa kuchezea, nimeishi Marekani na ninajua visasi!” Aliongea Tonny huku mkono wake wa kuume ukipiga piga meza mara kwa mara, mama yake alibaki mdomo wazi akielewa tayari matatizo yalikuwa yametokea! Watu walikuwa wanatekwa kwenda kuuawa, kichwani mwake hakuwa na picha za watu wengine zaidi ya familia ya mzee Katobe.
*******
“Una uhakika ni yeye?”
“Asilimia mia moja kwani ndio kitu alichokisema!”
“Unao ushahidi?”
“Nina uhakika akihojiwa ataeleza ukweli!”
Nancy alitoa maelezo yote polisi kuanzia uhusiano wake na Tonny, alivyomwacha na kurejea kwa Danny jambo aliloamini lilimfanya alipe kisasi, maelezo yake ya karibu saa nzima yaliwafanya polisi waamini alichokisema na kuondoka haraka kwenda hotelini kwa Tonny, gari la polisi lilikuwa mbele likiwa na askari zaidi ya saba na Nancy alikuwa nyuma ndani ya gari la baba yake, hakuna kilichomfurahisha moyoni mwake wakati huo kama kukamatwa kwa Tonny na kufikishwa mbele ya sheria ili hatimaye aseme ni wapi alikompeleka Danny baada ya kumteka.
Walipofika hotelini, Tonny alikamatwa na kupigwa pingu kisha kuchukuliwa hadi kituoni, maelezo aliyoyatoa hayakutosha kuwafanya askari wamuachie huru, akawa ametupwa mahabusu ili aisaidie polisi katika upelelezi! Nafsi ya Nancy iliridhika kwa kitendo hicho na aliwaomba maaskari wamtese Tonny sana ili hatimaye aeleze ni wapi mchumba wake alikokuwa amefichwa.
“Hakyanani nitawapa pesa nzuri! Mkipiga kofi moja mia tano, teke elfu moja, kifuti elfu mbili, kila kirungu kitakachotua mwilini mwake elfu mbili na mia tano! Kazaneni kumpiga na mtunze kumbukumbu zenu ili nikija asubuhi niwakeshi mafaranga yenu!” Aliongea Nancy akitabasamu na maaskari wote waliokuwa wakimsikiliza waliitikia, jambo lililoonyesha wazi Tonny angeteswa usiku mzima mpaka aeleze ni wapi alikokuwa Danny.

Je nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 29
Mzee Katapila alikuwa ni jambazi aliyeutingisha mkoa wa Dar es Salaam miaka ya sitini na sabini, alijipatia mali nyingi sana kwa njia haramu hatimaye kujikuta ametajirika! Lakini pamoja na kuwa na mali nyingi bado hakuisahau kazi yake ya ujambazi, akawa ameunda genge lililofanya kazi ya kuvamia mabenki, watu binafsi na kuwaibia! Kundi hili aliliita Lambadamu.
Lilikuwa ni kundi maarufu kwa vitendo vya uharamia, hata polisi walilifahamu lakini halikuchukuliwa hatua yoyote kwa sababu tajiri mzee Katapila alilikingia kifua! Watu wengi waliotaka kulipa kisasi walimfuata mzee huyu na kumlalamikia, kwa malipo kidogo tu aliwakamilishia kazi zao.
Ni kwa mzee huyu ndiko Tonny alikwenda kueleza shida yake, akalipa kiasi cha pesa ili amfundishe Nancy adabu akidai kitendo alichofanyiwa kilikuwa cha kudhalilisha mno, akiwa amesahau ukatili aliomfanyia Nancy nchini China na kitendo cha kumlisha Yamini na kuharibu kabisa maisha yake.
Kuua, kuteka na kutesa ilikuwa kazi rahisi sana kwa kundi hilo la Lambadamu hivyo baada ya mzee Katapila kupokea maagizo kutoka kwa Tonny na kukabidhiwa hundi yake ya milioni mbili kukiwa na salio la milioni moja aliwaamuru vijana wake kuingia kazini muda huohuo.
********
Alipotoka kituoni Nancy alinyoosha moja kwa moja nyumbani kwao, moyoni mwake akiwa na furaha kwa sababu ya kuridhishwa na hatua zilizochukuliwa na polisi! Alitamani kufika nyumbani mapema ili awasimulie wazazi wake juu ya kilichotokea, alitegemea wangefurahi kama alivyokuwa amefurahi yeye kwani matumaini ya Danny kurejea yalikuwa makubwa!
Hali aliyoikuta nyumbani kwao ilimshangaza, kulikuwa na idadi kubwa sana ya majirani pamoja na maaskari! Moyo wake ulipasuka kwa mshtuko, hakuelewa ni nini kilikuwa kimetokea kwani kulikuwa na kila dalili ya jambo baya. Aliegesha gari upande wa pili wa barabara na kushuka kisha kuanza kutembea kwa haraka kuelekea nyumbani kwao.
“Vipi kimetokea nini?” Nancy alimuuliza mmoja wa majirani.
“Aiseee! Sisi tulifikiri hata wewe umo?”
“Nimo wapi?”
“Walikuja watu na gari, wakaanza kurusha risasi hewani hapahapa nyumbani kwenu kisha tukawaona wakitoka ndani pamoja na watu watatu, wawili niliwatambua, alikuwa baba pamoja na mama yako lakini watatu sikumwelewa! Baada ya hapo niliingia uvunguni mwa kitanda polisi walipokuja ndipo nikajitokeza! Nilifikiri na wewe umetekwa!”
Nancy hakujibu kitu, alimwaga machozi hapohapo na kuanza kutembea kwenda ndani, maaskari wakimfuata kwa nyuma! Sebuleni kwao kulijaa damu, kulikuwa na picha ya wazi kuwa wazazi wake walipigwa risasi kabla ya kutekwa! Alihisi kuishiwa nguvu miguuni, akaketi kwenye kiti na kuendelea kuwaza juu ya yaliyokuwa yakitokea! Ghafla alisikia sauti za watu wakiongea chumbani, alitoka mbio na kufungua mlango! Wadogo zake David na Catherine walilala kitandani wakiwa wamejifunika shuka.
Aliwachukua na kuanza kutembea nao kwenda nje ya nyumba huku yeye na wadogo zake wakiendelea kulia machozi, ilikuwa hali ya kusikitisha! Maisha ya Nancy yalikuwa yameingia kwenye dhoruba nyingine baada ya kutoka katika wendawazimu.
“Kwa mkono wangu nitawaokoa baba, mama, Danny na mzee Mwinyimkuu, nasema damu itamwagika!” Aliongea kwa uchungu Nancy.
Nancy alikuwa amechanganyikiwa kabisa, mambo yalionekana kumtokea kwa ghafla mno! Hakutegemea baba na mama yake wangetekwa, muda wote alikuwa akilia wadogo zake David na Catherine wakiwa mikononi mwake! Hakuacha kuapiza kwamba kwa mkono wake angewaokoa wazazi wake hata kama Polisi wangeshindwa kuwapata, alikuwa tayari kumwaga damu ili mradi wazazi paoja na mume wake mtarajiwa Danny warudi kutoka walikokuwa wamepelekwa.
“Kwa mkono wangu mimi Nancy nitawakomboa, ni bora mimi pia nipoteze maisha yangu! Sitaweza kuishi duniani bila mama na baba yangu!” Aliongea Nancy kwa jazba, hasira kali ilikuwa imemkamata, alielewa wazi yote yaliyotokea yalifanywa na Tonny kama kisasi cha kumkataa, hata hivyo kilikuwa kisasi kikubwa mno.
Baadaye Polisi walimchukua Nancy na wadogo zake hadi kituoni ambako alitoa maelezo ya nyongeza juu ya tukio lililojitokeza, Polisi waliahidi kufanya kila kilichowezekana kumpata mtu aliyefanya tukio hilo, walimhakikisha isingechukua hata siku tatu kabla mzee Katobe, mke wake pamoja na Danny hawajapatikana.
“Ah! Hii kazi ni ndogo kabisa wala usiwe na wasiwasi, wewe tulia sisi tutawaleta wazazi wako nyumbani na mhalifu tutamtia nguvuni! Hii ndio kazi yetu tulia!” Mmoja wa maaskari alisema.
“Nafurahi sana kusikia hivyo! Sijui nitawashukuruje lakini lazima kutakuwa na namna fulani ya kuwapeni shukurani zangu kama baba, mama na mchumba wangu watarudi, huyuhuyu Tonny mliyenaye mahabusu anaelewa kila kitu!”
“Atasema tu wala usiwe na wasiwasi! Tutakupigia”
Nancy aliondoka kituoni na wadogo zake kwenda nyumbani ambako aliendelea kusubiri taarifa za kukamatwa kwa majambazi waliowateka wazazi wake pamoja na mchumba wake Danny, hakubanduka pembeni mwa simu akisubiri simu kutoka kituo cha polisi cha Bagamoyo lakini hakuna simu iliyoingia kutoka Polisi zaidi ya zilizopigwa na watu waliompa pole.
Siku hiyo alilala mpaka asubuhi bila taarifa yoyote na ikapita hadi siku iliyofuata, siku ya tatu saa sita mchana simu iliita! Wakati huo alikuwa ametoka kwenda msalani, alikatisha starehe yake na kukurupuka hivyohivyo hadi sebuleni, kweli simu hiyo ilitoka Polisi.
“Tunakuhitaji uje mara moja hapa kituoni, hili ni agizo kutoka kwa Mkuu wa Kituo!”
“Nipe dakika tano nitakuwa hapo!”
“Tafadhali usichelewe!”
“Nakuja!”
Kabla ya kuondoka alikwenda chumbani kuangalia wadogo zake na kukuta wapo katikati ya usingizi, hakutaka kuwashtua kwani aliamini asingechelewa sana kituoni! Aliinamana na kuwabusu wote wawili usoni kisha kutembea hadi nje ambako aliwasha gari na kuondoka kwa kasi kuelekea kituo cha Polisi.
“Karibu Nancy!” Askari wa kike aliyekuwa mapokezi alimkaribisha, alishafahamika kwa maaskari wengi kituoni hapo
“Ahsante!”
“Umekuja kumwona Mkuu?”
“Ndiyo nimepigiwa simu!”
“Zunguka basi upande huu nikupeleke!”
Nancy alifanya kama alivyoombwa na kuongozwa hadi ofisini kwa Mkuu wa kituo, mzee mfupi mnene alikaa nyuma ya meza akiwa amevaa magwanda ya jeshi la Polisi, alimkaribisha Nancy kitini na baadaye askari aliyempeleka aliondoka na kuwaacha wawili.
Baada ya salamu maongezi kati yao yalianza, mzee huyo aliyejitambulisha kwa jina la Afande Alphonce alianza kumuuliza Nancy maswali juu ya tukio zima ambayo hayakutofautiana sana na maswali aliyokwishakuulizwa na maaskari wa upelelezi kabla. Yote aliyajibu kutegemea na ufahamu aliokuwa nao na mkuu wa kituo alimweleza hatua waliyokuwa wamefikia katika kazi ya kupeleleza.
“Unamhisi nani?”
“Hakuna mtu mwingine ninayemhisi zaidi ya Tonny!”
“Tumemhoji sana lakini inavyoonekana hakuna anachokifahamu na amedhaminiwa na mzee Katapila nafikiri unamfahamu yule tajiri mkubwa jijini Dar es Salaam!”
“Yaani amempa Tonny dhamana?”
“Ni haki yake kudhaminiwa!”
“Hapa lazima kuna kitu kimetendeka sio bure! Mtampaje dhamana wakati wazazi wangu, mzee Mwinyimkuu bado hawajapatikana!” Aliongea Nancy kwa sauti ya juu akisimama na kukiacha kiti, kifua chake kikiwa kimejaa pumzi na kumfanya ashindwe kuongea vizuri
“Nancy...! Tulia kidogo, tafadhali shusha jazba ili tuongee kwa utaratibu, hakuna ushahidi wa kutosha kuwa Tonny ndiye ameshiriki katika kuwateka wazazi wako!”
“Sawa tu! Lakini haki lazima itatendeka na nitahakikisha Tonny na wote walioshiriki wanaingia mikononi mwa sheria!”
“Tutashukuru sana kama utatusaidia maana hii kazi inaonekana kuwa ngumu, vijana wangu wanajitahidi sana lakini hawafanikiwi hata kupata picha ya mahali wazazi wako walipopelekwa na hatuna uhakika kama wapo hai ama wamekufa! Hata hivyo hatujakata tamaa, bado tunaendelea na kazi”
Nancy hakuwa na la kusema tena, muda wote alikuwa akilia! Alikuwa ameingia katika matatizo mengine mazito zaidi baada ya tu ya kuibuka katika tatizo la wendawazimu na yamini aliyokula! Alimlaumu Tonny kwa kila kitu kilichotokea maishani mwake, yeye ndiye alikuwa mkandarasi wa mabaya yote yaliyokuwa yakimtokea.
“Tonny hastahili kuishi!” Aliongea kwa sauti akiketi kitini na baadaye kunyanyuka tena na kumpa mkono mkuu wa Kituo ili waagane.
“Nakushukuru sana kwa kuja binti!”
“Ahsante sana Mkuu, kuna jambo jingine la kuongelea kabla sijaondoka?”
“Hapana! Nenda kama kuna kitu kitajitokeza tutakupigia simu tena”
“Ahsante!”
Nancy alitoka ofisini kwa mkuu wa kituo akijifuta machozi, moyo wake ulikuwa umeongezewa kidonda kingine! Kitendo cha Tonny kuwekewa dhamana na tajiri wakati yeye Nancy alikuwa na uhakika asilimia mia moja ndiye aliyehusika kila kitu juu ya kutekwa kwa wazazi wake, kiliashiria mazingira ya rushwa! Roho ilimuuma sana kugundua hata Polisi aliowategemea kuwa walinzi wa usalama wa Raia walionekana kutokuwa upande wake.
“Sina la kufanya kwa sasa lakini haki lazima itatendeka!” Aliwaza akiingia ndani ya gari akawasha na kuondoka zake akitimua vumbi, moyo wake ulijaa hasira na alikuwa na wasiwasi mwingi moyoni! Kwani maisha yake yalikuwa hatarini kama Tonny alikuwa huru, aliamini angeweza kumfanya chochote lakini yote alimwachia Mungu na tayari alishaanza kukata tamaa.
Aliendesha gari akilia hadi nyumbani kwao ambako aliegesha na kuingia ndani na kujimwaga kwenye kochi ambako aliendelea kulia akiwakumbuka wazazi wake pamoja Danny! Dunia ilikuwa imebadilika kupita kiasi, kwake hapakuwa mahali pa kuishi tena bali jehanamu ndogo. Alishindwa kuelewa angefanya nini kubadilisha hali iliyokuwepo ili mambo yarejee kuwa kama zamani, awe mke wa Danny na arudi Chuo Kikuu kuendelea na masomo yake.
Alikaa sebuleni hadi akapitiwa na usingizi, alipozinduka ilikuwa saa kumi na mbili ya jioni! Alishangaa kuona wadogo zake hawapo sebuleni, kwani kwa wakati huo mara nyingi walizoea kukaa sebuleni wakicheza! Kwa sababu wakati anaondoka kwenda kituoni walikuwa wamealala aliamini bado wapo chumbani, swala hili halikupitishwa moja kwa moja kichwani mwake kwani haikuwa kawaida ya David na Catherine kuwa chumbani muda huo ni hapo ndipo alipoamua kunyanyuka kwenda chumbani kuangalia.
Mlango ulikuwa wazi na kitandani hapakuwa na kitu! David na Catherine hawakuwepo, alitoka mbio na kuanza kukagua vyumba vingine vyote hadi chooni lakini bado hakuwaona! Wasiwasi ulianza kumwingia kuwa huenda akiwa kituoni, baada ya Tonny kupewa dhamana alikwenda nyumbani kwao na kuwateka watoto.
Alitoka ndani ya nyumba na kukimbia nyumba ya jirani kuulizia kama kuna gari lilifika nyumbani kwao mchana akiwa kituoni, hakuna aliyeonakana kufahamu! Nancy alizidi kuchanganyikiwa, alirudi tena ndani na kuendelea kupekua lakini David na Catherine hawakuwepo! Alilia kwa uchungu.
Hakuwa na la kufanya zaidi ya kupiga simu polisi kuwataarifu juu ya kilichotokea, aliunganishwa moja kwa moja na mkuu wa kituo na kumweleza mambo yaliyotokea akilitupia lawama jeshi la Polisi kwa kumwachia Tonny ili aende kuwateka wadogo zake pia.
“Hivyo ndivyo unavyofikiri?” Mkuu wa Kituo aliuliza.
“Ndio!”
“Basi shauri yako!” Aliongea Mkuu wa Kituo na kukata simu.
Nancy alibaki akilia machozi na aliendelea usiku mzima hadi asubuhi saa kumi na mbili aliposhtuliwa na mlio wa simu akanyanyuka na kuikimbilia akitegemea ingekuwa ni taarifa ya Polisi wakimweleza mahali baba, mama, Danny, wadogo zake na mzee Mwinyimkuu walikokuwa.
“Haloo!” Ilikuwa sauti ya mtoto mdogo na kwa kuisikiliza mara moja Nancy aliweza kuitambua, alikuwa mtoto David.
“Ndiyo! Mko wapi?”
“Tuko...!Tuko...!” Mtoto hakuweza kueleza, sauti nzito ya mwanaume ilisikika.
“Nancy za siku nyingi?”
“Nzuri nani anaongea?”
“Mimi? Umenisahau?”
“Siwezi kukumbuka kwenye simu mpaka uniambie unaitwa nani?”
“Unakikumbuka kisiwa cha Galu?”
“Ndiyo!”
“Unakumbuka wazee wawili wanaoitwa Mzee Kiwembe na Babu Ayoub?”
“Ndiyo!”
“Basi tulikuja kuchukua watoto wetu na hivi sasa tuko njiani kurejea kwetu!”
“Mlipafahamu vipi nyumbani na namba ya simu mmeitoa wapi?”
“Hiyo siyo kazi ngumu sana kwetu, tumekaa Bagamoyo kwa wiki nzima!”
“Kwa hiyo hata wazazi wangu mmewateka nyinyi?”
“Hapana, hatujahusika! Hatukuwa na sababu ya kufanya hivyo! Sisi pia tulisikia tu baba na mama yako wametekwa na watu wasiojulika.....!”
Simu ilikatika na Nancy alibaki kusubiri ilie tena lakini jambo hilo halikutokea, aliendelea kuwalilia wadogo zake! Alishawazoea na hakuwa tayari kuwaacha warejee mikononi mwa wazee hao hatari, aliamini siku moja lazima angewakomboa ingawa hakuelewa ni kwa njia zipi.
Saa nne na nusu za asubuhi simu ililia tena, alinyanyua na kuipokea akiamini ilitoka kituo cha Polisi, ilikuwa sauti ya mwanamke akiongea kwa nyodo!
“Halooo wewe ni nani?”
“Unataka kunifahamu?”
“Ndiyo!”
“Ni mimi mke mwenzio! Mambo uliyonifanyia kanisani sijayasahau, aibu niliyoipata siku hiyo sitoisahau pia ndio maana niliamua kuacha chuo ili nimfundishe adabu huyu mwendawazimu! Hebu kwanza ongea naye” Aliongea mwanamke huyo bila kutaja jina lake.
Sekunde chache baadaye sauti ya kiume ilisikika, alikuwa Danny akiongea huku akilia! Damu katika mwili wa Nancy ilikwenda kasi huku moja ukimdunda kwa nguvu kama uliotaka kuchomoka kifuani kwake! Danny alielezea mateso aliyokuwa akipata huku akilia, Nancy alishindwa kujizuia naye akajikuta akibubujikwa na machozi.
“Uko wapi?”
“Sijui mahali nilipo maana wakati naletwa hapa nilikuwa nimefungwa na kitambaa cheusi usoni!”
“Uko na baba na mama yangu?”
“Hapana!”
“Huyo mwanamke ni nani?”
“Ni Agness! Niliyemwacha kanisani siku ya ndoa kwa sababu yako, aliamua kukodisha watu kunileta hapa kuteswa! Kama unaweza kuja kuniokoa tafadhali fanya hivyo, wataarifu polisi kama wewe huwe......!”Hakuyamalizia maneno yake, kukatokea ukimya wa sekunde kadhaa ndipo baadaye ikaibuka sauti ya kike.
“Usijisumbue kutoa taarifa polisi! Kaa mbali na jambo hili kama unataka kuishi, vinginevyo utapoteza uhai wako!”
“Huwezi kuniua! Malaya mkubwa weee! Na ninakueleza kwa mkono wangu nitakufikisha mbele ya sheria na nitamkomboa Danny kabla hujamfanya lolote!”
“Unanitukana mimi? Unataka nikufanyizie?”
“Fanya lolote unalotaka!”
“Poa!” Agness alijibu na simu kukatika akimwacha Nancy mwenye wasiwasi mwingi juu ya maisha yake.

Je nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 30
Tayari Nancy amekwishagundua kuwa wadogo zake Catherine na David wametekwa na mzee Kiwembe pamoja na Babu Ayoub! Danny naye ametekwa na Agness, mchumba wake wa zamani aliyemwacha kanisani siku ya ndoa baada ya Nancy kurejea.
Mpaka sasa haelewi mahali wazazi wake walipo na kama wao pia walitekwa na Agness au Tonny! Amechanganyikiwa hajui la kufanya ingawa ni lazima awaokoe wazazi, wadogo, Danny na mzee Mwinyimkuu! Huu ni wajibu wake hawezi kuukwepa na yuko tayari kupoteza maisha yake kama itabidi lakini awaweke watu hawa huru.
Je, nini kinaendelea? Fuatilia...........

