Herbalist Dr MziziMkavu
JF-Expert Member
- Feb 3, 2009
- 42,318
- 33,125
Na Mhariri
Maoni ya katuni
Juzi Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam alitangaza kukamatwa kwa Mkuu wa kitengo cha Ardhi katika Manispaa ya Kinondoni jijini Dar es Salaam, pamoja na kusimamishwa kwa maofisa wengine saba wa idara hiyo, pia kufungwa wa ofisi hiyo kutokana na tuhuma za kughushi nyaraka na kuuza maeneo mawili ya wazi yaliyopo katika rasi ya Msasani.
Agizo la kuchukuliwa kwa hatua hizo zilitolewa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam baada ya kupata taarifa za kuwepo udanganyifu wa kuuza viwanja vya wazi, huku akiagiza uchunguzi zaidi wa kina ufanywe kubaini wahusika wengine wa vitendo hivyo ambavyo vimevuruga sana taratibu za mipango miji na kuleta migongano ndani ya jamii.
Hii ni mara ya kwanza kwa hatua kali na za haraka kuchukuliwa na kiongozi wa serikali hasa katika Jiji la Dar es Salaam juu ya kero kubwa ya uvamizi wa viwanja vya wazi, kughushi nyaraka na pia kusababisha wenye haki ya kutumia maeneo ya wazi kubaki wakitafuta maeneo ya kupumzika na kucheza kwa sababu maeneo yao yameuzwa kinyemela.
Tunajua kwamba Mkuu wa Mkoa aliamua kwenda mwenyewe kwenye ofisini hizo na kushuhudia mikakati ikipangwa kukamilisha kazi ya kugawa viwanja hivyo kwa raia wanaoshirikiana na watumishi wa umma kupindisha sheria kwa sababu ya vishawishi mbalimbali.
Katika uvamizi huo, imeelezwa kwamba nyaraka mbalimbali zilikamatwa zikiwemo barua zilizosainiwa na viongozi waandamizi waliowahi kuongoza Manispaa hiyo.
Tungependa kuchukua fursa hii kumpongeza Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam; kwanza, kwa ujasiri wa kuthubutu kufanya alichofanya, lakini la pili ambalo ni muhimu kuamua kupambana na kero ambayo kwa hakika imekuwa sugu kwa miaka na miaka.
Itakumbukwa kwamba mara baada ya kuchaguliwa kwa Waziri John Magufuli, kuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, mwanzoni mwa utawala wa Awamu ya Nne, alitangaza Manispaa ya Kinondoni kuwa moja ya maeneo ambayo yamekithiri nchini katika kuvuruga taratibu na kanuni za ugawaji ardhi.
Waziri huyo alitangaza kupambana na tatizo hilo, lakini kwa habati mbaya sana, hakudumu muda mrefu katika wizara hiyo, hivyo tangu aendolewe baadhi ya maofisa waliokuwa wametopea katika uvunjaji wa kanuni za kugawa ardhi, wakarejea kwenye utamaduni wao.
Ni bahati ya mtende kwamba sasa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam amaeona mambo ya ovyo yanayofanywa na watendaji hawa wa serikali ambao wanawajibika kuhakikisha kwamba kanuni na sheria za matumizi bora ya ardhi zinafuatwa, lakini zaidi sana wakiwa ndio vinara wa kuhakikisha kwamba taratibu za mipango miji zinafuatwa vilivyo.
Tatizo la uvamizi wa maeneo ya wazi katika miji mingi nchini ni kubwa; kwa mkoa wa Dar es Salaam ni tatizo kubwa mno; kwa wastani maeneo mengi ya wazi yameuzwa na yanaendelea kuuzwa kiasi cha kuufanya mji huo kuwa kama unaendeshwa bila kuwepo kwa mpango kabambe wa uendelezaji.
Ni Manispaa hii hii ambayo hivi karibuni ilikuwa imeamua kugawa eneo la ufukwe wa Coco kwa watu binafsi kuendesha, kama si kuingilia kati kwa viongozi wa juu serikalini, leo hii Coco Beach ingekuwa ni ufukwe wa mtu binafsi. Aibu tupu!
Kumekuwa na kesi nyingi mno za kugawa kiwanja kimoja kwa zaidi ya mtu mmoja; wapo walioshitakiana mahakamani, lakini wapo walioingia katika ugomvi mkubwa; huku wengine wakiingizwa kwenye hasara kubwa. Hawa ni wale wanaojikuta wamekwisha kutumia rasilimali zao nyingi kuendeleza viwanja vyao lakini baadaye kuja kugundua kwamba vilikuwa na mgogoro kwa kuwa viligawanywa kwa zaidi ya mtu mmoja.
Ni bahati njema kwamba baada ya maofisa hawa kuendelea na tabia ya kutokujali maadili ya kazi yao, kujitengenezea mazingira ya kujinufaisha binafsi na ofisi za umma, sasa ameibuka kiongozi mwingine anawamulika na kuwachukulia hatua stahili ili kurejesha misingi ya uwajibikaji katika Idara ya Ardhi ya Manispaa ya Kinondoni.
Ni katika misingi hii tunamuunga mkono Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam kwa ujasiri wa kuthubutu kuutafuna mfupa ambao umewashinda wengi, na kwa kweli kufanikiwa kuusaga kwa nguvu inayostahili. Sote tumuunge mkono kiongozi huyu.
CHANZO: NIPASHE