mawili ya watu. Wakatoka watoto wake wawili, ni mabinti wenye miaka kama kumi na nane na ishirini na mbili hivi.
“Hujambo kijana?” yule mama alinisalimia kwa furaha.
“Sijambo mama, shikamoo.”
“Marhaba.” Kisha akawaambia kitu wale watoto wake nao wakanikazia macho.
“Mama umewaona majirani zangu hapa?”
“Majirani zako akina nani?”
“Wapangaji wenzangu.”
“Kijana, kua uyaone ya dunia. We si umeshakua, utayaona ya dunia.”
Kauli hiyo iliniogopesha sana, nikashtuka na kumuuliza mama.
“Mama una maana gani?”
“Sisi hatutaki umbeya kijana.”
“We si umeambiwa utayaona kwa hiyo subiri tu,” alidakia binti yake mkubwa.
Miguu ilitetemeka, mwili uliisha nguvu, nikajikuta nataka kukaa, lakini sikuweza. Nilichoamua ni kuondoka huku nampigia simu yule dalali.
“Vipi hujambo bwana?”
“Mimi sijambo.”
“Za makazi mapya.”
“Si nzuri bwana.”
“Kwa nini tena?”
“Sielewielewi.”
“Kivipi?”
“Kuna mambo kama si ya kawaida.”
“Yapi hayo?”
“Wale wapangaji wenzangu siwaelewi kabisa.”
“Kivipi?”
“Ah! Watu gani mimi mgeni nimehamia washindwe kutoka kunisalimia ili angalau tufahamiane?”
Dalali alicheka sana kisha akasema:
“Wale ndivyo walivyo bwana, si unajua tena malezi, mwingine kalelewa vile, mwingine hivi. Ila ulichokisema ni kweli, haiwezekani nyumba mnayoishi mpate mgeni halafu msitambuane, sasa mkikutana njiani je?”
“Si ndiyo hapo sasa,” nilisema nikijifanya lawama zangu ni kwa ajili ya hilo tu, lakini kumbe nilikuwa na zaidi ya hapo.
Kazini siku hiyo nilishinda sina amani, sina raha, mwili ulikuwa kama umetoka kufanya kazi nzito ambayo sijawahi kuifanya kwa siku nyingi, wenyeji wa Pwani wanaita mavune.
Kwa upande mwingine nilitamani sana jioni ifike ili nikaone siku hiyo kitatokea kitu gani kipya kwenye nyumba ile. Jioni ilifika, nikaondoka kazini, sikutaka kupitia popote, dukuduku langu lilikuwa kwenda nyumbani tu.
Baada ya kufika nyumbani ilikuaje? Usikose Sehemu ya Tatu