Hakuna kilichomuumiza Agness moyo kama kitendo cha kuachwa na Danny kanisani mbele ya Padri kisa kikiwa ni kurudi kwa Nancy! Alilia kwa uchungu na kuondoka kanisani yeye na ndugu zake wakiwa wamejaa gadhabu, hakuna walichokifikiria zaidi ya kisasi kwa Danny kwa aibu aliyosababishia ukoo wao.
“Anastahili kufa! Hakuna kitu kingine kinachostahili kuwa adhabu kwa Danny isipokuwa kifo! Ametufanyia kitendo cha aibu sana katika familia yetu, hakika hastahili kuhurumiwa!” Walisema baadhi ya ndugu wa Agness wakiingia katika magari tayari kwa kuondoka eneo la kanisa.
Ilikuwa aibu iliyomkera kila mtu, Agness hakuwahi kuwaeleza ndugu zake juu ya msimamo wa Danny kuhusu msichana Nancy! Kwamba alikuwa naye lakini kama ingetokea akarudi basi angelazimika kumwacha na kurudiana na mpenzi wake wa zamani. Akiufahamu ukweli huo Agness aliwaunga mkono ndugu zake.
Kikao cha siri kilifanyika usiku wa manane nyumbani kwao Agness Jijini Dar es Salaam, mara tu walipowasili kutoka Bagamoyo! Pamoja na kusafiri umbali wa kilometa zaidi ya hamsini kutoka Bagamoyo mpaka Dar es Salaam bado mioyo ya ndugu wengi wa Agness hata wazazi wake ilijawa na hasira.
Mauaji ya Danny yalitawala mjadala katika kikao hicho, kila mtu alitaka Danny auawe tena kwa mateso makubwa iwe fundisho kwa watu wenye tabia za kudhalilisha watoto wa watu, Agness hakutetea kitu chochote hata yeye alikuwa tayari kuona Danny anakufa, muda wote alikuwa akilia machozi ya uchungu akilaani kitendo alichofanyiwa, hakutaka kukubali ukweli kuwa aliwahi kuelezwa na Danny juu ya Nancy.
“Ni heri tukose wote! Hata huyo mwendawazimu wake pia akose mume!” Aliwaza Agness akibubujikwa na machozi.
Familia ilikubaliana kufanya mauaji ya siri kubwa, mzee Elibariki Shao, baba mdogo wa Agness na mfanyabiashara maarufu jijini Dar es Salaam aliyemiliki vituo vingi vya mafuta aliahidi kushughulikia suala hilo yeye mwenyewe tena kwa gharama zake bila kushirikisha familia, alionyesha wazi chuki yake kwa Danny na kusema kilichofanyika ilikuwa ni aibu kwa ukoo mzima wa Shao.
Hapakuwa na mtu mwingine wa kutatua tatizo hilo, ni mtu mmoja tu ambaye mzee Shao alimfikiria! Hakuwa mwingine bali mzee Katapila, mtaalam wa mauaji tena kwa gharama nafuu! Baada ya kikao usiku huohuo kwa kutumia simu yake ya mkononi alipiga namba ya mzee Katapila na kupanga kukutana naye siku iliyofuata ili ampe kazi ya kufanya.
“Mtu kakuudhi nini?”
“Ebwanae duniani hapa hata ukitulia watu watakuchokoza!”
“Kakufanya nini?”
“Siwezi kuongea kwenye simu, simu zetu wengine zinasikilizwa nataka kukutana na wewe ana kwa ana!”
“Basi kesho saa nne asubuhi njoo ofisini kwangu!”
“Sawa rafiki!”
Walikuwa marafiki wa siku nyingi sana, waliowahi kushirikiana katika biashara mbalimbali na mzee Shao alikuwa na uhakika kwa kumtumia mzee Katapila kazi yake ingefanyika! Alisifika kwa kazi za ujambazi ingawa alikuwa mtu tajiri pengine katika nafasi ya pili au ya tatu jijini Dar es Salaam.
“Kazi imemalizika! Niachieni kila kitu na nitakifanya kwa uaminifu!” Mzee Shao aliwaambia ndugu wote waliokusanyika kabla hawajasambaa, ilikuwa tayari ni Alfajiri.
*********
Mzee Shao hakulala usingizi wala kukigusa kitanda chake, alichofanya baada ya kufika nyumbani kwake ni kuoga na kujiandaa kwenda ofisini kwake jengo la IPS katika ya jiji la Dar es Salaam, alijishughulisha na biashara ya kusafirisha mizigo ndani ya nje ya Tanzania akiwa na kampuni yake ya East African TransCargo.
Asubuhi hiyo ingawa ilikuwa siku ya Jumapili alikuwa na kazi za kufanya kabla hajaelekea ofisini kwa mzee Katapila na alimaliza kila kitu ilipogonga saa nne kasorobo na taratibu akajikongoja kwa miguu kuelekea kwenye ofisi ya mzee Katapila iliyokuwa ndani ya jengo lake refu la Katapila House lililokuwa mtaa wa Jamhuri.
“Binti naomba kumwona bosi!”
“Nimwambie nani?”
“Rafiki yake Elibariki!”
“Alishanitaarifu juu ya ujio wako, tafadhali karibu anakusubiri!”
“Ahsante!”
Mzee Katapila alimkaribisha mzee Shao ofisini kwake, baada ya salamu hakutaka kupoteza muda, alianza kueleza shida yake mara moja akionekana mwenye jazba aliyepania kufanya mauaji! Muda wote akiongea mzee Katapila alikuwa akitabasamu na kutingisha kichwa chake.
“Aisee! Hiyo ni kazi ndogo lakini lazima uhakikishe kuwa hutoboi siri mahali popote, kama ikitokea ukafanya hivyo basi hata wewe mwenyewe rafiki yangu maisha yako yatakuwa hatarini, nafikiri sifa zangu unazisikia!”
“Ah! Nakufahamu!”
“Nitakusaidia kufanya unavyotaka, lakini uwe tayari kunilipa milioni tano!”
“Hilo sio tatizo!”
“Nielekeze mahali anapoishi, baada ya kufanya kazi ndio utanilipa pesa!”
“Sina uhakika sana anaishi wapi labda jambo hilo nilifanyie kazi baada ya kutoka hapa!”
“Sasa bahati mbaya mimi ninasafiri kwenda Afrika Kusini nitarudi baada ya wiki moja, usiwe na wasiwasi kazi yako nitaifanya baada ya kurudi!”
“Nakutegemea wewe!”
Hapakuwa na maongezi zaidi baada ya hapo, waliagana mzee Shao akarudi ofisini kwake ambako baadaye aliwapigia simu baadhi ya ndugu akiwemo Agness wakakusanyika na kuliongelea suala hilo, kila mtu alikuwa bado amedhamiria kufanya mauaji ya Danny.
Wiki moja baadaye mzee Katapila alirejea na kupewa maelekezo yote juu ya mahali Danny alikoishi, hakuwa mahali pengine zaidi ya nyumbani kwa mzee Katobe akisubiri kufunga ndoa na Nancy! Jambo hilo ndilo lilitaka kuzuiliwa haraka iwezekanavyo, ilikuwa ni lazima Danny atekwe na kuuawa kabla ndoa haijafungwa.
“Ndoa haitafungwa! Leo hiihii nawatuma vijana wangu kwenda kufanya kazi huko huko Bagamoyo! Mnataka tumuue palepale?”
“Hapana! Ni lazima ateswe kwanza!”
“Kwa hiyo baada ya kumteka tumpeleke wapi?”
“Tafuta mahali tumhifadhi!”
“Ninalo ghala langu lililowahi kuwa kiwanda cha Fenicha huko Vingunguti, kwa hivi sasa halitumiki ila kuna walinzi wa Omega Security wanaolinda kwa nje, hawaruhusiwi kuingia ndani kwani kuna vitu vyangu muhimu na vya siri navihifadhi!Ninaweza kutoa chumba kimoja pale ili ateswe vizuri lakini itawalazimu mniongezee shilingi milioni moja!”
“Haina tatizo, tunachotaka sisi ni kutoa mfano, aliyekuwa bibi harusi mtarajiwa amekasirika sana!”
“Basi niachieni mimi, kesho usiku njooni nitawapeleka mahali atakapokuwa!”Mzee Katapila alimwambia mteja wake.
Jambo hilo lilifanyika, Danny akawa ametekwa kutoka nyumbani kwa mzee Katobe na kusafirishwa hadi Vingunguti akafichwa ndani ya ghala la mzee Katapila, siku hiyo hiyo Agness alifika ghalani na baadhi ya ndugu na mateso yakaanza rasmi kabla Danny hajauawa.
*********
Kugundua kuwa Danny hakutekwa na Tonny isipokuwa Agness kulimwongezea Nancy hasira! Aligundua ni kazi kubwa kiasi gani aliyokuwa nayo mbele yake lakini ilikuwa ni lazima aifanye kwani hapakuwa na mtu mwingine wa kuwakomboa wazazi, mchumba, mzee Mwinyimkuu pamoja na wadogo zake waliotekwa.
“Lazima niwakomboe! Hata kama kuna vitisho kiasi gani, Agness ni mwanamke kama mimi! Simjui kwa sura wala umbile lakini nitapambana naye!”Aliwaza Nancy.
Ni kweli hakumkumbuka Agness kwa sababu siku aliyoingia kanisani na kukuta ndoa kati ya Danny na Agness ikiwa mbioni kufungwa, alikuwa ni mwendawazimu ambaye hakuelewa chochote.
Alitamani kuwa mtaalam wa silaha ili aweze kupambana vizuri na alihitaji kuwa na bunduki yake lakini hakuwa na uwezo huo, alielewa wazi kupambana kwa mikono na watu wenye silaha lilikuwa jambo gumu kwake kupata mafanikio! Fikra za mafunzo ya Mgambo zilimwingia na siku hiyo hiyo alianza kufutilia suala hilo, ikawa kama bahati alipofika ofisini kwa mshauri wa Mgambo alikuta watu wakijiandikisha naye alifanya hivyo mara moja.
“Sasa kazi wataipata, mambo yanakwenda kama nilivyopanga!” Aliwaza Nancy.
Siku iliyofuata aliingia uwanja wa shule ya msingi Mwanamakuka, akiwa na kundi la vijana kama themanini na kuanza mafunzo, kwa wiki mbili kazi ilikuwa hiyo na tayari alishafundishwa jinsi ya kutumia bunduki aina ya SMG na hata mazoezi ya kulenga shabaha yalishafanyika, mafunzo yalikwenda haraka kuliko kawaida kwa sababu vijana waliohitaji mafunzo walikuwa wengi.
“Sihitaji kitu zaidi, nilichotaka mimi ni kuelewa kutumia bunduki basi hakuna zaidi!”Aliwaza Nancy.
Tangu siku hiyo hakwenda tena uwanjani, alishinda nyumbani akifikiria ni kitu gani cha kufanya na akiwawazia sana wazazi, wadogo na mchumba wake! Aliamini walikuwa mahali fulani wakisubiri msaada wake kuwaondoa katika mateso, alitamani kumfuata Tonny kumwomba msaada kwani alishagundua wazi hakuwa na hatia.
Akiwa katika mawazo hayo simu iliyokuwa mezani ililia na kwa unyonge alinyanyuka na kuifuata, mawazo yake yote yakaimini ilikuwa ni simu kutoka polisi ambao alikuwa hajasikia kitu chochote kutoka kwao.
“Halow!”Aliita lakini hakuitikiwa, alichokisikia upande wa pili ni kwikwi za mtu akilia kwa uchungu.
“ Wewe nani?” Alizidi kuuliza lakini bado hakujibiwa, wasiwasi ulizidi kumwingia.
“Mimi...! Mimi...!Ni mama yako!”
“Mama! Mama!Mko wapi?”
“Sielewi hapa tulipo ni wapi ila elewa tuko katika mateso makali na tunahitaji msaada wako, baba yako ana hali mbaya sana kama unaweza tafadhali njoo!”
“Mko na Danny?”
“Hapana! Tupo na baba yako pamoja na mzee Mwinyimkuu!”
“Wapi?”
Simu ilikatika kabla hajapewa jibu, Nancy akazidi kuchanganyikiwa na wajibu ukazidi kuongezeka, uchungu mkubwa ulimshika moyoni na kujikuta akiyaona maisha yake hayana thamani yoyote! Alikuwa tayari kufa lakini aokoe maisha ya wazazi wake, hakuna kitu kilichowahi kuumiza moyo wake kama kumsikia mama yake akilia kwa sauti aliyoisikia kwenye simu.
“Kwa ujuzi mdogo nilioupata, hakika nitawakomboa wazazi wangu! Si wazazi wangu tu bali pia Danny, wadogo zangu na mzee Mwinyimkuu!” Aliongea peke yake Nancy akikaa kitini, mwili wake wote ulikuwa ukitetemeka kwa hasira.
“Haiwezekani! Iko namna, lazima nijue hawa watu wanapiga simu kutoka wapi, huo ndio utakuwa mwanzo wa upelelezi wangu, polisi wamenitelekeza lakini nitafanya kazi mwenyewe mpaka niwafikishe wahalifu mbele ya sheria!”Aliwaza Nancy na kuyaona mawazo yake yalikuwa sahihi.
Alitoka nje na kuingia ndani ya gari tena bila kufunga mlango wa nyumba na kuondoka kuelekea ofisi za Kampuni ya Simu. Saa, dakika, sekunde za nyakati ambazo simu zote ziliingia alikuwa nazo kwenye kitabu chake kidogo! Hilo ndilo jambo muhimu alilokumbuka kufanya. Dakika kumi baadaye aliegesha gari mbele ya jengo la Kampuni ya Simu lililo kandokando ya barabara mara tu uingiapo Bagamoyo.
“Dada samahani!” Alianza kumwambia mfanyakazi wa kampuni ya simu baada ya salamu.
“Sema nikusaidie!”
“Naomba uniangalizie, kuna simu tatu zimeingia kwenye nyumbani kwetu, moja leo na nyingine mbili ni wiki mbili zilizopita lakini nakumbuka muda ambao ziliingia!”
“Sasa nikusaidiaje?”
Kabla Nancy hajasema lolote aliingiza mkono wake kwenye mkoba na kuchomoa noti nne za elfu tanotano akaziweka mezani, mfanyakazi wa Kampuni ya Simu alionyesha mshangao wa ajabu, hakuelewa fedha hizo zilikuwa za kazi gani.
“Hiyo siyo Rushwa ni shukrani kwa kazi utakayonisaidia, naomba tu uniangalizie hizo namba ni zipi na zilipigwa kutoka wapi!”
“Sawa lakini hapa siwezi kukusaidia! Hatuna huo mtambo acha nipige Dar es Salaam makao makuu kuna rafiki yangu atakusaidia!”
“Mungu akubariki sana!” Aliongea Nancy akionyesha meno yake nje kama dalili ya tabasamu, moyoni alikuwa akisali ili aweze kubahatisha kuelewa namba hizo zilipigwa kutoka wapi! Huo ndio ungekuwa mwanzo wa kazi yake ndefu.
Mfanyakazi wa Kampuni ya Simu akiwa amefurahishwa na fedha iliyokuwa mezani kwake, alinyanyua simu na kupiga Makao makuu na kuomba kuongea na rafiki yake aitwaye Linda na kumweleza shida yake, alimtajia namba ya simu ya nyumbani kwa mzee Katobe pamoja na nyakati ambazo simu hizo ziliingia. Dakika tano baadaye alikuwa na jibu.
“Hii ya leo ni namba 2181719, inatoka Dar es Salaam, mwenye simu ni Kampuni iitwayo Tanbrand Funitures Ltd na hii namba 0222468 inatoka Kilosa, inamilikiwa na mtu anayeitwa Abdulmarik Issa! Hii ya tatu ilipigwa kutoka Nzega, Shinyanga bahati mbaya jina la mwenye simu halikujulikana mara moja, inavyoonekana ni hizi simu za kupiga kwenye vibanda!”
“Ahsante sana dada! Umenisaidia kuliko unavyofikiria, chukua na hii!” Nancy alimkabidhi noti nyingine ya shilingi elfu tano meno yote thelathini na mbili ya mfanyakazi wa Kampuni ya Simu yakawa nje.
Nancy aliondoka na kurejea nyumbani ambako alijifungia chumbani na kuanza kulia, alielewa kazi iliyokuwa mbele yake ilikuwa ngumu na pengine yenye mateso mengi ambayo yangeweza hata kumgharimu maisha yake! Hakujihurumia hasa alipowafikiria wazazi na wadogo zake na alikuwa tayari kwa lolote.
Alilia usiku mzima mpaka kukacha, asubuhi hiyo alikuwa na azimio moja kichwani mwake! Kuanza na Dar es Salaam kabla hajaenda Kilosa na baadaye ziwa Tanganyika alikoamini wadogo zake walipelekwa.
“NAANZA NA DAR ES SALAAM! DAMU ZA AGNESS NA NDUGU ZAKE WOTE NI HALALI YANGU NI LAZIMA DANNY AWE HURU!”Alisema Nancy kwa uchungu.
Hakuwa na jambo jingine la kufanya Bagamoyo, hakuna kilichosalia kwake! Wazazi hawakuwepo, wadogo zake hawakuwepo na wote pamoja na mchumba wake Danny walikuwa katika mateso, alitoka ndani ya nyumba na kufunga mlango akaingia ndani ya gari la baba yake ambalo wakati huo lilikuwa ni kama mali yake, alipoiangalia nyumba yao machozi yalizidi kumtoka aliamini hiyo ilikuwa mara yake ya mwisho kuiona nyumba yao.
“Buriani!” Alitamka maneno hayo akiingia garini na kuondoka,hakuwa na uhakika kama angerudi tena Bagamoyo akiwa hai.

Je nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 31
Nancy amefanikiwa kumwokoa Danny kutoka katika ghala la mzee Katapila huko Vingunguti, wote wawili wanachukua gari la mzee Katapila hadi Kimara ambako wanakodisha teksi inayowapeleka hadi kijijini Tindiga huko Kilosa shambani kwa mzee Katapila.
Ni huko ndiko wazazi wa Nancy pamoja na mzee Mwinyimkuu wamefungiwa wakiteswa, lengo lao ni kuwaokoa na wanafanikiwa kuingia ndani ya ngome ya shamba hilo, Danny amepigwa mshale mbavuni na Nancy amewekwa chini ya ulinzi na mlinzi wa Kimakonde aliyeuvuta upinde wake sawasawa tayari kwa kuuachia ili uzame katika nyama za msichana huyu jasiri.
Je, nini kinafuata? Atafanikiwa kuwaokoa wazazi wake? Nini hatima ya Danny ambaye mshale umezama mbavuni kwake? Endelea.........

Nancy alibaki amepiga magoti chini pembeni mwa Danny akitetemeka mwili mzima, ingawa hali ilikuwa ya baridi alihisi jasho jembamba likimtoka na kulowanisha nguo zake! Mzee mfupi, mwenye misuli alisimama nyuma yake akiwa ameuvuta upinde wake sawasawa tayari kwa kuachia mshale, kulikuwa na kila dalili kama Nancy angejitingisha au kutotii amri aliyokuwa amepewa, mshale ungezama kifuani kwake na huo ndio ungekuwa mwisho wa maisha yake, yeye na Danny wangekufa kabla hata ya kuwakomboa wazazi wake.
“Mzee naomba usiniue, najua unao uwezo wa kufanya hivyo lakini tafadhali sana nisikilize!” Aliomba lakini mzee huyo hakumjali.
“Huchikii siyo? Nimesema uchijitingiche, uchigeuke, uchikae, uchichimame, uchicheke wala uchiheme!” Aliendelea kusisitiza mzee huyo akimaanisha Nancy asiongee chochote, kulikuwa na kila dalili hapakuwa na utani katika maneno yote aliyoyasema.
Kulikuwa na mambo mawili tu ya kuchagua kwa Nancy, aidha kusubiri kifo kwa mshale au kujaribu kujiokoa kwa namna yoyote ile! Hakuwa na uhakika kama chaguo lake la pili lingefanya kazi lakini pia hakuwa tayari kusubiri kifo chake kama kondoo, nguvu ya ajabu ilimwijia mwilini mwake, ilikuwa ni lazima aitumie bastola iliyokuwa pembeni mwake kujiokoa.
Akili yake ilifanya kazi kwa kasi, akayumba kidogo kuelekea kulia kisha kurudi haraka kushoto, alishangaa kuona mshale ukipita kwa kasi kuelekea mbele, ulikuwa umemkosa kidogo tu! Alimshuhudia mzee huyo akipinda mkono wake mgongoni kuchomoa mshale mwingine lakini kabla hajafanikiwa kufanya hivyo tayari Nancy alishainyakua bastola yake ardhini na risasi moja ilizama katikati ya kifua cha mzee huyo akaanguka chini bila kupiga kelele, kwa Nancy ulikuwa ni ushindi.
“Haleluya!” Nancy alijikuta akitamka maneno haya bila kutegemea, furaha kubwa ilimjaa moyoni kuona amekiepuka kifo.
Bila kuchunguza kulikuwa na walinzi wengine, alimgeukia tena Danny aliyekuwa kimya na kuanza kumwita huku kwa mara nyingine akijaribu kuung’oa mshale! Danny aliyekuwa kimya alipiga kelele kwa maumivu akimwomba auache kama ulivyo.
“Nia..che!Nia..che dar..ling, nenda kaja..ribu kuwaokoa wazazi kwangu mimi imeshindikana!” Aliongea Danny kwa taabu.
“Haiwezekani! Haiwezekani Danny, huwezi kufia hapa!”
“Sasa uta..fanya ki...tu gani?”
“Lazima kuna njia ya kuokoa maisha yake!” Aliwaza Nancy na kwa haraka alimsogelea mzee aliyempiga risasi, akamvua mashuka aliyovaa na kuyafunga mwilini akizifunika nguo alizovaa! Alimalizia kwa kuchukua kofia ya mzee huyo iliyotengenezwa kwa nyasi na kuivaa kichwani.
Nancy alitaka kujibadilisha afanane na walinzi wa shamba la mzee Katapila ili kufanya kazi ya ukombozi iwe rahisi, alikuwa amebakiza hatua moja tu, kuingia ndani ya jengo kubwa lililokuwa mbele yake na kuwakomboa wazazi wake lakini hatua hiyo aliamini ndiyo ilikuwa ngumu kuliko zote zilizotangulia.
Hakuelewa nguvu zilizomiminika mwilini mwake zilitoka wapi kwani hata siku moja hakuwa kutegemea angeweza kumbeba mtu mwenye uzito mkubwa kama Danny lakini alishangaa kuona anamnyanyua na kumweka begani kwake na kukimbia naye kusonga mbele bastola ikiwa mkononi.
Alipokuwa umbali kama wa mita hamsini kutoka kwenye jengo hilo, alimlaza Danny chini kwa uangalifu ili mshale usizidi kuzama, alikuwa kimya kabisa na hata alipomwita hakuitika! Nancy alilia na kupoteza kabisa matumaini ya kumwokoa mwanaume aliyempenda na kumhitaji maishani mwake.
“Danny!Danny! Danny!” Alizidi kumwita lakini bado aliendelea kuwa kimya.
Alinyanyuka na kusimama wima akimwangalia kwa macho ya huruma, muda ulikuwa ukizidi kusonga na giza kupungua, alielewa muda mfupi uliofuata ingekuwa alfajiri na ilikuwa ni lazima afanye kila kitu wakati bado kuna giza! Ni hapo ndipo alipojikuta akiamua kumwacha Danny mahali hapo na kusonga mbele, kila kitu akikikabidhi mkononi mwa Mungu! Aliamini kuna wakati binadamu anatakiwa kuchagua moja na haikuwa rahisi kukiongezea uhai kitu ambacho Mungu mwenyewe alikuwa ameamua kife.
Alipiga magoti tena akainamisha kichwa chake na kusogeza mdomo wake karibu kabisa na sikio la Danny na kuanza kuongea masikioni mwake maneno aliyoamini yalikuwa ya mwisho.
“Danny ninakupenda, najua unanisikia! Nakuacha hapa nasonga mbele, kuna mambo mawili yanayoweza kutokea, aidha ninaweza kuungana na wewe ahera muda huuhuu au ukanitangulia kidogo lakini nina uhakika siku moja lazima tutakutana! Penzi lako kwangu lilikuwa la kweli, hakuna mwanaume atakayenipenda kama ulivyofanya wewe!...” Nancy hakumaliza sentensi yake hasira ikampanda, kifo cha Danny kilimuongezea uchungu.
Alinyanyuka na kuanza kukimbia kusonga mbele, hali ilikuwa kimya na hapakuonekana mlinzi yeyote! Hata hivyo hakutaka kujiingiza hatarini, alianza kutambaa kwa tumbo kuelekea mbele ya nyumba alikoamini kulikuwa na mlango. Alifanya kila kitu kwa uangalifu mkubwa akielewa eneo alilokuwepo lilikuwa ni la hatari, mbele kwenye kona akiwa amelala kifudifudi alichungulia na kuona watu wawili wenye bunduki wakiwa wamesimama na kulilinda lango.
“Hawa hawa ndio naanza nao!” Alijisemea na kunyanyuka kisha kuruka kwenda mbele huku risasi zikifyatuka kutoka kwenye bastola yake, kila kitu kilikwenda kama alivyotaka! Walinzi wote wawili walikuwa chini, Nancy alijishangaa alifanya kazi kama mtu aliyepitia mafunzo ya Ukomandoo.
Alikuwa na uhakika kabisa bastola yake ilikuwa inakaribia kuishiwa risasi, alichofanya akiamini mbele yake kulikuwa na kazi kubwa ni kuchukua moja ya bunduki za walinzi waliolala mbele yake! Hapo akawa na uhakika wa kuendelea na mapambano zaidi.
Akiwa mlangoni alisikia sauti za watu wakilia ndani ya jengo hilo, bila kufikiria mara mbili alizitambua sauti, walikuwa ni baba na mama yake! Kulikuwa na sauti nyingine nzito ambazo hakuzitambua. Nancy aliikosa thamani ya maisha yake mwenyewe, hakuona sababu ya kuendelea kuishi wakati wazazi wake walikuwa ndani ya jengo hilo wakiteseka na wakimtegemea yeye kuwaokoa.
“Ni bora kufa!” Alijisemea maneno hayo alichungulia ndani kupitia kwenye tundu la mlango, kulikuwa na mwanga mkali sana ndani ya jengo hilo uliomfanya awaone wazazi wake wakiwa wamelala chini uchi wa mnyama na mwanaume mmoja mwenye nguvu akiwachapa! Alijaribu kumtambua mwanaume huyo kuona kama alikuwa Tonny lakini haikuwa sura ya mtu aliyemfahamu, alielewa walikuwa ni vijana wa mzee Katapila.
Hasira aliyokuwa nayo moyoni mwake ilikuwa haielezeki, alikuwa ni kama Simba aliyejeruhiwa! Tayari alishaua watu wengi na alikuwa amempoteza mpenzi wake, hivyo hakuona sababu ya kushindwa kuingia ndani ya jengo hilo na kujaribu kuwaokoa wazazi wake, ingawa hakuwa na uhakika wa kupata ushindi alikuwa tayari kujaribu.
“Mh! Kumbe mlango haujafungwa?” Alijiuliza baada ya kugundua mlango ulikuwa wazi na hapo hapo bila kusita aliusukuma na kuingia moja kwa moja ndani, mkono mmoja ukiwa umeshika bunduki aina ya SMG aliyoichukua kwa mmoja wa walinzi na mwingine ukiwa umeshika bastola yake ambayo awali ilimilikiwa na mzee Katapila.
Risasi zilimiminika kutoka kwenye SMG na kuwaangusha watu watatu waliokuwa wamesimama wakiwatesa wazazi wake, akasonga mbele mbio hadi mahali hapo akiangaza huku na kule kuona kama kulikuwa na adui mwingine, hakumwona! Kwa sababu hakuwa na uhakika kama maadui waliokuwa chini walikuwa wamekufa alilazimika kuwaongezea risasi nyingine mbilimbili kutoka kwenye bastola yake, akahakikisha alikuwa salama.
“Nan..cy! Nan..cy!Na..ncy, Nancy mwanangu umefi....” Sauti ya mama yake iliongea kwa taabu, hakuweza kuimaliza sentensi yake.
Wazazi wake walikuwa wamelala sakafuni wakiwa wamefungwa kwenye vipande vya magogo, miili yao ilijaa majeraha ya kuchapwa, mzee Katobe hakuwa hata na uwezo wa kuongea lolote na hata mzee Mwinyimkuu pia alikuwa kimya! Ilivyoonekana wanaume walipigwa zaidi kuliko mama yake.
“Namshukuru Mungu mama! Sikutegemea hata kuwatia machoni, nimepita katika magumu mengi na siamini kama nitaweza kuwaokoa lakini acha nijaribu!”
“Hata tusipookoka si mbaya, ili mradi nimekuona mwanangu, nilikuwa na masi...kitiko makubwa sana kufa bila kukuambia maneno ya mwi...sho, kwa hivi sasa niko tayari kufa!Hata baba yako alitamani sana ku..kuona lakini ba.hati mbay...a tan..gu jana hao...ngei” Aliongea mama yake Nancy kwa taabu.
Nancy hakutaka kupoteza muda zaidi ilikuwa ni lazima awafungue kwenye magogo na kuwaweka huru ingawa hakufahamu angeondoka eneo hilo kwa utaratibu gani! Ndio, aliliona gari aina ya Landrover nje wakati akiingia ndani ya jengo lakini hakuelewa ni nani alikuwa na ufunguo wa gari hilo.
Mara moja alianza kumfungua mama yake, kisha baba yake na mwisho kwa mzee Mwinyimkuu lakini kabla hajamaliza alisikia sauti ya Tonny nyuma yake, akitokea kwenye mlango wa nyuma wa jengo hilo! Alikuwa na bastola mkononi, hasira ya Nancy iliongezeka maradufu, alimchukia mwanaume huyo kuliko kiumbe mwingine yeyote lakini hakuwa na la kufanya kwani hakuwa na bunduki mkononi mwake wakati huo, aliiweka pembeni kipindi akimfungua mama yake kutoka kwenye gogo! Kitendo chochote cha kujaribu kuichukua kingemaanisha kifo chake, Tonny asingemwacha hai.
“Nakupongeza sana Nancy kwa kazi nzuri uliyoifanya, wewe ni mwanamke hodari kwa kweli umejitahidi sana kutaka kuwaokoa wazazi wako lakini nakuhakikishia hautafanikiwa kwa hilo! Mambo yalipofika ni pabaya na kuwaokoa kwako kutamaanisha mimi kuingia matatizoni na hatimaye kwenda jela, sasa ni kipi bora? Kwanini nisikuue wewe, kuwaua wazazi wako na baadaye mimi mwenyewe kujimaliza kwa risasi?”
“Tonny ni lazima ukumbuke kuwa mimi na wewe tuliwahi kuwa wapenzi na tulishirikiana mambo mengi, kwanini leo tumefika hapa?” Nancy alijaribu kubembeleza.
“Usijaribu kunilaghai ili baadaye unigeuzie kibao, lazima ufe Nancy! Tena sasa hivi sikupi hata muda wa kusali sala yako ya mwisho!” Alisema Tonny akiwa amemlenga Nancy katikati ya paji lake la uso.
“PAAAAAAAA!” Ndio mlio uliosikika ndani ya jengo hilo.

Je nini kitaendelea?
Je Nancy amepigwa risasi na kufa?
 
SEHEMU YA 32
Danny amechomwa mshale kwenye mbavu wakiwa ndani ya ngome ya shamba la mzee Katapila,hajitambui na kuna dalili kwamba tayari amekwishakufa! Nancy analia kwa uchungu na kukosa jambo analoweza kufanya ili kuokoa maisha ya mchumba wake, anaichukulia hiyo kama kazi ya Mungu na kuamua kusonga mbele hadi ndani ya jengo walimo wazazi wake pamoja na mzee Mwinyimkuu.
Kwa risasi ameua watu wengi na kuwafikia wazazi wake lakini wakati anawafungua kamba, mwanaume asiyempenda na aliyesababisha matatizo yote yanayompata katika maisha yake, Tonny! Anatokea akiwa na bastola mkononi na kumweka chini ya ulinzi akitaka kumuua, muda mfupi baadaye anasikia mlio wa risasi na anaamini risasi hiyo imemwingia yeye.
Je, nini kimetokea? Fuatilia........

