Simulizi ya Kijasusi: Hakuna aliye Salama

Simulizi ya Kijasusi: Hakuna aliye Salama

Hakuna Aliye Salama
Mtunzi: Robert Heriel
Chungu cha 07

Usiku uliofuata, Kinu na Moreen walikuwa wamejificha ndani ya nyumba ndogo ya mbao pembezoni mwa milima ya Bagamoyo. Walikuwa wakimsubiri mtu kwa jina la Jaji, aliyewahi kuwa mmoja wa waratibu wa DEKA miaka kumi nyuma, kabla hajajitoa kwa siri.

Mtu huyo alifika saa mbili usiku, akiwa amevaa koti la kuukuu na suruali ya kitambaa. Alikuwa na ndevu ndefu, nywele nyeupe zilizojificha ndani ya kofia.
“Naelewa nini mnachopitia,” alitamka kwa sauti nzito ya kizamani. “Niliwahi kuwa ndani ya jumba hilo. Niliona uovu ukizaliwa na kulelewa kama mtoto wa kifalme.”

Kinu alimsikiliza kwa makini.
“Nawapa jina moja,” Jaji aliongeza. “Jina la mtu aliye ndani ya DEKA, lakini moyo wake haupo nao. Amefungwa kwa hofu ya familia yake kuuawa. Anaitwa Profesa Daudi Luhanga. Alikuwa mtaalamu wa mawasiliano ya serikali. Sasa anafanya kazi kwa kulazimishwa. Anaweza kuwasaidia… lakini mkimpa tumaini na uhakika wa kushinda. Nilisikia habari za wale watu mliowafuata Tabora na Singida walivyouawa. Hii inanambia hata Mimi nipo mbioni'

Wakati huohuo, kwenye jumba la kifahari lililojaa mapazia ya damu za wazalendo, kikao cha siri kilikuwa kinaendelea.

Wahusika sita walikuwa wameketi kwenye meza ya mbao nyeusi. Wawili kati yao walikuwa wazee, mmoja akiwa na miwani yenye kioo cha rangi ya samawati na mwenzake akiwa na fimbo ya ndimu. Watatu walikuwa watu wazima waliovaa suti nyeusi. Na mmoja kijana, mwenye simu tatu na macho ya tahadhari.

Kiongozi wa DEKA, akiwa ameketi katikati, alisoma karatasi ndefu na kusema:
“Kinu na Moreen wamevuka mipaka. Wanapaswa kufunguliwa mashtaka. Kesi ya uhaini, uharamia wa mtandao, uchochezi wa kitaifa, na uhalifu wa kiusalama.”

Akainua mkono, akasema:
“Amri hii ipelekwe kwa Waziri wa Mambo ya Ndani, kwa Mwanasheria Mkuu, na kwa IGP. Hakuna kuchelewa. Wafunguliwe mashtaka mara moja.”

Na kweli…
Kesho yake, taarifa ilitoka kwa njia ya televisheni, redio na mitandao ya kijamii:

“Watu wawili wanaotuhumiwa kwa kupanga uasi dhidi ya taifa, uchochezi na uhalifu wa mtandao wamefunguliwa mashtaka. Wanajulikana kwa majina ya Kinu na Moreen. Serikali imeunda timu maalumu ya kuwakamata na kuwafikisha mahakamani.”

Moreen alikuwa akichota maji kisimani wakati aliposikia sauti ya redio hiyo. Alidondosha ndoo. Kinu alipokea ujumbe wa WhatsApp uliojaa viunga vya video zao wakitoa ushahidi. Sura zao zilitapakaa kila kona.
“Tumebambikiwa,” Kinu alisema, sauti yake ikiwa ya maumivu na hasira.
Usiku huohuo, polisi walivamia nyumba yao. Walifanikiwa kukimbia. Waliishi vichakani, kwenye miji ya watu masikini, wakibadilisha mavazi na mitindo Yao ya Maisha ya kila siku. Lakini DEKA na Polisi haikuacha kuwatafuta.

Kwa muda huo, harakati zilitulia. Watu waliokuwa wakisambaza ujumbe wa haki walinyamaza. Watumiaji wa mitandao walijificha Kwa kuogopa. Hofu ilimvaa Kila mtu.

Lakini Morris, jasusi wa zamani na Marcus, mwanaharakati kutoka Geneva, waliungana kwa simu ya siri na kumuandikia barua ya kuaminika Kiongozi wa Mabadiliko, aliyekuwa mafichoni Dodoma.

Barua yao ilikuwa na ujumbe mmoja:

“Siku ya Wanawake Duniani, tunaomba ruhusa ya maandamano ya kutetea Haki. Tutavaa vazi jeusi kama kiashiria Cha maombolezo Kwa waliokuwa, kupotezwa na kwaajili ya Kinu na Moreen. Hatutasema neno. Lakini miguu yetu itasema yote.”

Na kweli, tarehe hiyo ilipofika, maelfu ya wanawake walijitokeza barabarani wakiwa wamevaa nguo nyeusi na kubeba mabango ya upendo, amani, na uhuru. Hakuna aliyesema neno. Walitembea.

Lakini Polisi walikuja na mabomu ya machozi. Walikamata baadhi yao. Waliwatia watu hofu. Lakini picha za maandamano hayo zilisambaa ulimwenguni. Vyombo vya kimataifa viliripoti:
“Nchi inayoogopa wanawake wasiozungumza, ni nchi iliyokufa moyo.”

Maisha ya Mahabusu
Kinu alikamatwa kwenye stendi ya basi la mikoani alipokuwa akijaribu kutoroka kwenda Iringa. Alifungwa pingu kama jambazi hatari akiwa chini ya Ulinzi Mkali. Alipigwa. Akaingizwa ndani ya gari la polisi. Moreen alikamatwa baadaye, akiwa kwenye nyumba ya mwanamke mmoja aliyekuwa akimhifadhi.

Walipelekwa jela ya Keko. Vyumba vyao vilikuwa vya giza, na sakafu ya saruji iliyokuwa baridi kama moyo wa amphibia.
Kinu alipangiwa kazi ya kusafisha choo cha gereza. Moreen alipewa kazi ya kufua nguo za askari.

Kila walipopewa karatasi hata kama ni kipande cha gazeti waliandika ndani yake ujumbe:
“Usikubali kupotea. Ukipotea, dunia haina tumaini. Yashikilie Maisha Kwa nguvu zote. Tumaini la Taifa ni letu"

Walijua gereza halikuwa mwisho wa mapambano Yao. Isipokuwa ni hatua Moja inayosubiriwa na hatua nyingi zinazofuata.
*******

Mahabusu kulijaa mbu na kiza kilichojaa mipango mibaya kama mawingu ya radi yanavyolikaribia jangwa. Ndani ya gereza hilo lenye kuta nene za huzuni, mwanga wa bulb moja dhaifu uligawanya giza kwenye seli ya Kinu, ukilenga moja kwa moja kwenye uso wake uliokonda kwa mawazo.

Kinu alikuwa amelala kifudi fudi juu ya godoro lililofifia, lakini usingizi ulikuwa mgeni mwenye adabu mbaya ulikuja na kuondoka kabla hajamkaribisha.

Mlango wa chuma ulilia kama mtu anayeomboleza. Walinzi wawili waliingia. Mmoja alichukua ndoo, mwingine alimtazama kwa jicho la nyoka mwenye sumu.
“Kuna amri, umetumwa kusafisha korido ya ghorofa ya chini,” mmoja alisema.
Kinu hakusema neno. Alijua. Mara moja alijua. Ghorofa ya chini? Usiku wa saa saba? Hakuna choo kule, wala wafungwa.

Alivaa viatu vyake vya plastiki na kuchukua ndoo na beseni. Alitembea kimya kama kivuli na kibwengo. Wakampeleka kwenye korido ya mwisho, yenye taa iliyokuwa inatikisa kama mshumaa kwenye upepo wa ufukweni.
Alipofika, mlango wa nyuma ulifungwa kwa kishindo. Kabla hajageuka, kivuli kilimtokea nyuma. Mwanaume mrefu, mwenye sura iliyofichwa na barakoa nyeusi alimsogelea taratibu, akachomoa kitu kilichometameta kwenye mwanga hafifu.

“Kifo chako kimepitishwa,” sauti ya kiume ilisema kwa ukatili wa msumeno.

Lakini Kinu hakuwa mtoto wa jana. Aliruka ghafla, akamgonga adui kwa beseni kichwani. Kelele ya chuma na maumivu ilijaza korido hiyo. Wakati mwingine, uhai huja kwa sekunde chache za ujasiri usiopimika.

Kinu alikimbia akapita kwenye njia nyembamba, akateleza kwenye mapovu ya sabuni ya chooni, akaanguka. Lakini kabla hajainuka, Mwanaume mwingine alikuwa tayari nyuma yake.
Walimzingira. Wanne. Mikono yao ilikuwa na nyundo, kamba, na baruti ndogo ya umeme wa ganzi.

Walimshika, wakamvuta kwenye chumba kidogo, chumba kisichotumiwa, kilichojaa fangasi ukutani na harufu ya uozo. Wakamfunga kamba mikononi, wakampiga mfululizo tumboni, mgongoni, na kichwani.

Lakini wakati mmoja alipoinama kumpiga tena, Kinu alitumia kichwa chake kumpiga pua Mwanaume aliyembele yake. Damu ikamwagika. Alijirusha kwa nguvu, akakata kamba upande mmoja, akampiga mwingine teke la mbavu. Sasa ilikuwa vita ya kujitetea.

Ulikuwa ni vita ya mtu anayepigania haki, hata akiwa kifungoni. Walipopata nafasi ya kumpiga na bastola ya ganzi mlio wa filimbi ukasikika kutoka nje. Mlango wa nje ukafunguliwa kwa nguvu.
“kuna Nini hapa!” sauti ya askari wa kawaida ilisikika.

Watu waliokuwa wamemzunguka Kinu walitawanyika kama panya waliomwagiwa maji ya moto. Askari waliingia, wakamkuta Kinu akiwa amejaa damu usoni, jicho moja likiwa limevimba.

Hakusema kitu. Hakuwalaumu. Hakulia. Aliinua kichwa chake, akatazama juu kama mtu aliyemaliza maombi ya mwisho.
“Wataniua,” alisema kimoyomoyo. “Lakini si kabla sijasema ukweli.”

Usiku huo, upande wa wanawake
Moreen alipata ujumbe wa karatasi ulioingizwa kupitia chini ya mlango. Ulikuwa umeandikwa kwa kalamu ya wino mweusi:

“Kinu amejaribiwa kuuawa. Anaishi, baada ya kukabiliana vilivyo. Hiyo haimaanishi hawatarudi. Watajariby wawezavyo. DEKA imeingia gerezani. Hata ukuta hauna masikio tena sasa una macho.”
Aliweka karatasi hiyo kwenye shimo dogo alilolifukia kwa kijiti nyuma ya ndoo ya maji. Alilia kimya, machozi yakimulika historia ya upendo, ujasiri, na mateso. Alikumbuka tangu siku ya kwanza alipokutana na Kinu. Kutoka kuwa Mwanamke mpaka Make-up mpaka kuwa mwanaharakati mwenye kuahughulikia mambo ya hatari na magumu.

Alijua. Walikuwa wanawamaliza mmoja baada ya mwingine. Lakini pia alijua mtu hufa mara moja tu. Lakini sauti ya haki haiwezi kuzikwa na udongo wa gereza.
*****"""

Morris alikuwa ameketi ndani ya chumba kidogo cha kioo jijini Geneva, Uswisi, mbele ya kamati ya kimataifa ya haki za binadamu. Alikuwa amevaa suti ya buluu, tai isiyo na alama, lakini macho yake yalikuwa na uzito wa kilio cha mataifa yenye ukandamizaji wa haki za binadamu.

“Mimi ndiye shahidi wa kwanza wa mateso haya. Wako gerezani si kwa uhalifu, bali kwa kusema ukweli,” alisema kwa Kiswahili kizito kilichotafsiriwa papo hapo kupitia headphones za wajumbe kumi na wawili waliomkodolea macho.

Marcus alikuwa nyuma yake, akigawa nakala za picha, nyaraka, na rekodi za sauti za mateso na ukiukwaji wa haki. Ilikuwa ni mwanzo wa presha kubwa ya kidiplomasia, ripoti zilianza kusambazwa, barua zikaandikwa kwa wakuu wa mashirika ya haki duniani, na redio za kimataifa zikaanza kuuliza maswali kuhusu hatma ya Kinu na haki za waliopotezwa na kuuawa.

Lakini wakati dunia inaanza kusikia kilio cha gerezani, ndani ya kuta za gereza la wanawake, kisasi kilikuwa kinachanua kama sumu kwenye mti wa miiba.

Moreen alipata chai ya jioni, kama kawaida. Lakini ladha ya siku hiyo ilikuwa tofauti ilikuwa na utamu wa bandia na harufu ya unga wa viwandani. Dakika thelathini baadaye, alianza kutapika, macho yakawa mekundu, na ngozi yake ikaanza kutoa jasho la baridi.

Wafungwa wenzake walipiga kelele akapelekwa hospitali ya gereza kwa haraka. Daktari mmoja alipokuwa akimpa huduma ya dharura, alimnong’oneza,
“Hii ilikuwa sumu ya polepole, lakini unabahati kwani una allergy na kahawa. Wala usingejua umewekea Sumu. Ungekufa polepole ndani ya siku hizi thelasini.”

Wakati huo, katika kona ya giza ya jiji la Dar es Salaam, Mama Lutu alikuwa kwenye gari la abiria, akivua mavazi ya kawaida na kuvaa vazi la kininja. Alikuwa anatoroka,, tena baada ya mapambano ya hatari na Andrew Kamage kwenye ranchi ya ng’ombe.

Siku moja nyuma, Andrew alikuwa amemuita Mama Lutu ofisini mwake baada ya kugundua nyendo zake kupitia mfumo mpya wa ufuatiliaji alioujenga kwa siri. Walipokutana, kulikuwa na mazungumzo mafupi ya kistaarabu, kisha Andrew akafunga mlango kwa rimoti.

“Umechagua upande wa giza, upande wa udhalimu,” Andrew alisema.

“Na wewe umebaki kwenye ndoto za mabadiliko yasiyoishi, ndoto za alinacha ambazo haziwezi kutokea" Mama Lutu akajibu.

Kisha mapambano yakaanza, meza ziligonga ukuta, vioo vilipasuka, risasi zikaelekezwa kwenye dari. Mama Lutu alikuwa na kisu kidogo cha mfukoni; Andrew alikuwa na bastola ya risasi za ganzi.

Kwa zaidi ya dakika thelathini, walizunguka kila kona ya ranchi hiyo, wakipigana kama Simba wawili waliowekewa uzio mmoja. Hatimaye, Mama Lutu alifanikiwa kumchoma Andrew kisu begani na kukimbilia msituni kupitia sehemu ya nyuma ya shamba, lakini bila kujua Andrew alikuwa amepata mkoba wake wa siri uliokuwa na documents nyeti, majina ya mawasiliano ya DEKA, ratiba zao na ramani ya mikutano ya ndani ya mfumo.

