CHADEMA yalia rafu upatikanaji wa Vibali vya Helikopta kwa ajili ya ziara za Viongozi wake

BARD AI

JF-Expert Member
Jul 24, 2018
3,376
8,118
Kutopatikana kwa vibali vya usafiri wa Helikopta unaotumiwa kwenye ziara za kuimarisha Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kumekwamisha ratiba ya viongozi wa chama hicho kuendelea na mikutano katika Kanda ya Nyasa.

Suala la helikopta hiyo kukosa vibali lilidokezwa wiki iliyopita na Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Paul Makonda aliyeliweka kama utani lakini akahitimisha kwa kuziagiza mamlaka zinazohusika kutoa vibali hivyo ili vyama hivyo vishindane majukwaani.

Mwenyekiti wa chama cha CHADEMA, Freeman Mbowe ambaye awali alikuwa afanye ziara hiyo kuanzia Oktoba 13 alilazimika kuahirisha hadi Oktoba 22 alipoanza akitumia usafiri wa magari lakini ilibidi asitishe tena Oktoba 24 mwaka huu kwa kinachoelezwa ni kufuatilia suala hilo kwenye mamlaka husika.

Ingawa awali ilielezwa chama hicho, kimesitisha ziara kupisha mtihani wa darasa la nne uliofanyika Oktoba 25 na 26, mwaka huu, tangu wakati huo hakuna mikutano ya hadhara inayofanyika.

Kanda ya Nyasa inajumuisha mikoa ya Njombe, Songwe, Rukwa, Iringa na Mbeya, yenye majimbo 33.

Inaelezwa baada ya Mbowe kumaliza ziara kwenye mikoa hiyo angeunganisha Kanda ya Kusini yenye mikoa ya Ruvuma, Lindi na Mtwara.

Taarifa ambazo Mwananchi imezipata kutoka vyanzo vyake ndani ya Chadema mkoani Rukwa zinaeleza tatizo hilo limemlazimisha Mbowe arejee jijini Dar es Salaam kufuatilia vibali hivyo vinavyotolewa na Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA).

“Mwenyekiti ameamua kurudi Dar es Salaam kufuatilia suala hili la vibali kwani kwa ratiba ya mikutano yetu hatuwezi kutumia magari,” alisema kiongozi mmoja akiomba hifadhi ya jina lake na kuongeza.

“Hii mikutano wanaiona kama tishio, walidhani Chadema imekufa kama walivyodhani miaka hiyo, lakini ukweli kila mmoja anaona. Kila tunapopita unaona kabisa wananchi wanataka mageuzi, sasa wanaona kutupunguza kasi ni kutunyima kutumia chopa.”

Ratiba hiyo imevurugwa kwa kile kilichoelezwa usafiri wa magari hauwezi kuwafikisha katika maneno waliyopanga kuyafikia kwa muda husika.

Ziara hiyo inayojulikana operesheni +255 ‘Katiba Mpya ilianzia Kanda ya Magharibi yenye mikoa ya Katavi, Kigoma na Tabora. Kisha Kanda ya Ziwa Victoria yenye mikoa ya Geita, Mwanza na Kagera na kisha Kanda ya Serengeti yenye Mara, Simiyu na Shinyanga.

Kwa mujibu wa ratiba ya ziara hiyo ilipangwa kuwa ya siku 21 kuanzia Oktoba 21 hadi Novemba 6 kwa kutumia usafiri wa helikopta kwa timu ya Mbowe na timu nyingine ambayo ingekuwa ya makamu wake-bara, Tundu Lissu ingetumia magari.

Ratiba hiyo, inaonyesha timu zote mbili zingekuwa zinafanya jumla ya mikutano minane hadi kumi kwa siku. Mbowe akifungua mikutano hiyo, Tunduma Mjini, Oktoba 21 alisema watafanya mikutano zaidi ya 100 kwenye kanda hiyo.

Baada ya uzinduzi huo, Mbowe na baadhi ya wajumbe wa kamati kuu ya Chadema, walianza ziara ya Kanda ya Nyasa yenye mikoa ya Songwe, Mbeya, Rukwa, Iringa na Njombe, lakini walifanya mikutano katika mikoa ya Songwe na Rukwa pekee kabla ya kusitisha.

Mmoja wa wajumbe wa kamati kuu (jina limehifadhiwa), aliliambia Mwananchi kuwa “kulikuwa na mambo mawili, tulisimamisha ziara ili kupisha mtihani wa darasa nne, tuliona si vema kuwasumbua wanafunzi kwa sababu mikutano ilipangwa katika viwanja vilivyopo karibu na shule za msingi. Ujumbe wa Mbowe ulifanya mikutano majimbo ya Songwe, Ileje, Nkasi Kusini na Kaskazini, Tunduma, Kalambo na Kwela.

“Tulisistisha kwa siku mbili, lakini ilionekana bado kuna changamoto ya kibali cha chopa, ambayo hatujapata taarifa rasmi hadi sasa. Kwa ratiba ya Nyasa si rahisi kufanya mikutano kwa njia ya gari, la sivyo tuibadilishe kabisa…,” alisema mjumbe huyo.

Mjumbe mwingine alisema Serikali inatoa vibali viwili vya chopa kutua na kingine cha kuingia ndani ya nchi. Alisema helikopta waliyopanga kutumia ilikuwa inatoka Gaborone, Botswana ilikuwa lazima iwe na kibali cha kuingia nchini.

“Serikali ilitoa vibali vyote viwili, lakini siku moja kabla ya kuanza mikutano, walifuta kibali cha chopa kuingia nchini, tulianza kutumia gari tukiamini kitarejeshwa lakini hadi sasa bado, mwenyekiti (Mbowe) amesafiri kwenda Dar es Salaam kupambania kibali,” alisema mtoa taarifa huyo.

Jana, kwa nyakati tofauti gazeti hili lilimtafuta Mbowe kwa namba yake ya simu ya kiganjani bila mafanikio.

Naibu Katibu Mkuu wa Chadema (Zanzibar), Salum Mwalimu aliyekuwa mmoja wa wajumbe kwenye msafara wa Mbowe katika ziara hiyo, alipoulizwa alijibu kwa kifupi kuwa watatoa taarifa kwa umma, kuhusu suala hilo.

“Wewe nani kakwambia hizi taarifa kwamba tunafuatalia vibali, kama kuna watu wamekwambia basi waeleze wakuthibitishie. Nyie subirini taarifa kamili tutaitoa, tunajiandaa tutaotoa taarifa kamili kwa umma,” alisema Mwalimu aliyewahi kugombea umakamu wa Rais katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2020.

Ni taratibu tu

Mwananchi lilipomtafuta Mkurugenzi Mkuu wa TCAA, Hamza Johari kujua ukweli wa hilo, alisema “sasa hayo ni masuala ya compliance (kufuata taratibu)kama vitu havijakaa sawa, kama nyaraka hazijatimia. Haombi mtu kibali akapewa moja kwa moja kama kuna vitu fulani fulani havijatimia.

“Hiyo wiki iliyopita kulikuwa na nyaraka muhimu kwetu kwa ajili ya kuangalia usalama wa chombo (helikopta). Chadema, chama au mtu yeyote ni muhimu kulinda usalama wao. Kama chomo hatujakifahamu vizuri na nyaraka muhimu kutoka nchi husika hazijatimia, hatuwezi kutoa kibali,” alisema Johari.

Johari alisisitiza ni masuala ya compliance na si vinginevyo, akisema kila kitu kikienda sawa watapewa vibali kama ilivyokuwa siku za nyuma wakiomba wanapewa.

Maelezo hayo ya TCAA na Chadema yanakuja ikiwa ni takribani siku nne zimepita tangMakonda alipogusia suala hilo, akitaka Serikali kutoa vibali kwa vyama vya siasa ili kuondoa dhana kwamba CCM inabebwa.

Makonda alitumia sehemu ya hotuba yake ya mapokezi ndani ya chama hicho baada ya kuteuliwa kuitaka mamlaka hiyo ya usimamizi wa usafiri wa anga kuipatia vibali Chadema ili waendelee na mikutano.

“Kipindi cha nyuma nilimwona kaka yangu Mbowe (Freeman), akifanya ziara kanda ya ziwa akitumia helkopta, juzi nimemwona Songwe hana helikopta, naiagiza mamlaka ya anga wampe kibali aruke na helikopta, kama hana mafuta Rais Samia Suluhu atamchangia,” alisema

“Akiruka angani tutamfuata, akienda nchi kavu tutamfuata, akiingia kwenye boti tutamfuata, atapigwa kila kona kwa sababu hoja na uwezo na utekelezaji wa ilani ya CCM hauna shaka,” alisema Makonda wakati wa mapokezi yake yaliyofanyika ofisi ndogo za CCM, Lumumba.

Akizungumzia kauli hiyo ya Makonda, Mkurugenzi wa Itifaki, Mawasiliano na Mambo ya Nje wa Chadema John Mrema alisema hawafanyi siasa kwa sababu ya hisani, bali wanafanya hivyo kwa kuzingatia sheria ya vyama vya siasa na mikutano yao inazingatia sheria hiyo.

“Tunapotumia helikopta tunachangia mapato ya Serikali kwa sababu inapoingia nchini inalipia vibali mbalimbali na kila inapotua inalipia na rubani anapoingia analipa kodi, lakini pia hata mafuta tunayotumia tunalipa kodi,” alisema Mrema.

Chopa muhimu

Mdau wa masuala ya siasa na uchumi, Kiama Mwaimu alisema matumizi ya chopa katika mikutano ya hadhara yana manufaa makubwa ikiwemo kupunguza kuchoka kwa kiongozi au viongozi wanaohutubia katika mikutano hiyo.

“Kwanza una safari kwa raha, unafanya mikutano mingi kwa wakati mmoja tofauti na magari, matumizi ya chopa yana ufanisi mkubwa wa kuwafikia watu wengi kwa wakati mmoja.

“Kinachotakiwa mamlaka husika kukaa meza moja na Chadema vitu gani vimekosekana ili vikamilishwe, hatimaye chama hicho kikuu cha upinzani kiendelee na shughuli zake za mikutano ya hadhara. Wakae na kujadiliana kwa pamoja ili kumaliza sintofahamu hii,” alisema Mwaimu.

Si mara ya kwanza

Hii si mara ya kwanza kwa helikopta ya Chadema kukwama kutokana na sababu mbalimbali.

Mwaka 2014 helikopta ya chama hicho ilizuiwa kuruka kutokana na hali ya hewa kuwa mbaya ikiambatana ukungu na wingu zito.

Kuzuiwa kwa chopa hiyo kulisababisha ratiba ya mikutano ya chama hicho kuvurugika na baadhi ya mikutano kuahirishwa.

Hata Septemba 2020 helikopta ya chama hicho ilizuiwa kwa muda wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu kutokana na masuala yaliyohusiana na vibali.

MWANANCHI
 
Wamuone Komredi Makonda

Ninachofahamu Operesheni +255 Katiba Mpya Okoa Bandari zetu ilikuwa inafadhiliwa na Baadhi ya wanaccm na alipoteuliwa Makonda jambo la kwanza aliwataka wafadhili hao wa Ufipa st waamue kubaki CCM au wahamie Chadema ndio wale wazee wa Bukoba wameogopa na Operesheni kutamatishwa
 
Bila Mkono wa Chuma ni maini tu kama ya Tetere.....

Eti chama kongwe....siasa za kitoto na za kizamani

Ruhusuni Chopa lichakaze Mbeya kila kitongoji litatuwa hata kwenye mapaa...
 
Pilau bila nyama hua hainogi.
fb_img_1684849274867-jpg.2632462


Mh. Mbowe akiangalia Hedikopta. Unamuona hawezi akaipanda, kabisaa, kwani haina kibali😁
 
Wamuone Komredi Makonda

Ninachofahamu Operesheni +255 Katiba Mpya Okoa Bandari zetu ilikuwa inafadhiliwa na Baadhi ya wanaccm na alipoteuliwa Makonda jambo la kwanza aliwataka wafadhili hao wa Ufipa st waamue kubaki CCM au wahamie Chadema ndio wale wazee wa Bukoba wameogopa na Operesheni kutamatishwa
Mmmeufyata Bwashee.....Chopa limewatisha hapo Mbeya Mjini
 
Wamuone Komredi Makonda

Ninachofahamu Operesheni +255 Katiba Mpya Okoa Bandari zetu ilikuwa inafadhiliwa na Baadhi ya wanaccm na alipoteuliwa Makonda jambo la kwanza aliwataka wafadhili hao wa Ufipa st waamue kubaki CCM au wahamie Chadema ndio wale wazee wa Bukoba wameogopa na Operesheni kutamatishwa
Mbona mchafukoge huu mzee! Mara ccm kufadhili mara wazee wa Bukoba funguka mzee inaonekana una kitu utafika mbali.
 
Itashangaza sana kama CHADEMA watakuwa walishasahau mbinu za aina hii. Vivuko ndani ya Ziwa Viktoria waliwahi kufanyiwa hivi hivi.

Na bado. Wajiandae sana kuhujumiwa kwa hali ya juu sana kadri siku zinavyozidi kusonga.

Tatizo litakuwa kama watakuwa hawakujiandaa dhidi ya mbinu mjinga za namna hii.
 
Kuna costa na fordrenger ya cdm wiki sasa iko geita, naona chopa kikwazo, halafu manju yuko usa akiongea na first year,

Labda wajaribu kumtumia nay wa mitego,
 
Badala ya kupigania Mageuzi,wanalilia kuzurura na helikopter,
Huku hela ya nauli watachukua hukohuko Ccm.
Mnaita kuna Chama mbadala hapo
 
Ccm sometime wana akili kwa geographia ya kusini magharibi kwa gari hata wilaya moja umalizi kwa siku.

Pili wananchi wengi wa milimani hawajawai kuona chopo , kutua na chopa kungeongeza mwamko kwa wananchi

CCM wakaona usiwe tabu wakatia mpira kwapani
 
Watu hawaelewi haya mambo, ikitokea hiyo chopa imepatq hitilafu ikaanguka lawama zote zitarudi kwenye mamlaka ya vibali. Iliruhusiwa vip kuruka ikiwa haina Airworthiness certifications na haijafanyiwa inspection enough.

Kingine Anga halitumiwi na Chadema pekee, Anga linatumiwa na watu wengi inatakiwa proper schedule kwa all Airmen throughout NOTAM etc kote huko kuna procedures zake.

Wasipeleke mambo kienyej enyej
 
Watu hawaelewi haya mambo, ikitokea hiyo chopa imepatq hitilafu ikaanguka lawama zote zitarudi kwenye mamlaka ya vibali. Iliruhusiwa vip kuruka ikiwa haina Airworthiness certifications na haijafanyiwa inspection enough.

Kingine Anga halitumiwi na Chadema pekee, Anga linatumiwa na watu wengi inatakiwa proper schedule kwa all Airmen throughout NOTAM etc kote huko kuna procedures zake.

Wasipeleke mambo kienyej enyej
Hata basi la kimbinyiko haliwezi kupewa kibali siku hiyohiyo. Wasubiri utaratibu.
 
Back
Top Bottom