Hali ndani ya ghala la mzee Katapila iliwashangaza maaskari walioingia, maiti nne zililala chini moja ikiwa ya mwanamke ambaye hawakumtambua kwa jina! Hawakuamini macho yao walipomwona mzee Katapila ameanguka pembeni akilia kwa maumivu makali kutokana na risasi aliyopigwa pajani, mmoja wa maaskari alimsogelea na kuanza kumhoji maswali juu ya kilichotokea.
“Vipi mzee?”
“Majambazi!”
“Yamekuvamia?”
“Kabisa! Ina maana hamkukutana nayo?”
“Hapana!”
“Kuna gari mmepishana nayo muda si mrefu ikitokea hapa! Ni gari yangu yameondoka nayo!”
“Yakoje?”
“Siyakumbuki vizuri!”
“Yako mangapi?”
“Mawili tu! Mmoja mwanamke na mwingine mwanaume!”
“Pole sana kwa yaliyokupata maana naona wenzako wamefariki dunia! Inabidi tukupeleke hospitali!”
“Sina jinsi ili naomba kama mtawakamata hao majambazi waueni kabisa, askari atakayewapiga risasi nitampa milioni tano!” Aliongea mzee Katapila.
Alikuwa amedanganya kila kitu alichokisema lengo lake likiwa ni kuuficha ukweli na alitaka Nancy na Danny wauawe kabisa ili kuficha siri ya ukweli uliokuwepo, aliamini kama ingegundulika bado alijishughulisha na shughuli za ujambazi sifa yote aliyojipatia katika jamii ingepotea na angeingia matatizoni na pengine kupelekwa jela jambo ambalo hakutaka kabisa litokee.
“Unafikiri wameelekea wapi?”
“Wamedai wanakwenda Tindiga shambani kwangu kwenda kufanya ujambazi mwingine!” Alizidi kudanganya mzee Katapila lengo lake likiwa ni kuwafikishia maaskari ujumbe wa mahali Nancy na Danny walikokuwa wameelekea, hakuna alichokitamani kama kifo chao.
Maiti zote ikiwemo ya Agness zilisombwa na kupakiwa kwenye gari kisha mzee Katapila akafuatia na gari la polisi likaondoka kuelekea Muhimbili njiani kabla ya kufika hospitali maaskari waliwasiliana na wenzao waliolifuatilia gari lililowabeba Nancy na Danny walioamini lilikuwa la majambazi kwa taarifa walizopewa na mzee Katapila.
“Tumekuta limetelekezwa Kimara lakini tukapewa taarifa na wasamaria wema kwamba waliliacha na kukodisha teksi wakasonga mbele kuelekea Barabara ya Morogoro kama wanakwenda Tindiga basi tutawapata, afande Alphonce anasema anafahamu mahali shamba la mzee Katapila lilipo, msiwe na wasiwasi watatiwa mbaroni tu!”
“Tunawatakia kazi njema ila hali haikuwa nzuri ndani ya ghala la mzee Katapila, watu wanne wameuawa na mzee mwenyewe amepigwa risasi kwenye paja lakini hali yake sio mbaya sana!”
“Mnao wale walinzi wa Omega?”
“Ndiyo!”
“Mkihitaji msaada zaidi mnaweza kuwasiliana na kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Morogoro!”
“Sidhani kama tunahitaji msaada ila tafadhali pigeni simu Morogoro muwape taarifa juu yetu!”
Waliagana na maaskari ndani ya gari la polisi lililokuwa safarini kuelekea Morogoro liliongeza kasi nyuma yake likiwepo gari la Kampuni ya Omega Security lililojaza walinzi wenye silaha wakiongozwa na kamanda Yesaya, kijana mwenye mwili mdogo lakini mbinu nyingi za kijeshi. Dereva aliuelewa urefu wa safari iliyokuwa mbele yao.
Nusu saa baadaye walikuwa wakivuka kijiji cha Mgeta, gari lao likitembea kwa kasi ya kilometa mia moja na sitini kwa saa lakini bado walikuwa hawajafanikiwa kulipata wala kuliona mbele yao gari walilokuwa wakilifukuza, walishindwa kuelewa gari hilo liliendeshwa kwa kasi gani! Mpaka wanafika Dumila na kukata kona kuelekea Kilosa bado gari lilikuwa halijaonekana.
“Mh!”mmoja wa maaskari aliguna
“Vipi mbona umeguna?”
“Isijekuwa hawa watu wamenyoosha kuingia Morogoro mjini!”
“Haiwezekani! Nyie twendeni hukohuko Tindiga, kama watakuwa hawajafika tutawasubiri!”
Walikubaliana na kuendelea na safari yao, saa moja na nusu baadaye waliingia Kilosa ikiwa ni katikati ya usiku na kuendelea na safari yao hadi Tindiga shambani kwa mzee Katapila ambako waliegesha gari lao mbele ya lango la kuingilia, walinzi wawili walikuwepo na silaha zao mikononi.
“Habari zenu?”
“Nzuri tu habari yako bwana?” Maaskari walijibu.
“Safi tu! Niwasaidie nini?”
“Sisi ni maofisa wa Polisi!”
“Ndio!”
“Kuna majambazi wamemvamia mzee Katapila huko mjini na kuua vijana wake wanne na wakakimbilia huku, hebu tueleze kuna hali gani hapa? Au umeona jambo lolote lisililo la kawaida?”
“Hapana ila..!”
“Ila nini?”
“Kuna kipindi niliona taa za gari zikija lakini gari hilo halikufika hapa, likageuzia pale chini! Nilishindwa kuelewa ni kwanini nikahisi labda kuna watu wamesahau kitu chao mjini Kilosa!”Alieleza kwa kirefu mmoja wa walinzi hao, ni kweli aliliona gari lililowaleta Nancy na Danny lakini hakuwa na habari kama walipita kwenye nyasi na kuzunguka upande wa pili ambako walipanda ukuta na kuingia ndani kuendeleza mauaji.
“Tunaomba tuingie ndani kukagua!”
“Leteni kwanza vitambulisho vyenu, tutaaminije kuwa nyie ni maaskari!”
Maaskari pamoja na walinzi wa Omega Security Guards waliingiza mikono yao mfukoni, kutoa na kisha kuonyesha vitambulisho vyao, walinzi wote wakaamini lakini wakati bado hawajawaruhusu kuingia mlio wa bunduki aina ya SMG ulisikika ndani ya ngome, wote wakashtuka na kwa pamoja wakaanza kukimbia kuingia ndani silaha zao zikiwa tayari, walinzi wa ngome walishindwa kuelewa ni saa ngapi majambazi yaliingia ndani na kwa kupitia mlango gani.
Mlangoni mwa jengo pekee lililokuwemo ndani ya ngome walikuta maiti mbili, hawakutaka kuchelewa mara moja walisukuma mlango na kuingia ndani, mwanaume mmoja alikuwa amesimama wima akiwa na bastola mkononi iliyomlenga mwanamke aliyechuchuma! Bila kujiuliza mara mbili walielewa huyo alikuwa mmoja wa majambazi na askari mmoja aliachia risasi zilizompata mwanaume huyo moja kwa moja begani akadondosha bastola yake.
*****
Alisikia mlio wa risasi, badala ya kuwa imempenya yeye hakuamini kuona Tonny anaanguka chini! Alishindwa kuelewa ni nani aliyefanya kitendo hicho, fikra zake zilimpeleka kwa Danny lakini alilifuta wazo hilo mara moja alipoifikiria hali aliyomwacha nayo wakati anaondoka, hakuwa mtu wa kunyanyuka na kukamata bunduki.
Mara ghafla aliwaona wanaume wengi wakifika eneo hilo na bunduki zao mkononi, wakikimbia huku na kule kuangalia kama kulikuwa na mtu mwingine! Mmoja wao alimfuata akajitambulisha na kuanza kumhoji juu ya kilichotokea, Nancy alilia machozi ya furaha alipogundua walikuwa ni maaskari.
“Wazazi wangu pamoja na mchumba wangu, walitekwa na mzee Katapila akishirikiana na huyu mliyempiga risasi, anaitwa Tonny! Nilitoa taarifa polisi Bagamoyo lakini sikusaidiwa ndipo nikaamua mimi mwenyewe na mchumba wangu ambaye nilimwokoa huko Dar es Salaam kwenye ghala la mzee Katapi...! Lakini jamani kwanini tuzidishe maongezi, mimi naomba tuwachukue kwanza hawa wazee wangu tuwapeleke hospitali, mambo mengine tutaongea baadaye ni vyema tukaokoa maisha kwanza!” Alisema Nancy baada ya kusita.
Maaskari hawakuwa na ubishi, wote walisaidiana kubeba na kupakia maiti zote zilizokuwemo ndani ya jengo hilo na hata zilizokuwa mlangoni kisha kuwabeba wazazi wa Nancy waliokuwa hoi bin taaban kwenda kwenye gari na mara moja kuondoka kuelekea hospitali ya wilaya ya Kilosa iliyokuwa kama kilometa hamsini kutoka eneo hilo, lilikuwa tukio la kusikitisha lililowakosesha raha hata maaskari, walitaka sana kumhoji Nancy maswali juu ya kilichotokea lakini hakuwa tayari kuongea akidai angeeleza kila kitu baada ya kufika hospitali na wazazi wake kutibiwa. Muda wote alikuwa akilia.
******
Danny alizinduka ghafla baada ya fahamu zake kumrejea, alijaribu kusimama wima akashindwa, mwili wake haukuwa na nguvu kabisa! Alikuwa kama mtu aliyefumbua macho kutoka usingizini, kumbukumbu zake hazikuwa sawa! Alijaribu kuzivuta na kuzisogeza karibu ili alewe mahali alipokuwa ni wapi na alikuwa akifanya nini lakini hakufanikiwa kutuliza ubongo wake, mpaka dakika mbili baadaye alipomfikiria Nancy! Kila kitu kilirejea kichwani mwake.
Alikumbuka alivyopigwa mshale na kuanguka chini na mara ya mwisho alipoongea na Nancy, kwa mbali maneno ya kuagwa yaliyosemwa na mpenzi wake wakati akiwa katika upotevu wa fahamu yalimwijia akaelewa Nancy alikuwa ameondoka na kumwacha eneo lile akifikiri alikuwa amekufa baada ya kuchomwa mshale, hakutaka kukubaliana na fikra hizo na kuanza kuliita jina la Nancy.
“Nancy! Nancy!Nancy!” Aliita mara kadhaa bila kuitikiwa, hapakuwa na mtu kabisa ndani ya ngome hiyo hata walinzi waliondoka na magari ya polisi na Omega security Guard kuelekea hospitali ya Kilosa.
Pamoja na maumivu makali aliyokuwa nayo, Danny hakutaka kukata tamaa akazikusanya nguvu zake zote zilizobaki mwilini na kusimama wima akiyumbayumba na baadaye kuanguka chini, alihisi mshale aliochomwa ulikuwa na sumu sababu ya kizunguzungu alichokuwa nacho.
“Kusimama siwezi acha nitambae kuelekea mbele!” Alijisemea moyoni mwake na kunyanyuka tena, safari hii kama alivyowaza hakutaka kusimama alianza kutambaa kuelekea kweney jengo lililokuwa mbele yake! Moyoni mwake alijawa huzuni akiamini kwa vyovyote hata Nancy alishauawa mawazo hayo ndiyo yalimtia ujasiri zaidi, hakuogopa kulisogelea jengo hilo ili kama ni kuuawa basi wammalizie kabisa kuliko kuendelea na mateso aliyokuwa nayo.
Mbele ya jengo hapakuwa na mtu zaidi ya damu zilizotapakaa kila mahali na Danny hakutaka kuingia ndani, alichofanya ni kunyoosha moja kwa moja kuelekea langoni ambako pia hapakuwa na mtu akatoka hadi nje ya ngome na kwenda kulala katikati ya barabara akitarajia gari lolote ambalo lingepita maeneo hayo lazima lingesimama na kumchukua kumpeleka hospitali. Tayari mwanga wa alfajiri ulishaanza kuonekana.
Ghafla giza nene liliyatanda macho pake, moyo wake ukaanza kunywea taratibu, mapafu yakabana pumzi ikawa haiingii kifuani kama ilivyo kawaida huku mwili wake ukilegea, hakuelewa kitu chochote kilichoendelea baada ya hapo.
*********
Safari kuelekea Kilosa ilikuwa bado ikiendelea, Nancy naye alikuwa bado akibubujikwa na machozi akiwa katikati ya wazazi wake pamoja na mzee Mwinyimkuu waliokuwa hoi bin taaban! Hakuwa na uhakika kama baba yake alikuwa hai, muda wote alimwomba Mungu afanye muujiza.
“Ulisema kwamba ulikuja huku na mchumba wako?” Lilikuwa ni swali kutoka kwa mmoja wa maaskari lililorejesha kumbukumbu sawasawa katika kichwa cha Nancy, akanyanyuka na kusimama wima mikono yake yote miwili ikiwa kichwani kwake.
“Vipi?” Mmoja wa maaskari aliuliza baada ya kuugundua mshtuko aliouonyesha.
“Simamisha gari!” Aliamuru.
“Kwanini?”
“Tumemsahau!”
“Nani?”
“Mchumba wangu!”
“Alikuwa sehemu gani?”
“Nyuma ya jengo akiwa amechomwa mshale!”
“Mama yanguuu! Sasa kwanini hukusema?”
“Nilichanganyikiwa nikasahau! Tafadhali dereva simamisha gari!”
Dereva akakanyaga breki na baadaye kusimama, baadhi ya maaskari walihisi anawachanganya akili zao na kuwapa usumbufu, minongíono ya chinichini ilisikika wakati gari linasimama.
“Sasa tufanye kipi? Tuwapeleke wazazi wako hospitali au turudi kwa mchumba wako? Mbona unataka kutuchanganya? Kwanza mambo yenyewe hayajaeleweka, hebu chagua kitu kimoja tafadhali! Baba na mama au mchumba wako?”Meja Alphonce aliuliza na Nancy kukaa kimya, wote walikuwa na umuhimu mkubwa maishani mwake.

Je nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 33
Nancy amefanikiwa kuwaokoa wazazi wake pamoja na mzee Mwinyimkuu, waliotekwa na kufichwa shambani kwa mzee Katapila huko Tindiga Kilosa, yote haya yalifanywa na Tonny kama kisasi baada ya kumkataa, kwa juhudi zake Nancy amefanikiwa kuingia ndani ya ngome ya shamba hilo akiwa na Danny, mwanaume ampendaye ambaye kwa bahati mbaya amechomwa mshale na kuanguka chini, kupoteza fahamu jambo lililomfanya Nancy akate tamaa kwamba asingepona!Akiwa ndani ya jengo Nancy anawekwa chini ya ulinzi na Tonny aliyemlenga na bastola yake kwa lengo la kumuua lakini kabla hajafyatua risasi, Tonny anaanguka chini! Amepigwa risasi na maaskari waliokuwa wakiwafutilia Danny na Nancy kutokea Dar Es Salaam!
Nancy anakataa mahojiano yoyote na polisi kwanza anataka wazazi wake pamoja na mzee Mwinyimkuu ambao hali zao ni mbaya kutokana na mateso waliyoyapata wapelekwe hospitali, amesahau kabisa kuwa Danny yupo nyuma tu ya jengo hilo! Maiti ikiwemo ya Tonny zinabebwa na kupakiwa ndani ya gari na wazazi wa Nancy pamoja na mzee Mwinyimkuu wanapakiwa ndani ya gari jingine na safari ya kuelekea Kilosa hospitali inaanza.
Ghafla wakiwa njiani Nancy anajiwa na kumbukumbu za Danny, anagundua amemsahau mpenzi wake! Hapohapo anamwamuru dereva asimame na anafanya hivyo, Nancy anawasimulia kilichotokea baadhi ya maaskari wanaona anachowaeleza ni usumbufu na wanamwambia achague kimoja wazazi au mpenzi wake? Anachanganyikiwa na anashindwa achague lipi kwani wote ni wa muhimu kwake.
Je, nini kinaendelea? Fuatilia.......

“Chagua!” Askari alisema.
“Siwezi kuchagua!”
“Kwanini?”
“Wote ni wa muhimu kwangu!”
“Mshika mbili?”
“Moja humponyoka!” Badala ya Nancy kujibu askari mwingine alidakia.
Nancy alijitahidi kuwabembeleza kwa uwezo wake wote ili wakubali yeye ashuke kwenye gari lililowabeba wazazi wake, apande gari lililobeba maiti ambazo hazikuwa na sababu yoyote ya kuwahishwa hospitali kwa wakati huo ili wazazi wake wapelekwe hospitali haraka na warudi hadi shambani kwa mzee Katapila kumtafuta Danny! Aliwahikikishia kuwa mtu huyo alikuwa wa muhimu kiasi gani kwake, kiasi kwamba asingeweza kumwacha afie porini, wakati msaada ulishapatikana.
“Una uhakika atakuwa hai?”
“Sina uhakika lakini anaweza kuwa hajafa ingawa hali yake ilikuwa mbaya sana!”
“Kwa hiyo turudi?”
“Nitafurahi sana mkichukua uamuzi huo!”
“Ok! Basi nyinyi tangulieni, sisi tutarudi na huyu binti hadi shambani!” Kamanda Yesaya wa kampuni ya Omega alisema na wakakubaliana, gari likageuzwa na kuanza tena kurudi shambani kwa mzee Katapila, Tindiga. nusu saa baadaye walishafika na kuegesha gari, kabla ya kufika langoni walipishana na simba wawili! Mmoja jike na mwingine dume, walitishika kwani hawakutegemea kama wanyama kutoka Mikumi waliweza kufika maeneo hayo! Nancy akawa wa kwanza kurudi akifuatiwa na walinzi wengine wa Omega na kuanza kukimbia kwenda ndani hadi nyuma ya jengo, Nancy aliangua kilio alipokuta mwili wa Danny haupo mahali alipouacha! Alishindwa kuelewa alikuwa amekwenda wapi, alipita huku na kule kuzunguka maeneo hayo bila mafanikio ya kumwona.
“Una uhakika alikuwa hapa?”
“Kweli kabisa!”
“Nilimwacha hapahapa akiwa na mshale mgongoni!”
“Sasa atakuwa amekwenda wapi?”
“Kwa kweli hata mimi sifahamu!” Alijibu Nancy akilia, baada ya hapo wote walianza kuzunguka huku na kule shambani wakimtafuta bila mafanikio mwisho wakakata tamaa kabisa, muda wote huo Nancy alikuwa akilia mfululizo! Pamoja na kazi yote kubwa aliyoifanya kumwokoa Danny na baadaye wazazi wake alikuwa amempoteza mchumba wake! Walinzi wa Omega walimfariji kadri walivyoweza lakini hawakuweza kumzuia asiendelee kulia, saa nzima baadaye waliondoka shambani na kusafiri kwa kasi hadi hospitali ya wilaya ya Kilosa ambako waliwakuta wazazi wa Nancy pamoja na mzee Mwinyimkuu wakiwa wamelazwa chumba cha wagonjwa mahututi, Nancy aliomba kumwona daktari ili ajue nini kilichoendelea.
“Hali zao ni mbaya lakini watapona!”
“Kweli daktari?”
“Kabisa, matumaini yapo, tatizo lao kubwa lilikuwa ni njaa! Kwa muda mrefu sana hawakupata chakula cha kutosha, ndio maana tumewatundikia dripu za glucose ili kuongeza sukari kwenye miili yao, siku mbili kuanzia sasa watakuwa na uwezo wa kuongea vizuri!”
“Ahsante daktari! Lakini bado kuna tatizo moja linanitatiza!”
“Tatizo gani binti?” Aliuliza Dk. Muhombolage, aliyekuwa akiwashughulikia wazazi wa Nancy.
“Mchumba wangu!”
“Amekuwaje?”
“Tulikuwa naye pamoja wakati tunawafuatilia wazazi wangu, akachomwa mshale na kuanguka, nikamwacha sehemu aliyokuwa ameangukia na kuingia ndani ya jengo ambako niliwaokoa wazazi wangu, bahati mbaya sana nikamsahau wakati wa kuondoka kuja hapa hospitali! Nikarudia njiani kumfuata lakini sikumkuta, sasa sielewi ni wapi alipokwenda! Lazima kutakuwa na mtu amemchukua au kaliwa na Simba tuliokutana nao njiani! Maana kama angekufa tungeikuta maiti yake eneo lilelile!” Alieleza Nancy kwa kirefu daktari akimsikiliza, hakuwa na jambo la kumshauri zaidi ya kuulizia hospitali za jirani za eneo walilokuwa, alipiga simu hospitali ya Kilombero na kuulizia kama kulikuwa na mgonjwa wa aina hiyo aliyekuwa amepokelewa, jibu likawa hapana.
“Labda mtoe taarifa polisi!”
“Ninaoshughulika nao hapa ni polisi, wamekwishafanya hivyo mapema!”
“Basi atapatikana!”
“Haiwezekani daktari atakuwa amekufa!” Alijibu Nancy na kuondoka ofisini kwa daktari kurudi chumba cha wagonjwa mahututi ambako wazazi wake walilazwa, alikaa huko mpaka saa tatu na nusu ya asubuhi polisi walipokuja kutaka kuchukua maelezo yake kwa sababu taarifa walizokuwa wamezipokea kutoka mkoani Morogoro kwa Kamanda wa Polisi ni kwamba yeye Nancy pamoja na Danny ndio walikuwa majambazi waliokuwa wakisakwa baada ya kuvamia ghala la mzee Katapila lililopo Vingunguti jijini Dar Es Salaam, kuua watu, kumjeruhi mzee Katapila na kuondoka na kiasi kikubwa cha fedha!
Hivyo ndivyo mzee Katapila alivyowaeleza polisi na kwa sababu ya uwezo wake kifedha na heshima aliyokuwa nayo katika jamii kipindi hicho, aliaminika na Nancy pamoja na Danny kuonekana watu hatari, hapohapo hospitali Nancy alipigwa pingu mikononi na kubebwa mpaka kituo cha polisi cha Wilaya ya Kilosa, hakutakiwa kujibu chochote mara moja alipakiwa ndani ya gari jingine na kusafirishwa kwenda Dar Es Salaam alikotakiwa kujibu kesi ya mauaji. Alijaribu kuongea kadri alivyoweza kuonyesha hakuwa na hatia lakini hakuna mtu aliyemjali, hivyo ndivyo ilivyoeleweka, Nancy alikuwa muuaji.
Jijini alitupwa moja kwa moja mahabusu kituo kikuu cha polisi, alipotolewa baadaye ulikuwa ni wakati wa kutoa maelezo yake juu ya kilichotokea, jopo la maaskari wa ngazi za juu walikuwepo kusikiliza maelezo ya msichana huyo yakichukuliwa! Nancy huku akilia alianza kusimulia kila kitu kilichotokea maishani mwake tangu mwanzo wakiwa Bagamoyo na wazazi wake, walivyompokea Tonny nyumbani kwao, kuishi naye, kumsomesha mpaka nchini China wakitegemea angekuja kuwa mume mwema wa binti yao lakini ghafla akaja kubadilika, akawa nyoka na kumtelekeza Nancy kwa ajili ya msichana mwingine ambaye naye alikwenda kumfanyia unyama wa aina hiyohiyo ndipo akarudi nchini Tanzania na kutaka kumuoa tena Nancy ambaye kwa wakati huo tayari alikuwa na mchumba mwingine. Hakuyasahau mambo ya Bagamoyo kula yamini kwa mganga wa kienyeji ambayo baadaye ilikuja kumfanya awe mwendawazimu.
“Kuna mzee mmoja ambaye yuko Kilosa hospitali pamoja na wazazi wangu, anaitwa mzee Mwinyimkuu huyo ndiye mganga mwenyewe aliyenilisha yamini na baadaye akapatikana na kuiondoa ndio maana akili yangu ikarejea tena kawaida! Tonny akawa ameng’ang’ania kunioa lakini kwa mabaya aliyonifanyia nilikataa na kutaka kuolewa na Danny, hilo lilimkera ndio maana akamkodisha mzee Katapila ili awateke wazazi wangu! Lakini kuna kitu kingine hapohapo, Danny alipoamua kunioa mimi alimwacha msichana aitwaye Agness, huyo naye kwa hasira zake akamfuata mzee Katapila huyohuyo na kumkodi ili amteke Danny! Hilo likafanyika, akatekwa na kufichwa Vingunguti lakini mimi niliapa ni lazima nimkombe Danny, niwakomboe wazazi wangu na mzee Mwinyimkuu na baadaye wadogo zangu ambao walichukuliwa na wazee wawili waishio Kisiwani katikati ya ziwa Tanganyika!” Aliongea Nancy kwa karibu masaa mawili akisimulia kila kitu kuonyesha ni kiasi gani hakuwa na hatia na mtu mbaya alikuwa mzee Katapila.
“Kweli?”
“Sina sababu ya kudanganya! Huo ndio ukweli ila kama mtaamua kunigandamiza mimi sababu ya umasikini wangu, sawa! Sitakuwa na la kufanya ila niliyoyasema ndio ukweli!”
“Hivi sasa mzee Katapila yuko wapi?” Kamanda wa polisi wa mkoa alimuuliza Mkuu wa Upelelezi.
“Bado yuko Muhimbili!”
“Afungwe pingu hapohapo kitandani!”
“Sawa Afande!”
“Huyu msichana hana hatia! Tena ni miongoni mwa wasichana shujaa kuliko ambao nimewahi kukutana nao, amefanya kazi ya kipolisi wakati sisi tuko hapahapa!” Kamanda alifoka.
“Mheshimiwa Kamanda naomba nikueleze ukweli juu ya jambo hili, siku nyingi niliwahi kutoa taarifa kituo cha polisi Bagamoyo lakini hakuna aliyejali, nilionekana muongo! Maaskari wengi wanamuogopa sana mzee Katapila, hilo ndilo linamfanya awe mtu mbaya anayeonea watu kila siku na hachukuliwi hatua yoyote!”
“Suala hili nitaliingilia mwenyewe binti mpaka haki itendeke! Kwa hivi sasa tunakuacha huru, ukimaliza kutoa maelezo yako unaweza kuondoka lakini uripoti hapa siku ya Jumatatu, au mnaonaje?”
“Sawa Mkuu!” Wengi wote waliitikia.
Baada ya maelezo Nancy hakuwa na jambo jingine la kufanya kituoni, alimshukuru Mungu na kutoka nje ambako alikutana na waandishi wa habari wengi wakimsubiri na kuanza kumpiga picha huku wakimuuliza maswali mengi juu ya kilichotokea, aliwasimulia ingawa kwa kifupi na baadaye kuondoka mbio hadi stendi ya daladala ambako alipanda basi lililompeleka hadi kituo cha Mabasi cha Ubungo ambako alipanda basi la Shabiby lililomsafirisha hadi Morogoro ambako alipanda basi jingine lililomfikisha Kilosa, hiyo ikiwa ni siku ya Jumamosi saa kumi na mbili jioni.
Hali ya wazazi wake wodini ilikuwa nzuri, aliweza hata kuongea nao! Wote walimshukuru kwa ujasiri aliouonyesha hata mzee Mwinyimkuu lakini hawakuacha kuuliza wapi alikokuwa Danny, Nancy alilia wakati akiwaeleza alivyochomwa mshale maiti yake kupotea! Mpaka wakati huo aliamini Danny alikuwa marehemu, wazazi wake wote wakiwa kitandani walimwaga machozi hata mzee Mwinyimkuu hakuweza kujizuia, baadaye walikubaliana na ukweli huo na kuyaacha yote mikononi mwa Mungu.
“Yaani kweli Danny amefariki pamoja na wema wote aliokuwa nao? Haiwezekani!” Mama yake Nancy aliongea akiwa kitandani.
“Nina wasiwasi alilia na Simba!” Alisema Nancy.
“Kwanini unawaza hivyo?”
“Tulikutana na Simba wawili kabla hatujafika shambani!”

Je nini kitaedelea?
 
SEHEMU YA 34
Wazazi wa Nancy pamoja na mzee Mwinyimkuu wamepelekwa hospitali ya wilaya ya Kilosa kwa matibabu baada ya kuokolewa kutoka mikononi mwa wauaji! Hizi ni juhudi za mtoto wao Nancy aliyeapa kupoteza maishani ili kuwaokoa wazazi wake.
Lakini anafanya kosa moja kubwa la kumsahau shambani kwa mzee Katapila mchumba wake Danny aliyechomwa mshale mbavuni, analikumbuka kosa hili wakiwa njiani na kuwataarifu polisi, anawaomba wamrudie na wanakubali lakini walipofika mahali alipomwacha walikuta mwili wa Danny haupo, hisia zao zinawafanya waamini kijana huyo ameliwa na Simba kwa sababu walikutana na Simba wawili njiani.
Ni jambo hili ndilo Nancy anawasimulia wazazi wake baada ya kurudi hospitali kutoka shambani akiwa na uhakika Danny hakuwa hai! Je aliliwa na Simba kweli?

Sasa endelea......

“Kwa hiyo inawezeka aliliwa na Simba?” Mama yake Nancy aliuliza.
“Huo ndio wasiwasi wangu kwa sababu hatujamkuta mahali nilipomwacha akiwa amechomwa mshale!”
Kila mtu alisikitika, wazazi wa Nancy walilia machozi kila walipokifikiria kifo cha Danny, hakuna aliyekuwa tayari kuamini kwamba Danny alikuwa marehemu pamoja na wema wote alioufanya! Lawama zote walimtupia mzee Katapila baada ya Nancy kuwasimulia namna mzee huyo alivyoshiriki katika mikakati ya utekaji!
Hakuna alichostahili mzee huyo zaidi ya kifungo cha maisha gerezani au kunyongwa kabisa kwani alisababisha vifo vya watu wengi. Agness na Tonny walikuwa marehemu, mtu pekee aliyekuwa amebaki hai alikuwa mzee Katapila aliyekuwa hospitali akiendelea kutibiwa jeraha la risasi alilokuwa nalo lakini akiwa amefungwa pingu kitandani kwake..
Kitu kingine kilichowasikitisha zaidi wazazi wa Nancy ni watoto Catherine na David, kitendo cha kuambiwa walitekwa na mzee Kiwembe pamo ja na babu Ayoub na kurudishwa kisiwani kiliwachanganya na walishindwa kuelewa nini kingefanyika kuwakomboa watoto hao, Nancy aliwaondoa wasiwasi na kuwaeleza kazi hiyo ingekuwa yake mpaka kuhakikisha watoto wote wanarudi katika himaya ya wazazi wake.
“Utaweza?”
“Nitaweza baba!”
“Angekuwepo Danny mngeweza kusaidiana!”
“Msiwe na shaka na ninafikiri nitapata msaada wa polisi kwa sababu wamekwishaelewa tatizo liko wapi!”
“Itakuwa ni vyema kama nao watakombolewa!”
Mzee Mwinyimkuu alikuwa mtu kwanza kuruhusiwa kutoka hospitali, hakutaka hata kuishi siku mbili mjini Kilosa, alichofanya ni kuaga na kuondoka hadi Morogoro ambako alipanda mabasi yaliyomrejesha hadi Dar Es Salaam, kwa pesa kidogo alizopewa na Nancy aliweza kusafiri hadi Kigoma ambako aliendelea na safari yake kupitia ziwa Tanganyika hadi Kongo. Aliapa kutoyasahau yaliyompata Tanzania, wiki moja baadaye baba na mama yake Nancy walikuwa na hali nzuri pia wakaruhusiwa na kurejea Dar Es Salaam na baadaye Bagamoyo, wakawa wamerejea katika maisha yao ya kawaida.
Watu waliowafahamu, majirani na marafiki wilayani Bagamoyo walipopata habari ya kurudi kwao walifurahi kupita kiasi, ilikuwa ni sherehe kubwa lakini walisikitika walipoambiwa Danny alifariki dunia! Taarifa hizo baadaye mzee Katobe alipopata nafuu alirejea tena Dar Es Salaam wizara ya Mambo ya nchi za nje na kutoa taarifa ili wazazi wa Danny waliokuwa nje ya nchi kwenye ubalozi wajulishwe juu ya kifo cha mtoto wao, hata wafanyakazi wa wizara hiyo waliomfahamu Danny walilia machozi ya uchungu, si hao tu bali pia wanafunzi wa chuo kikuu cha Dar Es Salaam waliosoma naye darasa moja kabla hajakatisha masomo kwa ajili ya Nancy walisikitika na kuiomba serikali imchukulie mzee Katapila hatua kali kwa kitendo cha unyama alichokifanya.
Siku tatu baada ya mzee Katobe kutoa taarifa wizara ya Mambo ya nchi za nje, baba na mama yake Danny waliwasili nchini wakiwa na huzuni kubwa, Danny alikuwa mtoto wao wa pekee! Hivyo kifo chake kilimaanisha wasingekuwa na mtoto mwingine tena, ulikuwa msiba mkubwa sana kwao! Cha kushangaza hawakua na hamaki yoyote kwa mzee Katobe na familia yake, walichofanya wao ni kurudi tena shambani kwa mzee Katapila na kuendelea kuitafuta maiti ya mtoto wao, kwa wiki mbili walifanya kazi hiyo bila mafanikio hatimaye wakakata tamaa kabisa! Hapakuwa na mazishi ya Danny, lakini kila mtu aliamini mtoto huyo hakuwa hai.
“Kwa kweli tumeumia lakini hatuna la kufanya, ulikuwa mpango wa Mungu!”
“Poleni sana hata sisi pia tuna masikitiko makubwa sana! Matatizo yote yaliyotupata sisi tunayaona ni madogo sana kuliko kumpoteza Danny!”
“Hakuna shida! Lililopangwa na Mungu mwanadamu hawezi kulikwepa!” Mama yake Danny alisema.
Wote waliamini walikuwa wameumia lakini kama maumivu yao yangepimwa kwenye mzani, kuna mtu mmoja angewazidi wote! Kifo cha Danny kilikuwa pigo kubwa maishani mwake, hakika asingeweza kukutana na mtu mwingine kama yeye mpaka kaburini kwake! Huyo hakuwa mwingine bali Nancy, kwake kila siku kilikuwa ni kilio na majonzi pamoja na kufanikiwa kuwaokoa wazazi wake, haikutosha! Kutokuwepo kwa Danny maishani mwake lilikuwa pengo lisilozibika.
Hakula chakula kwa karibu wiki nzima, alikonda na kunyongíonyea mpaka ikafikia wakati wazazi wake wakaanza kuwa na wasiwasi angekufa kwa njaa na kulazimika kumpeleka hospitali ambako alitundikiwa dripu ya sukari zilizomtia nguvu mwilini mwake, kilichofuata baada ya hapo ni ushauri Nasaha uliomwimarisha na kumfanya aukubali ukweli wa yote yaliyotokea! Nancy akasimama imara tena na mipango ya kwenda kisiwani Galu kuwaokoa wadogo zake ikaanza kuzunguka ubongoni mwake na alitaka kuondoka wakati wowote lakini polisi walimzuia mpaka atoe ushahidi mahakamani.
“Kwani kesi hiyo haiwezi kuendelea bila mimi kuwepo?” Alimuuliza Mkuu wa kituo cha polisi Bagamoyo wakati akijiandaa na safari yake kwenda Kigoma.
“Haiwezekani! Ushahidi wako ni wa muhimu sana!”
“Nina kazi nyingine ya kufanya!”
“Kazi gani?”
“Nahitaji kuwafuatilia wadogo zangu!”
“Wadogo zako wapi?”
“Kwenye maelezo yangu nilishasema kuwa wadogo zangu nao walitekwa!”
“Na mzee Katapila?”Mkuu wa Kituo aliuliza.
“Hapana!”
“Na nani tena?”
“Wako wazee wawili waliowahi kuniteka mimi na mama yangu!”
“Lini tena? Mbona maisha yenu yamejaa historia za kutekwa?”
Ilibidi Nancy asimulie tena kilichotokea mpaka yeye na mama yake wakajikuta wapo katika kisiwa cha Galu ambako walipata mateso yaliyomfanya alie machozi wakati akisimulia, mkuu wa kituo alibaki mdomo wazi! Hakuwa tayari kuamini kama mambo yote hayo yalimpata msichana aliyekuwa mbele ya meza yake, ilionyesha kama Tanzania haikuwa na Serikali, isingewezekana mtu afanye ukatili wa aina hiyo na asichukuliewe hatua.
“Kwa hiyo huko Kisiwani ndio unakotaka kwenda?”
“Ndiyo!”
“Huhitaji kwenda! Jeshi la polisi litaifanya kazi hiyo!”
“:Siwaamini polisi! Si unakumbuka niliwahi kuwataarifu juu ya kutekwa kwa Danny pamoja na wazazi wangu lakini hamkutilia maanani!”
“Tuyasahau ya zamani, nitawasiliana na Kigoma na jeshi la polisi ndilo litakayokwenda hadi Kisiwani na kufanya ukombozi, hao wazee ni lazima wafikishwe mbele ya sheria, nakushauri utulie Nancy ili uwepo wakati kesi ikiendelea!”
“Kwa hiyo unanieleza kwamba niwaamini polisi?”
“Wala usiwe na shaka, utawala uliopo hapa Bagamoyo kwa sasa ni tofauti na zamani, mkuu wa kituo aliyekuwepo alihamishwa kwenda Makao makuu baada ya kufanya makosa fulani, likiwemo hilo la kutofuatilia mambo!”
“Ina maana wewe nikuamini?”
“Asilimia mia moja nitalifanyia suala lako kazi hadi wadogo zako wapatikane!”
“Acha nione!”
Akiwa bado yupo ofisini, mkuu wa kituo alinyanyua simu na kumpigia Kamanda wa Polisi mkoa wa Pwani na akimtaarifu juu ya tukio alilolisikia toka kwa Nancy, kwa kumwangalia machoni wakati akiongea, Nancy alielewa ni kiasi gani hata Kamanda wa Polisi wa Mkoa alikuwa ameshtuka, kwa maneno aliyoyasikia kutoka mdomoni kwa mkuu wa kituo, aliamini hatua za haraka zingechukuliwa! Mpaka anaondoka hicho ndicho kitu kikubwa alichokiamini, alipofika nyumbani aliwasimulia wazazi wake mambo yote yaliyojitokeza polisi nao wakamshauri jambo hilo hilo.
“David na Catherine ni watoto wetu lakini nina uhakika huko waliko, maisha yao hayako hatarini sana!Bado polisi wanaweza kuifanya kazi uliyotaka kuifanya wewe na kuikamilisha, waache waendelee! Wape mwezi mmoja kabla hujafikiria jambo jingine!” Mama yake Nancy aliongea.
Taarifa juu ya kuwepo kwa watoto waliotekwa na kufichwa katika kisiwa cha Galu kilichopo katikati ya Ziwa Tanganyika zilifika hadi makao makuu ya jeshi la polisi ambako amri ilitolewa kwa kamanda wa polisi wa mkoa wa Kigoma kuwa, kiundwe kikosi maalum kwa ajili ya ukombozi wa watoto hao! Jumla ya askari ishirini walikusanywa, wakakabidhiwa silaha na kuondoka ndani ya boti mbili ziendazo kwa kasi kuelekea kisiwani Galu, hakikuwa kisiwa kigeni kwao kwani mara kwa mara walikiona wakiwa katika doria za kusaka magendo na wavuvi haramu, lakini hata siku moja hawakuwahi kufikiri kuwa binadamu waliishi ndani ya kisiwa hicho.
Walikuwa na matumaini makubwa ya kurudi na ushindi, wakiwa na watoto pamoja na watekaji ambao wangefikishwa mbele ya sheria mara moja! Hiyo ndiyo kazi waliyokuwa wamepewa na Kamanda wa polisi wa mkoa wa Kigoma. Isingewezekana watu wawili washindane na askari ishirini wenye silaha waliokuwa tayari kuua ili mradi watoto David na Catherine wakombolewe.
“Jamani sikilizeni!” Mmoja wa maaskari alisema
“Vipi?”
“Tunakwenda kupambana na watu tusiowafahamu!”
“Kwa hiyo?”
“Mimi hawa wazee wa Kiha huwa siwaamini, wanaweza kuwa na ndumba halafu tusifanikiwe kufanya lolote!”
“Wewe acha bwana, umeshaanza imani za kishirikina, wewe twende kazini, acha kutuvunja moyo!”
Yalikuwa maongezi ndani ya boti moja ya polisi wakizidi kusonga mbele, kisiwa cha Galu kilishaanza kuonekana mbele yao! Walikuwa na uhakika katika muda wa dakika thelathini wangekuwa wanagoa kwenye ufukwe wa kisiwa hicho, kila mmoja wao aliweka bunduki yake tayari kwa kazi iliyokuwa mbele. ilikuwa ni lazima warejee na watoto hata kama watekaji wangeuawa, hilo ndilo lilikuwa lengo lao na walijua ingekuwa ni kazi ndogo sana kwao.
Ghafla wakiwa wamebakiza kama mita mia mbili hivi ili wagoe kisiwani, kitu kama kimbunga cha ajabu kiliibuka kutokea nyuma yao kikiyazungusha maji kwa nguvu isiyo ya kawaida! Pamoja na kusafiri siku zote katika ziwa Tanganyika, kila mmoja wao alikiri kimbunga hicho hakikuwa cha kawaida, bila kutegemea hofu ya kifo ilitanda! Hakikuwazungusha watu waliokuwa kwenye boti moja tu, bali ilikuwa hekaheka hata kwa boti ya pili! Walipiga kelele wakiitana na kuombana msaada lakini hapakuwa na mtu wa kumsaidia mwenzake, hali ilikuwa mbaya na muda mfupi baadaye boti zote mbili zilibinuliwa na kuwamwaga maaskari majini! Walishindiwa kuelewa ni kitu gani kilikuwa kimetokea kwani hata maji waliyodumbukia ndani yake yalikuwa na joto kali kama yaliyokuwa yakichemshwa jikoni, wote walilia kwa jinsi walivyoungua.
“Naungua!Naungua!Naungua!” Maaskari walisikika wakilia.
********
Kesi ya mzee Katapila ilivuta usikivu wa watu wengi jijini Dar Es Salaam, mahakama ilifurika kila ilipotajwa! Watu walichukizwa na kitendo alichokifanya, ingawa ujambazi ilikuwa ni sifa yake kwa muda mrefu lakini walishtuka, haikuwa rahisi mtu aliyesaidia jamii kama yeye kuwa bado aliendelea na tabia ya kikatili namna hiyo! Vyombo vya habari viliripoti maendeleo yote ya kesi, kwa sababu hiyo hapakuwa na njia yoyote ambayo mzee Katapila angeitumia kucheza na mfumo wa sheria, hakuna Hakimu aliyekuwa tayari kupokea rushwa ili kupindisha sheria kwani viongozi wote wa serikali waliifuatilia kesi hiyo kwa macho na masikio yao yote.
Hakuwa na namna ya kujitetea, ushahidi ulikuwa umembana kila upande! Hakuwa yeye peke yake katika keshi hiyo bali pia baba yake mdogo Agness mzee Shao, aliyekwenda kwake na kumlipa fedha ili afanye utekaji! Wote walikuwa na kesi ya kujibu na pamoja na kuwa na mawakili wazuri bado haikusaidia, walijikuta wakihukumiwa kwenda jela miaka thelathini kwa mzee Shao na Katapila alihukumiwa kifungo cha maisha! Badala ya kusikitika wakazi wa jiji la Dar Es Salaam waliruka juu na kushangilia.
Hata Nancy pamoja na wazazi wake pia walifurahi kupita kiasi lakini furaha hiyo haikutosha, kwani David na Catherine walikuwa bado hawajapatikana na taarifa zilizopatikana kutoka Kigoma ni kwamba maaskari waliotumwa walishindwa kukifikia kisiwa kwa sababu ya dhoruba kali iliyojitokeza kila walipokikaribia! Jumla ya askari sabini na sita walishapoteza maisha kiasi cha jeshi la polisi kuanza kukata tamaa hasa walipofikia roho zilizopotea wakilinganisha na walizokuwa wakijaribu kuziokoa. Maneno kuwa wazee waliokalia kisiwa hicho walikuwa wachawi yalitawala lakini jeshi la polisi halikuwa tayari kwenda kwa mganga wa Kienyeji ili lifanikiwe kufika kisiwani Galu, walidai hiyo haikuwemo katika PGO, yaani Police General Order, au maagizo ya namna polisi wanavyotakiwa kufanya kazi.
“Nafurahi mzee Katapila amehukumiwa kifungo cha maisha, lakini moyo wangu haujatulia mpaka David na Catherine wapatikane! Kama polisi wameshindwa basi nitakwenda mwenyewe!” Nancy aliwaambia wazazi wake.

Je nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 35 ILIPOTOKA...

Nancy amefanikiwa kuwakomboa wazazi wake ingawa ameshindwa kuokoa maisha ya Danny! Mzee Katapila anahukumiwa kifungo cha maisha gerezani na baba yake mdogo na Agness, mzee Shao amehukumiwa kifungo cha miaka thelathini jela kwa kushirikiana na mzee Katapila katika utekaji.
Kwa mtu mwingine yeyote kazi ingeonekana kuwa imekwisha lakini kwa Nancy, kazi bado! Hivi sasa anafikiria kwenda kuwakomboa wadogo zake waliotekwa kwenye kisiwa cha Galu katikati ya ziwa Tanganyika, kazi inayoonekana kulishinda jeshi la polisi sababu ya miujiza inayowapata maaskari wanaojaribu kwenda kisiwani humo, tayari maaskari sabini na sita wamekwishapotez
a maisha.
Je, Nancy atakwenda kisiwani? Endelea........

