beth
JF-Expert Member
- Aug 19, 2012
- 3,877
- 6,326
MKURUGENZI MTENDAJI WA HESLB, ABDUL-RAZAQ BADRU, PICHA MTANDAO
Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) imesema ina fedha za kutosha na hadi jana imeshapokea Sh. bilioni 186 kutoka serikalini kwa ajili ya malipo ya miezi mitatu iliyoanzia Oktoba.
Kauli hiyo imekuja ikiwa ni siku moja baada ya Mtandao wa Wanafunzi Tanzania (TSNP) kusema kama serikali haitaingilia kati kuhusu mikopo ya wanafunzi, mamia watashindwa kuendelea na masomo kutokana na kukosa haki hiyo.
Juzi, Katibu wa TSNP, Joseph Malekela, akizungumza na vyombo vya habari, alielezea kuhusu changamoto ambazo wanafunzi wanazipitia kwa sasa huku baadhi wakikosa mikopo na wengine kulipwa kwa kupunjwa.
Baada ya taarifa hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB, Abdul-Razaq Badru, jana katika taarifa yake kwa vyombo vya habari, alisema bajeti ya mikopo ya mwaka mzima wa masomo 2019/20 ni Sh. bilioni 450.
"Malipo kwa wanafunzi wote wenye sifa yamepelekwa vyuoni na ndiyo sababu ya utulivu unaoshuhudiwa vyuoni," alisema.
Badru alisema hadi jana wanafunzi wa mwaka wa kwanza waliopata mikopo kwa mwaka wa masomo 2019/20 ni 49,485 ambao wamepata mikopo yenye thamani ya Sh. bilioni 171.8.
"Idadi hii ni sawa na asilimia 74.8 ya jumla ya wanafunzi 66,164 ambao waliomba mikopo kwa usahihi katika taasisi mbalimbali za elimu ya juu," alisema.
Badru alisema kati yao, wanafunzi 698 wamepata mikopo yenye thamani ya Sh. bilioni 2.46 kupitia dirisha la rufaa.
"Kati ya wanafunzi hao 49,485 wa mwaka wa kwanza, wapo jumla ya wanafunzi 9,564 ambao ni yatima, wenye ulemavu ni 397, waliotoka kaya zinazohudumiwa na mpango wa TASAF ni 1,116 na wahitaji wengine 38,408 ambao uhitaji wao tuliothibitika baada ya uchaguzi wa maombi yao ya mkopo," alisema.
Alisema wanafunzi wote waliopata mikopo hadi sasa ni wale waliotimiza vigezo ikiwamo kuambatanisha nyaraka muhimu katika maombi ya msingi na rufaa.
Nyaraka hizo, alisema ni nakala za vyeti vya vifo vya wazazi, barua za madaktari zinazothibitisha ulemavu na barua zinazothibitisha ufadhili.
"Vigezo vingine ni mwanafunzi kuwa na udahili unaotambulika na kwa wanaoendelea na masomo wawe wamefaulu mitihani ya mwisho wa mwaka kuwaruhusu kuendelea na masomo," alisema.
Alisema uthibitisho huo ni muhimu ili kuhakikisha mikopo hiyo inawafikia walengwa tu na ambao waliokamilisha maombi yao kwa kuweka nyaraka sahihi zinazothibitishika na ambazo zitaiwezesha serikali kuwabaini wanufaika wanapomaliza masomo na kuanza kurejesha.
"Lengo la bodi ni kuhakikisha wanafunzi wote wenye sifa na ambao wametimiza vigezo wanapata mikopo kwa kuwa HESLB.
"Bodi ya mikopo inawashauri wanafunzi wote wanaokutana na changamoto mbalimbali vyuoni kuziwasilisha kwa maofisa wanaosimamia madawati ya mikopo vyuoni au menejimenti za vyuo ambao wamekuwa wakiwasiliana na HESLB moja kwa moja na kutatua changamoto hizo," alisema.
Kuhusu waliowasilisha maombi ya rufaa alisema siyo kila aliyewasilisha ombi la rufaa alikuwa na sifa.
"Si kila aliyewasilisha maombi ya rufani alikuwa na sifa. Ni kama uombaji wa mikopo, walioomba katika maombi ya msingi walikuwa 87,636 wakati walioomba vyuo na kupata nafasi za masomo walikuwa 66,154. Wengine hawakuwa na sifa hata za kupata vyuo," alisema.
Chanzo: IPP Media