HATUA ya kufutiwa uanachama huwa haieleweki vizuri kwa watu wengi. Kuna mambo mengi ya kufanya pale unapofutiwa uanachama.
Unaweza kukaa kimya. Ukakubali kuondoka katika chama na hata ukaanzisha chama chako au kujiunga na chama kingine.
Unaweza kukaa kimya na ukaendelea kufanya mambo ambayo yanaweza hata kukisaidia chama ambamo umetimuliwa na hata vyama vingine. Ukapata umaarufu kufikia hatua ya waliokufuta uanachama kuanza kukuchumbia.
Unaweza kusahau shughuli zote za vyama vya siasa. Ukang'ang'ania eneo ulilosomea, ulilopenda, unalofahamu fika; na kujisimika kikamilifu. Hapa waweza kutumia uzoefu wako katika shughuli za siasa, kujenga mtazamo mpya juu ya mwenendo wa mambo katika jamii. Kama ni mwalimu, mchumi, mwanasheria, mwandishi wa habari, mfanyabiashara, mchuuzi/mjasiriamali au hata mkulima au mfugaji, waweza kutumia kile ulichochuma katika mienendo ya siasa, kutolea mifano ya kuleta mabadiliko katika jamii.
Unaweza kwenda mahakamani – ukashitaki waliokuvua uanachama; na unaweza kushinda. Tatizo la kushinda mahakamani, katika siasa, ni kama kushindwa. Hii ni tofauti na kudai fedha. Unaweza kushinda na kujifariji kuwa umeonyesha jinsi ya kujipigania; lakini huwezi kushinda mahakamani na kurudi kufanya kazi za siasa na wale waliokuvua uanachama.
Unaweza kujiuzulu uanachama kabla hawajakufukuza; na bila kelele wala mikwaruzo. Hili nalo lina heshima yake hasa unapokuwa umeamua kuachana na malumbano na kukashifiana. Hatua hii inafanana kimya kinene na inaendana na eneo Na. 2 hapo juu, ambako unabaki katika jamii na sura yako ileile lakini ukiwa ‘ubongo rejea' kwa kila anayehitaji msaada wako.
Unaweza kuamua kujiua kisiasa, kijamii na kitaaluma; na wakati mwingine kiuchumi – kwa kujiingiza katika minyukano ya gharama kubwa – na wale unaowaita ‘wabaya' wako. Muda wako, fikra zako, rasilimali zako, hadhi na sura yako vinaweza kuteketea kwa mafao haba au bila mafao yoyote.
Unaweza kujiunga na wapinzani wakubwa wa chama chako ambamo umevuliwa uanachama. Ukatumika kwelikweli kukisema vibaya chama chako cha zamani. Ukapewa ujira mkubwa, ukabebwa juujuu na hata kuteuliwa kuwa mtu mkubwa katika siasa nchini mwako. Ukajiliwaza kwamba ‘afadhali nimewakomoa!'
Baada ya muda mfupi ukajizika mwenyewe. Mifano ya aina hii ni mingi Tanzania, hasa kwa wale waliochomoka/chomolewa kutoka upinzani na kuingia CCM wakitamba kuwa wana ‘siri' za upinzani wakati ni ama ulafi au njaa yao binafsi.
Uwanja ni mpana kwa wanasiasa wa kweli na wababaishaji; na kila uamuzi unaochukuliwa; kila mkondo unaochaguliwa una athari zake – mbaya au nzuri. Bali hakuna ramli. Ni kukaa na kufikiri, hasa kwa wale walioamua kwa dhati kwamba wanataka kutumikia siasa. Bali kwa wale ambao hawakujua tofauti kati ya siasa za vyama na uana-harakati, watateseka sana kabla hawajapata MSHAURI.
Katika mazingira ambamo siasa zinagusa maisha ya kila mtu kupitia mifumo – sera, sheria, kanuni, uamuzi mbalimbali – uwakilishi baraza la madiwani au bungeni, au uteuzi ikulu au kwingine kwenye madaraka; si njia pekee ya kufanya siasa. Hata wanaokana siasa ndio wanafanya siasa pevu ya kukana siasa bila mafanikio.
