Irene ana chuki zake mwenyewe kwa Nchimbi
Na Zephaniaanjela
Nimeisoma kwa makini makala ya Mwandishi Irene Mark ya kumtaka Mwenyekiti wa Taifa wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM), Dk. Emmanuel Nchimbi atulie kwa vile mwosha hatimaye naye huoshwa.
Katika makala hiyo iliyoanza kuchapishwa kwanza katika gazeti la Tanzania Daima Toleo la Jumapili Machi 9, 2008, Irene amejitahidi kwa kadri awezavyo "kumshambulia" Dk. Nchimbi kama mtu binafsi zaidi tofauti na chanzo kilichopelekea achukue hatua hiyo ambayo hakika inasikitisha!
Tatizo nililoliona katika makala yake hiyo ni kuingiza ushabiki na chuki binafsi, itikadi za kisiasa huku lengo lake hasa likiwa ni kutaka kumdhalilisha kwa maslahi anayoyajua mwenyewe.
Waliokuwepo katika mkutano wa Dk. Nchimbi na waandishi wa habari, Machi 5, 2008, wanajua kile alichozungumza na kujibu vizuri maswali yote aliyoulizwa na watu kama Muhibu Saidi wa gazeti la Mwananchi, hivyo kuja na madai nje ya kile alichosema katika kikao hicho ni sawa na kufanya ukuwadi wa kisiasa kwa niaba ya Chadema, na pia inawezekana amefanya hivyo kwa nia ya kutaka kumfurahisha mwajiri wake wa kweli, Freeman Mbowe.
Dk. Nchimbi anayehusishwa na historia ya kuunda na kusimamia makundi katika Umoja wa Vijana na CCM kama taasisi za kisiasa hata siku moja hajawahi kuhusika na hilo, badala yake waandishi wa habari wasiojua siasa kama Irene ndio wamekuwa wakihadithiwa uongo na wapinzani wa CCM na kuubeba kama ulivyo bila ya kutafiti.
Kwa mfano, ni ujinga mtupu kumhusisha Dk. Nchimbi kwa namna yoyote ile na suala la mgogoro na hatimaye kusambaratika kwa ndoa ya aliyekuwa Mbunge wa Viti Maalum kupitia UVCCM, hayati Amina Chifupa, mwaka jana.
Nimejaribu kuisoma makala yake hiyo kuanzia gazetini hadi katika mtandao, lakini sikuona popote alipothibitisha kwa namna moja ama nyingine kuhusu jambo hilo iwe kwa kuonyesha ushahidi wowote usio na mashaka, badala yake ametumia uvumi wa mitaani unaoweza kuzungumzwa na mtu yeyote wakiwemo makuwadi wa fitina kwa watu.
Uandishi wa kusukumwa na utashi wa kisiasa na kujifanya mpiganaji wa mstari wa mbele kuliko hata Mbowe, Dk. Slaa na viongozi wengine wa Chadema ni kushusha hadhi ya taaluma, hivyo Irene kama anataka kuingia katika siasa ni vuzuri akatangaza hadharani ili wanasiasa pia anaowatungia uzushi kama Dk. Nchimbi nao waweze kumjibu kwa haki majukwaani ama vinginevyo kuliko kubishana kwa njia anazotaka wafanye akidhani ni watoto kama yeye.
Ni makosa makubwa kushabikia kile anachoita "kumbukumbu" ama rekodi huku akijua kwa uhakika kabisa kuwa hazipo na kumhusisha mtu na jambo kubwa kama kusambaratisha ndoa ya mume na mke, tena kwa sababu za kisiasa, suala ambalo haliingia kichwani ila labda kwa mtu asiyekuwa na akili timamu!
Kwa mfano, hivi Irene akiulizwa kuwa ndoa ya Amina Chifupa na Mohammed Mpakanjia ilikuwa na uhusiano gani na ubunge, Uenyekiti wa Taifa wa UVCCM ama Unaibu Waziri wa Dk. Nchimbi atatoa ushahidi gani?
Atajitetea kwamba watu walikuwa wakizungumza na yeye akasikia ama atatoa ushahidi wa maandishi alioupata kutoka kwa Mpakanjia?
Au, kama ni kweli kuwa Dk. Nchimbi alifanya hila kuisambaratisha ndoa ya Amina ili kukidhi matakwa yake ya kisiasa, Irene anataka watu waamini kuwa Mpakanjia ana akili finyu kiasi cha kufikia hatua ya kumtaliki mkewe aliyezaa naye mtoto kwa kuamini uvumi wa barabarani?
Ni ujinga mwingine mkubwa kutaka kumlazimisha Dk. Nchimbi awe anajibu kila upumbavu na tuhuma za utumbo zinazotolewa na wapinzani wake kisiasa na kuacha shughuli zake za kuitumikia nchi yake kutokana na madaraka makubwa matatu ya kisiasa aliyonayo akiwa Mbunge wa Songea Mjini, Mwenyekiti wa Taifa wa UVCCM na Naibu Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa.
