Simulizi: Utajiri Wa Damu

Simulizi: Utajiri Wa Damu

Sehemu ya 19

Maggie aliishi kwa hofu tele, kila siku kichwa chake kiliendelea kumfikiria Andrea na kuamini kuna siku mwanaume huyo angekuja kumuharibia na hivyo kukosa mabilioni aliyokuwa akiyafikiria.

Moyo wake uliwaza kabisa kummaliza, hakutaka kuona akiishia kupata aibu na wakati alikuwa na uwezo mkubwa wa kubadilisha mambo, yaani kama yalikuwa hivi, sasa aliyapeleka na kuwa vile.

Siku ziliendelea kukatika, akili yake ilifikiria zaidi harusi ambayo aliambiwa angefunga na Gosling, alimuonyesha mapenzi ya dhati huku kila siku akimwambia katika maisha yake hakukuwa na mwanaume aliyekuwa na nguvu moyoni kama alivyokuwa yeye.

Hilo likamfanya Gosling kumwamini kwani kile alichokizungumza ndicho alichokuwa akifanyiwa na msichana huyo aliyejua kupenda, msichana ambaye aliweza kuubadilisha moyo wake na kuingia kwenye mapenzi mazito na wakati hakuwa akitamani hata siku moja.

“Yaani harusi ambayo tutafunga, nitataka ibaki vichwani mwa watu, yaani izungumziwe kila kona,” alisema Gosling huku akimwangalia Maggie.
“Kweli?”
“Niamini!”

Hilo ndilo alilolifikiria Gosling, alikuwa kijana mdogo ambaye alipambana sana mpaka kupata utajiri mkubwa, aliamini ili kumuonyeshea mwanamke unampenda sana ilikuwa ni lazima kumfanyia mambo makubwa ambayo yangekaa kichwani mwake maisha yake yote.

Baada ya kukaa wiki kadhaa akamwambia mchumba wake huyo achague sehemu ambayo angependa sana waende kutembea, iwe kwenye mbuga ya wanyama au sehemu yoyote ambayo angependa waende pamoja.
Msichana huyo hakuwa na pupa ya kuchagua, alihitaji muda na hivyo kuchukua simu yake na kuanza kuangalia mbuga za wanyama.

Macho yake yakatua katika mbuga kubwa ya wanyama ya Serengeti na Ngorongoro ambazo zilimfanya kusisimka na kumwambia Gosling alihitaji kwenda huko kwani moyo wake ungejisikia furaha kama angekwenda kuwaona wanyama.

“Hakuna tatizo,” alisema Gosling.
Alichojali ni kumuona Maggie akiwa na furaha tu, akajipanga na kuwaambia walinzi wake walitakiwa kujiandaa na safari ya kuelekea nchini Tanzania kutalii hivyo walitakiwa kufuatilia vibali vyote vya safari.
 
Sehemu ya 20

Hilo likafanyika na baada ya siku tatu wakawa na kila kitu mikononi mwao na hivyo marubani kuandaliwa tayari kwa kupaa kuelekea nchini Tanzania kwenda kutazama wanyama.

Ilikuwa ni safari nzuri, wakati wakiwa kwenye ndege binafsi, muda wote Maggie alikuwa pembeni ya mchumba wake huyo, alijisikia faraja, amani kupita kawaida na muda mwingi walikuwa wakibusiana kiasi kwamba hata kama ingekuwa siku yako ya kwanza kuwaona watu hao isingekuwa kazi kubwa kugundua kama walikuwa wapenzi waliopendana na kushibana.

Safari iliendelea huku wakiendelea kufanya mambo yao mengi ya kimahaba ndani ya ndege. Baada ya saa thelathini, ndege ikatua katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere ambapo walipumzika kwa saa moja na kupaa kuelekea Arusha.

Safari hiyo iliwachukua saa moja na nusu, wakatua katika Uwanja wa Ndege wa KIA ambapo hapo walipumzika na kupaa tena kuelekea katika Mbuga ya Wanyama ya Serengeti ambapo kulikuwa na uwanja mdogo wa ndege.

Baada ya dakika kadhaa, wakafika na kuelekea katika hoteli nzuri na ya kifahari iliyojengwa humo mbugani na kupumzika. Siku hiyo ilikuwa ni ya kuendelea kuyafurahia maisha yao ya uchumba, chumbani walipokuwemo walikuwa wakishikana hapa na pale, walicheza muziki wa bluzi na kisha kulala, kwa kifupi walifanya kila kitu kilichotakiwa kufanywa na wapenzi wawapo faragha.
 
Sehemu ya 21

Siku iliyofuata ilikuwa ni ya kutembea katika mbuga hiyo wakipiga picha vya kutosha na kuwaangalia wanyama. Ilikuwa ni safari ya kawaida lakini kila mmoja alionekana kufurahia safari hiyo.

Baada ya kukaa hapo kwa siku mbili, wakaambiwa kuhusu Mbuga ya Wanyama ya Ngorongoro, hawakutaka kusubiri, iliwavutia na hivyo kupanga safari ya kuelekea huko kwa gari maalumu la mbugani.

Safari haikuchosha, kila mtu aliifurahia na baada ya muda fulani, wakafika huko na kuendelea kukatalii kama kawaida.

“Kwa saa hivi hakuna wanyama wengi sana, twendeni tukapumzike halafu baadaye turudi,” alisema mwanaume aliyekuwa na kazi ya kuwatembeza, wakakubaliana naye na kwenda kuchukua chumba katika hoteli iliyokuwa hapo Ngorongoro.

Walikaa humo kwa saa tatu ndipo wakatoka, wakachukuliwa na kupelekwa katika gari jingine pamoja na watu wengine, wakaingia ndani na kutulia katika kiti cha pamoja wao wawili huku walinzi wao wakiwa wameambatana nao.

Wakati gari likitaka kuondoka, sauti ya msichana mmoja ikasikika ikimtaka dereva kutokuondoka, akafanya hivyo, msichana huyo akaanza kupiga hatua huku akikimbia, alipolifikia, akaingia ndani.

Kila mtu aliyemuona aliguna, alikuwa msichana mrefu, mweusi, aliyekuwa na figa namba nane iliyojichora vilivyo, kichwani alikuwa na nywele za wastani huku akiwa ametoboa pua na kuvaa kisketi kilichoyaacha mapaja yake wazi.

Alipendeza, sketi ile laini aliyoivaa iliifanya hata nguo yake ya ndani kuonekana kitu kilichomtamanisha kila mwanaume aliyemwangalia.

Kifuani hakuvaa kitu chochote kile, kilikuwa kimesimama kana kwamba ncha za misumali, kwa juu alivalia fulana ndogo ya kike ambayo iliifanya hata shanga aliyoivaa kiunoni kuonekana wazi, msichana huyo alikuwa Catherine.
|
|
|

Je, nini kitaendelea?
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom