Simulizi Ya Kweli : Niliwaroga Walimu Mpaka Basi

Simulizi Ya Kweli : Niliwaroga Walimu Mpaka Basi

Kanungila Karim

JF-Expert Member
Joined
Apr 29, 2016
Posts
20,746
Reaction score
25,638
SEHEMU YA 01:

Siku hiyo mvua ilinyesha sana halafu shuleni kulikuwa na mitihani na mama alinitaka nirudi nyumbani kufanya kazi fulani, kwa hiyo nikaamua kumfuata mwalimu mkuu ambaye alikuwa ofisini kwake kwa lengo la kumbadilisha akili aseme wanafunzi wote turudi nyumbani hadi kesho yake.
“Nilisimama nje ya mlango wake, nikainama kwa sekunde chache, nilipoinua uso, nilibadilika ghafla na kuwa mwanafunzi wa kiume wa pale shuleni anayeitwa Juma Amosi.
“Nilishika mlango na kuufungua, nikazama ndani. Mwalimu mkuu alikuwa akitafuta mafaili kwenye kabati kubwa la ofisini kwake. Alishtuka kuona mlango umefunguliwa bila kugongwa.
“Ilikuwa ukitaka kuingia kwenye ofisi ya mwalimu mkuu ni lazima ugonge mlango na ukaribishwe kwa sauti, kinyume cha hapo usimame mlangoni mpaka atakapotoka au kukukaribisha kama una uhakika alikusikia.
“Wewe Juma ni kwa nini umeingia bila kupiga hodi?” mwalimu aliniuliza. Nilisimama katikati ya ofisi kama mwanajeshi, nikamkazia macho badala ya kumjibu, niliulekeza mkono wangu usawa wake, ukamfikia kwa kurefuka, nikamshika kichwani.
“Palepale akaanza kutabasamu huku akisema nikapige kengele ili wanafunzi wakusanyike mstarini kwa ajili ya kuwaambia jambo la dharura.
“Nilipotoka kwenda kugonga kengele, nilisimama mlangoni tena, nikabadilika na kuwa mjusi, nikakimbia chini kwenda mpaka kwenye mti wa kengele, nikabadilika tena na kuwa Yusta yuleyule. Nikagonga kengele.
Kwa kengele ya muda ule kila mtu alijua kulikuwa kuna dharura, kwa hiyo wanafunzi wakatoka kwenda mstarini ili kusikiliza.
Nilikwenda mstarini kwa kuzunguka nyuma ya shule ambako haikuwa rahisi mtu kuniona kama mimi ndiye niliyegonga kengele, nikafika mstarini na kusimama.
Baadhi ya walimu walitoka ofisini kwao na kuja usawa wa mstari huku wakionekana kushangaa.
“Nani amegonga kengele?” aliuliza mwalimu mmoja aliyejulikana kwa jina la Cecilia Kizigo.
“Hatujui,” wanafunzi mbalimbali walijibu huku wengine wakiendelea kushangaa.
Mara, mwalimu mkuu alitoka akiwa ameshika kitabu mkononi. Alitembea mpaka usawa wa walimu wa kawaida, naye akauliza kengele ni ya nini?
Walimu wengine wakamjibu hawajui. Sasa ikawa nani kapiga kengele, nani kapiga kengele. Kumbe mwanafunzi mmoja aliniona nikipiga mimi kama Yusta, akanitaja. Kwanza kabla hajanitaja alinyoosha mkono, mwalimu wa zamu akamuita jina:
“Hamisa unasemaje?”
“Mwalimu mi nilimwona Yusta akipiga kengele.”
“Yusta toka mbele,” yule mwalimu aliniamuru, nikapita mbele nikiwa na wasiwasi, lakini si sana.
“Nani alikwambia ugonge kengele?” yule mwalimu wa zamu aliniuliza kwa ukali.
“Juma.”
“Juma gani?”
“Juma Amosi.”
Niliposema Juma Amosi tu, mwalimu mkuu akatingisha kichwa kama anayekubaliana na mimi.
“Kweli atakuwa Juma Amosi. Alikuja hata kwangu akasema kengele igongwe anataka kuzungumza jambo.”
Walimu walionekana kumshangaa sana mwalimu mkuu kwa kauli yake hiyo, pengine kwa sababu haijawahi kutokea siku mwanafunzi akataka kengele igongwe ili aongee, mara nyingi wafanyao hivyo ni viongozi wa shule.
“Juma Amos,” mwalimu wa zamu alimuita mbele, akatoka.
“Naam mwalimu.”
“Ulitaka kuongea kitu gani wewe mpaka ukaenda kwa mwalimu mkuu na kuomba kengele igongwe?”
Juma Amos alionesha kushangaa, akaniangalia mimi kwa macho ya kunisuta, lakini na mimi nilijikausha.
“Mwalimu mimi namshangaa sana Yusta, sijamtuma.”
“We!” mwalimu mkuu alikuja juu, akaendelea:
“Wewe hukuja ofisini kwangu ukasema unataka ugonge kengele ili uongee jambo?”
“Mwalimu sijaja.”
“Weee,” mwalimu mkuu aliwaka tena. Cha ajabu, Mwalimu Cecilia akamtetea Juma Amosi kwamba, yeye mpaka kengele inagongwa alikuwa darasa la akina Juma Amosi, hajamwona akitoka zaidi ya muda ule kengele ilipogongwa.
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 02

“Mimi kwa macho yangu amekuja ofisini kwangu, akasema kuna kitu anataka kuzungumza na wanafunzi wote, nikamwambia akagonge kengele, sasa mwalimu unapomtetea unafanya makosa. Na yeye anapokataa namshangaa sana,” alisema mwalimu mkuu.
Mimi nikamkazia macho Mwalimu Cecilia kama ninayemwambia aseme lingine, mwalimu mkuu ameshapigilia msumari. Lakini baadhi ya wanafunzi wa darasa moja na Amos niliwaona katika sura za kushangaa tukio la mwenzao kuambiwa alitoka darasani.
“Yusta,” aliita mwalimu mkuu.
“Bee.”
“Si Amos ndiyo amekwambia ukagonge kengele?”
“Ndiyo mwalimu.”
“Mwalimu Yusta ni mwongo sana,” alisema Amos.
“Mwalimu mimi si mwongo, ni mkweli.”
Mabishano kati yangu na Amos yalidumu kwa dakika moja nzima huku walimu wote wakiwa wametukodolea macho.
Nilipoona hakutapatikana mshindi, niliamua kuchukua uamuzi mwingine. Nilimkazia macho mwalimu mkuu, kisha nikasonya ndani ya moyo, palepale mwalimu akaanza kuchekacheka na kusema:
“Sasa sikilizeni. Mimi naamua, wanafunzi wote mrudi nyumbani mpaka kesho. Maana hapa mambo yameshaanza kuwa mabaya.”
Wanafunzi walifurahi sana, lakini walimu walionekana kutomwelewa mwalimu mkuu kwa uamuzi wake huo tena wa ghafla:
“Mwalimu, yaani suala la nani kamtuma Yusta akagonge kengele ndiyo litutoe nje ya shule muda huu hata saa tano bado huku leo tuna mitihani? Mimi sikubaliani hata siku moja,” alisema Mwalimu Cecilia.
“Hiyo hali ya hewa unayosema imeshakuwa mbaya ni ipi?” alihoji mwalimu mwingine ambaye tulizoea kumwiita Mikogo kwa jinsi alivyokuwa akitembea kwa kunesanesa na urefu wake.
“Mimi nikiamua jambo nimeamua, sidhani kama hapa kuna suala la mjadala, nimeamuanimeamua,” alisema mwalimu mkuu huku akigeuza na kurudi ofisini kwake.
Kufumba na kufumbua, wanafunzi tulishaanza kushika njia ya kurudi majumbani kwa mwelekeo mmoja. Kabla hatujamaliza kuondoka eneo la shule, kengele iligongwa tena, wanafunzi tukasimama kuangalia shuleni.
Tulimwona Mwalimu Cecilia akituita kwa ishara ya mkono, wengine walirejea lakini wengine, nikiwemo mimi tuliangalia mbele na kutokomea.
Nilimkuta mama akinisubiri. Aliponiona alikunja sura, akaniuliza:
“Kwa nini umechelewa?”
“Nilikuwa naweka mambo sawa mama. Kulitaka kutokea kikwazo.”
“Nani alitaka kuweka kikwazo. Niambie sasa hivi nimjue. Mimi sipendagi mambo ya kijingajinga wakati nina uwezo,” alisema mama akionesha hatanii.
“Mwalimu Cecilia na Mikogo.”
Mama aliingia ndani ghafla, nikamfuata. Alichukua ungo akaja nao sebuleni, akaubwaga kwenye kiti kisha akainua mikono juu kama mchungaji anayeomba dua.
“Agggggggh! Mwalimu Cecilia. Mmmmh! Agggggh! Mwalimu Cecilia.”
Palepale Mwalimu Cecilia alitokezea kwenye ungo akiwa amekaa ofisini kwake.
“Wewe mwalimu na huyo kikaragosi mwenzako, Mwalimu Mikogo, ole wenu kumwingilia mwanangu kwenye maisha yake. Nasema ole wenu,” mama alisema akimnyooshea kidole Mwalimu Cecilia pale kwenye ungo.
“Umenielewa?”
Mwalimu Cecilia alimwitikia kwa kubetua kichwa, kisha akapotea. Mama alichukua ungo na kuurudisha chumbani kwake, akatoka akisema:
“Inabidi ubadili nguo twende sasa.”
“Tunakwenda wapi mama?” mimi niliuliza.
“Kabadili nguo wewe.”
Nilitii. Nilikwenda chumbani kwangu uani, nikavua sare za shule na kuvaa gauni na khanga kwa kuizungushia.
Nilipotoka, mama alitoka nje, nikamfuata, akafunga mlango kwa funguo, nikahisi tunakwenda mbali na nyumbani. Alipiga magoti mbele yangu akaniambia nipande mgongoni mwake, nikafanya hivyo.
Baada tu ya kupanda, kufumba na kufumbua tulijikuta tupo mjini Handeni. Mama aliniambia tulikwenda kumsaidia mwenzake kuroga watu wenye watoto hospitalini. Yaani wanawake wenye watoto wamelazwa au wamewapeleka kliniki.
Ilivyo ni kwamba, kwa huku Handeni, wakati wa msimu wa kilimo cha mahindi, wakulima ndiyo huitumia nafasi hiyo kuroga au kufanya vitendo vya kishirikina ili kupata mazao mengi.
Unaweza kukuta mkulima anamiliki shamba la miguu ya mtu mzima mia moja tu kwa mapana na marefu yake, lakini mazao atakayoyatoa hapo utashangaa. Hatofautiani na mtu mwenye shamba la maeka kwa maeka. Hii mara nyingi hutokana na mambo au niseme vitendo vya kishirikina.
Tulifika hospitalini na kumkuta huyo mwanamke anayesaidiwa na mama. Alisimama pembeni ya geti lakini hakuna mwanadamu wa kawaida aliyekuwa na uwezo wa kumwona kwa macho ya kawaida.
Alipotuona, alituita kwa kufanya ‘tsii’. Hivi ndivyo wachawi wengi wanavyoitana. Kama umewahi kupita mahali ukasikia ‘tsii’ jua kuna wachawi hapo wameitana.
Mimi na mama tulitembea kumfuata pale, akatoa vitambaa vyeusi viwili, vyote akavipokea mama. Kimoja akajifunga kwenye paji la uso kuzungukia kisogoni, kingine akanipa mimi na kuniambia nijifunge kama yeye.
Nilifanya hivyo. Baada ya hapo tukaanza msafara wa kwenda ndani ya hospitali. Tulipofika mlango mkubwa, yule mwanamke akageuka, akawa anatembea kinyumenyume kwenda. Mama naye akafanya hivyo na mimi nikaiga bila hata kuelekezwa na wao.
Ili kujua kama wenzangu bado wananyoosha au wamekata kulia au kushoto, niliinama zaidi na kuwaangalia kwa kupitia katikati ya miguu, sikuwaona, nikashtuka na kusimama, nikageuka ili niwaangalie vizuri.
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 03


Niliwaona wamesimama nje ya mlango wa chooni. Nikawafuata kulekule ambapo mama alinielekeza nifike pale kwa kutembea vilevile tulivyoelekezana awali. Nilisimama, nikageuka na kuanza kutembea kinyumenyume mpaka pale.
Mama na yule mwanamke waliniingiza chooni na kunisimamisha jirani na bomba la maji kisha wakasema natakiwa kuwa pale nikiwa nimesimama wima hadi watakaporudi. Wakati wanaondoka, mama aliniambia kazi yangu itakuwa kupokea vitu watakavyokuwa wanavileta pale na kuvishika kwa kusubiri maelezo mengine.
Baada ya muda, yule mwanamke alikuja, akanikabidhi watoto wachanga wawili. Akaniambia wakitaka kulia tu, niweke mikono juu ya vichwa vyao ili watulie, kisha akaondoka.
Niliwashika wale watoto kwa umakini kwani walikuwa wazito sana. Baada ya muda, alikuja tena yule mwanamke, alikuwa amebeba watoto wawili, akanikabidhi, lakini nilikuwa sina pa kuwaweka, akasema niwabebe mgongoni. Alinisaidia kunibebesha halafu wale wawili nikaendelea kuwashika mkononi.
Dakika kama tatu baada ya yule mwanamke kuondoka, aliingia mgonjwa mmoja, akawa kama amenikazia macho mimi. Nilimnyooshea kidole kisha nikakielekezea kwenye mlango wa choo kimoja, naye akaingia huko.
Pale nilichofanya, niliishika akili yake na kuielekeza iingie kule kwenye choo. Wachawi wengi hufanya hivyo. Pale wanapokumbana na kikwazo mbele yao, hujihami kwa vidole, mchawi akikunyooshea kidole kisha akakielekezea kwenye moto mfano, utajikuta ukienda.
Ndiyo maana kuna watu wanagongwa na magari njiani kisha wanaoshuhudia wanashangaa kwamba, jamaa ilikuwaje akasogea barabarani wakati gari lilikuwa linatoka kwa mbele yake?
Kinachofanyika ni kwamba, kama kuna mchawi ametumwa kwako akumalize na ni ‘mwepesi’, yaani huna kinga yoyote, basi akishakupatia shabaha, anakuelekezea mahali pa hatari. Iwe kwenye moto, barabarani au hata kwenye maji, lazima utaelekea huko tu kwani wenyewe wanasema wanashika akili.
Basi, yule mwanamke aliingia kule chooni. Akafunga mlango na kujisaidia. Baada ya muda alitoka, akageuka kuangalia niliposimama mimi, nikamnyooshea tena kidole na kukielekezea mlango mkubwa, akatoka. Huku nyuma nikasonya.
Niliendelea kuwa pale nikiwa na wale watoto wachanga. Lakini huku nikiwa na maswali mengi, kwani uchawi wa kupata mazao mengi shambani kupitia watoto nilikuwa siujui. Mawazo yangu yaliamini kwamba, wale watoto tutaondoka nao kwenda nyumbani ili kuufanya huo uganga kumbe sivyo.
Baada ya dakika chache tena, alikuja mama, naye alibeba watoto wawili, akasema nikae chini ili niwapakate. Kulikuwa na ugumu kwani sasa nilikuwa na watoto wawili mgongoni na wawili mkononi nikiwa nimekaa chini.
Baada ya kuwakumbatia wale watoto, mama akaniambia nivumilie kwani bado mawili tena. Akasimama na kuondoka kwenda kuungana na yule mama.
Baada ya dakika tano, mlango ulisukumwa, akaingia mwanamke mmoja akiwa anavua gauni, akajisaidia nje ya mlango wa chooni. Nilikasirika sana kwa kitendo kile.
Ili kuikomesha tabia ile, niliwashika wale watoto vizuri kisha nikamnyooshea mkono, kidole kimoja nikakikunjua kukielekeza kwake na kukibatulia chini, akaanguka kama gunia, puu!
Aliposimama, nikasonya. Inaonekana alisikia kusonya kwangu kwani alitoka haraka huku akigeuka kuangalia nyuma. Kwa pale nilipokuwa nimekaa palikuwa wazi sana lakini aliyekuwa na uwezo wa kuniona mimi ni mmoja tu. Ni mtu mwenye nguvu za kichawi kama sisi.
Baada ya hapo, mama aliingia. Alikuwa ana watoto wawili, akawaweka kwa kuwachomeka kwangu lakini nilishindwa kuwabeba sawasawa. Aliwaacha hivyohivyo, mama akaondoka. Lakini baada ya dakika mbili alirudi akiwa ameongozana na yule mwanamke mwenzake. Hawakuwa na kitu chochote mkononi. Walipofika, walipiga magoti jirani yangu. Mama alianza kumchukua mtoto mmoja mmoja na kumkabidhi mwenzake ambaye naye aliwachukua na kuwaweka sakafuni.
Mama yeye, alikuwa akimchukua mtoto mmoja, anamuweka mkono kichwani kisha anampindua miguu juu, kichwa chini kabla ya kumpa mwenzake ambaye naye kila alipowapokea, aliwaweka kwa kuwalaza kifudifudi.
Walipowaliza watoto wote, mama alisimama, akanyoosha mkono mmoja juu, akasema:
“Mje mchukue watoto wenu haraka, sisi tunaondoka.”
Kufumba na kufumbua, kweli wanawake waliingia, kila mmoja akamchukua mwanaye, tena walikuwa wakigombeana na kuondoka. Hapa palikuwa na maswali mengi sana na nilipanga kumuuliza mama nyumbani.
Tuliondoka muda huohuo kwa njia ya kichawi hadi nje ya hospitali. Yule mwanamke akasimama getini na sisi pia. Aliangaza kulia na kushoto, akasema twende kwenye mti mmoja wenye matawi marefu na chini yake palikuwa na kivuli kikubwa.
Pale chini ya mti, yule mwanamke alimpa mkono mama na mimi, kisha akasema ameshukuru sana kwa ushirikiano wetu. Akasema ikitokea na sisi tuna shida kama yake au nyingine, tusisite kumwambia muda wowote hata kama itakuwa saa nane za usiku.
Mama alimwambia hakuna shida, akatoa mkono kwangu akauegemeza kichwani, akaniangalia akasema:
“Hakika wewe utafika mbali sana siku za usoni, jitahidi kuwa shupavu kama hivi. Mungu akulinde sana Yusta.”
Tulipofika nyumbani, nilimuuliza mama kama nilivyokuwa nimepanga. Kwamba, wale wanawake waliofika kugombea watoto wao walikuwa wanajijua?
Mama alisema hakuna hata mama mmoja aliyejua mtoto wake amechukuliwa. Ila akasema kwa wale ambao watoto wao walichukuliwa, dalili kubwa kwao ni watoto ‘feki’ waliowashika mikononi walikuwa wakilia sana hata pale mama zao walipowapa maziwa walizidi kulia mpaka kupatwa na kwikwi.
“Sasa mama, pale ulipowaita waje kuwachukua mama zao, kule ndani hospitali wao walijua wanakwenda wapi?”
Mama alinishika kichwani, akanisifia kwamba nina akili sana, kisha akasema:
“Wale hawakujijua chochote. Kila mmoja alipomchukua mwanaye na kurudi naye wodini waliendelea kujiona kama hawakutoka. Ila walijua watoto wao wametulia kulia baada ya kuwabembeleza sana.
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 04

“Mlizuia vipi mama? Sijaelewa.”
“Tuligundua ulichomfanyia. Kwa hiyo baada ya kufika wadini mimi nilimkimbilia na kumsukumia kitandani, alipotua pale ikawa ndiyo uzima wake.”
***
Usiku wa siku hiyo, mama aliniamsha kwa kunitingisha sana. Usingizi ulikuwa mzito sana siku hiyo. Nilipoamka akasema anaomba tukamalizie kazi ya yule mwanamke mwenzake. Nilimuuliza inamalizika usiku? Akasema ndiyo wakati wenyewe ndiyo ule.
Kimsingi alinishtua lakini sikuwa na jinsi zaidi ya kumkubalia kila alichotaka. Niliamka, nikavaa kaniki kwa staili ya kuizungusha mwilini, nikachukua na kibuyu cha dawa kisha nikatoka kumfuata mama ambaye alikuwa nje akinisubiri. Alinishika mkono na kupaa angani hadi nyumbani kwa yule mwanamke ambaye naye tulimkuta nje akitusubiri . Alisalimiana na mama kisha akanisalimia na mimi huku akisema:
“Binti kazi nzuri, wewe ni mwanajeshi mkubwa sana katika kazi yetu, unahitajika kuwa juu zaidi ya hapo maana nakukubali.”
Nilimjibu asante sana mama. Kisha yule mwanamke akamshika mkono mama na mimi kwa pamoja na kusema tuondoke.
Mawazo yangu yalikuwa juu ya namna ambavyo safari hiyo itakavyokuwa, nikawa mpole na kusubiri maelekezo. Kufumba na kufumbua tulikuwa ndani ya nyumba moja. Tulitembea kuingia kwenye chumba kimoja ambacho tuliwakuta wanandoa wawili wamelala. Ulikuwa ni usiku mnene na walikuwa wakikoroma.
Mama aliwaita kwa kutumia ishara ya mkono, wote wakainuka taratibu na kukaa kitandani wakiangalia mbele ukutani. Mama akaendelea kuwaita huku sisi tumesimama sambamba naye. Wale watu wakatoa miguu nje ya kitanda na kushuka kisha wakasimama.
Mama na yule mwanamke walinitangulia kisha wale watu wakawa wanawafuata kwa nyuma. Baada ya sekunde kadhaa, mama alinifuata na kuniambia nimpe kibuyu kilichokuwa na dawa ndani yake ambacho wakati wa kuanza safari yule mwanamke rafiki wa mama alinikabidhi kukishika.
Alitoa makaratasi mawili yenye dawa, akanipa mkononi na kuniambia:
“Changanya haraka hiyo nyeusi na hiyo ya kahawia. Ukimaliza, niambie.”
Nikatekeleza maagizo aliyonipa kisha nikamkabidhi. Tayari wale wanandoa wakawa kama wamechanganyikiwa kimiujiza.
Mama, aliwaamuru kuvua nguo walizovaa wakiwa kitandani, wakatekeleza hilo. Walikuwa kimya ingawa walionekana wanatamani kuzungumza chochote, nadhani walishindwa kwa sababu ya dawa walizofanyiziwa na mama.
Mama akawapaka dawa mgongoni, kwenye mapaja na miguuni huku akizungumza maneno ambayo sikuyaelewa maana yake na najua yalikuwa ya kichawi kwani siku zote wachawi wanaongoza kwa kusema maneno yenye ishara ya kunuwiza. Aliendelea kusema maneno hayo kwa muda huku sisi tukimuangalia. Mimi nilimkazia macho kabisa.
Kuna wakati nilishindwa kujizuia, ikabidi nimuulize mama kama anahitaji msaada wowote kwani alionekana kuzidiwa nguvu, alianza kurudi nyuma taratibu.
“Hawa wanaonekana waliwahi kujiwekea zindiko, ndiyo maana hii dawa niliyowapaka inaonekana haijawafaa sana,” alisema mama akiendelea kurudi nyuma.
“Kwa hiyo mama kama waliwahi kuwekewa zindiko tunatakiwa kufanya nini ili tukamilishe kazi yetu?” nilimuuliza.
***
Nyumba ya pili ambayo mama aliwahi kuwaroga zamani kama walishtuka baada ya mbwa kubweka mfululizo kuashiria kuna kitu kibaya kinaendelea maeneo yale.
Hapa nataka kusema kidogo kwamba, kati ya viumbe ambavyo Mungu amevipa uwezo wa kuwatambua wachawi ni mbwa. Asikudanganye mtu. Ukisikia mbwa wanabweka sana, hasa usiku mwingi ujue kuna wachawi hasahasa kama hutaona watu wakitembea kwa uwazi. Majirani waliamka na kutilia shaka ule ubwekaji wa mbwa, wakahisi kuna kitu kibaya kinaendelea usiku huo. Mara tuliwasikia majirani wakisali, mbwa nao walizidi kupiga kelele huku wakiizunguka ile nyumba ambayo sisi tulikuwa ndani tukiendelea na kazi zetu za kichawi.
“Mama lakini mbona hawa mbwa wanabweka sana na hawa watu wa humu ndani mbona hawasogei mbele tena kama walivyoamka kitandani?”
Mara tena tukasikia sauti ya mwanamke kutoka ile nyumba jirani wanayosali ikisema:
“Kutakuwa kuna kitu, si mnakumbuka hata sisi tuliwahi kuingiliwa? Cha msingi tuendelee kusali ili mabaya yasitukute.”
Hofu iliwajaa watoto pamoja na mama zao, walikumbuka namna walivyoteseka siku waliporogwa na kupata mateso makubwa.
Wakakumbuka neno ambalo waliambiwa na mchungaji John aliyekuwa maarufu maeneo hayo kwa kuombea mapepo. Aliwaasa juu ya kusali bila kikomo hasa wanapoona hali ya hatari kama hiyo.
Waliendelea kupiga maombi ambayo kwa kiasi fulani yaliathiri kazi tuliyokuwa tukiendelea nayo. Vurugu ya kelele za mbwa ilizidi kuwa kubwa.
***
Mama akabadili mbinu, akawaamuru wale wanandoa walale chini kwa kuwaelekezea mikono yake yenye kucha ndefu huku akiwatazama kwa macho makali ambayo yalimulika kama tochi.
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 05


Wale walitii hatua kwa hatua na mwishowe ushindi mkubwa ukawa kwetu.
Aliwaamsha, akawaamuru watembee mbele yetu hadi nje. Kufika nje, akawashika mkono mmoja mmoja kila mmoja, yule mwanamke shoga wa mama akanishika mimi, tukafutika, kufumba na kufumbua tukatua kwenye shamba kubwa lenye majani yaliyokauka.
Ni shamba lililoonesha kwamba mwaka uliopita lililimwa, kwa hiyo lilitakiwa kulimwa kwa mwaka mwingine. Nilihisi ni shamba la yule mwanamke mwingine maana sisi hatukuwa na shamba kama lile.
Baada ya kufika pale shambani, yule mwanamke alisimama kama askari kisha akanyoosha mkono mmoja juu na kusema kimoyomoyo. Baada ya sekunde kadhaa, jembe na mpini wake lilikuwa mkononi. Akampa mama.
Halafu akanyoosha tena mkono na kusema kama mwanzo, jembe jingine likatua palepale kwenye mkono, akaendelea kulishika mwenyewe huku akimfuata mama.
Waliwapa majembe wale watu, kila mmoja na lake na kuwaamuru waanze kulima haraka sana. Palepale, walianza kulima kuanzia kwenye mpaka wa shamba kuelekea katikati. Mwanamke ndiye aliyetangulia kuchoka sana lakini mama akawa anamsukuma. Kwa hiyo ilibidi alime kwa nguvu.
Mimi, yule mwanamke na mama tulikuwa tunawafuata kwa nyuma baada ya kila hatua kadhaa za kulima. Nilipata mawazo ya kumuuliza mama kama wale watu wanajua nini kinaendelea kwao.
Mama akasema wanajua wanalima, lakini shamba liko wapi, la nani, kwa nini wanalima hilo hawalijui. Pia, akaniambia pale walipo japokuwa wanalima kwa pamoja lakini hakuna anayejua kama mwenzake yupo pembeni.
Kifupi ni kwamba, walikuwa wakilima kila mmoja akijijua yeye tu kwamba yupo shambani analima. Baada ya hapo nikamuuliza mama watarudi vipi kwao?
“Kwao tutawarudisha baada ya kumaliza kulima. Kwa sababu wanalima kwa nguvu za kichawi watamaliza leo, ila kesho watashinda wamechoka sana.”
Nilimuuliza mama itakuwaje wakiamka na kujikuta wamechafuka sana?
“Huo ni uchawi wa kizamani sana, mtu anakwenda kulima halafu asubuhi anajiona alivyochafuka kwa udongo au vumbi la shambani, lakini uchawi wa siku hizi mtu anaamka anahisi kuchoka kupita kiasi, wakati mwingine anaamini anaumwa lakini kumbe alikuwa shambani usiku akilima.”
Basi, wale watu walilima hadi kwenye saa kumi alfajiri ambapo tuliwachukuwa na kuwarudisha nyumbani kisha sisi tukaondoka zetu kurudi majumbani.
Asubuhi, niliwahi kuamka kwani nilitakiwa kwenda shuleni kama kawaida. Kufika shule, mwalimu Cecilia aliniita kwenye ofisi ya walimu wenzake. Akaniuliza:
“Wewe ni kwa nini jana tulipogonga kengele wanafunzi wote warudi wewe hukufanya hivyo na ulikuwa bado hujafika mbali?”
Nilifanya kibuli, sikumjibu na sikuwa namwangalia usoni. Macho yangu yalicheza kwenye miguu yake.
“Mimi nakuuliza wewe hujibu siyo? Halafu ni kwa nini unanikodolea miguuni na hiyo mimacho yako mikubwa?”
Pia sikumjibu. Ndipo waalimu wenzake wakasema mimi ni mjeuri tangu siku nyingi na dawa yangu ni moja tu, fimbo. Mwalimu Cecilia akasema nikachukue fimbo mwenyewe.
Nilitoka kwenda kutafuta fimbo kisha nikarudi nayo. Aliniambia nilale kifudifudi ili anipige fimbo saba, nikalala. Kwa kweli fimbo ziliuma sana. Alipofika ya tatu ilikuwa shida kukubali kuendelea.
Walinilazimisha kwa maneno makali mpaka zikatimia fimbo zote saba, makalio yalikuwa yanauma na yakavimba ghafla. Niliposimama nikashindwa kuvumilia nikamwambia Mwalimu Cecilia: “Utaona wewe.”
Akasema: “Ha ha ha! Wewe mtoto mdogo unaweza kuniambia maneno hayo mimi mwalimu wako, rudi haraka sana. Njoo nikupe viboko vingine vinne ili nione vizuri.”
Nililazimika kurudi kupigwa viboko vingine vitano ambapo safari hii makalio kidogo yatoke maji ya malengelenge. Nililia sana tena kwa sauti ya juu. Baadhi ya wanafunzi walikuja kwenye madirisha ya ofisi ya walimu kutaka kujua kinachoendelea.
Nilitoka nikiwa bado nalia lakini moyoni niliendelea kumwambia yule mwalimu ataona kwani ukweli ni kwamba nilipanga kumshughulikia. Tena si yeye tu na walimu wote walioonesha kumuunga mkono Mwalimu Cecilia.
***
Muda wa kurudi nyumbani ulipofika tuliruhusiwa kuondoka. Nilipofika nje ya nyumba yetu nilijiangusha na kuanza kulia kwa sauti. Mama alitoka mbio, aliponiona alinifuata na kuniinamia akiuliza:
“Mwanangu umekumbwa na nini?”
Nilijishika makalio huku nikiendelea kulia.
“Yamefanyaje?” mama aliniuliza huku akinisimamisha, nikamwambia kuna mwalimu amenichapa fimbo.
“Mwalimu akuchape wewe na fimbo, amekuzaa?” mama alikuja juu.
“Amekuchapa fimbo ngapi?”
“Kumi na mbili mama.”
“Ha! Ha! Ha! Mwanangu mimi, achapwe fimbo kumi na mbili na mwalimu wake, sikubali hata kidogo.”
Nilidhani mama atasema twende hukohuko shuleni akapambane na huyo mwalimu lakini sivyo, akasema:
“Huyo leo ana mimi, lazima na yeye nimchape viboko vyake ishirini na nne muwe sawasawa.”
“Nitafurahi sana mama,” nilisema huku nikijifuta machozi na kuingia ndani na mama.
***
Usiku uliingia, tukala, kisha tukakaa sebuleni kuongea. Mama alikuwa akinisimulia hadithi mbalimbalai za zamani huku mimi nikicheka. Ghafla, kwenye saa tano huko alisimama na kusema tukalale. Lakini akaongeza:
“Usilale sana mwanangu nitakuja kukuchukua twende kwa mwalimu akapate viboko vyake.”
“Sawa mama.”
Nilikwenda kupanda kitandani, nikapitiwa na usingizi. Niliamshwa na mama kwenye saa nane usiku. Alisimama chumbani kwangu, mkononi alishika fimbo nyingi sana.
“Twende sasa mwanangu, muda umefika,” mama aliniambia kwa sauti ya upole.
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 06

Niliamka kutoka kitandani, nikashusha miguu chini na kuanza kutembea kuelekea sebuleni ambapo mama alikuwa amenitangulia.
Pale sebuleni, mama aliusogelea ukuta mkubwa na kusimama akiutazama. Na mimi nikamfuata, nikasimama nyuma yake. Aligeuka kuniangalia, alipojiridhisha nipo, alipiga kofi ukuta, kufumba na kufumbua tukawa tupo nje ya nyumba ya Mwalimu Cecilia.
Hapa niseme kidogo, uchawi wetu mimi na mama ulikuwa wa kisasa zaidi. Tulikuwa tukitaka kutoka nyumbani, nguo tulizovaa zinajivua zenyewe, tukirudi zinajivalisha tena. Kwa hiyo mama alipopiga ukuta, nguo zetu zilijivua palepale, ina maana sisi tulitoka uchi wa mnyama.
Basi, tulifika nje ya nyumba ya Mwalimu Cecilia, mama akapiga kofi mlango, ukafunguka na kuzama ndani. Kule ndani tulitokea sebuleni. Mama akasimama na kunyoosha mkono huku akizunguka, akafika mahali akaganda, akasema:
“Huku ndiko chumbani kwake.”
Hapo alikuwa amenyoosha mkono kuelekea kwenye mlango mmoja wenye pazia limeandikwa maandishi ya kufuma yanayosomeka: Muomba Mungu Hachoki
Tulielekea kwenye huo mlango. Mama akaupiga kofi tukazama ndani.
Mama alisimama katikati ya chumba akainua mkono juu. Midomo ilionekana kusema maneno fulani, mara mkononi kwake kukajaa fimbo kama kumi hivi.
Alichukua moja akanipa na kuniambia nianze kumchapa mwalimu yule. Nilifanya hivyo. Lakini mwalimu mwenyewe kwa wakati ule alikuwa amelala chali. Kwa hiyo kabla sijaanza kumchapa mama alikwenda akamfuta macho kwa kiganja cha mkono wake wa kushoto, mwalimu akageuka na kulala kifudifudi.
Nilianza kumtandika. Nilimchapa mwalimu akawa analalamika huku akijishika makalio kwa maumivu makubwa. Mama aliniambia nikazane kumchapa, nilimchapa sana.
Mwalimu Cecilia aliendelea kulalamika huku mimi nikizidi kumchapa. Fimbo ya kwanza iliisha, mama akanipa nyingine, nikaendelea na adhabu yangu kwa mwalimu. Lakini nilikumbuka kwamba, mama alisema atampa mwalimu huyo fimbo kumi na mbili. Kwa wakati huo zilifika hata mia.
Nilianza kuingiwa na huruma, kwani nilihisi makalio ya mwalimu yalianza kuvimba kwa kuchapwa. Nilimwangalia mama kwa ishara ya kumuuliza niendelee au niache, akaninyanyulia mkono juu akinihimiza niendelee kumchapa.
Ghafla mama akanishika mkono kisha akaninyang’anya fimbo. Nilijua sasa basi, kumbe alitaka iwe zamu yake. Alimchapa sana Mwalimu Cecilia huku akisema ni kwa nini amekuwa akinionea.
Mwalimu hakuwa anajibu kwa sababu hakujua kinachoendelea. Yeye alikuwa akitesekea usingizini kama ndoto lakini maumivu yalikuwa ya kweli.
Mama alimchapa zaidi kuliko mimi. Nilianza kuona damu inachuruzika sehemu ya makalio, nikajua mama ameshamuumiza mwalimu. Mama naye aliiona ile damu, akaacha kumchapa lakini huku akitingisha kichwa kama anayekubaliana na kipigo alichompa.
Tulitoka kurudi nyumbani, kila mtu aliingia chumbani kwake.
Asubuhi na mapema, mama alikuwa wa kwanza kuamka, akaja kuniamsha na kuniambia nisije nikachelewa shule nikapigwa. Usingizi ulikuwa bado kwani safari ya usiku kwa Mwalimu Cecilia ilinifanya nichelewe kulala.
Nilifika shuleni kwa muda mwafaka, nikawa naangaza macho kila upande kama nitamwona Mwalimu Cecilia, lakini sikumwona. Nilijikuta nikimwambia mwanafunzi mmoja:
“Mwalimu Cecilia hawezi kuja leo.”
“Umejuaje?” aliniuliza yule mwanafunzi lakini sikumpa jibu maana nilijishtukia kwamba nilichokifanya sicho.
Tulifanya kwanza usafi kisha baadaye tukapigiwa kengere na kwenda mstarini kwa ajili ya kuingia madarasani kuanza masomo.
Tulipoingia tu darasani, mwalimu wa somo la kwanza alikuja. Lakini alisahau kitabu kimoja kwenye ofisi ya walimu, akanituma mimi niende kumchukulia kwenye meza yake.
Nilipofika kule, mwalimu mmoja akaniuliza ninachokitaka, nikamwambia kitabu cha Mwalimu Paschal. Aliangalia mezani kwa mwalimu huyo na kuniambia kile cha kijani pale.
Wakati nakifuata kitabu hicho, Mwalimu huyo akasema:
“Basi unaambiwa ameamka asubuhi ya leo makalio yote yamechanika na vidonda juu. Huko alipo hawezi kusimama wala kukaa. Ni maumivu tu. Wachawi bwana.”
Mwalimu mwingine aitwaye Mage akadakia:
“Tena nasikia wachawi wanaweza kukuchukua ukaenda kulima. Mimi kuna dada’angu alichukuliwa na wachawi akaenda kulimishwa shamba kubwa, alipoamka asubuhi alikuwa amechoka mwili wote, hana hamu nao.”
Mwalimu mwingine akadakia pia:
“Sasa hao wachawi wampige bakora Mwalimu Cecilia shida yao nini hasa? Au wanamuona anaringa mtaani?”
Mara akadakia mwalimu mwingine na kusema:
“Mchawi hana sababu. Lakini mwenyewe nilipoongea naye kwenye simu amesema ataenda kwa mganga ili awatoe roho waliomchezea, hivi pale alipo anasubiria kupona tu.”
Niliondoka kwenye ofisi hiyo nikiwa na jibu kamili. Na utabiri wangu ulitimia hapo. Kwamba Mwalimu Cecilia asingefika shuleni siku hiyo.
Wasiwasi wangu mkubwa ulikuwa juu ya tamko la mwisho la yule mwalimu aliyesema hivi:
“Mchawi hana sababu. Lakini mwenyewe nilipoongea naye kwenye simu amesema ataenda kwa mganga ili awatoe roho waliomchezea, hivi pale alipo anasubiria kupona tu.”
Nilijikuta nikiogopa. Nilijua Mwalimu Cecilia anataka kuniua mimi na mama. Hivyo nilisoma kwa tabu sana siku hiyo. Akili yangu yote ilitaka nirudi nyumbani kumwambia mama juu ya madai ya Mwalimu Cecilia kutaka kutuendea kwa mganga. Nilijua mama angekasirika sana na pengine usiku wa siku hiyo tungerudi tena nyumbani kwake kumfanyia kitu kibaya zaidi.
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 07


Nilijikuta nikiogopa. Nilijua Mwalimu Cecilia anataka kuniua mimi na mama. Hivyo nilisoma kwa tabu sana siku hiyo. Akili yangu yote ilitaka nirudi nyumbani kumwambia mama juu ya madai ya Mwalimu Cecilia kutaka kutuendea kwa mganga. Nilijua mama angekasirika sana na pengine usiku wa siku hiyo tungerudi tena nyumbani kwake kumfanyia kitu kibaya zaidi. SASA ENDELEA … Muda wa kutoka shuleni ulipofika naweza kusema mimi nilikuwa mwanafunzi wa kwanza kuwa mbele ili niwahi nyumbani. Baadhi ya wanafunzi wanzangu walinishangaa, wengine waliniita lakini sikugeuka kuwasikiliza, moyoni nilisema si wao tu, hata kama mwalimu mkuu ndiyo angeniita nisingegeuka. Kufika nyumbani niliita mara mbili bila kumsikia mama akiitika. Nikaita mara ya tatu, nikasikia akiitika kwa sauti nzito sana kama ya kiume na mwanaume mwenyewe mzee, lakini mwenye nguvu zake. “Unasemaje wewe?” Sauti hiyo ilitokea chumbani kwake , nikaingia bila kupiga hodi. “Mama. Nasikia Mwalimu Cecilia amepanga kutuendea kwa mganga wa kienyeji.” “Kwa ajili gani? We umesikia kwa nani?” “Nimesikia walimu wakisema, kwa sababu tumemchapa fimbo usiku.” “Hao walimu wamejua ni sisi?” “Hapana, hakuna aliyesema ni sisi, ila nimemsikia mwalimu mmoja akisema Mwalimu Cecilia amesema atakwenda kwa waganga ili awashughulikie wachawi waliomchapa usiku.” Mama alicheka sana, alicheka mpaka akakaa chini. Hapo alikuwa na sauti yake ya kawaida na nilikuwa nataka tumalize hili ili nimuulize kisa cha kunitolea sauti nene kama ile. Alipomaliza kucheka mama alisema: “Namtaka huyo mwalimu aliyesema. Na yeye leo itakuwa zamu yake, sitaki ujinga mwaka huu.” “Ah! Mama! Yaani Mwalimu Cecilia tumemshughulikia, sasa unataka na mwalimu huyu naye?” “Ndiyo, tena lazima leoleo ashughulikiwe.” “Mama, mimi naogopa sana,” nilijitetea, lakini mama akaja juu akisema ni lazima akale fimbo yule mwalimu. Lakini ghafla akaniuliza: “Kwanza hebu nipe maelezo kamili yalivyokuwa mpaka ukajua hilo suala la huyo mwalimu kwenda kwa mganga wa kienyeji.” Niliamua kumsimulia mama kwa kuanza kumwambia kuwa, niliingia ofisi ya walimu, nikamsikia Mwalimu Paschal akisema kuwa, Mwalimu Cecilia aliamka asubuhi ya leo makalio yakiwa yamechanika na vidonda juu. Huko nyumbani kwake alipo hawezi kusimama wala kukaa. Ni maumivu tu. Akasema wachawi bwana! Mama akaniuliza, sasa kwa kusema hivyo ndiyo ameahidi kutuendea kwa mganga wa kienyeji? Nikamwambia asubiri kwanza nimalize mazungumzo. “Haya mwanangu, nakusikiliza, malizia basi.” “Mwalimu mwingine anaitwa Mage akadakia, akasema, ‘tena nasikia wachawi wanaweza kukuchukua ukaenda kulima. Mimi kuna dada ‘angu alichukuliwa na wachawi usiku akaenda kulimishwa shamba kubwa, alipoamka asubuhi alikuwa amechoka mwili wote, hana hamu nao.’ “Sasa hapo ndiyo ina maanisha watatuendea kwa mganga mwanangu?” alidakia tena mama. “Mama, subiri kwanza nimalize.” “Haya binti yangu, sema mpaka mwisho sasa.” “Kuna mwalimu mwingine pembeni akadakia, akauliza, sasa hao wachawi wakampige bakora Mwalimu Cecilia shida yao nini hasa? Au wanamuona anaringa mtaani?’ “Yule Mwalimu Paschal naye akajibu, akasema, ‘mchawi hana sababu. Lakini mwenyewe nilipoongea naye kwenye simu amesema ataenda kwa mganga ili awatoe roho waliomchezea, hivi pale alipo anasubiria kupona tu.’” Mama alicheka tena huku akisema: “Huyo Mwalimu Paschal usiku wa leo tunaye. Tena nataka wewe mwanangu ndiyo uifanye kazi hiyo. Tutakwenda wote, lakini tukifika, mimi nitabaki nje, wewe utaingia ndani. Ukifika umchape mpaka wewe mwenyewe uridhike, sawa?” “Sawa mama.” Tuliendelea na mambo mengine ya nyumbani. Mama aliniambia usiku wa siku hiyo mimi ndiyo niende kumwamsha kwa ajili ya safari ya kwa Mwalimu Paschal. Mimi siku hiyo ndiyo nilitangulia kwenda chumbani kwangu. Nilipopanda kitandani sikuchukua muda mrefu, usingizi ukanipitia. Niliamka nikiwa najisikia nashikwashiwa miguu, nikashtuka. Kuangalia hivi kumbe mama. “Mbona hujaamka, utaiweza kazi hii kweli?” “Nitaiweza mama,” nilimjibu huku nikinyanyuka kitandani. Alinishika mkono kama anayenipokea. Tukatoka nje ambako mama aliniamuru mimi ndiyo niongoze safari ya kwenda kwa Mwalimu Paschal. Ilikuwa kufumba na kufumbua, tulitua nje ya nyumba ya mwalimu huyo. Hali ya hewa ilikuwa ya upepo mkali kila kona. Tulitembea kuelekea upande wenye mlango mkubwa, tukaingia ndani huku mimi nikiwa mbele ya mama. Ghafla mama akanishika mkono, nilipogeuka akaniambia: “Mimi nakusubiri nje, hakikisha unamshikisha adabu huyo mwalimu.” Nilimwitikia kwa kutingisha kichwa kisha nikaendelea kwenda ndani, mama akarudi nje. Nilisimama sebuleni, nikaangaza kulia na kushoto kisha nikanyoosha mkono mbele ili kupata mwelekeo wa chumba cha mwalimu huyo, nikabahatika kukipata. Nilikwenda kusimama mlangoni, nikapiga mlango kwa kofi moja tu, ukafunguka wenyewe. Nilipoingia ndani, hakuwepo Mwalimu Paschal wala mdogo wake achilia mbali binadamu mwingine yeyote yule. Nilisimama nikiwa nimechoka sana, nikapiga mwayo mmoja na kutoka nje. Nilimkuta mama amekaa kwenye jiwe, aliponiona akasimama ghafla. “Imekuwaje?” “Hayupo.” “Haweizekani!” “Kitandani hamna mtu mama.” “Hata mke wake?” “Hata nduguye. Kitanda cheupe.” “Sasa umeshindwa kupata mwelekeo wa mahali alipo?” “Nilitaka kusikia kwanza wewe unasemaje?” “Mtafute haraka sana.” Nilisimama, nikanyoosha mkono ili kupata mweleko wa alipo Mwalimu Paschal. Je, unajua nini kilitokea hapo?
 
SEHEMU YA 08


“Imekuwaje?” “Hayupo.” “Haweizekani!” “Kitandani hamna mtu mama.” “Hata mke wake?” “Hata nduguye. Kitanda cheupe.” “Sasa umeshindwa kupata mwelekeo wa mahali alipo?” “Nilitaka kusikia kwanza wewe unasemaje?” “Mtafute haraka sana.” Nilisimama, nikanyoosha mkono ili kupata mwelekeo wa alipo Mwalimu Paschal. SASA ENDELEA … “Ni huku mama, mahesabu yanasema hivyo,” nilimwambia mama naye akaniambia niende, nishughulike naye halafu mimi nimkute palepale aliposimama. Nilifanya mambo yangu, kufumba na kufumbua nilijikuta nipo kwenye kijumba kimoja cha ajabuajabu sana, mwanamke mmoja mtu mzima alisimama nje huku akisemasema maneno ambayo yaliashiria hakuwa na akili timamu. Nilimwamkia akawa anacheka ndipo nilipobaini ni kichaa. Nikajigeuza kurudi katika hali ya uchawi kwani mpaka namwamkia nilikuwa nimejibadili kuwa binadamu kama yeye. Niliingia ndani ya nyumba hiyo kwa ujasiri nikiamini ningemkuta Mwalimu Paschal. Nilipofika kwenye chumba kimoja nilikuta mtoto mdogo amelala, lakini pia dira yangu ya kichawi ikaonesha kwamba, Mwalimu Paschal hakuwepo ndani ya ile nyumba. Niliwaza kwenda kugombeshwa na mama kwa kushindwa kumpata mwalimu huyo. Nilitoka hadi kwenye mti mmoja, nikasimama hapo. Giza lilikuwa nene, hakukuwa na mlio wowote zaidi ya vijidudu vya usiku ambavyo milio yao huashiria eneo hilo kuna msitu jirani. Niliinua mkono juu, nikaita Mwalimu Paschal. Mwalimu Paschal. Nilitumbua macho nikitaraji kumwona mwalimu huyo akija juu angani na kutua miguuni pangu lakini wapi. Niliendelea kuita kwa zaidi ya mara sita, ya saba Mwalimu Paschal alitua miguu pangu akiwa amevaa bukta tu. Sikujua alitokea kwake au ndani ya nyumba ile lakini kama ni ndani ya nyumba ile mbona dira ilinikatalia hakuwepo! Nilinyoosha tena mkono juu nikaziita fimbo ambazo zilitua kwenye kiganja cha mkono wangu wa kulia. Palepale nilianza kumchapa mwalimu huyo kwa nguvu zangu zote huku nikimwambia: “Ni kwa nini unashabikia mambo yasiyokuhusu, ni kwa nini lakini na wewe ni mwalimu?” Mwalimu Paschal hakuwa akinijibu wala kujitetea kwa njia nyingine yoyote ile zaidi ya kujishika zile sehemu ambazo nilikuwa namchapa na fimbo. Nadhani alifanya vile kuondoa maumivu kidogo. Fimbo moja ilipokaribia kwisha na mwalimu wa watu alionesha kuchoka kupita kiasi ndipo nilipoamua kumwachia huku nikimwonea huruma. Nilisimama, nikanyoosha mkono wa kulia kuelekea juu, nikasema maneno yangu ya kichawi, Mwalimu Paschal akayeyuka kama barafu. Hapo ina maana alirudi nyumbani kwake, kama ni chumbani haya, kama ni sebuleni sawa. Nilirudi alipo mama, nikamkuta. Aliponiona tu aliangua kicheko cha nguvu huku akinyoosha mkono kunipa ili anipongeze. Na mimi nilimpa mkono wangu, mama akaniambia: “Wewe ni jasiri kuliko wanaume wachawi wanaojiita majasiri. Ulimpomkosa mwalimu nyumbani naona ukaamua kumleta palepale ulipokaa.” Hapa niseme kidogo. Kwa kawaida, wachawi hata wanapokuwa majumbani wamekaa, huwa wanaona mambo ya kichawi yanayofanywa na wenzao. Mfano, mchawi amekaa mahali akiendelea na shughuli zake nje ya uchawi, sasa kama kuna wachawi wanapita kwenda kuwanga mahali yeye anawaona na anajua ni wachawi, ila mwiko mkubwa kabisa hataweza kusema. Basi, baada ya hapo mimi na mama tulirejea nyumbani. Mama akasema nikalale yeye anakwenda kukutana na wenzake wachawi kwa ajili ya kwenda kuwanga au kuroga mahali kwingine. *** Ilikuwa asubuhi yenye wasiwasi mkubwa sana kwani ndani ya nafsi kama nilisikia nikijiambia mwenyewe kwamba Mwalimu Paschal alijua kila kitu. Kwamba alijua niliyempiga ni mimi. Nikataka nisiende shuleni ikabidi nimshirikishe mama, akaniambia nimuondolee ujinga wangu, akasema: “Toka lini umesikia hayo, mchawi amempiga mtu usiku halafu akamjua ni nani? Ikitokea hivyo labda huyo aliyepigwa pia ni mchawi na kama ni hivyo hataweza kupigwa.” Kidogo nilijisikia nafuu na amani ilirejea moyoni, nikajiandaa na kwenda shuleni. Nilikuta walimu wote, hadi mwalimu mkuu wamesimama nje ya ofisi, walionekana walikuwa katika mazungumzo mazito maana hata muda wa mstarini ulipofika, hakuna mwalimu aliyekuja kusema lolote na kwa kawaida lazima mwalimu mmoja aje na kusema kisha sisi wanafunzi tuingie madarasani. “Kiranja ingiza wanafunzi madarasani,” alisema mwalimu mkuu huku walimu wengine wakiwa wanaendelea na mazungumzo yao. Tulikaa madarasani kwa saa tatu hakuna mwalimu aliyejitokeza kufundisha ndipo nilipoanza kuingiwa na wasiwasi kwamba huenda bomu la Mwalimu Paschal lilifika shuleni kwa walimu wenzake, moyoni nilijipa ujeuri na kusema kwamba endapo atatokea mwalimu wa kuchongachonga naye nitamfanyia stahiki yake kama Mwalimu Paschal. Siku hiyo pia Mwalimu Cecilia hakutokea shuleni na haikujulikana alikuwa akiendeleaje huko kwake. Mara kengele ya dharura iligongwa. Nasema ya dharura kwa sababu iligongwa kabla ya saa nne muda wa mapumziko. Wanafunzi wote tulikwenda mstarini. Cha ajabu, tuliwakuta walimu wote wameshasimama wakitusubiri sisi wanafunzi. Mwalimu mkuu alionesha ana hamu ya kutaka kuzungumza. “Nyamazeni kidogo,” alisema mwalimu mkuu maana wanafunzi tulikuwa tunaongeaongea sana. “Tumewaiteni kwa ajili ya dharura kubwa, Mwalimu Cecilia alipata matatizo ya kishirikina juzi usiku, aliingiliwa na wachawi, wakamtesa sana, wakampiga sana hivi tunavyoongea hali yake imekuwa mbaya zaidi amekimbizwa hospitali kwa ajili ya kupatiwa matibabu zaidi. Lakini kabla la Mwalimu Cecilia halijakaa sawasawa, usiku wa kuamkia leo, Mwalimu Paschal naye... Je, nini kilitokea hapo?
 
SEHEMU YA 09


“Tumewaiteni kwa ajili ya dharura kubwa, Mwalimu Cecilia alipata matatizo ya kishirikina juzi usiku, aliingiliwa na wachawi, wakamtesa, wakampiga sana hivi tunavyoongea hali yake imekuwa mbaya zaidi, amekimbizwa hospitalini kwa ajili ya kupatiwa matibabu zaidi. Lakini kabla la Mwalimu Cecilia halijakaa sawasawa, usiku wa kuamkia leo, Mwalimu Paschal naye… SASA ENDELEA … Amekumbwa na tatizo kama hilo, ameingiliwa, akapigwa sana huku akionywa eti aache tabia ya kimbelembele. Bahati nzuri, Mwalimu Paschal yeye anasema aliyemfanyia kitendo hicho kama anamjua ni mwanafunzi wa hapahapa tena ni wa kike ila ameomba apewe muda ili amkumbuke sawasawa.” Palepale niliinama kidogo nikashika tumbo, nikajibadili kuwa kiumbe mwingine, lakini mstarini nilibaki mimi kama mimi, nikatoka hadi nyumbani kwa njia ya kichawi. Nilimsimulia mama kinachoendelea shuleni. Mama bila kuchelewa, akanishika mkono tukafutika na kutua shuleni, mbele ya mwalimu mkuu, mama akamwekea mkono kwenye kichwa, mara mwalimu mkuu akabadili maneno, akasema: “Lakini hata hivyo mimi binafsi siamini uchawi. Nitamwambia Mwalimu Paschal aachane na mawazo hayo, kwani anaweza kusema ni mwanafunzi Fulani kumbe siye, ni ibilisi tu anataka kumgombanisha.” Niliwaona walimu wengine wakimkazia macho huku wakitingisha vichwa maana ilionesha mwalimu mkuu ametoa kauli ya kuwageuka. Baada ya hapo, mimi na mama tulifutika na kutua nyumbani kwa Mwalimu Paschal. Tulimkuta amekaa nje ya nyumba yake huku akijikanda kwa maji ya moto sehemu mbalimbali za mwili wake zilizokuwa zimevimba. Nilimwangalia mama ambaye naye aliniangalia mimi. Kwa pale, Mwalimu Paschal hakujua kama kuna ugeni umefika kwake. Mama alimshika kichwa na kukigeuzia juu, yaani akawa anaangalia juu bila ridhaa yake lakini haikuwa rahisi kwa yeye kujua kama anafanya kitendo hicho. Baada ya hapo, mama alimshika mkono na kumsimamisha, mwalimu akasimama wima kama mwanajeshi, lakini uso wake ulionesha anajisikia maumivu makali sana. Baada ya hapo alimshika na kumkalisha kwenye kiti, mwalimu akaa bila kupenda, ndipo alipoanza kusomewa mashitaka yake na mama. Alimwambia hivi: “Kama umekuja kwa lengo la kufundisha wanafunzi pale shuleni basi fuata hayo, kama umekuja kwa ajili ya kupambana utaondoka bado kijana mdogo. Wewe ni mtu wa kusema unamjua aliyekuchapa usiku? Unamjua ni nani? Hebu nitajie.” Mwalimu Paschal akiwa amekaa kwa unyonge alijishika kifuani na kusema: “Mimi kama nilimwona mwanafunzi wa shule ninayofundisha!” “Ulimwona wa kike au wa kiume?” “Wa kike.” “We mjinga nini? Sema ulimwona mwanafunzi wa kiume.” “Nilimwona mwanafunzi wa kiume.” “Ndiyo, ukiulizwa ujibu hivyohivyo, ulimwona mwanafunzi wa kiume.” “Nilimwona mwanafunzi wa kiume.” “Sawasawa.” Mara kwa mbali, watu wawili walikuwa wakija uelekeo wa pale kwa mwalimu. Mama akamshika kichwa Mwalimu Paschal kisha mkono mmoja akawanyooshea wale watu. Kidole kimoja ndicho kilichokuwa kimewanyookea zaidi wale watu, hivyo walitembea kwa kufuata maagizo ya kile kidole, yaani walikuwa wakienda jinsi kidole kinavyotaka. Walipita mbali na pale tulipokuwa tumesimama. Wakaingia kwenye uchochoro mmoja na kuendelea na safari lakini kiukweli haja yao ilikuwa kuja pale kwa mwalimu. Ghafla tena kwa mbali tuliwaona walimu, akiwemo mwalimu mkuu. Walikuwa wakija pale, mama akamwacha kumshika mwalimu, akanishika mimi na kusimama pembeni jirani kabisa na mlango mkubwa wa kuingilia ndani. Walimu walipofika walimsalimia mwenzao huku wakimpa pole. Wengine walimuuliza kama anaweza kutembea, akasema anaweza ila si kama ilivyokuwa kabla hajapigwa. “Eti nasikia aliyekuchapa ni mwanafunzi, ni kweli?” mwalimu mkuu alimuuliza. “Ni kweli.” “Wa palepale shuleni kwetu?” “Ndiyo.” “Mwanamke mwanaume?” “Mimi niliyemwona ni mwanaume.” “Pole sana.” “Asante sana.” Aliposema aliyemwona ni mwanaume, nilimwangalia mama, akawa anatingisha kichwa kukubaliana na kauli ya mwalimu yule. Hapa napenda sana kusema machache kuhusu tabia hiyo. Wapo wachawi wana uwezo huo, wanaweza kukupa maelekezo ya cha kusema mahali na ukafanya hivyo bila ridhaa yako. Na unaweza kukuta mtu anatoa jibu fulani na watu wanashangaa, halafu baada ya hapo hata yeye mwenyewe anashangaa. Mambo haya hutumika zaidi katika mahakama. Wapo watu wana kesi mbaya na wanakwenda kwa waganga wakubwa wakifika kule wanapewa dawa ambazo zitamfanya aliyemshitaki kusema maneno ya kumshangaza hakimu na wasikilizaji wengine. Basi, wale walimu waliendelea kuwepo pale mpaka mimi nikakasirika. Nikawasogelea na kusimama usawa wao kisha nikawanyooshea kidole na kukielekeza kwingine, palepale waliaga na kuondoka. Mimi na mama tukamrudia Mwalimu Paschal. Safari hii mama aliniangalia mimi tu. Nilimwambia mwalimu kama atadiriki kwenda kwa waganga ili kuturoga sisi ataanza kufa yeye na ukoo wake wote. “Tena nakwambia, ulisikie vizuri, kama utakwenda kwa waganga, wewe na ukoo wako wote mtateketea.” “Sitakwenda kwa waganga.” “Niangalie vizuri.” Mwalimu Paschal alinitumbulia macho kuniangalia vizuri. “Mimi nani?” “Wewe?” “Mimi ndiyo.” “Weweee. Wewe sikujui.” Nilimgeukia mama huku nikihema kwa nguvu. Je, unajua nini kilitokea hapo?
 
SEHEMU YA 10


“Tena nakwambia, hili ulisikie vizuri, kama utakwenda kwa waganga wewe mwalimu, wewe na ukoo wako wote mtateketea.” “Sitakwenda kwa waganga.” “Niangalie vizuri.” Mwalimu Paschal alinitumbulia macho kuniangalia vizuri. “Mimi nani?” “Wewe?” “Mimi ndiyo.” “Weweee. Wewe sikujui.” Nilimgeukia mama huku nikihema kwa nguvu. ENDELEA SASA… Nilijua angenitaja jina. Na kama ingetokea hivyo palepale ningempachika gonjwa baya ile afe na kupoteza ushahidi wa siku za baadaye. Baada ya hapo mimi na mama tulirudi nyumbani kwa njia ya kichawi. Lakini tulichofanya kabla ya kuondoka ni kumshika kichwa Mwalimu Paschal na kusema maneno ya kichawi kisha tulipomwachia alirejea katika hali yake ya kawaida na alionesha dalili kama aliyezinduka kutoka kwenye hali ambayo kwake hakuitambua. Nyumbani mimi sikukaa, nilikwenda shuleni ambapo nilikuta wenzangu wote wapo madarasani. Na mimi nilikwenda darasani kwangu, nikaenda kwenye kiti changu, nilimgusa yule mtu aliyenibadili naye akapotea nikakaa mimi. Hakuna aliyejua kama kulikuwa na binadamu feki ndani ya darasa kwani kila jambo lilikuwa likienda kama kawaida sanasana labda watu waliniona nimekuwa mpole sana siku hiyo kabla ya kurudi mimi mwenyewe. Mwalimu wa kipindi siku hiyo alikuwa mkali sana, sijui kwa nini. Na alikuwa miongoni mwa wale waliokuja kwa Mwalimu Paschal. “Sasa ni muda wa kujibu maswali kwa kila mwanafunzi mmoja mmoja atakayeshindwa nitamchapa viboko viwili, sawa?” Wanafunzi tukaitikia sawa. Alimsimamisha mwanafunzi wa kwanza, akapatia, akaja wa pili, akapatia, mimi nikawa wa saba na walionitangulia wote walipatia. Swali nililoulizwa mimi lilikuwa gumu sana, nikajua nitakosa, kabla ya kujibu nikapuliza upepo hewani. Mwalimu akawa kama anaweweseka. “Ngoja nikubadilishie swali wewe, ngoja kidogo. Halafu wewe! Lakini nadhani tuwe tumefikia mwisho wa maswali,” alisema yule mwalimu. Nilinyoosha mkono chini kwa chini, nikanyoosha kidole changu cha kulia na kuanza kukitembeza kutokea usawa wa pale aliposimama mwalimu na kuelekea mlangoni. Palepale mwalimu akachukua vitabu vyake na kuanza kuondoka. Wanafunzi wote walisimama, wengine wakawa wanacheza, wengine wanarukaruka, wako walionifuata na kuniuliza nilimfanya nini mwalimu yule mpaka akaamua kuondoka ghafla, sikuwajibu. Hatimaye darasa likawa kimya, kila mtu alikuwa amerudi kukaa akijisomea. Darasa nililokuwa nasoma mimi wanafunzi tulikuwa na uwezo wa kuwaona walimu wakiwa nje ya ofisi yao, hivyo nilikuwa nachungulia upande ule kila wakati kama nitaona jambo jipya. Mara mwalimu mkuu alitoka, akasimama akiwa amejishika kiuno. Alikuwa akiangalia upande wa darasani kwetu huku kama anazungumza. Ilionekana alikuwa akizungumza na walimu ambao walikuwa ndani ya ofisi yao. Mara walimu wengine watatu walitoka, wakasimama na mwalimu mkuu. Hapo mapigo ya moyo wangu yalianza kwenda kwa kasi, nilijua kuna jambo walimu wamelipata kutoka kwa walimu wenzao. Ghafla tena akatoka yule mwalimu aliyefungasha virago vyake, akasimama na wenzake, na yeye akawa anaongea. Sikujua nini kilikuwa kikiendelea, ghafla nikamwona mwalimu mkuu akianza kutembea kuja upande wa darasani kwetu, wenzake wakamfuata kwa nyuma, nikajua tatizo lipo kubwa sana, nilijiinamia kwa kuweka mikono kwenye dawati na kusema maneno fulani. “Nyie walimu wanakuja, walimu wanakuja tulieni,” mwanafunzi mmoja anayeitwa Simon alisema kwa sauti ya chini kidogo. Na mimi nikainua uso. Mwalimu mkuu alizama ndani, walimu wengine na wao wakaingia huku wakiwa na nyuzo za hasira. Kilichonishangaza zaidi ni kwamba, walimu wote wakanitupia macho mimi jambo ambalo lilinikera sana, nikakielekeza kidole changu kimoja chini, halafu nikawa nakichezesha kama mkia wa ng’ombe vile, walimu wakatulia. “Lakini walimu wenzangu, hili jambo tuliangalie kwa umakini zaidi, mimi nadhani twendeni tukakae ofisini kwangu na kuzungumza kwa kirefu zaidi,” alisema mwalimu mkuu. Walimu wengine wakasikika wakiunga mkono huku yule aliyetoka darasani mwanzo kabisa akiwa ametangulia. Nilizama chini ya dawati, nikafumba macho kwa muda nilipofumbua nilibadilika na kuwa mtu mwingine mchawi, lakini pale kwenye dawati langu alibaki mimi wa asili ambapo hata wanafunzi wenzangu walijua mimi nipo. Nilitoka kwa mwendo wa polepole kuelekea mlango mkubwa huku miguu nikiirusha kwa juu. Kama wanafunzi wenzangu wangeniona nilivyokuwa kwa wakati ule wote wangekimbia nje kupitia madirishani. Nilitembea kichawi hadi ofisini kwa walimu. Walimu wote, hata wale ambao hawakuwa wamekuja na wenzao darasani walikuwa kwa mwalimu mkuu. Na mimi niliingia na kusimama pembeni wao wakiwa hawanioni. “Sasa walimu ni hivi, kinachoonekana ni kweli yule mwanafunzi anaweza kuwa na nguvu za kishirikina, lakini nina wasiwasi kwamba hata yeye mwenyewe hajui,” huyo aliyesema hayo alikuwa mwalimu mkuu. “Anajua bwana, huwezi kuwa mchawi au mshirikina halafu usijue kitu,” alidakia mwalimu mwingine. Yule mwalimu aliyedakia nilimnyooshea mkono lakini sikumgusa halafu nikafanya kama namkaba koo lake kwa nguvu. Alianza kujishika koo na kutaka kuongea lakini akawa anashindwa na maneno yakamtoka kama mtu aliyekabwa. Kila alipojitahidi kusema ndipo na mimi nilipozidisha kukaba hewa lakini kwake ilikuwa kazi, akatoa macho. Lengo langu ilikuwa nimtoe roho lakini nikasita, nilijua nitasababisha balaa kubwa shuleni na hata kwenye kile kitongoji. Je, unajua nini kilitokea hapo?
 