Wakati Irene akisema mwishoni mwa makala yake kuwa Dk. Nchimbi ni mwanasiasa asiyependa kuzungumza na vyombo vya habari, mimi nasema kiongozi huyo hapendi kuzungumzia "umbea" na majungu, na pia hapendi kuongea na waandishi wa habari wanaoandika maoni yao zaidi katika habari zao badala ya kutoa taarifa sahihi walizoziona, kusikia au kuhadithiwa kwa kuambatana na ushahidi na vielelezo vya dhati pale inapobidi kufanya hivyo.
Mwandishi wa habari anayekusanya "umbea" na kudai ni kumbukumbu zilizosemwa zamani huku mtuhumiwa akiwa kimya na bila popote pale alipojaribu angalau kumtafuta iwe kwa simu ama ofisini kwake bila mafanikio
Waandishi waliosheheni "umbea" kama Irene ndio wanaweza kuja na uvumi kutoka uchochoroni kwamba Dk. Nchimbi alimpoteza Amina kutoka kwenye anga za siasa kwa kumtengenezea zengwe kutokana na sababu anazozijua mwenyewe.
Kila ninapotaka kumshangaa mtoto huyo wa kike anayekuzwa na kulelewa Bilcanas Club ninashindwa.
Hivi Amina alikuwa na kitu gani kinachoweza kusababisha Dk. Nchimbi apoteze ubunge wake, apoteze Uenyekiti wa Taifa wa UVCCM au Unaibu Waziri alionao kama siyo uongo na upeo mfupi wa kuchambua mambo?
Iko wapi nguvu anayodaiwa kuwa nayo Amina katika ulingo wa kisiasa iwe katika UVCCM, CCM na kadhalika? Angewezaje kuwa na nguvu na kufikia hadi kumtisha Dk. Nchimbi wakati alikuwa chini kabisa katika matawi akiendesha kampeni za kusaka ukamanda wa Vijana ili angalau apate jukwaa la kusemea?
Nani asiyejua kuwa Amina alikuwa akifanya hadi utapeli kwa kuahidi kutoa misaada ya kifedha kwa UVCCM kama alivyofanya katika mkoa wa Dar es Salaam, lakini "akaingia mitini" na kuwaacha solemba chipukizi aliodai kuwa angewapeleka mkutanoni Dodoma?
Kama Irene haamini haya aende kwa Katibu wa UVCCM wa Mkoa wa Dar es Salaam, Sixtus Mapunda katika jengo ilipo Studio ya Redio Uhuru, jirani na Ofisi Ndogo ya Makao Makuu ya CCM akaambiwe ukweli huo, tena kwa kuonyeshwa kumbukumbu za maandishi na siyo kwa hadithi za kuchonga kama anazokuja nazo yeye.
Akitoka huko aende pia awaulize Makatibu wa Umoja wa Vijana wa CCM wa Wilaya za Temeke, Ilala na Kinondoni ili katika sehemu hizo zote nako apewe uthibitisho na kisha atoe hukumu mwenyewe.
Katika hali hiyo hata bila kuzungumzia matatizo mengine makubwa aliyokuwa nayo Amina, hivi mwanasiasa kama huyo angewezaje kumtisha Dk. Nchimbi na katika jambo lipi?
Tukiachana na Amina, Irene pia anaonyesha kuwa ni mbumbumbu mkubwa kabisa wa masuala ya kisiasa anapokuja na mfano mwingine dhidi ya Dk. Nchimbi kuhusu kile anachodai ni mgogoro uliokaribia kuzuka kati yake na aliyekuwa mpinzani wake katika kinyang'anyiro cha Uenyekiti wa Taifa wa UVCCM, Jane Claude Mihanji.
Pamoja na kuishia kusema tu kuwa Dk. Nchimbi alihusishwa hadharani na mambo mazito kwamba alijaribu kumfanyia Mihanji, hilo nalo haliwezi kukubalika hata kidogo na ndiyo maana hata Jeshi la Polisi liliona kuwa ni uongo uliotungwa kwa malengo "machafu".
Jane alidai aliitwa nyumbani kwa Dk. Nchimbi huko Tabata jijini Dar es Salaam, na kwamba wakati wakiwa pamoja sebuleni wakizungumza na kujadiliana mambo kadhaa ya kisiasa, ghafla alikuja mtu dirishani na kupuliziwa sumu asiyoyajua, tuhuma ambazo hata mjinga kabisa hawezi kuzikubali.
Namshauri Irene aulize watu wanaojua undani na ukweli kuhusu uongo huo ili wamwambie kwa ushahidi namna Jane alivyokuwa ameahidiwa ubunge wa kuteuliwa na hatimaye Unaibu Waziri wa Habari na mmoja kati ya "vigogo" waliokuwa na nia ya kugombea urais mwaka 2005 ili amtumie kukidhi matakwa yake ya kisiasa.
