Abdallahking
JF-Expert Member
- Mar 19, 2018
- 3,985
- 10,845
SIMULIZI HII IMEKAMILIKA
IMEANDIKWA NA : NYEMO CHILONGANI
CHANZO : BURE SERIES
SEHEMU YA KWANZA
Msichana mrembo mwenye asili ya Kihindi, Nahra Patel alikuwa akilia huku akikimbia kwa kasi kuelekea sehemu kulipokuwa barabara ya lami. Jasho lilimtoka, alikuwa akihema kwa nguvu, japokuwa alionekana kuchoka lakini hakutaka kusimama.
Miguuni mwake hakuwa na viatu na alikimbia katika sehemu zilizokuwa na mibamiba, lakini Nahra hakusimama, aliendelea kusonga mbele, cha ajabu hata miba haikumchoma, na kama ilimchoma, hakusikia maumivu yoyote yale.
Machozi yalitiririka mashavuni mwake, moyo wake ulikuwa kwenye maumivu makali, hakuamini msichana mrembo kama yeye, aliyesifiwa na wanaume kwamba alikuwa mithili ya malaika, leo hii alikuwa amefukuzwa kama mbwa na mwanaume ambaye kila siku alimuona kuwa ndoto ya maisha yake.
“Deo, mimi? Hapana! Kwa nini? Nimekufanya nini?” aliuliza maswali mfululizo lakini hakupata jibu, wakati huo alikuwa akikaribia barabara ya lami.
Alipofika barabarani, akatulia chini, pembezoni kabisa mwa barabara hiyo na kuanza kulia huku akiwa amekiingiza kichwa chake katikati ya mapaja yake. Machozi yaliendelea kumtoka, kila alipokumbuka namna alivyokimbizwa na mwanaume aliyemchukulia kama mume wake wa baadaye, moyo wake ulimuuma mno.
Hakuwa na sehemu ya kwenda na wala hakuwa na fedha. Wazazi wake hawakutaka kumuona kabisa kwa sababu alikuwa amebeba mimba ya kijana mwenye ngozi nyeusi na wakati yeye alikuwa Mhindi.
Mapenzi yake ya dhati, kung’ang’ania kwake kuwa na Deo ndiyo kulimfanya leo kuwa katika hali hiyo. Hapo barabarani, alikuwa mtu wa kujuta tu, kila alipokumbuka maisha aliyopitia, alibaki akimlaani Deo.
“Ubungo buku...Ubungo buku,” ilisikika sauti ya kondakta wa daladala moja iliyokuwa ikipita mahali hapo.
Nahra akauinua uso wake na kuiangalia daladala iliyosimama mbele yake, akasimama na kuanza kuifuata, alipoifikia akaingia ndani na kuondoka.
Ndani ya daladala, kila mwanaume alikuwa akimwangalia kwa matamanio, alikuwa msichana mrembo wa Kihindi mwenye sifa zote za kuitwa Malkia Cleopatra. Kwa sababu ilikuwa ni usiku na gari halikuwa na taa ndani, hakukuwa na mtu aliyeyaona machozi yake japokuwa uzuri wake ulionekana.
“Unalia nini tena Kajool?” aliuliza mwanaume aliyekaa naye, alimuita jina la muigizaji maarufu wa kike wa filamu za Kihindi, Nahra hakujibu swali hilo, bado kilio cha kwikwi kiliendelea kusikika.
Kuanzia hapo Kibaha mpaka anaingia Dar es Salaam, alikuwa mtu wa kulia tu, kumbukumbu za maisha aliyokuwa akiishi na Deo zilijirudia kama mkanda wa filamu kitu kilichomuumiza na kumliza zaidi.
Mpaka daladala inaingia Ubungo, tayari ilikuwa saa mbili usiku, Nahra akateremka na kusimama kituoni pamoja na watu waliokuwa wakisubiri usafiri.
“Niende wapi?” alijiuliza Nahra, jibu lililokuja ni kwamba alitakiwa kwenda kwa wazazi wake waliokuwa wakiishi Masaki.
Baada ya dakika kumi, akapanda daladala iliyokuwa ikielekea Masaki na safari ya kuelekea nyumbani kwao kuanza. Kama kawaida, bado alikuwa mtu wa kulia tu, kilio chake cha kwikwi hakikuisha, baada ya dakika thelathini, akafika nje ya geti la nyumba yao, akaanza kugonga.
“Nahra, umefuata nini, baba yako ataniua,” aliuliza mlinzi aliyefungua geti, hakuamini kumuona Nahra mahali hapo tena.
“Naomba niingie, nataka kuonana na baba,” alisema Nahra.
“Hapana. Naogopa Nahra. Siku ile alitaka kunipiga risasi, siwezi kukuruhusu,” alisema mlinzi huyo huku akianza kulifunga geti hilo.
“Ninataka kuingia ndani Chichi, niache niingie nikaongee na baba yangu,” alisema Nahra huku akianza kulia tena, akaanza kulisukuma geti ili mlinzi asilifunge.
Msimamo wa mlinzi ulikuwa uleule, hakutaka kumruhusu Nahra kuingia ndani. Baada ya kulazimisha sana tena kwa kusukumana, Nahra akafanikiwa kuingia ndani ya eneo la nyumba yao. Akaanza kuufuata mlango wa kuingilia sebuleni na kuanza kuugonga.
Baada ya dakika tano, mlango ukafunguliwa na wazazi wake wote wawili kutoka ndani. Macho yao yalipotua kwa binti yao aliyekuwa akilia huku akiomba msamaha, baba yake, mzee Patel akabadilika, akakunja uso kwa hasira.
“Umefuata nini hapa? Umefuata nini wewe mbwa?” aliuliza mzee Patel huku akionekana kuwa na hasira kali, Nahra hakujibu kitu, alichokifanya mzee huyo ni kurudi ndani, kama kawaida yake alikuwa ameikumbuka bunduki yake.
Mama yake, bi Aishani alimtaka Nahra aondoke kwani alijua fika mumewe alifuata bunduki lakini Nahra hakutaka kuondoka, alikuwa tayari kupigwa risasi na kufa, ila si kuondoka nyumbani hapo.
Msimamo wa Nahra ulikuwa palepale, hakutaka kuondoka mahali hapo, alikuwa radhi kumuona baba yake akimpiga risasi na kufa lakini si kukubali kirahisi kuondoka nyumbani hapo.
Alikuwa akilia, alijiona kunyanyaswa kwa kile kilichotokea, kitendo cha kutengwa na ndugu zake kisa alikuwa na mimba ya mtu mweusi kilimuumiza mno.
Hakukuwa na mtu aliyemuelewa, hata mama yake, mtu pekee aliyekuwa akimuonyeshea mapenzi ya dhati siku za nyuma, katika suala hilo alikuwa tofauti naye.
Mlango ukafunguliwa, mzee Patel kutoka huku mkononi akiwa na gobole, alichokifanya, huku akionekana kutetemeka kwa hasira, akamnyooshea Nahra gobole lile tayari kwa kumfyatulia risasi.
“Niue tu, we niue baba, ila jua kwamba nilimpenda Deo na nisingeweza kumuacha, kama mnaona nilifanya makosa, wewe niue tu kwani hata wewe utakufa tu,” alisema Nahra, alikuwa amepiga magoti huku akilia kama mtoto.
Bila bi Aishani kulipiga gobole lile, basi risasi iliyotoka ingeweza kumpiga Nahra kifuani. Mdomo wa gobole ukaenda pembeni, risasi ikatoka na kupiga ukutani. Japokuwa mtoto wao alikuwa amefanya makosa yaliyoonekana kuwa makubwa kwa kuzaa na mtu mweusi lakini hakuwa radhi kumuona Nahra akipigwa risasi na kufa.
“Punguza jazba,” alisema bi Aishani huku akimsihi mume wake asimuue Nahra.
“Usinizuie, niache nimuue huyu malaya, ametuzalilisha sana, acha nimuue,” alisema mzee Patel huku akionekana kuwa na hasira mno.
Bado Nahra aling’ang’ania kubaki mahali hapo, hakuwa na pa kwenda usiku huo, kama walivyokuwa wazazi wake, hata ndugu zake wa Kihindi walikuwa wamemtenga, sababu ilikuwa ni ileile ya kuwa na mimba ya mwanaume mweusi.
Mbali na ndugu zake, mwanaume aliyekuwa amempa mimba, Deo alikuwa amemfukuza nyumbani kwake. Hakutaka kuondoka, kama kuuawa, alikuwa tayari kufa lakini si kuondoka nyumbani hapo.
“Chichi, mtoe huyu mbwa mara moja,” alisema mzee Patel, mlinzi akasogea Nahra na kumshika Nahra, akaanza kumbeba juujuu.
Japokuwa hakupendezwa na jambo lile lakini hakuwa na jinsi, alitekeleza amri ya bosi wake kwamba Nahra alitakiwa kutolewa ndani kinguvu.
“Niacheeee, nimesema niacheeee, nimesema sitokiiiiiiiii,” alisema Nahra huku akipiga kelele.
Hiyo wala halikusaidia, Chichi akafanikiwa kumtoa Nahra ndani ya nyumba hiyo. Kwa sababu mvua ilianza kunyesha na ardhi kuanza kulowanishwa na maji, Nahra hakujali, akakaa chini na kuendelea kulia.
Katika maisha yake yote, hicho kilikuwa kipindi kigumu kuliko vyote, hakuamini kama kweli wazazi wake walimfukuza kama mbwa kisa tu alizaa na mwanaume mweusi. Hata kama alikuwa Muhindi, akajikuta akianza kuwachukia Wahindi wote kwa kile alichokuwa amefanyiwa.
“Sitorudi tena nyumbani na sitorudi tena kwa Deo, acha niendelee na maisha yangu,” alisema Nahra na kisha kusimama, akaanza kuondoka.
Alitembea kwa mwendo wa taratibu, mvua kubwa iliendelea kunyesha na kumlowanisha mno lakini hakusimama sehemu kwani nyumba zote za Masaki zilikuwa za kifahari zilizokuwa na uzio mkubwa.
Wakati mwingine alijuta kupewa mimba na Deo kwa kuwa tu jamii yake ilimtenga lakini kuna kipindi aliona kwamba hakutakiwa kujilaumu, kile kilichokuwa kimetokea, kilitokea hivyo alitakiwa kusonga mbele.
Dakika ziliendelea kusonga mbele, mpaka anafika kituoni, tayari ilikuwa ni saa tano usiku, akakaa hapo na kuanza kusubiri daladala japokuwa mkononi hakuwa na fedha yoyote ile. Baada ya dakika thelathini, daladala ndogo (hiace) ikasimama hapo na kupanda.
Safari ya kuelekea Magomeni ikaanza, hakuwa na ndugu yeyote lakini kitu pekee alichokitaka ni kufika huko tu. Mawazo yalimtawala, hakujua ni sehemu gani alitakiwa kwenda kuishi. Huku akifikiria ni wapi alitakiwa kwenda, kichwani mwake likaja jina la mwanaume mmoja, huyu aliitwa Mithun, mwanaume wa Kihindi ambaye alimpenda lakini alimkataa kwa sababu alikuwa na Deo.
“Nitakwenda Kariakoo kwa Mithun, nitamuomba anisaide,” alijisemea Nahra.
Alipofika Magomeni, akadaiwa nauli lakini hakuwa nayo. Kondakta hakuwa mkorofi, kwa muonekano wa Nahra alionekana kuwa na matatizo, akamruhusu kuondoka, safari ya Kariakoo ikaanza huku ikiwa ni saa nne usiku.
Akaanza kutembea kwa miguu, sehemu pekee aliyokuwa akiihofia ilikuwa ni Jangwani tu. Huku akiwa amefika maeneo hayo ya hatari, mbele yake akawaona vijana wawili wakiwa wamesimama, naye akasimama, ila kabla hajafanya kitu chochote, akashtukiwa akipigwa kofi moja zito kwa nyuma.
Wakati anaugulia maumivu, akajikuta akibebwa msobemsobe na kuingizwa vichakani, wanaume wengine wanne waliokuwa na pensi walikuwa wakimsubiri huku wakionekana kuwa na tamaa ya ngono, walitaka kumbaka Nahra. Alijaribu kupiga kelele ili asaidiwe lakini hakukuwa na msaada wowote ule.
Nahra aliendelea kupiga kelele, wanaume wanne waliokuwa wamesimama mbele yake walikuwa wakihangaika kufungua bukta zao huku wakizichana nguo zake. Hakukuwa na mtu yeyote aliyesikia kelele hizo alizokuwa akipiga japokuwa zilitoka kwa sauti ya juu.
“Naanza mimi,” alisema mwanaume mmoja.
“Fastafasta, usinogewe na mtoto wa Kihindi,” alisema jamaa mwingine.
Usiku huo ulikuwa ni usiku wa kuumiza mno maishani mwake, wanaume hao wanne wakaanza kumuingilia kinguvu tena kwa zamu. Alipomaliza huyu, alikuja yule.
Nahra alisikia maumivu makali, kiuno chake kikaanza kukaza, kelele alizokuwa akizipiga, zikaanza kupungua kwani kadiri muda ulivyozidi kwenda mbele na ndivyo alivyokuwa akiumia zaidi.
Hakuchukua muda mrefu, huku akiendelea kuingiliwa kichakani pale, mbele yake akaanza kuona giza, akajitahidi kuyafumbua macho yake, haikuwezekana, hapohapo akapoteza fahamu huku wanaume wale wakiendelea kumuingilia kama kawaida, tena kwa zamu.
Deo alikuwa kimya chumbani kwake, machozi yalikuwa yakimbubujika mashavuni mwake, hakuamini kile kilichotokea, kumfukuza Nahra nyumbani kwake kilikuwa moja ya vitendo kilichomuuma mno.
Alimpenda Nahra kwa mapenzi ya dhati, hakuwa tayari kumuona msichana huyo akipata shida yoyote ile, japokuwa alikuwa msichana wa Kihindi, kwake haikuwa tatizo, alikuwa akimpenda hivyohivyo.
Wazazi wa Nahra walionekana kuwa tatizo kwake. Mara baada ya kumpa mimba msichana huyo na kuhamia kwake kwa kuwa wazazi wake walimfukuza, wazazi hao wakawatuma wanaume wawili waliokuwa na bunduki, walichokuwa wakikitaka ni kuona Deo akimfukuza Nahra nyumbani hapo, vinginevyo, wangemuua.
Huo ulikuwa mtihani mkubwa maishani mwake, alimpenda Nahra, hakutaka apate tabu yoyote ile, kitendo cha kuambiwa amfukuze msichana huyo kilikuwa kigumu, akakataa.
Watu hao walipoona kwamba kitu hicho hakikufanyika, wakarudi kwa mara ya pili, wakati huu walionekana kuwa na hasira zaidi, kila walipomwangalia Deo usoni, waliyakumbuka maneno ya mzee Patel ambaye aliwaambia wamuue tu.
“Kijana, fanya tunachokwambia. Tumeagizwa tuje kukuua, hatuwezi, tunakuonea huruma. Fanya hivyo, tunakupa siku moja ya ziada, kesho tukija, tunakuja na sura tofauti na hizi,” alisema mwanaume mmoja huku akimwangalia Deo usoni.
Kwa jinsi walivyoonekana, kwa maneno yao yaliyowatoka midomoni mwao ilionyesha kabisa watu hao walimaanisha kile walichokiongea, Deo akakubaliana nao kishingo upande.
Siku hiyo usiku ndiyo ilikuwa siku ya kumfukuza Nahra nyumbani hapo. Alifanya hivyo huku moyo ukimuuma mno, kila alipomwangalia msichana huyo, alijisikia huruma, moyo wake ulikuwa kwenye maumivu makali.
“Nahra, naomba unisamehe, sikutaka kukufukuza, wazazi wako ndiyo waliolazimisha kufanya hivi, ninakupenda Nahra,” alisema Deo huku akimuona Nahra akikimbia, machozi yalikuwa yakimmbubujika msichana huyo, baada ya hapo, hakujua Nahra alikimbilia wapi, usiku huo, kwake ukawa usiku wenye mateso mengi.
“Nitamtafuta tu,” alisema Deo huku akijipa uhakika kwamba angeweza kumuona tena Nahra aliyekuwa na mimba yake.
****
Nahra alikuja kupata fahamu asubuhi, alikuwa katika majani yenye unyevuunyevu, mwili wake ulikuwa ukimuwasha. Pamoja na kuwashwa huko, alikuwa akisikia maumivu makali chini ya kitovu.
Akaanza kujiuliza sababu ya yeye kuwa mahali hapo, hakukumbuka kitu chochote kile, alibaki akishangaa mpaka kumbukumbu zilipokaa sawa na kuanza kukumbuka kila kitu kilichotokea usiku uliopita, Nahra akaanza kulia, akajiangalia, sehemu zake za siri zilikuwa zimeharibiwa vibaya, akaendelea kulia mfululizo huku akijiinua kuelekea barabarani.
Kila mtu alibaki akimshangaa, alionekana msichana mrembo mno lakini muonekano wake ulikuwa tofauti kabisa, alikuwa msichana mchafu mno, kwa jinsi uzuri wake ulivyokuwa, hakutakiwa kuwa kama alivyokuwa.
“Hata kama nimechafuka na hata kama nimebakwa, bado ninahitaji kumuona Mithun, ni lazima nimfuate na anisaidie, sina kimbilio jingine zaidi yake,” alisema Nahra.
Kila alipopita, watu walimshangaa, hakuwa akitembea kawaida, alikuwa akichechemea kama mtu aliyekanyaga mwiba. Alitembea hivyohivyo mpaka alipofika maeneo ya Fire ambapo akaunganisha mpaka Mtaa wa Twiga, mtaa uliokuwa na maghorofa mengi, huko ndipo alipokuwa akiishi Mithun.
“Mungu, naomba Mithun anikubalie, anisamehe kwa kila kitu niweze kuwa naye, asahau kila kitu kilichotokea maishani mwetu,” alisema Nahra, tayari alikuwa amefika katika mlango wa nyumba ya kina Mithun, akaanza kugonga mlango, moyo wake ulijawa hofu.
Wala hazikupita dakika nyingi, mlango ukafunguliwa, mtu aliyekuwa akimuhitaji ndiye aliyefungua mlango, alikuwa Mithun.
Mwanaume huyo alibaki akimwangalia Nahra huku uso wake ukiwa kwenye mshangao mkubwa. Hakuamini kama yule aliyesimama mbele yake alikuwa Nahra yule aliyekuwa akimfahamu au alikuwa mtu mwingine.
Alikuwa mchafu mno, nguo zake zilikusanya majanimajani huku zikiwa zimetapakaa tope, kwa kumwangalia tu, Mithun alijisikia kinyaa.
“Nikusaidie nini?” aliuliza Mithun huku akijitahidi kujizuia kupumua kupitia pua yake, maji yaliyokuwa yameilowanisha nguo ya Nahra, yalikuwa yakinuka.
“Naomba unisamehe,” alisema Nahra huku akijitahidi kupiga magoti chini.
Alikuwa akilia kwa maumivu makali, alijua kwamba alifanya makosa kumkataa mwanaume huyo aliyekuwa na lengo la kumuoa na kumkubali Deo aliyekuwa amemfukuza kama mbwa.
Macho yake yalionyesha kila kitu, alikuwa akiomba msamaha lakini Mithun hakujali. Alikumbuka vema kila kitu kilichotokea katika maisha yake ya nyuma na binti huyo.
Alimpenda Nahra na kuahidi kumuoa lakini maamuzi ya msichana huyo yalikuwa kwa Deo, mwanaume mweusi aliyempa mimba na kumtimua.
“Unanuka Nahra,” alisema Mithun maneno yaliyomuumiza mno Nahra, ila kwa kuwa alikuwa na uhitaji, akavumilia.
“Naomba unisamehe Mithun.”
“Nikusamehe ili iweje? Na hicho kitumbo ukipeleke wapi? Nikusamehe wewe? Ulivyonikataa kwa maneno ya dhihaka! Nahisi umepotea njia. Kwanza unanuka sana, hivi ulioga jana?” alisema Mithun na kuuliza kwa dharau.
Kilio cha Nahra kikaongezeka zaidi, hakuamini kama maneno yale yote yalitoka Mithun. Alijitahidi kuomba msamaha lakini matokeo yale aliambulia maneno ya kejeli tu, hakutaka kuendelea kubaki mahali hapo, akaondoka zake huku akilia.
“Nitakwenda wapi mimi? Nitaishi vipi mimi? Bora nikajiue tu, siwezi kuendelea kuishi,” alijisemea Nahra na huku akipiga hatua kuelekea nje ya ghorofa hilo.
Huo ndiyo ulikuwa uamuzi alioufikia, hakutaka kuendelea kuishi tena, mateso na maumivu aliyoyapitia yalitosha kabisa kumfunza, hivyo alitaka kujiua kwa kuamini kwamba angekwenda kupumzika.
Akaanza kukimbia kuelekea Kariakoo Relini huku lengo lake kubwa ni kwenda Mivinjeni. Hakukuwa na kitu alichokifikiria zaidi ya kujiua tu, alitaka kuiondoa roho yake kwa kulala kwenye reli na treni kupita juu yake.
Mara baada ya kufika Kariakoo Relini, akachukua Barabara ya Kilwa na kunyoosha nayo kama alikuwa akienda Bandarini. Alipofika Mivinjeni, akaanza kuelekea katika reli iliyokuwa chini ya daraja ambako kulikuwa na vyumba vingi vya reli ya kati.
“Nitajiua tu,” alijisemea Nahra na kujibanza sehemu huku akisubiria treni ipitie na yeye kulala relini. Aliyachoka maisha yake hiyo ndiyo sababu iliyompelekea kutaka kujiua siku hiyo. Hakutaka kuendelea kuishi na wakati watu wote aliokuwa amewaamini hawakutaka kuishi na yeye.
Moyo wake ulimuuma, hakukuwa na kitu kingine alichokiona kuwa suluhisho la maisha yake zaidi ya kujiua tu. Alidhamiria kufanya hivyo kwa kuamini kwamba asingeweza kuumizwa tena, asingeweza kulia tena, huko atakapokuwa, angeishi maisha matamu milele na kuepuka ghadhabu za dunia hii.
“Pooooooo,” ilisikika honi ya treni ya mizigo, alipoisikia honi hiyo, akachungulia kwa jicho moja kutoka pale ukutani alipojibanza. Treni ile ya mizigo ilikuwa ikija kwa kasi.
Ilikuwa imetoka kituoni na kuanza safari yake, alipoiona treni hiyo kwa mbali, Nahra akasubiri mpaka ikaribie na ndiyo aende kujilaza relini na hatimaye aweze kufa na kuyaepuka mateso aliyokuwa akiyapata.
“Nisamehe Mungu! Mateso yamezidi, acha tu nijiue ili wazazi wangu wapumzike, wasinichukie tena. Pia nisamehe kwa kukiua hiki kiumbe unachokitengeneza tumboni mwangu. Mungu, sifanyi hivi kwa kupenda, najua unayajua maisha ninayopitia,” alisema Nahra huku treni ile ikiendelea kusogea zaidi.
Nahra aliendelea kuisubiria,treni ilibakisha kama hatua mia mbili kabla ya kufika pale alipotaka kujilaza. Kichwa chake kilitawaliwa na mawazo tele, alikuwa tayari kujiua lakini si kuendea kuishi kwa mateso kama aliyokuwa akiishi.
“Bora nife tu, sina haja ya kuendelea kuishi,” alisema Nahra.
Baada ya sekunde kadhaa, treni ilikuwa mbali kama hatua mia moja, alichokifanya Nahra, akakimbilia relini na kujilaza. Machozi yalimbubujika mashavuni mwake, hakuamini kama maisha yake yote aliyokuwa akiishi, mwisho wa siku alikuwa amefikia hatua ya kujiua.
“Nisamehe Mungu, sikupenda kujiua, ila sina jinsi. Acha nife na mwanangu aliyepo tumboni,” alisema Nahra, treni ya mizigo ilikuwa ikija kwa kasi, na ilibakisha hatua arobaini tu za miguu ya binadamu kabla ya kumkanyaga pale relini alipokuwa amelala. Muda wote treni ilikuwa ikipiga honi lakini Nahra hakutoka relini, alidhamiria kujiua kwa kukanyagwa na treni hiyo.
Huku treni ikiwa imebakiza kama hatua thelathini za miguu ya binadamu huku Nahra akiendelea kulala relini pale na macho yake yakiwa yamefumba, ghafla akashtuka akishikwa mikono na kuanza kuvutwa.
Hapo, akayafumbua macho yake kuangalia ni nani aliyekuwa akimvuta. Macho yake yakatua kwa kijana mmoja mchafumchafu, aliyevalia pensi ya jinzi chakavu huku mdomoni mwake akiwa na sigara.
“Toka hapo, njoo huku,” alisema kijana yule huku akimvuta Nahra kutoka katika reli ile.
Kwa kuwa kijana yule alikuwa na nguvu Nahra akajikuta akitolewa katika reli ile na treni kupita kwa kasi kubwa.
“Unataka kujiua?” aliuliza jamaa yule huku akimwangalia Nahra machoni, alikuwa akimshangaa tu.
“Ungeniacha nife, sitaki kuishi, naomba uniache nife,” alisema Nahra huku akilia kama mtoto.
“Hapana. Kwani kuna nini? Mbona msichana mrembo unataka kujiua, hebu nieleze, kuna nini,” alisema kijana yule huku akimwangalia Nahra usoni.
Kwake, Nahra alikuwa msichana mrembo kuliko mwanamke yeyote aliyewahi kumuona machoni mwake, kitendo cha binti huyo kutaka kujiua kilimshtua mno.
Nahra hakusema kitu, alibaki akilia tu. Bado moyo wake ulikuwa kwenye maumivu makali, kiu ya kutaka kujiua iliendelea kumkamata moyoni mwake. Lawama zake zote zilikuwa kwa mwanaume huyo aliyemtoa relini, hakujua ni aina gani ya maisha aliyokuwa akiyapitia, hakujua ni jinsi gani moyo wake ulikuwa kwenye chuki kubwa dhidi ya wazazi wake na hata ndugu zake.
“Kuna nini Mhindi wewe?” aliuliza mwanaume yule.
“Nataka kufa.”
“Kwa nini? Umechoka kula ugali?”
“Hapana kaka, nataka kufa tu.”
“Hebu kwanza tutoke hapa, unaweza kuniletea msala,” alisema mwanaume yule na kuanza kuondoka mahali pale.
Wakatoka sehemu ile karibu na reli ile na kwenda juu kulipokuwa na daraja ambapo wakavuka na kuanza kutembea pembezoni mwa Barabara ya Kilwa huku wakielekea Kariakoo Relini.
Nahra alikuwa akilia tu, alikitamani mno kifo kuliko kitu chochote kile, hakuamini kama kweli mwanaume huyo alikuwa amemuokoa na wakati alidhamiri kujiua.
Alikasirika, alimkasirikia kijana huyo. Hakutaka kuzungumza chochote kile, machozi yaliendelea kumbubujika tu mashavuni mwake.
“Nini kinaendelea?” aliuliza mwanaume yule.
Hapo ndipo Nahra alipoanza kusimulia kile kilichokuwa kimetokea maishani mwake tangu alipoanza kuwa na uhusiano wa kimapenzi na Deo, alipopata mimba iliyompelekea kufukuzwa na wazazi wake na hata ndugu zake ambao hawakutaka hata kumuona.
Historia ya maisha yake ilimshtua mwanaume yule aliyejitambulisha kwa jina la Issa, naye akajikuta akianza kuwachukia Wahindi.
“Kwa hiyo hauna pa kuishi?” aliuliza Issa.
“Sina. Sina chochote katika maisha yangu.”
“Basi poa, kama vipi wapotezee tu, twende tukaishi gheto kwangu,” alisema Issa kwa lafudhi za kihuni.
“Unaishi wapi?”
“Tandale Kwa Mtogole.”
“Mmmh!”
“Nini tena?”
“Gari unapandia wapi?”
“Hahah! Hapa hakuna gari, tunakwenda kwa ngondi tu, tunazama hapo mbele, tunaibukia Jangwani, tukizama tena Magomeni, tunaibukia Tandale, dakika tano tu, tupo gheto,” alisema Issa huku akicheka, alikuwa akiongea maneno ya mtaani zaidi.
Kutoka katika maisha ya fedha aliyokuwa akiishi, kutembelea magari, leo hii, kila kitu kilikuwa kimebadilika. Japokuwa Issa alionekana kijana mhuni asiyekuwa na chochote, lakini hakutaka kukataa kwenda kuishi kwake. Hakuwa na kitu, huyo Issa aliyeonekana kuwa mhuni, kwa matatizo aliyokuwa nayo, kwake alionekana kuwa msaada mkubwa. Hivyo akakubaliana naye na kuanza kwenda naye huko Tandale.
****
Alichoka sana, kila wakati alikuwa akipumzika, jua lilimchoma mno huku akitokwa na jasho jingi. Issa hakutaka kujali, bado walikuwa wakiendelea na safari kwa miguu kama kawaida. Alipokuwa akipumzika, Issa alisimama na kumsubiri huku akimtia moyo kwamba ilibakia umbali kidogo kufika Tandale hivyo alitakiwa kuvumilia.
Kwa muonekano tu, Issa alikuwa kijana masikini asiye na kitu chochote cha maana nyumbani kwake. Alionekana kupigwa mno na maisha na kila alipofikiria kama kijana huyo angekuwa msaada mkubwa kwake, moyo wake ukakataa hilo.
Walichukua zaidi ya saa moja na nusu, wakafika Tandale Kwa Mtogole. Chumba kilikuwa shaghalabaghala, hakikuwa na mpangilio, kilionekana kwamba kwa zaidi ya mwezi mzima hakukuwa na usafi wowote uliofanyika.
Nahra akashusha pumzi ndefu, muonekano wa chumba kile uliomchosha mno. Aliyaonea huruma maisha yake, hakuamini kama kuanzia siku hiyo hapo ndipo alipotakiwa kuishi.
“Hapa ndiyo gheto, karibu sana mrembo,” alisema Issa huku akiachia tabasamu pana.
“Mmmh! Kuzuri,” alisema Nahra, harufu mbaya ya chumbani mule, ikaanza kuiumiza pua yake. Hilo wala hakujali sana, alichokuwa akikihitaji, ni sehemu ya kuishi tu.
Kadiri siku zilivyozidi kwenda mbele na ndivyo moyo wa Deo ulivyozidi kuuma, hakuamini kama tayari msichana aliyempenda kwa moyo wote, Nahra hakuwa mikononi mwake tena.
Moyo wake ulikuwa kwenye majuto makubwa, japokuwa alipewa vitisho vya kuuawa endapo tu asingemfukuza Nahra lakini kumuachia likaonekana kuwa kosa kubwa kwake kwani hata kama angemchukua na kuondoka naye kwenda kuishi sehemu nyingine, aliamini watu hao wasingeweza kumpata.
Hakutaka kukaa nyumbani, alijiona kuwa na uhitaji mkubwa wa kumtafuta msichana huyo aliyeondoka nyumbani kwake usiku wa saa mbili.
Alichokifanya siku hiyo ni kuondoka nyumbani, sehemu ya kwanza ambayo ilimjia kichwani mwake ni kwenda kumuulizia nyumbani kwao, Msasani.Alipofika huko, mtu wa kwanza kabisa kuonana naye alikuwa mlinzi, Chichi.
“Namuulizia Nahra,” alisema Deo huku akionekana kutokuwa sawa.
“Daah! Deo, hata salamu?”
“Nimechanganyikiwa kidogo. Mambo vipi!”
“Poa. Nahra hayupo.”
“Hayupo! Si alikuja hapa jana usiku? Chichi, usinifiche bwana, mimi mweusi mwenzako, naomba uniitie Nahra,” alisema Deo huku akionekana kutokuwa sawa kabisa, alikuwa kama mtu aliyechanganyikiwa.
“Deo, siwezi kukuficha kitu, mbona zamani nilikuwa nakuitia freshi tu. Jana Nahra alikuja hapa home, mdingi wake aliwaka kinoma, akamtimua kama mbwa,” alisema Chichi.
“Unasemaje?”
“Ndiyo hivyo. Mzee katili sana, alimfukuza kama hamjui. Hapa unaweza kuniletea msala, mzee akikuona anaweza kukuua na kunifukuza kazi, kama vipi wewe jiachie tu,” alisema Chichi.
“Sawa. Haina noma, niende wapi sasa? Nikamtafutie wapi?”
“Sijajua. Popote pale wewe nenda tu,” alisema Chichi, akaingia ndani na kufunga geti.
Deo akabaki nje, alichanganyikiwa, hakujua ni wapi alitakiwa kuanzia kumtafuta msichana wake, bado alichanganyikiwa mno na hakujua mahali alipokuwa msichana wake aliyekuwa na ujauzito wake.
Hakuwa na jinsi, kwa sababu alitakiwa kuondoka na hapo nyumbani ndiyo sehemu pekee ambayo aliamini angeweza kumkuta Nahra, akaondoka zake na kurudi nyumbani huku uso wake ukiwa na huzuni mno.
*****
ITAENDELEA