Yah: Uyoga, Vipepeo na Midoli Bunge la Watanzania

Mzee Mwanakijiji

Platinum Member
Mar 10, 2006
33,476
39,995
Bungeni-Dodoma.jpg

Ugomvi wa Kifikra: Mojawapo ya upotoshaji mkubwa uliotokea ni kuwaaminisha watu kuwa ipo haki fulani inaitwa "ya kupata habari live". Kwamba, usipopata habari "live" basi haki yako hiyo imevunjwa. Haki hii haipo mahali popote duniani, na haijawahi kutambuliwa na serikali yoyote duniani! Hakuna haki ya kupata habari "live"!


Ipo haki ya kupata na kutoa habari. Haki hii ni miongoni mwa haki za msingi za binadamu. Haki hii imeanishwa katika Azimio la Wote la Umoja wa Mataifa juu ya Haki za Binadamu la 1948 (Kifungu cha 19) ambalo nchi nyingi duniani nazo zimeikubali.


Tanzania nayo inatambua haki hii na tumeiweka Katika Katiba yetu Ibara ya 18. Haki ya kupata habari ni haki ya msingi ya binadamu, kwamba huwezi kumnyima mtu habari. Ningekuwa miongoni mwa watu ambao wamekasirika na kuja kuu kama Serikali ya Magufuli ingedai au hata kupendekeza kuwa Watanzania wasiambiwe au wasisikie kinachotokea Bungeni. Ningeungana na wengine kupinga vikali endapo angesema kuwa Serikali imeamua kuwa kuanzia sasa habari za Bunge hazitawekwa wazi kwa wananchi. HIlo lingekuwa ni kuvunja Ibara ya 18 ya Katiba na kwenda kinyume na Azimio la Umoja wa Taifa la Haki za Binadamu ambayo Tanzania ni miongoni mwa nchi zilizoliridhia.


Kama Magufuli na Serikali yake wangekuja na pendekezo kama hilo nina uhakika kesi rahisi kabisa ya Kikatiba ingeweza kufunguliwa dhidi ya uamuzi huo na kwa asilimia 100 Serikali ingeshindwa.


Binafsi naamini ipo haki kubwa zaidi ambayo inatishia Watanzania kupata habari sahihi kutoka kwa wawakilishi wao Bungeni. Wabunge wamechaguliwa na wananchi kuwawakilisha Bungeni; nii ni pamoja na kushiriki mijadala, kutoa maoni, kusimamia serikali, lakini kubwa zaidi kutunga sheria na kubadilisha sheria mbalimbali. Mbunge ambaye haendi Bungeni, au ambaye anatoka Bungeni kwa sababu tu hajapenda uamuzi fulani wa Kiti cha Spika au kupinga maamuzi fulani ya kisiasa anawanyima wananchi waliomwakilisha kupata habari sahihi - kwani akija na kuulizwa kuhusu jambo ambalo yeye hakuwepo Bungeni hawezi kutoa habari sahihi na hivyo atakuwa anawanyima wananchi haki yao chini ya Ibara ya 18 ya Katiba na chini ya Azimio la UM la Haki za Binadamu.

Ndugu zangu, kama kuna sababu ya wabunge kulumbana na kucharuka ni kuhusiana na wao kutokuwepo “live” Bungeni wakati mijadala mbalimbali inafanyika na wao kutoa mawazo au kutoa hoja na kupendekeza Sheria au Mabadiliko ya Sheria mbalimbali Bungeni. Kuna faida gani kwa wananchi kuona kinachotokea Bungeni “live” kama wale waliowatuma huko Bungeni hawapo “Live”. Mwananchi wa jimbo fulani atafurahia nini kuona Bungeni kinachofanyika “live” wakati Mbunge wa jimbo lake hayupo “live” Bungeni?

Mwananchi ambaye anamuuliza Mbunge wake kuhusu suala fulani ambalo alitakiwa awe ametolea maoni nay eye hakuwepo “live” Bungeni atafaidika nini kuambiwa kuwa ameona jinsi watu walivyozungumza kwa ukali mambo ambayo yeye hayamgusi na mbunge wake hakuwepo Bungeni? Hili ndilo jambo hasa la kulizungumzia.

Binafsi, ningekuwa na uwezo nisingejali sana hili la kuona au kutoona “live”; ningejali zaidi kile kinachofanyika “live” Bungeni hata kama mimi mwenyewe sioni kwa macho! Kwa sababu macho siyo chombo cha kuaminiwa sana kwa kukupa taarifa sahihi; vinginevyo, mazingaombwe yangekuwa yanaamini ni ukweli. Kuona tu haitoshi; tunataka tujue nini kinafanywa na wabunge wetu Bungeni.

Lakini ningeenda mbali zaidi; na ninatumaini Serikali ya Mabadiliko ya J.P. Magufuli itakuja na mabadiliko ya sheria ambayo wabunge wote watafurahia ambayo yataweka adhabu kwa wabunge watoro Bungeni. Kama wafanyakazi wengine kwenye makampuni wanapewa kiasi tu (limited) cha siku ambazo anaweza kusema alikuwa mgonjwa wabunge nao wapewe siku (na zisizidi siku saba) kwa mwaka (ambapo kikao cha Bunge kinafanyika) ambapo ataweza kutoa udhuru kuwa hawezi kuwepo Bungeni. Isipokuwa kwa Mbunge ambaye yuko mahututi amelazwa au amepewa leave na Daktari kwa muda fulani. Wengine wote watatakiwa wawepo Bungeni au kwa kila siku, saa ambayo hawapo wakati vikao vya Bunge vinafanyika “live” watakatwa kwenye mishahara yao shilingi 50,000 kwa kila saa ambayo hawapo Bungeni au kwenye vikao ambavyo wanatakiwa wawepo. Hatutaki tuone Bunge “live” tunataka tujue wabunge wako “live” bungeni – mbele ya Luninga au hata nje ya luninga!

Nje ya hapo, ni lazima tukatae sanaa za maigizo ambazo zinajaribu kuwashikisha Watanzania wanasesere na kuwaambia waimbe “mtoto, mtoto!” na wengine kweli wanadakia “ni mtoto mtoto!” ati kwa vile mdoli huyo unafumba na kufumbua macho na unacheka kwa sauti zinazotokana na spika zinazoendeshwa na betri tumboni! Wakati wa kuwalazimisha Watanzania washike vipepeo na kuimba “uyoga uyoga” umepita! Tusiwafanye watu wetu waamini haki ambazo hazipo zipo na zile haki zenyewe za msingi wasijue kuwa zipo na wanatakiwa kuzidai!

Lakini kuna kubwa zaidi; kama kweli Wabunge wanataka kulazimisha kitu fulani kifanywe na chombo cha serikali ni wao wenye jukumu la kutunga sheria na kutenga fedha kwa chombo chochote cha serikali. Kama Nape ameona kuwa ni gharama kubwa kurusha vipindi “Live” badala ya kususa na kukasirika wabunge wanaweza hata kutoa hoja ya dharura ikajadiliwa Bungeni na kuamuliwa ili Serikali ipeleke fedha za ziada kwa TBC ili irushe Bunge live. Na hata Bunge likirushwa “live” masaa 24 – wabunge wawemo au viti tu vinavyozunguka zunguka – bado Watanzania watakuwa wanadai haki yao ya kuona wabunge wao wapo Bungeni “live” na wanashiriki ipasavyo kwenye mijadala muhimu na inayogusa maisha yao.

Mengine haya ni vipepeo na uyoga tu! Sidandii hata.

MMM
 
huyu mzee na mzee mwenzie padri slaa tokea walambishwe hela za magamba na limbwata la kihaya wamekuwa kama mahayawani!we mzee usiyepiga hata kura hapa tanzania funga bakuli lako unatupigia kelele!hivi slaa bado analala sebleni kwako huko marekani?!!
 
Ohh wabunge wawepo live
lakini watanzania waoneshwe edited na recorded version sio?
kweli hapa kazi tu


Huwo ulive wa Wabunge umeanza lini? Yaani tangu lini wabunge wanaonyeshwa live mpaka leo hii iwe dhambi kubwa wao kutokuonyeshwa live?
 
Haki ya kupata habari live haakuna na wala si haki ya msingi, ila haki ni kupata na kutoa habari, sasa the boss mbona gazeti la mawio limefungiwa kama sio kufutwa kabisa?
Au mtu mzima umepotoka kidogo au ndio mambo yetu haya ya siasa za maji ya mferjini?
 
Duh..Mwanakijiji siku hizi umekuwa apologist wa CCM na serikali yake [ingawa unaweza kukataa na kunihoji ni wapi umeitetea CCM].
NN, of course siwezi kuitetea CCM bado sijapata sababu; Napenda ukweli tu. Fikiria watu wanasema "haki ya kuona Bunge live". Na wapo watu wanaamini kweli haki kama hiyo ipo! Wanalilia "haki yetu kuona live". Ama neno "haki" lina maana au halina. Na kama lina maana hakuna mahali popote haki hiyo imewahi kutambuliwa. Tatizo utaona ni kuwa wapo watu wanafikiria wapinzani wakisemana kusimamia jambo basi jambo hilo linakuwe la kweli! Sijawahi kuwa shabiki tu wa kufuata watu wanaoshabikia ati kwa sababu nikipinga nitaonekana sijafuata ushabiki.

Unafikiri kweli hiyo haki ipo kweli hadi watu wagome na kutoka Bungeni?
 
Haki ya kupata habari live haakuna na wala si haki ya msingi, ila haki ni kupata na kutoa habari, sasa the boss mbona gazeti la mawio limefungiwa kama sio kufutwa kabisa?
Au mtu mzima umepotoka kidogo au ndio mambo yetu haya ya siasa za maji ya mferjini?

Kwani limefungiwa sababu ya kutoa habari? lakini mimi ni muumini wa uhuru wa maoni na siamini katika mambo ya kufungia magazeti au chochombo chochote cha habari kwa sababu tu kimetoa maoni ambayo hatuyapendi.

Hata hivyo, ni jambo moja kutoa habari na kutoa maoni na ni jambo jingine kabisa kutoa habari ambayo si ya kweli ikawaaminisha kuwa ni kweli; hayo sasa siyo maoni na zipo taratibu za kushughulikia. Tatizo letu ni kuwa taratibu zetu zilivyo hadi sasa bado zinaishi katika ulimwengu wa vita baridi.
 
NN, of course siwezi kuitetea CCM bado sijapata sababu; Napenda ukweli tu. Fikiria watu wanasema "haki ya kuona Bunge live". Na wapo watu wanaamini kweli haki kama hiyo ipo! Wanalilia "haki yetu kuona live". Ama neno "haki" lina maana au halina. Na kama lina maana hakuna mahali popote haki hiyo imewahi kutambuliwa. Tatizo utaona ni kuwa wapo watu wanafikiria wapinzani wakisemana kusimamia jambo basi jambo hilo linakuwe la kweli! Sijawahi kuwa shabiki tu wa kufuata watu wanaoshabikia ati kwa sababu nikipinga nitaonekana sijafuata ushabiki.

Unafikiri kweli hiyo haki ipo kweli hadi watu wagome na kutoka Bungeni?

Mbona unajitoa ufahamu?
hujui kama tv haipo live itakuwa ni edited news? na edited news tayari imeshamkosesha mtu
habari kama ilivyo? huvyo kumkosesha mtu haki ya kupata habari isiyo na upendeleo au isiyopikwa?
hujui edited news yaweza kuwa ni propaganda? huku wewe mwenyewe unafanya propaganda...
 
Kwani limefungiwa sababu ya kutoa habari? lakini mimi ni muumini wa uhuru wa maoni na siamini katika mambo ya kufungia magazeti au chochombo chochote cha habari kwa sababu tu kimetoa maoni ambayo hatuyapendi. Hata hivyo, ni jambo moja kutoa habari na kutoa maoni na ni jambo jingine kabisa kutoa habari ambayo si ya kweli ikawaaminisha kuwa ni kweli; hayo sasa siyo maoni na zipo taratibu za kushughulikia. Tatizo letu ni kuwa taratibu zetu zilivyo hadi sasa bado zinaishi katika ulimwengu wa vita baridi.
Huo siyo uzee bali unaingia kwenye umatonya na sasa umeshaanza kujishushia hadhi kwa kisa tu kuvuta
 
Hata Jamiiforum tunaweza ulizana hapa imeanza lini hadi iwe dhambi kuifungia......au iwe na umuhimu


Na kwa nini JF ifungiwe? Kwani TBC imefungiwa? Nijuavyo mimi Serikali imesema Bunge litarekodiwa na kuonyeshwa jioni na kurudiwa wkend sasa sijui tatitzo liko wapi hapo?

Na hii siyo TZ peke yake nchi nyingi Duniani hata zile tunazoziiga kwa mambo ya kiutawala ambazo kila siku hulaumu Serikali yetu kwa nini haifanyi kama wao hufanya hivi kwamba Bunge huonyeshwa jioni!
 
Miongoni mwa mambo yaliyonishawishi kujiunga na JF miaka km7 iliyopita ni hoja maridhawa za Mzee Mwanakijiji. Nakumbuka ile doc ya Buhemba na scandal za EPA. Naposoma makala zake leo naona km huyu ni mtu mwingine. Je.hapa JF kuna uuzaji wa majina km vile makampuni ya magazeti yanavyouzwa?
 
Na kwa nini JF ifungiwe? Kwani TBC imefungiwa? Nijuavyo mimi Serikali imesema Bunge litarekodiwa na kuonyeshwa jioni na kurudiwa wkend sasa sijui tatitzo liko wapi hapo?

Na hii siyo TZ peke yake nchi nyingi Duniani hata zile tunazoziiga kwa mambo ya kiutawala ambazo kila siku hulaumu Serikali yetu kwa nini haifanyi kama wao hufanya hivi kwamba Bunge huonyeshwa jioni!

Hujui recorded ni edited version?
yatapunguzwa , kuongezwa na hata kutengeneza muonekano maalum..
 
Back
Top Bottom