Andrew, akiwa na jeraha, alishika mkoba huo kwa mikono yenye damu na kusema taratibu,
“Umenitoroka lakini umeniachia ushahidi WA Siri"

Usiku huo, Andrew alituma baadhi ya nyaraka kwa Marcus na Morris kwa njia salama ya kimtandao. Ulimwengu ukawa na ushahidi wa kwanza wa kielektroniki wa uwepo wa DEKA.

Moreen, akiwa katika kitanda cha chumba cha uangalizi maalum, alipokea ujumbe wa maandishi kutoka kwa Marcus:
“Hujafa. Na sasa dunia inajua. Anza kupona. Vita inaanza.”
Kinu naye, gerezani, alipokea barua ya mkono, yenye maneno machache sana lakini yaliyokuwa na uzito kama ardhi:

“Tunakutoa nje. Uhai wako ni ujumbe wa dunia.”
*******

Mlango wa gereza kuu la Keko ulisikika ukilia kwa sauti ya ajabu majira ya usiku, sio mlio wa funguo, mashine maalumu ndizo zilizokuwa zinatumika. Kamera za uangalizi zilikuwa zimesimama zilikuwa zimedhibitiwa na kifaa kidogo cha kielektroniki kilichokuwa kimetundikwa kwenye dari la maktaba ya gereza.

Ndani ya seli, Kinu alikuwa amejilaza kama mfu aliyeishiwa matumaini. Lakini ndani yake kulikuwa na msisimko wa vita, vita ya mabadiliko. Alijua: usiku huo haukuwa wa kawaida.

Mlango wa chuma ulifunguliwa kwa sauti ya kuunguruma kama ya simba aliyejeruhiwa. Mtu aliyevaa sare ya mlinzi wa gereza, lakini mwenye mwendo wa jasusi, aliingia. Alitoa ishara, ishara ya wanajeshi wa zamani waliokuwa katika kikosi cha vipuli vya vifaru.

“Twende,” aliongea kwa sauti ya chini, macho yakiwa hayatembei kwenye uso wa Kinu, bali kwenye kuta na kona za chumba.

Safari ya kutoka ikaanza kupitia njia za chini ya ardhi katika mtaro wa maji taka uliosahaulika kwenye ramani ya matumizi. Harufu ya kutapika na mchanganyiko wa kinyesi na historia ya unyanyasaji ya wafungwa wa kisiasa, ilijaza mapafu yao.

Baada ya dakika thelathini, walifika kwenye mlango mdogo wa chuma uliokuwa umefichwa chini ya paa la karakana ya magari ya magereza. Mlango ulifunguliwa kwa alama ya kidole.
Gari aina ya Land Cruiser lilikuwa likisubiri nje. Kinu aliingizwa ndani, kofia ya sura bandia akavalishwa. Gari lilitokomea gizani.

********
Asubuhi ilipochomoza, taarifa zilianza kutiririka kama mto wa habari uliotokana na mvua zilizonyesha usiku mzima.

“Mfungwa wa kisiasa atoroka Gereza la Keko kwa njia isiyojulikana.”
“Wizara ya Mambo ya Ndani yatoa tamko la kuunda tume ya uchunguzi.”

Lakini kilichoanza kama uchunguzi wa kawaida kiligeuka kuwa karaha ya ndani ya mfumo wa usalama. Kaimu Mkurugenzi wa Usalama wa Taifa, Benedicto Mlauzi, alipokea ripoti ya siri iliyokuwa na jina moja lisilosomeka kwa watu wa kawaida, DEKA-6.

“Ni nini hiki?” aliuliza.
Afisa wa kitengo cha uchunguzi alitoa faili lenye majina, ramani, na mawasiliano ya kikundi cha ndani kilichojipenyeza kwenye taasisi za dola.

Benedicto alijua DEKA haikuwa hadithi ya mtaani. Ilikuwa kichaka kilichojengewa kasri ndani ya moyo wa taifa... Ndani ya mihimili inayoshililia nchi.

Lakini hakukubaliana na uozo huo. Akaitisha kikao cha siri. Wajumbe wanne waliingia. Wengine wawili walikuja kwa kuchelewa. Waliketi kimya, kila mmoja akiwa na ajenda tofauti mioyoni mwao.

“Nina uhakika kuna watu humu wanafanya kazi na DEKA,” Benedicto alisema. “Lakini hiyo haijalishi. Tumeanza vita sio kwa mabomu, bali ya ukweli. Kupambana kulinda Taifa, wote tunakumbuka tuliapa. Sasa kama sisi walinzi wa taifa hili ndio tumegeuka Mbwa mwitu wa kulirarua Taifa hili. Unafikiri Nini hatma ya kizazi chetu"
Wengine walinyamaza. Mmoja alitabasamu, akajifuta jasho. Mwingine alitoa simu na kuandika kitu kwa haraka.
********

Katika kona ya Chuo cha Sayansi ya Habari, Profesa Daudi Luhanga alikuwa amekuwa kivuli chake. Mwanaume aliyejulikana kwa nadharia za uhuru wa mawasiliano, sasa alikuwa chini ya uangalizi wa DEKA, akilazimishwa kutumia akili yake kulinda uongo, Ufisadi, dhulma na mauaji kinyume na sheria na haki za binadamu.

Lakini alipopewa ujumbe wa mkono kutoka kwa Benedicto, moyo wake ulianza kuamka.

“Tunajua bado una nafsi,” uliandika ujumbe huo. “Tuonyeshe mlango wa ndani.”

Profesa Luhanga alijibu kwa kipande cha ramani na nukuu ya maneno:
“Mamlaka inayojificha ni mamlaka ya giza. Nuru huwa haina makazi ya kudumu, lakini huja kila inapohitajika.”

Usiku huo, kikao kilifanyika ndani ya nyumba ya kale yenye paa la bati lenye kutu na ukuta wa chokaa. Kinu, akiwa na kovu jipya usoni, Moreen aliyeponea kifo, Marcus, Morris, na Benedicto walikaa pamoja.

Profesa Luhanga alisimama.

“Acheni niwaonyeshe mtandao uliopo ndani ya mifupa ya taifa. Wako serikalini. Wako mahakamani. Wako ndani ya chombo cha habari. Na wako pia… hapa.”

Kimya kilitanda. Kila mtu alimkodolea macho, akiwa na swali moja kichwani:

"Je, tutavunjaje mfumo unaojua jinsi ya kuishi hata ndani ya damu yetu wenyewe? Mfumo unaotutazama na kutufuata kama kivuli Kila tuendako?"
*******

Hakuna kilicho bora duniani kama muungano wa watu wanaotoka pande tofauti, lakini wakakutana kwenye lengo moja. lengo la ukombozi. Hicho ndicho kilichotokea kati ya Benedicto Mlauzi, Kinu, na Moreen. Kila mmoja alikuwa na majeraha yake, historia yake, na maumivu yake, lakini wote walikuwa na ndoto moja: kuvunja minyororo ya DEKA, kulikomboa taifa liwe mikononi mwa wananchi wote. Na sio kikundi Cha watu wachache wanaotumia siasa na Dola kujinufaisha wenyewe huku wakiacha mamilioni ya wananchi wakiumia na kutesaka katika Lindi la umaskini.

Mpango wa kuwatoa Kinu na Moreen kutoka mikononi mwa DEKA ulianza kimyakimya baada ya Benedicto kupata taarifa ya ndani kutoka kwa Afisa mmoja wa gereza aliyekuwa amekuwa na mashaka kwa muda kuhusu mizengwe ya ndani ya mfumo. Afisa huyo, kwa jina la Aaron, alikuwa na kumbukumbu za mateso aliyoyaona gerezani, lakini alikuwa akinyamaza kwa kuhofia maisha yake.

Lakini ilipofika siku ya jaribio la kumuua Kinu, Aaron alituma ujumbe wa siri kwa Benedicto kupitia laini ya kielektroniki ya ndani ya usalama:
“Huyu mtu ni zaidi ya mfungwa. Ana ujumbe mkubwa. Tafuta njia ya kumtoa.”

Benedicto aliunda kikosi kidogo kisicho rasmi, akitumia vijana wa kitengo cha usalama wa data, walinzi waaminifu wachache na mtaalamu wa kielektroniki, kijana mwenye ujuzi mkubwa anayeitwa Titus. Kupitia njia ya chini ya ardhi, walimtoa Kinu na baadaye Moreen, na kuwapeleka kwenye eneo la siri la kupumzika, lililojengwa chini ya jengo la zamani la ukaguzi wa barabara lililoachwa miaka mingi nyuma, maeneo ya Upanga Magharibi.

Walikutana usiku mmoja wa jumatano, kwenye chumba kilichojaa ramani, vishikwambi, na taarifa nyingi za siri. Benedicto alitembea polepole, macho yake yakikazia kila picha ya uso wa DEKA iliyowekwa ukutani.

“Hamko peke yenu tena,” alisema kwa sauti iliyojaa ukomavu wa vita ya kiakili. “Tumeanzisha vita ya ndani ya mfumo. Na ninyi mko mstari wa mbele.”

Moreen aliketi kando ya Kinu. Alikuwa bado anapona taratibu baada ya sumu aliyopewa gerezani. Kinu alimtazama Benedicto, macho yake yakiwa na mchanganyiko wa shaka na matumaini.

“Je, tunaweza kuwaamini? Mfumo huu umewatupa wengi wetu,” Kinu alisema.

“Ndio maana nataka tufumue mfumo huo kutoka ndani,” Benedicto alijibu. “Na tunaanza na mtu ambaye anawajua wote.”

Mama Lutu

Wakati huo, Mama Lutu alikuwa amejificha katika nyumba ya kulala wageni eneo la Kunduchi, akitumia jina la bandia: Mariam Saidi. Hakujua kama taarifa zake tayari ziko mikononi mwa Andrew Kamage, wala hakujua kuwa kamera moja ya ndani ya hoteli ilimnasa akiwasiliana na mtu asiyejulikana usiku wa manane.

Aliendelea kutuma ujumbe kwa DEKA, akijifanya bado yuko ndani ya mpango wa Benedicto. Lakini moyo wake haukuwa na amani. Alihisi kama anayesogelea mdomo wa simba akiwa na ngozi ya nyati.

“Ulinzi wa ndani umevurugika,” aliandika kwa simu ya kisiri. “Lakini naendelea na kazi.”

Moreen alikuwa tayari amepata dondoo kutoka kwa Titus, mtaalamu wa data, kuwa simu moja inayohusishwa na Mama Lutu ilikuwa ikituma ishara kwenye mlingano mmoja na minara inayotumika na DEKA.

Kinu akasema, “Tunamjua. Ila tusimwambie. Tusiwanyime maadui nafasi ya kuamini wameshinda. Kufanya haraka sana kunaweza kusababisha makosa ya kimedani. Pia inaweza wapa DEKA nafasi ya kuwa na hofu jambo ambalo litawafanya watumie nguvu zaidi. Hii inaweza kuvuruga na kuumiza wasiohusika walionje ya mpango"

Profesa Luhanga alifika kwenye kikao kilichofanyika siku hiyo usiku. Alikuwa amevaa shati la mikono mirefu, suruali ya kaki, na sura ya uchovu ilionekana dhahiri. Aliweka kwenye meza ramani mpya ya mtandao wa DEKA, alama za mawasiliano, na namba za akaunti zinazotumiwa kufadhili mashambulizi ya kisiasa na mauaji ya siri.

“Kama tukiwa wakweli, tupo kwenye bomu la taifa ambalo linaweza kulipuka na kuangamiza nchi yetu. Tunapaswa tuwe waangalifu,” alisema. “Wengi walioko kwenye mfumo ni watu wakiwa wenye nguvu, lakini hawawezi kuzuia tunachokifanya. Kazi yetu ni kuwazindua.”

Benedicto akainuka. “Tutahitaji zaidi ya ushahidi, tunahitaji ushawishi, tunahitaji ushiriki wa wananchi. Propaganda za mitandaoni, vibonzo, memes ziendelee,” alisema. “Na hilo tutalipata kupitia nguvu ya watu. Tuanze sasa.”…
*******.
Mipango ya Siri hufanyika katika giza Nene. Usiku wa Manane. Mipango ya mafanikio hupangwa Kwa Siri. Gizani, usiku wakati watu wa kawaida wakiwa wamelala.
Ndivyo ilivyo Kwa kazi za kijasusi. Yadaiwa usiku hasa katikati ya usiku na asubuhi ndio muda ambao ufunuo wa roho hushuka katika ulimwengu wa watu. Hivyo ndivyo ilivyokuwa.

Usiku ulijificha kwenye vichochoro vya jiji kama mtu aliyejeruhiwa anayejificha asipate kudhihirika. Dar es Salaam ilikuwa imevaa vazi la hofu, anga lake limetandikwa na wingu la kiza Cha tahadhari. Hakuna aliyekuwa salama, wala hakuna aliyethubutu kunyanyua mdomo. Wakati haukuwa umefika lakini haukuwa mbali.

Ndani ya pango la chuma lililojengwa chini ya ardhi, lililojificha chini ya kiwanda cha reli ya zamani ya Tanganyika, walikuwepo watu wachache waliokaa kimya. Miale ya chemli moja ya betri ilichora taswira za nyuso zao ukutani kama sanamu za mashujaa waliolala. Mashujaa wa kweli waliopigania uhuru. Uhuru ambao sasa ulikuwa umeporwa.

Benedicto Mlauzi alisimama mbele ya ramani kubwa ya taifa, iliyokuwa mbele kwenye ukuta, kwenye skrini ya kioo, akitazama kwa makini kama mchora ramani na mtaalamu wa GIS. Mikono yake miwili iliambatana na vishikwambi vitatu, kila kimoja kikionesha picha tofauti: maandiko ya upinzani, video ya askari akimnyanyasa kijana wa mtaani, na ramani ya njia za chini za mji.

“Wameifunga nchi kwa minyororo ya hofu, hawataki watu waseme maovu yao. Na Kila atakayesema humwinukia na kumuangamiza” alisema kwa sauti ya kuumauma midomo “lakini sisi tutatumia haki na kweli. Watatufunga miguu lakini si ndimi zetu. Wataua miwili yetu lakini sio dhamira na nia zetu"

Mioyo ya vijana wale ilijaa mshindo wa mapambano Maneno ya Benedicto yaliamaha hisia na shauku ya ukombozi. Kinu alikuwa ameketi upande wa kushoto wa chumba, macho yake makini, uso wake ukiwa umejaa makovu, makovu ya mateso gerezani, makovu ya usaliti, na Moreen alikuwa kando yake, sura yake ikiwa imetulia, lakini ndani ya nafsi yake kulikuwa na radi isiyosikika.

Benedicto aliinua kidole na kugusa picha ya msanii maarufu, Jay Razz, msanii wa muziki wa mitaani mwenye sauti ya utetezi wa watu wanyonge.

