Jospina
JF-Expert Member
- Apr 19, 2013
- 2,421
- 1,387
Angetile Osiah
Siku chache baada ya Katibu Mkuu wa Shirikisho la Soka (TFF) aliyepewa likizo ya lazima, Angetile Osiah kulalamika juu ya kitendo alichofanyiwa na kamati mpya ya utendaji ya shirikisho hilo kumtaka akabidhi ofisi usiku, wadau wa soka nchini wamekosoa hatua hiyo huku baadhi yao wakiiita ni ya kinyama.
Mwishoni mwa wiki Osiah alilalamikia kitendo cha uongozi mpya wa shirikisho hilo kumnyang'anya gari la ofisi usiku 'mzito' na kumuacha bila usafiri wa kurudi nyumbani kwake.
Aidha, Osiah ambaye alipewa likizo hiyo ya lazima inayoambatana na malipo muda mfupi tangu rais mpya wa TFF, Jamal Malinzi aanze kazi rasmi, alilalamikia kuamriwa akabidhi Ofisi za TFF usiku mzito.
Osiah aliamriwa kukabidhi ofisi na mali za TFF mara baada ya mkutano wa kwanza wa kamati mpya ya utendaji iliyoketi katika hoteli moja ya jijini Dar es Salaam usiku wa Novemba 2, mwaka huu.
Wakizungumza na NIPASHE kwa nyakati tofauti tangu Osiah aweke wazi aliyofanywa na uongozi mpya wa shirikisho hilo, wadau hao walisema kitendo hicho kwa kiasi kikubwa kililenga kumdhalilisha katibu mkuu huyo.
Mmoja wa wajumbe wa Kamati ya Utendaji ya TFF, ambaye aliomba hifadhi ya jina lake, alikosoa vikali kitendo hicho huku akikihusisha na visasi ambavyo baadhi ya wajumbe wa kamati hiyo wamejipanga kuvifanya dhidi ya watu ambao hawakuwa upande wao wakati wa mchakato wa Uchaguzi Mkuu wa TFF uliofanyika usiku wa Oktoba 27, mwaka huu jijini Dar es Salaam.
"Sikuona sababu ya Angetile kulazimishwa kukabidhi ofisi na gari la TFF usiku huo. Kungelitokea tatizo gani kama angelikabidhi asubuhi iliyofuata? Huu ni unyama na visasi visivyo na maana yoyote kwa maendeleo ya soka letu," alisema mjumbe huyo.
Ofisa mmoja wa Jeshi la Polisi jijini Dar es Salaam, ambaye pia aliomba jina lake lisiandikwe gazetini, alisema kitendo alichofanywa Osiah hakikuzingatia misingi ya sheria na haki za binadamu.
"Bendera ya Taifa ilikuwa imeshashushwa, walipaswa kusubiri hadi siku iliyofuata. Vile vile Osiah kama mfanyakazi, ana haki zake, unapomnyang'anya gari usiku mnene kiasi hicho na kumtelekeza ni kukiuka haki za binadamu," alisema ofisa huyo.
Mmoja wa ‘vigogo' wa mabingwa wa Tanzania Bara 1999 na 2000, Mtibwa Sugar (jina linahifadhiwa) alisema jana kuwa alishtuka baada ya kusikia malalamiko ya Osiah na kuutaka uongozi mpya wa TFF kuepuka kuliongoza shirikisho kwa visasi.
Katika hatua nyingine, Katibu Mkuu wa kilichokuwa Chama cha Soka Tanzania (FAT sasa TFF), Michael Wambura aliunga mkono kitendo alichofanywa Osiah kwa vile ‘ni cha kujitakia'.
"Nilionya mapema kwamba watendaji wa TFF wasijihusishe na mchakato wa uchaguzi mkuu. Yaliyotokea dhidi ya Osiah ni sahihi kabisa. Anapaswa kushukuru kwa kukaa kwa wiki moja zaidi kwa sababu alipaswa kung'oka siku hiyo hiyo ya uchaguzi baada ya matokeo kutoka," alisema Wambura.
"Waliamua kumnyang'anya gari usiku huo huo kwa sababu huenda angelificha baadhi ya nyaraka muhimu. Alitaka aachiwe gari usiku huo kama nani wakati nafasi ya Katibu Mkuu wa TFF tayari ilikuwa na mtu mwingine?" Alihoji Wambura.
Osiah amepewa likizo hiyo mpaka mkataba wake utakapomalizika Desemba 31, mwaka huu bila kuambiwa sababu yoyote, na tayari mchakato wa kupata mtendaji mpya wa TFF umeshaanza wakati Ofisa Habari, Boniface Wambura akikaimu.
Awali wakati wa mchakato wa uchaguzi, Osiah alikuwa na malumbano makali na Naibu Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Amos Makala kwa kile alichodai waziri huyo kuingilia mchakato wa Uchaguzi Mkuu wa TFF ambao baadaye ulisimamishwa na Fifa baada ya Malinzi kuenguliwa.
Osiah pia alihusishwa na jina la Agape Fue ambaye aliweka pingamizi na kuifanya iliyokuwa Kamati ya Rufaa ya Uchaguzi ya TFF kumuengua Malinzi katika kinyang'anyiro cha Urais wa TFF mwishoni mwa mwaka jana.
Ilifahamika baadaye kwamba Fue ni mkazi wa jijini Mbeya ambaye alikiri kuweka pingamizi dhidi ya Malinzi na kueleza kuwa hakuwa na uhusiano wowote na Osiah.
CHANZO: NIPASHE