Makala hii imeandaliwa na Ndimara Tegambwage, ipo kwenye gazeti la Tanzania Daima la tarehe 8 Jan 2014.
Unaweza kukaa kimya. Ukakubali kuondoka katika chama na hata ukaanzisha chama chako au kujiunga na chama kingine.
Unaweza kukaa kimya na ukaendelea kufanya mambo ambayo yanaweza hata kukisaidia chama ambamo umetimuliwa na hata vyama vingine. Ukapata umaarufu kufikia hatua ya waliokufuta uanachama kuanza kukuchumbia.
Unaweza kusahau shughuli zote za vyama vya siasa. Ukang'ang'ania eneo ulilosomea, ulilopenda, unalofahamu fika; na kujisimika kikamilifu. Hapa waweza kutumia uzoefu wako katika shughuli za siasa, kujenga mtazamo mpya juu ya mwenendo wa mambo katika jamii. Kama ni mwalimu, mchumi, mwanasheria, mwandishi wa habari, mfanyabiashara, mchuuzi/mjasiriamali au hata mkulima au mfugaji, waweza kutumia kile ulichochuma katika mienendo ya siasa, kutolea mifano ya kuleta mabadiliko katika jamii.
Unaweza kwenda mahakamani – ukashitaki waliokuvua uanachama; na unaweza kushinda. Tatizo la kushinda mahakamani, katika siasa, ni kama kushindwa. Hii ni tofauti na kudai fedha. Unaweza kushinda na kujifariji kuwa umeonyesha jinsi ya kujipigania; lakini huwezi kushinda mahakamani na kurudi kufanya kazi za siasa na wale waliokuvua uanachama.
Unaweza kujiuzulu uanachama kabla hawajakufukuza; na bila kelele wala mikwaruzo. Hili nalo lina heshima yake hasa unapokuwa umeamua kuachana na malumbano na kukashifiana. Hatua hii inafanana kimya kinene na inaendana na eneo Na. 2 hapo juu, ambako unabaki katika jamii na sura yako ileile lakini ukiwa ‘ubongo rejea' kwa kila anayehitaji msaada wako.
Unaweza kuamua kujiua kisiasa, kijamii na kitaaluma; na wakati mwingine kiuchumi – kwa kujiingiza katika minyukano ya gharama kubwa – na wale unaowaita ‘wabaya' wako. Muda wako, fikra zako, rasilimali zako, hadhi na sura yako vinaweza kuteketea kwa mafao haba au bila mafao yoyote.
Unaweza kujiunga na wapinzani wakubwa wa chama chako ambamo umevuliwa uanachama. Ukatumika kwelikweli kukisema vibaya chama chako cha zamani. Ukapewa ujira mkubwa, ukabebwa juujuu na hata kuteuliwa kuwa mtu mkubwa katika siasa nchini mwako. Ukajiliwaza kwamba ‘afadhali nimewakomoa!'
Baada ya muda mfupi ukajizika mwenyewe. Mifano ya aina hii ni mingi Tanzania, hasa kwa wale waliochomoka/chomolewa kutoka upinzani na kuingia CCM wakitamba kuwa wana ‘siri' za upinzani wakati ni ama ulafi au njaa yao binafsi.
Uwanja ni mpana kwa wanasiasa wa kweli na wababaishaji; na kila uamuzi unaochukuliwa; kila mkondo unaochaguliwa una athari zake – mbaya au nzuri. Bali hakuna ramli. Ni kukaa na kufikiri, hasa kwa wale walioamua kwa dhati kwamba wanataka kutumikia siasa. Bali kwa wale ambao hawakujua tofauti kati ya siasa za vyama na uana-harakati, watateseka sana kabla hawajapata MSHAURI.
Katika mazingira ambamo siasa zinagusa maisha ya kila mtu kupitia mifumo – sera, sheria, kanuni, uamuzi mbalimbali – uwakilishi baraza la madiwani au bungeni, au uteuzi ikulu au kwingine kwenye madaraka; si njia pekee ya kufanya siasa. Hata wanaokana siasa ndio wanafanya siasa pevu ya kukana siasa bila mafanikio.
Makala hii imeandaliwa na Ndimara Tegambwage, ipo kwenye gazeti la Tanzania Daima la tarehe 8 Jan 2014.