BAK
JF-Expert Member
- Feb 11, 2007
- 124,769
- 288,331
Tafakuri Jadidi
Tunawachekea Wachina huku wakitubamiza
Johnson Mbwambo
Toleo la 324
6 Nov 2013
- Wenzetu Niger, Gabon, Chad tayari wanajuta
WIKI iliyopita vyombo vya habari nchini viliripoti kukamatwa kwa pembe za ndovu 706 katika nyumba moja ya Mikocheni, Dar es Salaam wanakoishi wafanyabiashara watatu wa Kichina.
Operesheni ya kuwakamata Wachina hao na pembe hizo iliongozwa na Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Khamis Kagasheki kwa kushirikiana na jeshi la polisi.
Pembe 706 za ndovu maana yake ni kwamba tembo wapatao 353 waliuawa nchini. Katika nchi kama Tanzania ambayo idadi ya tembo katika mbuga zake inapungua kwasi, huhitaji kuwa mtaalamu kufahamu kuwa tukiwachekea Wachina tembo watakwisha kabisa nchini.
Labda nikumbushe hapa kwamba hiyo si mara ya kwanza kwa Wachina kukamatwa na pembe za ndovu. Na wala pembe za ndovu si biashara pekee haramu ambayo Wachina hujishughulisha nayo Tanzania; kwani rekodi zinaonyesha kuwa, hushiriki pia katika biashara haramu za magogo na madini.
Akiwa China, Waziri Mkuu Pinda aliambiwa ya kuwa zaidi ya Watanzania 120 wamo katika magereza mbalimbali ya nchi hiyo kwa kukamatwa na madawa ya kulevya. Baadhi yao tayari wameshahukumiwa vifo na wanasubiri tu kutekelezwa kwa adhabu hizo.
Tumefahamishwa kwamba, juhudi zote za Pinda za kuwaombea Watanzania hao wasinyongwe zimegonga mwamba kwa kuwa Serikali ya China haina mzaha na wafanyabiashara wa dawa za kulevya.
Kimsingi, ukiondoa unyama na athari za biashara ya madawa ya kulevya kwa jamii, kosa la kushiriki biashara hiyo haramu ni jinai tu kama yalivyo makosa ya kujishughulisha na biashara nyingine haramu kama vile pembe za ndovu, madini au magogo, na hivyo yote yanastahili adhabu kali.
Lakini wakati ambapo zaidi ya Watanzania 120 wamo katika magereza ya China kwa kukamatwa na madawa ya kulevya, sitashangaa kuambiwa kwamba hakuna hata Wachina watano waliofungwa katika magereza ya Tanzania kwa kukamatwa wakishiriki katika biashara haramu za pembe za ndovu, madini au magogo!
Kwa maneno mengine, sitashangaa pia kuona Wachina hao watatu waliokamatwa na pembe 706 za ndovu wakiachiwa katika mazingira ya kutatanisha au kila wakifikishwa mahakamani kesi zao kupigwa danadana, na mwishowe kuachiwa huru!
Kwa mtazamo wangu, kiwango cha ushiriki wa Watanzania katika biashara haramu ya madawa ya kulevya huko China kinalingana kabisa na kiwango cha ushiriki wa Wachina katika biashara haramu za pembe za ndovu, magogo na madini hapa nyumbani Tanzania.
Tofauti pekee ni kwambva kule China wanapokamatwa Watanzania hufungwa magerezani, na ndiyo maana idadi yao imefikia zaidi ya 120, lakini hapa Tanzania ni nadra kuwakuta Wachina wapo magerezani kwa kukamatwa na pembe za ndovu, madini au magogo!
Ni kwa nini hali iko hivyo? Ni kwa sababu Serikali ya Tanzania inaiona China kuwa ni rafikiye mkubwa na mwekezaji mwenye nia njema na nchi yetu, na hivyo haitaki kuiudhi kwa namna yoyote ile kama vile kuwafunga gerezani raia wake wanaokamatwa nchini wakifanya biashara haramu.
Kwa hiyo, wakikamatwa Wachina hapa Tanzania, zitafanyika juhudi za chini chini za kidiplomasia kuwaachia huru; lakini wakikamatwa Watanzania kule Beijing, diplomasia hiyo haifanyi kazi kwao kuwanusuru Watanzania wenzetu na vifo au vifungo! Kwa maneno mengine, ni diplomasia ya upande mmoja tu.
Ndugu zangu, ninachojaribu kueleza hapa, na ambacho nilishawahi kukieleza huko nyuma ni kwamba; China si rafiki wa kweli wa Tanzania kama ambavyo watawala wetu wanajaribu kutuaminisha.
