SIHUSIKI - 14
Kitu kizuri ni kwamba mfadhili wa asasi yao ya kiraia alikuwa ameshatoa fedha za kutosha kwa ajili ya masuala ya aina hiyo na hakukuwa na sababu yoyote ambayo ingekwamisha taasisi yao kushindwa kufuatilia. Baada ya kusoma magazeti yote mawili, alichukua daftari lake dogo na kuanza kuandika mambo muhimu kuhusu sakata hilo.
Aliandika jina la msichana aliyeuawa kwa sumu, umri wake, klabu aliyokuwa akifanya kazi, sumu inayodaiwa kumuua ambayo kwa mujibu wa habari alizosoma ilionekana pia kwenye chupa ya bia iliyokutwa chumbani alimokuwa na jina la nyumba ya kulala wageni alimofia.
Alichukua pia majina ya watu ambao wanaweza kuwa mashahidi muhimu katika kesi hiyo ambao ni pamoja na mlinzi katika nyumba ya wageni alimofia Agnes, mhudumu wa mapokezi, rafiki aliyekuwa akiishi na marehemu pamoja na meneja wa klabu ya Tanga Raha.
Maswali ambayo yalitakiwa kujibiwa ni nani alifanya uhalifu huo na sababu za kufanya hivyo. Ingawa sababu zilikuwa hazijatajwa lakini kutokana na uzoefu wake, kwa asilimia zaidi ya 70 alihisi zitakuwa zinatokana na masuala ya mapenzi.
Alihisi kwamba huenda mwanaume aliyekuwa na baamedi huyo ni mpenzi wake wa siku nyingi na huenda alitaka kumbinafsisha lakini msichana huyo mrembo ambaye picha yake ilikuwa kwenye gazeti akawa mgumu kukubaliana naye. Alihisi pia kwamba huenda mwanaume aliyemuua ndiye alizaa naye mtoto wake wa kwanza na pengine alitaka warejeane lakini msichana huyo akawa hataki.
“Kama waandishi hawa wangekuwa makini wangelimtafuta huyu baba wa mtoto wake au pengine wanamtafuta. Anaweza kuwasaidia,” alijisemea.
Ofisi yao ilikuwa pia imewahi kushughulikia matukio ya akina dada kuuawa na watu waliozaa nao au wapenzi wao wa zamani waliokuwa wanalazimisha kuwaoa au kuwamiliki tena bila mafanikio na ndio maana akapata hisia hizo.
Lakini pia miongoni mwa kesi walizowahi kuzifuatilia ni za mtu mmoja ambaye alikuwa akichukizwa na uwepo wa machangudoa mitaani. Mtu huyo akadhamiria kuwamaliza kwa kuwaua ambapo alikuwa anawachukua kama mteja na kwenda nao kwenye nyumba za kulala wageni ambako aliwaua kwa kuwanyonga, wengine kwa sumu na wengine kuwachoma visu kutegemea na mazingira. Mtu huyo kila alipokuwa akiua aliacha ujumbe usemao ‘Makahaba mjiandae’. Hata hivyo, mtu huyo aliwekewa mtego na kukamatwa akijiandaa kuua msichana wa saba.
Jambo moja lililokuwa limemtia faraja Salome katika gazeti la siku hiyo ni kauli ya Mkuu wa Jeshi la Polisi mkoani Tanga kwamba jeshi lake linakaribia kabisa kumnasa muuaji. Lakini pia alihisi hayo yanaweza kuwa maneno tu ya kuwatia moyo wasomaji na wananchi ili walione jeshi kwamba liko kazini na siku ipite!
Baada ya kuandika mambo muhimu kuhusu kesi hiyo, Salome alinyanyuka kuelekea ofisini kwa bosi wake, Dk. Jumanne Marijani. Huyu udaktari wake haukuwa wa uzamivu (PhD) bali udaktari bingwa wa tiba za binadamu, hususani magonjwa ya akina mama.
Alimkuta pia akisoma gazeti na Salome alihisi bila shaka atakuwa anasoma habari hiyo hiyo ya baamedi wa Tanga Raha Club. Kutokana na shughuli zao zilizojielekeza katika mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia wanaofanyiwa akina mama na watoto, kila aliyekuwa akishika gazeti anaanza kwanza kutafuta habari za aina hiyo kabla hata ya kusoma habari inayoongoza kwa siku hiyo.
“Bosi, bila shaka unasoma habari ya mauaji ya msichana wa Tanga,” aliuliza Salome baada ya kumjulia hali bosi wake ambaye walikuwa hawajakutana asubuhi hiyo.
“Ndio. Salome, inasikitisha sana. Ninaifuatilia tangu Jumamosi nilipoiona ikitangazwa kwenye vyombo vya habari,” alijibu Dk. Marijani.
“Kilichonileta ni habari hiyo hiyo. Jana nilitingwa na shughuli nikasahau kuizungumzia. Ninataka tuifuatilie kwa karibu na huyu mtuhumiwa atakapokamatwa tuongeze nguvu za kisheria. Ninataka ikiwezekana hii iwe kesi yangu ya kwanza kusimama mahakamani kama wakili wa marehemu na kwa mantiki hiyo kusaidiana na Serikali ili kukomesha haya mauaji. Ninataka huyu mwanaume aliyefanya haya tumshikishe adabu,” alisema Salome aliyekuwa akiongea kwa hisia kali akijitahidi kuzuia machozi.
“Bila shaka Mama Malima. Hata wakati ninasoma hii habari nilikuwa ninafikiria wapi sisi tunaweza kuingilia ili kutoa mchango wetu katika kukomesha mauaji ya wasichana wasio na hatia,” alisema.
“Ninashukuru bosi kwa hilo. Kwa hiyo mimi ninaanza kufuatilia. Nataka kuwasiliana na Kamanda wa Polisi wa Tanga kujua maendeleo ya hii kesi na kisha nimweleze nia yetu ya kulisaidia Jeshi la Polisi.”
“Utaniandalia tu mpango kazi wako na bajeti. Kama utataka kusafiri kwenda Tanga utaonesha kwenye mpango kazi wako. Lakini nadhani mpango mzima utaanza baada ya mtuhumiwa kukamatwa na hapa nimeona askari wakijigamba kwamba wanakaribia kumkamata.”
“Ndio Bosi. Ndio maana nimesema nataka kuwasiliana na polisi Tanga.”
“Ninakutakia kila heri Mama Malima. Kama kesi hii utaisimamia vyema hadi mwisho kwa kushirikiana na mawakili wa Serikali na mhusika kupewa adhabu anayostahili, wafadhili wetu watafurahi sana. Usisahau kuwashirikisha waandishi wa habari hasa wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake kwa kila hatua utakayochukua.”
“Sawa bosi.”
* * *
Wakati vuta nikuvute ikiendelea ndani ya kikao cha Bodi huku wajumbe wakikubali kwa shingo upande msisitizo wa mwenyekiti kwamba mtu atakayevaa viatu vya Matakwali ni Jackson Malima, karani wa Matakwali aliingia kwenye chumba cha mkutano ghafla na kumfuata mezani alikokuwa amekaa bosi wake.
Alipofika akamnong’oneza kwamba Jackson alikuwa amekamatwa muda ule na polisi. “Wameshuka naye sasa hivi na pengine watakuwa getini,” alisema karani yule.
“Inakuwaje mtu anakuja kukamatwa hapa ofisini bila mimi kutaarifiwa?” Alihoji kwa hamaki Matakwali.
“Walianzia ofisini kwa bosi Mapunda. Nadhani bosi Mapunda, aliona kwa kuwa upo kwenye kikao kizito ndio akaamuru waendelee na kazi yao. Ndiye pia kanituma nikuletee huu ujumbe,” alijibu yule karani.
“Kama hao askari hawajaondoka naye kawaambie wanisuburi. Fanya haraka. Ondoka,” alisema Matakwali aliyeonekana kushitushwa na habari hizo. Wakati karani anaondoka, Matakwali alisimama na kuwaambia wajumbe wa bodi alichoambiwa na karani wake.
“Tafadhali mnisubiri mara moja niongee na hawa askari, ninakuja mara moja,” alisema Matakwali akinyanyuka na kutoka haraka.
Alishuka ngazi kutoka ghorofa ya tatu walikokuwa kwenye ukumbi wa mikutano kueleka chini haraka na kukuta askari wale wakiomba wafunguliwe geti waondoke kwa sababu walikuwa hawana sababu ya kusubiri mtu huku karani aliyetumwa na Matakwali akiwaambia askari wa getini wasifungue kwanza hadi Mkurugenzi afike.
Matakwali alipofika alikwenda hadi kwenye gari lao na kuwasalimia kisha akajitambulisha. “Ndugu zangu, mnafika kwa mtu, mnachukua familia yake bila kujitambulisha kwake?” Alihoji.
“Kuna bosi mmoja alishatupokea na kutupa baraka zote. Isitoshe sisi tukija kukamata mhalifu si lazima tupate ruhusa ya mtu,” alijibu mmoja wao mwenye cheo cha sajini.
“Haya niambieni, mmemkamata ofisa wangu mwandamizi kwa kosa gani?”
“Mtuhimiwa anajua lakini kwa faida yako ni kwamba kaua baamedi aliyekuwa naye gesti kule Tanga Ijumaa iliyopita.”
Usikose kufuatilia mkasa huu wa kusikitisha...