nngu007
JF-Expert Member
- Aug 2, 2010
- 15,862
- 5,797
Friday, 11 November 2011 21:20 |
Kizitto Noya,Dodoma WABUNGE wamehadharisha kwamba Muswada wa Sheria ya Ununuzi wa Umma wa mwaka 2011, utamwingiza Mkenge Rais, endapo kipengele hicho hakitaondolewa. Kipengele hicho kinamtaka kiongozi huyo wa nchi kuthibitisha manunuzi ya mbalimbali.Wakichangia Muswada huo kwa nyakati tofauti, wabunge hao walisema baadhi ya watendaji wasiokuwa waaminifu wanaweza kutumia fursa ya kumshirikisha rais, kufanya ufisadi na baadaye kashfa kubaki kwa rais aliyeidhinisha matumizi hayo haramu. Mbunge wa Kisarawe Seleman Jafu, alitaka kipengele hicho kiondolewe ili rais asihusishwe kuidhinisha manunuzi, kwa kuwa mazingira ya Tanzania, atapata kashfa ya ufisadi."Kwa kipengele hiki, kuna watu watamwingiza mkenge rais na sisi hatukubali rais wetu aingie mkenge. Watu watajenga maghorofa kwa kifungu hiki halafu rais atapata kashfa," alisema Seleman Jafu. Jafu alisema kifungu hicho kisingekuwa na tatizo endapo watendaji wote wa serikali wangekuwa waaminifu, lakini kwa historia ya Tanzania, watu watatumia saini ya rais kuhalalisha ufisadi wao. "Hapa kuna utata na tunapaswa pia kusema watu wakivunja kanuni tutawajibisha vipi, hata kama itatulazimu kutumia sheria za China. Kesho (jana) nitaleta amendment ya kifungu hiki cha kumhusisha rais kwenye sheria hii,"alisema. Jafu alisema baadhi ya watu wanaweza kutumia upungufu wa sheria, kutekeleza agenda binafsi ya kumchafua rais kwa kutumia saini yake kujinufaisha. "Wazo ni jema, lakini tatizo ni uadilifu,"alisema. Kauli hiyo ya Jafu iliungwa mkono na Subiri Mgalu, Mbunge wa Viti Maalumu (Chadema) ambaye alisema siyo vyema rais kuhusishwa kwenye suala la manunuzi badala yake kuwekwe utaratibu mwingine. "Mimi nasema tusimshirikishe rais kwenye manunuzi haya. Baraza la Mawaziri lisihusike kuidhinisha matumizi,"alisema Magalu. Mbunge wa Wawi, Hamad Rashid Mohamed alisema Muswada huo wa Sheria ya Ununuzi ya Umma ni mzuri, lakini tatizo ni jinai ya kusimamia sheria. Kikubwa ni uadilifu na uaminifu. Hapa Tanzania kuliwahi kutokea kashfa katika Shirika la Ndege la Tanzania, watu wakanunua ndege mbovu na waziri na Mkurugenzi mkuu wakapoteza kazi. Shida hiyo ya uzalendo na uadilifu bado tunayo Tanzania. Asilimia 55 ya manunuzi yanatokana na watu kutowajibika katika kusimamia sheria. Linapotokea tatizo watu wawajibishwe haraka. Tujiulize kwenye sheria hii ni kanuni gani tunatumia kudhibiti ufisadi? Mimi kwa mawazo yangu rais angehusika moja kwa moja kwenye suala hilo la manunuzi ili kuwe na udhibiti mzuri,alisema. Hamad alipendekeza njia ya kupunguza tatizo la ufisadi katika sheria hiyo mpya ya ununuzi kuwa ni kupunguza ushuru kwa vifaa vipya na kuongeza ushuru kwa vifaa chakavu. Mbunge Viti Maalumu (CCM) Diana Chilolo, alipinga wazo la kununua vifaa vilivyotumika badala yake akataka vinunuliwe vifaa vipya ili kuzuia ifisadi. Ester Matiku Viti Maalumu (Chadema) aliwataka wabunge bila kujali itikadi zao za vyama kuupinga muswada huo kwa kuwa baadhi ya watendaji serikalini hawana historia nzuri ya uadilifu. Murtaza Mangungu (Kilwa Kaskazini) alikiponda kifungu cha 66 cha Muswada huo kinachotoa fursa ya kununua vifaa vilivyotumika alisema: kipengele hiki kinahitaji kuangaliwa vizuri zaidi. Alisema pamoja na Baraza la Mawaziri kuthibitisha manunuzi hayo, ni bora kamati za bunge zikahusishwa kikamilifu ili kupunguza mwanya wa rushwa. Asumpta Mshana (Nkenge) alisema: Siungi mkono hoja ya kununua vyombo chakavu. Hatuwezi kukaa hapa watu wazima tunazungumzia kununua vifaa chakafu. Watu hawana uzalendo, watajinufaisha na kifungu hiki. Mbunge wa Mbozi Mashariki, Godfrey Zambi alipendekeza Muswada huo uboreshwe kwa sheria zake zitakazotumika ziandikwe kwa Lugha ya Kiswahili ili madiwani waelewe wanachofanya. "Ni bora sheria hizo ziandikwe kwa lugha inayoeleweka na ikiwezekana iwe kwa lugha mbili; Kiswahili na Kiingereza ili madiwani wajue wanachotaka kumshauri Mwenyekiti wa halmashauri,"alisema. Katika mchango wake, mbunge wa Iringa Mjini Peter Msigwa aliponda kifungu cha 66 cha Muswada huo kinachotaka kutoa ruhusa kwa serikali kununua vifaa vilivyotumika kwa kuwa mawazo hayo ni ya kimaskini. "Hii ni poverty mentality (haya ni mawazo ya kimaskini). And I don't understand ..(na sielewi) eti sasa tunasherehekea miaka 50 ya uhuru. Tunasherehekea kitu gani kama mawazo yetu hayataki kubadilika? "Kipengele hiki cha kununua vifaa vilivyotumika kitupiliwe mbali, tununue vitu vipya. Mawazo hayo ni sababu ya umbwe la uongozi. Dhana kwamba hatuna fedha ni umaskini. Sisi siyo maskini ila tuna mawazo ya kimaskini, hatuwezi kupanga. yaani viongozi wa CCM mmekaa ana kutafakari kununua vitu chakavu?"alihoji. Naye Waziri wa Uchukuzi, Omary Nundu aliwatoa hofu wabunge na kuwasihi waipitishe sheria hiyo ya ununuzi wa umma akiamini kwamba mambo hayatakuwa mabaya kiasi hicho. |