KATIBU Mkuu wa Chama cha
Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Dk. Willibrod Slaa, amesema Rais
Jakaya Kikwete anapaswa kuomba hekima kwa Mwenyezi Mungu kutokana na
matukio yanayotokea sasa nchini.
Alisema hali inayotokea sasa ni matokeo ya wananchi kupuuzwa na
kutokusikilizwa katika suala zima la uwekezaji unaofanyika sehemu
mbalimbali za nchi. Dk. Slaa alitoa kauli hiyo jana katika kijiji cha
Giroda Babati vijijini, wakati akihutubia mkutano wa hadhara katika
ziara yake ya siku tisa ya ujenzi wa Chama mkoani Manyara.
Kabla ya kutoa kauli hiyo Dk. Slaa aliwaomba wananchi wasimame kwa muda
wa dakika moja, kuomboleza vifo vilivyotokea mkoani Mtwara.
Aliongeza kuwa kuendelea kuwapuuza wananchi wa Mtwara ni kuendelea
kucheza na jipu linalopaswa kutumbuliwa na kwamba njia sahihi ni kukaa
na kuwasililiza wananchi katika uwekezaji na kufikia muafaka pasipo
kutumia nguvu. Alisema wanachotaka wananchi wa Mtwara ni kujua namna
watakavyonufaika kwa kile alichoeleza kuwa katika uwekezaji wowote
wanufaikaji wa kwanza wanapaswa kuwa wananchi.
Alisisitiza kuwa katika hali ya Mtwara kulihitajika busara za kawaida
za kutatua msingi wa tatizo badala ya wananchi kupigwa mabomu, risasi na
kisha kukamatwa.
Ni jambo la aibu kuwapiga mabomu wananchi wanaodai kunufaika na
rasilimali za nchi yao hapa kunahitajika elimu ya kuwafahamisha haki zao
ni zipi na siyo mabomu.,alisema Dr Slaa.
Source:Tanzania Daima.