Habari za kisiwa cha Galu na maajabu yaliyokuwa yakitokea, vilivuta usikivu wa kila mtu mjini Kigoma na Tanzania nzima kwa ujumla! Idadi ya polisi waliopoteza maisha ilipofikia mia moja na ishirini ilibidi jeshi la polisi nchini liamue kusitisha operesheni hiyo, baadhi walianza kutoamini kuwa kweli kulikuwa na watoto wawili katika kisiwa hicho waliotekwa! Kulikuwa na kila dalili kuwa uchawi ulitumika, miujiza iliyotokea ilimshangaza karibu kila mtu.
“Kisiwa gani hiki kisichoingilika?” Ndilo swali walilojiuliza wakuu wa Polisi, karibu wakuu wote wa jeshi la polisi walikuwa mjini Kigoma.
“Hata sisi tunashangaa, visiwa vyote katika ziwa Tanganyika vinaingilika lakini hiki kimetushinda kabisa!”
“Au mzizi?”Mkuu wa ufuatiliaji wa majanga katika jeshi la polisi, Kamshina Aziz aliuliza
“Hivyo ndivyo inavyoaminika na mimi nalazimika kukubaliana na jambo hilo kwani ukikikaribia kisiwa cha Galu hali hubadilika ghafla, mawimbi makubwa hujitokeza na hata mkifanikiwa kufika kila atakayekanyaga ardhi ya kisiwa huanza kusikia moto unamuunguza mwili mzima!”
“Jeshi la Polisi haliwezi kujiingiza katika mambo ya kishirikina, mfano kwenda kwa waganga kuagulia ili kuelewa nini cha kufanya hata hivyo lazima tutafute mbinu ya kuingia katika kisiwa hicho na kuwakomboa watoto waliotekwa!”Mkuu wa jeshi la Polisi nchini alisema.
“Lakini Kamanda, huoni kama tumepoteza idadi kubwa ya maaskari kwa sababu ya watu wawili?”
“Hatuwezi kuacha ni lazima tuendelee ila simamisheni kwanza zoezi, turudi Dar Es Salaam tukajipange upya!”
Hayo ndiyo yalikuwa maamuzi ya jeshi la polisi nchini, jitahada zote zilizokuwa zikifanyika kwa lengo la kuwakomboa watoto David na Catherine, zilisimama! Hivyo ndivyo vyombo vya habari vilivyoripoti na Nancy pamoja na wazazi wake kuzipata habari hizo, haikumwingia Nancy akilini ni hapo ndipo alipoona kulikuwa na kazi ya ziada ya kufanya, hakuwa tayari kuwapoteza wadogo zake kama alivyompoteza Danny kwa kuliwa na Simba.
“Baba!” Alimwita baba yake.
“Naam mwanangu!”
“Haiwezekani!”
“Kwanini?”
“Siwezi kupoteza watu watatu kama nimefanikiwa kuwakomboa wewe na mama, vivyo hivyo ningependa kuwakomboa Catherine na David!”
“Ni sawa lakini...”
“Lakini nini baba?”
“Kwa jinsi tunavyosikia, kisiwa cha Galu kina mambo mengi mabaya, tusingependa kukupoteza wewe pia! Tutakuwa hatuna mtoto kabisa, maisha yetu yameharibika sana tunakuhitaji sana Nancy!”Mzee Katobe alimwambia binti yake.
“Nakuelewa baba lakini hatuwezi kuwaacha David na Catherine wakae kisiwani Galu katika mateso! Mimi nawapenda na bila shaka nyinyi pia, au sio mama?”
“Ni kweli lakini inabidi tukubaliane na ukweli uliopo!” Mama yake alijibu.
Wazazi wake wote walikuwa na huzuni na walionyesha ni kiasi gani mioyo yao ilikuwa na wasiwasi, walimpenda sana Nancy na hawakutaka kumpoteza! Walijaribu kadri ya uwezo wao wote kumshawishi Nancy abadili msimamo wake lakini haikuwezekana, aliendelea kusisitiza ni lazima aende ziwa Tanganyika hadi kisiwani Galu na kuwakomboa wadogo zake, aliamini jambo hilo liliwezekana ingawa si kwa asilimia mia moja, alielewa ilikuwa ni kazi ngumu sana kwani idadi ya maaskari walipoteza maisha ilimtisha! Lakini haikumvunja moyo na kumfanya ahofie kwenda kisiwani.
Kwa wiki nzima waliongea na Nancy lakini haikuwezekana kabisa kumbadili mwisho wakamruhusu aende, mzee Katobe alikwenda benki na kuchukua sehemu ya akiba iliyokuwa imebaki na kumkabidhi Nancy milioni mbili zimsaidie katika kazi yake! Hawakutaka kumwacha aondoke hivyo hivyo ilibidi tambiko la kijadi lifanyike, mzee Katobe na mke wake walitafuta maziwa yaliyokamuliwa katika ng’ombe asubuhi, wakayaleta nyumbani na kumwosha mtoto wao kwa maji ya mtungini wakimsugua kwa mtama uliosagwa kwenye jiwe na walipomaliza walimkalisha mlangoni wakawa wanabugia maziwa mdomoni na kumpulizia mtoto wao mwili mzima huku wakiomba baraka zimwogoze na kumlinda aendako!
Kazi ilipomalizika Nancy alifungiwa ndani ya nyumba bila kuruhusiwa kutoka na jioni ya siku hiyo ilifanyika sherehe iliyohudhuriwa na watu watatu tu, Nancy, mama na baba yake! Ilikuwa ni kama pasaka, siku ya kuagana na wazazi wake! Hakuwa na uhakika wa kurudi salama katika operesheni aliyokuwa anakwenda kuitekeleza, yeye mwenyewe aliita Operesheni kata roho! Hakuogopa wala kuwa na wasiwasi moyoni mwake, hakuona sababu ya kuendelea kuishi kama maisha yake yalishaharibika na mwanaume aliyempenda alikuwa ni marehemu! Hivyo kwa Nancy kifo kilikuwa kitu sahihi kwa wakati huo, isitoshe alielewa mwisho wa maisha ya kila mwanadamu ni kifo.
“Sasa kwanini nisife wakati najaribu kuokoa maisha ya wadogo zangu? Sina sababu ya kuishi kama Danny alishafariki dunia, watu wakuwaonea huruma ni baba na mama yangu lakini sina jinsi kwa sababu pia jukumu la kuwaokoa Catherine na David ni langu!” Aliwaza
Siku iliyofuata Nancy aliondoka Bagamoyo na kusafiri hadi Dar Es Salaam ambako alipanda treni lililomsafirisha hadi Kigoma na kufika baada ya siku tatu akiwa amechoka hoi bin taaban, ingawa Polisi walishasitisha zoezi la kuwakomboa Catherine na David bado siku iliyofuata Nancy alipoamka na kutoka katika hoteli ya Lubumbashi aliyofikia alikwenda moja kwa moja Makao makuu ya polisi ya mkoa wa Kigoma ambako aliomba kuonana na Kamanda wa Polisi wa mkoa, haikuwa kazi ngumu sana kumpata hasa alipojitambulisha kwa kutaja jina lake na uhusiano aliokuwa nao na watoto waliokuwa kisiwani! Jina lake lilishakuwa maarufu masikioni mwa polisi kutokana na kitendo cha kijasiri alichokifanya wilayani Kilosa na kuwakomboa wazazi wake.
“Unataka kumwona Kamanda?”Msichana wa mapokezi alimuuliza.
“Ndio!”
“Subiri kidogo nimuulize kama ana nafasi ya kukuona!” Alijibu msichana huyo na baadaye kupiga namba ya bosi wake, yeye pia hakuwa na kizuizi Nancy akaruhusiwa na kupandisha ngazi hadi ofisini kwa Kamanda ambako Nancy alieleza nia yake ya kujaribu kwenda Kisiwani Galu kuwakomboa ndugu zake, Kamanda wa polisi alimwangalia kwa macho ya huruma yaliyoonyesha wazi ilikuwa kazi ngumu kiasi gani kwa mtoto wa kike kama yeye kuweza kufanya kazi iliyowashinda wanaume tena askari wa Jeshi la Polisi..
“Utaweza binti?”
“Sina uhakika lakini nataka kujaribu!”
“Bahati nzuri nimepokea ujumbe wa polisi kutoka Dar Es Salaam kuwa kuna kikosi maalumu kinatumwa kwa ndege leo na kitafika hapa mchana, labda ungewasubiri askari wetu uongozane nao!”
“Nipo tayari kufanya hivyo!”
“Basi hakuna tatizo!” Kamanda alijibu na kumruhusu Nancy aondoke, kabla hajatoka alikumbuka kitu akageuka na kumwangalia Kamanda.
“Vipi?”
“Nitajuaje kama wamefika?”
“Aha! Nakushauri uje hapa saa sita mchana!”
“Ahsante!”
Habari aliyopewa na Kamanda ilimpa matumaini zaidi na kumtia nguvu zaidi ya alizokuwa nazo, alirudi hotelini ambako alijifungia chumbani kwake na kuendelea kuvuta fikra juu ya kazi iliyokuwa mbele yake, alikuwa ameamua kuwakomboa wadogo zake hata kama ingegharimu maisha yake mwenyewe, alipenda kusinzia mpaka muda aliopewa ufike lakini haikuwa hivyo, alikuwa macho mpaka saa tano na nusu alipoondoka kurejea kituoni, hali aliyoikuta kituoni mchana huo ilimshangaza! Ilikuwa tofauti na asubuhi alipofika kituoni kuonana na Kamanda, kulikuwa na idadi kuwa ya maaskari waliovaa tofauti na askari wa kawaida! Walionekana wazi ni wazamiaji wa majini, bila kuuliza alielewa ndio waliokuwa wakitegemewa kutoka Dar Es Salaam, alichofanya ni kupandisha moja kwa moja hadi ofisini kwa Kamanda wa Polisi.
“Wamekwishafika na nusu saa ijayo mtakuwa safarini kwenda Kisiwani Galu, una silaha?”
“Hapana!”
“Unategemea kupambana na nini?”
“Silaha itapatikana hukohuko!”
“Basi jiandae!” Kamanda aliongea akionyesha wasiwasi mwingi na mwisho wa maongezi yake alijaribu kumshawishi Nancy abaki Kigoma ili polisi waende peke yao na kumletea taarifa au kuja na watoto kama wangefanikiwa kuwakomboa lakini Nancy alikataa katakata na kusisitiza aruhusiwe kuambatana na Polisi.
“Lakini una uhakika watoto wako Kisiwani?”
“Asilimia mia moja kwa sababu waliowateka ninawafahamu!”
“Kivipi?”
Ilibidi Nancy amsimulie Kamanda kila kitu kilichotokea maishani mwake mpaka akajikuta yupo kisiwani Galu, ni maneno hayo ndiyo yalimfanya Kamanda aone umuhimu wa Maaskari kuongozana na Nancy kwa sababu alikielewa vizuri kisiwa hicho! Nusu saa baadaye kweli waliondoka hadi ziwani kulikokuwa na boti zilizoandaliwa tayari, wote walipanda na safari ya kwenda Galu ilianza!Maaskari wote waliokuwa ndani ya boti walivaa kizamiaji wakiwa na mitungi ya hewa ya oksijeni migongoni mwao na mpira uliofungwa moja kwa moja kwenye pua zao, Nancy pia alifungiwa mtungi mmoja mgongoni pia akavishwa boya moja kifuani kwake ili limsaidie kama ingetokea boti ikazama.
Safari yao hadi Kisiwani Galu ilitegemewa kuwa ya saa mbili na ndivyo ilivyokuwa, hali ya ziwa ilikuwa shwari lakini kisiwa kilipoanza kuonekana mbele yao kikiwa kama kilometa mbili kutoka mahali walipokuwa mambo yalianza kubadilika, hali ya hewa ikaanza kuchafuka! Uliiubuka upepo mkali kama kimbunga uliyoyazungusha maji na hata boti zao, maaskari walianza kuingiwa na hofu wakijua mambo waliyoyasikia ndiyo yalikuwa yanatokea lakini walijipa moyo kwa sababu wote walivaa vifaa maalum vya kuzamia. Hali ilizidi kuwa mbaya kadri dakika zilivyosonga, kilometa mbili zilikuwa mbele yao zilionekana kama kilometa mia moja, hawakuweza kusonga mbele hata hatua kumi! Boti zao zikabinuka na kuwamwaga majini.
Kelele zilizikika kila mahali, boya alilovaa Nancy lilimsaidia akajikuta akielea majini, lakini kitu kimoja kilimshangaza alikiona kiumbe kisicho cha kawaida kikiogelea katikati yake na maaskari wengine, kilikuwa ni kama binadamu lakini si binadamu wa kawaida! Kilimwogopesha, kila kilipowafikia maaskari kiliwavua mtungi wa hewa na kuwaacha wakitapatapa majini! Wote walifanyiwa hivyo na kilipomfuata Nancy alipoteza fahamu hamu hapo kwa sababu ya woga na kuzinduka akiwa ufukweni katika kisiwa cha Galu saa tano baadaye, alipofungua macho yake alimkuta mzee mmoja amekaa pembeni mwake! Haikumchukua hata sekunde mbili kumtambua, alikuwa Babu Ayoub!
“Umejileta! Nilikumisi sana!” Aliongea mzee huyo akitabasamu.
Mwili wa Nancy ulitetemeka, hakuamini kama alikuwa ameingia mikononi mwa mzee huyo aliyemtesa kwa kipindi kirefu kisiwani, machozi yalimtoka hakuwa na uhakika wa kurudi alikotoka tena! Maaskari wote aliokuwa nao katika safari ya kwenda kisiwani walikuwa wamekufa maji baada ya mitungi yao ya hewa kung’olewa, muda mfupi baadaye akilia mzee Kiwembe aliwasili akiwa na Catherine pamoja na David! Afya zao zilikuwa mbaya na za kusikitisha.
“Karibu kisiwani Nancy, hakuna mtu atakayefanikiwa kuja kukutoa hapa tena!Tumejizatiti vya kutosha!” Aliongea mzee Kiwembe akitabasamu.
Ingawa alikuwa akilia Nancy alishindwa kuvumilia, akanyanyuka mahali alipokuwa amekaa na kwenda kuwakumbatia wadogo zake! Alikuwa katika himaya nyingine alikotegemea mateso makali na pengine maisha yake yote yaliyobaki kuishia katika kisiwa hicho! Hakuwa na uwezo wa kupambana na nguvu za uchawi walizokuwa nazo wazee hao wawili.
*******
Danny hakufa. Wakati akihangaika barabarani usiku alipopigwa mshale na kuachwa shambani kwa mzee Katapila, alitokea mwindaji akitoka porini kutega mitego yake! Alipomwona alishtuka, akasimama na kuanza kumulika na tochi, Danny aliuona huo ndio msaada pekee na kuanza kupiga kelele akiomba msaada. Mwindaji alimsogelea na kumuuliza nini kilichompata, Danny alisimulia kila kitu kwa taabu kubwa akimwonyesha mwindaji huyo mshale uliokuwa mbavuni mwake.Cha kushangaza Mwindaji hakuonyesha mshtuko wowote, alichofanya ni kusimama ubavuni kwa Danny kwa miguu yake yote miwili mshale ukiwa katikati na kuukamata kwa mikono yake yote miwili akaanza kuuvuta kwa nguvu zake zote, Danny alilia kwa maumivu mpaka akapoteza fahamu.
Mshale ulipochomoka damu nyingi ilivuja, mzee huyo mfupi mwenye misuli ambaye pia alibeba upinde na mishale, alikifungua kibuyu kilichokuwa kiunoni mwake, akakifungua na kumwaga dawa nyeusi kwenye mkono wake wa kushoto na yote akaiweka kwenye kidonda kilichokuwa kinamwaga damu! Danny akiwa amepoteza fahamu alibebwa begani hadi kwenye kibanda alichoishi mzee huyo katikati ya pori la Tindiga ambako alilazwa chini na mzee kuchukua pembe ya Mbuzi iliyochomekwa kwenye paa la nyumba. Sehemu pana iliyokuwa wazi aliifunika kwenye jeraha na nchani kulikokuwa na tundu dogo alifunika na mdomo wake kisha kuanza kunyonya hewa iliyokuwemo ndani ya pembe na kuifanya pembe iung’ang’anie mwili wa Danny! Kisha akachukua kitu kama Nta na kuliziba tundu, pembe ikabaki wima! Wakati yote hayo yanafanyika bado Danny alikuwa hajarejewa na fahamu zake.
****
Mzee huyo aliendelea kunyonya damu chafu na nyeusi kutoka kwenye kidonda cha mshale, alifanya hivyo kwa muda mrefu mpaka Danny akaanza kujitingisha na baadaye kufungua macho yake na kuangalia huku na kule! Alishangaa kujikuta yu mahali asipopafahamu, aliyemshangaza zaidi ni mzee aliyekuwa pembeni mwake! Hakumtambua na alishangazwa na shughuli aliyokuwa akifanya kwa kutumia pembe iliyofanana na ya mbuzi. Kwa muda aliendelea kujiuliza maswali mengi kichwani mwake fahamu zikiendelea kumrejea taratibu hatimaye akawa mtu kamili lakini hakuelewa kilichotokea mpaka akawa mahali hapo.
“Shikamoo!” Aliamkia
“Marahaba hujambo? Kama umeweza kuniamkia basi utapona, sikuwa na matumaini! Naitwa mzee Ibrahim, wewe?”
“Danny, kimetokea nini?” Danny aliuliza
“Sumu!”
“Sumu ya nini?”
“Ya mshale! Ilitaka kukuua kabisa, nani alikuchoma?” Swali hilo lilirejesha kumbukumbu zote kichwani mwa Danny, kitu kama mkanda wa sinema kikaanza kuonekana akili mwake, aliona namna alivyosafiri na Nancy kutoka Dar Es Salaam hadi Tindiga shambani kwa mzee Katapila, alivyoruka ukuta na baadaye kuchomwa mshale! Kufikia hapo hakukumbuka kitu zaidi ya giza lililotanda usoni mwake, alilia kwa sauti ya juu akiita jina la Nancy kiasi cha kumfanya babu atake kujua mtu huyo alikuwa nani.
“Ndiye aliyekuchoma mshale?”
“Hapana!”
“Ni nani?”
“Mchumba wangu!”
“Ilikuwaje?” Babu aliuliza.
Kufikia hapo ingawa kwa taabu, mzee Ibrahim akiwa amesimamisha zoezi zima la kunyonya sumu kwa kutumia pembe ya Mbuzi, Danny alilazimika kusimulia kisanga chote hadi kufika shambani kwa mzee Katapila, mzee Ibrahim alishangaa sana! Hakuamini hata kidogo kama mzee Katapila angeweza kuwa amefanya kitendo hicho kwani alikuwa mtu mwenye moyo wa kusaidia sana watu wa vijiji vilivyozunguka shamba lake, Danny alipozidi kumsisitizia ilibidi akubali na kuamua kumsaidia tiba za jadi mpaka apone.
“Nitakutibu kwa tiba za jadi, ukienda hospitali hawan uwezo wa kuiondoa sumu ya mshale mwilini! Utakufa!”
“Lakini nataka kuonana na mchumba wangu!”
“Usiwe na wasiwasi hayo yatafanyika baadaye, kitu cha muhimu kwako hivi sasa ni afya kwanza!”
“Sasa atajuaje kwamba niko hapa?”
“Hilo haliwezekani mpaka utakapopona ndipo utakwenda!”
Baada ya maongezi hayo mzee Ibrahim aliendelea kunyonya sumu kutoka kwenye kidonda, damu nyingi nyeusi ilizidi kutoka na kumhakikishia Danny kuwa hiyo ndiyo ilikuwa sumu ikitoka, mpaka asubuhi alikuwa bado akimfanyia tiba za jadi na kumkanda kwa maji ya moto baadaye alitoka nje na kurudi na majani aliyoyapikicha mikononi mwake kisha kuyabandika kwenye kidonda, maumivu aliyoyapata Danny yalikuwa ni afadhali yale ya mshale, mzee Ibrahim alicheka akimwambia hiyo ndiyo ilikuwa tiba yenyewe.
Matibabu hayo ya jadi yaliendelea kwa wiki mbili mfululizo kidonda kikawa kinazidi kupungua na mwili wa Danny kurejewa na nguvu, aliishi na mzee kwenye kibanda chake wakila nyama za porini pamoja, mawazo yake kila siku yalikuwa kwa Nancy, altamani siku moja apone arejee Dar Es Salaam na baadaye Bagamoyo ambako yeye na mchumba wake wangefunga ndoa! Ilipogota wiki ya tatu kidonda kilishafunga lakini tatizo liliendelea kuwa kifua, kulikuwa na maumivu makali mno ndani ya kifua cha Danny. Alikandwa na maji ya moto kila siku lakini haikusaidia.
“Hiki kifua naona kitanishinda, kidonda kimepona lakini dawa zangu naona hazina uwezo wa kutibu ndani!”
“Sasa?”
“Itabidi uende hospitali! Sina ujanja tena, hata hivyo nimejitahidi na Mungu ametusaidia!” Alisema mzee Ibrahim.
Kwa Danny habari hiyo ilikuwa njema pamoja na kwamba alikuwa bado na maumivu makali kifuani, aliamini hospitali angepona upesi zaidi baada ya kupigwa picha ya kifua kuona mshale ulimuumiza kiasi gani, bado aliamini ndani kulikuwa na matatizo tena makubwa! Alikuwa ameishi na mzee Ibrahim kwa muda mrefu lakini muda wa kuondoka ulikuwa umefika, alimshukuru kwa wema wake na kwa ndani kidogo alisikia huzuni kutengana na mtu aliyeokoa maisha yake bila kufahamu angekutana naye tena lini.
“Sijui kama tutaonana tena mzee Ibrahim!” Danny alisema kwa huzuni.
“Usihuzunike sana Danny, wewe nenda na kama tulivyokutana basi tutakutana tena hivyohivyo, Mungu anafahamu!”
Walikumbatiana na mzee Ibrahim alimsindikiza Danny hadi barabarani karibu kabisa na lango la kuingia shambani kwa mzee Katapila, alimwonyesha mahali alipomkuta akiwa amelala hoi bin taaban! Danny alikumbuka kila kitu baada tu ya kuiona ngome ya shamba hilo, alimkumbuka Nancy pia na alishindwa kuelewa kama alikuwa hai ama alikufa katika mapambano ya siku hiyo. Muda mfupi wakiwa barabarani lilitokea lori lililobeba mbao, ni mzee Ibrahim aliyepunga mkono likasimama na kumwombea Danny msaada wa usafiri! Bahati nzuri lilikuwa likielekea Kilosa, aliruhusiwa kupanda nyuma na kusafiri hadi Kilosa.
Hakuwa na kitu kingine cha kufanya baada ya kufika mjini Kilosa zaidi ya kutembea hadi hospitalini umbali wa kama kilometa tano kutoka mahali aliposhushiwa, ilikuwa saa tatu na nusu wakati anafika mapokezi na kuandikisha jina lake, mfukoni hakuwa hata na senti tano, alishukuru Mungu hospitali ilikuwa ya serikali, baada ya kujiandikisha aliingia chumba cha daktari na kutoa maelezo yake, yaliyomshtua daktari hasa baada ya kuliona jereha lililokuwa ubavuni mwa Danny.
“Kwa hiyo ulichomwa mshale?” Daktari aliuliza kwa mshangao.
“Ndio!”
“Kwenye mapambano ya wakulima na wafugaji wa Kimasai au?”
“Hapana!” Alikataa Danny na kumsimulia daktari juu ya tukio lilitokea shambani kwa mzee Katapila, bahati nzuri daktari huyo alishasoma kila kitu kama magazeti na hakuona sababu ya kuendelea na matibabu bila kuitaarifu polisi, muda mfupi baadaye maaskari walifika lakini hawakuchukua maelezo ya Danny mpaka alipotoka chumba cha kupigwa picha ya kifua! Maaskari hawakuamini kama Danny waliyekuwa wakiongea naye ndiye ambaye habari zake ziliandikwa katika magazeti kwamba aliliwa na Simba.
“Wewe ndio Danny?” Mmoja wa maaskari aliuliza.
“Ndio afande!”
“Ulikuwa wapi?”
“Porini!”
“Hukuliwa na Simba?”
“Afande ningeliwa na Simba ungeniona hapa?”
“Basi tueleze kilichotokea!”
Danny alitoa maelezo yake kwa mara nyingine, wakati anamaliza tayari picha ya X-ray ilishakuja na daktari alimtaarifu kwamba kulikuwa na damu iliyokuwa imevuja kifuani na ilikuwa inagandamiza dayaframu hivyo kumsababishia maumivu makali kifuani, Daktari alimthibitishia kuwa hapakuwa na tiba nyingine zaidi ya operesheni ya kifua ambayo hata hivyo isingeweza kufanyika katika hospitali ya wilaya, isipokuwa hospitali ya mkoa wa Morogoro! Siku hiyo hiyo alisafirishwa hadi Morogoro ambako alifanyiwa upasuaji na damu iliyoganda kifuani kwake kuondolewa, alizinduka masaa kumi na sita baadaye na kujikuta kitanda chake kimezungukwa na watu aliowafahamu, tena wakilia machozi.
“Danny!” Ilikuwa sauti ya mzee Katobe!
“Naam baba!”
“Upo hai?”
“Kabisa! Mungu ni mwema, ameokoa maisha yangu!”
“Kila mtu anaamini uliliwa na Simba, tuliposikia taarifa ya habari kuwa umepatikana hatukuamini, tuliondoka Bagamoyo saa hiyohiyo na tumefika masaa mawili yaliyopita! Unajisikiaje sasa?”Mama yake Nancy alimuuliza Danny.
“Nafuu kidogo ingawa bado kuna maumivu, kuna jambo moja tu nataka kuuliza! Nilikosa kabisa mtu wa kumuuliza, hata polisi sikudiriki kuwauliza, nilikuwa naliogopa jibu ambalo ningepewa lakini bora mnieleze ukweli!”
“Nini mwanangu?” Mzee Katobe aliuliza.
“Mchumba wangu Nancy! Yupo hai au ni marehemu?” Jibu la Danny liliishia na swali.
Mzee Katobe na mke wake waliangaliana, Danny akaishuhudia ishara fulani kwenye jicho la mama yake Nancy! Alielewa kilichoendelea, kuna siri iliyokuwa ikifichwa bila hata kuelezwa alihisi Nancy alikuwa marehemu, alilia hadi mwisho wa uwezo wake na kusababisha kidonda chake cha upasuaji kuuma kupita kiasi na hata damu kuanza kuvuja! Daktari alipoitwa aliamuru Danny apewe dawa za usingizi, akalala na kuzinduka siku iliyofuata asubuhi! Mzee Katobe na mkewe wakiwa pembeni mwa kitanda chake, waliyaelewa madhara ya kumweleza ukweli, hawakuwa na njia zaidi ya kumdanganya alipohitaji kuelezwa wapi Nancy alikokuwa, hata wao walichofahamu ni kwamba Nancy hakuwa hai! Taarifa walizosoma katika vyombo vya habari kuwa askari wote alioongozana nao walikufa, ziliwafanya waamini hata mtoto wao hakuwa hai..
“Ni mzima tu!”
“Sasa kwanini yeye hakuja?”
“Alisafiri kwenda Kigoma kumsindikiza mzee Mwinyimkuu!”
“Naye alinusurika?”
“Tulinusurika pamoja naye, Nancy alituokoa!”
“Ni msichana jasiri sana, ninafurahi kuwa na mchumba kama yeye!” Alisema Danny uso wake ukionyesha tabasamu kidogo.
Wiki tatu baadaye aliruhusiwa kutoka hospitali akaondoka na wazazi wa Nancy hadi Bagamoyo ambako watu walishikwa na mshangao kumwona akiwa hai karibu wakazi wote wa mji wa Bagamoyo waliamini Danny alishaaga dunia, kwani ndivyo ilivyotangazwa! Kuonekana kwake akiwa hai kuliibua furaha ya ajabu na kufanya nyumbani kwa mzee Katobe kuwa na kitu kama sherehe kubwa ya mtoto kurudi nyumbani, Mbuzi alichinjwa na damu yake kunyweka kwenye sherehe hiyo ili kuondoa nuksi mwilini kwa Danny! Wakati watu wakisherehekea mawazo ya Danny yalikuwa kwa Nancy, hakulala wala hakuwa na kitu kingine kilichoendelea kichwani mwake! Alimhitaji Nancy si kwa jambo jingine ila wafunge ndoa baada ya mateso na kusubiri kwa muda mrefu.
“Atakuja tu!”
“Lini?”
“Tutajaribu kufanya naye mawasiliano!”
Hayo ndiyo yalikuwa majibu ya wazazi wa Nancy, Danny alipojaribu kudadisi juu ya Nancy lakini minongono ilisikika katika watu waliokuwa katika sherehe hiyo na kumfikia Danny kuwa mchumba wake alifariki dunia pamoja na maaskari wengine waliokuwa wakisafiri pamoja kwenda kisiwani Galu kuwakomboa wadogo zake Catherine na David! Danny alilia tena, ilibidi mzee Katobe na mkewe wamweleze ukweli! Hakuwa tayari kuukubali ukweli huo.
“Haiwezekani! Hawezi kuwa amekufa, siwezi kuamini mimi ni kama Thomaso mpaka nikuguse kwa mikono yangu, nitasafiri mwenyewe mpaka huko Kigoma na baadaye kwenda Kisiwani Galu hata kama nikifa ni sawa tu! Lakini sauti ninayoisikia moyoni mwangu ni kwamba, Nancy yupo hai na yupo katika mateso makali!” Aliongea Danny akilia na kuwafanya mzee Katobe na mke wake pia wabubujikwe na machozi, walimweleza hatari zilizokuwepo kisiwani Galu na idadi kubwa ya maaskari waliopoteza maisha lakini bado Danny hakukubali alitaka kwenda kujaribu na kujionea mwenyewe.
“Acha tu mwanangu! Sisi tulishapoteza na tumezoea!”
“Haiwezekani wazazi wangu, nawaombeni sana mniwezeshe kusafiri hadi Kigoma ili nimfuatilie Nancy, hajafa yupo hai! Hivyo ndivyo moyo wangu unavyonieleza!” Aliendelea kusisitiza Danny lakini mzee Katobe na mkewe waliendelea kumkatalia katakata, siku iliyofuata asubuhi walishangaa kukuta Danny hayupo chumbani akiwa ameacha ujumbe kuwa alikuwa amesafiri kwenda Kigoma na baadaye Galu kumfuatilai Nancy na wadogo zake..
“.......Lolote litakalonipata ni halali yangu sitakuwa na mtu wa kumlaumu, maisha yangu yamejaa mateso ni bora nikayamalizie huko huko Galu!” Ndivyo ulivyomalizia ujumbe huo.
*****
Tayari Nancy alikuwa kisiwani Galu tena, mikononi mwa mzee Kiwembe na babu Ayoub! Hakuwa na matumaini ya yeye kurejea nyumbani tena, safari yake ya kwenda kuwaokoa wadogo zake ilikuwa imemrudisha utumwani! Hakuwa na la kufanya, aliyarudia mateso aliyoyakimbia! Babu Ayoub alifurahi sana kumwona na alitaka mambo yale yale ya zamani yaendelee, amgeuze Nancy mke wake jambo ambalo Nancy hakukubaliana nalo kabisa, kila siku ulikuwa ni ugomvi tena mkubwa, hakuwa tayari kufanya tendo la ndoa na mzee huyo! Kitendo hicho kilimkera babu Ayoub akalazimika kufungua kisanduku chake na kutoa dawa fulani ambayo kila alipompulizia nayo Nancy puani alilala usingizi na kilichofuata baada ya hapo hakikuwa kingine zaidi ya ngono! Yalikuwa mateso makubwa tena makali, kwa mara nyingine alifanywa mtumwa wa ngono.
Ilikuwa siku moja ikawa wiki, hatimaye mwezi ukaisha akiwa kisiwani! Mwisho akalazimika kuyazoea mazingira, hapakuwa na njia ya kutoroka kuondoka kisiwani hivyo alihamishia nguvu zake katika kuwatunza wadogo zake ambao afya zao zilikuwa mbaya kwa wakati huo! Akazoea na kukubali kuwa mke wa babu Ayoub, aliamua kujifanya mjinga lakini akiwa na moja kichwani! Alitaka kuelewa siri iliyokuwepo katikati nguvu za giza za wazee hao zilizowaua maaskari kila walipojaribu kuingia kisiwani hapo na hakuwa na njia nyingine zaidi ya kujifanya yu katika mapenzi mazito na babu Ayoub.
“Nitafahamu tu! Kama Delila aliweza kufahamu siri ya nguvu za Samson, mimi nitashindwaje wakati mimi ni mwanamke kama yeye?” Aliwaza Nancy akiamini lazima siku moja afahamu siri ya nguvu walizokuwa nazo wazee hao wawili, ingawa hakuelewa ni lini lakini alikuwa na uhakika siku moja angefahamu na hiyo ndiyo ingekuwa siku ya ukumbozi wake.
Akawa mama wa nyumbani, akiwatunza na kuwajali wazee hao wawili pamoja na ndugu zake! Lakini kumbukumbu za nyumbani hazikumpotea, kitu kikubwa alichokiomba ni Mungu kumsaidia asipate ujauzito, hakulipenda kabisa jambo hilo! Hakutaka kuzaa na babu Ayoub, hakutaka makosa yaliyojitokeza kwa mama yake mpaka kuwazaa wadogo zake Catherine na David yatokee kwake.
“Laiti nigekuwa na vidonge vya majira ningekunywa lakini kwa hivi sasa sina, namwomba Mungu anisaidie mpaka nitakapoondoka hapa kisiwani!” Hayo ndiyo yalikuwa mawazo yake kila siku.
Mateso yaliendelea kila siku Nancy alitamani kuondoka lakini hapakuwa na njia ya kufanya hivyo, alikuwa chini ya ulinzi mkali akila samaki kila siku mchana na jioni, hakuna siku aliyofurahia maisha, kila siku ilikuwa huzuni lakini akiwa mbele ya mzee Kiwembe na babu Ayoub alijifanya hana kitu kilichomsumbua mpaka wakajikuta wamemzoea kabisa na kumwona ni sehemu ya maisha! Kila siku usiku ilikuwa ni ngono babu Ayoub naye akitafuta mtoto kutoka kwa Nancy lakini hakufanikiwa. Ni fikra juu ya Danny ndizo zilizomuumiza zaidi Nancy, alisikitika kwamba alikuwa marehemu, aliamini ni mwanamume pekee aliyempenda chini ya jua la Mungu! Alipokifikiria kifo chake kwa kuliwa na Simba aliumia zaidi na kuna wakati alijitupia lawama yeye mwenyewe kwa kusahau kumchukua wakati wanaondoka shambani kwa mzee Katapila, Tindiga.
Pamoja na shida zote zilizokuwepo kisiwani Galu, Nancy aliwapenda wadogo zake kupita kiasi na aliwalinda, kuwepo kwake kisiwani humo kulibadilisha hata afya zao! Ghafla wakawa ni watoto wenye afya njema ambao pia walilia kila walipowafikiria wazazi wao! Jambo hilo lilimtia huzuni sana Nancy na kufanya aumize kichwa ni kwa njia gani angeweza kuondoka na wadogo zake na kurudi Kigoma na baadaye Dar kisha Bagamoyo, hakuna siku angefurahi maishani mwake kama siku ambayo angerudi hadi Bagamoyo, hakika ingekuwa sherehe kubwa! Alitamani kuokolewa lakini alijua mpaka wakati huo hakuna mtu angeweza kumwondoa kisiwani, nguvu za giza za wazee hao wawili zilikuwa za kutisha.
“Mpaka nitakapozielewa mimi mwenyewe namna nguvu hizo zinavyotumika ndipo nitaweza kuondoka kisiwani hapa na wadogo zangu na kazi hii inaanza leo, maana babu Ayoub amekwishaanza kuniamini!”
Usiku wa siku hiyo Nancy alifanya kila alichokiweza kumburudisha babu Ayoub, alimfanyia mambo ambayo mzee huyo hakuwahi kufanyiwa na wakiwa katikati ya starehe alianza kumuuliza maswali juu ya nguvu alizozitumia! Badala ya kupata jipu zuri alishangaa kuona mzee huyo akinyanyuka kitandani na kusimama wima uso wake ukiwa umekunjwa kuonyesha hamaki aliyokuwa nayo.
“Unafikiri unaweza kunilaghai kwa njia hiyo? Huwezi! Hutaelewa nguvu hii milele, kama unataka kuelewa ili utoroke basi umekwama!” Aliongea babu Ayoub na kuendelea kufoka hadi asubuhi, siku hiyo hawakuongea kitu kabisa walishinda wamenuniana, Nancy alishindwa kuelewa ni kwa njia gani angeondoka kisiwani! Mpaka wakati huo aliamini ni lazima Jeshi la Polisi lilikuwa likijitahidi kuingia kisiwani lakini lilishindwa kwa sababu ya uchawi ambao wazee hao walikuwa nao.
*********
Danny alisafiri kwa treni hadi Kigoma na kuingia siku tatu baadaye akiwa amechoka kupita kiasi, jambo la kwanza aliloamua kulifanya ni kwenda kituo cha polisi cha kati mjini Kigoma na kuulizia mahali ambako jeshi la polisi lilikuwa limefikia katika juhudi zake za kwenda kuwakomboa watoto Catherine na David kisiwani Galu, jibu alilolipata kituo cha polisi lilimsikitisha sana, kwamba hapakuwa na uhakika kama kweli kulikuwa na watu katika kisiwa hicho! Hivyo polisi walikuwa wameamua kusitisha zoezi kwani wasingeendelea kufanya kazi kufuata maneno ya kusemwa tu ukizingatia kulikuwa na upepo mkali sana uliosababisha vyombo kuzama na askari wengi kupoteza maisha.
“Kwahiyo mmeamua kuacha mambo hivyo hivyo?” Danny alimuuliza Mkuu wa upelelezi wa Mkoa alipopata nafasi ya kuonana naye.
“Ndio!”
“Haiwezekani! Hata siku moja, yaani jeshi la polisi lishindwe kukomboa watu walioko kisiwani?”
“Ungekuwa wewe ungefanya nini kijana?”
“Ningefanya lolote linalowezekana mpaka nifike kisiwani!”
“Basi wewe fanya kama unaweza!”
“Na hilo ndilo lililonifanya nisafiri kuja Kigoma, siamini kama mchumba wangu Nancy alikufa, lazima nifuatilie kama nyie mmeshindwa basi juu yenu!” Alisema Danny na hapohapo alinyanyuka na kuanza kuondoka, alitembea hadi nje ambako pia hakusimama! Alitamani kusafari siku hiyo hiyo kwenda kisiwani Galu lakini hakuwa na fedha za kukodisha boti ambayo ingemfikisha katika kisiwan hicho hatari, hakuogopa kupoteza maisha yake ilimradi alikuwa akimfuatilia Nancy! Kwake kufa ilikuwa ni sawa na kuungana na mchumba wake ahera kama kweli alikuwa marehemu! Alishanusurika kufa mara ya kwanza hakuogopa kifo hata kidogo.
Alishuka moja kwa moja hadi ziwani ambako aliona mitumbwi mingi ya wavuvi, kichwani mwake kulikuwa na wazo moja tu! Kutafuta kibarua ambacho kingemwezesha kupata fedha ya kufanyia jambo moja, kukodisha boti ambayo ingemfikisha kisiwani! Siku hiyo hakubahatisha kupata kibarua lakini siku iliyofuata alipata kazi ya kuvuta, kokoro lililotumika kutega samaki wadogowadogo, siku hiyo peke yake alipata shilingi elfu tano! Kwa wiki nzima alifanya kazi hiyo na kupata shilingi elfu ishirini, pesa hiyo aliingiza katika biashara ya samaki na kuwa anapata faida ya shilingi elfu kumi kila siku aliponunua na kwenda kutembeza katika nyumba za watu sehemu iliyoitwa Mwanga. Alikuwa na hamu ya kutimiza shilingi laki moja na elfu ishirini, kwani alishapeleleza na kuambiwa gharama ya kukodisha boti yenye injini kwenda hadi Kisiwani Galu ilikuwa ni shilingi elfu themanini, alihitaji shilingi elfu ishirini zaidi kwa ajili ya kununulia panga, mkuki, upinde na mishale, hakuwa na uhakika wa kupata bunduki hivyo alilazimika kutafuta silaha za jadi.
Wiki tatu baadaye pesa ilishatimia, akanunua silaha alizozihitaji na kukodisha boti yenye injini mbili kumpeleka Kisiwani Galu! Alielewa ugumu wa safari yake kwa sifa alizokwishakuzisikia lakini hakuogopa, alishaamua kuyatoa maisha yake kwa ajili ya Nancy! Waliondoka Kigoma saa tisa na nusu za alasiri, masaa manne baadaye giza likianza kuingia walianza kukiona kisiwa cha Galu mbele yao, Danny akaanza kuwa na matumaini.
“Si ndio kile?”
“Haswa!” Alijibu Nahodha aliyeendesha boti ambayo Danny alikodi.
“Kumbe sio mbali?”
“Ni kwa sababu boti yangu inakwenda kwa kasi sana!”
“Kweli kabisa!”
“Unakwenda kisiwani kufanya nini?”
“Mimi ni mwindaji wa wanyama, huwa nasafirisha kwenda nje!”
“Kazi hiyo itakuchukua siku ngapi?”
“Mbili hivi!”
“Kwa hiyo tutakuwa kisiwani kwa siku mbili?”
“Hivyo ndivyo!”
“Itabidi uongeze pesa kidogo!”
“Hakuna shaka!” Danny alimdanganya Nahodha huyo kila kitu alichosema, asingeweza kumwambia ukweli juu ya sifa za kisiwa walichokuwa wakienda lakini baada ya kuwakomboa Nancy na wadogo zake ndio angeweza kusema ukweli wake
Walizidi kusonga mbele wakikaribia kisiwa na giza lilizidi kuongezeka, wakati huo kisiwa kilionekana kuwa kama mita mia moja kutoka mahali walipokuwa, moyo wa Danny ulikuwa ukipiga kwa nguvu ukijua sasa kazi ya ukombozi ilikuwa imewadia! Alikuwa na uhakika ndani ya moyo wake kwamba Nancy alikuwa hai na ilikuwa ni lazima amwokoe na kama hakuwa hai basi bado alikuwa na wajibu wa kuwaokoa Catherine na David na kurudi nao hadi Kigoma na baadaye kwenda nao Bagamoyo.
“Mh!” Nahodha aliguna ghafla.
“Vipi?”
“Sikioni!”
“Nini?”
“Kisiwa!”
“Kweli eh? Si kilikuwa hapa mbele yetu?”
“Yaani nashangaa! Kimepotea ghafla, ni kitu gani kinatokea?” Nahodha aliuliza na kabla Danny hajajibu chochote kilitokea kimbunga cha ajabu na kuanza kuyazungusha maji kama ilivyotokea kwa maaskari waliopoteza maisha yao majini, Nahodha alianza kupiga kelele na muda mfupi baadaye boti yao ilibinuliwa wakamwagwa majini, Danny alijaribu kuogelea lakini hakuwa na uwezo huo, maishani mwake hakuwahi kufanya mazoezi ya kazi hiyo! Alianza kunywa maji kisha kuzama, akaibuka juu na kuzama tena, alifanya hivyo kama mara tatu akinywa maji alipoibuka mara ya nne hakuwa na fahamu kabisa.
*****
Nancy alikuwa nje ya kibanda cha babu Ayoub akiwa mwenye mawazo mengi kichwani mwake, alijaribu kufikiria mambo yaliyokuwa yakijitokeza maishani mwake, tabu alizokuwa akizipata akiwa kisiwani Galu na kujiona ni mtu mwenye mkosi!
Alitamani kuwa huru na kuishi maisha yasiyo na maumivu kama aliyokuwa akiishi kisiwani humo akifanywa mtumwa wa ngono na babu Ayoub jambo ambalo hakulifurahia hata kidogo! Wadogo zake Catherine na David walikaa pembeni mwake nje ya kibanda chao.
Kulikuwa na giza kila mahali lakini hawakuogopa kwani walishazoea maisha ya kisiwani, ghafla aliwaona mzee Kiwembe na Babu Ayoub wakitokea ufukweni wakiwa wamebeba kitu kizito mikononi mwao, hakutaka kujiuliza maswali mengi, aliamini labda alikuwa ni samaki mkubwa waliyemnasa siku hiyo. Wazee hao wawili hawakusimama walinyoosha moja kwa moja hadi nyuma ya kibanda kulikokuwa na kibanda kingine kidogo walichokitumia kuhifadhi samaki waliowakausha.
Nancy hakuwajali, aliendelea kukaa kimya akiwa amewakumbatia wadogo zake waliokuwa wakiwindwa na usingizi, ilikuwa ni kawaida yake kuwasimulia hadithi kila siku jioni kabla ya kulala na kuwakumbusha historia ya mahali walipotokea na kwamba siku moja wangerejea tena nyumbani kwao ambako wangeishi kwa raha mustarehe!
Muda mfupi baadaye aliwashuhudia tena babu Ayoub na mzee Kiwembe wakitokeza kutoka nyuma ya kibanda, wote wawili wakicheka! Haikuwa kawaida yao kuwa na sura hizo kila walipotoka ziwani kwa shughuli za uvuvi, Nancy alijikuta akitaka kufahamu ni kitu gani kilikuwa kimetokea.
“Vipi jamani mbona meno nje?”
“Tumemleta!”
“Nani?”
“Aliyejifanya bingwa kuliko wenzake!”
“Nani?”
“Mumeo mtarajiwa!” Alisema babu Ayoub, mara nyingi Nancy alishamsimulia juu ya Danny na namna alivyokufa na ni kiasi gani alimpenda.
“Mume wangu mtarajiwa nani?”
“Danny!”
“Danny?”
“Ndio!”
“Mmemtoa wapi?”
“Ziwani! Tulipata taarifa kwa njai tunazozifahamu kuwa anakuja na tukaenda kumpokea!”
“Yuko wapi?”
“Nyuma kwenye kibanda cha samaki!”
“Mnanitania!”
“Nenda kaangalie mwenyewe!”
Nancy akiwa amepigwa na butwaa bila kuamini alichokisikia kwa masikio yake alinyanyuka na kukimbia moja kwa moja hadi nyuma ya kibanda kulikokuwa na kibanda kingine kidogo, kwa jinsi kilivyokuwa kifupi alipiga magoti chini na kukifungua!
Kweli binadamu alikuwa ndani yake kwa sababu ya giza lililokuwepo hakuweza kuelewa mara moja kama kweli alikuwa Danny! Alinyanyuka na kukimbia hadi ndani ambako alichomoa nyasi kwenye paa la kibanda chao na kuziwasha na moto kisha kukimbia hadi nyuma ambako alimulika ndani ya kibanda na kumwona vizuri mtu aliyekuwa amelala ndani yake!
Haikuwa rahisi kuamini kuwa kweli mtu huyo alikuwa ni Danny ingawa ndicho kitu macho yake yalichoshuhudia, alihisi ni ndoto hata hivyo alijikuta akiutupa moto pembeni na kwa mikono yake miwili akaanza kumvuta Danny kumtoa ndani ya kibanda, aliyafanya yote hayo huku babu Ayoub na mzee Kiwembe wakishuhudia.
“Danny!Danny!Danny!” Aliendelea kuita Nancy lakini Danny hakuitika.
Alikuwa kimya kabisa kiasi cha Nancy kushindwa kuelewa kama alikuwa hai au mfu, kwa mara nyingine alipiga magoti chini akainamisha kichwa na kuweka sikio lake kifuani sehemu ya moyo na kuanza kusikiliza, aligundua moyo wake ulikuwa bado ukidunda.
Hakupata jibu ni namna gani Danny aliweza kusafiri hadi kisiwani hapo, wakati alichoamini kabla ya kuondoka Bagamoyo ni kwamba alikufa kwa kuliwa na Simba! Pamoja na hayo yote bado kichwani mwake alihisi ni ndoto na kufikiri muda si mrefu angezinduka na kujikuta yuko peke yake katika mateso kisiwani Galu.
Alichokiona kwa macho yake kiliendelea kuwa ukweli na hakuchoka kumtingisha huku akilia na kumwita kwa jina, picha iliyoonekana iliwaonyesha babu Ayoub na mzee Kiwembe ni kiasi gani Nancy alimpenda Danny.
“Unampenda sana sio?”
“Siwezi kusema uongo, ni kweli na mimi na yeye tulipanga kuoana muda mrefu uliopita, bila matatizo yaliyojitokeza hivi sasa mimi ningekuwa mke wake!” Nancy alijaribu kuwa mkweli kadri alivyoweza ili kuwaelewesha wazee hao ni namna gani alimpenda Danny, mwisho kabisa aliwashukuru kwa kumwokoa.
“Tumemwokoa kwa makusudi! Ili tuje tumuue mbele yako!”
“Jamani nawasihi msifanye hivyo!”
“Kwanini?”
“Nampenda!”
“Kwahiyo unataka kuondoka naye?”
“Si hivyo lakini nawaomba msimuue kwa mara nyingi nawashukuru sana mmemwokoa!”
“Tunasema tumemleta hapa kumuua mbele ya macho yako na wewe ukileta ubishi pia utauawa! Sisi si watu wa kuchezea hata kidogo!”
“Naelewa!”
“Mzee Kiwembe hebu mwonyeshe mfano!” Babu Ayoub alisema na mzee mwenzake akakimbia kwenda kwenye kibanda chake kilichokuwa jirani tu ambako alichukua fimbo ya Kiboko na kutoka nayo kisha kutembea nayo hadi mahali alipolala Danny akiwa hajitambui.
Kwa fimbo aliyokuwa nayo mzee huyo alianza kumchapa Danny mbavuni na sehemu nyingine za mwili baada ya kuwa amemvua nguo zote! Ngozi ya Danny ilichanikachanika na damu nyingi kumtoka! Nancy alijaribu kutaka kumzuia mzee Kiwembe asiendelee na zoezi alilokuwa nalo lakini haikuwezekana, babu Ayoub alimshika na kumzuia hata kusogea karibu.
Nancy alilia akiwaomba wasiendelee kumchapa lakini hawakusikia na mzee Kiwembe alipochoka alimkabidhi babu Ayoub fimbo na yeye kuendelea kumchakaza Danny kwa fimbo, walikuwa wamedhamiria kumuua kwa kumchapa na fimbo! Hata watoto Catherine na David pia walilia kushuhudia Danny akichapwa kiasi hicho.
Saa nzima baadaye zoezi lilisitishwa mzee Kiwembe akawachukua Catherine na David kwenda nao kwenye kibanda chake na Nancy alivutwa na babu Ayoub kwenda chumbani kwao. Kwa nguvu zake za kike alijaribu kuzuia asipelekwe lakini alishindwa, hakuwa na ubavu wa kupambana na mzee huyo, wakiwa ndani alilazimishwa kulala kitandani, huku akilia alitii amri hiyo na kujitupa kitandani. Mpaka wakati analala kitandani bado Nancy aliamini kilichokuwa kikiendelea kilikuwa ni ndoto ndefu! Isingewezekana hata kidogo Danny awe hai wakati aliliwa na Simba huko Kilosa mkoani Morogoro, isingewezekana tena awe Kisiwani Galu maelfu ya kilometa kutoka Bagamoyo.
Nancy aliendelea kuwaza na kuyalinganisha mambo yaliyokuwa yakitokea na ukweli! Usiku huo tofauti na siku nyingine zote hakuna kilichofanyika kati yake na babu Ayoub lakini kitu cha kwanza alichokifanya asubuhi ni kunyanyuka kitandani na kutembea hadi nje kwenda kuhakikisha kama kweli alichokiona jana yake kilikuwa ni kweli au ndoto, alishindwa kufanya hivyo usiku kwa sababu mlango ulifungwa na babu Ayoub na ufunguo kufichwa lakini kulipokucha aliufungua mlango.
********
Nancy aliamini alichokiona jana yake kilikuwa si ndoto baada ya kumwona Danny akiwa ameketi kitako ardhini na kunyoosha miguu yake huku akilia, ni kweli alikuwa yeye, macho yake hayakumdanganya! Alikaa pembeni mwake na kuanza kumwita kama alivyofanya jana yake,Danny alimwangalia kwa macho ya huruma bila kuitika wala kusema chochote pia alionekana kutoamini alichokuwa akikiona mbele ya macho yake. Wote wawili walikuwa wakilia na Nancy hakukata tamaa, aliendelea kumwita mpaka alipoitika.
“Nili..jua hu....jafa Nancy, hatimaye nimekuona, siyaamini macho yan...gu hivi sasa nipo tay...ari kufa ili mradi nime...kuona kwa mara nyingine!” Aliongea Danny kwa taabu.
“Siamini macho yangu, kama nimekuona tena! Nilikuwa naamini ulikufa kwa kuliwa na Simba, umefikaje hapa kisiwani Galu?!”
Danny alianza kumsimulia Nancy kila kitu kilichotokea ingawa kwa taabu kubwa, alielezea mateso aliyoyapata tangu shambani kwa mzee Katapila, nyumbani kwa mwindaji alikoishi akitibiwa kwa tiba za jadi! Operesheni aliyofanyiwa hospitalini Kilosa, hatimaye kuruhusiwa kutoka hospitali na wazazi kumweleza kila kitu kilichompata mchumba wake na kuamua kuwatoroka wazazi wa Nancy kwenda Kigoma, alieleza namna alivyopata pesa na kukodisha boti iliyomleta hadi karibu na Kisiwa cha Galu ambacho hata hivyo kilipotea machoni pao na baadaye dhoruba kubwa kutokea.
“Kwa hiyo baba na mama wanaamini mimi nilikufa?”
“Kweli kabisa na si hao tu, kila mtu ana....amini wewe ni ma....rehemu hata mimi nilitu....mia uja....siri tu!” Aliongea Danny kwa shida.
“Hawa wazee ni wachawi sana Danny, hata siku nilipokuja mimi yalinikuta mambo kama yaliyokukuta wewe! Dhoruba kali ilijitokeza na maaskari wote niliosafiri nao walikufa maji, mimi peke yangu nafikiri ndiye niliyenusurika ni wao waliofanya ninusurike na wameniambia walipata taarifa za kuja kwako wakaja kukupokea, kwa hiyo uliyekuwa umemkodisha lazima atakuwa amekufa maji!” aliongea Nancy.
“Sasa tufanyaje kuondoka hapa kisiwani kwani ni lazima tuondoke!”Alisema Danny
“Kweli kabisa Danny, lazima tuondoke hapa twende tukafunge ndoa yetu, mambo ninayofanyiwa hapa sijui kama utaweza kuyavumilia lakini mpaka sasa sielewi tutatumia njia ga..!” Kabla Nancy hajamaliza sentensi yake mlango wa banda la babu Ayoub ulianza kufunguliwa, alishtuka akijua mateso kwa Danny yalikuwa yanaanza upya.
“Rudi chini, lala chini haraka Danny! Jifanye huna fahamu au umekufa, huyu mzee anayekuja ni hatari!” Alisema Nancy harakaharaka na Danny alitii na kujitupa chini akatulia tuli!
Babu Ayoub alitembea taratibu kuelekea mahali Nancy alikokuwa ameketi pembeni mwa Danny aliyelala chali akijifanya hana fahamu, mkononi mzee huyo alibeba panga lenye makali kotekote, uso wake ulionekana kujawa na hasira! Nancy alielewa jambo lililokuwa mbioni kutokea.
*****
Nancy akielewa kilichokuwa kikitaka kutokea alinyanyuka mara moja na kumfuata babu Ayoub na kuanza kumbembeleza asimtendee Danny kitendo chochote cha kikatili, aliongea akilia machozi huku akimwambia mzee huyo hapakuwa na sababu yoyote ya kumuua Danny kama yeye Nancy alikuwa tayari ni mke wake!Babu Ayoub alionekana kutoyajali maneno yaliyotoka mdomoni mwa Nancy, alizidi kusonga mbele kumfuata Danny! Alikuwa amedhamiria kumuua mbele ya Nancy ili aweze kummiliki mwanamke huyo moja kwa moja, Nancy hakuchoka alizidi kumbembeleza mwisho alipiga magoti chini na kumshika miguu akimwomba arudishe moyo wake nyuma na kumhurumia Danny.
“Hana makosa! Kama ni mimi na yeye kupendana ilikuwa ni zamani babu Ayoub, tafadhali usimdhuru ni bora umwache hai hata kama utakuwa unamfungia kwenye kile kibanda kidogo, inatosha kuliko kuitoa roho yake!” Aliendelea kuongea Nancy na katika hali ambayo hakuitegemea kabisa alishangaa kumwona babu Ayoub akinyoosha mkono wake na kumkabidhi Nancy Panga, kwa fikra zake Nancy alifikiri labda angeelezwa alirudishe panga hilo ndani lakini alishangaa alipoyasikia maneno yaliyotoka mdomoni mwa babu Ayoub.
“Mcharange!”
“Unasema?”
“Nasema umkatekate wewe mwenyewe mpaka afe!”
“Jamani babu Ayoub! Kwanini unanipa mtihani mgumu kiasi hiki? Unajua kabisa siwezi kumuua Danny ingawa simpendi tena, nakupenda wewe!”
“Achana na hayo ninachosema mimi ni kwamba nataka umkatekate kwa panga akatike vipandevipande!”
“Siwezi! Labda ufanye mwenyewe!”Aliongea Nancy akilia.
Danny alikuwa kimya akijifanya mfu wakati alielewa kila kitu kilichoendelea, moyoni mwake hakuwa na uhakika na kitu ambacho kingetokea dakika kumi baadaye! Alifahamu Nancy asingeweza kumkatakata kwa panga kama alivyokuwa akiamriwa lakini alielewa babu Ayoub alikuwa na uwezo wa kufanya hivyo, muda wote akiwa amefumba macho alimwomba Mungu muujiza utokee ili asiweze kuuawa, hakuwa na msaada mwingine wowote isipokuwa kwa Mungu!
Babu Ayoub alilinyakua panga toka mikononi mwa Nancy na kuunyanyua mkono wake juu tayari kwa kushusha na kumkatakata Danny, Nancy alikuwa akilia na kumbembeleza mzee huyo asifanye kitendo alichotaka kufanya, alimhakikishia yeye na Danny kusingekuwa na kitu tena! Alitumia kila aina ya maneno kubadilisha msimamo wa mzee huyo aliyeonekana wazi kumchukia Danny! Katika mshangao ambao Nancy hakuutegemea babu Ayoub alishusha panga lake chini huku akihema kwa nguvu, huruma ilikuwa imemwingia! Aliyaamini maneno ya Nancy na kuamua kuahirisha mauaji aliyotaka kuyafanya, mwili wa Danny ulikuwa umekufa ganzi akisubiri panga lishuke mwilini mwake hapo ndipo angeanza kupambana.
“Huyu hajafa!”
“Bado amezimia!”
“Nancy!”
“Bee!”
“Namwacha hai kwa sababu yako, nakupenda sana na sitaki kukuumiza lakini sitaki kuona uhusiano wa karibu kati yako na yeye na siku yoyote nitakapogundua kuna jambo linaendelea mtakiona cha mtema kuni, nitamuua yeye na wewe!”
“Sawa! Ahsante sana mpenzi, hautaona chochote kibaya! Kumbuka mimi ninakupenda na simpendi Danny tena, ilikuwa zamani wa sasa hivi ni wewe!” Aliongea Nancy akitetemeka bila kuamini kilichokuwa kimetokea, maneno yake ya kubembeleza yalikuwa yamefanya babu Ayoub aahirishe mauaji.
Si kwamba hakumpenda Danny, alimpenda kuliko kitu kingine chochote! Yote aliyoyafanya yalikuwa ni kumdanganya babu Ayoub, fikra zake zilikuwa kutoroka yeye na mchumba wake pamoja na wadogo zake! Ili hilo liwezekane ilikuwa ni lazima ajenge uhusiano wa karibu zaidi na babu Ayoub ili kumpumbaza na baada ya hapo ndio mipango ya kutoroka ingeendelea, alishuhudia babu Ayoub akimbeba Danny na kwenda kumfungia kwenye kibanda kidogo kilichokuwa nyuma ya nyumba, kilikuwa kidogo mno kiasi cha kushindwa hata kujigeuza lakini humo ndimo alimotakiwa kuishi siku zote akiwa kisiwani.
Muda mfupi baadaye mzee Kiwembe aliwasili akiwa na nyavu zake mkononi na kumtaka babu Ayoub waondoke kuelekea kazini, aliondoka akifuatana na Nancy hadi ndani ya kibanda chao, bado Nancy aliendelea kumpa shukrani kwa wema aliuofanya, yote hiyo ikiwa ni kumpumbaza mzee huyo! Hakuwa na kitu cha kuchukua ndani zaidi ya nyavu na kutoka hadi nje ambako aliungana na mwenzake na wakashuka kuelekea mwaloni ambako walipanda mitumbwi yao na kuelekea ziwani kwa shughuli zao za uvuvi, nyuma Nancy hakuwa na kitu kingine zaidi ya kwenda kwenye kibanda akiwa na wadogo zake na kuanza kuongea na Danny! Alimpa matumaini makubwa ya kuondoka kisiwani wakiwa salama na alimwomba awe mvumilivu, alimtayarishia chakula asubuhi hiyo hiyo akala lakini akiwa ndani ya kibanda! Nancy aliogopa kumtoa ingawa alikuwa na uwezo huo, hofu yake kubwa ilikuwa kurudi kwa babu Ayoub ghafla..
“Tutaondokaje?
“Hiyo itakuwa ni kazi yangu! Lazima tuondoke kisiwani, niachie mimi Danny! Haiwezi kuwa ghafla lazima nimlainishe kwanza huyu mzee!”
“Nitavumilia Nancy! Kumbuka mimi na wewe tuna ahadi ya kufunga ndoa na tumepoteza mambo mengi sana maishani mwetu ikiwemo elimu sababu ya uhusiano wetu, nakusihi tusiache jambo hili lipotee hivi hivi!”
“Halitapotea Danny! Wewe vumilia tu, kila siku natafuta mbinu ya kutuondoa hapa kisiwani!”
Ilikuwa siku moja mwisho ikatimia wiki, hatimaye mbili mwisho mwezi! Danny akiwa ndani ya kibanda, kitu pekee ambacho Nancy alikuwa amefanikiwa kukifahamu mpaka wakati huo ni mahali mtumbwi wa wazee hao wawili ulipofichwa, hilo peke yake lilimpa matumaini ya kuondoka kisiwani! Alipomwambia Danny juu ya jambo hilo pia alimpongeza, kilichobaki kikawa ni lini waondoke tena bila kumwacha mtu kisiwani zaidi ya mzee Kiwembe na babu Ayoub.
“Hilo linahitaji uvumilivu kidogo!”
“Lakini angalau umekwishajua nini cha kufanya!”
“Ndio!”
“Babu Ayoub anasemaje kuhusu mimi?”
“ ila siku anasema utakaa ndani ya kibanda hiki mpaka mwisho wa maisha yako, anadai uko katika kifungo cha maisha!”
“Wewe huwa unamwambiaje?”
“Sina cha kumwambia zaidi ya kumkubalia lakini nikiwa na moja kichwani!”
“Jitahidi Nancy, jambo hili lifanyike mapema nateseka sana kuishi katika kibanda kidogo kama hiki!”
“Naelewa mpenzi lakini hawa wazee si wakuwaendea haraka, inabidi tuwe makini sana katika zoezi tunalota
 
SEHEMU YA 36
“Naelewa mpenzi lakini hawa wazee si wakuwaendea haraka, inabidi tuwe makini sana katika zoezi tunalotaka kulifanya, vumilia tu Danny, hatutamaliza wiki mbili hapa lazima tutakuwa tumeshaondoka kwa kutumia mtumbwi wao, kinachonisumbua ni namna gani tutaweza kuondoka wote!”
“Kwanini?”
“Nilikuwa nafikiri kuondoka usiku wakati babu Ayoub akiwa usingizini lakini nashindwa kuelewa tutawachukuaje Catherine na David ambao wanalala na mzee Kiwembe!”
“Hapo kweli ni kazi ngumu!”
“Sitaki kuwaacha Catherine na David hapa kisiwani, hiyo ndiyo kazi iliyonileta na wewe ulikuja kunifuata mimi!”
“Sasa tutafanyaje?” Danny aliuliza.
“Subiri nitafikiria!”
Siku mbili baadaye katikati ya usiku Danny alishtukia mlango wa kibanda alichofungiwa ndani mwake ukifunguliwa, ni kitendo hicho ndicho kilimuamsha usingizini, alishindwa kuelewa ni nani alikuwa akifungua mlango kwa harakaharaka aliamini ni babu Ayoub amekuja kumuua bila Nancy kuwepo lakini sauti iliyofuata ikinong’ona haikuwa ya babu Ayoub, alikuwa ni Nancy.
“Danny! Danny!” Iliita.
“Naam!”
“Toka twende!”
“Wapi?”
“Tutoroke!”
Danny alichomoka haraka kutoka kibandani na kusimama wima, swali lake la kwanza lilikuwa watoto, alitaka kujua ni wapi walikokuwa Catherine na David! Nancy hakutaka kumjibu, alimshika mkono na kuanza kukimbia naye wakipita katika ya vichaka kuelekea ufukweni ambako hisia za Danny zilimfanya afikiri Catherine na David walikuwa wakiwasubiri, ufukweni hapakuwa na watoto lakini mtumbwi ulikuwa tayari.
“Panda!”
“Watoto?”
“Wewe panda!” Nancy alisisitiza na Danny akapanda bila kuuliza maswali zaidi, Nancy alianza kupiga kasia na mtumbwi ukaanza kusogea mbele taratibu, hali ya ziwa ilikuwa shwari kabisa na kulikuwa na dalili za mvua! Ingawa walielewa uchawi na miujiza ya babu Ayoub na mzee Kiwembe hawakuogopa walikuwa tayari kupoteza maisha yao wakijaribu kujiokoa kuliko kuendelea kuteseka, mpaka wakati huo Danny hakuelewa ni wapi walikokuwa Catherine na David na hakuuliza tena! Kilometa kama kumi katikati ya maji, kukiwa na giza kila upande Nancy alichoka na kumkabidhi Danny kasia, akaiendeleza kazi na kusonga mbele kilometa ishirini zaidi! Alipochoka naye alimkabidhi Nancy kasia wakaendelea kubadilishana kwa mtindo huo mpaka kufika mbali kabisa mahali walikoelewa si babu Ayoub wala mzee Kiwembe ambaye angeweza kuwapata tena.
******
Saa kumi na nusu ya usiku, babu Ayoub alizinduka usingizini kitu cha kwanza ilikuwa ni kupapasa upande wake wa kushoto ambako mke wake siku zote alilala! Hakukuta kitu akafikiri labda alikuwa amekwenda kujisaidia kwa sababu mlango ulikuwa wazi lakini aliposubiri kwa saa nzima alishtuka, ikabidi atoke nje harakaharaka na kuanza kuangaza huku na kule lakini hakumwona Nancy mahali popote. Kilichomwijia kichwani harakaharaka ni Nancy alikuwa ametoroka pamoja na Danny, ili kuhakikisha jambo hilo alizunguka nyuma kwenye kibanda na kukuta kibanda kiko wazi na Danny hayupo ndani yake.
Alikimbia moja kwa moja hadi kibandani kwa mzee Kiwembe akagonga mlango na kufunguliwa kisha kumkalisha chini na kumweleza kila kitu kilichotokea usiku huo, mzee Kiwembe hakuamini kwa sababu Catherine na David walikuwepo, aliamini Nancy asingeweza kuondoka kisiwani na kuwaacha wadogo zake aliowapenda kiasi hicho.
“Sasa wako wapi?”
“Twende ufukweni tukaangalie!”
“Sawa!”
Waliondoka mbio kuelekea ufukweni mwa ziwa kuangalia kama Nancy na Danny walikuwepo, walishangaa kukuta mtumbwi wao haupo jambo lililoashiria kuwa kweli walikuwa wametoroka! Roho ilimuua babu Ayoub, alisonya na kuapa wasingefika mbali! Wote wawili waliondoka mbio kurudi vibandani mwao ambako walichukua zana zao zote za uchawi ili wavuruge hali ya hewa ziwani, Danny na Nancy wazame na baadaye watume mashetani yao kwenda kuwakamata na kuwarudisha kisiwani.
“Wakirudi hapa hakuna kitu kingine cha kufanya zaidi ya kuwachinja, wanacheza na mimi ngedere hawa!”
Moto uliwashwa, dawa nyeusi kutoka kwenye kibuyu zikamwagwa ndani yake na moshi ukaanza kupanda kwenda juu na kimbunga kikubwa kikajitokeza, wote wakasimama na kuanza kusema maneno kwa kabila yao wakiamuru kibunga hicho kiende kikawalete Nancy na Danny!
******
Pamoja na kuwa wamekwenda umbali mrefu majini kwa kupiga kasia na kuwa na uhakika walikuwa wamefanikiwa kuwatoroka babu Ayoub na mzee Kiwembe, ghafla hali ya ziwa lililokuwa limetulia ilibadilika! Upepo mkali ulijitokeza ukivuma kutoka Kaskazini kwenda Kusini na kusababisha mawimbi makubwa pamoja na dhoruba isiyo na maelezo, mara moja Nancy alielewa kilichokuwa kikiendelea, babu Ayoub na mzee Kiwembe walikuwa wamefanya mambo yao! Matumaini ya kunusurika yalianza kupotea, picha ya ndoa yao iliyokuwa imeanza kujijenga kichwani ilianza kufutika, hali ilizidi kuwa mbaya na wote wawili waliamini kifo kilikuwa haki yao! Walikumbatiana wakiwa hawana matumaini kabisa na kulia machozi kwa pamoja.
“Tufanye nini darling?” Danny aliuliza.
“Kwa kweli sielewi!”
“Unafikiri huu ni upepo wa kawaida?”
“Hapana!”
“Sasa ni nini?”
“Hii ni kama ile siku ya ulipozama wewe na niliyozama mimi, hawa ni wale wale wazee na uchawi wao!”
“Ndio nakuuliza tufanyeje?”
“Kwa kweli sielewi! Kuna uwezekano tukajikuta tuko huko huko kisiwani!”
Kwa muda wa saa mbili hali iliendelea kuchafuka, mawimbi yalikuja makubwa kama nyumba na kuujaza mtumbwi wao maji! Hali ilikuwa mbaya, katika maisha yao hawakuwahi kukumbana na dhoruba kali kiasi hicho, machozi waliyolia yote yalikwenda na maji! Haukupita muda mrefu mtumbwi wao ukawa umepinduka na kujifunika chini juu, wote wakamwagwa majini! Danny alifanikiwa kujivuta na kupanda juu ya mtumbwi na kuketi akishuhudia Nancy akihangaika majini, hakuwa na uwezo hata mdogo wa kuogelea! Roho ilimuuma kwani hakuwa tayari kushuhudia kifo cha Nancy, ingawa yeye pia hakuwa na uwezo wa kuogelea, alichofanya ni kujitupa tena majini na kukamata gauni la Nancy kwa mkono wa kulia huku mkono wa kushoto ukiwa umeushika mtumbwi na kumfanya aelee.
Alimvuta Nancy na kumsogeza karibu yake na kuzuia asizame tena kwenda chini huku akiendelea kunywa maji, Danny alifurahi kuona amefanikiwa kulifanya jambo hilo aliloamini lilizuia kifo cha mwanamke aliyempenda kuliko wote, kwa nguvu zake zote alijivuta na kufanikiwa kupanda tena juu ya mtumbwi na kulala juu yake huku mkono wake wa kulia ukiwa umeshikilia gauni la Nancy aliyekuwa majini, kichwa peke yake ndio kikionekana juu ya maji! Hakuwa na uwezo wa kuongea chochote, alikuwa kimya kiasi cha kumfanya Danny ahisi labda alishakufa tayari na moyo wake kuuma kuliko kawaida, hakuwa tayari kabisa kukubaliana na ukweli huo kwani alikuwa amehangaika sana na mwanamke huyo, fikra zake zilipomrudisha chuo kikuu walikosoma pamoja, matatizo waliyoyapata katika mapenzi yao na mahali walipokuwa wakati huo Danny alijikuta akipita kelele na kukataa kabisa kuwa Nancy alikuwa bado hajafa..
“Nancy!Nancy!Nancy!” Alimwita mara tatu mfululizo bila kuitikiwa! Jambo hilo lilimfanya azidi kuamini mchumba wake hakuwa hai pamoja na kuukata ukweli huo, maji aliyokuwa amemeza yalikuwa yamemdhuru, pengine yalijaa kwenye mapafu na kumfanya ashindwe kupumua, Danny alitamani wawe nchi kavu ili aweze kumkamua maji yatoke tumboni lakini hapakuwa na uwezekano huo, pamoja na hali hiyo bado hakukata tamaa, hakuwa tayari kumwachia kwa mkono wake wa kulia uliendelea kushikilia gauni la Nancy akiwa amelala juu ya mtumbwi.
Mara kadhaa alijaribu kumvuta ili ampandishe juu ya mtumbwi lakini haikuwezekana, Nancy alikuwa mzito kupita kiasi na hali ya hewa ilikuwa ikiendelea kuwa mbaya kadri saa zilivyozidi kupita, mtumbwi ulikosa muelekeo na kuanza kupelekwa na maji kufuata mkondo na upepo! Hakuelewa tena walikuwa wakielekea wapi lakini bado hakumwachia Nancy aliyekuwa kimya kabisa! Hatimaye ikawa jioni na usiku ukaingia haliya hewa ilikuwa bado ni mbaya, majira kama ya saa saba na nusu ya usiku alimsikia Nancy akijitingisha na alipomwita aliitika, Danny akafurahi kupita kiasi, lilionekana kuwa jambo ambalo hakulitegemea kabisa.
“Tuko wapi?”
“Majini!”
“Nini kimetokea?”
“Tumezama!”
Jibu hilo la Danny lilimfanya Nancy akumbuke kila kitu na kuelewa kumbe alipoteza fahamu muda mfupi baada ya mtumbwi wao kuzama, kumbukumbu zilizidi kumiminika hasa alipouona mtumbwi wao na Danny akiwa juu yake na aliamini kila kitu kilichokuwa kikitokea ilikuwa kazi ya wazee wawili hatari, mzee Kiwembe na babu Ayoub! Lakini kwa sababu walikuwa hai mpaka wakati huo aliamini wasingekufa na alimwomba Danny aendelee kumshikilia kwani mwili wake haukuwa na nguvu, alikuwa amelegea na alikuwa na na ganzi kali mwilini iliyosababishwa na ubaridi wa maji, hicho ndicho kilifanya ashindwe hata kupanda juu ya mtumbwi pamoja na msaada wote aliopewa na Danny.
Ikawa asubuhi, ikawa jioni siku ya pili! Na ikawa tena asubuhi, ikawa jioni siku ya tatu na hatimaye siku ya nne na ya tano bado wakielea majini, Danny akibadilisha mikono kutoka kushoto kwenda kulia kumshikilia Nancy aliyekuwa bado yupo ndani ya maji, kama ilivyokuwa mwanzo alikuwa haongei kitu tena na si yeye tu bali pia Danny hakuwa na kauli! Baridi kali iliyokuwepo ziwani, dhoruba iliyosababishwa na mvurugiko wa ziwa pamoja na njaa ya siku tano bila kula chakula iliwamaliza nguvu kabisa, walikuwa ni kama maiti, ingawa walihema hawakuwa na matumaini ya kupona! Walijihesabu ni wafu, matumaini ya kunusurika yalishafutika..
“N...an....cy!” Aliita Danny akitetemeka.
“B..e..e!” Nancy naye aliitika meno yake yakigongana, huku kitu kama moshi kikimtoka mdomoni sababu ya baridi, nguzo yake wakati huo ilikuwa Danny kama mkono wake ungemwachia basi angezama majini na kufa mara moja!
“Na....kup..enda!”
“Nak...pe.....nda..pia!”
“Na ni...natamani tuo....kolewe ili tuka....funge nd..oa ye..tu!” Aliendelea kuongea kwa taabu Nancy.
“Ha..ta mi...mi pia nat...am...ani!”
“Lakini mikono yangu ime...choka kukushikilia Nancy! Nashi.......ndwa kue.....ndelea, nalazi....mika kuku....achia! Sio kwa.....mba siku....pendi lakini kwa sa....babu siwezi tena mpenzi, misuli yote inaniuma na mikono imekufa ganzi! Naomba usinielewe vibaya, tangulia na mimi nakufuata, tutafunga ndoa yetu pep....oni ka...ma tukifa...nikiwa ku...fika huko! Kumbuka kutubu dhambi zako zote, mimi na we...we tuli....ua watu wengi sana!” Aliongea Danny mkono wake ukilegea na kuanza kumwachia Nancy.
“Danny! Danny! Tafa..dhali usini...achie! Jika...ze kidogo, sita...ki kufa!” Aliongea akilia Nancy na machozi yakimtiririka na kujichanganya na maji ya ziwa.
Pamoja na kulia akiomba asiachiwe haikuwezekana tena, vidole vya Danny vilimwachia taratibu, Nancy akaanza kuzama macho ya Danny yakishuhudia hatimaye kichwa kikamezwa na maji.
********
Kikao kilikuwa kikiendelea ndani ya ofisi ya Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kigoma, karibu uongozi wote wa jeshi la polisi nchini ulikuwa ndani ya ofisi hiyo, mpaka Inspekta Jenerali aliyewasili asubuhi ya siku hiyo kwa helkopta kutokea Dar Es Salaam! Suala la Kisiwa cha Galu na watoto waliodaiwa kutekwa na kufichwa pamoja na idadi ya maaskari waliopoteza maisha lilishakuwa la Kitaifa, ilikuwa ni aibu kwa jeshi kushindwa kuingia katika kisiwa hicho na kuwakomboa watoto waliokuwepo.
“Mnafikiri tufanye nini?” Inspekta Jenerali aliuliza akitaka kufahamu kama kulikuwa na mawazo yoyote tofauti baada ya operesheni hiyo kusitishwa kwa kipindi.
“Labda twende Kasulu, yupo mzee mmoja anaitwa Kazaroho!” Kamanda wa Polisi alisema.
“Wa nini?”
“Ni Mganga maarufu sana wa jadi!”
“Atusaidie nini?” Inspekta Jenerali aliuliza
“Ninachoamini mimi ni kwamba kisiwa cha Galu kina mambo ya kishirikina ndio maana vijana wetu wanapoteza maisha, mzee ninayemwongelea anaweza kutupa ndumba angalau za kuzuia upepo ili tuweze kufika kisiwani, vinginevyo tutaendelea kufa Kamanda!”
“Yaani wewe katika Karne ya ishirini na moja unataka kuliingiza jeshi la polisi katika mambo ya uchawi na ushirikina? Hufai! Mara ishirini ungeniambia tutafute mchungaji twende naye akafanye maombi ili nguvu za giza zipambane na nguvu za Mungu hapo ningekuelewa” Inspekta Jenerali alifoka na Kamanda wa polisi alibaki kimya kabisa.
Watu wote waliokuwemo katika kikao hicho walitoa mawazo yao lakini wazo lililoonekana kukubalika zaidi ni la Mkuu wa Kituo cha Kati mjini Kigoma Inspekta Ibrahim Katole, yeye alishauri helkopta aliyokwenda nayo Inspekta Jenerali ndiyo itumike kuwasafirisha askari mpaka kisiwani, kila mtu alipiga makofi kulishangilia wazo hilo hata Inspekta Jenerali alikubali akiamini kama njia ya maji ilikuwa haiwezekani basi njia ya anga ndiyo iliyotakiwa kutumika.
“Labda hao wazee na hali ya hewa wanaweza kuichafua halafu helkopta yetu ikaanguka?”
“Sidhani!”
“Potelea mbali lolote litakalojitokeza niko tayari! Suala hili limenifanya nionekane siwezi kazi, Kamanda andaa vijana ili waondoke sasa hivi kwenda kisiwani Galu, wape silaha za kutosha! Nataka watakaporudi hapa wawe na hao wazee wawili pamoja na hao watoto!”
“Sawa afande!” Aliongea Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kigoma akipiga saluti kuonyesha heshima kwa mkubwa wake wa kazi na huo ndio ukawa mwisho wa kikao.
Kilichofuata baada ya hapo yalikuwa ni maandalizi ya safari ya kwenda Galu,maaskari kumi na tano wenye uwezo wa kupambana walipangwa kwa ajili ya operesheni hiyo na kupewa zana zote za kazi, majira ya saa saba ya mchana helkopta iliondoka kuelekea kisiwani Galu, maaskari wote wakiwa wamapania kupambana kwa nguvu zao zote hata kama ingebidi wapoteze maisha lakini wawaokoe watoto waliokuwa kisiwani! Wasiwasi wao ulikuwa mmoja tu, NGUVU ZA GIZA! Hawakuwa na uhakika kama wazee wachawi waliokuwa kisiwani wasingeweza kuitungua helkopta yao kwa makombora ya kichawi na kuwateketeza.
“Tutafika?” Waliulizana.
“Lolote litakalokuwepo mbele ni halali yetu ili mradi tuliamua kwa hiari yetu kuingia jeshini! Au kuna mtu alilazimishwa?”
“Hapana!”
“Basi kazi ni moja tu!” Mkuu wa msafara huo Inspekta Ibrahim Katole aliwaambia vijana wake, pamoja na maneno hayo hakuna aliyekuwa na uhakika wa kufika kisiwani salama, sifa za wazee wawili hatari walioishi katika kisiwa hicho ziliwatisha..
*****
Helkopta ya jeshi la polisi ilikuwa ikipita juu ya maji katikati ya ziwa Tanganyika kuelekea kisiwani Galu, ndani yake kulikuwa na maaskari waliokuwa na hamu kubwa ya kufika katika kisiwa hicho ili kukabiliana na wazee wawili wachawi, tayari walikuwa wakiona kisiwa hicho kwa mbali na walitegemea katika muda wa dakika tano wangekuwa wakitua kisiwani humo! Ghafla mmoja kati ya maaskari alipiga kelele akiwaita maaskari wenzake ambao wote macho yao yaliangalia mbele.
“Vipi afande?”
“Jamani hebu angalieni pale!”
“Kuna nini?”
“Kuna watu wamezama na mtumbwi!”
“Yaani wewe umewaona kwa macho yako?”
“Hapana nimetumia hiki kiona mbali!”
“Hebu!”Mkuu wa kikosi hicho aliomba kiona mbali na kuanza kuangalia chini majini, kweli aliwaona watu wawili mmoja akiwa juu ya mtumbwi na mwingine akiwa amezama kichwa peke yake kikiwa juu ya maji!
“Umewaona?”
“Kweli kabisa!”
“Sasa tufanye nini? Tunyooshe Galu au tuwaokoe kwanza?”
Wawili kati yao waliamua safari iendelee ili watimize kazi waliyotumwa na jeshi lakini wengi walisema wafanye kila kilichowezekana kuokoa roho za watu hao, kauli ya wengi wape ilipita na helkopta ikaanza kushushwa taratibu kuelekea majini eneo ambalo watu hao walionekana, huku kamba zikitayarishwa kwa ajili ya mmoja wa maaskari kushuka hadi majini na kutoa msaada! Lakini kabla hawajafikachini karibu zaidi askari aliyekuwa na kiona mbali alipiga kelele kuwaeleza wenzake kuwa tayari aliyekuwa majini amezama kabisa!
Kamba ilishushwa haraka na mmoja wa maaskari akapita katika moja ya milango na kushuka moja kwa moja kwa kutumia kamba hadi majini, wakati anafika ndio Nancy alikuwa akiibuka kwa mara ya kwanza huku akinywa maji mengi, askari alimdaka na kumfunga kamba mkononi kisha kuwaonyesha ishara wenzake na mashine maalumu ya kuvuta kamba iliyokuwemo ndani ya helkopta ilianza kufanya kazi yake na wote wawili wakavutwa hadi juu na kusadiiwa kuingia ndani.
Kamba nyingine ilitupwa tena majini ikiwa imemfunga askari mwingine ambaye alikwenda moja kwa moja hadi chini karibu na mtumbwi ambao Danny alilala juu yake, aliipitisha kamba shingoni na kumfunga kifuani kisha kuonyesha ishara kama alivyofanya mwenzake na hapohapo akaanza kuvutwa kuelekea juu! Ilikuwa operesheni ya dakika zisizozidi tano, wote wawili wakawa wameokolewa!
“Mh! Huyu msichana nimemkumbuka! Ndiye aliyeondoka na maaskari wetu mara ya kwanza kabisa, na tukaamini kwamba amekufa! Nashangaa sana kumwona yuko hai!”Alisema mmoja wa maaskari wakati wakijitahidi kumkamua Nancy maji aliyokuwa ameyameza katika wakati wa kuzama.
“Aisee ni kweli kabisa!”
“Lakini taarifa tulizozipata ni kwamba alikufa pamoja na maaskari wetu?”
“Hivyo ndivyo ilivyosemekana!”
“Na huyu kijana?”
“Huyu simkumbuki!”
“Au ni mmoja wa watekaji?” Waliulizana na Danny alisikia kila kitu kilichoongelewa.
“Hap....ana jamani mimi sio mte.....kaji na mimi pia nilit....ekwa na wazee wa.....wili wana....oitwa Kiwembe na Ayoub!” Aliongea kwa taabu Danny, mashavu yake yalikuwa bado yameng’ang’aniana kwa sababu ya baridi..
“Wewe ni nani?”
“Naitwa Danny! Mchu.....mba wa.....ke na Na...ncy! Nawa...shukuru sana kwa kut....uokoa, nani amewa....eleza kwa...mba tuko hapa?”
“Hatujaelezwa na mtu ila tulikuwa safarini kwenda kisiwani Galu kuwakomboa watoto wawili waliotekwa muda mrefu na wazee uliowataja!” Mmoja wa maaskari alisema, hapo Danny aliwaeleza kila kitu kilichotokea ingawa kwa taabu, Nancy akiwa kimya akiendelea kukamuliwa maji tumboni., ilikuwa ni bahati kubwa sana kwao kuokolewa kwani walishakata tamaa kabisa ya maisha.
Uamuzi uliochukuliwa ni kuwarejesha Nancy na Danny Kigoma haraka iwezekanavyo kabla safari ya kwenda Galu haijafanyika, hali zao zilikuwa mbaya na ziliwatisha maaskari wote waliokuwemo ndani ya helkopta hiyo ya polisi, waliwasiliana haraka na Kamanda wa Polisi wa Mkoa kumtaarifu juu ya kilichokuwa kikiendelea, tayari ilishakata kona kuelekea Kigoma ambako walifika dakika ishirini baadaye na kutua na Danny na Nancy wakashushwa na kupakiwa katika magari ya wagonjwa yaliyokuwa yameandaliwa tayari na kuondoka muda huo huo kuelekea hospitali ya Mkoa wa Kigoma, Mlugwanza.
Askari nao hawakutaka kupoteza muda bado walikuwa na safari ya kwenda kisiwani Galu, ilikuwa ni lazima siku hiyo wafike na kuwatia nguvuni mzee Kiwembe na babu Ayoub waliotisha kwa uchawi! Hiyo haikuwa kazi pekee bali pia kuwaokoa watoto David na Catherine ambao tayari walikuwa na uhakika kwa maelezo waliyopewa na Danny kwamba kuwa walikuwepo kisiwani! Dakika thelathini baadaye helkopta yao ilitua Kaskazini mwa kisiwa cha Galu kilometa ishirini kutoka mahali makao ya wazee hao wawili yalipokuwa.
“Twendeni!” Kiongozi wa maaskari aliamuru.
“Sawa afande!”
“Tuko tayari afande!” Maaskari waliitikia mfululizo na wote walianza kutembea silaha zikiwa mikononi mwao kuelekea sehemu walikoviona vibanda ambavyo waliamini vilikuwa vya watu waliokuwa wakiwatafuta, walikuwa na uhakika hakuna aliyegundua kwamba walikuwa wametua kisiwani hapo.
Nusu saa baadaye wakipita chini ya miti walitokeza eneo hilo, kitu cha kwanza walichokiona ni watoto wawili wakiwa wamekaa nje wakiota jua, afya zao zilikuwa mbaya na waliamini ni watoto hao waliokuwa wamewafuata! Hawakuwaona wazee waliokuwa wakiwatafuta mahali popote, pamoja na maaskari wengine kudai wawachukue watoto kiongozi wa kikosi alikataa na kusema inabidi wavumilie mpaka watakapotokeza ili wawakamate na kuondoka nao!
“Lakini afande tungechukua kwanza watoto!”
“Hapana!”
“Basi tukaangalie inawezakana wapo ndani!”
“Tulieni kwanza kama wapo ndani tutawaona wakijitokeza!”
Maaskari wote walitii amri ya kiongozi wao na kubana katika nyasi, eneo ambalo waliona kila kitu kilichoendelea katika vibanda vya wazee hao, watoto waliendelea kukaa nje na muda mfupi baadaye mzee Kiwembe na babu Ayoub walifika wakikimbia kutoka eneo la chini na kuingia ndani ya vibanda vyao na walipotoka waliowanyakua watoto na kuanza kukimbia kuelekea walikotokea! Ni hapo ndipo maaskari walipojitokeza na kuwaweka chini ya ulinzi.
“Mpo chini ya ulinzi hamtakiwi kufanya lolote tafadhali wekeni hao watoto chini!”
Mzee Kiwembe na babu Ayoub waliwaweka David na Catherine chini na kunyanyua mikono yao juu, hawakuwa na ujanja tena! Uchawi wao haukuwa na uwezo nchi kavu zaidi ya majini, maaskari wawili wenye pingu walitembea kwenda mbele na kuwafunga mikono yao pamoja na kuwabeba David na Catherine, safari ya kuelekea mahali ilipokuwa helkopta ilianza, maaskari walishangaa jinsi ambavyo kazi ya kuwakamata wazee hao ilivyokuwa rahisi tofauti kabisa na walivyofikiria.
“Ah! kumbe tulikuwa tunaogopa bure!” Mmoja wa maaskari alisema wakati helkopta inaiacha ardhi ya kisiwa cha Galu.
“Usiseme hivyo! Hawa wazee wanatisha majini, wenzetu wengi sana wamepoteza maisha! Shukuru Mungu tumetumia helkopta hata sisi tusingepona kama tu tungejaribu kutumia boti!”
Dakika tano baadaye wakiwa angani, lilijitokeza wingu zito tena kwa ghafla ambalo lililowashangaza wote na kusababisha giza lililomfanya rubani ashindwe kuona mbele, wote walianza kuingiwa na hofu kuwa huenda nguvu za giza za wazee hao hatari zilikuwa zimeanza kufanya kazi.
*****
Taarifa za kuokolewa kwa Danny na Nancy zilitangazwa katika taarifa ya habari ya siku hiyo mchana ambayo pia mzee Katobe na mkewe waliisikia, hawakuamini! Walifikiri labda masikio yao yamesikia kitu kingine hasa mtangazaji aliposema kwamba, jeshi la polisi lilikuwa limekwenda kwa helkopta kisiwani Galu kuwakomboa watoto wengine waliobaki na kuwatia nguvuni wazee waliowateka ili wafikishwe mbele ya sheria.
Hawakutaka kupoteza muda walichofanya ni kwenda benki kuchukua fedha na kusafiri hadi Dar Es Salaam ambako walipanda ndege iliyowasafirisha moja kwa moja hadi Kigoma, safari nzima mama yake Nancy alikuwa akilia na alishindwa kuelewa machozi yalimtoka kwa sababu ya furaha au huzuni alitamani kuwaona watoto wake alioamini walikuwa wafu tayari! Mpaka anafika hospitali ya Murugwanza kutoka uwanja wa ndege wa Kigoma alikuwa bado hajaamini kama kweli waliookolewa walikuwa ni Nancy na Danny, alihisi labda ni watu wengine lakini walipofika wodini na kuwaona, machozi zaidi yalimtoka, hayakuwa machozi ya huzuni isipokuwa furaha! Aliinama na kumbusu Danny kisha kwenda kwa Nancy na kumbusu pia, vivyo hivyo ndivyo alivyofanya mzee Katobe..
“Poleni wanangu!”
“Ahsante mama!” Alijibu Danny.
Nancy hakuwa na uwezo wa kuongea, yaliyokuwa yakitokea kwake yalikuwa ni kama ndoto, hakuamini kama kweli alikuwa amewaona wazazi wake baada ya mateso ya muda mrefu! Machozi yalikuwa yakimbubujika mfululizo, kwake pia yalikuwa ni machozi ya furaha si huzuni, lakini furaha yake ilikuwa haijakamilika mpaka David na Catherine pia waokolewe.
“Taarifa ya habari imesema kwamba polisi kwa kutumia helkopta iliyowaokoa ninyi wamerudi tena kisiwani kuwafuatilia Catherine na David ikiwa ni pamoja na kuwatia nguvuni wazee waliowateka!”
“Baba wazee hao ni wakatili na ni wachawi sina uhakika kama kweli watafanikiwa kukamatwa!”
“Wacha tusubiri matokeo! Namshukuru Mungu ameokoa maisha yenu na kama alivyowaokoa ninyi ndivyo atakavyookoa maisha ya wadogo zenu! Hivi sasa tuendeleze maombi, kila siku tulikuwa tukiwaombea na hatutachoka mpaka watoto wetu wengine wameokolewa!” Aliongea mzee Katobe akiwa amemshika Nancy kichwani hakika ilikuwa ni siku ya furaha lakini isingetimia mpaka Catherine na David nao waokolewe.

