Simulizi: Mke Wangu Juliana

Simulizi: Mke Wangu Juliana

Milima haikutani binadamu wanakutana
SEHEMU YA 72

“Wewe ndiye Deborah?” aliuliza mwanaume huyo, alikuwa meneja kwenye kampuni hiyo.

“Umenijuaje?”
“Uliomba kuja kuonana nami kutoka huko Kigoma, ama si wewe?” aliuliza.
“Ndiye mimi!”

Walizungumza, alimwambia kuhusu hali ya mume wake, alifanya kazi kwa miaka sita, alikuwa mtu mwenye sifa nzuri katika kampuni hiyo, hivyo waliongea mambo mengi na meneja huyo, Bwana Kinyora alimwambia angefanya kila juhudi mume wake aajiriwe kwenye kampuni hiyo.
“Nitajitahidi kwa hali na mali!” alisema mwanaume huyo.

Baada ya kumaliza mazungumzo hayo, akatoka na kurudi hotelini, alipofika njiani, akaamua kununua Gazeti la Nipashe ambapo kulikuwa na taarifa ya mwanaume mmoja aliyekuwa akitafuta msaada wa watoto wake walioungana kupelekwa nchini India kwa ajili ya kutenganishwa.

Aliiangalia habari hiyo, hakuona picha ya mwanaume huyo wala watoto hao walioungana lakini alipoangalia namba ile ambayo walitakiwa wasamaria wema watume pesa, aliifahamu vilivyo, ilikuwa namba ambayo haikuwahi kutoka kichwani mwake.

“John!” alijikuta akisema kwa mshtuko, akaamua kuipiga, mwanaume huyo akapokea.
“Halooo!” aliita.
“Halo John!” aliita msichana huyo.
“Deborah?”

“Ndiyo! Ni mimi hapa!” alijibu Deborah! Tayari machozi yakaanza kumtoka, kile alichokuwa amekisoma kwenye gazeti kilimuumiza kupita kawaida.

Yule John, kijana masikini alikuwa akihitaji kiasi cha shilingi milioni hamsini na tano ili watoto wake walioungana wakatenganishwe nchini India.
|
|

Je, nini kitaendelea?

Sent using Jamii Forums mobile app
 
Sehemu ya 74

John alikuwa akitetemeka, moyo wake ulikuwa na hofu kupita kawaida, ile sauti ya moyoni mwake iliyomwambia mke wake alifariki dunia iliendelea kusikika kichwani mwake.
Ilimtisha na kumfanya kulia kama mtoto mdogo, mashavu yake yalilowanishwa na machozi yaliyokuwa yakiendelea kumbubujika kama kawaida.

Baada ya sekunde kadhaa, wakaingia ndani ya ofisi ya daktari yule, akakaa kwenye kiti na kuanza kuzungumza naye. Alimwambia hali halisi, mkewe alijifungua watoto walioungana, wote walikuwa wa kiume lakini hakuwa kwenye hali nzuri, walitakiwa kumuacha apumzike kwani hakujifungua kwa hali ya kawaida, alifanyiwa upasuaji.

“Pole kwa matatizo!” alisema daktari.
“Mke wangu amepona?”
“Ndiyo! Tulimfanyia upasuaji!” alijibu daktari.
John akatoka kwenye kiti, akapiga magoti na kuiinua mikono yake juu, akaanza kumshukuru Mungu kwani kile kilichotokea kwake kilikuwa muujiza mkubwa.

Alishindwa ni kwa namna gani alitakiwa kumwambia Mungu ahsante kwani hata neno lenyewe aliona kama halikutosha kumshukuru kwa yote aliyokuwa amemfanyia.

“Mungu wewe ni mwema kwetu, umetupa watoto walioungana, nilishukuru kwa hilo, nilipohisi mke wangu amefariki, bado ukamponya. Ninakushukuru Mungu, wewe ni Mungu muumba mbingu na nchi, ni Mungu ambaye matendo yako ni makuu mno, nashukuru sana kwa kumpa mke wangu nafasi ya kuishi te.....” alishukuru pale alipopiga magoti, hakumalizia maneno yake, akaanza kulia kwa uchungu uliochanganyikana na furaha nzito.

Daktari akasimama alipokuwa na kumfuata, akamuinua na kuanza kumbembeleza kwani kwa jinsi alivyokuwa akilia, hakuonyesha kama angenyamaza.

“Pole sana John!”
“Usinipe pole. Ninamshukuru Mungu kwa matendo yake. Si kwamba nyie ndiyo mmemponya mke wangu na kujifungua salama, ni Mungu, miujiza yake ni mikubwa sana daktari...” alisema John.

“Mshukuru sana Mungu!”
“Nitamshukuru mpaka ninaingia kaburini!” alisema John.

Baada ya kuzungumza machache wakiwa wamesimama, wakakaa kwenye viti na kuendelea. Daktari alimwambia kuhusu hali za watoto wake, jinsi walivyoungana kulikuwa na nafasi kubwa ya kutenganishwa na kuwa kama watoto wengine.
 
Sehemu ya 75

“Kuna aina nane za watoto kuungana! Hivi ni vitu muhimu sana ambavyo ningependa sana uvifahamu na ujue watoto wako wapo kwenye kundi gani,” alisema daktari huku akimwangalia John.
“Sawa,” aliitikia kwa unyonge.

“Kundi la kwanza linaitwa Cephalopagus. Hawa ni wale mapacha ambao wameungana kwa mbele, yaani wameungana kuanzia tumboni, kifuani mpaka kichwani, na ukiwaangalia kwa jinsi uso ulivyo unaweza kusema ni uso wa mtu mmoja, ila ukiwaangalia vizuri utagundua ni watu wawili kwani muonekano wa huwa tofauti na watu wengine,” alisema daktari na kuendelea:

“Kundi la pili linaitwa Thoracopagus. Hawa ni mapacha walioungana kwa kuangaliana. Wameungana sehemu za tumboni, kwa maana hiyo hawa watu wanachangia utumbo mmoja, inawezekana hata kuwatenganisha ikawa vigumu,” alisema na kuendelea:

“Kundi la tatu linaitwa Omphalopagus. Kundi hili ukiliangalia fufanana na kundi hilo la mwanzo ila hili kuungana kwao kuanzia tumbo mpaka kifuani huwa ni kwa kiasi kikubwa sana,” alisema na kuendea:

“Na kundi la nne limaitwa Ischiopagus. Hili kundi huwa baya sana kwani watoto wanaungana na huwa na muonekano kama kenge ama mamba, wengi wakiungana kwa namna hii, hawachukui muda mwingi huwa wanakufa,” alisema huku akimpa kikaratasi kilichokuwa na picha ya watoto wote walioungana.

“Kundi la tano linaitwa Parapagus. Hili kundi watoto wanaungana kuanzia kiunoni kwenda chini. Huwa wanachangia miguu miwili tu waliyokuwanayo, huwa hawana miguu minne, huwa na miwili tu,” alisema na kuendelea:

“Kundi la sita huitwa Craniopagus. Hili kundi watoto huungana vichwa kwa kuangaliana, yaani paji la nyuso zao, kuwatenganisha huwa vigumu kwa sababu wanashea misuli ya vichwa vyao, hivyo huachwa hivyohivyo,” alisema.

“Kundi la saba huitwa Pygopagus. Hili kundi watoto huwa wameungana kwenye makalio kwa nyuma, ni kundi jepesi kuwatenganisha, ila hadi kwa watalaamu,” alisema na kuendelea:
 
Sehemu ya 76

“Kundi la mwisho huitwa Rachipagus. Kundi hili watoto huwa wameungana makalioni kwa nyuma mpaka migongoni mwao. Ni vigumu kuwatenganisha kwa kuwa huchangia uti wa mgongo mmoja,” alisema daktari.

“Watoto wangu wapo kundi gani kati ya haya?”
“Hilo la saba!” alijibu daktari, John akashusha pumzi.

“Pygopagus?”
“Ndiyo! Wanaweza kutenganishwa, ila mpaka kwa watalaamu, kwa hapa Tanzania hatuna kwa sababu huwa na misuli mingi hapo kwenye makalio,” alijibu.

“Kwa hiyo wasafirishwe?”
“Ndiyo! Wapelekwe nchini India.” Huo ndiyo ulikuwa uamuzi wa hospitali hiyo, ilikuwa ni lazima watoto hao wasafirishwe na kuelekea nchini India kwa ajili ya kutenganishwa kama alivyoshauri daktari.

Kazi kubwa ambayo ilikuwa mbele ya John ni pesa za kuwasafirisha kwenda huko, aliuona ugumu mbele yake, hakuwa na pesa za kutosha, ilikuwa ni lazima atafute pesa hizo kama tu alitamani kuona watoto wake wakitenganishwa na kuwa tofauti.

Kwenye akaunti yake alikuwa na kiasi cha shilingi milioni saba ambazo alizidunduliza mpaka kufikia kiasi hicho ukiachana na milioni sita ambazo zilikuwa katika akaunti ya mkewe.

Hakujua ni kwa namna gani angeweza kupata kiasi kilichobaki. Alizungumza na daktari, alimwambia kuhusu ugumu uliokuwa katika kufanikisha kuzipata pesa hizo, na kitu pekee alichomwambia ni kutafuta msaada kwa wananchi.

“Niende nikaombe mitaani?” aliuliza John.
“Hapana! Taarifa itolewe kwenye magazeti, weka namba yako na watu wakitaka kukusaidia, watakusaidia,” alisema daktari huyo.

Hilo ndilo lililofanyika, siku iliyofuata haraka sana John akaondoka nyumbani na kuelekea katika ofisi za magazeti ya Nipashe na alipofika huko, akawapa habari hiyo, hivyo waandishi wakaondoka na kuongozana naye mpaka Muhimbili ili kupata uhakika wa kile alichokuwa amekisema.

Walipofika huko, wakaonana na daktari ambaye aliwaambia kweli watoto wa mwanaume huyo walitakiwa kusafirishwa mpaka nchini India ambapo gharama zake ingekuwa kiasi cha milioni hamsini na tano.
Huo ndiyo ulikuwa mwanzo wa kutoa taarifa hiyo gazetini mpaka Deborah kukutana na tangazo hilo na namba ya John na kumtafuta.
 
Sehemu ya 77

“Unaishi wapi?” aliuliza msichana huyo.
“Nipo Kijitonyama, ila muda mwingi nipo hospitali!” alijibu.

“Unamaanisha mkeo alijifungua mapacha walioungana ama nimesoma vibaya?” aliuliza Deborah, ukimya kidogo ukaingilia, Deborah akaita.

“Ndiyo! Mungu ametujalia watoto ila kwa mapenzi yake ikawa hivyo!” alijibu John, sauti yake tu ilisikika kama mtu aliyekuwa na maumivu makali.

“Naomba nije hospitali kukuona!”
“Sawa. Nitashukuru!” alisema John.
Simu ikakatwa na haraka sana msichana huyo kuelekea hospitali kuonana na John. Njiani alikuwa na mawazo tele, kichwa chake kilikuwa na mawazo, hakujua nini kingetokea mara baada ya kuonana na mwanaume huyo aliyempenda kwa moyo wa dhati ambapo ilipita miaka mingi pasipo kuonana.

Moyo wake ukaanza kurudi tena kwa John, akaanza kukumbuka mambo mengi yaliyowahi kutokea kipindi cha nyuma baina yake na John, akahisi yale mapenzi yakirudi kwa kasi na ni kama yalifufuliwa kwa kasi kubwa.

Baada ya dakika kadhaa akafika hospitali na kuanza kwenda alipoelekezwa na mwanaume huyo. Akafika huko, macho yake yalipotua kwa John tu, akahisi mapenzi mazito yakija moyoni mwake.

Akashindwa kuvumilia, akamkimbilia na kumkumbatia na kumwagia mabusu mfululizo. Hakutaka kujali kama kulikuwa na watu, alikuwa mke wa mtu na John alikuwa na mke, alichokijali ni kuuridhisha moyo wake tu.

“John!” alisema Deborah, kwa jinsi alivyochanganyikiwa kwa furaha, machozi yakaanza kumtoka.
“Naam Deborah!”
“Umekonda sana!” alisema msichana huyo.
“Ni matatizo!”

“Pole sana. Mungu ndiye anapanga kila kitu, imekuwaje kwani?” aliuliza msichana huyo.
Hapo ikabidi wote wakae kwenye benchi na kuanza kumsimulia kila kitu kilichokuwa kimetokea tangu walipoachana.

Deborah alikuwa kimya akimwangalia John, alimsikiliza kwa makini, kile alichokuwa akikizungumza kilimuhuzunisha na moyo wake ukakiri kwamba John aliletwa duniani kwa ajili ya kuteseka tu, hapakuwa na kitu kingine.
“Kwa hiyo inahitajika milioni hamsini na tano?” aliuliza Deborah.

“Ndiyo! Ila nina milioni kumi na tatu, kwa maana hiyo imebaki kama milioni arobaini na mbili!” alijibu John.
 
