Wanajamvi!
Tuko katika kipindi ambacho mijadala mikubwa katika maeneo mengi hapa nchini ni suala la uchaguzi mkuu na hasa katika nafasi ya urais. Inavyooneka ni kwamba mmoja kati ya Lowasa au Magufuli atashinda nafasi hii kubwa ya uongozi hapa nchini. Hii ni kutokana na mijadala na mivutano ya wengi iko juu ya hawa watu wawili.
Magufuli amekuwa akitajwa na wengi kwamba ni mchapa kazi lakini pia ni mtu anayesimamia sera na sheria lakini anatoka katika chama ambacho kwa miaka mingi kinatuhumiwa kwenye suala la ufisadi na kushindwa kuwa na vipaumbele katika suala la maendeleo ya taifa letu na mahitaji ya wakati huo. Kwa hiyo kuna watu wanaoona kuwa sasa hivi kipaumbele kiwe ni kuitoa CCM madarakani bila kujali mgombea wao ni mtu wa aina gani.
Lowasa pia amekuwa akitajwa na watu wengi kuwa ni mchapa kazi na mtu mwenye maamuzi magumu (sijayajua haya maamuzi magumu ni yapi, huenda ni kujiuzuru uwaziri mkuu ndo maamuzi yenyewe magumu). Kwa upande mwingine Lowasa amekuwa akitajwa mara nyingi sana kwa suala la ufisadi (sijui kama ushahidi upo au haupo) na hata matumizi makubwa ya pesa katika harakati za kuusaka urais. Huyu ndiye mgombea wa urais aliyesimamishwa na Chadema na hata UKAWA nzima imekubaliana. Chadema na UKAWA nzima siku zote wamekuwa msitari wa mbele kupiga vita ufisadi na kumtaja Lowasa kama Fisadi hali inayowafanya baadhi ya watu washindwe kuiamini tena chadema katika yale wanayoyasema siku zote hasa pale wanapojitokeza leo na kusema "Lowasa siyo fisadi".
Mimi ni mmoja wa watu waliobaki njia panda ya kufanya maamuzi ya "nimpigie nani kura ya urais". Naomba tujadili kwa pamoja bila ushabiki kwa masilahi ya taifa letu, kizazi chetu na kizazi kijacho; Ni lipi bora, kumchagua Lowasa na tuhuma zake zote akiwa Chama kinachopiga vita ufisadi au kumchagua magufuli ambaye hana tuhuma za ufisadi (kama anazo hazijulikani sana) lakini anatoka chama kinachotuhumiwa kwa ufisadi?