Hamasa ya uchaguzi mwaka huu iko juu sana, hivyo lolote linaweza kutokea baada ya uchaguzi. Ni vizuri wadau wa uchaguzi (wananchi, vyama vya siasa, polisi, jeshi, serikali, tume ya uchaguzi, mahakama, vyombo vya habari na taasisi mbalimbali) kuweka akiba ya vitendo vyetu tunavyofanyiana na maneno tunayosema na kuandika kwenye kipindi hiki. Tuhakikishe kuwa kila mtu anafanya, kusema na kuandika kwa kuzingatia kilichoko kwenye katiba ya nchi, sheria za nchi, kanuni na taratibu za taaluma/kazi yako na kanuni na sheria za jumuiya za kimataifa pia ili ujiridhishe kuwa uko sawa kabla ya kutenda, kusema na kuandika hasa kwenye kipindi hiki cha uchaguzi.
Tukumbuke kuwa kuna watu ambao watawaruka na kuwakana watu wengine na kuwaachia mzigo wa lawama, tuhuma, kesi mahakamani, kifungo jela, na ushahidi pale mambo mabaya (mungu pishia mbali) yatakapojitokeza kwa sababu ya uchaguzi wao ndio walioagiza yafanyike. Lakini pia tunaweza kushindwa kutazamana usoni na kushirikiana baada ya uchaguzi kumalizika kwa salama kutokana na vitendo na maneno yetu wakati wa uchaguzi.
Kila mtu afanye, eseme na aandike kitu ambacho ataridhika kuajibika nacho bila kumlalamikia mtu mwingine kuwa ndiye aliyemsababishia hayo kwa kumtuma afanye, aseme au aandike jambo kwa niaba yake ambalo ndio chanzo cha shida itakayomkabili baada ya matokeo ya uchaguzi kutoka. Kila mtu atumie taaluma yake na kanuni zake katika kumuepusha na hukumu na mateso mbalimbali ya baada ya uchaguzi, maana uchaguzi huu unaweza kuishia kwa kupelekana mahakama za ndani na nje ya nchi, kuumizana, kununiana, kulipiziana visasi, n.k. Usije ukatumika vibaya na mwisho wa siku ukabeba lawama wewe mwenyewe na familia yako huku aliyekutuma akiwa yupo salama na familia yake nchini au nje ya nchi.
Tusiwe kama maroboti wanaotekeleza maagizo bila ya kutumia weledi na taaluma. Mfano, Mh. Mwakyembe kwenye ripoti yake ya Richmond alilazimika kuweka hadharani nusu tu ya ukweli kuhusu Richmond na kubakisha nusu nyingine ambayo hutujui ilikuwa na madhara gani kwa watu wengine zaidi ya akina Lowassa. Hii inaonyesha kuwa akina Lowassa waliachiwa zigo looote la richmond na watu ambao hatujui ni akina nani. Sakata la escrow liliwakumba watu waliowekewa pesa Mkombozi bank tu na kufichwa wale waliowekewa Stanbic bank. Hii ni kusema kuwa siku zote kuwa tayari kuwajibika kwa kile ulichokitekeleza wewe kwa mikono, mdomo au kalamu yako sio kile ulichotumwa au kuagizwa na mtu mwingine, unaweza kwenda jela mwenyewe na kumuacha aliyekutuma. Kila mtu anapaswa kuilinda katiba na sheria za nchi, kama mtu atakuagiza ufanye kitu kinachokinzana na katiba na sheria kataa kukitekeleza hata kama ni boss wako. mkumbushe kuhusu katiba na sheria zinavyosema kuhusu jambo analokutaka utekeleze.