nngu007
JF-Expert Member
- Aug 2, 2010
- 15,862
- 5,797
JUMATATU, NOVEMBA 26, 2012 05:29 NA GABRIEL MUSHI, DAR ES SALAAM
*Waliohusika watiwa mbaroni
*Kardinali Pengo awaasa waumini
MIGOGORO ya kidini, imeendelea kushika kasi baada ya watoto wawili waumini wa dini ya Kiislamu, kudaiwa kuchoma moto vitabu 10 vya uchambuzi wa Biblia ndani ya madhabahu ya Kanisa Katoliki la Msumi lililopo Mbezi mjini Dar es Salaam.
Tukio hilo limetokea Novemba 22, mwaka huu saa 10 jioni, wakati waimbaji wa kwaya wa kanisa hilo walipokuwa wakijiandaa kuingia kwa ajili ya kufanya mazoezi.
Akizungumza na MTANZANIA, msimamizi wa Kanisa hilo, Katekista Costantine Safi, alisema watoto hao wenye umri kati ya miaka 11 hadi 13, walichoma vitabu hivyo wakati yeye akiwa anafanya usafi nje ya kanisa.
Hawa watoto walivizia nikiwa nje ya kanisa, nikiwa nafanya usafi, wakati huo wanakwaya walikuwa wanajiandaa kuingia kanisani kwa ajili ya kufanya mazoezi, hivyo nilifungua milango ya kanisa ili waingie.
Lakini ghafla watoto hao, waliingia hadi kwenye altare (madhabahuni) na kukuta vitabu 10 vya shajara ambavyo ni vipya na vililetwa na uongozi wa kanisa kwa ajili ya kuwagawia waumini.
Kama ilivyo kawaida mbele ya kanisa huwa kunakuwa na viberiti kwa jili ya kuwashia mishumaa, kwa maana hiyo walitumia viberiti hivyo kuchoma moto vitabu hivyo.
Badaa ya baadhi ya wanakwaya kuanza kukaribia kuingia ndani, watoto hao walikimbilia barabarani na kujichanganya na makundi ya vijana waliokuwa wakienda kucheza mpira, lakini kwa kuwa tayari walikuwa wameshabainika na kuanza kukimbizwa na wanakwaya hao, tuliweza kuwakamata na kuwapeleka katika Ofisi ya Serikali ya Mtaa wa Msumi.
Hata hivyo, Ofisa Mtendaji wa Mtaa huo, alitushauri kuwa suala hili tulipeleke polisi kwa kuwa ni kubwa, tuliandikiwa barua ya maelezo, tukaiwasilisha kwa Paroko wa Kanisa letu Father Anthony, ambaye alitushauri tuonane kwanza na wazazi wa watoto hao ili tuwasamehe.
Ndipo tukaenda kwa wazazi wa watoto hao, ambapo mzazi wa kwanza ni Ismail Sadick na wa pili Ismail Said, tuliwaeleza tukio hilo, lakini tukawaambia tumewasamehe watoto hao ambao ni wanafunzi wa Shule ya Msingi Msumi, wakafurahi na kuunga mkono hatua hiyo.
Tuliona ni vyema tutoe taarifa kwenye uongozi wa jimbo, ambapo tulienda kuonana na Askofu Msaidizi wa Jimbo la Dar es Salaam, Eusebius Nzigirwa, alitushauri tutoe taarifa polisi.
Askofu wa Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Mwadhama Policarp Kadirnali Pengo ameshauri hivyo hivyo ili yasije yakazuka mengine makubwa zaidi.
Tulienda kuripoti na kupewa RB namba MKB/RB/918/2012 ya Novemba 23, mwaka huu, alisema.
Baadhi ya waumini, walidai kumekuwapo na kikundi cha waumini wa dini ya Kiislamu, ambao wanadaiwa kutoa fedha kwa vijana wanaowatuma kuharibu mali za makanisa ya Kikristo.
Ingawa hapa kwetu hatuna uhasama kabisa na hawa wenzetu, tumeshindwa kuelewa kwa nini wametufanyia hivi kwa sababu kwanza vitabu hivi ni vipya na vimenunuliwa kwa gharama kubwa ya zaidi Sh 200,000.
Pia tumeshaanza kupatwa na wasiwasi, kwa sababu tumesikia kuwa kuna kikundi cha Waislamu kinafadhili vijana, wanaotumwa kuharibu mali za madhehebu yetu, inasemekana wanalipwa kati ya Sh 100,000 na kuendelea, hivyo tunatoa wito kwa Serikali kuwa makini katika kushughulikia masuala haya ili yasije yakazua mgogoro mkubwa zaidi, alisema mmoja wa waumini wa kanisa hilo.
Hili ni tukio la pili kubwa kutokea, baada ya lile lilitokea Mbagala ambapo inadaiwa mtoto wa muumini wa dini ya Kikristu, alikojolea Quaran na kuzua mtafaruku na vurugu ambazo zilizimwa na jeshi la polisi.