"Kigogo" huyo wa CCM hakutaka Dk. Nchimbi agombee Uenyekiti wa Taifa wa UVCCM kwa sababu alijua kuwa angeibuka mshindi, hivyo ili kuzuia jambo hilo akapanga kumwibulia kashfa na kumtafuta Jane ambaye bila hiyana akaingizwa "mkenge" na kujifanya kapuliziwa madawa yenye sumu sebuleni ili apofuke macho au afe kabisa.
Hata madaktari kama Maua Abeid Daftari walihoji kwenye kikao cha Kamati Kuu na "kigogo" aliyekuwa akimtumia binti huyo akashindwa kutetea uongo wake ni namna gani sumu hiyo ipulizwe sebuleni walipokuwa wawili, lakini imfuate Jane peke yake na kumuacha Dk. Nchimbi utadhani ina akili na macho.
Mkakati huo ulikuwa ni jaribio la pili la kutaka kumwengua Dk. Nchimbi baada ya awali kuletwa hoja ya umri kuwa mwanachama wa Umoja wa Vijana wa CCM aliyevuka miaka 30 hata kama hajafikisha 35 asigombee Uenyekiti wa Taifa wa UVCCM, lakini likagonga mwamba na kusambaratishwa.
Kilichoulizwa na watu wenye busara katika Kamati Kuu ya CCM ni jinsi gani sharti hilo liwepo katika ngazi ya taifa peke yake huku kwenye matawi, kata hadi wilayani wanachama wa Umoja wa Vijana wenye umri wa zaidi hadi miaka 34 wakiwa wamegombea uenyekiti na nafasi nyingine za kuchaguliwa katika ngazi hizo na kushinda.
Wakashindwa kujibu swali la kama uchaguzi huo katika ngazi hizo zote nchini kote ufutwe na kuanza upya au kama sharti hilo la dharura lilikuwa ni maalum kwa ajili ya mtu mmoja, hivyo ikaamuliwa kuwa kanuni hiyo ya uchaguzi ianzie uchaguzi mkuu wa UVCCM unaofanyika mwaka huu kwa sababu ilichelewa kuletwa.
Hata hivyo, wale waliokuja nayo mwaka 2003 wakiwa na umri wa miaka 26 hivi leo wanasaga meno kwa vile tayari wana umri wa miaka 31, ule ambao kama walivyotaka iwe mwaka huo hivi sasa hawana sifa ya kuwania uongozi wowote katika UVCCM.
Hata madai kuwa Dk. Nchimbi ni mmoja katika kile kinachoitwa ni kundi la wanamtandao linaloaminika kuwa kinara wa siasa za kuchafuana na kupakana matope nao pia ni uongo mwingine.
Wanasiasa dhaifu ndani na nje ya CCM ndio wanaeneza uvumi huo, lakini hawataki kabisa kuzungumzia ukweli kuwa kinachowakera wengi akiwemo Irene na wale wanaomtuma kuonyesha ujinga wake ni ubora wa mikakati ya wana CCM waliokuwa wakimuunga mkono aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Jakaya Kikwete katika harakati zake za kuwania uteuzi wa kugombea urais mwaka 2005.
Katika mbio hizo, jumla ya wana CCM 11 walichukua fomu za kuwania nafasi hiyo. Mbali na Kikwete, wengine waliojaribu bahati zao ni Mzee John Malecela, Frederick Sumaye, Salim Ahmed Salim, William Shija, Idd Simba, John Shibuda, Ali Abeid Karume, Abdallah Kigoda, Mark Mwandosya na Patrick Chokala.
Hivyo, idadi hiyo ilisababisha kuwe mitandao 11 ya kusaka wadhifa huo, lakini unaong'ang'aniwa na waandishi wenye chuki zao wenyewe ni mtandao wa Kikwete utadhani Mwandosya, Malecela, Sumaye, Kigoda au Salim Ahmed Salim hawakuwa na ya kwao.
Inaeleweka kuwa Mei 3, 2005, mitandao yote hiyo iliishia hapo baada ya Kikwete kuteuliwa kuwa mgombea urais, lakini wajinga wa kufikiri na wale wenye chuki zao bado wanaeneza majungu dhidi ya viongozi kama Dk. Nchimbi waliokuwa katika kundi hilo lililoshinda kwa ubora wa mikakati.
Kina Irene hawasemi hata kidogo kama Mbowe naye alikuwa na mtandao wake alipokuwa akichuana na kina Anna Maulida Komu, Hebron Mwakagenda na wengineo katika kinyang'anyiro cha kuwania uteuzi wa kugombea urais kutoka Chadema.
Hawasemi kabisa kuwa mitandao yote ya harakati hizo huishia pale mshindi anapopatikana na kubakia mmoja tu unaowaunganisha wanachama katika ujumla wao, hivyo wanachofanya wale wanaong'anga'ania kuwepo "mtandao" wa Kikwete hadi leo katika CCM na kuwahusisha wanasiasa mahiri kama Dk. Emmanuel Nchimbi wana chuki zao wenyewe!