Tangu muda mrefu gazeti la Mwananchi limekuwa likiandika kuhusu kinachoitwa mgogoro ndani ya CHADEMA limekuwa likiandika mambo mengi sana ya uongo kuhusiana na mambo mbalimbali na haswa kuhusu Kafulila na CHADEMA Kigoma Kusini.
Soma hapa;
Date::11/22/2009
Swahiba wa Zitto akimbilia NCCR
Ramadhan Semtawa
DAVID Kafulila, aliyejitoa Chadema kutokana na kuondolewa kwenye sekretarieti ya chama hicho, amejiunga rasmi na NCCR Mageuzi ambayo ina ngome kubwa kisiasa kwenye jimbo la Kigoma Kusini, ambako amepanga kuwania ubunge mwakani.
Kafulila, ambaye hadi sasa bado ni mshirika mkubwa wa naibu katibu mkuu wa Chadema, Zitto Kabwe, alijitoa kwenye chama hicho wiki iliyopita kutokana na kile alichokieleza kuwa ni kunyimwa haki ya kuchaguliwa na mizengwe ya baadhi ya viongozi wa juu.
Jana Kafulila, ambaye alikuwa ofisa habari wa Chadema, alitangaza uamuzi wake akisema: "Nimejiunga NCCR kutokana na dhamira yangu binafsi, kupokea ushauri kwa watu ninaowaamini na kuwaheshimu pamoja na wapigakura wangu."
"Huu ni wakati wa kufanyakazi ya siasa, si kupiga kelele na malumbano. CCM imeshindwa kuongoza nchi kwa hiyo kazi iko kwetu ili tuweze kuingia kwa wingi bungeni."
Kafulila, akiwa na mwenyekiti wa NCCR, James Mbatia na mkuu wa idara ya haki za binadamu na sheria, Dk Sengodo Mvungi, alisema hata waliompa ushauri, walimweleza kuwa dhamira yake itatimia akijiunga na NCCR.
"Walionishauri ni watu ninaowaheshimu... nilijiridhisha na ushauri wao na walinihakikishia kuwa njia sahihi ya kutimiza ndoto ya kile ninachokiamini ni kuingia NCCR."
Takwimu za matokeo ya uchaguzi wa serikali za mitaa uliofanyika Oktoba, zinaonyesha kuwa NCCR ni chama chenye wafuasi wengi katika jimbo la Kigoma Kusini ikifuatiwa na Chadema.
NCCR inashikilia vijiji 11 ambavyo vingi viko katika tarafa ya Nguruka ambayo ina asilimia 40 ya wapigakura wote katika jimbo hilo huku Chadema ikiwa na vijiji 12 eneo la mwambao wa Ziwa Tanganyika likiwa na wakazi wachache, lakini nguvu hiyo pia ikielezwa kutokana na ushawishi na juhudi binafsi za Kafulila.
Kafulila alisema wapigakura wa jimbo hilo walimweleza kupitia viongozi mbalimbali kwamba maamuzi yaliyokuwa yakifanywa dhidi yake ni hujuma.
Alifafanua kwamba wapigakura hao walimuwekea bayana kwamba hata afanyiwe nini, hawatasita kumpa kura katika uchaguzi wa ubunge mwakani.
Kafulila aliongeza kwamba angependa ndoto yake itimie kwa vyama vya upinzani kujizolea viti vya ubunge katika uchaguzi mkuu ujao ili viweze kufanya maamuzi mazito ndani ya Bunge.
"CCM imeshindwa kutuongoza, wengine wanasema afadhali ya mkoloni. Mwaka 1959 watu waliokuwa wameunganishwa na kupata umeme ilikuwa ni asilimia 15 sasa hivi imeshuka, mwaka 1974 takwimu za idadi ya watu wasiojua kusoma ilikuwa ni asilimia 10 mwaka 2007 ilifikia asilimia 30,"alifafanua Kafulila.
"Ndiyo maana, ningependa kuona siku NCCR inapata viti 30 vya ubunge, Chadema nayo labda viti 30, CUF nayo pia... hapo tutakuwa na nguvu ya kufanya maamuzi bungeni."
Alisema mapungufu hayo yanaonyesha umuhimu mkubwa wa vyama kufanya kazi ya siasa na kuacha kupiga kelele na akaongeza: "Kukosoana ndani ya vyama ni jambo zuri kwani linalenga kutupa nafasi ya kujisahihisha."
Swahiba huyo wa Zitto alitumia fursa hiyo pia kutoa ufafanuzi kwamba alijiunga katika siasa akiwa kidato cha pili mwaka 1998, na kuweka sawa rekodi akisema hakuna mtu wa makao makuu ya Chadema aliyemwingiza kwenye siasa mwaka 2005.
"Sasa anapotokea mtu akisema aliniingiza kwenye siasa mwaka 2005, sijui anakuwa anamaanisha nini; kwamba au ili uwe mwanachama ni lazima uwe makao makuu Dar es Salaam," alihoji.
Naye Mbatia alisema umefika wakati sasa vijana wenye uwezo wa kuongoza wapewe nafasi na akataka wanasiasa watende yale ambayo wanahubiri na yaliyokubaliwa katika ilani na katiba zao.
Alisema mfumo uliopo sasa unamweka kijana katika nafasi ngumu kutokana na baadhi ya watu kukataa kuwapa fursa na kuhoji, :"Kila siku vijana ni taifa la kesho, tunao viongozi wakuu humu wana miaka hata 70."
Mbatia aliongeza kwamba mfumo huo mbovu ambao unanyima fursa vijana umehamia na kutafuna hadi kambi ya upinzani nchini ambayo ilipaswa kuwa chachu ya mageuzi.
Alisema NCCR imempokea Kafulila atakuwa na uhuru wa kukosoa kwa mujibu wa katiba na taratibu za chama, katika mambo ambayo yameanishwa katika nyaraka mbalimbali za chama hicho.
Dk Mvungi alisema vyama vingi ni njia ya kufikia malengo ya kulinda uhuru wa kiuchumi na kisiasa na kuongeza kwamba, endapo mtu ataona chama fulani kinajiendesha kwa mfumo wa chama dola kama CCM, yuko huru kuhamia kwingine ili kufanya mageuzi.
Dk Mvungi aliongeza kwamba huu si wakati wa kushambulia wanaohama chama kimoja kwenda kingine, bali ni wakati wa kuhakikisha vyama vinashiriki katika mageuzi yaliyokusudiwa wakati wa kuanzisha mfumo wa vyama vingi.
Alisema ndio maana NCCR imekuwa kimya licha ya baadhi ya wanachama wake kukimbilia vyama vingine kwa kuwa kazi kubwa imekuwa ni kufanya mageuzi.
Kafulila na mwenzake Danda Juju walifukuzwa na katibu mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa wiki moja iliyopita kutokana na kile kilichodaiwa kuwa ni utovu wa nidhamu na kuvujisha siri za chama.
Hata hivyo, Zitto ameonekana kupinga uamuzi huo, akiwataka viongozi wenzake kuwa waaangalifu katika maamuzi, hasa katika kipindi hiki ambacho Chadema imetikiswa kutokana na uchaguzi wa viongozi wake wa juu.
Na leo wameandika tena uongo mwingine ,
maswali ya kujiuliza ni kama yafuatayo;
1.Je? Gazeti la Mwananchi lina masilahi gani?
2.Wanaandika kwa masilahi ya nani?
3.Wametumwa na nani?
4.Waandishi wa habari hizi kila siku ni ama Ramadhani Semtawa au Fidelis Butahwe.
5.Gazeti la Mwananchi mara nyingi limekuwa likiandika kuwa CHADEMA wana nguvu kubwa Kigoma kusini , leo wanasema ni NCCR je? wanataka kutrupeleka wapi?
Nimekuwa nikijiuliza maswali haya sana kwani linaonekana linafanya kazi maalum na haswa linapokujua suala la CHADEMA .
Wanaojua watuelimishe hapa,.