Simulizi: Muhanga Wa Mapenzi

Sehemu ya 27

ILIKUWA mnyonge asubuhi, mchana, na jioni. Zilikuwa ni nyakati mbaya mno katika maisha yangu ya ujana. Nilikuwa nikijifungia ndani na kulia kama mtoto.
Wadogo zangu Peter na Daudi, ambao kama nilivyosema awali, kwa nyakati hizo kila mmoja alikuwa na maisha yake.

Walipobaini dada yao nilikuwa nikijihusisha na kazi ya ukahaba mitandaoni, kwa kweli ndugu zangu wale, walichukizwa mno.

Kila mmoja alikuwa akinilaumu kwa kumwaibisha maishani mwake. Hakuna aliye kumbuka msaada wangu kwao ulitokana na kazi hiyo hiyo ya ukahaba, ambayo wao waliona nimewadhalilisha.

Kila mmoja, katika maisha yake alikuwa katika mafanikio, kwani walikuwa na miradi yao mbalimbali ambayo niliwafungulia kupitia pesa niliyoipata kwenye shughuli ya ukahaba.
“Heri tungebakia na umasikini, kuliko aibu hii?”alisema Peter, uso wake ulikuwa na hasira kali.

“Umetuabisha sana Sofia, kama ningalijua msaada wako unatokana na kazi ya kujiuza mitandaoni, kamwe nisingekubali kusaidiwa na wewe,” Daudi naye alishadadia.
Nilisemwa na ndugu zangu wale kiasi cha kushikwa na aibu kubwa.

Waliondoka na kunitenga. Tukio la kukimbiwa na mchumba masaa machache kabala ya ndoa kwa sababu ya kuvuja kwa picha zangu, ilikuwa ni mwiba mkali moyoni.

Habari hiyo ilisambaa kila mahali. Kila nilipopita nilisindikizwa na minong’ono, watu walinisonta vidole wakisimuliana kisanga cha kukimbiwa na mwanaume kisa umalaya.

Nilikonda na kubakia mifupa, dunia ilikuwa sehemu moja ngumu sana. Katika nyakati hizo ndipo nilipojiingiza kwenye tabia ya ulevi.

Niliingia kwenye ulevi wa pombe kwa mantiki moja tu. Kupunguza mawazo, niliamini pombe inaweza kuniondolea msongo wa mawazo na kuweza kumsahau kabisa Alex.

nikawa nakwenda viwanja mbalimbali, huko nikawa nabwia ulabu. Nilipolewa chakari nikawa nacheza muziki, naimba imba kama mwendawazimu, wakati mwingine nikawa naongea kilevi peke yangu.

Ulevi ulikuwa unaniondolewa mawazo nyakati nilipolewa tu, pombe ilipokwisha, tatizo lile lilinirudia upya akilini mwangu. Moyo wangu ukawa mzito kumsahau Alex.
 
Sehemu ya 28

Siku moja nililewa chakari, nikaendesha gari hadi nyumbani kwa mchumba wangu huyo wa zamani. Nilipofika nikaanza kulia na kumsihi mwanaume huyo anisamahe.
Alex aliniburuzia nje, akanifukuza kama mbwa koko.

“Nani akutake kiruka njia kama wewe, hebu niondokee!” nilifukuzwa. Nikatukanwa matusi yote ya nguoni.
Lakini kwa kuwa nilikuwa nimelewa pombe, sikukoma. Nilirudi nikaanzisha timbwili, nikaangua kilio na kugaragara kama mtoto.

Watu walikusanyika wakanizunguka, wakanifotoa picha, kisha wakazituma katika mitandao ya kijamii. Baadhi ya wasamaria wema wakanisaidia, nikarejeshwa nyumbani. Pombe zilipokwisha na niliposimuliwa tukio lile, ilikuwa ni aibu kubwa. Nilitamani ardhi ipasuke nitumbukie huko milele.

Mapenzi yalikuwa yanakaribisha ukichaa maishani mwangu. Niliharibikiwa na kuvurugwa. Hayo ndio yakawa maisha yangu kwa kipindi kirefu.

Hapa kuna jambo moja nimesahau kulielezea. Iko hivi: Katika nyakati zile ambazo nilikuwa nikipitia majaribu maishani, ndugu zangu, Peter ana Daudi, pamoja na kwamba walikuwa wamenitenga, niliwaomba jambo moja. Wanisaidie kusimamia miradi yangu ya biashara.

Pamoja na kwamba ndugu wale walikuwa na hasira na mimi lakini angalau nawashukuru kwa jambo lile, waliweza kusimimamia biashara zangu ipasavyo, walinisaidia kusimamia masoko na fedha kwa uaminifu mkubwa. Na huwa nakiri waziwazi, kama sio Peter na Daudi ningalifilisika mapema mno. Mapenzi jamani mapenzi! Yasikieni tu.

Tabia ya ulevi iliendelea bila kukoma, nakumbuka kuna siku nilikunywa pombe nyingi sana, kiasi cha kushindwa kabisa kuendesha gari, sikumbuki ni kitu gani kilitokea, ila ninacho kumbuka.
Nilipoamka kitandani nikajikuta katika hali isiyo ya kawaida.

Nilikuwa kama nilivyozaliwa kitandani kwangu. Ilikuwa majira ya saa nne asubuhi. nilipojikagua maungoni mwangu nikabaini nilikuwa nimeingiliwa kimwili.

“Nimebakwa!!” nilimaka. Ilikuwa ni baada ya kujichunguza kwa kidole na kuona nilikuwa na mbegu za kiume sehemu zangu za siri.

Sikujua ni nani hasa aliyenifanyia jambo lile kwa vile usiku wa kuamkia siku hiyo, nilikuwa nimekunywa pombe nyingi kiasi cha kutojitambua.

Nilijaribu kukumbuka mara ya mwisho nikiwa kilabu cha pombe nilikuwa na nani.
 
Sehemu ya 29

Hapo nikamkumbuka mwanaume mmoja, mrefu mweusi, mwili wake ukiwa umejengeka kimazoezi.

Ni yule baunsa wa kilabuni ndio kanifanyia hivi? Nilijiuliza kimoyomoyo. Nilikumbuka baada ya kulewa sana , mwanaume yule ndiye alinikokota na kunipeleka nje, katika gari langu.

Kumbukumbu zangu zilishia hapo. Sikujua tena kilichoendelea hadi nilipo zinduka asubuhi ya siku mpya. Nikiwa uchi kitandani, nilikuwa na maumivu sehemu zangu za siri, mbegu za kiume zikiwa zimenitapakaa.

“Ni nani amenibaka?” nilijiuliza tena kwa sauti ya fadhaa.

Akili yangu ikafanya kazi haraka sana. Nikasimama nikiwa nimefura kama koboko. Nikatoka na kumkabili dada wa kazi aitwaye Nasra ili anieleze ni mwanaume gani niliingia naye chumbani kwangu

“Nasra nataka uniambie jambo moja” nilianza kuongea na dada wa kazi, Nasra.
“Jambo lipi dada?” “Ni nani jana usiku alinileta nyumbani?”

“Wanaume wanne.”
“Unasema!!!” “Walinimbia wote ni rafiki zako na mtalala wote hapa.” “Mungu wangu!!!!” nilihamaki. Moyo ukapiga ‘paa’ nilipata jibu.

Nilibakwa na wanaume wanne nikiwa nimelewa. “Na wewe ukawaruhusu walale na mimi!!”
“Ningefanya nini na wewe mwenyewe uling’angania.”

“Pumbavu!! Hivi unajua walichonifanyia?” “Walikubaka?” Nasra aliniuliza swali la kijinga, nilitamani nimtandike vibao.

“Fungasha mizigo yako uondoke, huwezi kuruhusu jambo baya kama hilo ndani mwangu.”

“Dada mimi kosa langu ni lipi hasa?”
“Nasema ishia zako,” nilikang’aka.
Machozi yalinibubujika, nilijutia ulevi wangu, nilijilaumu mwenyewe, sikujua kama wabakaji hawajaniambukiza Ukimwi, ama kunipachika mimba.

Nilirudi chumbani na kuangua kilio kama mtu aliyefiwa, kitendo cha wanaume washenzi kufaidi uroda wangu kirahisi kiliniumiza mno.

Kufumba na kufumbua majirani wakafurika ndani kwangu, kutokana na kilio nilichokua nikikiangua kila mtu aliamini kama sijafiwa na ndugu wa karibu basi nina jambo kubwa lililonikuta.

“Umepatwa na nini Sofia?”
“Nani amefariki?” Kila mtu aliuliza. nilibaki njia panda kama natakiwa kueleza ukweli juu ya maswahibu yaliyonikuata ama laa!.

Hata Nasra, msichana wangu wa kazi naye alipoulizwa juu ya kilio changu, naye alibakia na kigugumizi.
 
Sehemu ya 30

Aliogopa kusema kama kilio kile kilitokana kubakwa na wanaume wanne usiku kucha, nikiwa nimelewa pombe.
“Niacheni peke yangu,” ndio kitu pekee nilichowambia majirani zangu.
“Kwa nini unalia?” jirani yangu mmoja aitwaye baba Zinira alihoji.

“Ni mambo binafsi?”
“Lakini unatutisha sana jirani.”
“Sana, jamani unatutisha, kwa nini usituambie labda tunaweza kukusaidia,” mwingine alishadadia.

“Niseme mara ngapi ni mambo binafsi.” niliunguruma. Sikuwa tayari kabisa kuwaleza watu kwamba nilibakwa na wanaume wanne. Aibu iliyoje.
Mwanamke kuwa mlevi kiasi cha kubakwa na lundo la wanaume, ukiwa hujitambui ni fedheha mbaya.

Kimoyomoyo niliapa kutomwambia mtu yeyote tukio hilo.
“Naombeni mniache peke yangu.” “Una uhakika huitaji msaada wetu Sofia?”
“Sihitaji.”

Majirani hawakuwa na namna, iliwabidi waondoke nyumbani kwangu. Wakati huo Nasra alikuwa akifungasha mizigo yake tayari kwa kuondoka.

Niliona suala la Nasra kuondoka lingekuwa zuri zaidi kwa kuwa ni yeye pekee aliyekuwa anatambua kwa nini nilikuwa nikilia. Kama angeondoka na kurudi kwao, siri ya kubakwa kwangu, ningebakia nayo mwenyewe.

“Sijawahi kuona binti tutusa kama wewe. Heri uondoke tu.” Niliendelea kumsema Nasra. “Dada Sofia naondoka, lakini ni wewe ulienifundisha kutii kila kauli itokayo kinywani mwako.

Ningefanya nini kuzuia usingie chumbani na wanaume ilihali mwenyewe ulisema ni rafiki zako? Ningefanyaje?” Nasra aliuliza kwa uchungu.

“Nasra ishia zako, unashindwa kuelewa hali ya mtu? Unashindwa kutambua nikiwa timamu na mlevi, hili somo nalo ulitaka upate mwalimu wa ziada?
“Maelekezo yako kwangu niliyachukulia kama sheria na....” “Sina muda wa malumbano. Ishia zako.” Nilimkatisha.

Nilimpa mshahara wake siku hiyohiyo nikamtakia maisha mema huko aendako. Nasra aliondoka. Nikabaki peke yangu. Hata hivyo siku mbili tu badaye, maneno yakasambaa kwa kasi kubwa mtaani.

Kile nilichodhani kitakuwa siri, kikavuja. Kila mtu akafahamu kwamba nilibakwa na wanaume wanne kwa mpigo nikiwa nimelewa pombe.

Wakaendelea kufahamu kwamba msichana wangu wa kazi nilimfukuza kwa kushindwa kunilinda na tukio hilo.

“Alimwonea.” Baadhi ya watu waliambiana.
 
Sehemu ya 31

Ndio alimwonea, tena huyu mwanamke alitaka mwenyewe abakwe, maana hata polisi hakwenda.”

“Inawezekana ndio michezo yake.”
“Ndio zake, kwani umesahau kama aliachwa na mwanaume masaa machache kabla ya ndoa baada ya jamaa kubaini alikuwa akijiuza kupitia mitandao.”

“Wacha wee!”
“Ulikuwa hujui?”
“Nilikuwa sijui?”
“Huyo mwanamke kimeo sana.”

Mazungumzo hayo niliyasikia moja kwa moja masikioni mwangu. Kwa mara nyingine nilikuwa nimeingia kwenye aibu mbaya maishani.

Nilitambua kivyovyote Nasra ndiye mvujishaji wa siri ile. Lakini ningefanya nini? sikuwa na la kufanya.

Angalau mkandamizo wa ile skendo chafu ya kubakwa na wanaume wanne, ilinifanya nijikite katika kuwaza zaidi suala hilo kuliko hata kumfirikia Alex.

Ukiachilia mbali kashfa hiyo, lakini nilikuwa nina wasiwasi mno na afya yangu, nilikuwa nina mashaka kama wale jamaa hawajanipachika ujauzito ama kuniumbukiza magonjwa ya zinaa ikiwemo Ukimwi.

Mwezi ulipopita na nilipoziona siku zangu, nikafarijika moyoni, wale washenzi hawakunipachika ujauzito. Mtihani ukabakia kwenye magonjwa.

Sikuwa na uhakika na afya yangu , na kwa kweli nilikuwa naogopa mno kwenda kupima.
Kwa kuwa pombe, na moyo wa kupenda, ndio mambo yaliyokuwa yamevuruga maisha yangu, niliamua kuyaweka kando kwa muda.

Nakumbuka nilikuwa nimeamua kujisajili pale Maktaba kuu ya Tafa. Kila siku nilikuwa nikiendesha gari na kwenda kushinda nikisoma vitabu mbalimbali hasa vya riwaya.

Tabia ya kupenda kusoma vitabu ambayo nilikuwa nayo tangu nikiwa shule, ilinisaidia sana katika kipindi hicho, nakumbuka kwa miezi mitatu tu, nikajikuta nimekuwa mtu mpya.

Nilimsahau Alex, sikutamani tena Pombe. Kuna wakati nikajilaumu kwa kuchelewa kutumia dawa ile kunisahulisha na machungu ya maisha na mapenzi
Vitabu vilikuwa vimenisaidia kunisahaulisha mkandamizo maishani. Ndani ya miezi minne badaye, nikarudi kwenye biashara zangu kama kawaida.

Nikaapa kutojiingiza tena kwenye uhusino wa kimapenzi na sikuwa na hamu ya ndoa tena. Haiba yangu ya Urembo ikanirejea, mtoto wa kike nikawa gumzo kila nilipopita.

Lakini kwa kuwa moyo wangu ulikwisha poa, wanaume wengi waliishia kula kwa macho, walijigonga, wakababaika na urembo wangu.
 
Sehemu ya 32

Bahati mbaya hakuna aliyeambulia kitu.
Sikwahi kupata wala kujua habari za Alex ingawa niliwahi tu kusikia tetesi kwamba baada ya kuachana na mimi hakuoa mwanamke yoyote tena.

Kwa kuwa nilikuwa nimeamua kuwa na maisha mapya, sikupenda kujua habari zake zaidi, hasa ukizingatia kwa nyakati hizo niliapa kutotoka na mwanaume kimapenzi.

Nilikuwa na misimamo mikali sana kwa mwanaume yeyote aliyenisogelea. Watu walinishangaa. Lakini mimi sikujali. Nilishia katika falsafa moja tu:
Mapenzi ni kama mtego umwingizao mtu matatizoni.

Niliishia kwa misingi hiyo kwa muda mrefu tu hadi siku moja lilipoibuka tukio moja ambalo lilitengeneza simulizi mpya maishani mwangu. Tukio hilo lilitokea ndani ya maktaba kuu ambako nilizoea kwenda kusoma vitabu mbalimbali.

Ilikuwa ni siku moja tarehe na mwezi nisiyoweza kuisahau maishani mwangu. Kama kawaida yangu, siku hiyo nilikuwa niko zangu Maktaba, nimechukua nafasi katika kona moja, nimezama kwenye riwaya maarufu ya enzi hizo iitwayo ‘pili pilipili’ .

Hadithi ile ilikuwa imenichota hisia zangu na kutembea kwenye matukio yaliyokuwa yamesimuliwa na mwandishi wa kitabu hicho kiasi cha kusahau kama niko Maktaba.

Kumbe wakati nikiwa nimezama kwenye simulizi ile, mwanaume mmoja alikuja akanisimamia karibu yangu akawa sijui ananiambia nini, kwa kuwa nilikuwa nimezama kwenye simulizi ile sikumsikia.
“Hellooooow!!” Jamaa alibweka kwa sauti.

Nilishituka nikakitupa kitabu chini. Alikuwa amenishitua kwa sauti kali.
“Uko mbali sana na kitabu chako.” Mwanaume mrefu mweusi, mwenye macho makubwa alisema.

“Kwa nini umenishitua ghafla hivi?” nilimuliza kwa ukali.
“Sio ghalfa, nimekusemesha muda mrefu hunisikii,” macho makubwa alinijibu.

“Unasemaje?” niliuliza kwa kiburi.
“Nimeambiwa nikuulize gari lililopaki kule kwenye mauwa ni lako...” “Umeambiwa na nani uniulize?”
“Na mwenye gari mwenzio.”
“Nani?”
“Simjui.” “Shida nini?” “Ni lako?”

akauliza
“Sema shida yako?”
“Kama ni lako inatakiwa ukalisogeze kidogo, mwenzio anataka kutoa lake.”
 
Sehemu ya 33

Nilimwangalia kwa chati mvulana yule, alikuwa ni mwanaume mzuri tu ambaye wasichana wa hadhi yake wangeweza kupigana vikumbo na kumgombania kila wakati, alijaliwa mwili fulani hivi laini laini, hata hivyo alioanekana amepigika na maisha, japokuwa kwa jicho jingine alionekana kama mtoto wa mama tu.

Mbele yangu hakuwa na hadhi yoyote, nilimwona mshamba mmoja tu awezaye kukomba chai kwa kidole.

Alikuwa amevaa shati kubwa, baya ambalo naweza kusema lilimvaa mwili wake, chini alivaa kipensi ambacho kiliyashika vema mapaja yake, miguuni alikuwa kwenye buti kubwa nyeusi. Nilitabasamu kisha nikwambia: “Nakuja. ” Akondoka.

Aliondoka kinyonge ni kama vile aliataka kusema unasubiriwa wewe tu ili mwezio atoe gari lake, lakini alisita kutokana na uso kiburi na dharau niliomwonyeshea.

Nilirudi kwenye kitabu changu na kuendelea kusoma kurasa za riwaya ile ya Faraji Katalambua.

Kama baada ya dakika kumi kupita, nikiwa nimezama tena kwenye ile hadithi mara sauti ikatokea pembeni yangu:

“Bado umekaa!” Nilitizama harakaharaka mtu aliyeongea kauli hiyo. Macho makubwa alikuwa amerudi, alisimama pembeni yangu akinitizama kwa mshangao.

“Kwa nini unanisumbua wewe?” nilifoka.
“Gari lako limeziba njia, magari mengine yanashindwa kutoka!” naye alisema kwa sauti ya hamaniko.

“We unafanya kazi hapa?” nikamuuliza nikiwa nimemtolea macho makali. Sikuwa na woga na macho yake makubwa, Sikutaka mzaha kabisa na vivulana vishenzi shenzi.

“Ndio.”
“Kitengo gani?”
“Ni Creaner.”
“Nilijua tu.” Nilisema kwa dharau, nikamuliza tena.
“Unajua kuendesha gari?”
“Kidogo.”

“Haya shika funguo nenda kalitoe njiani gari, kisha rudisha funguo sasa hivi.”
Mr Macho makubwa, alibaki akinishangaa huku macho yake makubwa akiwa ameyakodoa kama kinyonga.
 
Sehemu ya 34

“Shikaa.” Alinyakua funguo, akaenda kusogeza gari langu. Dakika tano badaye, akarudisha funguo zangu.

“Umeridhika?”
“Dada mkubwa wewe mtata kama pilipili. Jina la muhusika wa kitabu hicho unachosoma.” Alisema huku akiachia tabasamu mwanana.
Mungu wangu!!! Tabasamu lake jamani tabasamu!!.

Lilikuwa ni tabasamu la kukata na shoka. Picha ya uzuri wa mvulana yule ulitambaa kwenye mifreji ya mishiapa yangu ya damu, ikasafiri na kugota ndani ya moyo wangu. Nilikufa na kuoza.

Mwanaume yule alikuwa ni vishimo kwenye mashavu yake ambavyo akicheka ama kutabsamu vilibonyea kwa ndani na kuleta picha isiyoisha hamu kutazamika. Meno meupe kama sufi yalipangika vizuri kinywani mwake mithili ya kibunzi cha muhindi.

“Umewahi kusoma hiki kitabu?” nikamuuliza. Nilificha hisia zozote zitakazomjulisha mvulana yule kama nimedata na – ‘handsome boy’ wake.
.
“Zaidi ya mara tano...” alisema.
Nilimpa tabasamu lililosema: Nashukuru kwa muda wako. Mr Macho makubwa hakuwa na nyongeza, aliondoka. Hata hivyo hadi anaishilizia, mtoto wa kike nilikuwa sijiwezi kwa mvulana yule.

Angalau nilijisikia uhuru kwa kuondoka kwa mtu yule, lakini hapo hapo nikawa najilaumu ndani kwa ndani kwa kutomuuliza jina lake au hata kumwomba namba yake ya simu.
“Lakini angeniona najirahisisha kwakwe.” Nilinong’ona.

Nitamuuliza kesho jina na nitamwomba namba ya simu. Nilijiambia kimoyomoyo: Sikuweza tena kuwa na utulivu. kitabu hakikusomeka kabisa. Kila wakati nilikuwa namfikiria kijana yule mwenye macho makubwa.

Nilisimama na kuondoka zangu. Wakati naanza kutoka na gari nje ya jengo la maktaba. Nikasikia sauti ikisema:
“Dada pilipili kwa heri!!” alikuwa ni Mr macho makubwa.

Dada pilipili tena!!!. Alikuwa amenipachika jina la utani ambalo aliniita wazi wazi kama mimi nilivyompachika jina la ‘Mr macho makubwa’ ingwa sikumwita waziwazi.

Hata hivyo na mimi nilimpuinga mkono, kisha nikapandisha kioo huku nikitabasamu. jina nililopachikwa na kijana yule chakalamu. Lilinifurahisha. ‘Dada pilipili’

Mvulana yule alikuwa amenichanganya mno. Kwa muda mfupi sana, akili yangu ilishindwa kufanya kazi vizuri.
Ile misimamo yangu ya kutohitaji mwanaume iliyeyuka kama bonge la barafu juani.
 
Sehemu ya 35

“Yule kijana kama sio mwanga basi atakuwa jini yule,” nilijisemea kimoyomoyo wakati naingiza gari ndani ya ngome ya nyumba yangu ya kifahari huko Mbezi Beach.

Siku hiyo nilishinda kama mgonjwa, sura ya mwanaume niliyemwona mara moja tu lishindwa kabisa kubanduka kichwani mwangu. Mapenzi ya ajabu yalinivaa. Usiku kucha nilikuwa nikitamani kukuche upesi nikakutane tena na Mr Macho Makubwa.

Niliona kama masaa yanakwenda taratibu kuliko kawaida. Hatimaye asubuhi ya siku ya pili ilifika. Nilijiandaa harakaharaka kwani nilikuwa nimechelewa kuamka kutokana na kukawia kulala kwa kumfikiria mwanaume aliyejaliwa Macho ya mahaba.

Nilikwenda kazini mbiombio, baada ya kugawa majukumu kwa wafanyakazi wangu, saa tano kamili nilikuwa kwenye gari langu nikielekea katikati ya jiji la Dar es salam.

Makataba kuu ya Taifa, kumwona mwanaume aliyeugusa moyo wangu kiasi cha kunifanya niwe mpumbavu kwa masaa 28 yaliyopita.

“Leo lazima niongee naye” nilijisema mwenyewe wakati naingiza gari kwenye maegesho ya maktaba. Nilikuwa nimefika.

NILITEREMKA garini nikaangaza huku na kule kama nitamwona Mr macho makubwa. Hata hivyo, bahati mbaya, sikumtia machoni.

Nilitamani niwaulize walinzi juu ya mvulana yule, lakini nilisita. Sikuwa nalijua jina lake ningeulizaje? Na hata kama ningeelezea haiba yake, walinzi wangenionaje? namtaka wa nini Mr macho?

Niliingia ndani ya maktaba na kukichukua kitabu nilichokuwa nasoma jana, nikaketi sehemu ile ile niliyoketi jana, nikaanza kufunua kurasa za kitabu kile.

Pamoja na kwamba nilikuwa nikisoma maandishi ya riwaya ile, hata hivyo siku hiyo haikuniingia kabisa hadithi ile, sikuwa na utulivu wa nafsi hata kidogo. Mawazo yangu yote yalikuwa kwa Mr macho makubwa.

Muda ulivyozidi kwenda dalili za kutomwona kijana yule zilionekana. Kuna wakati nikatamani hata ningelipaki tena gari langu njiani ili ‘handsome boy’ yule aje kuniita kulitoa kama ilivyokuwa jana.
 
Sehemu ya 36

“How can i do?” Nilinong’ona kwa kimombo uso wangu ukiwa umesawijika.
Nilisimama na kutoka nje ya maktaba.

Nikazuga kama nawasiliana na mtu simuni, lengo langu ilikuwa ni kuangaza kwenye bustani ya maktaba nione kama nitamwona Mr Macho makubwa .

Mvulana yule hakuwepo. Nilijisikia kukosa raha, shauku ya kuuliza nayo ikawa kubwa zaidi, nilimpenda mno mwanaume yule, moyo wangu ulikuwa haujiwezi kabisa dhidi yake.

“Wewe mbwa macho makubwa uko wapi? kwa nini unanitesa hivyo.” Nilinong’ona nikahisi donge kavu likinikaba kooni.
Niliamini yule mwanaume hakustahili kutesa moyo wangu kiasi kile.

Mtu mwenyewe hana mbele wala nyuma, halafu ananikosesha amani mimi mtu mzima na pesa zangu, Ujinga huu.
Yeye ndiye alitakiwa kubabaika hivi sio mimi. Nina pesa.

Nina gari na nyumba nzuri. Naweza kuwa na mwanaume yeyote mzuri na mwenye hadhi inayofanana na mimi. Vipi nibabaike na vivulana vyenye hadhi ya huko Tandale kwa Bi nyau!!.

Fedheha hii. Nilitembea kuliendea gari langu, nilidhamiria kuondoka kabisa maktaba. Halafu nikajitia kupuuza kabisa jinamizi la pendo kwa mtu yule. Sikupenda kabisa kuona namfikiria mwanaume yule.

“Jitu lenyewe lina macho kama bundi... Hovyoo!” Nililiondoa gari na kushika barabara ya Ally Hassan Mwinyi. Siku hiyo hakukuwa na foleni, dakika tano tu badaye, nilikuwa nalivuka daraja la salenda.

Nikakanyaga mafuta injini ya gari langu nayo ikalalama kwa sauti tulivu. Dakika 20 badaye nilikuwa njia panda ya Moroco nikingojea taa ya kijani ili niweze kuchepuka upande wa kulia. taa ya kijani iliporuhusu nikashika njia ya kuelekea Msasani.

Safari yangu ikaishia katika hotel ya Breez Lounge Msasani. Ni moja ya hotel za daraja la juu na ghali hapa jijini Dar, wapumbavu kama akina Mr macho makubwa hawezi kufika viwanja kama hivi.

Nilikwenda na kuketi sehemu ya nje ambapo kulikuwa na viti maridadi vilivyowekwa vema. Nilichukua nafasi katika sehemu moja nzuri. Kipupwe kilinipuliza na kiniodolea fikra zote za Mr macho makubwa.

Sehemu ile ilikuwa tulivu, kilichosikika ni maji ya bahari na vicheko vya chini chini vya wapenzi waliokuwepo eneo lile, kadhalika, kulikuwa na sauti ya muziki nyororo kutoka kwenye spika za kaunta.
 
Sehemu ya 37

Muda si mrefu muhudumu alifika, alikuwa akisubiri oda yangu, nilipitia ‘menu’ nikaona kuna: ‘Hand-Batter fish, Chunky chips, British Beef and Ale Pie, Ham Hock, Pea Pie’ Breaded Whole nk.

Nilete Spaghetti Bolognese na Heinken baridi sikupenda kuagiza chakula ambacho ningekula halafu badaye kinishinde, nilitambua Spaghetti Bolognese ni kama tambi tu ningweza kuzimaliza.

Nilihudumiwa ule msosi, kwa kuwa nilikuwa na njaa, dakika tu, sahani ilikuwa nyeupe, nikabakia nakunywa Henken yangu ya baridi huku upepo wa bahari ukinipa burudani ya aina yake.

Tafuta pesa bwana wewe, maisha ndio haya haya. Burudani kama hizi ukiwa kapuku utaendelea kuzisoma kwenye riwaya na kuziona kwenye filamu.

Kuna wakati nikiwa naendelea kubugia kinywaji changu kile niliona kama niko katika pepo fulani hivi duniani.
Nikiwa pale, katika utulivu wa nafsi na akili mara nikakutwa na iliyo niondolea utulivu wote.

“Hey miss.” Nilisikia sauti niliyoitambua ikiniita. Sauti hiyo ilitokea nyuma yangu. Ilikuwa ni sauti nzuri ya kiume. Sauti ya Mr macho makubwa!!!.
****
Kwa mshituko glasi ya Henken ikaanguka chini bila kujua. Glasi ikavunjika Mr Macho makubwa akanivuta kwa pembeni nikae mbali na vipande vya chupa vya glass iliyovunjika.

Watu wote wakawa wananiangalia, aibu ilinishika asikwambie mtu. Mr macho makubwa alinishika mkono kisha akaniongoza kunipeleka sehemu nyingine.

Namna alivyonishika mkono na namna alivyokuwa akiniongoza, ilikuwa kama kondoo apelekwaye machinjioni na mchungaji wake. “Wajionaje mrembo?” Mr Macho makubwa alinisalimu baada ya kunikalisha na utulivu kurudi kwenye hali yake.

Mwili wangu ulikuwa unachuruzika jasho, kwa kweli kitendo cha kumwona mvulana yule katika eneo lile lilikuwa ni shambulio la moja kwa moja moyoni mwangu.
Ile nadhiri ya kumfuta na kumsahau moyoni mwangu sijui hata iliyeyukia wapi. Nikajikuta nafurahia uwepo wake.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom