UTATA WA KIFO CHA RAIS JF KENNEDY
SEHEMU YA PILI
Katika sehemu iliyopita nilijadili mfululizo wa matukio yaloyopelekea kukamatwa kwa Lee Harvey Oswald na kuhusishwa na kifo cha polisi J.D Tippit na baadae kuhusishwa na kifo cha Rais JF Kennedy.
Katika sehemu hii ya tano nitajadili kuhusu utata unaozunguka uhusishwaji wa Oswald na kifo cha Kennedy na muingiliano uliopo na magenge ya uhalifu pamoja na vyombo vya ulinzi unaoonhesha dalili ya uhusika wao katika kifo cha Kennedy.
Tuendelee…
OSWALD CHINI YA MIKONO YA POLISI NA KIFO CHAKE
Baada ya Oswald kukamatwa kutoka jumba la kuonyesha sinema la Texas Theatre, moja kwa moja akapelekwa makao makuu ya polisi ya Dallas.
Akiwa hapo kituoni Oswald alihojiwa na Asifa wa FBI, Special Agent James P. Hosty pamoja na Afisa mkuu wa Polisi kituo cha Dallas Captain Will Frizt.
Oswald alikana kuhusika kabisa na mauaji yote mawili, yaani mauaji ya Rais Kennedy na mauaji ya polisi J. D Tippit.
Akajieleza kwamba siku ya tukio ni kweli alikuwa kwenye jengo la Texas School Books Depository na hakukuwa na ajabu yeye kuwepo hapo kwa kuwa anafanya kazi kwenye jengo hilo.
Akaendelea kujieleza kuwa wakati tukio linatokea alikuwa anakula chakula cha mchana kwenye ghorofa ya kwanza na hakuwa anajua kinachoendelea huko mtaani na baada ya kumaliza kula chakula akapanda mpaka ghorlfa ya pili ili kwenda kuchukua soda aina ya coca cola kwenye 'vending machine'. (Ndio hii soda ambayo nilieleza kwenye sehemu iliyopita kwamba kuna mama secretary wa jengo hilo alimuona Oswald ameibeba akiwa anatoka nje ya jengo).
Oswald akaeleza kuwa akiwa anarejea kutoka ghorofa ya pili kwenda ghorofa ya kwanza alikuta na wafanya kazi wengine wawili weusi ambao nao ni waajiriwa wa jengo hilo. Oswald aliwaeleza kumtambua mfanya kazi mmoja kwa jina la 'Junior' na mwingine hakuwa anamkumbuka kwa jina.
Polisi baadae waliwahoji wafanyakazi weusi wanaofanya kazi kwenye jengo hilo na walijitokeza wafanya kazi wawili Junior Jarman na Harold Norman ambao walikiri kwamba walimuona mtu akiwa kwenye chumba cha chakula au 'Domino Room' kama ambavyo walizoea kukiita lakini walikiri kuwa hawakuwa makini kumuangalia ni nani hivyo hawakumbuki.
Oswald akaendelea kueleza kuwa aliporejea kwenye chumba cha chakula na kuketi ili ajiburudishe na soda yake ya coca cola, ndipo ghafla alishituka anaingia polisi ambaye baadae alikuja kumtambua kama Marion Baker na kumnyooshea bastola.
Licha ya maelezo yote haya lakini bado waliendelea kumbana na kumlazisha kukiri uhusika wake kwenye kumdungua Rais Kennedy.
Walimuonyesha Picha ambayo ilionyesha Oswald akiwa ameshikilia bunduki ambayo iliaminika kumdungua Rais Kennedy.
Oswald alikanusha na kudai kuwa picha hiyo imetengenezwa.
Wakamuonyesha pia risiti za ununuzi wa bunduki hiyo kwa kutumia jina bandia la "A.J Hidell" lakini bunduki hiyo ilitumwa kwenye anuani ya nyumbani kwake.
Oswald akakanusha kufanya manunuzi hayo na kusisitiza kuwa huo ni "mchoro" kuna watu wanajaribu kumsingizia yeye shutuma hizo ili kuficha wahusika halisi.
Kitu pekee ambacho Oswald alikiri ni kumiliki bastola 0.38 revolver na alidai kuwa anaimilili kwa mujibu wa sheria na ulinzi binafsi.
Pia ikumbukwe kuwa Oswald aliwahi kutumikia jeshi la Marekani kikosi cha Marine Corps.
Oswald pia alikataa kabisa kuwakilishwa na mawakili wa utetezi qa serikali au wale ambao serikali ilikiwa tayari kumlipia kama haki yake ya kiraia, Oswald alidai kuwa hakuwa na imani na watu hao au serikali kumtendea haki kwenye suala hili.
Wakili pekee ambaye Oswald alikubali amuwakilishe kwenye mahojiano na kipindi cha kesi kusikilizwa alikuwa ni Bw. John Abt ambaye alikuwa anatokea American Civil Liberties Union.
Lakini ajabu ni kwamba kwa siku zote mbili za mahojiano ya Oswald, John Abt alikuwa hapatikani kwenye simu yake ya nyumbani wala sehemu yake ya kazi.
Sekunde chache kabla ya Lee Harvey Oswald Kuuwawa... Tazama huyo mkono wa kulia pembeni anayemsogelea Oswald na silaha huku wanausalama wakimtazama
Mahojiano ya polisi na Oswald yaliendelea kwa muda wa siku mbili mfululizo.
