Mbeki: Afrika imeangushwa na wasomi
na Ratifa Baranyikwa
RAIS wa Afrika Kusini, Thabo Mbeki, amesema wasomi barani Afrika, hawatakiwi kulalamikia matatizo yaliyopo, kwani wao ndio chachu ya suluhisho ya matatizo hayo.
Akizungumza katika mdahalo uliofanyika juzi katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Rais Mbeki aliwapa changamoto wasomi nchini, nao kuacha kulalamika na badala yake watoe mchango wao katika kushughulikia matatizo.
Alisema wasomi nchini ndio wana jibu sahihi kuhusu matatizo yanayotokana na umaskini. Alisema thamani ya vyuo ni kutoa fikra zitakazowezesha kuchangia shughuli za maendeleo na kuwataka wasomi hao kufanya tafiti kuhusu hali za nchi zao katika kushughulikia matatizo ambayo yanazikabili.
Mbeki alisema Tanzania na Afrika Kusini wanaweza kukaa pamoja na kutafuta suluhisho kuhusu tatizo la umaskini na matatizo mengine ambayo yanakwamisha maendeleo ya kiuchumi iwapo wasomi watafanya ipasavyo yale wanayopaswa kuyafanya.
Nchi zetu zina maliasili nyingi za kutosha kama maji, madini na kadhalika, sasa tunazitumiaje maliasili zetu katika kuzungumzia umaskini, ndilo jambo ambalo wasomi wanatakiwa kutoa mchango wao. Tumekuja kwa wasomi kusema nini tufanye kuhusu maliasili zilizopo Tanzania, hii ni changamoto, nyinyi kama wasomi kushirikiana na serikali zenu, alisema Mbeki.
Alisema kama nchi za Afrika ziliweza kuwaondoa wakoloni, sasa ni wakati wa kuondoa umaskini kwa kutumia maliasili zilizopo, lakini pia kwa mchango wa watu wenye ujuzi ambao ni wasomi.
Mbeki alisema hivi sasa nchi hizo mbili zimeanzisha ushirikiano ambao una lengo la kuleta maendeleo na kusema kuwa, katika mkutano wake na Rais Kikwete (uliofanyika juzi kabla ya kuhutubia wanafunzi wa chuo hicho), nchi hizo zilikubaliana kuanzisha Tume ya Maendeleo ili kupambana na umaskini.
Mbeki ambaye aliingia katika ukumbi wa chuo hicho wa Nkuruma majira ya saa 9 alasiri, alihutubia kwa muda wa saa mbili bila kupumzika mbele ya umati wa wanafunzi waliojaa kupita kiasi na kuwalazimisha baadhi yao kusikiliza mdahalo huo wakiwa nje ya ukumbi.
Alisema: Hatuhitaji watu wengine kutoka nje kuwa waangalizi katika mambo yetu ya kimaendeleo, Waafrika wenyewe tunapaswa kuwa waangalizi wa masuala yanayohusu nchi zetu.
Aidha, Rais Mbeki alisema kati ya matatizo ya kiuchumi ambayo viongozi wa Kiafrika wanatakiwa kuyavalia njuga, ni biashara. Akita mfano, alisema kiasi cha dola za Kimarekani milioni 500 zilipaswa kukusanywa kutokana na mauzo ya Tanzania nje ya nchi, lakini takwimu zilizopo zinaonyesha kuwa kiasi kilichokusanywa ni dola milioni nane tu.
Alisema hii inatokana na uchimbaji na usafirishaji wa madini hayo, ambao si halali na kutokuwa na uhalali wa kuuza madini hayo nje. Alisema kwa mantiki hiyo, mchango wa wasomi hasa wa kifikra, ni muhimu sana kwa serikali zao kwa kushauri nini kifanyike kutokana na nchi zao kuwa na maliasili nyingi ambazo hazitumiki ipasavyo.
Mbeki alikuwa ameambatana na balozi wa Afrika Kusini nchini, pamoja na mawaziri kadhaa wa Afrika Kusini akiwemo Waziri wa Viwanda, Waziri wa Mawasiliano na Uchukuzi, Waziri wa Kilimo, Waziri wa Mambo ya Nje na mshauri wake wa mambo ya sheria.
Wenyeji wake aliokuwa ameongozana nao ni Waziri wa Elimu ya Juu Sayansi na Teknolojia, Profesa Peter Msola pamoja na Waziri wa Viwanda, Biashara na Masoko, Basil Mramba.
Akimkaribisha Rais Mbeki awali, Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Rwekaza Mukandala, alimshukuru Rais Mbeki kwa kutenga muda wake na kukutana na wanafunzi hao na kutambua mchango wa wasomi.
Wakizungumza na gazeti hili baada ya hotuba hiyo, baadhi ya wanafunzi walisema kuwa, alichokisema rais huyo ni changamoto kwa serikali, pia kuhakikisha kuwa inaboresha elimu nchini.
Tanzania Daima: 7 Aprili 2007