SEHEMU YA 11


“ANAJUA bwana, huwezi kuwa mchawi au mshirikina halafu usijue kitu,” alidakia mwalimu mwingine. Yule mwalimu aliyedakia nilimnyooshea mkono lakini sikumgusa halafu nikafanya kama namkaba koo lake kwa nguvu. Alianza kujishika koo na kutaka kuongea lakini akawa anashindwa na maneno yakamtoka kama mtu aliyekabwa. Kila alipojitahidi kusema ndipo na mimi nilipozidisha kukaba hewa lakini kwake ilikuwa kazi, akatoa macho. Lengo langu ilikuwa nimtoe roho lakini nikasita, nilijua nitasababisha balaa kubwa shuleni na hata kwenye kile kitongoji. SASA ENDELEA … “Jamani ni nini hii?” aliuliza mwalimu mkuu huku akiwa anasimama na kumshika yule mwalimu niliyemtenda makuu. Alishindwa kusema, akabaki amejishika koo. Walimu wengine walisimama wakiwa wanamwangalia wasijue cha kufanya. “Mimi naona tumpelekeni hospitali,” alisema mwalimu mkuu. Hakuna mwalimu aliyeunga mkono wazo hilo zaidi ya mmoja wao kusema: “Hili kwa mtazamo wangu si tatizo la hospitali, labda tumpeleke tu kwa sababu sisi ni walimu.” “Sasa tumpeleke wapi akapate msaada?” mwalimu mkuu alihoji. Nilimtumbulia macho yule mwalimu niliyemtenda, tukawa kama tunaonana, yaani yeye alifanikiwa kuniona kwa macho yake mawili, akanyoosha mkono kama aliyetaka kusema: “Jamani huyu hapa ndiye mbaya wangu,” lakini nikampulizia upepo, akapitiwa na uwezo wa kuniona ukapotea. Niliamua kumsamehe kwa kushusha mkono na kuacha lile tendo la kama kumkaba. Mwalimu akarejea katika hali ya kawaida na kutulia, alijiachia, akakohoa sana na kupiga chafya. “Pole sana,” mwalimu mkuu alimwambia. Walimu wengine walimpa pole pia, akaitika asante huku akijishikashika sehemu mbalimbali za mwili kama anayelalamikia kwamba sehemu hizo ndizo zinazomuuma. “Kwa sasa unajisikiaje?” mwalimu mmoja aliuliza. “Kama nafuu, lakini nashangaa sana mwenzenu.” “Unashangaa nini?” “Kama nimemwona…” kabla hajamalizia kusema nilimpulizia tena upepo, akanyamaza. “Kama umemuona nani?” mwalimu mkuu alimuuliza tena. Palepale nilimnyooshea kidole mwalimu mkuu kama ninayemwonya kutojihusisha na masuala ya watu wengine, nikafanya kama namkaba koo, akakohoa ghafla, nikamwachia na yeye akatulia kimya. Mama alinifundisha kwamba ukitaka mtu unayemwangia asikukumbuke kabisa hata kama alikuona kwa bahati mbaya mfute uso kwa kiganja cha mkono wa kushoto. Na mimi nilifanya hivyohivyo, nilimfuata yule mwalimu nikamfuta uso kwa kiganja cha mkono wa kushoto. Wakati namfuta, alihisi anazibwa macho hivyo alishtuka na kupeleka mkono wake usoni kisha akafikicha macho. Nilipotoka kwa huyo nikamfuta mwalimu mkuu pia japokuwa yeye hakuwa ameniona hata mara moja, naye akapeleka mkono usoni kwa mshtuko na akasema: “Khaa! Mbona kama macho hayaoni sawasawa?” “Ooo, kumbe yanaona bwana,” alisema akiwa amekaa. Ofisi ilikuwa kimya, walimu walikuwepo lakini hakuna aliyesema lolote, walikuwa wakimwangalia mwalimu niliyemtenda. Ilionekana kila mmoja amekuwa mwoga kutoa sauti akiamini atapata matatizo kama mwenzao na ndiyo maana mwalimu mmoja alisema tatizo la yule si la kulipeleka hospitalini. Nilitoka polepole huku nikiwasonya lakini hawakusikia. Nilirudi darasani, nikapita mpaka kwenye dawati langu na kujirudishia ubinadamu kisha nikakaa. Nilipokaa tu na yule niliyemwacha akiwa ameshapotea, mwanafunzi mmoja aliniuliza: “Hivi leo una nini wewe?” “Kwani vipi?” nilimuuliza kabla sijamjibu. “Umekuwa mpole muda mrefu.” Hapa nataka kuzungumza jambo moja ili watu wajue. Katika jamii tunamoishi haya mambo yapo, tena makubwa sana. Unaweza kukaa hata kwenye siti ya daladala na binadamu wa ajabu lakini ukawa hujui. Kinachotokea ni kwamba, mtu huyo anakuwa kama boya, mwenyewe halisi anakuwa katika kuwanga. Mfano mzuri kwenye daladala, mchawi anaweza akakaa na wewe siti moja, ghafla akataka kufanya mambo yake ndani ya daladala hilohilo ndipo anapoamua kumuweka binadamu wa uongo na yeye kuanza kuwanga. Sasa, mara nyingi kama mchawi huyo utakuwa unamfahamu, atabadili tabia. Atakuwa na hali ya kinyume na ile unayoijua, hasahasa wengi huwa wapole, wasiotaka kutoa sauti au kujisogezasogeza kutoka pale walipokaa. Basi, nilimjibu yule mwanafunzi kwamba, sikuwa najisikia vizuri lakini kwa wakati huu kidogo najihisi nafuu. Ghafla mwalimu mmoja anaitwa Msafiri aliingia na kusema: “Hamjambo wote?” “Hatujambo, shikamoo mwalimu,” tulimsalimia tukiwa tunasimama. “Marhaba, nimekuja badala ya mwalimu aliyetoka kwani hajisikii sawasawa. Pale alipoishia mimi nitaanzia pale, sawa?” “Sawa.” “Haya, kaeni.” Moyoni nilijiuliza, mwalimu huyo anamaanisha ataanza kwa kuuliza maswali kama mwalimu mwenzake au? “Nina maswali hapa, hata kama yalijibiwa lakini kwa mimi yataanza upya bila kujali yaliyopita.” Huyu mwalimu alionekana kuongea kwa ujasiri kama vile alishaambiwa kilichomtokea mwenzake yeye akasema hakitamtokea, maana alikuwa akitoa sauti nzito tofauti na kawaida yake. Kingine kilichonipa mawazo zaidi ni kwamba, wakati nilipoingia kule kwenye ofisi za walimu na kuwakuta wenzake wote, yeye hakuwepo. Wengine wote walikuwepo isipokuwa wale niliowachapa usiku, yaani Mwalimu Paschal na Mwalimu Cecilia ndiyo hawakuwepo. “Lakini tukubaliane, ukikosea swali viboko, hilo sitaki mtu abishe wala apinge, sihitaji mtu aseme sawasawa au si sawasawa.” Je, unajua nini kilitokea hapo?
 
SEHEMU YA 12



KINGINE kilichonipa mawazo zaidi ni kwamba, wakati nilipoingia kule kwenye ofisi za walimu na kuwakuta wenzake wote, yeye hakuwepo. Wengine wote walikuwepo, kasoro wale niliowachapa usiku, yaani Mwalimu Paschal na Mwalimu Cecilia. “Lakini tukubaliane, ukikosea swali viboko, hilo sitaki mtu abishe wala apinge, sihitaji mtu aseme sawasawa au si sawasawa,” alisema. SASA ENDELEA … Nilikasirika sana, nilimwona ni mwalimu aliyekuja kwa sababu maalum na si ajabu alinilenga mimi kwani wakati anasema atakayekosa atamchapa viboko alikuwa akiniangalia. Niliamini ili anyooke, alihitaji adhabu kali itakayomshikisha adabu moja kwa moja na kuacha tabia hiyo. Kabla hata hajaanza kuuliza hayo maswali yake nilijibadili palepale nilipokuwa nimekaa. Kwa mtu mwingine aliniona nipo kama nilivyo, lakini mwenyewe sikuwa hivyo. Nilimnyooshea mkono nikafanya kama nampiga makofi ya mashavuni, kukasikika mlio wa pa! Pa! Pa! Wakati mlio huo unasikika yule mwalimu alikuwa akinesea kulia na kushoto kama inavyokuwa kwa mtu anayepigwa vibao. Wanafunzi wote walikuwa wakilishuhudia tukio hilo huku wakishikwa na mshangao. Mwanafunzi mmoja aliyekuwa kwenye dawati la jirani yangu alinigeukia na kuniuliza kama naona mwalimu anavyofanya, nikamjibu ndiyo. Yeye aliniona mimi nipo kawaida kumbe mwenzake nilikuwa namshughilikia yule mwalimu. Nilipoacha, mwalimu akasimama kwa muda, akajishika mashavu yote huku akijisugua, alikuwa akisikia maumivu makali sana. Mara, alituangalia wanafunzi wote kwa zamu kisha akasema: “Endeeleni na kujisomea, mwalimu atakuja baadaye.” Alitoka kurudi ofisini huku mkononi amebeba vitabu vyake alivyokuja navyo. Darasa lilibaki kimya kwa muda, baadaye minong’ono ya hapa na pale ilitawala, kila mwanafunzi alionekana akiongea na mwenzake. Yule mwanafunzi jirani yangu akanigeukia na kuniuliza: “Hivi hawa walimu wanakumbwa na kitu gani wakiingia humu darasani?” “Mh! Sijui wenyewe bwana. Mimi sijui lolote. Kwanza akili yangu haiko sawasawa,” nilimjibu hivyo, lakini akaendelea kuuliza: “Au humu darasani siku hizi kuna majini?” “Huenda. Unajua shule nyingi zina majini siku hizi.” “Yatakuwa yanatoka wapi?” “Baharini.” “Aaa. Sasa mbona madarasa mengine hayana?” “Majini yanaanza na darasa moja baadaye yanahamia darasa lingine.” Hayo yalipita, wanafunzi walikuwa wamekaa kwa majonzi, hofu na wasiwasi, lakini mimi sikuwa na hali hiyo kwa sababu nilikuwa ndiye niliyesababisha matukio yote. Mara, mwalimu mkuu aliingia. Alionekana anataka kusema jambo, alisimama kwa muda mbele karibu na ubao lakini hakutoa sauti. Alituangalia wanafunzi wote kisha akatoka. Nilijua wanakwenda kufanya kikao lakini moyoni niliamua safari hii nisiende halafu nijue nini matokeo yake. Mara tukasikia kengele ikigongwa, wanafunzi tukatoka kwenda mstarini. Mwalimu mkuu peke yake ndiye aliyekuja mstarini. Alisimama kwa muda kama mtu aliyekuwa akisubiri wanafunzi watulize kelele ndipo aongee alichotaka kuongea. Baada ya kama sekunde fulani hivi walimu wengine walitokea wakaja kusimama jirani na mwalimu mkuu huku wakionesha sura za simanzi. Ilikuwa hali mbaya sana kila mwanafunzi alikuwa ametulia mstarini. Mwalimu mkuu akaanza kwa kusema: “Nadhani kila mmoja anajua tunapopiga kengele nje ya utaratibu wa siku zote, yaani saa nne, mchana na muda wa kuondoka basi kuna sababu maalum, si ndiyo jamani?” Wanafunzi wote tuliitikia ndiyo. Akaendelea: “Kuna tatizo kubwa limeingia hapa shuleni kwetu. Baadhi ya walimu limewatokea majumbani, lakini wengine limewatokea hapahapa shuleni. Si vizuri niliweke wazi hilo tatizo, ila sisi kama walimu tumekaa, tumejadiliana na kuamua kuwapa likizo ya muda.” Cha kushangaza, baadhi ya wanafunzi walipiga mayowe ya furaha, mwalimu mkuu akashangaa. Mwalimu mmoja akamwambia kuwa wengine wanafurahi kwa sababu hawalijui hilo tatizo, wangelijua wasingeshangilia. Hata hivyo mwalimu mkuu hakuwa tayari kuliweka wazi. Alisema tuondoke mpaka siku tutakayoitwa tena kurejea shuleni hapo. Palepale wanafunzi tulitawanyika, wengine walirudi madarasani kuchukua madaftari yao, wengine waliyokuwa nayo waliondokea hapo kwenda majumbani. Lakini njiani wanafunzi walionekana wakitembea makundimakundi huku wakijadiliana. Wengine walikuwa wakitaka kujua kuna nini kilitokea shuleni. Wanafunzi wa darasani kwangu ndiyo waliokuwa wakijua na kuwaambia nini kimetokea. Nilipofika nyumbani, nilimkuta mama anachambua mboga ya kisamvu, aliponiona akashtuka na kuniuliza: “Kuna nini tena leo?” Niliachia tabasamu na yeye akacheka. Alishajua hakuna kitu kizito sana ndiyo maana nilitabasamu. Nilikaa jirani yake na kuchukua majani ya ile mboga na kuanza kumsaidia kuchambua. “Mama walimu wameturudisha majumbani. Wamesema wametupa likizo fupi hadi hapo watakapotuambia turudi shuleni.” “Kisa?” mama aliniuliza akiacha kchambua majani aliyoyashika mkononi. Nilimweleza kisa chote mwanzo hadi mwisho yaani hadi vile nilivyowafanyia wale walimu. Mama akawa ananisikiliza huku amenitumbulia macho. Nilipomaliza alicheka sana akanipa mkono ili kuugonga, nikafanya hivyo. “Unajua kwanini wamewapa likizo?” aliniuliza mama. “Sijui mama.” “Wanataka kuleta mganga shuleni.” “Ili?” “Ili wamjue ni mwanafunzi gani mwenye uchawi.” “Mama wakinishika mimi je?” “Hapo ndipo pa kupashughulikia sasa.” “Tufanyeje?” “We si unajua kila kitu? Kazi ni kwako tu.” Yale majani ya mboga niliyoyashika kwa ajili ya kuchambua niliyarudisha kwenye ungo na kuwaza maneno ya mama na jinsi ya kuyafanyia kazi. Je, unajua nini kilitokea hapo? Usikose
 
