Hoja muhimu kuliko zote, hata kama hati ipo, je, lipo wapi azimio la baraza la mapinduzi kuidhinisha muungano? Kama halipo zanziba hawakuridhia muungano kihalali
Kutokana na mvutano huu, gazeti hili [Mwananchi] limefanya mahojiano maalumu na aliyekuwa Katibu wa Baraza la Mapinduzi mwaka 1964, Salum Rashid ili kupata ufafanuzi wake juu ya jambo hilo hasa baada ya Katibu wa Bunge la Tanganyika, Pius Msekwa kueleza anayojua kuhusu suala hilo.
Swali: Ni changamoto zipi hizo ambazo tangu mwanzo, zilionekana?
Jibu: Kuna mengi, lakini kikubwa ilikuwa ni usiri wa jambo hili, kwani mimi kama Katibu wa Baraza la Mapinduzi sikujua ila hili la Zanzibar kumezwa tangu wakati huo lilionekana.
Swali: Je, kidogo una ufahamu ilipo Hati ya Muungano? Kuna ambao wanasema ipo Umoja wa Mataifa, wewe unasemaje kwani ulikuwa kiongozi wa Serikali wakati huo?
Jibu: Ninachokumbuka ni kwamba hati haikupelekwa Umoja wa Mataifa (UN), bali kilichopelekwa ni taarifa ya ya kuungana Tanganyika na Zanzibar.
Swali: Katika Bunge linaloendelea sasa kuna mijadala mingi imeibuka kuhusiana na hati ya sheria ya Zanzibar kuridhia Muungano je, una taarifa gani juu ya hati hii?
Jibu: Hati ya Sheria ya Zanzibar Presidential Decree kukubali Muungano, hiyo haipo na wala wasihangaike kuitafuta.
Swali: Kuna hati ya sheria namba 22 ya mwaka 1964, ilisainiwa kwa upande wa Tanganyika na Rais wa Tanganyika wakati huo, Hayati Julius Nyerere, Katibu wa Bunge Pius Msekwa na Spika wa Bunge hilo, Adam Sapi Mkwawa, Aprili 25 mwaka 1964. Je, kwa upande wa Zanzibar hamkupata hati hii?
Jibu: Mimi kama Katibu wa Baraza sijawahi kuiona hiyo Sheria (Presidential Decree) ambayo ilipaswa kusainiwa na Rais wa Zanzibar hayati Abeid Karume na mimi. Mimi ndiye nilikuwa Katibu wa Baraza la Mapinduzi na Baraza halikuwahi kuridhia Muungano, kilichofanyika ni kupewa taarifa tu .
Swali: Je, unadhani ni kwa nini sheria hii haijasainiwa na wewe?
Jibu: Unajua haya mambo yalikuwa siri sana na kuna mambo mengi yanapotoshwa kuhusu muungano..
Swali: Je, hujawahi kuona Hati ya Muungano na wewe ulikuwa kiongozi mkubwa wa serikali wakati huo?
Jibu: Mimi niliona ile draft (rasimu) ya kwanza ya muungano na nilipoiona nikiwa na hayati Karume nilimshauri vitu vingi na tulirekebisha na baadaye ilirudi Dar es Salaam.
Swali: Je, baada ya kukamilika uliwahi kuiona tena?
Jibu: Hapana, sijaiona nilikuwapo Zanzibar wakati huo, lakini jambo hili baadaye lilifanywa siri kubwa sana, Nyerere hakutaka mtu yeyote ajue na upande wetu Zanzibar hatukupata ushauri wa kisheria hata Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar alikuwa hana taarifa, lakini Tanganyika walikuwa na ushauri wa kisheria.
Rashid: Muungano ulikuwa siri ya Nyerere na Karume - Katiba - mwananchi.co.tz