Robert Heriel Mtibeli
JF-Expert Member
- Mar 24, 2018
- 34,071
- 79,437
HAKUNA ALIYE SALAMA
Mtunzi: Robert Heriel
0693322300Chungu cha 01
Kinu alikuwa ameketi kwenye wheelchair, akitingisha kichwa chake kwa taratibu, udenda ukimtoka mdomoni. Macho yake yalikuwa matupu kwa nje, lakini kwa ndani yakiwa kama rada ya kijeshi. Nyuma yake alikuwa amesimama Moreen, mwanamke aliyefunga kilemba na kuvaa mavazi ya kushangaza—mchanganyiko wa Pamba iliyochanika na blauzi ya rangi ya dhahabu iliyopoteza hadhi ya urembo.
Kazi ya Moreen ilikuwa rahisi: kumzungusha Kinu maeneo ya katikati ya Jiji la Dar es Salaam kila siku, kuanzia Posta, Mnazi Mmoja, kufikia Kariakoo na Upanga. Alifanya kazi hiyo kwa moyo wote. Haikuwa kazi rasmi, wala haikuwa ajira ya kudumu—ilikuwa mpango wa muda mfupi, lakini wenye masharti magumu: Usiulize maswali. Usijue sababu. Usizungumze na mtu yeyote kuhusu kazi hii.
Kwa watu wa mitaani, Kinu hakuwa chochote zaidi ya ombaomba. Suruali yake ya kaki ilikuwa na viraka vitano, fulana yake ilikuwa imechanika kifuani na kufuliwa mara nyingi bila sabuni ya kutosha. Machoni mwao, Kinu alikuwa na utindio wa ubongo, huenda ni usonji. Lakini haikuwa hivyo. Kinu hakuwa mgonjwa. Wala hakuwahi kuumwa akili hata siku moja.
Kinu alikuwa Jasusi. Jasusi wa kiwango cha juu, aliyefanyiwa mafunzo ya hali ya juu huko Bulgaria, India na Ujerumani. Alikuwa katika kazi hatari sana, kazi ambayo ilimlazimu kujivika mwili wa maskini, akili ya mgonjwa, na maisha ya kuhurumiwa na kila mtu.
Na Moreen? Hakuwa jasusi. Wala hakuwa na historia yoyote ya kijeshi. Alikuwa msanii wa make-up maarufu ambaye ofisi yake ipo Mbezi Beach, mtaalamu wa kubadili sura za watu, ama kuwafanya waonekane kama malaika au kama mapepo. Kazi yake hapa ilikuwa moja tu: kumpaka Kinu hadi asitambulike. Au Kwa namna yoyote atakayoagizwa na Kinu, boss mpya.
Siku hiyo Moreen alikuwa amemvalisha Kinu mavazi ya ajabu—suti iliyochakaa, viatu vya plastiki visivyofanana, na kofia ya kaniki. Alihakikisha uso wake umejaa vipodozi vya kuharibu sura, akamwekea kovu bandia shavuni. Kinu alionekana kama mtu aliyepoteza kila kitu duniani.
Lakini macho ya Kinu, licha ya udenda, yalikuwa makini. Aliyaelekeza kwenye kila upande wa barabara, akihifadhi kila harakati, kila sura, kila jengo. Akili yake ilikuwa kama kamera yenye uwezo wa kuzoom, kuscan, na kuhifadhi data kimya kimya.
“Unaona yule kijana mrefu mwenye Kofia nyekundu?” Kinu aliuliza kwa sauti ya chini mithili ya mtu anayegugumia mate, huku Moreen akimsogeza karibu na barabara ya Libya, kuelekea Samora Avenue.
Moreen alimtazama yule kijana harakaharaka. “Ndio, anaonekana kama mteja wa kawaida wa mtaa.”
“Anavaa Kofia nyekundu kila Jumatatu, anasimama eneo lilelile kwa dakika 17, huondoka bila kusema na mtu yeyote,” Kinu alisema. “Hana simu, hana begi, lakini anatoka katika jengo la ‘Eagle Holdings’.”
Moreen alikenua midomo. “Na unafikiri ni nani?”