“Tutaanza na sauti. Tutamwomba aimbe nyimbo ya waliopotezwa. Tutampa majina na picha zao. Atazungumza kwa lugha ya mtaa, lugha ya watu wa kawaida.”

Halafu akawageukia Kinu na Moreen. “Mitandao ya kijamii ni jukwaa letu. Tumieni influencers. Wapewe hadithi za kweli. Wapewe takwimu. Wapewe nyuso za watu waliopotea. Na mjue, kila mfuasi mmoja ni risasi yetu ambayo itatufaa katika vita hii”

Moreen alikumbuka wimbo wa Jay Razz uliokuwa ukisambaa kama moto wa volcano, Sauti ya Mtaa. Ulikuwa na maneno kama sumu inayopenya mishipa ya ubongo
“Kama sauti yetu ni kosa, basi nchi hii imekosea… Kama kukosoa ni uhaini, basi uhuru huu ni mtego...”

Kwa mbali, kelele za mitaani zilianza kusikika, si za magari wala honi, bali za nyimbo na mikono ya waandamanaji waliovaa fulana nyeupe zenye maandishi makubwa: “Nimechoka Kuishi Kwa Hofu”.

Benedicto hakuishia hapo. Alitamka neno moja lililowafanya waliokuwepo wote kutikisa vichwa: “Tutawateka.”
“Tutamchukua kiongozi wa chama cha madereva. Tutamchukua yeye na familia yake. Tutamtuma ujumbe, si wa bastola, bali wa uhai. Tukishamtisha hatakuwa na chaguo. Ataitisha mgomo na wakati huohuo, chama cha upinzani kitapaza sauti mitaani.
Huu ndio ulikuwa mpango. Wakuitisha vuguvugu la maandamano na mgomo mkubwa wa kudai haki lakini zaidi kuipa serikali na kundi la DEKA wakati mgumu kuwafuatilia Kinu, Moreen, Andrew na Benedicto.

Siku ya Mgomo,
Siku hiyo ilifika kwa upesi. Saa moja asubuhi, magari ya abiria, mabasi, daladala, na boda boda vilisimama katikati ya jiji kana kwamba vilikuwa sanamu za Shaba

Kufumba na kufumbua, mabango yalijitokeza. Watu walivaa kofia nyeupe, wengine walivaa nguo za matambara zenye picha za waliopotea. Waliimba:
“Tutembee na sauti zetu, tupaze sauti zetu kudai haki zetu. Haki za ndugu zetu. ” “Mama yangu alilia, si kwa kuwa mimi muhalifu, bali kwa kuwa nilisema ukweli.”

Katika vurugu hizo, Serikali ilimkamata Ludovick Mchopa, kiongozi wa madereva. Lakini mgomo haukusimama. Kwa sababu tishio halikuwa tena kwa kiongozi, bali kwa moyo wa familia.
Viongozi wa madereva familia zao zilikuwa zimetishiwa kudhuriwa na kundi la Benedicto.
Abiria na wananchi walianza kulalamika na uvumilivu ulipoteza nafasi katika mioyo Yao.

Siku hiyohiyo, tangazo lilitolewa kutoka Ikulu: Benedicto Mlauzi atenguliwa na kuhamishiwa kama balozi nchini Guinea Bissau.

Lakini alikuwa tayari ameotesha mbegu ya mapinduzi. Alikuwa amewaachia kina Kinu ramani ya mioyo ya wananchi waliokuwa tayari kuamka. Na sasa alikuwa kivuli kinachotembea ndani ya maboresho ya historia ya nchi.
**********

Katika Ranchi ya Andrew Kamage, mwanga mmoja mdogo wa taa ya mafuta ulizunguka korido ya nyumba ya mbao, ukitengeneza kivuli cha mzee huyo aliyevaa miwani.

Andrew alifungua jalada lililoandikwa “Mama Lutu.” Ndani yake kulikuwa na ramani ya kila eneo alilowahi kuingia Mama Lutu, mawasiliano yake ya siri, na barua moja ya mkono isiyo na jina, yenye maneno:
“Yuko ndani lakini si wetu.”
“Tunamfuatilia,” Andrew alijisemea. “Lakini mwisho wake unakuja.”
*******
Kwa mbali, ndani ya chumba kimoja kilichojaa harufu ya chakula kilichoharibika. Mama Lutu alikuwa akizungumza na mtu kupitia redio ya kisasa ya digitali.

“Ndiyo. Benedicto ametoweka. Kinu na Moreen bado mafichoni. Lakini ramani yao ninayo.”
Akatabasamu. Tabasamu la mtu aliyeshinda kwa siri, lakini pia aliyejua anacheza na moto wa mionzi.

Mama Lutu alitazama skrini ya simu yake iliyokuwa inaonyesha ramani na kiduara chekundu kilichokuwa kinamwekua mwekua. Ilikuwa inaonyesha mahali walipokuwa Kinu na Moreen, mafichoni.
Mama Lutu alitabasamu huku kumbukumbu zake zikionyesha jinsi alivyoiweka chip ya GPS kwenye Saa ya mkononi ya Moreen.
Hiyo ndiyo ilikuwa inampa kujiamini kuwa Bado alikuwa na nafasi ndani ya DEKA.

Itaendelea
 
Hakuna Aliye Salama
Mtunzi: Robert Heriel

Chungu cha 07

Usiku wa kwanza wa Benedicto Mlauzi katika jumba la kifahari la balozi lililopo Guinea Bissau ulikuwa kimya mno. Kimya chenye sauti ya miali ya moto wa ndani. Aliangalia dirisha kubwa linalotazama bahari, macho yake yakichora ramani ya kile alichokiacha nyuma. Moyo wake haukuwa umeganda, bali ulikuwa ukipika ndoto mpya ndoto ya kuona nchi mpya katika ardhi ileile aliyozaliwa.

“Wanaanza…” alijisemea, akiiangalia barua ya karibisho kutoka kwa Rais wa nchi hiyo. Lakini hakuwa na muda wa kustarehe, aliendelea kuandika barua za mkono zenye majina, namba, na maelekezo akiwatumia wale aliowaamini katika vita hii. Hata hivyo alijua fika kuwa nyendo zake zilikuwa zikifuatiliwa usiku na mchana. Umakini haukuuacha pembeni.
----------

Wakati huo huo, ndani ya giza la korido za mifereji ya zamani chini ya jiji la Dar, Kinu na Moreen walikuwa katika maficho mapya, sehemu ambayo hata ramani za Serikali hazikuonesha tena. Yalikuwa maeneo ambayo yalisahauliwa na kupuuzwa. Kulikuwa na unyevunyevu kwenye kuta, na sauti ya maji yaliyodondoka kwenye vyuma vyenye kutu na fangasi ilisikika kama mapigo ya moyo wa mji unaoumia Kwa maumivu yasiyosikia ganzi.

Walikuwa wamehama kutoka maficho ya Benedicto siku tatu kabla ya Mama Lutu kutoa taarifa. Saa ileile ambayo chip ya GPS kwenye saa ya Moreen ilianza kuonesha mwelekeo tofauti, chip hiyo waliitoa na kuiweka kwenye paka la mtaani kisha wakamuachia paka huyo aendelee kuzurura. chip hiyo iliyokuwa imewekwa kwenye paka wa barabarani ilianza kutoa location ya uongo. Kila hatua ya DEKA ilikuwa imechezwa Kwa akili ya kishindo. DEKA walikuwa nyuma kimbinu bila ya wao kujua.

Mama Lutu, akiwa kwenye kituo cha mawasiliano ya kisasa kilicho katika nyumba ya siri maeneo ya Kurasini, alituma sauti ya dharura:

“Na repeat, location confirmed. Maficho ya Kinu na Moreen yapo barabara ya Shimo la Udongo, nyuma ya ghala la zamani. Waraka wa uthibitisho uko hapa.”
Muda huo huo, magari ya usalama yalianza kujaa eneo hilo. Wanaume waliovaa kiraia, wengine na silaha nzito, walizunguka kila pembe. Helikopta ya usalama iliruka juu, ikiangaza taa kali kana kwamba ilitafuta roho iliyojificha ardhini.

Lakini ghala hilo lilikuwa tupu. Lilikuwa limeachwa kwa makusudi, na kila dalili ya uwepo wa binadamu ilikuwa ya kupangwa. Mifuko ya kahawa, vyombo vya plastiki na hata nguo chafu zilizoonesha kutumika zilikuwa sehemu ya mtego wa kisaikolojia. Waliokuwa mafichoni walishaondoka kitambo. Lakini waliondoka kimwili wakiwa wameacha macho ya kiteknolojia katika jengo hilo.
--------------

Maandamano yaliendelea. Kama sauti ya bahari inayopiga mawe ya ukingo wa nchi, watu waliendelea kupaza sauti.

“Tunataka haki. Tunataka ndugu zetu waliopotea. Tunataka serikali isiyoua!”
Bango moja lilikuwa limechorwa kwa damu ya kondoo “Ukimya wetu haukuwa ridhaa.”
Jingine " sisi tunautu. Sisi sio panya"

Wasanii wachache waliovaa majina ya mapambano, akiwemo Jay Razz, walipanda majukwaani na kuimba nyimbo zilizogeuka silaha. Kila mstari ulikuwa mshale, kila mdundo ulikuwa mlio wa risasi wenye moto uliounguza masikio na moyo ya watawala dhalimu na DEKA.

Polisi walipambana nao vilivyo. Lakini sauti ya watu haikupungua. Maandamano yakaenea Mbeya, Mwanza, Arusha na Tanga. Mabango yale yale, sauti zile zile. “DEKA waondoke. Tunataka Nchi yetu.”
------------

Ndani ya chumba cha udhibiti wa DEKA, mmoja wa wakuu alisema kwa hasira:
“Tuna mbwa wapo kila kona, lakini harufu ya hawa wawili hatuihisi. Mnahakika Mbwa hawa wanamafunzo ya kutosha"

Kiongozi wa DEKA alijibu kwa sauti nzito, ya kupasua ukuta wa giza:
“Basi tumia mbwa wa ndani.”
Mama Lutu alitabasamu kwa mbali. “Tayari nimeshavuta pazia. Litawafunua popote walipo"

Lakini hakujua kuwa pazia alilovuta, lilikuwa limefungwa kwa misumari ya dhamira. Na upande wa pili, Andrew Kamage alishika jalada la siri, lililoandikwa jina moja: “Rosemary Lutulia” — Mama Lutu.
__________________

Andrew Kamage alikuwa ameketi pekee ndani ya jumba lake la mbao lililojengwa pembezoni mwa ranchi, usiku ukimfunika kama vazi la kifalme. Dirisha kubwa la vioo lilikuwa wazi, upepo wa usiku ukipuliza pazia taratibu, mithili ya pumzi ya mnyama mkubwa aliyelala porini. Mbele yake, mezani, kulikuwa na faili moja tu, limefunguliwa, kurasa zake zikiwa zimebandikwa picha, picha ya mwanamke aliyeficha siri nyingi sana. Rosemary Lutulia.

Kwa jina lake la sasa anaitwa Mama Lutu, lakini asili yake ilianzia Dodoma, alikosomea saikolojia na baadaye kuingia katika mashirika ya haki za wanawake na watoto. Alipata umaarufu wa kitaifa kabla hajafunikwa na shuka la uovu, akawa mjumbe wa kamati za ndani, mshauri wa maadili, kisha mpelelezi asiye rasmi. Lakini miaka minane iliyopita, alipotea ghafla katika anga la harakati, akarudi akiwa Mama Lutu, mwanamke mwenye ushawishi.

Faili hilo lilikuwa la siri kubwa. Na ndani yake, lilikuwa na jina jingine la ajabu… Edwin Ndugai Mnyika, jina la mtu ambaye kwa miaka mingi amekuwa kivuli kinachotawala nyuma ya DEKA.

Mnyika alikuwa mwanasheria, kiongozi wa zamani wa kijeshi aliyefukuzwa jeshini kwa kuongoza mapinduzi ya kiitikadi dhidi ya utawala wa wakati huo. Alijificha kwa miaka kadhaa, akihamia Ulaya Mashariki, akapata mafunzo ya kijasusi, na alirejea miaka ya 90 na kuasisi kundi la siri la ulinzi wa taifa dhidi ya ‘wahalifu wa ndani.’ Lakini lengo hilo lilibadilika. DEKA ikageuka kuwa genge la watekaji, wauaji na wafujaji wa mali za umma. Na sasa Mnyika, ndiye baba wa nguvu hizo za giza.
---

Ndani ya ukumbi uliowekwa kamera zisizoonekana, kikao cha Siri cha DEKA kilikuwa kinaendelea. Watu watano walikuwa mezani, wawili wakiwa ni wazee waliovaa suti ndefu, wakiwa na bastoni za mbao ngumu, wengine watatu wakiwa watu wa makamo, na mmoja akiwa kijana aliyevaa koti la kijeshi.

Edwin Mnyika aliingia akiwa amevaa koti la kahawia iliyochafuka na buti ndefu. Sura yake ilikuwa imetulia, lakini macho yake yaliongea mengi kuliko midomo.

“Andrew Kamage ametusaliti,” alitamka kwa sauti ya hisia za maumivu na hasira“Na Kinu pamoja na mwanamke wake Moreen… wamegeuka sumu ndani ya mfumo wetu. Tumewapa nafasi ya kutoka kistaarabu, wamechagua moto. Basi na uwawakie.”

Waliangalia picha za satelaiti, walikagua rekodi za simu, walifungua ramani za familia.
“Je, Kinu ana familia?” mmoja aliuliza.
“Rekodi zinaonyesha hakuwa na familia ya karibu. Anaishi kama mlowezi”

“Na huyu Moreen?”
“Tuna taarifa mpya. Ana mtoto wa kike, miaka nane. Anaitwa Amani Moreen. Mtoto anaishi kwa rafiki wa mama yake, aitwaye Lucy Mwasilu, mmiliki wa saluni moja kule Mbezi Beach. Lucy anaishi Kawe.”

Mnyika alitabasamu kwa uchungu. “Watoto ndio nyaya za moyo wa mama. Tukizigusa, tunapata umeme wa siri. Siri zote zitatujia hapa"
Akaongeza, “Tuma ujumbe kwa Lucy. Mwambie mtoto anaumwa. Mwambie amtumie ujumbe Moreen kwamba hali ni mbaya. Atakuja. Na tutamchukua.”
---
Jioni ya saa kumi na mbili, Lucy alikuwa ameketi peke yake ndani ya sebule ya nyumba yake ya Kawe, macho yake yakiwa hayajatulia. Simu yake ilikuwa imelowa jasho. Kwenye meza, kulikuwa na bastola ndogo ishara ya shinikizo alilopewa na DEKA. Alikuwa hana namna.

Alituma ujumbe:
“Dada Moreen, mtoto anaumwa sana. Amekuwa akikutaja. Tafadhali njoo usiku huu hata kwa dakika tano.”
Aliambatanisha picha ya Amani akiwa amelala kitandani, sura yake ikiwa imehaririwa na kubadilishwa haraka na DEKA. Ilionekana kama mtoto anaumwa kweli.

