CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimemwandikia barua kali Msajili wa Vyama vya Siasa, John Tendwa, kikisema kuwa hakiko tayari kutoa maoni kuhusu vurugu zilizotokea hivi karibuni mjini Dodoma.
Sababu kubwa iliyotajwa na chama hicho ni kwamba suala hilo ni la kijinai na msajili hana mamlaka ya kushughulikia makosa ya namna hiyo.
Msimamo huo wa CHADEMA unakuja siku chache baada ya Tendwa kupitia barua yake ya 05/02/2013, yenye Kumb. Na. AB.115/123/01A/45 kumtaka Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk. Willibrod Slaa, atoe maoni yake juu ya vurugu zilizotokea mwishoni mwa juma lililopita.
Katika vurugu hizo wanachama wa CCM, wakiwemo viongozi, wabunge na makada waandamizi, waliwavamia na kuwashushia kipigo wanachama na viongozi wa CHADEMA.
Vurugu hizo zilitokea eneo la Mwanga Bar baada ya wafuasi wa CCM wakiongozwa na mbunge wa Tabora Mjini, Ismail Rage, kungoa mlingoti na kushusha bendera ya CHADEMA kisha kufanya mkutano wa maadhimisho ya miaka 36 ya kuzaliwa chama hicho.
CHADEMA katika barua hiyo ambayo imesainiwa na Idara ya Sheria ya chama hicho kwa niaba ya katibu mkuu wake, yenye Kumb. Na. C/ADMMSJ/04/04 ya 06/02/2013, wanasema chama hakiwezi kutoa maoni yake, kwa sababu suala hilo ni la kijinai.
Viongozi wake mkoani Dodoma, wameshafungua mashtaka, hivyo kumtaka Tendwa awasiliane na mamlaka zinazohusika na makosa ya jinai.
Nimeagizwa na katibu mkuu nikujulishe kuwa hatatoa maoni kuhusu tukio lililotokea Dodoma siku ya tarehe Februari 3, 2013 kwa kuwa suala hilo ni la jinai na viongozi wa CHADEMA Mkoa wa Dodoma, wameshafungua mashtaka polisi, ilisomeka sehemu ya barua hiyo.
Batua hiyo inaongeza kuwa kutokana na suala hilo kuwa la jinai, Msajili wa Vyama vya Siasa hana mamlaka ya kulishughulikia.
Source:Tanzania Daima/Nipashe