Labda niende mbali zaidi na kusema kuwa, katika dunia ya sasa hakuna kitu kama rafiki wa kweli kwenye mahusiano ya kimataifa. Kila nchi huwa inajali kuangalia na kulinda maslahi yake tu, na hivyo mahusiano yanapaswa kuwa ya nipe nikupe.
Kwa bahati mbaya, watawala wetu wanajipendekeza mno kwa China kiasi kwamba tunachotoa hakilingani na tunachopata. Na bahati mbaya zaidi, watawala wetu wanashindwa hata kujifunza kutoka kwa nchi kama Niger, Chad na Gabon ambazo zimelizwa na Wachina katika uwekezaji, na sasa zinahaha kurekebisha mikataba ya kifisadi zilizoingia nayo.
Sitaki msomaji wangu nikuchoshe kukuelezea kinachoendelea Gabon na Chad kuhusu mahusiano ya sasa ya kiuwekezaji ya nchi hizo na China, lakini mfano wa Niger unanishawishi nikusimulie kidogo.
Mwaka 2008 Niger ilikuwa chini ya mtawala dikteta na fisadi mpenda fedha kupindukia anayeitwa Mamadou Tandja. Huyu aliingia mikataba kadhaa ya siri na mashirika ya mafuta ya China iliyowezesha nchi hiyo kuchimba mafuta Niger na kuyapeleka China.
Mikataba hiyo ilibaki kuwa siri hadi dikteta huyo alipopinduliwa na wanajeshi mwaka 2010, na ndipo mikataba hiyo ilipoanikwa hadharani na kubainika kuwa kumbe Mamadou Tandja alilipwa binafsi na Wachina dola milioni 300 kama bonasi ya kusaini mikataba hiyo ya kifisadi, na ndiyo maana ilifanywa siri!
Hivi sasa watawala wa Niger moja ya nchi masikini kabisa duniani ingawa ina mafuta, imeiwekea ngumu China, na inaendesha nayo majadiliano mapya kurekebisha mikataba yote hiyo ya Mamadou Tandja ili iwe na manufaa kwa taifa hilo.
Mafuta ndiyo utajiri pekee tulionao Niger. Tukiyatoa kiholela kwa wageni, hatutaweza kamwe kujiondoa kwenye umasikini, ndivyo Waziri wa Mafuta wa Niger, Foumakoye Gado, alivyokaririwa na gazeti la New York Times toleo la Septemba 17, 2013.
Sina hakika majadiliano hayo mapya kati ya Niger na China kuhusu mikataba hiyo ya kifisadi ya Mamadou Tandja yamefikia wapi; lakini lililo dhahiri ni kwamba, nchi hiyo imewageuzia kibao Wachina na imechukua hatua kujihami, na hilo ni funzo kubwa kwa watawala wetu Tanzania.
Ni funzo kubwa kwa watawala wetu Tanzania kwa sababu nasi tuna mikataba na Serikali ya China ambayo, mpaka sasa, inafanywa siri, na pengine itaendelea kufanywa siri mpaka hapo Serikali ya CCM itakapotoka madarakani.
Mfano wa mikataba hiyo inayofanywa siri ni ule wa ujenzi wa bandari mpya huko Bagamoyo utakaofanywa na Serikali ya China. Kwa sababu ya usiri wake, kuna minongono mingi mno kuhusu yaliyomo kwenye mkataba huo.
Kwa mfano, kuna madai kuwa China itagharimia ujenzi wa bandari hiyo itakayokuwa kubwa na ya kisasa kushinda nyingine zote Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara, kwa sharti kuwa menejimenti ya bandari hiyo iwe ya Kichina kwa miaka 35!
Kama hilo ni kweli, na kwa kuzingatia ushiriki wa Wachina katika biashara haramu za pembe za ndovu, magogo na madini barani Afrika, basi, maana yake ni kwamba watakuwa wamejipatia bandari yao wenyewe ya kusafirisha magendo hayo kupeleka nyumbani China bila kubugudhiwa na vyombe vyetu vyovyote!
Kama bado hawana bandari wanayoisimamia wenyewe hapa nchini ya kupitishia magendo yao, na bado pembe nyingi za ndovu wanaouawa hapa nchini na majangili zinaishia China (kama ilivyo pia kwa magogo), hali itakuwaje siku wakiwa na bandari yao (Bagamoyo) wanayoisimamia wenyewe kwa miaka 35?
Tuambizane ukweli; taifa lolote linalotia saini mikataba ya siri na watawala madikteta na mafisadi wa Afrika kama vile Mamodou Tandja wa Niger, ni taifa ambalo urafiki wake na bara la Afrika ni wa kutilia shaka.
Ndugu zangu, China si rafiki mwema kama tunavyodhania!
Tafakari.