SEHEMU YA 13



Nilimweleza kisa chote mwanzo hadi mwisho yaani hadi kile nilichowafanyia wale walimu. Mama akawa ananisikiliza huku amenitumbulia macho. Nilipomaliza alicheka sana akanipa mkono ili kuugonga, nikafanya hivyo. “Unajua kwanini wamewapa likizo?” aliniuliza mama. “Sijui mama.” “Wanataka kuleta mganga shuleni.” “Ili?” “Ili wamjue ni mwanafunzi gani mwenye uchawi.” “Mama wakinishika mimi je?” “Hapo ndipo pa kupashughulikia sasa.” “Tufanyaje?” “We si unajua kila kitu. Kazi ni kwako tu.” Yale majani ya mboga niliyoyashika kuchambua niliyarudisha ndani ya ungo na kuanza kuwaza maneno ya mama na jinsi ya kuyafanyia kazi. SASA ENDELEA … “Mh! Mbona kama kazi kubwa, nitaweza kweli? Ina maana mama yuko tayari mimi mwanaye niadhirike? Maana nikishikwa uchawi mimi watu wote watajua nimefundishwa na mama,” nilisema moyoni. Niliamua jambo moja kutoka moyoni, kushughulika na walimu ili kama kweli kuna zoezi la kuwaleta waganga shuleni life haraka sana. “Nitakusaidia mwanangu, naona kama unawaza sana,” alisema mama, maneno hayo yaliamsha furaha ndani ya nafsi yangu. “Sikia mwanangu, usiku wa leo mimi na wewe tutatoka, tutakwenda kushughulika na walimu hao, tutajua cha kufanya, hakuna litakalofanyika kuhusu wewe. Hakuna mganga wala mganguzi atakayekuja shuleni, tulia.” Baada ya hapo niliendelea na mambo mengine ya nyumbani, nilikwenda kuteka maji bombani, nikaenda kununua vitu fulani sokoni kisha nikasubiri usiku uingie ili tukatimize lile la kutoka na mama kwenda kufanya mambo yetu. Usiku wa siku hiyo, mama alikuja chumbani kwangu akiwa amevaa vazi aina ya kaniki. Alivaa kwa mtindo wa kukatiza kiunoni na nyingine kwenye mabega. Hakuniamsha kwa kuwa alinikuta sijalala. Tulipokutananisha macho aliinua mikono juu kama anayeniambia njoo hapa. Nilinyanyuka kitandani polepole kisha nikashusha miguu chini na kusimama, nikatembea kumfuata pale alipo. Nilipomfikia, mama alinishika kichwa, kufumba na kufumbua tukatua chini ya mti mmoja mkubwa. Wakati natoka kitandani sikuwa nimevaa nguo zaidi ya nguo ya ndani tu. Mama alivua upande mmoja wa kaniki na kunivisha huku akisema: “Usionekane na binadamu mwenye macho ya kawaida kama walimu wako.” Tulitembea kwa miguu kutoka pale chini ya mti hadi kwenye kichaka chenye majani makavu. Hiki kichaka kilikuwa kimezungukwa na pori, mpaka leo hii sijajua lile ni eneo gani na wala sikuwahi kumuuliza mama, naye hajawahi kuniambia. “Hiki ni kichaka chenye dawa ya kutuliza ubongo, unaijua dawa hiyo?” “Siijui mama, kazi yake nini?” “Kazi yake ni kuushika ubongo wa binadamu kuwa kama mpira, binadamu hawezi kuwaza kitu unachokikusudia. Walimu wote tutawapa, hakuna atakayewaza kumfuata mganga, maana watasahau hata kuongelea habari za huyo mganga” alisema mama. Ulikuwa usiku mnene, lakini tuliweza kwenda kwenye mti mmoja mkavu, una majani mapana yaliyokauka, matawi madogo madogo. Ukiuangalia kwa makini unaweza kuufananisha na mkungu lakini wenyewe mdogo. Mama alisema mizizi ya mti ule ndiyo dawa ya kuuzubaisha ubongo wa binadamu. Alisema mti ule una tabia ya kutoota pamojapamoja jambo ambalo wahenga waliamini kizazi chake kinasahau tofuti na miti mingine ambayo huota kwa kufuatana. Kuitoa ile mizizi hatukuwa tunachimba bali mama alisimama, akaangalia juu, akasema maneno mawili matatu, mizizi yenyewe ikaanza kutoka kuja juu ya udongo na kujipanga kama kuni ndogo. Baada ya hapo tuliichukua na kurejea nyumbani. Hatukuweza kulala. Kwenye saa nane usiku, tulianza kazi ya kuisaga ile mizizi hadi kuwa unga baada ya hapo tukachanganya na unga wa kawaida, kisha akasema: “Huu unga, kila mwalimu anatakiwa ale kwenye uji, chai au ugali, lakini hata kwenye mboga, ndipo dawa yetu itafanya kazi vizuri.” “Kwa hiyo kumbe anaweza kula kwenye chakula chochote kile?” nilimuuliza. “Ee, ilimradi ale.” “Lini sasa?” “Lini sasa maana yake nini? Wewe umesema mmerudishwa shule hadi mtakapotangaziwa unadhani na wao suala la kumleta mganga shuleni watakaa nalo wiki nzima? Uende usiku huu kabla hakujakucha.” “Ha! Mama si nitawakuta wamelala?” “Sasa ukiwakuta wamelala si ndiyo vizuri watakuwa wamekurahisishia kazi.” “Sasa si watakuwa hawajapika mama?” “Wewe usiwe mjinga, chukua unga ndani humu. Changanya na maji, halafu tia hiyo dawa, nenda kwa walimu wako, kila mmoja umlishe akiwa usingizini.” Ndipo nilipoanza kupata picha kwamba, kumbe naweza kuwalisha ile dawa walimu wakiwa kitandani. Sikumuuliza mama swali lingine, ila nilisimama, nikaenda jikoni ambako nilichota unga kwenye bakuli, nikapitia maji na kurudi kuchanganya na ile dawa. Baada ya kukoroga vizuri, nikawa nimeshika bakuli lenye uji mzito sana. Nilimuaga mama kwamba aniombee kwa Mungu nifike salama na nifanikiwe kuwalisha dawa walimu wote wa shuleni. Nilishika bakuli mkono wa kulia, nikatoka hadi nje na kusimama katikati ya uwanja wa nyumba yetu. Niliinua mguu mmoja na kuupiga chini, kufumba na kufumbua nilitua kwenye genge la wachawi ambako ndiko tunakokutania mara kwa mara. Mzee mmoja alishangaa kuniona peke yangu tena nikiwa na bakuli mkononi, akauliza: “Lengo lako lilikuwa kufika wapi?” Nilicheka sana, kwani ni kweli sikuwa na lengo la kutua pale ila nilifanya makosa wakati natoka nyumbani sikupiga dira mapema. Mchawi anapotaka kwenda mahali kwa njia ya uchawi ni lazima awe na dira kama atakosa dira atajikuta anafika kwenye genge au kambi ya kukutania wachawi wa eneo lake. Basi, sikumjibu, nikashika njia ya dira ya kufika kwa Mwalimu Cecilia. Kufumba na kufumbua nikatua nje ya nyumba yake. Nilitembea hadi kwenye mlango mkubwa. Nilisimama na kujinyoosha sana kisha nikapiga mwayo, ghafla nikatokea sebuleni. Nikasimama kwenye mlango wa kuingilia chumbani, nikafanya kama pale nje, kufumba na kufumbua nikawa chumbani kwa mwalimu huyo. Je, unajua nini kilitokea hapo?
 
SEHEMU YA 14



Basi, sikumjibu, nikashika njia ya dira ya kufika kwa Mwalimu Cecilia. Kufumba na kufumbua nikatua nje ya nyumba yake. Nilitembea hadi kwenye mlango mkubwa. Nilisimama na kujinyoosha sana kisha nikapiga mwayo, ghafla nikatokea sebuleni. Nikasimama nje ya mlango wa kuingilia chumbani, nikafanya kama pale nje, kufumba na kufumbua nikawa chumbani kwa mwalimu huyo. SASA ENDELEA … Nilimkuta amelala usingizi ule wa fofofo, hajitambui kwa lolote lile, tena alikiwa akikoroma kwa sauti ya juu. Nilipanda kitandani, nikasimama kwa muda halafu nikashuka. nilifikiri kwa muda mfupi, nikapata wazo kwamba kabla ya kumlisha dawa mwalimu huyo nimpe adhabu kidogo. Nilimwita kwa ishara ya mkono naye akaamka na kutoka kitandani polepole, akasimama akiniangalia. Katika hali hiyo ingwa alikuwa ameamka na kusimama huku akiningalia lakini mwenyewe hakuwa kijua kuwa amemka na yupo na mimi chumbani mle. Niliangaza kila kona ndani ya chumba chake nikaona boksi la vitabu, nikaliendea. Nilipolinyanyua lilikuwa zito sana, nikamwamuru alibebe, akalibeba kisha nikamwamuru atembee mpaka mlangoni, akatembea akiwa bado amebeba boksi lile. Nilimfungulia mlango, akatoka na boksi lake kichwani hadi sebuleni huku akiwa amekunja uso kuashiria kuwa ameelemewa na uzito. Kule sebuleni nilimtangulia, nikasimama pembeni, nilichofanya nikawa namnyooshea kidole ambapo yeye akawa anafutisha, kidole changu kilipoelekea, akaenda mpaka ukutani na kumrudisha hadi chumbani. Nilimfanyia hivyo kama mara ishirini hadi nilimwona amechoka, jasho jembamba lilimchuruzika kwa sababu ya uzito wa lile boksi na vitabu vyake ndani pamoja na kule kutembeatembea kwa nenda rudi, nenda rudi. Tulirudi chumbani akatua boksi, nikampandisha kitandani, haikupita muda mrefu akarudi katika hali yake ya usingizi kama nilivyomkuta pale nilipokuwa nikiingia. Baada ya muda mfupi akiwa anakoroma kwa usingizi ndipo nilipomnywesha ile dawa. Hapa kabla ya kuendelea kusimulia niweke wazi jambo ambalo pengine wengi mlikuwa hamlifahamu. Ni kwamba, mchawi anapokulisha dawa yake wewe ukiwa usingizini, utakuwa unaota ndoto na ndoto hiyo utakuwa unaota uko kwenye shughuli yoyote ile yenye watu wengi mnakula nyama. Hivyo kama itatokea unota unakula nyama kwenye shughuli ujue kuwa kuna uwezekano ulikuwa ukinyeshwa dawa au kulishwa nyama na mchawi. Mara nyingi sana unapotokewa na hali hiyo, yaani kulishwa dawa au hata nyama, ukiamka asubuhi utajikuta tumbo limejaa au kuhisi kitu kama kuvimbiwa. Wengine wanaweza kushinda mchana kutwa wakiwa hawajisikii vizuri. Basi, baada ya kumlisha zile dawa nilitoka nje kwa staili ileile kama nilivyoingia na kuondoka zangu. Sikurudi nyumbani, nilisimama nje nikatafuta mwelekeo wa kwenda kwa mwalimu mwingine kumnywesha dawa hiyo. Usiku huo nilizunguka sana kwa kwenda kwa kila mwalimu hadi ilipofika saa kumi alfajiri nilikuwa nimewamaliza wote na kurudi nyumbani. Nilimkuta mama amekaa nje akinisubiri. Lakini alikaa katika hali ya kichawi, yaani kama angetokea mtu wa kawaida asingejua kama pana mtu pale nje. Alinipokea kwa furaha hadi ndani huku akinipongeza kwamba nimezidi kuwa jasiri na kunihakikishia kuwa sasa kazi nilikuwa naiweza vilivyo. “Si umewamaliza wote?” aliniuliza mama kwa shauku. “Nimbakishe nani mama? Walimu wote hawana kazi. Halafu nikawa nawapa adhabu, mwalimu mmoja nilimbebesha boksi la vitabu, mwingine nilimtoa hadi nje na jembe akalima kwanza mpaka nilipohakikisha kuwa amechoka ndipo nikamlisha dawa na kwenda kwingine. Mwalimu mwingine nilimpigisha deki nyumba nzima, alipomaliza akiwa hoi kwa kuchoka ndiyo nikamlisha dawa yangu. Mama alicheka sana, alicheka hadi akataka kuanguka. Kwake ilikuwa furaha sana kuona naweza kufanya mambo makubwa kama hayo tena nikiwa peke yangu. “Wewe binti yangu ni kiboko. Umeweza kweli!? Umekua sasa, wewe ni zaidi ya mama yangu mzazi, nakupenda sana mwanagu,” mama aliniambia huku akinishikashika sehemu mbalimbali za mwili wangu. Kesho yake asubuhi, mwalimu mmoja alipita kila nyumba na kusema wanafunzi wote tunatakiwa turejee shuleni kesho kutwa yake ili tuendelee na masomo yetu. Tulipofika shuleni keshokutwa yake, kama kawaida masomo yalianza. Sikusikia cha uchawi wala nini, dawa niliyowalisha walimu iliwafanya washindwe kutekeleza jambo walilokuwa wamepanga. Ila sasa kwa kuendelea kuwakomesha nikaanza kuwachezea walimu palepale shuleni bila ya wao kujua kinachoendelea. Mfano wa hilo, siku moja walimu walituagiza kwenda na majembe kwa ajili ya kulima shamba la shule. Mimi nilipofika na jembe langu wakati wa kulima ulipofika, nilimshikisha mwalimu mmoja bila mwenyewe kujua, akaenda kulima lakini akionekana anayelima ni mimi. Je, unajua nini kilitokea hapo?
 
SEHEMU YA 15



Tulipofika shuleni keshokutwa yake, masomo yalianza. Sikusikia cha uchawi wala nini. Ila sasa kwa kuendelea kuwakomesha nikaanza kuwachezea walimu palepale shuleni. Mfano siku moja, walimu walituagiza kwenda na majembe kwa ajili ya kulima shamba la shule. Mimi nilipofika na jembe langu, nilimshikisha mwalimu mmoja bila mwenyewe kujua, akaenda kulima lakini akionekana anayelima ni mimi. SASA ENDELEA … “Huyu mwalimu alilima mimi nikiwa nimesimama na walimu wengine wakadhani ni yule mwalimu anayelima. Ilifika mahali niliwachukua walimu wengine na kuwashikisha majembe ya wanafunzi wengine ili na wao waanze kulima. Walimu wote wakawa wanalima na wanafunzi waliokosa walimu wa kuwapokea majembe. Walilima bila wao kujijua kama wanalima na wanafunzi walijua wanalima wenyewe bila walimu, lakini usahihi ni kwamba walimu walikuwa sambamba nao ila kwa macho ya kawaida haikuwa rahisi kwa mtu ambaye si mchawi kuona. Ilifika mahali mwalimu mkuu akasema wanafunzi turudi shuleni. Nilimnyang’anya jembe langu yule mwalimu kisha nikawasukumia upepo wanafunzi wengine ambao nao walikwenda kunyang’anya majembe yao kwa walimu. Hayo yote yalifanyika kimazingara. Baada ya walimu kuachia majembe yetu, nikawaachia ufahamu ambapo walijikuta wamechafuka sana miguuni kwa sababu udongo wa shamba la shule ni ule mwekundu. Walimu wote walishtuka na kukimbiakimbia huku na kule wakisema wamepatikana na wachawi. “Ni nini jamani? Hata mimi?” mwalimu mkuu naye alisema akiruka kutoka sehemu aliyosimama kwenda nyingine. Bahati nzuri ni kwamba, wanafunzi waliokuwa wakilima na sisi tusiolima wote tulichafuka miguu, kwa hiyo hawakuwa na wa kumsingizia kwamba anahusika. Mwalimu mkuu aliamuru wanafunzi na walimu wote tukimbie kurudi shuleni ambako mambo yote yangejulikana. Tukiwa njiani, baadhi ya walimu walilalamika kuchoka, mmoja akasema ameumia kidole lakini hakumbuki ni wapi alijiumiza. Tulipofika shuleni mwalimu mkuu akasema wanafunzi wote tusimame katika mstari mmoja ili aongee, walimu wake wakaenda kusimama jirani na yeye. “Jamani wanafunzi, wote kilichotokea kule mmekiona, walimu wenu si mnawaona, wamechafuka miguuni mpaka kwenye magoti, tena afadhali sisi walimu wa kiume, wa kike wao wamechafuka zaidi sababu wanavaa sketi na magauni.” Nilitamani kumuuliza mwalimu mkuu kwa hiyo hoja yake ni nini kwa maneno yake yale, lakini nilijizuia tu kwa sababu ya heshima. “Sasa kinachoonekana hapa walimu walikuwa wakilimishwa na wachawi,” alisema mwalimu mkuu. Wanafunzi wote tulibaki kimya, naamini kila mmoja wetu alikuwa akiwaza linalomjia kwenye ubongo wake. Sikuwa na wasiwasi kwa sababu nilishawatengeneza wote, hakuna aliyekuwa na ubavu wa kusema waletwe waganga ili kumkamata mchawi shuleni. Wakati mwalimu mkuu akiendelea kuzungumza, nilijigeuza, nikatoka mstarini huku taswira yangu ikiendelea kuonekana mstarini. Niliwafuata walimu, nikawapulizia upepo wa kutoka kinywani mwangu kisha nikawachukua wanafunzi nane waliokuwa mstarini wakaja kusimama pale wakawa walimu, wale walimu nikaenda nao kwenye darasa moja ambapo niliwabebesha madawati. Kila mwalimu mmoja alibeba dawati moja lenye kuchukua wanafunzi wawili. Baada ya kubeba madawati, niliwatoa hadi mstarini kisha nikawazungusha sehemu mbalimbali za shule. Madawati ni mazito sana, lakini walilazimika kubeba kwa sababu ya nguvu za kichawi. Nilimwona mwalimu mkuu akizogoana na wale wanafunzi waliosimama jirani yake. Alikuwa akiwaambia waongee wanachotaka lakini wakawa wanagoma, sasa akawa anawaambia kama wao wenyewe hawataki kuongea nani ataongea badala yao? Kumbe hakujua kama wale ni wanafunzi ambao nao akili zao zilivurugika kwa sababu ya uchawi. Wale walimu niliowabebesha madawati walianza kutokwa na jasho sasa, waliloa nguo, mashati ya walimu wa kiume yalikuwa chapachapa na vumbi juu, nikawaamuru warudishe madawati kwenye darasa husika. Walipomaliza, tulitoka nao nje, tukarudi mstarini ambapo kufumba na kufumbua kila mhusika alitwaa nafasi yake. Yaani wale wanafunzi walirudi mstarini pamoja na mimi na wale walimu waliokuwa na kibarua cha kubeba madawati nao walirudi sehemu yao. Mwalimu mkuu alishtuka na kusema: “Haa! Walimu wangu, nini kimewapata muda huu?” Wanafunzi nao walijishika vinywa, hata mimi pia. Tulikuwa tukishangaa wale walimu, walikuwa wamechoka sana. Nilimwona mwalimu mmoja wa kiume akiingiza mkono mfukoni mwake, akatoa kitambaa na kujifuta jasho ambalo lilikuwa likimchuruzika kama yuko kwenye mvua. Hakuna mwalimu hata mmoja aliyesema neno kwa wakati huo kwa kuwa walikuwa wakihema kwa kasi, si unajua kubeba kitu kizito kwa muda mrefu. Mwalimu mmoja akanyoosha mkono juu, mwalimu mkuu akamruhusu azungumze. “Mwalimu, hii hali itatufikisha pabaya sana. Kuna mtu anacheza huu mchezo, najua kule tumelimishwa, hapa hata sijui tumefanywa nini, lakini kama tulibeba kitu kizito kichwani.” “Ina maana walimu nyie wenyewe hamjui mlichobeba, eti walimu?” “Hatujui.” “Mimi nahisi gunia la mahindi,” alisema mmoja, wanafunzi tukacheka sana. Mwalimu mkuu alikuja mbogo kwa sisi kucheka, akauliza kisa cha kucheka, hakuna aliyekuwa na jibu. Lakini kusema ule ukweli wale walimu walichafuka sana. Ilibidi mwalimu mkuu awaruhusu warudi majumbani kubadili nguo kwani walionekana kama vichaa, chukulia walichochafuka shambani halafu na ile shughuli ya kubeba madawati. Baada ya walimu kuondoka, mwalimu mkuu aliongea kama kwa kubembeleza. Alisema kama kuna mchawi kati yetu sisi wanafunzi aache kwani kwa kuendelea nao, walimu watashindwa kufundisha vizuri na matokeo yake wanafunzi hatutafanya vizuri katika masomo yetu. “Na kama huyo mchawi hapatikani katika nyinyi wanafunzi basi mkirudi nyumbani leo mkawaambie wazazi wenu kilichotokea, ni mengi yametokea lakini sitaki kuyasema,” mwalimu mkuu alilalamika sana. Kabla hajaendelea, mimi nilinyoosha mkono juu ili nipewe nafasi ya kusema mawili matatu. Je, unajua nini kilitokea hapo?
 
SEHEMU YA 16


“Na kama huyo mchawi hapatikani katika nyinyi wanafunzi basi mkirudi nyumbani mkawaambie wazazi wenu kilichotokea leo, ni mengi yametokea lakini sitaki kuyasema,” mwalimu mkuu alilalamika sana. Kabla hajaendelea, mimi nilinyoosha mkono juu ili nipewe nafasi ya kusema mawili matatu. SASA ENDELEA … “Wewe unataka kusema kuhusu nini?” “Niongee kidogo mwalimu.” “Kuhusu la uchawi au una lako jingine?” “Hilihili la uchawi.” Nilimwona mwalimi mkuu amenitumbulia macho kama asiyeamini alichokisikia kutoka kwangu. Sababu kubwa ya kutoamini nadhani ni kitendo cha mimi kutaka kuongelea hilo wakati kuna wanafunzi wakubwa zaidi yangu walikuwa kimya. “Enhe, ongea unachotaka kuongea wewe.” Nilimuuliza mwalimu hivi: “Niliwahi kusikia serikali yetu haiamini mambo ya kichawi, uongo kweli?” Mwalimu mkuu akajibu ni kweli kabisa. Nikaendelea kumuuliza: “Je, sasa hayo maagizo unayotupa tukapeleke nyumbani si kuifanya serikali iamini ushirikina maana shule hizi si za serikali?” Mwalimu mkuu akanifokea, akasema nikomee hapohapo, yeye kama mwalimu mkuu hawezi kuiona shule inaangamia kwa sababu ya kuogopa serikali haiamini uchawi. “…ni kweli serikali haiamini uchawi lakini mimi naamini, na mimi ndiye mwalimu mkuu wa shule hii. Hapa shuleni uchawi umezidi sana au wewe unawa…” Sikusubiri amalize kwani nilijua anataka kusema nini, nikamtumbulia macho huku moyoni nikisema maneno yangu ya kichawi, akashikwa na ububu wa muda. Hata kutuamuru tuondoka mstarini alitumia ishara ya mikono, wanafunzi tukatawanyika. Siku hiyo nilipofika nyumbani nilimwambia mama kilichotokea, nikamwambia ushauri wangu ni kuachana na walimu kwani wote wameonesha hawajiwezi. “Kama ni kuwachezea, tumewachezea sana, tumewaumiza sana, tuwaache tu sasa, mimi wamenichosha sana,” nilimwambia mama, akasema sawa lakini akasema anachofurahi ni kwamba, nimewaroga walimu wangu hadi nimechoka mwenyewe, tukacheka na kuendelea na mambo mengine.

MWISHO
 
ishiii xax na we umekaa kbx kwa akil zak timamu ukaamua utuletee hyo xtor yak ya kipuuz kwaiy xax unatufundisha kwmb 2we tunawarog walimu wa2 wengn bhn
 
Back
Top Bottom