Mh. Raisi,
Salaam.
Nasikitika sana ukikosea na wengine wote wanakosea. Siamini wanakosea kwa bahati mbaya ila ni kwa sababu umewasabisha wakosee.
Umeongelea maandamano ya Chadema kwenye hotuba yako. Wengine wamekurupuka wanazungumza pia. Wanalaani.
Kama umeshasema nilitegemea kitu cha kufuata ni utekelezaji wa amri yako (najua hukutoa) au maagizo yako. Sasa wote mnatoa kauli, mnatuchosha kutuambia ambayo sisi tunayajua.
Ni nani amekwambia kuna mtu anapenda kutembea juani kilomita 10? Je Mh. Raisi unafikiri watu wanapenda kutumia mafuta yao ya pikipiki na kuacha vibarua vyao watembee tu barabarani?
Mnawaita wazururaji, je umesikia Bank au mwajiri yeyote amelalamika mfanyakazi ameacha desk akaenda kwenye maandamano? Hujiulizi kwanini wanazurura?
Mheshimiwa Raisi, na hao waliofeli kidato cha nne kwa maelfu wataacha kuzurura? Au unafikiri wameenda wapi baada ya kufeli? Yakitokea maandamano wakae nyumbani kisa amani na utulivu?
Mnatoa kauli za kejeli badala ya kujibu hoja na kuongoza nchi. Waziri Mkuu anapotoa kauli 'hao chadema wenyewe waoga wakipigwa mabomu wanakimbia' anaitakia hii nchi amani? Kuanzia sasa polisi wakipiga mabomu hatutakimbia, tutajibu kwa mabomu ya petroli si ndicho anachotaka?
Anayechochea hapa ni nani? Anayekejeli wananchi wakikimbia au anayekimbia? Kwa sababu anataka watu wasikimbie basi asubiri aone. Wapige tena mabomu.
Mh. Raisi, umezungukwa na watu wasiofikiri wala hawana msaada kwako. Mbona hawakuongea kabla hujaongea wewe? Wassira, Vuai nk walikuwa wapi? Tendwa alikuwa hajui kuhusu hili mpaka sasa? Acheni kutuona wajinga. Mkituheshimu tutawaheshimu.
Mnataka kusujudiwa na kuogopwa. Hapana. Nchi ina matatizo na matatizo ni yaliyopo sasa hivi sio historia ya 'oooh tumeitoa nchi mbali'. Mbali wapi?
Mheshimiwa Raisi, hao wakina Wassira, Tendwa na Jumuiya ya Wazazi nk ni wanafiki na hawana maana. Hawakwambii ukweli na ukikosea wanazidi kukupoteza.
Mh. Raisi, waandamanaji ni wananchi. Ni watanzania. Wanaipenda amani yao. Wao ndio sababu ya amani na utulivu. Sio ccm wala chadema.
Wananchi ndio wanailinda amani hiyo. Sio ccm wala chadema.
Wanapokimbia ili amani na utulivu viendelee Waziri Mkuu anawaita waoga. Take it from me, hawatakimbia tena halafu tuone.
Mh. Raisi, tafadhali waongoze viongozi wako. Wafundishe adabu na heshima kwa wananchi wa taifa hili. Dharau na kejeli zao zitaleta majuto.
Mh. Raisi, jitahidi kutatua kero za wananchi. Yote yanayozungumzwa yapo. Ndio maana wananchi wanaandamana. Hawalazimishwi kushiriki. Ni shida zao ndio zinawafanya waamue kueleza kilicho moyoni mwao.
Mh. Raisi, nashindwa kukuelewa. Wananchi wanakwambia hatuna kazi, maisha magumu, tunafeli mitihani, nchi yetu inaibiwa nk wewe unasema wanatishia amani!! Kweli umeshindwa kuona kwamba kinachotishia amani ni hizo sababu na sio wananchi wala chadema?
Mh. Raisi, narudia kusema, wanaoandamana ni wananchi. Sio chadema. Wengi wa waandamanaji hao walikupigia kura 2005 na 2010. Tafadhali wewe na viongozi wako msiwadharau.
Kama waliwachagua wakiwa wanazurura basi msiwatupe baada ya kuwachagua kisa eti ni wazururaji.
Chadema ni waandaaji. Washiriki ni wananchi, watanzania.
Huna wa kukwambia, ukikosea wewe wamekosea wote. Hilo ni tatizo.