Kama watu tunavyofahamu kwa hivi sasa, kila kona ya nchi hii, wananchi wanalalamikia makali ya maisha wanayokabiliana nayo kutokana na kupanda kwa bei ya umeme kwa asilimia 40, tokea Januari mosi mwaka huu.
Uniti moja ya umeme hivi sasa inauzwa kwa zaidi ya shilingi 300 toka bei yake ya awali ya shilingi 221, wale wanunuzi wa Luku, ambapo hapo kabla walipokuwa wanakwenda na shilingi elfu 10, walikuwa wakipata uniti 37 kama weshakatwa service charge, hivi sasa ukienda na elfu 10 hiyo hiyo mwanzo wa mwezi, unaambulia uniti 8 peke yake!!
Hata hivyo TANESCO wametoa taarifa ambayo imenukuliwa na vyombo vya habari ya kuwa wanazidai Taasisi mbalimbali za serkali yetu, kiasi kisichopungua shilingi bilioni 174!!
Sasa swali la kuwauliza TANESCO, kumbe operesheni zao zote za kata umeme huwa wanawalenga wananchi wanyonge wa majumbani wenye vibili vidogo vidogo vya shilingi elfu 10 au 20, wakati wale wadeni sugu, hususani Idara mbalimbali za serikali, kama vile majeshi ya ulinzi, Polisi, Vyuo mbalimbali vya Umma na wizara za serikali, wakizigwaya, ambapo kumbe huwa hawathubutu kuzigusa, wakati wanajua wanawadai mabilioni ya shilingi!!
Hili la TANESCO "kuwang'ang'ania" wateja wadogo wanaodaiwa "vijisenti" na kuwaacha wateja wakubwa wanaodaiwa mabilioni wakiendelea kupeta wakitumia umeme "bure" sasa hawawezi tena kulikanusha, kwa kuwa ni tamko lililotolewa na wenyewe TANESCO, na kunukuliwa na vyombo mbalimbali vya habari.
Swali lingine ambalo tungependa kuwauliza TANESCO, ni kwa nini wanapata "kigugumizi" kuyakatia umeme hayo mashirika na Taasisi mbalimbali za serikali, wakati kila bajeti ya kila mwaka, Idara hizo za serikali na Taasisi zake hutengewa bajeti maalum za kulipa bili hizo za umeme, ambapo pesa hizo ni kodi zetu sisi wananchi?!
Swali lingine ambalo tungependa kuwauliza EWURA ni kwa vipi wanabariki upandishaji mkubwa wa umeme, wakati wakijua fika kuwa, chanzo cha uzorotaji wa utendaji wa TANESCO ni uzembe wao wa kutokusanya madeni yao toka serikalini?!
Lipo swala lingine ambalo tungependa kuwauliza EWURA, ni kwa vipi wamekubali ongezeko hilo la umeme, wakati wanawaidhinishia watumishi wa TANESCO watumie umeme wa "dezo" wa uniti 750 kwa kila mwezi, kwa kila mfanyakazi wa TANESCO?!
Mimi nadhani watanzania tumeonewa kiasi cha kutosha, tumegandamizwa kiasi cha kutosha, na unyonge wetu ndiyo uliotufanya tuonewe hivyo na kugandamizwa, na sasa tunapaswa kutamka sasa BASI, hatutakuwa tayari kuonewa tena na kugandamizwa tena, na tunapaswa kuzikomesha kwa vitendo kauli za kifedhuli zinazotolewa na viongozi wetu tuliowakabidhi dhamana za kutuongoza, kama ile kauli iliyotolewa na Naibu Waziri wa Nishati na Madini, George Simbachawene, ambaye alidiriki kuwakebehi watanzania, kwa kiwango cha kutisha, pale alipotamka kuwa, wale wote ambao watashindwa kumudu bei mpya za umeme, ni bora wakawasha vibatari au wakalala giza majumbani mwao!!!