Je nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 37
Baada ya kuteseka ziwani Nancy na Danny wanaokolewa na kurudishwa Kigoma ambako wanalazwa hospitali na baadaye kukutana na wazazi wao! Ni furaha kubwa kwa kila mmoja wao lakini furaha hiyo haijatimia mpaka watoto wengine Catherine na David walioko kisiwani Galu wapatikane.
Polisi waliokwenda kisiwani wanafanikiwa kuwakamata mzee Kiwembe na babu Ayoub na kuwaokoa watoto Catherine na David kisha kuondoka nao kwa helkopta ya jeshi waliyokwenda nayo, maaskari wote wanasema kazi imekuwa rahisi kuliko walivyotegemea lakini ghafla wakiwa angani mambo yanaanza kuwaharibikia baada ya wingu zito kutokea angani na kusababisha giza nene kiasi cha rubani kushindwa kuona alikokuwa akielekea! Hali hii inatisha kila mmoja wao anahisi ni nguvu za giza za wazee wawili hatari waliowakamata.
Je, nini kinaendelea? Fuatilia.............
Ilikuwa ni furaha kubwa kwa mzee Katobe na mke wake hatimaye kukutana tena na Nancy pamoja na mchumba wake Danny, watu waliokuwa wamepoteza matumaini ya kuwaona tena! Wakiamini walikufa kisiwani Galu, lakini kama walivyosema wazee hao furaha yao ilikuwa haijakamilika mpaka Catherine na David, watoto wao wengine wapatikane! Ingawa hawakuwa watoto wa kuwazaa yeye, mzee Katobe aliwapenda sana watoto hao, hakuwabagua kama ilivyokuwa kwa Nancy ndivyo ilivyokuwa kwa David na Catherine.
“Mama!” Nancy alimwita mama yake.
“Bee mwanangu!”
“Kama nikipona sitakwenda Bagamoyo, bado nitakuwa na sababu ya kurudi tena kisiwani Galu kuwafuatilia Catherine na David, sijakata tamaa!”
“Sawa lakini polisi ndio wanafuatilia kwa hivi sasa, kama nilivyokuambia Helkopta ipo kisiwani Galu, ni vyema ukawa mvumilivu!”
“Siwaamini polisi kabisa! Walishindwa kutusaidia mwanzo watawezaje leo?”
“Sawa, inawezeka walikuvunja moyo lakini wape nafasi nyingine!”
“Haiwezekani!”
Nancy hakuwa na imani kabisa na jeshi la Polisi na hiyo ilitokana na historia ya nyuma tangu walipotekwa wazazi wake pamoja na Danny na yeye kwenda kutoa taarifa polisi lakini bado hawakumsaidia chochote mpaka yeye mwenyewe kwa mikono yake akaamua kwenda mstari wa mbele na kupambana na mzee Katapila pamoja na kundi lake la majambazi hatimaye kumwokoa Danny na baadaye kuwaokoa wazazi wake shambani Tindiga walikokuwa wamefichwa, jambo hilo lilimfanya asiwe na imani na jeshi la polisi kabisa ndio maana aliongelea suala la yeye mwenyewe kwenda kisiwani Galu kuwakomboa wadogo zake, hawakuwa na imani kabisa kama askari waliodaiwa kwenda kisiwani kwa helkopta wangeweza kurudi Kigoma wakiwa na Catherine na David.
“Nancy!” Danny alimwita mchumba wake.
“Bee!”
“Sikiliza maneno ya mama kwanza, naelewa una uwezo wa kurudi hadi kisiwani Galu na kuwakomboa wadogo zetu na uelewe wazi ukienda wewe ujue wazi hata mimi nitakufuata, siwezi kukuacha uende peke yako lakini nakushauri tutulie kidogo tuendelea kuwaombea Catherine na David mpaka polisi watakaporejea kutoka Galu!”
“Sawa lakini...!” Alikubali Nancy ingawa kwa shingo upande.
Siku nzima walishinda vizuri huku wakiangalia hali za wagonjwa wao, Nancy alikuwa akiendelea vizuri zaidi kadri saa zilivyopita, alishaanza hata kutabasamu! Dripu aina ya Glucose alizowekewa katika mishipa yake zilimfanya apate nguvu harakaharaka, hakuwa na jeraha mahali popote mwilini mwake! Hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa Danny, yeye tayari alikuwa na uwezo wa kusimama, kutembea na kuzungukazunguka nje ya wodi! Kulikuwa na matumaini makubwa sana ya kupona na kurejea katika maisha yao ya kawaida, mapambano yalikuwa yamekaribia kufika mwisho, kitu pekee kilichokuwa bado kinasumbua akili zao ni wadogo zao lakini kama wao pia wangekuwa huru basi kitu pekee ambacho kingekuwa kimebaki mbele yao ni ndoa na baadaye kurudi tena chuo kikuu kuendelea na masomo mahali walipokomea, hata kama wangetakiwa kuanza mwaka wa kwanza walikuwa tayari.
Kila alipoyakumbuka maisha aliyopitia Danny, aliogopa! Alitishwa na historia yake, alikuwa ametoka mbali kimaisha mpaka kufika hapo alipokuwa, lilikuwa ni jambo ambalo hakuna mtu angeamini kama angemsimulia kuwa alihangaika kiasi hicho na mpaka kujikuta akiua watu kwa sababu ya msichana aliyempenda! Aliamini wengi wangeiona ni historia tu ama hadithi ya kubuni ambazo watu huziandika katika magazeti na vitabu.
“Historia ya maisha yangu inatosha kabisa kuandika kitabu, nikimsimulia mtu kama Chriss Magori anaweza kuandika hadithi kwenye magazeti yake ya Kasheshe na Komesha!”Aliwaza Danny.
Ni kweli kabisa, Danny alikuwa amepitia maisha magumu kupita kiasi, kila alipokumbuka siku ya kwanza aliyokutana na Nancy chuo kikuu alisikitika lakini hakujuta! Aliamini kila kilichotokea ulikuwa mpango wa Mungu, alimkumbuka pia Tonny, hata yeye hakumchukia, kilichomsikitisha tu ni kwamba alikuwa marehemu! Kichwa chake kilijaa mawazo mengi sana lakini yote hayo hayakuwa na maana tena katika kipindi hicho, ilikuwa ni historia cha muhimu ilikuwa ni kuwaokoa Catherine na David kisha maisha kusonga mbele kuanzia hapo.
Walisubiri taarifa za polisi kuwa wenzao waliokwenda kisiwani Galu walikuwa wamerejea na watoto lakini hazikuja, kila mkuu wa kituo alipokuja kuwaona Nancy na Danny alikuwa na jibu moja tu “Hatuna mawasiliano kabisa na helkopta! Hata sisi tunashindwa kuelewa ni kitu gani kimetokea!” Maneno hayo machache yalimchanganya akili karibu kila mtu, Nancy alilia akiamini wadogo zake wasingeonekana tena kwani aliuelewa uwezo wa mzee Kiwembe na Babu Ayoub katika mambo ya mazingara.
“Nina uhakika kabisa hao polisi waliokwenda na helkopta hawajafika kisiwani Galu! Lazima helkopta yao imezama na hata kama wamefika na kuwachukua watoto pamoja na hao wazee sidhani kama watafika salama hapa Kigoma, nawaelewa wale wazee ni wachawi sana!”
“Sasa wewe uliokokaje?” Aliuliza Mkuu wa Kituo.
“Hata mimi sielewi!”
“Basi hivyo hivyo ulivyookoka wewe ndivyo watakavyookoka wadogo zako!”
“Siamini! Kazi hii lazima niifanye mwenyewe na kama Danny atakubali kuongozana na mimi itakuwa vizuri zaidi natoa muda wa saa sabini na mbili kama hawajaonekana basi mimi nitarudi tena kisiwani Galu, nitapambana kwa namna yoyote mpaka niwaokoe wadogo zangu!” Aliongea Nancy kwa uchungu, alimaanisha alichokisema na hakuwa na utani hata kidogo, wazazi wake walilielewa jambo hilo, siku zote. Nancy alipoongea katika sura iliyoonekana usoni kwake hapakuwa na namna yoyote mtu angeweza kumzuia. Maneno ya Nancy hayakumfurahisha mkuu wa kituo na kulazimika kuondoka wodini kurudi kazini kwake, hata yeye alikuwa na mawazo mengi sana juu ya vijana wake na zaidi ya yote helkopta ya mkuu wake wa kazi, Inspekta Jenerali aliyekuwa mjini Kigoma kufuatilia suala hilo.
“Hivi saa sabini na mbili ni siku ngapi?” Mama yake Nancy aliuliza akiwa amemwangalia mume wake usoni.
“Siku tatu!”Danny alijibu kabla mzee Katobe hajasema lolote.
“Basi tusubiri!”
Siku ya kwanza ikapita hali ya Nancy ikazidi kuwa nzuri, ikaja ya pili na hatimaye ya tatu bila polisi kuwa na taarifa yoyote juu ya helkopta iliyokwenda kisiwani Galu, kila mtu katika jeshi hilo alikuwa amechanganyikiwa! Hisia kwamba ilikuwa imezama hawakuzipa kipaumbele katika fikra zao kwa sababu boti zilizunguka huku na kule katika ziwa Tanganyika bila kuona mabaki ye helkopta lakini baadhi ya polisi walihisi pengine ilizama hadi chini kabisa ya ziwa kama ilivyozama ndege iliyoua wacheza wa timu ya taifa ya Zambia.
“Kama ni hivyo basi haitapatikana kabisa maana ziwa Tanganyika kina chake ni kirefu kuliko ziwa lolote Afrika na sijui ni dunia nzima?”
“Mimi kwa kweli sielewi lakini kama hivyo ndivyo, hili ni pigo kubwa sana kwa jeshi la polisi na Tanzania kwa ujumla, hivi hawa wazee wana uwezo gani? Sijawahi katika maisha yangu kuona mtu anayeteketeza binadamu wenzake kiasi hiki!” Maaskari waliendelea kujadili, kila mtu alisema lake lakini hakuna aliyekuwa na jibu sahihi juu ya mahali walipokuwa maaskari na helkopta ya jeshi.
Tayari Nancy alishaanza kusisitiza safari yake ya kwenda Galu, hakuwa na maongezi mengine zaidi ya kuondoka kwenda kufanya ukombozi mwingine! Wazazi wake walimwona kama mtu aliyechanganyikiwa na akili kwani pamoja na ushauri wote waliompa bado hakukubaliana nao, hata Danny alishindwa kumhamisha Nancy kutoka kwenye msimamo wake.
Hawakuwa hospitali tena tayari walisharuhusiwa na kuhamia katika hoteli maarufu mjini Kigoma iitwayo, Lubumbashi ambako walipanga vyumba wakisubiri ujio wa Catherine na David, Danny na Nancy walilala chumba kimoja na mzee Katobe aliyewachukulia chumba cha kulala watu wawili, jambo lililoonyesha wazi kuwa mzee huyo alishahalalisha na kutangaza kuwa walikuwa mtu na mke kabla hata ya ndoa.
“Danny mimi kesho naondoka!”
“Kwenda wapi mpenzi?”
“Nimekwishasema kuwa narudi kisiwani kuwakomboa wadogo zangu!Siwezi kuwaacha wateseke peke yao Kisiwani kama ni maisha yangu ni bora yapotee wakati nikiwatafuta Catherine na David!”
“Lakini kwanini usivute subira kidogo?”
“Nimevumilia vya kutosha! Nilitoa saa sabini na mbili lakini bado polisi hawajawaleta na kila siku wanadai helkopta yao imepoteza mawasiliano, inawezekana hakuna lolote linalofanyika ni uongo tupu!” Aliongea Nancy kwa msisitizo usiku wa manane wakiwa chumbani kwao.
“Unaondoka lini?”
“Kesho asubuhi!”
“Huniachi hapa Kigoma!”
“Kama uko tayari twende sawa lakini kama unasikiliza maneno ya baba na mama baki!”Aliongea Nancy kwa kujiamini, hakuwa mwanamke wa kawaida kwa jinsi alivyokuwa na msimamo mkali, akili yake ilishabadilika kabisa kutoka na mambo aliyoyafanya.
*****
Asubuhi kulipokucha mambo yalikuwa tofauti kwa mzee Katobe na mke wake, siku zote walizoea kuzinduliwa usingizini na Nancy pamoja na Danny wakiwasalimia lakini siku hiyo mpaka saa moja na nusu hakuna mtu aliyegonga mlango wao, waliingiwa na wasiwasi mwingi na kujikuta wote kwa pamoja wakinyanyuka kwenda kugonga chumbani kwa watoto wao.
“Mh!” Mama yake Nancy aliguna kukuta mlango uko wazi, wakabisha hodi lakini hawakuitikiwa mwisho wakaamua kuingia ndani ya chumba, hawakuamini macho yao kukuta hakuna mtu.
Walikimbia hadi nje kuangalia wakifikiri labda walikuwa nje ya hoteli wakifanya mazoezi lakini hawakuwaona mahali popote! wakarudi mpaka mapokezi na kujaribu kuulizia kwa msichana aliyekuwe nyuma ya meza kubwa.
“Mbona wameondoka saa kumi na mbili asubuhi?”
“Kwenda wapi?”
“Walisema wanasafari kidogo na wamewaaga!”
Wazazi wa Nancy hawakutaka kuongea kitu kingine zaidi, tayari watoto wao walishatoroka kurudi tena kisiwani Galu, jambo ambalo wao waliamini lilikuwa ni hatari kubwa kufanyika kwa wakati huo ukizingatia hata helkopta ya polisi ilikuwa bado haijarejea.
“Yaani wameshindwa kutusikiliza?” Mzee Katobe aliuliza, mama yake Nancy hakuwa na uwezo wa kujibu swali hilo zaidi ya kumwaga machozi,walitoka mbio hadi nje tena na kukodisha teksi iliyowapeleka hadi Bandarini ambako baada ya kupeleleza walipewa taarifa kuwa, Nancy na Danny walikodisha boti iwapeleke kisiwani Galu! Ilikuwa habari ya kusikitisha zaidi.
****
Tayari Nancy na Danny walikuwa katikati ya ziwa Tanganyika ndani ya boti ambayo Nancy aliikodi kutokana na pesa alizopewa na baba yake mara tu baada ya kutoka hospitali, Nahodha wa boti alikuwa akiipeleka kwa kasi isiyo ya kawaida, hayo yakiwa ni maelekezo kutoka kwa Nancy aliyetaka wafike kisiwani Galu haraka iwezekanavyo, hakuna alichokifikiria zaidi ya ukombozi wa wadogo zake Catherine na David! Ndani ya boti kulikuwa na mapanga mawili yaliyonolewa kotekote, mikuki miwili pamoja na pinde na mishale yake! Hizo ndizo silaha walizoziandaa kwa ajili ya kupambana na wazee wawili hatari, Kiwembe na Babu Ayoub.
Hawakuwa na uhakika wa kupata ushindi walikokuwa wakielekea, hasa walipozifikiria nguvu za giza walizokuwa nazo mzee Kiwembe na babu Ayoub, mawazo hayo yaliwatisha wote wawili lakini hawakutaka kabisa yawakatishe tamaa! Walikuwa tayari kupambana mpaka wawakomboe wadogo zao na huo ndio ungekuwa mwisho wa vita, vichwani mwao hawakufikiria kabisa kuwa walikokuwa wakielekea hapakuwa na Catherine, mzee Kiwembe, babu Ayoub wala David, watu hao wote walishaondoka kisiwani Galu kuelekea Kigoma baada ya Polisi kuvamia kisiwa na helkopta kisha kuwaweka chini ya ulinzi wazee hatari na kuwakomboa watoto wawili wadogo. Nancy alikuwa akimwangalia Danny kwa jicho la upande, ukimya wake ulimfanya awe na wasiwasi! Alielewa wazi ni kiasi gani mchumba wake hakufurahishwa na safari hiyo lakini alilazimika kumfuata kwa sababu alimpenda.
“Unajisikiaje?” Nancy aliuliza.
“Safi tu!”
“Mbona unatetemeka?”
“Baridi!”
“Kweli au unaogopa?”
“Nini?”
“Wazee wawili tuowafuata!”
“Hawanitishi tena! Mambo tuliyoyapitia mimi na wewe ni makubwa, hata kama ningekuwa naogopa siwezi kukuacha uende peke yako! Mapanga, mikuki na hii mishale ni halali yao!” Danny aliongea kwa kujiamini.
Saa nzima na nusu baadaye tayari walikuwa wakiwasili kisiwani Galu, siku hiyo walishangazwa na hali ilivyokuwa shwari tofauti na mara ya kwanza wote wawili walipofika kisiwani hapo, ambapo dhoruba kali ilichukua roho za watu! Hawakuamini kama walikuwa wamefika katika hali ya utulivu namna hiyo, boti ilipogoa wote wawili walirukia majini wakachukua silaha zao na kuanza kutembea hadi nchi kavu ambako waligeuka na kumpungia nahodha wa boti mkono.
“Mtachukua muda gani?” Nahodha wa boti aliwauliza.
“Haitachukua muda mrefu sana ingawa kazi ya uwindaji ni ngumu! Tuvumilie, tukishaua hata mnyama mmoja tutarudi haraka iwezekanavyo tuondoke!” Danny alimwambia nahodha wa boti, hivyo ndivyo walivyomdanganya wakati wakimkodi, kwamba walikuwa wakienda Kisiwani Galu kuwinda wanyama wa porini ambao hawakupatikana Bara.
“Basi msichelewe nitawasubiri hapa!”
“Sawa!” Wote wawili waliitikia.
Safari ya kupandisha juu kutoka mwaloni ambako boti iligoeshwa ilianza, Danny na Nancy walikuwa wamedhamiria kufanya ukombozi na walitembea harakaharaka hadi eneo la karibu kabisa na vibanda vya mzee Kiwembe na babu Ayoub, kulikuwa na mita kama mia moja na hamsini tu mbele yao! Wakasimama na kuangaliana, saa ya kazi ilikuwa imewadia.
“Tupige magoti tumwombe Mungu atusaidie!”
“Ni vyema na haki maana hakuna anayeelewa kitakachotokea mbele yetu!”
Walipiga magoti chini na kusali wakiomba ulinzi na baada ya hapo walianza kunyata wakielekea mbele hadi nyuma ya kibanda cha babu Ayoub, walishangazwa na ukimya wa ajabu uliokuwepo! Hawakusikia sauti ya mtu yeyote, si Catherine wala David! Hofu ilianza kuwaingia kuwa huenda watoto hao walikwishauawa au wametoroshwa kwenda upande mwingine wa kisiwa. Walisonga hadi mbele ya kibanda hicho walishangaa kukuta kiko wazi, ikabidi waingie ndani ambako walikuta hakuna mtu lakini vyombo na mizigo mbalimbali ya babu Ayoub ikiwa mahali pake! Wakizidi kuingiwa na wasiwasi walitembea tena kuelekea kwenye kibanda cha mzee Kiwembe nako walikuta hali hiyo hiyo, wakapata uhakika kabisa kwamba watoto waliokuja kuwakomboa hawakuwepo.
“Kuna mawili tu hapa!” Nancy aliongea.
“Yapi?”Danny akauliza
“Aidha wametoroshwa au wameuawa!”
Nancy aliishiwa nguvu mwilini, hakutaka lolote kati ya mambo hayo mawili liwe limetokea! Aliwapenda wadogo zake na alitaka kuwa nao, alikaa chini na kuweka silaha zake chini huku akimwangalia Danny aliyekuwa akitembea huku na kule katika nyasi kuona kama kulikuwa na dalili yoyote ya watu kuwa wameondoka sehemu hiyo muda mfupi kabla, kwa sababu ilikuwa imenyesha mvua siku hiyo alitegemea kuona alama za miguu ardhini lakini haikuwa hivyo!
Walibaki sehemu hiyo kwa muda mrefu wakitafakari nini cha kufanya bila kupata jibu hatimaye wakawa wameamua kuzunguka huku na kule kisiwani kuona kama kulikuwa na dalili yoyote ya mahali mzee Kiwembe na babu Ayoub walikopita lakini bado hawakufanikiwa, jioni wakiwa wamekata tamaa kabisa waliamua kurejea kwenye boti iliyowaleta tayari kwa kurejea Kigoma wakiwa wamenyongíonyea kabisa.
“Vipi?”
“Hatukufanikiwa kuua mnyama yoyote!”
“Kwa hiyo?”
“Turudi zetu Kigoma!” Hilo ndilo lilikuwa jibu la Nancy ambaye mashavu yake yalilowa machozi sababu ya kuwalilia Catherine na David, alikuwa na uhakika kabisa hawakuwa hai! Lazima kwa hasira mzee Kiwembe na babu Ayoub waliamua kuwaua baada ya yeye na Danny kutoroka, ndani ya moyo wake alianza kujilaumu ni kwanini aliwaacha wadogo zake wakauawa lakini hakumwambia Danny juu ya jambo hilo na hakutaka litawale ubongo wake, yote alimwachia Mungu.
“Mh!” Danny aliguna.
“Nini tena?”
“Ule sio mtumbwi wao kweli?”
“Uko wapi?” Nancy akauliza.
“Pale kwenye nyasi!” Danny aliongea akiwa amenyoosha mkono wake wa kuume na kusonta kwenye nyasi zilizokuwa jirani na eneo hilo.
“Ndio! Ni wenyewe, sasa wameondoka na nini?”
“Hata mimi sijui!”
“Tufanye nini sasa?”
“Lazima wapo! Turudi tukawasubiri, hatuwezi kurudi Kigoma mikono mitupu, kama hatuendi na watoto basi twende na wao!”
“Akina nani?” Nahodha aliwauliza baada ya kuwa wameongea muda mrefu bila kumshirikisha lakini hakuna aliyemjibu badala yake Nancy alimuuliza gharama ya kuwasubiri kwa masaa mengine matatu zaidi.
“Shilingi elfu tano kwa saa!”
“Nitakulipa!” Aliongea Nancy na mara moja yeye na Danny walishuka na kuanza kukimbia hadi kwenye vibanda vya babu Ayoub na mzee Kiwembe ambako walijificha nyuma ya kichaka na kusubiri kama kweli wazee hao walikuwa wametoka kwenda mahali basi wangerudi na kuwakuta lakini hata baada ya kusubiri masaa matatu bado hawakuweza kuwaona, wakakata tamaa kabisa na kuamini hawakuwemo kisiwani! Wakiogopa kumuudhi mwenye boti walirejea na kupanda boti yao kurejea Kigoma wakiwa wamechoka hoi bin taaban.
Nancy alilia machozi njia nzima wakielekea Kigoma na ilikuwa kazi ya Danny kumbembeleza, nahodha wa boti hakujisumbua kuuliza swali juu ya kilichomfanya Nancy alie, alichukulia haikuwa shughuli yake, kitendo cha kutojibiwa alipouliza mara ya kwanza kilimuudhi kupita kiasi! Tangu wakati huo alichojali yeye ni kazi yake, kama saa nne na nusu hivi ya usiku waliwasili Kigoma na kunyoosha moja kwa moja hadi Lubumbashi hoteli na kupokelewa na wafanyakazi wa hoteli hiyo.
“Mlikuwa wapi? Wazazi wenu wamewatafuta sana!”
“Tulisafiri kidogo!”
“Bila kuwaaga?”
“Ilikuwa ghafla!”
“Wako wapi sasa?í Nancy aliuliza kwa mshangao.
“Walikuwa hapa muda si mrefu ila wamefuatwa hapa na gari la polisi!”
“Kwenda wapi?”
“Nafikiri kituoni!”
“Kuna nini?”
“Hawakunieleza kitu chochote ila niliona mama yako analia sana, neno helkopta likitajwa mara mbili mbili kisha wakaondoka haraka ndani ya gari!”
Danny alimwangalia Nancy usoni, wakagonganisha macho, wote walikuwa wamepatwa na mshtuko juu ya habari hizo, kichwani mwa Nancy hisia huenda helkopta ilifika kisiwani na kuwakomboa Catherine na David lakini baadaye kupatwa na ajali zilianza kutawala, kitu hicho ndicho kiliendelea akilini mwa Nancy! Wote wawili wakaamua kuondoka mbio hadi kituo cha polisi ambako walikuta watu wengi wamejaa wakishangaa kitu ambacho Danny na Nancy hawakukielewa, hawakutaka kupoteza muda walichofanya ni kukimbia moja kwa moja hadi ndani ya kituo ambako waliomba kuonana na mkuu wa kituo, maaskari wote waliowakuta mapokezi walionyesha kuwashangaa.
“Nyie mlikuwa wapi?”
“Kwa nini?”
“Mmewahangaisha sana wazazi wenu!”
“Wako wapi hivi sasa?”
“Wamekwenda hospitali ya Maweni!”
“Kuna nini?”
“Wamekwenda kuwatambua......!” Hakuweza kuikamilisha sentensi yake baada ya askari aliyekuwa jirani yake kumkonyeza, kitendo hicho pia Nancy alikishuhudia na kuzidi kuingiwa na wasiwasi moyoni mwake na kuamini kulikuwa na tatizo limetokea, kwa sababu hata wao walipafahamu hospitali hawakutaka kupoteza muda wa kuuliza maswali zaidi ilibidi waondoke hadi stendi ambako walikodisha teksi iliyowapeleka moja kwa moja hadi hospitali ya mkoa wa Kigoma kushuhudia walichokwenda kutambua wazazi wao ambacho askari hakutaka wakielewe.
Nusu saa baadaye tayari walishafika hospitalini na kuanza kuzunguka huku na kule wakiwatafuta mzee Katobe na mkewe.
*******
Hali ya hewa angani ilikuwa mbaya kwa karibu masaa mawili, rubani wa helkopta ya jeshi akihangaika kusonga mbele lakini alishindwa kabisa kwa sababu ya giza lililokuwepo na uzito wa hewa! Alishindwa kuelewa nini kingetokea mbele yao na kulazimika kuwaomba watu wote waliokuwemo ndani ya helkopta hiyo wamwombe Mungu afanye muujiza ili kuokoa maisha yao!
Alikuwa amehangaika na helkopta hiyo kwa karibu masaa mawili bila mambo kubadilika mpaka taa ya mafuta ikaanza kuwaka jambo lililoashiria hatari kwani kama injini zingeishiwa mafuta kabisa zingezima na baadaye helkopta ingeanguka na kulipuka na wote wangekufa.
Hapo ndipo alipofikiria suala la kutafuta mahali pa kutua na kuanza kutupa macho yake chini lakini kila upande alioangalia kulionekana kuwa na maji hatimaye aliamua kukata kona kuelekea ufukweni ambako alitua kwa usalama bila kuelewa palikuwa ni mahali gani, muda mfupi baadaye walishangazwa kundi la watu wafupi kupita kiasi ambao kwa idadi hawakupungua hamsini waliofika eneo hilo na kuizunguka helkopta.
Maaskari waliweka silaha zao tayari kwa lolote ambalo lingetokea lakini hakuna vurugu yoyote iliyojitokeza! Hakuna aliyeshuka wala kudiriki kufungua mlango, muda wote walikuwa wakijaribu kuwasiliana na kwa njia ya simu ya upepo ili waje waokolewe au kuletewa msaada wowote lakini hapakuwa na mafanikio yoyote.
Walibaki eneo hilo kwa siku tatu bila chakula njaa ikizidi kuwasumbua na Mbilikimo hawakuondoka walisubiri kwa uchu, kwa sababu walishasikia habari za mbilikimo wala watu wa Kongo! Waliamini kabisa watu wafupi waliozunguka helkopta yao ndio wao, ndio maana hakuna mtu aliyediriki kuugusa mlango kwa kuogopa kuwa kitoweo.
Pamoja na njaa rubani hakuchoka kutafuta mawasiliano, katika hali ambayo hawakuitegemea kabisa siku ya tano wote wakiwemo babu Ayoub na mzee Kiwembe wakiwa wamelegea kabisa, mawimbi ya redio yalinasa wakawa wameinasa Kigoma na kuongea na Kamanda wa Polisi na kumweleza kila kitu juu ya mahali walipokuwa.
Lilikuwa ni suala lililohitaji haraka kwa jeshi la polisi ili kuokoa maisha ya maaskari wenzao waliokuwa wamekwama porini na helkopta, kikao cha haraka kiliitishwa na kupitishwa uamuzi wa kutafuta helkopta ya kukodi kutoka jijini Dar Es Salaam lakini kabla ya kufanya hivyo waliamua kujaribu kwanza kuulizia kwenye mashirika ya Wakimbizi.
Kama bahati walifanikiwa kupata helkopta kutoka shirika la kuhudumia wakimbizi, UNHCR! Muda huo huo ikaondoka kwenda eneo waliloelekezwa, kwa kutumia viona mbali haikuwachukua muda mrefu kugundua mahali helkopta ya jeshi la polisi ilipokuwa na wakatua!
Nao pia walishangazwa na umati wa mbilikimo waliokuwepo, hata hivyo risasi zilimiminika na kuwasambaza wote ndipo maaskari wakakimbia na kwenda kuvunja mlango wa helkopta ya jeshi na kuingia ndani, watu wote walikuwa hoi kwa njaa walichofanya ni kuanza kuwasomba mmoja baada ya mwingine mpaka kuwamaliza na helkopta ikaruka kurejea Kigoma ambako walikimbizwa hospitalini na kuanza kupewa matibabu.
Muda huo huo taarifa zilitumwa hoteli ya Lubumbashi kuwataarifu mzee Katobe na mkewe juu ya kupatikana kwa watoto wao na wakaondoka mbio kwenda hospitali usiku huo huo ambako waliwakuta Catherine na David katika hali mbaya, walikuwa chumba cha wagonjwa mahututi na matumaini ya kuokoa maisha yao yalikuwa kidogo sana, muda mfupi baadaye Nancy na Danny walifika wakikimbia.
“Jamani Nancy mlikuwa wapi?”
“Tuliwafuatilia Catherine na David kisiwani Galu!”
“Mbona tayari wako hapa!”
“Wako hapa?”
“Ndio, lakini hali zao ni mbaya!”
“Wamefikaje?”
Mzee Katobe alianza kuwasimulia taarifa aliyopewa na polisi juu ya namna watoto walivyookolewa na hatimaye kufika Kigoma! Ilikuwa ni kama hadithi lakini huo ndio ulikuwa ukweli, siku mbili baadaye baada ya matibabu ya kina hali za Catherine na David zilirejea katika hali ya kawaida, dripu za maji ya sukari walizopewa ziliwapa nguvu na kuwafanya wazima kabisa.
Ilikuwa furaha kubwa mno kwa familia hii kuungana tena, mzee Kiwembe na mwenzake babu Ayoub walifikishwa mbele ya sheria kwa kosa la utekaji na utesaji na wakahukumiwa kwenda jela miaka kumi na tano, pamoja na mzee Kiwembe kujitetea kuwa watoto Catherine na David walikuwa wake hakuna aliyejali! Sheria ilichukua mkondo wake, baada ya hukumu hiyo mzee Katobe, mke wake, Danny, Nancy, Catherine na David walirejea Bagamoyo! Kila mtu alishangaa kuwaona tena, familia iliyosambaratika ilikuwa imeungana upya na hakuna kilichosubiriwa isipokuwa ndoa ya Nancy na Danny!
Wazazi wa Danny walipelekewa taarifa juu ya kupatikana kwa mtoto wao jambo ambalo hawakuliamini, ilibidi wasafiri kurejea Tanzania kufurahi pamoja na mzee Katobe na familia yake, waliunga mkono ndoa na ikafungwa wiki mbili tu baadaye, hatimaye Danny na Nancy wakawa mtu na mke wake! Ilikuwa ni kama sinema ya Kihindi lakini ulikuwa ukweli mtupu na baada ya ndoa hiyo walishauriwa kurudi tena chuo kikuu kuendelea na masomo yao, hakuna aliyebisha! Mwaka uliofuata walijiunga tena na chuo kikuu kwa masomo ya sheria, yaliyotokea maishani mwao yalikuwa historia na hawakutaka kabisa kuyaongelea mauaji yote waliyofanya, walitubu dhambi zao na kurejea kanisani! Maisha yao yalikuwa ya raha mustarehe chuoni wakiishi chumba kimoja na kufanya kila kitu pamoja.
“Unamkumbuka Tonny?” Nancy alimuuliza Danny siku moja wakiangalia mchezo wa televisheni uitwao Days of our Lives ambao huonyeshwa na channel Ten.
“Sitaki kumkumbuka, yaliyopita si ndwele.....tugange?”
“Yajayo!” Nancy aliitikia na wote wakacheka.
“For sure we have been through Blood, Kisses and Tears!”(Kwa hakika tumepita katika vipindi vya damu, mabusu na machozi!) Alimaliza Danny akitabasamu.

Tumefikia mwisho wa hadithi yetu ndefu! Ahsanteni kwa uvumilivu wenu, penye mafundisho, naomba upachukue ili yaweze kukuongoza kwenye maisha yako

MWISHO
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom