Askofu Mkuu wa Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Mhadhama Polycarp Kardinali Pengo,akiagana Sitta.
Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba, Samuel Sitta, jana alikutana kwa nyakati tofauti na Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, na Mufti wa Tanzania, Sheikh Mkuu, Issa bin Shaaban Simba, kwa lengo la kuwaeleza lilipotokea Bunge hilo, lilipo na linakotaka kwenda.
Sitta, ambaye pia ni Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, alimtembelea Kardinali Pengo katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Joseph na Mufti Simba, Makao Makuu ya Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (Bakwata), jijini Dar es Salaam.
Akizungumza baada ya kuwatembelea viongozi hao, Sitta alisema lengo la ziara yake ni kuwaeleza mambo hayo, pia kuwaomba kuwa na maombi ya kuliombea Bunge hilo na mchakato huo kwa jumla.
KAULI ZA PENGO, SIMBA
Kwa mujibu wa Sitta, Mufti alishukuru kwa ugeni huo na kujua linaloendelea kwenye mchakato huo.
"Kama kiongozi mkuu ndani ya jamii hapaswi kuyapapasa masuala ya mchakato wa Katiba mpya ndiyo maana nimekuja kumueleza kwa undani na kupata ushauri wake…kubwa zaidi ni maombi yao ili mambo yawe mepesi na tuweze kumaliza mchakato salama na kupata Katiba bora,"alisema.
Kardinali Pengo alisema ameridhishwa na mchakato huo na anaendelea kuliombea Bunge ili umalizike salama.
Aidha, Sitta alisema ataendelea na ziara yake kwa makundi mengine kama ya vijana; asasi za kiraia na taasisi nyingine za kidini, ili kuwajulisha kinachoendelea kwenye Bunge kuliko kuwaacha wakipata taarifa kupitia vyombo vya habari pekee.
Hata hivyo, alitumia nafasi hiyo kuwaomba wajumbe wa Bunge hilo kuacha kulumbana kuhusu muundo wa serikali mbili au tatu bali wajikite katika kujadili kupata Katiba yenye Taasisi imara zenye kusimamia nchi katika misingi ya sheria na maadili.
Mwenyekiti huyo alisema tatizo kubwa kwa sasa maadili yameporomoka hivyo Katiba mpya ndiyo itakayosaidia kutengeneza sheria zenye meno ili kuwabana watumishi wa serikali wasio na maadili mazuri.
"Lazima Katiba mpya iwe na sheria kali ili kuondokana na watumishi wababaishaji, lazima nchi iende kwa maadili," alisisitiza Sitta.
Bunge Maalum la Katiba lilianza Februari 18, mwaka huu, kwa wajumbe kuchagua Mwenyekiti wa muda, kujadili Rasimu ya Kanuni kwa siku 21 na baadaye kumchagua Mwenyekiti na Makamu wa kudumu, Samia Suluhu.
Baada ya uchaguzi huo kanuni zilianza kufanyakazi kwa Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba, kuwasilisha Rasimu ya Katiba Bungeni na Rais Kikwete hufungua rasmi.
Aidha, kwa takribani wiki moja sasa, Bunge hilo limegawanyika kwenye Kamati 12 zenye jukumu la kujadili Rasimu ya Katiba, huku kukiwa na kamati za kitaalam tano.
CHANZO: NIPASHE