Siku mbili zilipopita yaani siku ya Novemba 24, 1963 vyombo vya ulinzi viliazimia kumuhamisha Lee Oswald kutoka katika mahabusu ya polisi kituo cha Dallas na kumpeleka gerezani kwa ajili ya kushikiliwa kwa usalama zaidi akisubiria mahojiano zaidi na kesi yake kuanza kuunguruma.
Muda wa saa 5 na dakika 15 asubuhi, Oswald alifunguliwa na kutolewa kwenye selo na baada ya kusainiwa kwa makaratasi yake ya kuhamishwa kutoka hapo kituoni ili apelekwe gerezani.
Saa 5 na dakika 19 Oswald alikuwa anakaribia kufika kwenye mlango wa ghorofa ya chini kabisa (basement) ili kupelekwa kwenye gari maalumu lisilopenya risasi ambalo lilikuwa linasubiri ili kumbeba na kumpeleka gerezani.
Tukio hili lilikuwa limeteka hisia za taifa zima na lilikuwa linafuatiliwa kila kona ya nchi ya Marekani na duniani kote kwa hiyo vituo vingi vya televisheni lilikuwa vinarusha tukio hili moja kwa moja, mubashara kabisa.
Saa 5 na dakika 20 polisi wawili walitoka mlangoni ili kuhakikisha usalama na sekunde chache baadae Oswald akiwa amefungwa pingu na kuzungukwa na wanausalama kila kona alitoka kwenye mlango wa jengo kuingia basement ili aweze kupelekwa kwenye gari inayowasubiri.
Oswald na maaskari waliokuwa wamemzunguka walipiga kama hatua tano tu au sita na ghafla akajitokeza mtu aliyekuwa pembeni yao amekaa pamoja na wana Habari, na mkononi mwake alikuwa ameshika bastola akiielekeza moja kwa moja kwa Oswald.
Hii lilikuwa ni saa 5 na dakika 21.
Kabla wanausalama hawajafanya lolote, mtu huyu alimfyatulia risasi ya tumboni Oswald na moja kwa moja Oswald akadondoka chini.
Wanausalama wakafanikiwa kumdhibiti mtu huyu na kumkamata na moja kwa moja wakamuingiza ndani kwenye kituo cha Polisi pamoja na Oswald.
Mtu huyu aliyempiga risasi Oswald anaitwa Jack Ruby na ni moja ya watu maarufu sana Dallas katika kipindi hicho kutokana na kumiliki Klabu kubwa ya usiku mjini hapo.
Dakika chache baadae Oswald alichukuliwa na gari ya wagonjwa na kupelekwa moja kwa moja hospitali ya Parkland Memorial Hospital (hospitali ile ile aliyofia Kennedy siku mbili nyuma).
Risasi aliyopigwa Oswald iliingia ubavu wa kushoto na ilikuwa imeenda kuharibu kabisa bandama, aorta, vena cava, figo, ini, diaphragm na mbavu ya kumi na moja ya kushoto na ikakwama katika ubavu wa kulia.
Vile vile pia baada ya "juhudi kubwa" za madaktari kuokoa maisha ya Oswald kutozaa matunda hatimaye muda wa saa 7 na dakika 7 siku hiyo ya Novemba 24, Dallas Police Chief Bw. Jesse Curry aliutangazia uliwengu kuwa mtuhumiwa pekee wa mauaji ya Rais JF Kennedy, Bw. Lee Harvey Oswald amefariki dunia.
Mara moja baada ya habari hii kutangazwa iliwafanya watu wengi waanze kukuna vichwa.
Siku mbili nyuma mara baada ya Rais Kennedy kupigwa risasi kulianza kuibuka minong'ono mitaani kwamba huo ulikiwa ni 'mchoro' wa watu wenye nguvu kwenye 'system'!
Baadae siku hiyo hiyo ilipotangazwa kuwa muuaji wa Kennedy amekamatwa, sintofahamu ikaongezeka zaidi kuwa imekuwaje mtu ambaye ametekeleza mauaji makubwa hivyo akamatwe 'kizembe' na kwa haraka namna hiyo.
Lakini ilipotolewa taarifa ya Oswald kuuwawa, huko mtaani asilimia kubwa ya wananchi wazo moja kuu lilitawala vichwani mwao, kuwa "Oswald alikuwa amenyamazishwa"! Kuna uwezekano mkubwa wahusika halisi wa kifo cha Kennedy walikuwa wanahofia kesi ya Oswald kuanza kuunguruma kwani walihofia labda Oswald "angemwaga mchele!"
Pia kilichosgangaza zaidi ni mtu aliyempiga risasi Oswald. Jack Ruby ni mfanyabiashara mkubwa, mtu mwenye 'status' hapo Dallas.
Inawezekaje mtu wa hadhi yake afanye kitu cha kipuuzi kiasi hicho kwa kumpiga mtu risasi hadharani mbele ya vyombo vya habari kwa suala ambalo alimuhusu moja kwa moja?? Ana maslahi gani kufanya hivyo??
Sasa ilikuwa dhahiri kwamba, kuna jambo kubwa zaidi linafichwa nyuma ya pazia… kuna wahusika halisi wa kifo cha Kennedy!!
Ni kina nani?? Na kwa nini walimuua Kennedy??
Hakuna mwenye majibu kamili ya asilimia mia, lakini nitajitahidi kuleta kwenu vidhibiti kadhaa ambavyo vitasaidia kila mmoja kufikia conclusion yake binafsi!!
Tazama Video jinsi ambavyo Jack Ruby alimpiga risasi Oswald mbele ya Wanausalama na vyombo vya habari
Itaendelea...
The Bold - 0718 096 811