Simu ya Moreen aliyokuwa anatumia kuwasiliana na Lucy ambayo haikuwa na usajili wa Moreen, ilipopokea ujumbe huo, aliketi kimya kwa dakika tatu. Moyo wake ulianza kumdunda kwa kasi. Aliinuka, akatazama dirishani. Akamwambia Kinu:

“Nahitaji kwenda kumuona Amani. Anaumwa.”
Kinu alinyamaza. Alijua, hilo lingeweza kuwa mtego. Lakini hakusema. Alitazama macho ya Moreen na kusema:

“Tunaweza kuipoteza dunia, lakini si mtu tunayempenda.”
---

Katika giza la barabara ya Mbezi kuelekea Kawe, magari matatu ya watu wa DEKA yalikuwa tayari yamejipanga. Usiku ulikuwa kimya, lakini ndani yake kulikuwa na mapigo ya moyo wa hofu, na kwenye kona ya mwisho ya tumaini, Moreen alikuwa karibu kuingia kwenye tanuru la usaliti wa rafiki na moto wa hila.
__________

Moreen alipokuwa akitayarisha pochi yake ili kutoka kuelekea Kawe, macho ya Kinu hayakuwa yametulia hata kidogo. Macho yake yalikaribia kulia, lakini moyo na akili yake vilikuwa vikikazana kupanga njama ya kumuokoa Moreen. Alijua, huo ulikuwa mtego. Na alikuwa na dakika chache tu kuuvuruga.

Aliinua simu yake, akabonyeza namba moja: Titus. Rafiki yake wa Zamani, aliyewahi kuwa mtaalamu wa uchunguzi wa mifumo ya kompyuta, kabla hajajitosa kwenye biashara ya burudani aliyokuwa akiifanya kama geresha lakini nyuma akiwa Jasusi wa vikundi vya kizalendo.

“mchukua Moreen klabu ya usiku ya Savannah Vibe, saa tano kamili, lazima awe pale kabla ya DEKA hawajagundua,” alisema Kinu kwa haraka.

Moreen alitaka kuuliza maswali, lakini Kinu alimkatiza.
“Unaniamini?”
“Ndiyo.”
“Basi fuata kila ninachokuambia. Dakika kumi zijazo, kila sekunde ni pumzi au kaburi lako"

Wakafungua milango ya gari, Moreen akaingia upande wa kulia. Kinu akaongeza mwendo. Magari matatu ya DEKA yalikuwa yameshaliona gari lao. Shughuli ikaanza, yaliwashambulia kwa nyuma kama fisi wanaofukuzia mkia mtoto wa nyumbu. Gari la Kinu lilikuwa Toyota Fortuner ya kijivu iliyochoka, lakini injini yake Bado ilikuwa na nguvu.

Walipokaribia makutano ya Afrikana, Kinu akapunguza kasi ghafla.
“Shuka! Kimbia upande wa kushoto, ingia kwenye Savannah Vibe. Titus atakuchukua mle ndani. Usiangalie nyuma.”

Moreen hakusema neno, akatoka kama risasi iliyokosa shabaha. Alikuwa amevalia koti la kijani kibichi lenye Kofia Kwa nyuma, akanyanyua kofia na kujificha usoni kama msanii anayeficha umaarufu. Akaingia ndani ya klabu, muziki mkali ukipiga, taa zikimwekuamwekua rangi kama miale ya mawingu ya kisulisuli.

Titus alikuwa tayari amefika, mwenye suti nyeusi na miwani ya usiku. Waliangaliana kwa sekunde mbili kabla hajamwambia:

“Njoo.”
_________

Wakati huo huo, magari ya DEKA yalikuwa tayari yameshaanza kumzingira Kinu kama chatu aina ya anakonda. Kinu akaongeza mwendo, tairi zikipiga mayowe barabarani. Akaelekea
uelekeo wa Bagamoyo, kupitia njia ya Pwani, akijua walikuwa wakimfuata kama kivuli kisichochoka.

Wakafika maeneo ya Hifadhi ya Taifa ya Saadani, sehemu ya ajabu nchini Tanzania, hifadhi pekee ya taifa iliyopo kando ya bahari. Saadani ilikuwa paradiso ya wanyama na mawimbi ya bahari. Wanyama kama simba, tembo, pundamilia, na swala walionekana kwa mbali, lakini vilio vya ndege na makelele ya fisi vilichangamana na sauti ya upepo wa Bahari ya Hindi.

Ghafla, tairi ya mbele ya gari la Kinu ililipuka! Paah! Ilikuwa imepasuka. Gari likachezacheza kama mtu mlevi kisha likapinduka mara mbili, na kisha kugonga kichaka cha miba. Vumbi likapanda kama moshi wa majani mabichi yachomwapo.

Kinu akajikokota kutoka ndani ya gari, damu ikitoka puani, kichwa kikizunguka. Alikuwa amejeruhiwa, lakini Bado alikuwa mzima. Akasikia milio ya injini ya gari nyuma yake, DEKA walikuwa karibu. Akachuchumaa, akakimbia kuelekea mtoni.

Mbele yake ulikuwepo Mto Wami, wenye maji ya kahawia, yaliyobeba uvundo wa majani ya porini na samaki waliokufa. Lakini zaidi ya yote, mto huu ulikuwa maarufu kwa mamba wakubwa wenye mita tano kwa urefu.

Kinu alitazama nyuma. Miale ya taa ikimfuata kama mshale wa mwisho wa vita. Hakukuwa na njia nyingine.
Akainua mikono, akavuta pumzi ndefu kama anayetoa dua ya mwisho. Kisha akajitosa ndani ya mto.

Maji yalikuwa baridi, lakini hatari. Aliposogea ndani zaidi, alisikia miguno ya mamba, mifupa ya maji ikiwa inasongea na kumkaribia. Akaogelea kwa wepesi, akijaribu kutulia kama gogo. Akapita karibu na mamba wawili waliokuwa kimya kama mizimu ya kale.
_________.

Itaendelea....
 
HAKUNA ALIYE SALAMA
Mtunzi Robert Heriel
Chungu cha 08

Maji ya Mto Wami yaliufunika mwili wake huku anga likifunikwa na vumbi la magari ya DEKA waliokwishasimama ukingoni, wakitazama kwa mshangao ule upumbavu wa jasusi kujirusha mtoni penye simba wa majini.

Waliamini hakuna binadamu anayevuka mto huo akarudi na akili timamu au kurudi na Uhai.
Giza lilizidi kumeza kila kitu. Miti, vichaka na anga lote likajawa na nyota. Nyota zilimezwa na mdomo wa mawingu meusi yaliyokuwa yametanda. Kinu, akiogelea kwa ustadi wa kifalme, alijua sheria moja kuu ya mto: Usizidishe uwiano wa uzito na hofu. Harufu ya hofu huvuta wanyama wakali kama damu ilivyo kwa mbu. Uzito huyafanya maji yapate uhai na kuwa kiumbe chenye njaa kinachoweza kukula.

Kwa kutumia hewa iliyobakia puani, aliingia kwenye nyasi ndefu za ufukweni. Akajifuta uso kwa vazi lake la ndani, macho yake yakichungulia upande wa pili wa mto. Kulikuwa kimya kama kuzimuni.

Aliinama, akachukua tope na kujipaka usoni, mikononi na shingoni. Sasa hakuwa tena Kinu, alikuwa kama dudu baya lenye kutisha.

Akatambaa hadi chini ya miamba midogo, alafu akapumua kwa mara ya kwanza kwa uhuru, baada ya dakika ishirini ndani ya maji yaliyojaa midomo ya mauti.

“Kama mamba hawajala kiapo, basi nami nitakula kiapo mbele yao,” alinong’ona.

Wakati Huohuo, Ngome ya DEKA – Mjini

Katika ghorofa la siri lililojengwa chini ya Jumba la mawasiliano, kikao cha dharura kilikuwa kikiendelea. Edwin Mnyika, kiongozi wa DEKA, alisimama mbele ya jedwali la kioo lililokuwa na ramani ya Saadani.

“Tuna hakika hajavuka. Huo mto ni kaburi la mashujaa,” alisema kwa sauti ya shaka iliyojificha ndani ya kiburi.

Lakini haikuwa hivyo kwa Rosemary Lutulia, mwanamama wa makamo, mwepesi wa tabasamu lakini mkali kama wembe wa ngariba. Akitazama rekodi za kamera za anga, aliguna.

“Kwa nini hatujaona mwili wake?" aliuliza.
“Hana mwili wa kuibuka. Mamba hawatoi risala ya rambirambi,” Mnyika akajibu kwa kejeli.
Lakini ndani ya moyo wake, alikuwa na jasho la baridi. Kinu alikuwa jasusi wa mzoefu, mtu asiyeishi kwa sheria za kawaida.
________
Kando ya Mto, Porini, Saa Tisa Usiku

Kinu alikuwa ameweka kambi ya muda. Aliwasha moto mdogo kwa kutumia kijinga cha gesi kidogo alichokibeba tangu alipojua anazidi kukaribia “point of no return.”
Alichukua kifuko kidogo cha plastiki kwenye mkoba wake wa bega, ndani yake kukiwa na kifaa kidogo cha mawasiliano cha satelaiti, Model C-5.

Alibonyeza namba ya siri. Muda mfupi baadaye, sauti ikajibu.
“Salamu za Saadani,” alisema Kinu.
Sauti ya upande wa pili ikacheka. Ilikuwa ya Titus.
“Salamu zimefika, lakini hatujui kama unazizungumza kama mtu hai au mzimu.”
“Nimesalimika,” alijibu. “Moreen yuko salama?”

“Yuko salama. Amehifadhiwa kwenye bunkeri ya Daraja la Pili, Pugu. Hakuna hata mdudu anajua.”
“Nahitaji mipango ya kuondoka kwenye eneo la mto, ndani ya saa moja,” alisema Kinu. “Tuma ndege ya kawaida ya wanyamapori, nitajificha kama msaidizi wa mbio za utafiti.”

“Unayo ID?”
Kinu akatabasamu kimya kimya, akachomoa pochi yake ya siri. Ndani yake kulikuwa na vitambulisho vitatu: cha mtafiti, cha rubani msaidizi, na cha mwanahabari.

“Najua jina la ndege, nahitaji wewe uratibu rubani.”\n\n“Roger that,” alijibu Titus.\n\nKinu akaifuta simu na kuitupa ndani ya mto. Mamba mmoja mdogo alijitokeza mbali, lakini akaogopa mwako wa moto mdogo uliokuwa unatoa mvuke.

§ Saa 10:45 Usiku, Viwanja vya Hifadhi, Saadani

Helikopta ndogo ya utafiti ilitua kwa heshima ya dharura. Kinu alikuwa tayari keshajificha kwenye boksi kubwa la vifaa vya kimaabara, akiwa amevaa koti la kijani na glovu. Aliingia, akakaa nyuma ya rubani. Walipaa juu, na ndani ya dakika thelathini, walikuwa hewani wakikatiza anga la Pwani.

Kinu alitazama chini; pori, mito, na mawimbi ya bahari vilikuwa vinamkumbatia kama mama anayemshukuru mwanawe kurudi nyumbani akiwa hai. Alifumba macho na kusema:

“Leo nimezaliwa mara ya pili. Sasa sina muda wa kufa, nina kazi ya kukamilisha. Alikumbuka simulizi ya Mtibeli yenye jina la ajabu, Siku yangu ya kufa Ilipita, akahisi naye ni miongoni mwa wahusika katika simulizi hiyo ya kushangaza.
---
Katika bunkeri ya Daraja la Pili, Pugu, Moreen alikuwa ameketi kimya, macho yake yakiwa yamevimba kwa uchovu na hofu iliyobeba silika ya mwanamke. bunkeri ile ilikuwa imejengwa kama sehemu ya kujificha wakati wa vita, lakini sasa ilitumika kulinda harakati za mapambano.

Amani, binti yake, alikuwa amelala, usingizi wa mtoto uliochanganyika na kivuli cha mashaka, Titus alikuwa nje, akihakikisha hakuna mdudu wa DEKA anayejua mahali pale. Mpango wa kumtorosha Amani uliratibiwa na Kinu siku ile. Wakati akikimbizwa na DEKA, nyumba Titus alikuwa ameenda kumchukua Amani kisha akamhifadhi sehemu Salama.

Moreen alichukua daftari dogo, akaandika kwa wino mwekundu, “Nilikuwa Make-up artist, nikawa Mama, sasa nimekuwa Mwanamke mpiganaji, mwenye kupitia mkondo wa kijasusi. Leo wanataka kumtumia mwanangu kama chambo kunikamata. Sitakubali"
****

Benedicto Mlauzi alikuwa amepokea taarifa kutoka kwa Kinu, alijua sasa DEKA walikuwa wamevuka mstari mwekundu, kumtumia mtoto wa moreen katika mapambano haya, ilikuwa ni tangazo la vita.

Alichukua bahasha ya ngozi, akafungua ramani ya zamani ya makao ya DEKA, palikuwa na alama tatu nyekundu, alijua mahali pa kuanza, alafu akamtumia ujumbe mmoja tu kwa njia ya satelaiti ya siri, “Tunasonga, kuvamia makao Yao ndiyo mkakati wetu”
******
Mama Lutu alikuwa ameketi katika chumba cha kioo, pembeni mwa jukwaa la skrini kubwa, mikono yake ilikuwa kwenye vitufe vya kudhibiti mitambo, lakini akili yake ilikuwa mbali, Dodoma, miaka mingi iliyopita, alipokula kiapo cha kuwahifadhi walio dhaifu, lakini sasa, alikuwa mlinzi wa mfumo uliowaua dhaifu.

Akiwa amevaa blauzi ya kijivu iliyotengenezwa kwa pamba ya Misri, alitazama skrini moja iliyokuwa na picha ya mtoto, Amani, picha ile haikuondoka, haikufutika, Mama Lutu alipumua kwa nguvu, kisha akachora herufi tatu kwenye kitufe cha siri, R.L.K.

Rosemary Lutulia Kosa.
*******
Kinu alikuwa ameshafika kwenye jengo dogo la utafiti wa mimea porini, ambalo lilijengwa na taasisi moja ya Wajerumani, wafanyakazi wa kawaida walikuwa bado hawajafika, aliingia kwenye chumba cha chini, akachomoa mkoba wake, ndani yake kulikuwa na silaha tatu, bastola ya sig-sauer, kisu kilichotengenezwa kwa chuma cha Damascus, na kifaa cha kutambua mikrowevu za kamera za siri.

Lakini zaidi ya silaha hizo, alikuwa na silaha kubwa kuliko zote taarifa. Taarifa alizotumiwa na Benedicto pamoja na zile walizokusanya na Andrew Kamage.
Alijua DEKA walikuwa wakimtafuta, na sasa alikumbuka jalada moja alilotumiwa, lililotajwa na Andrew Kamage, jalada lililokuwa na jina, OPERATION: SIMBA WA GIZA.

Mpango wa kuanzisha kambi za mafunzo ya siri kwa watoto wa mtaani, kuwaandaa kuwa wapelelezi wa DEKA kwa vizazi vijavyo.

Kinu alipiga picha ya jalada hilo ambalo tayari lilikuwa limenaswa kwenye flash iliyofichwa katika simu bandia aliyoiokota kutoka jengo la zamani la DEKA Kurasini, ndani yake, alikuwa na jina la mtoto mmoja aliyenusurika mafunzo hayo, mtoto aliyekuwa mwerevu, aliyepotea, aliyefichwa, Amani Moreen.

DEKA walikuwa wakitaka kumchukua si kwa Moreen tu, bali kwa kuwa ndiye mlango wa ushahidi na namna ya kumdhibiti Kinu na kundi lake. Waliamini wakimchukua Amani, Moreen atakuwa hana ujanja.

Amani Binti mdogo ni miongoni mwa watoto waliosoma katika shule za kawaida za serikali, ambao walibahatika kupata udhamini na Shirika binafsi liitwalo Hug the Kids ambalo Kwa siri lilikuwa linadhaminiwa na kundi la DEKA. Akahamishwa kutoka shule ya kawaida na kupelekwa shule binafsi za kimataifa zilizopo nchini. Moreen alifurahia Msaada huo wa Hug the Kids kwani aliona ndoto za mwanaye zinaenda kutimia.

Lakini Mambo hubadilika muda wowote. Kwa Moreen sio tuu yalibadilika bali yalimbadilisha hata yeye.
*******

Sauti ya alama nyekundu ililia ghafla, Mama Lutu alishtuka, akasoma ujumbe kutoka kwa mmoja wa askari wa DEKA, “Tunaamini mtoto yuko njiani kuelekea Lugalo, Lucy ametoka.”
Mnyika alikimbia hadi kwenye skrini, “Siwaamini tena,” alisema kwa hasira, “Mama Lutu, futa, kila kitu, tuanze upya, tumia Mpango Mwaka 0.”
Mama Lutu akageuka taratibu, macho yake yakidondoka kwenye picha ya Amani iliyokuwa bado imefunguka kwenye skrini, moyo wake ukawa unapiga Kwa nguvu, akaonyeza kitufe, na taa zote zikawaka rangi ya nyekundu.

Kinu alikuwa amevalia mavazi ya dereva wa ambulensi, gari lilikuwa limeegeshwa kwenye kona, tayari kwa hatua ya mwisho ya uokoaji, alikuwa ametuma ujumbe mmoja tu kwa Titus, “Chukua picha ya mtoto na Moreen, tuma kwa vyombo vya habari vya kimataifa, fungua jalada la Simba wa Giza, ikiwa DEKA wakienda mbali—tutaenda mbali zaidi.”

Moreen alipokea picha ya Amani akiwa salama, alilia kwa mara ya kwanza tangu mapambano yaanze.
Tumechoka kukimbia, sasa tutakimbia mpaka lini. kila hatua ni vita.
Hivyo ndivyo ilivyokuwa;

Itaendelea;
 
HAKUNA ALIYE SALAMA
Mtunzi; Robert Heriel
Chungu Cha 09


Benedicto Mlauzi alionekana kuwa na afya njema siku hiyo ya mwisho. Alikuwa amekutana na ujumbe maalum wa Umoja wa Mataifa kwenye mgahawa wa kifahari jijini Bissau, sura yake ikiwa tulivu kama bahari isiyo na upepo. Aliongea kwa ufasaha, akasisitiza juu ya umuhimu wa kulinda haki za binadamu na kuunga mkono harakati za kujenga mataifa huru barani Afrika.
Lakini usiku huohuo, aliporudi kwenye nyumba yake ya balozi, hali yake ilianza kubadilika. Akaanza kukohoa kwa nguvu, macho yake yakageuka kuwa mekundu, na ngozi yake ikaanza kutoa jasho la homa kali. Alipojaribu kuongea, sauti yake ilivunjika kama kioo kilichopasuka kwenye Sakafu ya vigae. Wahudumu wake walimkimbiza kumpeleka hospitali ya karibu, lakini hali yake ilizidi kuwa mbaya.

Siku iliyofuata, aliambiwa kuwa atasafirishwa kwa haraka hadi Afrika Kusini kwa uchunguzi zaidi. Ndani ya ndege ya matibabu, alilala bila fahamu. Alipofikishwa Pretoria, katika moja ya hospitali kubwa, madaktari walishindwa kuelewa sumu iliyokuwa inamsumbua. Ilikuwa aina ya sumu isiyoonekana kwenye vipimo vya kawaida. Ndani ya masaa arobaini na nane, moyo wa Benedicto ukasimama. Alikufa akiwa peke yake, mwili wake ukipambwa na kimya kilichojaa maswali.

Habari za kifo chake zilitangazwa kama “kifo cha ghafla kutokana na matatizo ya kiafya yasiyojulikana.” Lakini kwa Kinu, Moreen na Andrew Kamage, hiyo ilikuwa taarifa ya kawaida ya kuuficha ukweli. Walijua. DEKA walimfunga na kamba shingoni kwa staili ya kitaalamu, sumu ya kimfumo, yenye uwezo wa kutoweka ndani ya damu. Huo Ulikuwa ni ujumbe. Ujumbe wa kuwakumbusha kuwa hata walio mbali, hawako salama. Na waliokaribu wakae kwa tahadhari.

Wakati huo, Mama Lutu alikuwa ameketi katika chumba chake cha faragha, macho yake yakitazama taarifa za kifo cha Benedicto kwenye televisheni ya kisasa. Aliinuka taratibu, miguu yake ikisonga kwa uzito wa dhamira iliyovunjika. Aliwahi kumchukia Benedicto. Lakini hakuwahi kutamani afe. Alikuwa mpinzani aliyefahamiana naye kwa miaka kumi na Tano. adui wa mwili lakini rafiki wa moyo wake siku zote. Sasa DEKA walikuwa wamevuka mpaka ambao ulivunja uvumilivu wake.

Alihangaika usiku mzima. Roho yake ilianza kulia kwa sauti ya ndani ambayo haikusikika kwa mtu mwingine. Ilikuwa ni sauti ile ile iliyomwita miaka mingi iliyopita alipokuwa binti wa saikolojia, akiwa chuoni Dodoma, akiamini kuwa haki inaweza kusimama hata mbele ya risasi. Usiku huo, alifungua kabati la mbao lililokuwa limefichwa nyuma ya maktaba yake. Ndani yake kulikuwa na koti lake la zamani alilonunuliwacna Benedicto,. kitambulisho cha zamani cha mashirika ya haki za binadamu, na bastola ndefu ya Colt.

Alijua ilibidi arudi uwanjani. Hata msaliti ananafasi ya kurejesha uaminifu hata kama ingebaki sekunde Moja.

Aliamua kuanza safari moja t, kwenda kwenye ranchi ya Andrew Kamage. Pengine bado alimwamini. Pengine alihitaji kuomba msamaha. Alipofika, lango lilifunguka taratibu, lakini hakuona mtu. Nyasi zilikuwa zimenyeshewa, lakini hazikuwa na alama za miguu ya karibuni. Alitembea hadi kwenye jumba kuu, akafungua mlango mkubwa wa mbao kwa msukumo wa polepole. Ndani kulikuwa kimya. Vumbi kidogo, lakini kila kitu kilionekana kuachwa kwa makusudi.

Akaingia sebuleni, macho yake yakitazama picha ndogo iliyowekwa ukutani. Picha ya Andrew akiwa kijana, akiwa na bastola begani. Mama Lutu akapumua kwa nguvu. Alijua Andrew hakumuamini tena.

Alijua alikuwa anatazamwa. Uzoefu wake kuhusu watu kama Andrew ulimhakikishia kuwa jicho la Andrew lilikuwa eneo lile.
Hakujua ni kamera gani, wala wapi ilipo, lakini alihisi jicho likimtazama. Aliketi kimya kwenye kiti cha mbao, akatoa pochi yake, ndani akatoa karatasi na peni ya bluu. Akaandika kwa haraka lakini kwa umakini. Maneno machache tu. Maneno yenye maana kwa Andrew pekee. Alipomaliza, akaikunja karatasi na kuiweka juu ya meza ya kioo. Kisha Alisimama, akatulia kwa sekunde chache, halafu akaondoka bila kusema neno.

Na kweli, Andrew alikuwa anatazama. Akiwa kwenye eneo lingine la siri, chumba kilichojaa skrini na kompyuta za hali ya juu, alimtazama Mama Lutu kwa jicho la mtu aliyeshindwa kupima mapenzi dhidi ya maumivu. Aliona namna alivyotembea polepole, namna alivyoketi, na jinsi alivyoandika ile karatasi. Na alijua: Mama Lutu alikuwa amevunja kiapo cha DEKA.

Wakati huohuo, Kinu alikuwa tayari amekamilisha mpango mpya, kuingia kwenye sherehe rasmi ya DEKA, ambazo mbele ya umma zilijulikana kama "Maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika." Lilikuwa tukio la hadaa, ambapo DEKA walijivika sura ya wafadhili, walinzi wa watoto, wakati nyuma ya pazia walipanga mipango ya kudhibiti kizazi kijacho.

Kinu akatengeneza utambulisho bandia, akaingia ndani ya ukumbi wa sherehe akiwa amevaa suti nyeusi, suruali yenye mikato ya kijeshi na miwani nyeusi. Titus na Moreen walikuwa nje, wakihakikisha kuwa kamera za usalama zimedukuliwa na mifumo ya DEKA kuharibiwa kwa dakika chache tu za kutosha kwa Kinu kufanya jambo moja muhimu.

Kinu Alitembea ndani ya ukumbi akipitia watu waliovaa vizuri, viongozi wa serikali, wanasiasa waliouza nafsi zao Kwa matendo ya kidhalimu, na maafisa wa DEKA waliovaa vyeo vya kiutu ndani yao kukiwa na majeshi ya mazombi yanywa damu. Muziki wa watoto ukawa sauti ya hadaa, ilhali silaha na sumu zikiwa mezani nyuma ya jukwaa. Alipofika ukingoni mwa meza kuu, ndipo macho yake yalipokutana kwa mara ya kwanza na mtu aliyemtafuta kwa miaka, ndiye Edwin Mnyika.

Mnyika alikuwa ameketi, akizungumza na afisa wa ngazi ya juu kutoka SADC. Uso wake ulikuwa umetulia, lakini macho yake yakiwa ya chuma kilichovutwa na Sumaku. Kinu alipomuona, kila chembe ya damu yake ilicheza. Alitaka kumsogelea, amvute kwa mikono, amuumize, amuonyeshe kuwa maisha ya Benedicto hayakuwa ajali. Amuonyeshe waliotekwa na kupotezwa nao walihitaji kuishi. Lakini mazingira yalimdhibiti. Watu wengi. Kamera. Mashahidi. Alijua hiyo haikuwa wakati sahihi, ilikuwa saa ya ushahidi.
Akatabasamu kidogo, akapita kando ya meza, na bila hata kugusa kiti, alijua vita halisi imeshatangazwa.

Kwa mara ya kwanza, uso wa Kinu ulionekana kwenye skrini ya DEKA. Kwa mara ya kwanza, Mnyika alimwona adui wake akiwa hai.
Na kwa mara ya kwanza, DEKA wakaanza kuhisi hofu ya kupoteza udhibiti.
---

Karatasi ile iliachwa juu ya meza ya mbao kama njia ya mawasiliano. Ilikuwa imekunjwa mara mbili, peni ya rangi ya bluu ikiwa bado imeacha doa dogo pembeni. Maneno yaliyoandikwa kwa mkono wa Mama Lutu yalikuwa mafupi, ya moja kwa moja, lakini yenye uzito wa lugha za kijasusi:

“Wamevuka mstari mwekundu. Sitaki tena kuwa mlinzi wa giza. Ninarudi upande wa Nuru. Sauti ya watu. Nitatoa majina, ramani, na walipo waliopotea. Tafuta alama ya waridi kwenye jiwe la mwisho. Tupo upande mmoja sasa. – R.L.K.”

Andrew Kamage alisoma ujumbe huo kwa macho ya mtu aliyezoea kuishi maficho. Alijua watu waliokuwa kama Mama Lutu Akili zao zinafanyaje kazi. Alinyamaza kwa dakika nzima, kisha akampigia Kinu kwa njia salama:

“Yuko ndani. Amerudi.”
“Unamaanisha nani?” sauti ya Kinu ilikuwa ya haraka na kali.
“Rosemary. Mama Lutu. Amejiondoa DEKA. Ameacha ujumbe. Anasema amerudi kwenye mapambano.”
Kinu alikaa kimya kwa muda, kisha akavuta pumzi ndefu.
“Andrew… usipuuze uwezekano wowote. Huu unaweza kuwa mtego. Huyu mwanamke anajua kila sehemu ya mfumo wetu. Tayari alishaiuwa Msaliti. Anaweza kuja kutumaliza. Siwezi kumuamini bado. Si haraka namna hii”

Andrew akatabasamu kwa uchungu. “Nimekuelewa. Lakini bado kuna upande wa moyo unaoamini. Nitamfuatilia mwenyewe.”

Wakati huo huo, maandalizi ya mazishi ya Benedicto Mlauzi yalikuwa yamekamilika. Taarifa zilianza kurushwa kwenye vyombo vya habari. Msiba mkubwa, maziko ya kitaifa, kufanyika katika makaburi ya viongozi na watu mashuhuri wenye heshima na matajiri, nje kidogo ya jiji. Mabalozi walialikwa, viongozi wa dini walithibitisha kushiriki, na Rais mwenyewe alitarajiwa kutuma mwakilishi wake.

Kinu alikuwepo, lakini hakuonekana. Alikuwa ameketi kwenye mstari wa pili nyuma ya waombolezaji wa kawaida, sura yake ikiwa imebadilishwa kabisa na make-up aliyotengenezewa na Moreen. Hata kamera za usalama zilimwona kama mgeni wa kawaida, raia wa kigeni labda. Moreen alikuwa amevaa koti refu la rangi ya kahawia. miwani nyeusi na skafu ya rangi ya udongo. Walikaa kimya, wakitazama, wakisoma kila nyuso, kila jicho, kila harakati.

Hotuba ya msiba ilicheleweshwa kwa dakika chache. Watu walikaa kwenye viti vya plastiki vyenye mikeka, wengine wakisimama chini ya mahema meupe. Mke wa Benedicto alisimama, akipokea kipaza sauti kwa mikono iliyoonekana dhaifu kwa nje lakini iliyobeba ujumbe wenye kilio kinachohitaji mbembelezaji.

Sauti yake ilikuwa tulivu, lakini yenye mwangwi uliopenya hadi ndani ya mioyo ya watu waliohudhuria

“Leo hatujakusanyika hapa kumlilia tu mume wangu, bali kumuaga askari wa haki, shujaa ambaye alisimama hata pale ambapo watu walikaa kimya. Benedicto hakuwa malaika, lakini alikuwa na dhamira. Na leo, si mimi, sio wewe. Yeyote! Hakuna aliyesalama ikiwa tutaacha giza litawale katika macho ya wenye mboni. Wahalifu waliojilinda kisheria, waovu walioajiriwa na mifumo na kulipwa kwa kodi za watu maskini, mbwa mwitu waliovaa rozali na kanzu kama makuhani waaminifu, wataua wasiridhike! Tunaowajibu wa kushikamana pamoja, sio kulilia hapa maisha ya Benedicto shujaa aliyeyatoa maisha yake kwa ajili ya taifa, bali kuungana kutetea dhamira ya haki aliyotuachia.”

Akanyamaza kwa sekunde kadhaa, machozi yakianza kujaa katika macho yake malegevu, lakini yaliyoshikiliwa na misuli inayopenda Kuona haki inafanyika;

“Tunahitaji haki kwa waliotekwa, waliopotezwa, na waliopo jela kwa makosa ya kisiasa, waliosingiziwa kwa hila. Wakati tunaulaza mwili wa mume wangu, ni muda wa kusafisha taifa letu, siyo kwa risasi kama wahalifu wanavyo fanya. Au Kwa sumu kama waovu walivyomfanyia Mume wangu, bali kwa uamuzi wa pamoja. Sitaki sifa kwa mume wangu, nataka haki kwa nchi yake.”

Watu walikaa kimya. Kisha mmoja mmoja akaanza kupiga makofi. Polepole. Makofi yaliyogeuka sauti ya mapinduzi yaliyokuwa kama mche wa mchicha wakati wa ukame.

Katikati ya umati, Andrew Kamage alikuwa amemweka Mama Lutu kwenye jicho lake ambalo linasifa ya kutokupepesa. Alimtazama akisogea polepole hadi sehemu ya wageni wa familia. Lakini kabla hajamfuata, msichana mmoja aliyevalia Kaunda suti ya kijivu na kilemba cha ugoro alimsogelea na kumpa karatasi ndogo, bila kusema neno. Alikuwa na uso wa kawaida, mtu wa mtaani, asiyevutia kutiliwa mashaka. Yule msichana akamletea Andrew kile kikaratasi.

Andrew aliisoma karatasi hiyo kwa haraka.
“Jioni hii. Mlimani City. Restaurant ya Wachina. Kaa kwenye meza yenye kiti kilichowekewa kitambaa cha kijani chenye kipepeo cheusi.”
Aliitunza karatasi hiyo ndani ya pochi ya mkono wake wa suti, halafu akarudia kazi yake ya kufuatilia mienendo ya Mama Lutu.

Ilipofika jioni, Andrew alivaa koti lake la bluu na kofia ya kijani iliyochakaa makusudi, akaingia Mlimani City kwa njia ya nyuma ya maegesho. Alitembea kwenye kivuli cha paa la ukumbi, akichunguza kila kona ya Restaurant ya Wachina. Taa za njano zilikuwa zikiangaza kwenye dari, lenye mapambo ya kituruki na kichina yaliifanya sehemu hiyo ionekane kama sinema ya kuvutia.

Alipofika, aliona meza mbili zilizotengwa pembeni. Kiti kimoja kilikuwa na kitambaa cha kijani kilichoshonwa kipepeo mweusi. Lakini kilicho mkanganya zaidi, ilikuwa meza ya pili iliyokuwa na kitambaa cha buluu chenye alama ya umbo la nyuki. Viti viwili, alama mbili tofauti. Na hakuna mtu aliyeonekana kuwa na haraka ya kumkaribia.

Aliamua kusubiri. Kwa dakika kadhaa, aliangalia kila mpita njia. Hakuna aliyetambua uwepo wake. Lakini ndani ya nafsi yake, alijua hakuna alama isiyo na maana. Leo ilikuwa jioni ya kujaribu roho yake. Au kuikomboa.

Aliweka mkono wake kwenye mfuko wa koti lake, karibu kabisa na bastola ndogo ya dharura. Akavuta pumzi. Akajiandaa kwa chochote.

Kwa sababu sasa, kila ishara ni hatua. Na kila hatua ni vita.
_____&__

Itaendelea.

Kesho mambo yasipokuwa Mengi.
Maoni yako hasi na chanya ni muhimu.
 
HAKUNA ALIYE SALAMA
Mtunzi: Robert Heriel
Chungu cha 10
---

Andrew Kamage alikaa kwenye meza kwa ukimya wa kimkakati, macho yake yakihama kati ya meza yenye kitambaa cha kijani chenye kipepeo mweusi, na ile ya pili—iliyokuwa kimya lakini imesheheni hila, kitambaa cha buluu chenye alama ya nyuki kilionekana kana kwamba kilikuwa kinamuuliza: Upo upande gani wa historia?

Dakika tano zikasonga. Hakuna aliyeingia. Muziki wa Kichina ukapiga kwa sauti ya taratibu, mdundo wa vinanda vya jadi na filimbi zenye sauti kama za upepo uliofungwa kwenye chupa ya kioo. Wahudumu walipita kwa mwenendo wa kawaida, wakitoa menu bila kuuliza. Hakukuwa na shaka yoyote ya wazi, lakini kila sekunde iligeuka sauti ya bomu likisubiri kulipuka ndani ya moyo wa jasusi aliyezoea kupima hatari kwa pumzi.

Akaamua kusogea. Kwa utulivu wa mtu aliyepitia majaribio la kuuawa mara nyingi, Andrew alisogea na kuketi kwenye kiti cha kijani kilichokuwa na alama ya kipepeo kama alivyoelekwzwa. Dakika mbili baadaye, kiti kilicho mkabala na chake alikaa mwanamke aliyevaa gauni refu, sura yake ikiwa imefichwa kabisa. Hakuongea Wala hakutoa sauti. Aliweka pochi ndogo mezani, akasukuma karatasi kuelekea kwake.

Andrew aliisoma haraka:
"Karibu kwenye kiti cha mabadiliko. Kiti cha buluu ni fursa, cha kijani ni hatima. Tazama nyuma yako. Uamuzi hauko mezani, uko mlangoni."

Akageuza shingo na macho kwa tahadhari. Alipotazama nyuma, hakuona kitu cha ajabu, lakini dirisha la kioo lilionesha kivuli cha mtu aliyesimama pembeni ya jengo, sura yake ikiwa imefichwa na miwani mikubwa ya jua na kilemba cha rangi ya mchanga.
Hapo alielewa, huu haukuwa mkutano, ulikuwa mtihani wa uaminifu. Jaribio la kuona kama bado alikuwa ndani ya mfumo wa usaliti, au tayari ameweka mguu kwenye mto wa mapinduzi.

Akaamka polepole, macho yake yakimfuata mtu huyo yule, lakini alipotoka nje, mtu huyo hakuwa pale tena. Alikuwa amepetoa kama Jini la Oman.

Wakati huohuo, Kinu na Moreen walikuwa ndani ya ghala lililotelekezwa, mashariki ya jiji, wakipitia taarifa mpya kutoka kwa Andrew kuhusu ujumbe wa karatasi ya Milimani City. Kinu alisoma taarifa hiyo kwa macho yaliyojaa mashaka.

“Huu ni mchezo. Hatujui kama huu ni mkono wa Mama Lutu au wa mnyama mwingine anayejifanya alama mpya ya ukombozi”

Moreen akamtazama, “Lakini bado kuna ishara ya kweli. Maneno haya sio ya DEKA. DEKA hawatoi fumbo lenye mwelekeo. Wao huandika vitisho, si alama.”

Kinu akawaza. Akakumbuka barua ya Mama Lutu. Ilikuwa na maneno yaleyale ya kishairi, mafumbo yaliyojaa ramani zilizofichwa kwenye majina. “Tafuta alama ya waridi kwenye jiwe la mwisho...” Ilikuwa njia yake ya kusema: Kuna ukweli chini ya kaburi la uongo.

“Tutakutana naye,” Kinu akasema. “Lakini kwa masharti yetu. Tutamtengenezea Njia ya kufuata. Si wao.”

Wakati huo, Mama Lutu alikuwa amefika mahali palipoandikwa katika ramani yake, eneo dogo lililojengwa karibu na msitu wa Kawe, nyumba ya ghorofa, ambayo zamani ilitumiwa kama kituo cha usimamizi wa viwatilifu. Ilikuwa haitumiki hasa gorofa ya juu Kabisa, kulikuwa bado na kiti kimoja cha mbao na meza ya chuma, pazia lilining’inia kama mnyama aliyekatwa mguu mmoja.

Akasimama mbele ya kioo kilichopasuka nusu, akajiona kama kivuli cha mtu aliyekuwa mwanaharakati, mwanasaikolojia, mlezi, msaliti, na sasa… mkombozi wa mwisho.

Aliongea na kioo:
“Wameua mtu wa mwisho aliyenibakiza na chembe ya uvumilivu. Walidhani ni Balozi tu, lakini waliua kiapo changu cha mwisho. Sasa watalipa kwa matendo yao.”

Aliweka flash ndogo mezani, yenye kumbukumbu ya mpango wa siri ulioitwa MK0: Mwanzo wa Mwaka Sifuri, mpango wa kufuta wakosoaji wote, wa kuwakamata watoto wa wapinzani na kuwatumia kama vichocheo vya utii mpya. Mpango huo ulikuwa tayari umeanza. Hapo ndipo alijua, huu si wakati wa mazungumzo.

Mama Lutu alichomoa simu yake ya dharura, akaandika ujumbe:
“Tayari kwa mkutano. Si milimani tena. Nakupeleka kwenye kaburi lao.”
Aliutuma kwa jina moja tu: Kamage.

Ndani ya saa moja, Andrew alipokea ujumbe huo akiwa ameketi kwenye chumba cha chini kabisa cha usalama, ndani ya ngome yake mpya iliyo ndani ya jengo la kibiashara—ambapo kila ofisi ilikuwa mnara wa taarifa. Alimsomea Kinu ujumbe huo.

“Yuko tayari.”

“Bado siiamini,” Kinu alisema. “Lakini kama analeta majina ya waliopotezwa na mpango wa Mwanzo wa Mwaka Sifuri, basi ana thamani kwetu"

Andrew alimtazama, “Kwa mara ya kwanza, tunaye mtu kutoka ndani ya DEKA ambaye yuko tayari kuhimili mzigo wa ukweli. Lakini hii ni ndoto ya ajabu. Tutalipa gharama.”

Kinu akavua koti lake, akaweka bastola kiunoni. “Ni muda wa kulipa gharama hizo.”

Na wakati huohuo, Mnyika alikuwa kwenye chumba cha rangi ya kahawia, meza mbele yake ikiwa na ramani ya vituo vya mikakati. Aliketi kimya, akimsikiliza mmoja wa maafisa wake akimwambia:
“Tumepoteza mawasiliano na Mama Lutu kwa siku mbili. Flash moja ya Mk0 imeibiwa. Inawezekana Kamage au Kinu wanajua kila kitu.”
Mnyika alinyamaza. Akasogea kwenye kioo kikubwa mbele yake. Akasema maneno manne tu, kwa sauti ya mwisho:

“Basi… tuanze kuwachoma.”
Kwa sababu sasa, kivuli cha kweli kimeanza kuingia katika nuru.

Na vita si ya siri tena. Ni ya hatima. Tutaua yeyote. Mmoja baadaye mwingine bila kuwapa nafasi.
--------+

Flash ndogo ya metali nyeusi, yenye nembo ndogo ya kijasusi, ilizungushwa kwa vidole vya Kinu kwa umakini kama mtaalamu wa silaha anayekagua kombora kabla ya kulifyatua. Ndani ya kifaa hicho, kilichoibiwa na Mama Lutu kutoka ghorofa la chini la DEKA, ndiko kulikokuwa na ukweli mzito kuliko uzito wa silaha yoyote waliyo nayo sasa.

Walikuwa wamejificha ndani ya chumba cha giza, ndani ya jengo la zamani la posta lililo katikati ya jiji, mahali ambako satelaiti haziwezi kuona, kwani mitambo ya DEKA ulikuwa imewekewa ‘jammer’ ya kijanja iliyotengenezwa na Titus, ambaye kwa sasa alikuwa amejificha kwenye meli ya mizigo iliyokuwa njiani kwenda Cape Town.

Kinu aliunganisha flash hiyo kwenye kompyuta isiyo na intaneti. Mara tu faili lilipofunguka, kimya kilifunika chumba. Kelele pekee ilikuwa ni pumzi za Andrew na Mama Lutu, wakisubiri kusikia ukweli waliokuwa wanauhisi, lakini hawakuwahi kuuona.

Faili kuu lilikuwa na jina: MFUMO 0: MISINGI YA DEKA

Ndani yake kulikuwa na picha za zamani, nyaraka za mikono, sauti zilizorekodiwa miaka ya tisini, na zaidi ya hapo, ramani ya mfumo mzima wa DEKA, ikiwa na ngazi zake za viongozi, wahusika wake, na mahali walipo.
Lakini kilichoitingisha dunia yao hakikuwa muundo tu, bali faili moja maalum lililopewa jina: “DIRA KUU – IKULU / ENEO SIRI – RED SECTOR.”

Faili hilo lilikuwa na maelezo kuwa ndani ya Ikulu, kwenye sehemu ya chini ya jengo la kihistoria lililojengwa enzi za ukoloni, palikuwa na chumba cha maktaba, sehemu ambayo haikuwepo kwenye ramani yoyote ya Serikali, isiyoonekana hata kwa marais waliopita. Sehemu hiyo ilikuwa na makubaliano ya awali ya kuanzishwa kwa DEKA kwa msaada wa mataifa makubwa ya Ulaya, hasa Ujerumani na uingereza na sehemu ya shirika la kiintelijensia la kimataifa lililowekewa nembo ya “Kondoo mwenye pembe.”

Dira hiyo ilikuwa na mikataba ya siri, taarifa juu ya wanasiasa waliowekwa madarakani na DEKA, majina ya majaji waliolipwa kuharibu kesi za haki za binadamu, na hata maelezo ya waandishi waliopotezwa. Ilikuwa mzizi wa mfumo mzima wa DEKA.

Moreen alipohakikisha taarifa zipo salama, akasema kwa sauti ya kuganda, “Hiki si kielelezo tu, ni kaburi lenye miili mingi. Miili ya wasio na hatia na waliouawa Kwa kutaka kukiuka amri za DEKA. Kielelezo Kama hiki kitawekwa wazi…”

Andrew akamalizia, “...kitaunguza na kuangusha serikali nzima.”

Wakati huo huo, walipokea taarifa ya kiintelijensia kuwa mpango wa maandamano ya mwisho ulishindikana. Serikali kwa kutumia DEKA ilifanikiwa kuvunja mawasiliano, kuzuia mitandao ya kijamii, na kuwatia nguvuni waandaaji wakuu kabla siku ya maandamano kufika.

Mama Lutu alitikisa kichwa, “Tumepoteza nafasi ya kuchochea watu. Sasa hatuwezi tena kutegemea nguvu ya umma wa ndani. Tutahitaji shinikizo la nje.”

Andrew akasisitiza, “Tutafute vyombo vya kimataifa, UN, AU, Jumuiya ya Ulaya... tusukume taarifa hizi huko.”
Lakini Mama Lutu alitabasamu kwa huzuni, akawaangalia kwa jicho la mtu aliyechoka kucheza mchezo wa hadaa.

“Hamjui bado? DEKA si tuu watu wa ndani ya nchi tuu.. Wanahisa wa nje wana maslahi pia. Baadhi ya nchi hizi mnazotegemea, zimesaini mikataba ya siri na DEKA. Wamewekeza. Wanafaidika. Wamesaidia kufadhili ‘Mwaka Sifuri’ kwa kutumia majukwaa ya misaada ya maendeleo.”

Kimya kikatawala tena.
Kinu aligonga meza kwa mkono, “Basi tunabaki na njia moja. Tunahitaji faili lile lililopo Ikulu. Lile lenye jina la ‘Red Sector.’ Hilo likitoka, kila aliye ndani ya mfumo ataanguka.”

Andrew akauliza, “Utaingiaje?”
Kinu alinyanyuka, akaanza kutembea chumba chote akipanga akilini mwake, kisha akaanza kueleza:

“Mpango huu hauitaji bastola. Unahitaji hila, muda na mtu mmoja ndani.”
Alifungua ramani ya jiji, akaonyesha sehemu ya nyuma ya Ikulu. “Hapa kuna lango la kale lililokuwa linapitisha wapishi na wafanyakazi wa zamani wa mkoloni. Lango hili sasa linatumiwa na mafundi wa matengenezo. Siku ya jumatatu, kuna kibarua wa mkataba wa kampuni ya lift, jina lake ni Oscar Daudi. Ataingia saa tatu asubuhi. Tumejua ni mlevi na mzembe. Nitachukua nafasi yake. Nitavaa mavazi ya kazi, nitatumia ID yake, na kuingia kama fundi.”

Andrew akamkatiza, “Utaingiaje kwenye Red Sector? Si iko chini ya usimamizi wa wakuu wa kiusalama wa Rais mwenyewe?”
Kinu akatabasamu. “Ndani ya begi la zana, nitakuwa na kifaa cha kudukua digital locks. Lakini zaidi ya hapo, nitatumia gesi ya Chloromethane kwa dozi ndogo, kuwazimisha walinzi kwenye korido ya chini. Tutakuwa na dakika saba pekee.”

Moreen akaongeza, “Tutakuwekea tracker kwenye bega la suti yako. Na kamera kwenye penseli"
Mama Lutu akauliza, “Ukishalipata faili, utatoka vipi?”

Kinu alimtazama kila mmoja, kisha akasema, “Sitoki. Nitatuma faili kwa Titus kupitia mfumo wa satelaiti wa dharura aliouweka kwa majaribio. Nitatuma taarifa nje kabla sijatoka na hawajanipata.”

“Hiyo ni kazi ya kujitoa mhanga,” Moreen akasema, sauti yake ikitetemeka.

“Nimeshaishi maisha yangu mara mbili, na tangu siku ile, siku yangu ya kufa ilipita” Kinu alijibu. “Ni muda wa kuacha urithi ambao hauwezi kufutika.”
Baada ya muda mfupi, walikusanyika wote watatu katika chumba kingine, meza ya chuma mbele yao ikiwa na ramani, flash, bastola, simu za dharura, na daftari lililoandikwa Taarifa za siri.

Mama Lutu alisimama, macho yake yakiwa na ari ya kweli sasa. Alikuwa amevalia blauzi ya kijani na suruali ya kimasai ya zamani, sura yake ikiwa na utulivu wa mtu anayejua mwisho wake.

“Bado kuna njia moja,” alisema.
Andrew na Kinu walitazamana, kisha kumgeukia.

“Kuna mtego mmoja wa mwisho. Ukitumika, DEKA watajikanyaga hadharani. Ni mbinu ambayo walificha kwa miaka mingi kwa hofu ya nguvu yake. Wanaiita ‘Mfumo wa Kioo.’ Ni mfumo uliopo kwenye kituo cha zamani cha redio, kilichoingizwa mitambo ya ndani kwa ndani. Kikitumika, kinarusha moja kwa moja kwa mitandao ya kimataifa yote, bila udhibiti wa ndani. Kinafunguliwa na alama tatu tu:

Kinu akauliza, “Unajua mahali pake?”
Mama Lutu akatabasamu kwa uchungu.
“Niliwahi kulinda ufunguo wake. Na bado nakumbuka.”

Andrew akaweka mkono juu ya meza.
“Basi tukiweke kwenye hesabu zetu”

Na kwa mara ya kwanza, Kinu, Andrew, na Mama Lutu walitazamana bila hofu, bila hila, bila usaliti. Wakiwa wameunganishwa na dhamira moja: kuiangusha Deka.
_______

Kinu aliingia kama alivyojipanga, akiwa amevalia sare ya mafundi wa matengenezo ya lift, akiwa na begi la zana, kofia ya kazi kichwani, na kitambulisho halali cha Oscar Daudi kilichotengenezwa na Moreen mwenye mikono ya dhahabu. Mfumo wa usalama ulimtambua, akaruhusiwa kupita kupitia lango dogo la chini, upande wa nyuma wa jengo kuu la Ikulu. Ilikuwa ni saa tatu na robo asubuhi.
Kilichokuwa tofauti na hesabu za Kinu ni kitu kimoja tu: maktaba ya zamani aliyoijua kulingana na maelekezo haikuwepo tena kwenye eneo lake la awali.

Korido za chini ya Ikulu zilikuwa zimebadilika. Walijenga upya, wakahamisha. Mlango wa maktaba ya zamani ulifungwa, ukuta wake ukageuzwa kuwa sehemu ya ghorofa ya chini ya ofisi ya mawasiliano ya Ikulu. Hakukuwa na dalili ya mlango, wala harufu ya vitabu aliyokuwa ameitegemea. Ilibidi apoteze dakika tano zingine badala ya saba, kama dakika tano za kuzama kwenye mto uliojaa mamba.

Wakati huohuo, katika mnara wa usalama wa Ikulu, waliokuwa wakifuatilia harakati za kila mfanyakazi kupitia chip zilizopandikizwa kwenye viatu au mikanda, waligundua kuwa Oscar Daudi aliyepaswa kuwa fundi wa lift, hakuwa na mwenendo wa kawaida. Mabadiliko ya hatua zake yalikuwa yasiyolingana na historia ya tabia yake. Kwa mujibu wa data, alipaswa kuwa ndani ya jengo la wafanyakazi pembeni, lakini chip yake ilionekana kupotea kwa saa kadhaa kisha kurudi ghafla akionekana upande wa chini wa Ikulu, Kisha ikapotea Tena na haikurudi. Ni kama chip ilikuwa imezimwa au kuharibiwa.

Afisa mmoja wa usalama akasisitiza, “Check buti za magari yaliyopita saa moja kabla ya shift kuanza. ”

Ndani ya dakika kumi, walimkuta Oscar akiwa kwenye buti ya gari la huduma, mdomo wake umefungwa na plasta, mikono na miguu yake ikiwa imefungwa kwa waya wa plastiki.
Baada ya kuondolewa na kupewa huduma ya haraka, alipoamka alianza kueleza kwa sauti dhaifu, “Nilikuwa club usiku. Nilikutana na mtu mmoja… sijawahi kumwona. Alikuwa akizungumza nami… kisha nikahisi kichwa kizito… nilipozinduka nipo buti. Na ninyi ndio wakwanza kuwaona tangu nilipopotea ufahamu"

Afisa mmoja akainamisha kichwa, akashika radio, “Tunaye mtu ndani ya jengo. Aliingia kwa jina la huyu kijana. Tumevamiwa. Tuanze msako mara moja.”

Wakati huo, Kinu alikuwa ndani ya korido za chini za Ikulu, akihangaika kwa utulivu wa kijeshi. Kamera zilizoko kwenye maeneo ya chini hazikuweza kumuona vyema. Alivaa kapero nene lililofunika paji la uso, na mashavu yake yalikuwa yamepakwa wanja wenye kivuli cha kijivu uliotengenezwa na Moreen, alivyoonekana kwenye kamera, angeweza kuwa mfanyakazi yeyote wa Ikulu.

Waliomwona kupitia skrini walishangaa zaidi si kwa sababu ya sura isiyoeleweka, bali kwa uwezo wake. Aliweza kufungua milango ya chuma kwa kutumia kifaa maalum alichokuwa nacho mkononi. Alijua codes ambazo hata baadhi ya walinzi wa Ikulu hawakuwa nazo. Wengine wakaanza kujiuliza, “Huyu mtu ni nani hasa? Alipata wapi ramani hizi? Nani alimfundisha njia hizi?”

Katika moja ya milango, Kinu aliweka kifaa chake pembeni, akabonyeza kwa mlolongo wa herufi tatu: R-L-K. Mlango ukaguna, kisha ukafunguka taratibu. Ndani kulikuwa na korido nyingine, ikiongoza hadi kwenye ngazi ya chini zaidi ambayo haipo kwenye ramani ya kisasa ya Ikulu.

Akiwa huko chini, Kinu alipumua mara moja kwa kina, akashika simu yake ya dharura, ile yenye teknolojia ya satelaiti ya hali ya juu, aina ya simu ambazo bado hushika mtandao hata ukizama mita ishirini chini ya ardhi. Akamwandikia Andrew:
“Nimepata njia ya chini. Nadhani iko hapa. Ipo. Lakini hawajanigundua bado. Kama watanipata, tafuta simu hii kupitia beacon ya mwisho.”
Akakata simu, akaiweka silent kisha Akashuka ngazi hadi ghorofa ya tatu chini ya ardhi. Taa za korido zilikuwa hafifu, rangi ya manjano yenye moshi kama ukungu. Kuta zilijengwa kwa mawe makubwa ya kale, ishara kuwa sehemu hiyo ni ya enzi kabla hata ya uhuru.

Ndipo alipoikuta.
Maktaba.

Mlango wake ulikuwa na herufi tatu zilizochakaa: ARQ. Ilikuwa si jina, bali code ya ndani inayosimama kwa: Ardhini Rasmi ya Quarantine, mahali ambapo hati na taarifa zenye hatari ya kisiasa zilikuwa zikiwekwa mbali na mikono ya walio hai.

Alipoingia, vitabu na mafaili vilikuwa vimepangwa kwa makini kwenye makabati makubwa ya chuma. Vumbi lilikuwa limetanda, lakini milango ya makabati ilikuwa na mafuta ishara kuwa bado kuna mtu huja mara Mojamoja.

Kinu alianza kuchunguza. Kila faili lilikuwa na nembo. Alikuwa anasoma moja baada ya jingine “Mbinu za Mawasiliano Kati ya DEKA na Jeshi la Pili,” “Taarifa za Kikao cha Mwaka 2001 cha Mawaziri wa Ndani,” “Operesheni KIMYA 2005,” lakini yote hayo hayakuwa lengo lake. Alikuwa anatafuta faili moja tu: DIRA KUU - RED SECTOR.

Dakika zikayoyoma. Taa ya saa yake ya mkononi ikawaka taa nyekundu.
Taa hiyo ilimaanisha kitu kimoja tu: amegundulika.

Kinu alitazama juu ya paa la chumba kisha kwenye ukuta. Akatembea nyuma ya kabati kubwa, macho yake yakaona. Kamera ndogo, ya siri, iliyoingizwa ndani ya kifaa cha taa, haikuwa ikitoa sauti, lakini ilikuwa inarekodi. Alikunjua koti lake, akatoa bastola ndogo ya risasi moja yenye silencer. Akaelekeza juu, pakaa!
Kamera ikazima. Video ikakatika.

Ndani ya chumba cha usalama cha Ikulu, picha ilikata ghafla. “Tumempoteza! Kamera imelipuliwa. Huyu mtu… anajua kila kitu. Yuko wapi sasa?”

Hakuna aliyejua.
********

Inaendelea
 
HAKUNA ALIYE SALAMA
Mtunzi: Robert Heriel
Chungu cha 11

---
Ukimya wa ghorofa ya chini kabisa ya Ikulu ulikuwa mrefu kwa kiasi cha kutosha. Ulikuwa ukimya unaolia. Ukimya wa matambara ya historia yaliyozikwa bila msalaba. ukimya katika nchi iliyopoteza Makaburi ya wazalendo. Ukimya wa majivu ya falsafa ya utu na kuijtegemea ambazo zilibadilishwa kuwa uozo wenye Kunuka.

Kinu alipenya kwenye mlango ulioandikwa namba tatu tu kwa vibanzi vya chuma, "03", maandishi yaliyofutika kwa kutu, lakini yakibeba uzito wa kaburi la taifa. Aliuvuta taratibu, mlango ukalia kama koo la mtu aliyepaliwa na mfupa, Ndani kulikuwa giza, lakini macho yake, yaliyokuwa yameshazoea giza, yaliona. Kuta zilijengwa kwa mawe yenye michoro ya zamani, kama jela ya kifalme ya karne ya kumi. Chumba hicho kilikuwa kidogo, lakini hewa ndani yake ilikuwa nzito kwa kumbukumbu ambazo bado zilikuwa hai.

Aliangaza kwa tochi ya kichwani. Kulikuwa na kabati moja kubwa lenye rangi ya udongo, vumbi likiwa limekaa kama barafu juu yake. Kinu alilifikia polepole, akalifungua. Bawaba zililia, na mlango wa kabati ulijifungua ukichechemea.

Ndani kulikuwa na begi dogo la ngozi, lililozeeka, lakini limeshikilia historia kwa misuli ya ngozi yake ya ng’ombe. Akalitoa kwa makini, lakini mkono wake ukagonga kona ya chini ya kabati, na kwa bahati mbaya begi likateleza kidogo likaanguka, mdomo wake ukiwa umefunguka na karatasi pamoja na picha moja ya zamani zikaanguka chini.

Karatasi zilivurugika, lakini macho ya Kinu yalisimama kwenye picha moja tuu, picha iliyobeba majibu ya maswali yote aliyokuwa nayo kuhusu Mama Lutu.

Ilionyesha sura mbili za vijana. Msichana mrefu, mweusi, mwenye macho ya kujiamini lakini uso wa upole wa kisomi. Alikuwa ni Mama Lutu au kwa jina lake la awali, Rosemary Lutulia, akiwa kijana wa miaka kama ishirini na tatu. Pembeni yake alikuwa kijana mwingine, mwenye tabasamu jembamba, shati la mistari, mikono yake ikiwa imemkumbatia Rosemary. Alikuwa ni Benedicto Mlauzi, aliyefariki siku chache zilizopita.

Kinu alishtuka. Aliikamata picha kwa mikono miwili akawa anaiangalia macho yake yakiwa yametekewa. Dunia ilijitanda kwenye moyo wake. Ndipo akatambua, Mama Lutu na Benedicto walikuwa zaidi ya washirika wa zamani. Walikuwa wapenzi. Na zaidi ya hapo, waliwahi kuwa kitu kimoja kabla DEKA haijawapokonya kila kitu.

Sasa alianza kuelewa. Mama Lutu hakurudi kwa sababu tu ya dhamira. Alirudi kwa sababu aliuawa mtu aliyebeba sehemu ya roho yake, mtu ambaye pengine bado alimhifadhi ndani ya vichochoro vya moyo wake vilivyofungwa kwa miaka mingi. Mapenzi yaliyogeuzwa kuwa kiapo cha ukimya. Na sasa, kimya hicho kilikuwa kinapigana kutoka kaburini.

Kinu akafungua karatasi nyingine iliyokuwa karibu na picha. Ilikuwa barua, iliandikwa kwa mkono, kwenye karatasi ya iliyopoteza rangi yake, ilikuwa ya zamani, ya barua pepe.
---

"Rosemary,
Sijui kama barua hii itakufikia, au kama utawahi kuwa na muda wa kuisoma. Niliandika kwa sababu nilijua siku moja, mfumo huu tutakaojenga utatumeza sisi sote.
Siku zote nilijua DEKA sio mwisho, bali mwanzo wa kaburi letu. Tulijaribu kuwaweka salama watoto wa taifa hili, lakini tukageuka kuwa kuta za nyasi ambazo, cheche moja tuu. Moja tuu! Ingetosha kuteketeza maisha yetu.
Niliwaamini wenzetu, lakini walitusaliti. Walinunuliwa. Tulifungwa. Tukasahauliwa.
Lakini kuna kitu kimoja nilikiweka mahali salama, DIRA KUU.
Faili hilo halipo katika maktaba hii moja kwa moja, bali nililificha nyuma ya kabati la vitabu vilivyohamishwa kutoka jumba la zamani la Wazungu, kabati lililowekwa namba ‘IV-X’.
Nimeacha alama ya X kwenye kona ya juu ya mlango wake wa kioo.
Ukikuta faili hilo, ulifikishe pale palipo haki.
Na kama umeweza kusoma hii barua, basi upo katika nafasi nzuri ya ukombozi.
Usinisamehe kwa kuwa muoga. Nisahau kama mpenzi wako wa zamani.
Nikumbuke kama mtu aliyebeba sehemu ya aibu ya taifa hili.
– B"*
---

Barua hiyo ilimsimamisha Kinu kwa sekunde. Akaweka picha na barua ndani ya koti lake. Hakuwa na muda wa kuendelea kushangaa. Aliinuka haraka, akaanza kuangaza kila kabati kwenye kile chumba.

Akaona kabati moja kubwa la mbao lililoonekana kuwa halina umuhimu, likiwa na vitabu vingi vya zamani vya historia ya wakoloni, baadhi vikiwa vimeandikwa Kijerumani. Aliangaza juu ya kona ya mlango wa kioo wa kabati na hapo palikuwa na alama ya X ndogo, iliyoandikwa kwa rangi ya kahawia, karibu ifanane na ukungu wa mbao.

Kinu akavuta kabati hilo taratibu kutoka ukutani. Kwa ndani kulikuwa na mfuniko wa siri, umeandikwa kwa kificho:
“03-RedX-Log”

Aliweka kifaa chake cha kudukua kwenye sehemu ya chini ya kifungo. Dakika tatu zilitosha. Mfuniko ukafunguka. Ndani yake kulikuwa na faili lenye jalada jekundu, juu likiwa na nembo ya Serikali na DEKA.

DIRA KUU – SEHEMU YA MKATABA WA KIMATAIFA WA KUASISI DEKA.

Alilifungua, macho yake yakianza kusoma kurasa za kwanza. Kulikuwa na saini za wanasiasa wa zamani kutoka nchi tatu za Ulaya—ujerumani, ufaransa, na Uingereza. Kulikuwa na jedwali la mgao wa hisa wa siri, na maelezo ya kuajiri wanasheria, majaji, wanahabari, na hata viongozi wa dini waliokuwa tayari kulamba damu kwa mikataba ya ukoloni Mamboleo.

Kinu alijua hana muda. Alijua alikuwa sasa ndani ya moyo wa joka. Na joka lilikuwa limeanza kuhisi mwiba tumboni.

Akatumia kifaa maalum kilichokuwa kwenye saa yake ya mkononi kupiga picha kila ukurasa, moja baada ya nyingine. Akaunganisha kifaa na simu ya satelaiti, akaituma data yote kwa Titus, ambaye kwa sasa alikuwa kwenye meli iliyovuka bahari ya Hindi kuelekea Durban.

Wakati huohuo, katika chumba cha usalama cha Ikulu, maafisa walikuwa wamegundua kuna vyumba vya chini visivyo kwenye ramani. Walikuwa wameona kupitia kamera moja iliyowahi kumnasa Kinu akiwa amevalia kapero na koti la kazi, sura yake ikiwa nusu imefichika.

“Si Oscar huyu. Huyu ni mtu mwingine. Anaingia sehemu ambazo hata sisi hatufahamu. Anafungua milango kwa codes ambazo hazijatumika kwa miaka.”

“Huyu mtu… si wa kawaida.”
“Sasa hivi yuko wapi?”
“Hatujui. Kamera za ghorofa ya chini ya tatu zimekatika. Lakini tunaamini bado yuko ndani. Weka Ikulu lockdown. Hakuna anayetoka wala kuingia. Weka walinzi wa ndani. Akionekana, mpige kwenye mguu, si kichwa. Tunamhitaji akiwa hair. Tunahitaji ajibu maswali.”

Waliingia hatua ya pili ya msako. Ikulu ilijifunga yenyewe kama mzoga wa nyoka uliohisi ukeketaji.
Lakini Kinu tayari alikuwa anaondoka kwenye ghorofa hiyo ya chini, akipitia njia ya pili ya dharura ambayo Mama Lutu aliwahi kuitaja kwenye barua nyingine, mlango wa nyuma wa kutokea chini ya bustani ya maua ya wakuu wa zamani karibu na fukwe za bahari.

Moyo wake ulikuwa mzito, lakini fahamu yake ilikuwa hai yenye nguvu kama risasi.

Sasa alikuwa anajua, si tu kwamba alikuwa anapambana na DEKA.
Alikuwa anapambana na kizazi cha uongo kilichoasisiwa na mikono ya mataifa makubwa, na kulindwa na wasomi wenye shahada lakini wasio na roho ya uzalendo. Watu walioungana na mataifa ya ulaya kuwanyonya watu wa nchi Yao wenyewe.

Na sasa, kwa mara ya kwanza, alikuwa na silaha ya kweli.

DIRA.
---

Mwili wa Kinu ulikuwa umejaa mvutano wa ndani. Alitembea kupitia bustani ya nyuma ya Ikulu, iliyokuwa ufukweni, kwa hatua za kijeshi zenye tahadhari, akipitia njia ya dharura aliyoifunua kutoka kwenye barua ya Benedicto. Bustani ile, ambayo mara nyingi huonekana kwenye televisheni kama mandhari ya diplomasia na mikutano ya viongozi, leo ilikuwa imevamiwa kimyakimya. Kinu alikuwa amebeba mfuko mdogo wenye picha, barua, na faili lenye uzito wa usioweza kupimwa kwenye mizani —DIRA KUU.

Alifika kwenye ukuta wa mwisho, akapanda kwa kutumia nyaya ndogo alizojitengenezea siku mbili kabla. Aliposhuka upande wa pili wa Ikulu, alihisi hewa ya bahari kutoka mbali. Mvua nyepesi ilikuwa inaanza kushuka. Giza la asubuhi lilikuwa limechanganyika na hewa ya moto ya miale jua lililokuwa linakazana kuchomoza, milio ya ndege wachache waliobaki jiji hili waliimba nyimbo za onyo.

Hakukimbia. Alitembea haraka. Dakika sitini baadaye, alikuwa kwenye pikipiki ndogo aliyokuwa ameificha karibu na kituo cha mafuta. Alivaa helmet, akawasha injini kimyakimya, na kuelekea kwenye eneo la maficho, mahali ambapo alikuwa akitegemea kuwakuta Andrew, Moreen, na Mama Lutu wakiwa salama, wakisubiri hatua inayofuata.

Lakini alipoanza kuukaribia msitu mdogo uliokuwa ukizunguka nyumba ya maficho, hewa ilibadilika. Alihisi harufu ya moshi, harufu ya risasi zilizopigwa saa chache zilizopita. Alipofika karibu, aliona mlango wa mbele wa jumba la maficho ukiwa wazi kwa huzuni kama kaburi lililoachwa likisubiri mfu wake arudi.

Kinu alishuka kwenye pikipiki, akaacha mlango wazi kama alivyoukuta, bastola ikiwa mkononi, akaingia ndani.

Ndani kulikuwa kimya kilichohifadhi sauti za maumivu ya tukio baya lililotokea. Viti vilikuwa vimeangushwa, meza kuvunjika. Kila kitu kiliparanganywa. Kuta zilichafuka kwa madoa mekundu ya damu.

Alitembea polepole hadi sebuleni, akaona mwili mmoja wa kiume, umelala kifudifudi, bastola ikiwa imeanguka pembeni. Alipomsogeza, alitambua, hakuwa wao. Hakuwa Andrew, wala Moreen. Huyo alikuwa mwanachama wa DEKA. Alikuwa mmoja wa waliovamia eneo hilo, lakini hakuwa ametoka salama. Alikuwa amekufa kwa kupigwa risasi.

Ndani ya sekunde chache, Kinu alielewa mahali hapa palishambuliwa. DEKA walikuwa wamewafikia. Kitu kigumu kichwani kilimshtua.

Mikono akaiinua juu ghafla,nyuma yake. Amri kali ikapigwa kama risasi.
“Simama! Mikono juu! Geuka taratibu, kijana!”

Aligeuka polepole, bastola akiwa ameitupa chini. Wanaume wawili walikuwa mbele yake, wakiwa wamevalia nguo za kiraia lakini bastola zao zikiwa za kijeshi. Walikuwa askari wa DEKA waliobakia nyuma kama mtego. Walijua Kinu angefika.

Mmoja akamsogelea, akampekua, akachukua faili, barua na ile picha ya Benedicto na Mama Lutu.
“Hiki ndicho mlichokuwa mnatafuta? Hiki hapa, ndio kitatufanya tuwatafute kwenye ramani. ,” mmoja akasema.

Wakaanza kumpiga. Makofi mazito. Mateke tumboni. Swali likarudiwa kila baada ya kipigo:
“Ulikitoa wapi hiki? Nani anahusika? Uliyatoa wapi majina?”
Kinu alinyamaza. Kichwa chake kilikuwa kikizunguka, lakini moyo wake haukuyumba. Alijua wasingeweza kumwua kwa sababu bado walitaka kujua zaidi. Lakini muda haukuwa upande wao.

Ghafla, milio ya risasi ikasikika kutoka nje.
PAP! PAP!

WanaDEKA wale wawili walianguka haraka, kama miti iliyokatwa na tingatinga. Walianguka chini, mmoja akiwa bado na bastola mkononi, mwingine akitoa sauti ya mwisho kama mtu anayeanguka shimoni akiwa ndotoni. Kinu alijitupa pembeni, akavuta bastola yake lakini hakuhitaji kuitumia.

Mlango wa nyuma ulikuwa umefunguliwa.
Na mlango huo alimwona Mama Lutu akiwa amesimama, mkononi akiwa ameshikilia bastola yake, lakini mwili wake ulikuwa dhaifu. Alikuwa amejeruhiwa vibaya kwenye upande wa kushoto wa tumbo. Damu ilikuwa inamtoka kwa kasi. Nguo zake zililowa damu, na uso wake ulikuwa wa mshindi na shujaa ambaye anayejua hatarudi tena nyumbani.

Alianguka taratibu, bastola ikidondoka pembeni. Kinu alimkimbilia haraka, akamuegemeza kwenye mapaja yake, akajaribu kumuinua lakini mwili wa Mama Lutu ulikuwa mwepesi kama karatasi iliyokosa hewa.
“Mama Lutu… Rosemary…” Kinu alizungumza kwa sauti ya maumivu, “Ulirudi. Ulirudi kwa ajili yetu wote…”
Mama Lutu alitabasamu. Sura yake ilikuwa ya upole, hata ndani ya kifo kilichokuwa kikiingia. Akasema kwa sauti ndogo, yenye mate ya damu pembeni ya midomo yake. “Nilijua watanifuata. Lakini ilibidi nifike kabla yako…”

Akapumua kwa nguvu, akavuta hewa chungu.
“Samahani… kwa usaliti… niliukubali kwa hofu. Niliukumbatia kwa uoga. Lakini siku zote… moyo wangu haukuwahi kusahau… Haki ... Kupigania wa..wa.wanaoonewa"

Kinu alitoa picha kutoka kwenye koti lake. Akamuwekea karibu na macho.
Picha ile ya yeye akiwa na Benedicto, miaka mingi iliyopita. Mama Lutu alitazama kwa macho yaliyojaa machozi. Alionekana kama msichana wa miaka ishirini tena, akimtazama mpenzi wake aliyepotea. Akawa kimya kwa sekunde. Kisha machozi yakaanza kudondoka, polepole, yakiingia kwenye vidonda vya damu vilivyokauka. Aliikumbatia picha ile kwa mikono miwili, karibu na kifua chake kilichokuwa kinapoteza joto.
“Aliapa… ataandika ukweli… kabla hajafa…” alisema kwa sauti ya buriani. “Na mimi… nilikataa. Nilimlazimisha… tusirudi nyuma…”

Kinu alibaki kimya, macho yake yakiwa yamejaa wingu la huzuni. Alimshika kwa nguvu zaidi.
Mama Lutu alipumua kwa nguvu, akamtazama Kinu moja kwa moja.
“Mtafute… tafuta yule ambaye… ambaye…"
Alishindwa kumalizia. Kichwa chake kilianza kulegea. Kinu alisogea karibu na kifua chake. Alijaribu kumbembeleza, lakini alikuwa anaishiwa nguvu.
Ndipo sauti ya mwisho ikatoka kwa kugugumia, kwa pumzi ya mwisho, neno moja:

“Max…”
Kisha… ukimya. Mikono yake ilianguka pembeni. Picha ikaanguka chini. Macho yake yalibaki wazi, yakiangalia nafasi ambayo imepeperuka isiweze kurudi tens

Mama Lutu, jasusi wa zamani, mlinzi wa watoto, msaliti wa watu wake, mshindi wa dhahiri, alikuwa ameondoka.

---

Inaendelea

Riwaya zilizosokoni
1. Wakala wa Siri
2. Mlio wa risasi Harusini
3. Kaburi la Mwanamuziki
4. Dar es salaam protocol
5. Siku yangu ya kufa Ilipita.
6. Mtoto wa Msukule.

Kila Kimoja Tsh 15,000/=


Riwaya ambazo zitarushwa Mtandaoni!
1. Hakuna Aliye Salama
2. Nitamlea
3. The Church of the Unborn ( itaanza Leo tarehe 11/07/2025.

Tunaanza na The Church of the Unborn sasa hivi, vyuma vinashuka sio muda.

Usikubali kuhadithiwa...
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom