Fahamu uhusiano wa TB na ukimwi

kilimasera

JF-Expert Member
Dec 2, 2009
3,068
268
TANGU ugonjwa wa ukimwi ugunduliwe duniani pamekuwepo na mkanganyiko miongoni mwa jamii kuhusu mgonjwa mwenye ukimwi anavyokuwa.

Hali hii aghalabu imesababisha watu wengi kuamini kuwa kila abainikaye kuwa ana Kifua Kikuu (TB) bila shaka ana ukimwi na hata kinyume chake.

Ni katika mtazamo huu nimesukumwa kuandika ufafanuzi huu kuhusu uhusiano uliopo baina ya magonjwa haya mawili ambayo kusema kweli ni tishio kwa maisha ya watu duniani kote.

TB kama wengi wanavyouita, ni ugonjwa unaosababishwa na vimelea vijulikanavyo kwa kitaalamu kama Tuberculoid Bacilli.Vijidudu hivi viligunduliwa zaidi ya karne moja iliyopita na mtafiti mmoja Mjerumani, Dk. Robert Koch, baada ya kuyachunguza makohozi ya mgonjwa aliyekuwa anakohoa sana.

Utafiti wake ulikuja kubaini kuwa wadudu hawa huenea na kumuingia mtu mwingine kwa njia ya hewa hususan pale mgonjwa anapokohoa, anapocheka au anapopiga chafya na mtu mwengine mzima anapovuta hewa ile wakati wa kupumua kawaida.

Aidha, ifahamike pia kuwa yapo mazingira yanayochangia sana kurahisisha kuenea kwa ugonjwa huu wa TB ya mapafu.

Mazingira yenye msongamano wa watu kama vile kwenye shule, chuo, kambi, harusi, ngoma na sherehe mbali mbali hurahisisha watu kushirikiana kuvuta hewa pamoja.

Kwa upande mwingine ugonjwa wa ukimwi nao umegundulika takriban miongo miwili hivi, na unasababishwa na aina ya virusi ambavyo vikimuingia mtu hushambulia chembechembe za kinga mwilini.

Ilishabainika mapema kuwa majimaji au damu kutoka kwa mgonjwa vipatapo nafasi ya kuingia kwenye damu ya mwingine, huyo naye hupata shida hiyo.

Hivyo michubuko na majeraha pamoja na vifaa vya kutogea masikio, kutahiria na kunyolea huchangia maambukizi ya ukimwi.

Magonjwa haya mawili pamoja na malaria ndiyo yanayoongoza kwa kuchukua maisha ya watu hasa kwa nchi zinazoendelea kwa idadi kubwa kuliko nchi zilizoendelea.

Katika kuchunguza mahusiano kati ya magonjwa haya ya ukimwi na TB tafiti zimebainisha kuwa kila ugonjwa huongeza kasi ya athari ya ugonjwa mwingine na kufikirika kuwa huenda kuna hali ya kutegemeana kwa magonjwa haya.

Lakini kitokeacho ni kwamba virusi vya ukimwi vyenye tabia ya kushambullia kinga asili ya mwili wa mtu aliyeambukizwa, kwa hali hiyo muathirika anapokuwa hana kinga ya kutosha dhidi ya magonjwa humwia rahisi zaidi kwake kupata maambukizi ya magonjwa mbalimbali ukiwemo huu wa TB.

Hivyo kutokana na mazingira ya makazi ya watu wa nchi zetu za ulimwengu wa tatu inakuwa rahisi sana kwa vimelea vya TB kupata urahisi wa kuwaingia watu wanaokuwa mara nyingi kwenye misongamano ya mabasi, sherehe na mikusanyiko kama hiyo.

Hii ina maana kuwa ongezeko la maambukizi ya TB kwa sehemu kubwa lina uhusiano na kuwepo na maambukizi ya ukimwi, maana mwenye virusi vya ukimwi amepungukiwa na kinga ya asili mwilini mwake kwa hiyo ana uwezekano mkubwa kupata TB mara kumi zaidi ya mtu asiye na virusi hivyo.

Pia ni vema ifahamike kuwa TB inaongoza miongoni mwa magonjwa mengine kwa kusababisha takriban asilimia 30 ya vifo kwa watu, maana vijidudu vya TB navyo vinashambulia chembe chembe nyekundu za damu. Kwa sababu hii mgonjwa mwenye magonjwa haya hunyong’onyea kwa haraka zaidi na kukabiliwa na kukosa damu ya kutosha na nguvu kupungua.

Ugonjwa wa TB unatibika, unapaswa utibiwe kama ambavyo maradhi mengine yampatayo mwenye ukimwi yanavyoweza kutibiwa na kupona. Hivyo ifahamike kuwa mgonjwa wa TB apatapo tiba stahiki anaweza akapona endapo atakamilisha kipimo chake alichopangiwa na daktari licha ya kwamba anao ukimwi.

Pengine nitahadharishe kuwa si kila mgonjwa wa TB ahesabike kuwa ana ukimwi pia, kwani kama nilivyoeleza hapo juu kwamba kila ugonjwa una kidudu chake tofauti ambacho kinaweza kushughulikiwa kipekee.

Baada ya kufahamu mahusiano hayo ya TB na ukimwi, ni imani yangu kwamba ufahamu huo utakusaidia na kukuhamasisha uingie kwenye mapambano dhidi ya tatizo hili la maradhi haya na hivyo taifa litarajie mafanikio na ushindi pale sote tutakapotoa ushirikiano kwa serikali na mashirika yanayopambana na shida hii pia.

Imeandaliwa kwa msaada wa mtandao.
 
Sababu kubwa pia inayosababisha wanaopungukiwa kinga kushambuliwa kirahisi na TB ni ile kinga iliyofanywa awali Hegeuka kuwa adui badala ya rafiki na mlinzi pindi nguvu za mwili zipunguapo. na hili ndilo linalosababisha watu kuamini kwamba UKIMWI na TB ni kama mapacha. Kufutika kwa dhana hii itachukua muda...
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom