Parabolic
JF-Expert Member
- Dec 3, 2013
- 2,843
- 3,072
Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimetangaza nia ya kuwachukulia hatua za kisheria watu wanaojitambulisha kuwa viongozi wa chama hicho bila uhalali, kikidai wamekuwa wakikibagaza chama hicho na kumkashifu Makamu Mwenyekiti wa Chadema Bara, John Heche.
Hali hiyo ilianza kujitokeza kufuatia kusambaa kwa taarifa katika mitandao ya kijamii baada ya kikao cha Kamati Kuu ya Chadema kilichofanyika mkoani Kigoma, zikidai Heche alitumia vibaya michango ya kampeni ya 'Tone Tone' kwa kujinufaisha binafsi badala ya chama.
Soma pia: Pascal Anthony: Heche ameleta Mpasuko ndani ya chama, tunajiandaa kufanya maandamano
Hata hivyo, Katibu Mkuu wa Chadema, John Mnyika, aliwahi kukanusha tuhuma hizo hadharani, akisema fedha za kampeni hiyo ziko salama.
Licha ya ufafanuzi huo, baadhi ya watu waliodai kuwa viongozi wa Chadema waliendelea kutoa matamko wakimtaka Heche ajiondoe madarakani ili kupisha uchunguzi.
Akizungumza na waandishi wa habari Agosti 2, 2026, katika makao makuu ya Chadema yaliyopo Mikocheni, jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Kanda ya Magharibi wa chama hicho, Wakili Dickson Matata, amesema watu hao si viongozi halali wa Chadema na wamekuwa wakilitumia jina la chama kwa masilahi yao ya kisiasa.
Amesema vitendo vya kufanya mikutano ya waandishi wa habari na kutoa taarifa zinazokichafua chama pamoja na viongozi wake vinapaswa kukomeshwa kwa kuwachukulia wahusika hatua za kisheria.
Amedai matukio ya watu kujitambulisha kwa uongo kama viongozi wa Chadema yamekuwa yakijitokeza katika maeneo mbalimbali nchini, ikiwemo Kanda ya Pwani na Nyasa, ambapo baadaye viongozi halali wa chama hulazimika kujitokeza na kukanusha madai hayo.
Kupitia mkutano huo, Matata pia amemshauri Heche kufungua kesi ya madai dhidi ya watu hao ili wadaiwe fidia kwa kile alichodai ni kumchafulia jina kwa tuhuma ambazo hazijathibitishwa na zisizo na msingi.
Chanzo: Mwananchi