Josephat Isango
ILIKUWA ni kama mzaha, lakini sasa ni kweli. Ilikuwa ni kusimuliwa kuwa yanatokea nchi jirani, lakini sasa yanatokea kwetu, tulizoea kusimuliwa lakini sasa tunayaona wenyewe na kushuhudia.
Tuliwaonya wengine sisi tukajisifu, sasa sisi tutaanza kuonywa na kuonyana sisi kwa sisi. Ilikuwa mbali sana lakini sasa ni karibu tena ndani ya nchi. Ilikuwa ndoto sasa ni uhalisia, ilikuwa ni mambo ya kusadikika sasa yanaonekana. Umetufikisha hapa kwanini Rais Jakaya Mrisho Kikwete?
Yawezekana tulikuwa tunafikiri ni utani, lakini sasa mzaha mzaha mbwa anaingia msikitini, mzahamzaha tunaanza kutumbuka usaha.
Tuliandika, tukarudia tukaonekana tunaandika uchochezi pale tulipoionya serikali. Serikali yetu inayosemekana ni sikivu haikutusikia. Tumefika pabaya, tulishasema hayo, tukapuuzwa, lakini sasa wametufikisha tupo katikati tunaogelea katika nchi isiyo na sheria, au kama ina sheria basi utekelezaji wake unategemea wewe ni nani? Upo wapi na unafahamiana na nani?
Tulipoandika kuhusu ukweli tulikejeliwa. Kwa huzuni kabisa, mbele ya Mungu na malaika, nakumbuka kiongozi mmoja wa serikali, tena mkubwa tu, alipoona nimeandika maovu yake kwa ukweli wote, aliniita ofisini kwake na kunipa ‘kavu kavu'.
Kwa ujasiri bila woga, bila aibu, bila kujali umri wake na umri wangu, bila kujali masilahi mapana ya Watanzania tunaowatetea aliniambia hivi. "Isango, kuandika utaniandika sana, ila ukumbuke Watanzania watasoma siku moja, siku ya pili Watanzania watafungia nyama hilo gazeti, na siku ya tatu kipande kilichobaki watu watachambia, siku ya nne watasahau kabisa na huna lolote la kunifanya".
Kauli hii inaumiza sana kwa kila mtu mwenye dhamiri iliyo hai. Bahati mbaya tulipoandika kuhusu serikali, tulionywa, tukakejeliwa, na bahati mbaya wenzetu wengine wamepigwa mapanga, wakatishiwa na wengine magazeti yao yakafungiwa yote haya ni kusaidia tusiseme ubaya wa serikali au kuanika maovu yao.
Bungeni Dodoma, Mbunge wa Ubungo (CHADEMA), John Mnyika, alitamka maneno haya: "Tumefika hapa kwa sababu ya udhaifu wa Rais Jakaya Kikwete, kwa uzembe wa Bunge na kwa sababu ya upuuzi wa CCM." Badala ya kauli hiyo kuchukuliwa kuwa ni changamoto tuifanyie kazi, tulikimbilia kumwomba afute kauli, kwa tafsiri za ‘kitoto'' kuwa amemtukana rais. Lakini je, uongozi wa Kikwete ni imara? Kama ni imara kwanini tumefikia hapo kama yeye hakukusudia kutupeleka huko?
Kwa uongozi wa serikali iliyo thabiti, nani alitegemea tuanze kuchomeana nyumba za ibada kuzivunja na kuiba vifaa na samani zake? Kama serikali ingekuwa imara unadhani watu wangeweza kujipanga wakasema hadharani maovu wanayokusudia kuyafanya?
Kwamba mikakati inapangwa, sirini mfano kususa sensa, mikakati inakuja kutangazwa redioni, wanaweka mabango kuwa sisi hatutafuata sheria, wanatekeleza hadharani kutofuata sheria, mnawakamata waliokataa kutii sheria, mnawaacha walioshawishi, mnaacha redio inayoshawishi watu wasifuate sheria, redio inayokashifu imani za wengine, redio na televisheni inayofundisha watu kuchoma nyumba za ibada za dini nyingine imeachwa tu, na watu wa mamlaka ya mawasiliano (TCRA) wapo tu, polisi wapo tu na watu wa usalama wapo. Hapa ndipo Kikwete alitaka tufike?
Tumefika mahali ambapo tukitaka kuandika idadi ya makanisa yaliyochomwa moto au kuvunjwa idadi yake inahesabika, idadi inatisha, lakini idadi hiyo ipo kwenye takwimu, tunahesabu vitendo vya uchomaji makanisa huko Zanzibar, Mwanza, Mdaula, Mto wa Mbu, Tunduru, Rufiji, Kigoma Mbagala na Yombo . Ni idadi ya uvunjaji wa makanisa isiyo na wavunjaji.
Tangu makanisa yaanze kuchomwa kuna kesi ngapi mahakamani na watuhumiwa wangapi wamehukumiwa kwa kosa hilo? Kama hawahukumiwi wataachaje kuendelea kuchoma? Kama hawahukumiwi wataachaje kujiimarisha hadi kuwachinja polisi? Huku ndiko Kikwete umetufikisha bila kutarajia lakini asante, historia itakuhukumu.
Tumefika pale ambapo magazeti yanayoandika ukweli yanafungiwa na yale yanayoandika uongo yanaweza hata kusaidiwa ili yajiendeshe ikiwezekana yagawiwe bure kwa kusaidia kusambaza habari za uongo.
Tunaweza kujiuliza MwanaHalisi lilifungiwa kwanini? Kati ya MwanaHalisi na serikali nani anachochea chuki za wananchi? Ikulu inakanusha kitu gani? Ikulu inakanusha kuwa Abeid Ramadhani Ighondu si mfanyakazi wake? Tangu atajwe kwanini hajawahi kuhojiwa? Kama tumefika katika wakati ambao Ikulu inahusishwa na mauaji Hatuponi! Tulidhani utani lakini sasa tumefika, ukijitia kidomodomo, ukijitia kuandika andika kama ninavyofanya mimi, basi utakuwa rehani kama MwanaHalisi.
Asante sana Rais Kikwete, umetufikisha mahali ambapo wizara zetu zinaweza kuvamiwa mchana kweupe na kushinikiza kuachiwa kwa watuhumiwa wa uhalifu na polisi kweli wakawaachia watuhumiwa kwa hofu ya wanaharakati wa dini, tena kwa muda ambao wanahitaji wao iwe ni kwa kufuata utaratibu au la.
Kama Wizara, tena ya Mambo ya Ndani inaweza kuvamiwa vile, tuna ulinzi gani sisi kwenye nyumba zetu za ibada ambako hatuna mabomu, bunduki wala fimbo? Kikwete ameyaona haya, akayapalilia, sasa yanatugharimu. Asante sana Kikwete, umetufikisha ulipokusudia.
Tumeshuhudia vituo vya polisi vikichomwa moto; mahakama zikilazimishwa kufunga shughuli zake, misikiti ikitekwa, wanaoteka misikiti wanajiita wanaharakati, na sisi tunaendelea kuwatunuku jina hilo pamoja na tabia haramu inayohatarisha usalama wa nchi, Kikwete umeyaona hayo?
Uhai wa viongozi wa dini ukitishiwa hadharani, Mufti wa Tanzania anatishiwa hadharani, anapangiwa siku za kuwepo madarakani, lakini serikali ya Kikwete ipo, wanaomtishia Mufti wapo Dar es Salaam, na Kikwete yupo Dar es salaam.
Kwa aibu kabisa tukashuhudia kiongozi mstaafu wakizabwa vibao hadharani kwa sababu ya zinazoitwa harakati za kidini. Mzee wetu Mwinyi alizabwa, hatuoni hatua zozote zilizochukuliwa dhidi ya mtuhumiwa. Ikaonekana ni suala la uanaharakati. Kama Mzee Mwinyi, Rais Mstaafu anachapwa vibao, usalama wa baba zetu ambao hawajawahi kuwa hata mabalozi wa nyumba kumi uko wapi? Kikwete unatupeleka wapi?
Wanafalsafa lazima tuwasaidie watu kuhoji, tunasema wanaharakati hawa wavamie nini ndipo hatua zichukuliwe? Je, mpaka wavamie Ikulu? wanaharakati hawa wachome nini ndipo viongozi wenye dhamana ya kulinda mali na uhai washtuke? Mpaka wachome nyumba ya Said Mwema ndio serikali ishtuke? wanaharakati hawa wamuue nani ndipo iaminike kuwa watu hawa ni tishio kwa usalama wa taifa letu?
Kwa nini dhana ya kuua watu sasa inatajwa kuwa ni moja wapo ya kashfa za Ikulu? Dk. Ulimboka Stephen wiki iliyopita ametamka wazi kuwa aliyehusika na kutekwa, kupigwa, kusukumizwa kwenye gari, kunyofolewa kucha na meno, aliyefanya yale ni ofisa wa Ikulu.
Iwe alikuwa ametumwa au amejituma, lakini Ikulu hadi sasa haijatoa ruhusa kwa ofisa huyo kuhojiwa. Ikulu ingesema kama labda wana ugomvi upi na Dk. Ulimboka mpaka aseme kuwa aliyemtesa ni wa Ikulu? Pamoja na hayo yote, Kikwete kimyaa…. sawa, tunaendelea na safari, muda si mrefu tutafika unapokusudia kutupeleka.
Rais Kikwete umetufikisha mahali ambapo Jeshi la Polisi linaua kwa makusudi, au kutoa amri za kulipiza kisasi kwa kuua wananchi lakini upo kimya. Hivi ndivyo unavyotaka utawala uwe? Kwanini umetufikisha huku? Au kuna kauli nyingine hauzisikii? Lakini mbona Rais Kikwete si kiziwi? Kweli kuna mengine huyaoni?
Kauli ya Manumba kuwa polisi walipize kisasi uliipokeaje? Unasubiri ilete madhara tuje kuanza kutumia nguvu kama unazohitaji sasa kumdhibiti Ponda na Wana Uamsho waliodanganywa na mafisadi kuchoma makanisa? Unasubiri kauli ya kulipa kisasi ilete madhara ndipo tuanze kuombana radhi baada ya ndugu zetu kuuawa? Kwanini Kikwete unatufikisha huku.
Na sisi tunaopelekwa hebu tusimame tujiulize, huku ndiko tulikubaliana kwenda wakati tunamwambia Kikwete awe kiongozi? Kama hatukukubaliana mbona anatuleta na sisi tunakubali tu? Ni pagumu hapa, nahitaji majibu ya kifalsafa. Tukubali au tukatae, Kikwete anajua kwanini ametufikisha huku.
Source: Tanzania Daima
My take: Watanzania tuwe makini na Rais ambaye UVCCM-Pwani walisema Kikwete atatuchagulia. Watanzania tufunguke tulipofikishwa hatukustahili hata kidogo