Kulikuwa na wimbi kubwa la matangazo na mauzo ya mayai ya ndege mdogo aina ya kware. Mayai yake yalisifiiwa sana na kushawishi watu wengi kuyatumia. Wapo hata walioanza na kuimarika katika ufugaji wa kware.
Mayai ya kware na ufugaji wa kware kwa ujumla vimeishia wapi?
Kama alivyoishia Babu wa Loliondo.
Tanzania tunasumbuliwa na tatizo kubwa la "uelewa mpana wa mambo ya kawaida". Kwa hiyo watu wenye nia ya kujitajirisha hutumia "ujinga" wa walio wengi kujineemesha. Wanatengeneza matatizo ya kiafya akilini mwa watu, na kisha huja na "solutions" kwa ajili ya matatizo hayo baada ya kuona wananchi wametishwa na hayo "matatizo yao".
Ushauri wangu ni kuwa sisi tulio wazazi wa kizazi kipya, tuwasisitize watoto wetu kujifunza na kuitafuta elimu pana ya maisha yao. Tusiwakomalie tu kujifunza mkondo wao wa elimu husika maana watajikutwa wanadanganywa na watu wa upande ule mwingine.
Tusisitize holistic education ili kuwakinga na wanyonyaji wa kizazi kipya kama wauza mayai ya kware, kikombe cha babu na bibi na shangazi, na wauza dawa ambapo dawa moja inaweza kutibu hata magonjwa 150 yakiwemo ya kuambukiza, yasiyoambukiza, ya virusi, bakteria, protozoa, mzio, auto-immune, n.k. Yaani magonjwa yasiyohusiana kwa namna yanavyojengeka, namna yanavyodhihirika na kuathiri mwili wala namna yanavyotibika yote unaambiwa yanatibiwa na dawa moja tu.
Tukiokoe kizazi kijacho ndipo hata taifa litapata maendeleo.