Mwanasheria Mkuu
wa Chadema, Tundu Lissu amesema
ni vigumu kuziba pengo la Dk
Willibrod Slaa kwenye nafasi ya
katibu mkuu wa chama hicho, kwa
kuwa “viatu vyake ni vikubwa”,
hivyo anahitajika mtu mwenye
uwezo wa kuvivaa na kumuenea.
Lissu alisema hayo alipoulizwa na
Mwananchi kuhusu taarifa kuwa
Waziri Mkuu wa zamani, Frederick
Sumaye atachukua nafasi ya katibu
mkuu wa Chadema iliyoachwa wazi
na Dk Slaa, ambaye alijivua
madaraka na kujiuzulu siasa za
vyama Julai mwaka jana.
Dk Slaa, ambaye alishapitishwa
kugombea urais kwa tiketi ya
Chadema, alijiondoa kwenye chama
hicho akipinga uamuzi wa
kumkaribisha Waziri Mkuu wa
zamani, Edward Lowassa na muda
mfupi baadaye kumpa fursa ya
kugombea urais.
Tangu wakati huo, nafasi ya Dk Slaa
imekuwa ikikaimiwa na Salim
Mwalimu, ambaye ni naibu katibu
mkuu wa Chadema Zanzibar.
Akijibu swali hilo, Lissu alisema
kiutaratibu, mwenyekiti wa
Chadema anatakiwa kuangalia mtu
anayefaa na kupendekeza jina lake
kwenye Baraza Kuu ambalo hufanya
uamuzi.
“Nafasi hiyo lazima ijazwe,
mwenyekiti ataangalia mambo
kadhaa, ikiwamo katibu mkuu kuwa
na uwezo wa kuweka heshima ndani
ya chama. Lazima (katibu) awe mtu
ambaye akisema kitu chama
kinasikiliza na nchi inasikiliza, pia
awe mtu anayekifahamu chama
vizuri,” alisema Lissu.
“(Katibu) anapaswa kuwa na uwezo
wa kuvaa viatu vya Dk Slaa ambavyo
si vidogo, ni vikubwa kwelikweli.
Kama atakuwa Sumaye itakuwa
sawasawa na ikiwa mtu mwingine
itakuwa sawasawa pia,” alisema
Lissu.
Alisema nafasi ya katibu mkuu ni ya
kukimbia kimbia, hivyo anahitajika
mtu anayeweza kukimbia.
Dk Slaa alijiondoa CCM mwaka 1995
baada ya jina lake kuondolewa
kwenye kinyang’anyiro cha ubunge
wa Jimbo la Karatu licha ya kushinda
kura za maoni, akajiunga na
Chadema ambayo ilimpa fursa ya
kugombea na akashinda ubunge.
Alishinda tena kwenye chaguzi za
mwaka 2000 na 2005, kabla ya
Chadema kumpitisha kugombea urais
mwaka 2010.
Baraza la Mawaziri Kivuli
Akizungumzia muundo wa Baraza
Kivuli la Mawaziri ambalo huundwa
na kambi ya upinzani bungeni, Lissu
alisema litakuwa lile linaloweza
kuisimamia kikamilifu Serikali
iliyoko madarakani.
Alisema itakuwa vigumu kwa kuwa
muundo wa wizara kama ya Mambo
ya Nje ambayo pia inashughulikia
Mambo ya Afrika Mashariki na
Kikanda, kwenye bajeti kwa kuwa
tayari wizara mbili zimekuwa moja
hivyo haieleweki kama bajeti yake
itakuwa moja au mbili.
Alisema itakuwa ngumu zaidi kwa
upinzani kwa kuwa kwenye Kanuni
za Bunge hotuba za upin ani za
bajeti zinasomwa kwa nusu saa,
hivyo kupata muda wa kuzungumza
masuala mengi ndani ya nusu saa
haitawezekana.
“Tutajikuta hatufanyi kitu. Muda wa
kujadili mambo ya Serikali bungeni
utakuwa mdogo kama kanuni
zitabaki hizihizi za sasa,” alisema
Lissu ambaye ameteuliwa na Spika
kwenye kamati ya kuboresha kanuni
za uendeshaji Bunge.
Lakini akawataka wananchi
kutegemee upinzani moto zaidi.
Lowassa ni mali
Akijibu swali kuhusu umuhimu wa
aliyekuwa mgombea urais kwa tiketi
ya Chadema, Edward Lowassa baada
ya kumalizika kwa uchaguzi huo,
Lissu alisema mbunge huyo wa
zamani wa Monduli amefanya kazi
kubwa.
“Mwaka 2010 tulikuwa wabunge 94
upinzani wote, hivi sasa ni wengi.
Haijawahi kutokea tukafikisha
theluthi moja, lakini tutafika, hivi
sasa tumekosa wabunge wachache.
Wote hao ni wabunge wa Lowassa na
Lowassa ni Ukawa,” alisema Lissu
tofauti na Dk Slaa ambaye alionyesha
shaka kama Lowassa ni mzigo au
mali kwa chama hicho.
Lissu alisema Lowassa ameiteka Dar
es Salaam kwa kuwa tangu upinzani
uingie nchini haujawahi kulishika jiji
hilo. Pia, ameteka majiji mengine
matatu ambayo ni Mbeya, Tanga na
Arusha.
“Lowassa amefanya kazi kubwa
kushinda kwenye majiji hayo. Pia
Zanzibar kwa upande wa Unguja
kwa mara ya kwanza upinzani
umepata wabunge tisa. Tumepunguza
kura za wabunge wa CCM hasa wa
viti malumu,” alisema Lissu.