[h=2]Msuya azungumzia uwezo wa Tanzania kiuchumi EAC[/h]
Na Salome Kitomary
2nd September 2011
B-pepe
Chapa
Maoni
Waziri Mkuu Mstaafu, Cleopa Msuya
Waziri Mkuu Mstaafu, Cleopa Msuya, amesema Tanzania bado haijaimarika kiuchumi na biashara hivyo bado haiwezi kujiunga na Jumuiya ya Afrika Mashari (EAC) na kushindana na nchi za Kenya na Uganda ambazo tayari uchumi wao ni mzuri.
Msuya aliyasema hayo jana wakati wa mahafali ya 10 ya wahitimu 156 wa kidato cha nne katika Shule ya Sekondari St. Mary Goreti, ya mjini hapa.
Alisema awali Tanzania ilikuwa imeimarika katika viwanda, biashara na uchumi na ndio maana nchi nyingine zilihofia kuungana nayo katika EAC, lakini kwa sasa hali ya uchumi si nzuri.
Alisema kwa sasa serikali inakabiliwa na changamoto kubwa ya utandawazi inayoongozwa na sayansi na teknolojia, ambapo mataifa mengine yanayoendelea kama Tanzania yatakuwa kama vijiji katika ulimwengu huu mpya.
Msuya alisema ulimwengu huu utaongozwa na kumilikiwa zaidi na sayansi, teknolojia na mitandao ya mawasiliano, hivyo kuwataka Watanzania kuweka ufanisi wao katika umoja utegemee zaidi katika kufaulu masomo
ya sayansi.
Alisema Tanzania inapoelekea kusherekea
miaka 50 tangu kupata ya uhuru, sekta ya elimu imefanikiwa kwa kiasi kikubwa tofauti na hapo awali, ambapo wasomi wa Shahada ya Chuo Kikuu walikuwa 12 na kwa sasa wanahesabika kwa maelfu.
Msuya alisema kuwa taifa katika sekta ya elimu imepiga hatua kubwa katika kuimarisha na kuboresha elimu tangu kupatikana kwa uhuru, ambapo alibainisha sababu za mafanikio hayo ni kutokana na amani na uongozi bora uliowekwa na muasisi wa taifa, hayati Mwalimu Julius Nyerere.
Alisema uboreshaji wa huduma ya elimu imechangia kwa kiasi kikubwa kuongezeka kwa wasomi na wataalamu ambao kwa sasa wanafanya kazi katika mataifa mbalimbali tofauti na awali.
Idadi hii ya wasomi imeongezeka kwa sababu ya kujenga shule nyingi za msingi, sekondari na vyuo vikuu, pamoja na kutoa uhuru kwa watu binafsi, mashirika na taasisi mbalimbali kushirikiana na serikali katika kutoa elimu, alisema Msuya.
Alifafanua kuwa kabla ya kupata uhuru , Tanganyika ilikuwa na jumla ya wasomi wa shahada ya chuo kikuu wapatao 12 ambapoi jumla ya shule za sekondari zilikuwa 41, ikilinganishwa na sasa kuwepo kwa
shule za sekondari 4,266 pamoja na vyuo vikuu 41 hali iliyochangia idadi kubwa ya wenye Shahada za Chuo Kikuu.
Aliwaomba wadau wa elimu kutoa ushirikiano wao mzuri kwa serikali katika kuendelea kutoa na kuboresha elimu ya hapa nchini, kuanzia chekechea hadi vyuo vikuu lengo likiwa ni kushindana na soko la ajira.
Meneja wa shule hiyo, Sista Phina Mushi, alisema shule hiyo inakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa thamani na vifaa
vya maabara vyenye thamani zaidi ya Sh. milioni 43.
Nyingine ni ukosefu wa kompyuta za kisasa zenye thamani ya Sh. milioni 140, hali aliyosema imechangia kwa kiasi kukubwa wanafunzi kuhitimu masomo bila kutumia kompyuta.
CHANZO: NIPASHE
Mtazamo: Hongera sana mheshimiwa Msuya unaonyesha jinsi gani ulivyokuwa makini na kujali maslahi ya watanzania. Niliwahi kusema na narudia tena EAC iwe kwa manufaa ya Watanzania. Tuige mfano wa Uingereza na EU kwamba tunaungana katika maeneo tunayaona tuna faida nayo kama hatuna faida nayo tuwaachie wenyewe mojawapo ardhi yetu, sarafu na uzalishaji vibakie kwanza kwa watanzania hadi hapo baadae. Vyenginevyo tutauma na kusaga meno na umoja huu.