Kinu aligeuza macho yake kuelekea gari jeupe lililoegeshwa kwa umbali kidogo. Kwenye kioo cha mbele kulikuwa na stika ya shirika lisilojulikana. Ndani kulikuwa na mtu mmoja aliyevaa miwani meusi na fulana ya kijani. Kwa macho ya kawaida hakuwa wa maana. Lakini kwa Kinu, huyo alikuwa link ya kwanza kwenye mlolongo wa hatari.
“Kama nitatoweka, Moreen,” Kinu aliongea kwa sauti ya chini zaidi, “usiende nyumbani. Rudi kwa mama yako Mtwara. Usimwambie mtu chochote. Wala usijaribu kunitafuta.”
Moreen alitetemeka. Hakuwa jasusi, lakini tangu aanze kusaidia kazi hii ya ‘kuigiza’ na Kinu, alishaanza kuhisi joto la dunia ya watu wa vitengo vya siri. Na sasa alihisi kuwa hakuwa tena msanii wa vipodozi tu—amekuwa sehemu ya jambo kubwa, zito, na hatari.
“Lakini…” alisema kwa sauti ya kupasua ukimya, “mbona kila mtu anayetuzunguka huwa hacheki? Kama vile wanajua kitu.”
Kinu alimtazama kwa jicho la upande, akavuta pumzi, kisha akasema kwa sauti ya kitetemeshi;
“Kwa sababu wanajua. Na ndio maana nakuambia, Moreen… Hakuna Aliye Salama.”
/
Moreen alikumbuka siku ya kwanza alipokutana na Kinu.
Ilikuwa jioni ya Jumamosi, studio yake Mbezi Beach ilipokuwa imejaa wateja wa harusi. Mwanamke mmoja aliyekuwa na vipodozi vya dhahabu usoni alikuwa anapigwa picha za harusi, wakati mwingine aliyetoka China alikuwa anafanyiwa “skin blend” kwa uso.
Ndipo mlango ulipofunguliwa kwa taratibu. Mtu mmoja mrefu aliingia akiwa amevaa koti refu jeupe, kofia ya mchirizi na miwani meusi. Alikuwa mgeni wa aina yake. Hakuonekana mwenye haraka, hakuwa na sura ya mtu wa harusi, lakini macho yake yaliongea zaidi ya mdomo.
“Wewe ndiye Moreen?” aliuliza kwa sauti ya chini yenye ukakamavu.
“Ndio,” Moreen alijibu kwa mashaka, “unataka huduma gani?”
“Huduma tofauti. Si make-up ya picha, si ya harusi. Tafadhali. Dakika mbili nje tuzungumze"
Moreen hakubisha, aliaga wateja wake kisha akatoka nje.
"Nataka unitengeneze uso wangu kila siku… ili nisiwe mimi. Na pia nikupe kazi nyingine ya ziada, kuniendesha mtaani kwenye wheelchair. Kazi ya siku 21 tu. Nitalipa pesa nzuri.”
Moreen alicheka kwa kejeli. “Hiyo ni kazi ya maigizo?”
“Hapana,” yule mgeni alisema kwa sauti ya kutisha kidogo. “Ni kazi ya maisha na kifo. Sitaki ajue mtu mwingine. Sitaki picha. Sitaki maswali. Sitaki urafiki. Nataka uigize kuwa dada yangu au msaidizi wangu. Kila siku utapewa shilingi laki moja taslimu—kwa siku. Bila kuchelewa.”
Moreen alinyamaza. Shilingi laki moja kwa siku? Alipiga hesabu za haraka, kwa wiki tatu, maana yake alikuwa anaenda kupata milioni mbili na laki moja. Kiasi hicho hakijawahi kupita mkononi mwake kwa kazi ya mteja mmoja. Hakuwa mjinga wa kukataa pesa, lakini hakuwa pia mjinga wa kukubali bila tahadhari.
“Nataka kujua kama hii ni haramu. Kama ni biashara ya dawa za kulevya au silaha, sitaki kujihusisha,” alisema kwa msimamo.
“Hii ni kazi ya nchi. Lakini hutaambiwa mengi. Ukiuliza sana, nitatafuta mwingine"
Kwa moyo wa nusu nusu, sitaki nataka, Moreen alikubali. Lakini alijua, kazi hii ingegharimu taswira yake ya hadharani. Aliamua kuchukua hatua ya kwanza: kubadili uhusika wake kabisa.
Alienda kwenye duka moja la mitumba kule Mwenge, akanunua nguo za kawaida kabisa, alinunua blauzi zisizo na nembo, viatu vya plastiki vya Tanga. Alijifunza kutembea polepole, kumenyeka na kuongea kwa lafudhi ya mtaani. Kila alipokuwa karibu na jiji, alijifunga kilemba kikubwa na kuvaa miwani meusi. Hakutaka hata mmoja wa wateja wake wa mjini amtambue. Alijua mtu mmoja akimtambua, maneno yangetapakaa Instagram na TikTok kama moto wa nyika.
Kazi ilianza.
Kila siku asubuhi, kabla ya saa mbili, Moreen alikuwa anafika eneo la Kivukoni, akimkuta Kinu tayari keshajipaka udenda bandia, suruali yake ikiwa imepiga magoti, na uso wake ukionekana kama wa mtu aliyevurugikiwa akili. Kazi yake ilikuwa moja tu: kumsukuma, kumpeleka mitaani, na kuhakikisha anaonekana kama mtu wa kupuuzwa.
Moreen alizoea kazi hiyo haraka kuliko alivyotarajia. Lakini kila siku, alipomtazama Kinu, alihisi kama kuna kitu kingine ndani yake, nguvu isiyoelezeka, siri nzito ambayo haijafunuliwa, na hatari inayomnyemelea… hata yeye mwenyewe.
Na ndani ya moyo wake, Moreen alianza kuhisi kitu ambacho hakukitazamia: hofu ya kumpoteza mtu ambaye hakumjua vizuri, lakini alimwamini ajabu.
Na kwa mbali, ndani ya kivuli cha jiji, jua lkiwa limemaliza nusu ya anga kuisaka nusu nyingine, macho ya adui yalimtazama Kinu. Walijua anajua. Walijua anatambua. Na kwao, kulikuwa na amri moja tu:
/“Mwondoe kabla hajafika mbali.”
Jua lilikuwa kali kiasi cha kuunguza nywele zilizofichwa ndani ya kilemba. Moreen alikuwa amechoka. Siku hiyo walikuwa wamepitia maeneo ya Kisutu na sasa walielekea kwenye mtaa wa India Street, karibu na jengo la zamani la usalama wa taifa.
Kinu alikuwa kimya. Alikuwa kama sanamu. Lakini macho yake yalikuwa bize yanafuatilia kila mtu, kila mwendo, kila mlango unaofunguliwa na kufungwa kwa kasi isiyo ya kawaida.
Moreen alikosea njia kwa sekunde chache tu, akasogelea kona ya jengo la ‘Shanaz Towers’ badala ya kupita nyuma ya Askari Monument kama walivyozoea. Ilikuwa ni kosa dogo lakini kwa Kinu, kosa la aina hiyo lilitosha kuamsha tahadhari ya hali ya juu.
“Geuka nyuma,” aliongea kwa sauti ya chini sana, kama mtu aliyekonda kupita kiasi. “Haraka. Sema unataka ice cream pale barazani.”
Moreen alishangaa lakini hakupinga. Aligeuza wheelchair taratibu, kisha akasema kwa sauti ya kuigiza kama mtoto anayeng’ang’ania pipi, “Ngoja twende pale nipate barafu kidogo, jua kali bwana!”
Wakageuka.
Sekunde chache baadaye, gari aina ya Toyota Alphard nyeusi ilipita kwa kasi isiyo ya kawaida, ikapunguza mwendo mbele yao kisha ikasogea hadi kusimama upande wa pili wa barabara. Mwanaume mmoja wa miraba minne alishuka, akavaa miwani meusi na kujifanya kupokea simu, lakini macho yake yote yalikuwa kwao.
“Yule mwanaume… ni wa tatu leo,” Kinu aling’amua. “Wanajaribu kuthibitisha kitu.”
“Wananiangalia mimi au wewe?” Moreen aliuliza huku akizidi kuvuta kitenge chake kujificha zaidi.
“Wote wawili. Ila tatizo ni kwamba… sasa wameanza kuamini kuwa mimi siyo kichaa.”
Kabla Moreen hajajibu, simu ya Kinu—ile aliyokuwa ameificha chini ya blanketi la wheelchair—ilitoa vibrate moja ya haraka. Aliichukua kwa ustadi, akasoma ujumbe mmoja tu:
“DEKA-6 IMESHUKA DSM. KATIKA SAA 48, WATAJUA UPO HAI. TOKA ENEO LA KATI MARA MOJA.”
— Kituo-M
Macho ya Kinu yalibadilika ghafla. Aligeuza uso wake kama mtu asiyeelewa chochote, akakumbatiana na udenda wake kama kawaida. Lakini ndani ya akili yake, alishajua: sasa wanamfuatilia rasmi. Na Deka-6, kundi la wauaji wa kimyakimya ambalo lipo ndani ya nchi. Lakini halijulikani, halipo kisheria lakini lilikuwa na nguvu kuliko sheria.
Hawakuwahi kushindwa kazi waliyopewa.
“Moreen,” alisema taratibu. “Leo tunabadilisha mpango. Hatuendi tena Mtaa wa Azikiwe. Tutapitia uchochoro wa India Street, tutapotelea Gerezani. Kuna mtu nitakutana naye huko kwa dakika tatu. Ukiona mtu yeyote anapiga picha, usikubali, nipiganie kama ndugu yako. Ukiona mtu anatoa simu, zibua makelele. Usidharau mtu yeyote.”
Moreen alitaka kuuliza maswali, lakini alijizuia. Alimwelewa Kinu sasa: kila neno lake huwa lina maana zaidi ya linavyoonekana. Kila maelekezo yalikuwa kama kamba ya kuokoa maisha.
Na alipoanza kumsukuma kuelekea kwenye mtaa wa pembeni, walipishana na mwanamke mmoja aliyekuwa amebeba daftari na glasi ya kahawa. Alipowaona, mwanamke huyo alicheka kidogo kisha akawasha Bluetooth earphone yake.
Hakuna kilichoonekana cha ajabu.
Lakini Kinu alisema taratibu:
Moreen alijibu taratibu kwa sauti iliyotikiswa na hofu:“Huyo mwanamke si mpita njia. Hii vita ina sura nyingi. Na kumbuka nilivyokwambia, Moreen…”
/“Hakuna Aliye Salama…”
Mtaa wa Gerezani ulikuwa kama kawaida — kelele za wasafirishaji, vibaka waliogeuka wajasiriamali, wanawake waliouza chai kwa vikombe vya plastiki, na wauzaji wa vyakula waliopika kwenye ndoo za rangi ya bluu.
Hakuna mtu aliyekuwa anajua kuwa kati ya machinga hao, waliokuwa wakiuza miwani, soksi na vocha za mitandao, kulikuwa na wawili waliotumwa rasmi na Kituo-M, shirika la siri linalopambana na Deka-6 kimyakimya kwa kutumia jasusi wachache waliobaki waaminifu. Kinu alikuwa mmoja wao aliyebaki huru.
“Simamisha hapa,” Kinu alimwambia Moreen. “Mimi nitashuka. Nivute kidogo blanketi la miguuni, kisha geuza uso wako upande mwingine. Usimuangalie mtu. Usisikilize sauti yoyote itakayoita jina lako.”
Moreen alihisi moyo wake ukidunda kwa kasi. “Una uhakika ni salama?”
“Salama haipo. Lakini nina dakika tatu tu. Nikiwa na zaidi ya hizo, najua wamejua nilipo.”
Akatupa blanketi upande wa kushoto, akajigeuza taratibu kama mtu mwenye kupooza viungo vyote. Alishuka kwa msaada wa mikono yake tu, akasogea polepole kama mzigo wa mateso, hadi akajificha kwenye kivuli cha duka la vifaa vya elektroniki lililokuwa limefungwa.
Macho yake yaliangaza upande wa kushoto. Mwanaume mmoja mwenye t-shirt ya Free Palestine alisimama karibu na begi la plastiki. Kinu alimtambua. Alikuwa Mcharo — jasusi wa zamani, aliyefukuzwa kazini kwa kosa la kuvujisha siri, lakini aliendelea kusaidia nchi kwa kificho.
Kinu alipofika karibu, Mcharo hakumwangalia moja kwa moja. Alizungumza bila kumtazama.
“Wako karibu. Unapoteza muda kwa kila sekunde unayobaki hapa.”
“Unajua nani ananifuata?” Kinu aliuliza.
“Sitaki kujua majina. Nasikia tu minong’ono. Watu waliowekwa juu ya mfumo. Nje ya sheria. Nje ya uhalali. Wanaitwa Deka-6. Lakini hakuna anayejua walipoanzia. Hakuna anayefahamu sura zao. Hata vifo vyao huandikwa kama ajali za kawaida au kupotea ghafla.”
Kinu alipumua polepole. “Nahitaji majina mawili. Moja liwe wa mtu anayepeleka taarifa zao serikalini. La pili, mtu aliyeko karibu yangu. Ambaye naweza kuwa nimemwamini vibaya.”
Mcharo alimpa bahasha ndogo ya plastiki, ndani yake kulikuwa na picha moja ya mtu , alikuwa mwanaume wa makamo, mweupe kiasi, uso wa kirafiki, aliyevaa suti ya kawaida. Hakukuwa na jina, lakini picha hiyo ilikuwa kama bomu kichwani mwa Kinu.
Alitazama kwa sekunde tano tu. Kisha akaificha mfukoni.
“Ni yeye?” Kinu aliuliza kwa sauti ya chini.
“Ndio. Na hajui kuwa tayari tumemwona. Lakini yuko na wewe mara kwa mara. Anauliza sana. Anaonekana kupenda kujua unatembea wapi. Uwe makini. Ana macho mawili tu, lakini macho mengine yako kwenye simu yake.”
“Na yule wa pili?”
“Bahasha ya pili iko ofisini kwangu. Ila siwezi kuifikia tena. Jana usiku niliona watu watatu wamekaa kwenye gari jeupe nje ya mtaa wangu kwa saa mbili. Wala hawakushuka. Watakuwa wameniweka kwenye rada pia"
Kinu alikataa kuonyesha hofu. “Ina maana sasa wameingia hata kwenye familia za watu waliostaafu?”
Mcharo alitabasamu kwa uchungu. “Hakuna aliyestaafu kwa hawa watu. Ukijua jambo moja, tayari wewe si salama. Ukijua mambo mawili , basi umeshahukumiwa kifo. Unachongoja ni siku tu ya utekelezaji.”
Kinu alitaka kuuliza zaidi, lakini akasikia tone la kengele kwenye sikio lake la kushoto. Saa yake ya ndani ilikuwa imetimia , dakika tatu zilikuwa zimepita.
Akaanza kurudi taratibu.
Moreen bado alikuwa amegeuza uso wake. Hakumwangalia. Hakumsalimia. Alikuwa mtiifu kwa kiwango kisichoelezeka.
Lakini alipompandisha Kinu tena kwenye wheelchair, Moreen alisema kwa sauti ya kuongea mwenyewe na upepo;
“Watu wawili walipita hapa. Wote walikuwa na glovu nyeusi. Mmoja aliinua simu, mwingine akatoa sigara bila kuitia mdomoni. Walikuwa wakikuangalia.”
Kinu alijua kilichomaanishwa.
Glovu nyeusi, alama ya wajumbe wa Deka-6. Hawajifichi. Hawana haraka. Wanakufuata hadi uanze kuwa na wasiwasi mwenyewe.
“Leo,” Kinu alisema kwa sauti ya polepole, “tutarudi kwa njia ndefu. Tutapotea kwenye mitaa ya Mchikichini, halafu tutaunganisha hadi Mbagala kwa bajaji. Usilalamike. Usiongee.”
Moreen alimuangalia kwa jicho la mashaka. “Una uhakika tutakuwa salama?”
Kinu alijibu baada ya sekunde chache:
“Hata sielewi tena kama tutakuwa salama. Maana sasa naanza kuamini… hata sisi wenyewe… huenda tumeshatekwa kiakili.”
Wakaondoka.
Mbali kidogo, juu ya jengo la ghorofa moja, kamera ya usalama ya kibinafsi iliwafuata hatua kwa hatua. Mtu mmoja aliyekuwa kwenye chumba cha kuangalia ‘live footage’ alibonyeza kitufe kimoja. Kisha akatuma ujumbe mfupi kwa anwani iliyosajiliwa kwa jina bandia.
Ujumbe ulisomeka:
"Mzee Ameridhia. Muda umeiva. Mchakato uanze kesho. Moreen awe wa kwanza."
Itaendelea..