kilimasera
JF-Expert Member
- Dec 2, 2009
- 3,068
- 268
Mary Chatanda
WABUNGE na madiwani wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), jana walisusa kushiriki uchaguzi wa Jumuiya za Serikali za Mitaa Tanzania (ALAT) katika Mkoa wa Arusha.
Walifikia hatua hiyo wakipinga uwepo wa Mbunge wa Viti maalumu kupitia Jumuiya ya Wanawake (UWT) wa Mkoa wa Tanga, Mery Chatanda katika mkutano huo.
Mbunge wa Jimbo la Karatu, Mchungaji Israel Natse ambaye alitaka ufafanuzi wa Chatanda kuwepo katika kikao hicho, kwa kuwa kanuni za Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) wabunge wanaopaswa kuhudhuria kikao hicho, ni wa Mkoa wa Arusha tu na sio vinginevyo.
Hata hivyo, Mwenyekiti wa muda wa mkutano huo, Ismail Katamboi ambaye ni Diwani wa kata ya Kisongo, katika Halmashauri ya Arusha, alisema Chatanda ni mjumbe halali wa kikao hicho na kutaka shughuli za kikao hicho kuendelea.
Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya Karatu, Lazaro Massay alisimama na kumtaka Katamboi kueleza kama Chatanda ni Mbunge wa Arusha ama Tanga.
Lakini Katamboi hakutaka kujibu swali hilo kama alivyotaka Massay bali alisisitiza kuwa Chatanga ni mjumbe halali wa mkutano huo wa Alat na hakutoa ufafanuzi zaidi.
Baada ya jibu hilo, Diwani Julius ole Sekayane (CCM) ambaye alimwakilisha Meya wa Jiji la Arusha, alisimama na kuwataka wajumbe kuendelea mkutano kwa kuwa Chatanda ni mjumbe halali katika mkutano huo na anayedai kuwa sio halali amekosea.
Baada ya malumbano hayo, wabunge wa Chadema, Natse wa Karatu na Mbunge wa Arusha mjini, Godbless Lema na madiwani wote wa Chadema waliondoka ndani ya ukumbi wakisema hawako tayari kushiriki uchaguzi huo.
Natse akizungumza nje ya ukumbi, alisema Chatanda sio mjumbe halali na pili wao wanaungana na wenzao kusema kuwa hawamtambui Meya wa Jiji la Arusha Gaudence Lyimo kwani hakuchaguliwa kufuata kanuni za Tamisemi.
Mkutano huo wa Alat Mkoa wa Arusha hushirikisha wabunge wote wa mkoa, wenyeviti wa halmashauri za wilaya, wakurugenzi wa halmashauri zote na madiwani wawili waliochaguliwa na baraza la madiwani la wilaya husika.
Mkutano huo ulikuwa wa kumchagua Mwenyekiti wa Alat mkoa wa Arusha, mweka hazina, kamati ya utendaji na mbunge mwakilishi wa mkoa katika mkutano mkuu wa Alat Taifa.