Sehemu ya 78

“Mh! Ni kiasi kikubwa sana, ila nitajitahidi nipate hata nusu yake,” alisema Deborah kwa sauti ndogo mno.

Haraka sana akachukua simu yake na kumpigia baba yake, alihitaji kumsikia katika hilo. Hakutakiwa kumficha, ilikuwa ni lazima amwambie ukweli kila kitu kilichokuwa kimetokea, jinsi John alivyokuwa na tatizo mpaka kufikia hatua hiyo.

Baba yake alimsikiliza kwa makini, alichokiamini ni kwamba angemsaidia ama kumpa kiasi chochote kile lakini kitu cha ajabu kabisa, mzee huyo akamkatalia.

“Baba! Yaani unashindwa kutoa hata milioni tano na pesa zote hizo ulizokuwanazo?” aliuliza Deborah huku akiwa na uchungu.
“Kwanza kwa nini umekwenda kuonana na John?” lilikuwa swali lake la kwanza.

“Mkewe ni mgonjwa!”
“Hilo jibu halijaniridhisha! Unahisi mume wako atajisikiaje akisikia umekwenda kuonana na mwanaume huyo?” aliuliza.

“Baba! Hayo yote yametoka wapi? Umesema hauna pesa, ninajua unazo ila hauna moyo wa kusaidia. Bado una chuki sana na John, sijajua kwa nini! Ila ninaamini nitamsaidia, nitauza hata kiwanja changu ila ni lazima nimsaidie!” alisema Deborah huku akionekana kumaanisha.

John alikuwa kimya, mawazo yalimjaa na alishangaa ni kwa namna gani baba yake alikuwa na hasira juu yake na wakati aliachana na Deborah kama alivyokuwa ametaka.

Alipomaliza kuongea naye, alimwambia John kila kitu, alichomwahidi ni kwamba angeuza kiwanja chake kilichokuwa Kilimahewa kwa lengo la kumsaidia.

“Ninashukuru sana Deborah! Ninashukuru sana,” alisema John huku akitaka kupiga magoti, msichana huyo akamzuia.

Walizungumza mengi na mwisho msichana huyo akaondoka zake. Akiwa njiani akakumbuka kuhusu Bwana Kinyora, meneja wa makao makuu ya kampuni yao ambaye alizungumza naye siku hiyo kuhusu ajira ya mumewe.
 
Sehemu ya 79

Aliamini kwa jinsi mwanaume huyo alivyokuwa na roho nzuri angeweza kufanya jambo lolote lile kwa ajili ya John. Akampigia simu na kuomba kuonana naye, halikuwa tatizo, mzee huyo akakubali na hatimaye kuonana na kuanza kuzungumza.

Alimuhadithia kwa uchungu kuhusu John, alihitaji kumwambia ukweli kwani ndiyo ilikuwa njia mojawapo ya kupata msaada kwa kile kilichokuwa kimetokea.

Mzee huyo alimsikiliza kwa makini mno, maneno aliyomwambia yalimgusa moyo wake, hakuamini kama kulikuwa na watu walikuwa wakipitia maisha ya mateso kama aliyokuwa akipitia mwanaume huyo.
“Pole yake sana! Wewe kama Deborah utajitahidi kutoa kiasi gani?” aliuliza mwanaume huyo.

“Nadhani milioni kumi!”
“Kwa nini udhani?”
“Kwa sababu nina milioni tano! Nitakwenda kuuza kiwanja changu kwa shilingi milioni tano, jumla nitakuwa na kumi!” alijibu.
“Kwa hiyo imebaki milioni thelathini na mbili!” alisema mzee huyo.

“Sawasawa!”
“Kwa kuwa sisi pia tuna mfuko wetu, nitaongea na wafanyakazi, hiyo pesa tutamsaidia tu ili mradi watoto hao watenganishwe! Nadhani Mungu atatulipa kwa wakati wake,” alisema Bwana Kinyora.

Ni kama Deborah hakuamini alichokuwa amekisikia, akahisi moyo wake kama ukichomwa na kitu kikali, haraka sana machozi yakaanza kumtiririka mashavuni mwake, hakujua kama yalikuwa machozi ya furaha ama uchungu.

Akajikuta akisimama na kumkumbatia mwanaume huyo. Alimpenda sana John, ni kweli alitenganishwa naye lakini hakutegemea kuona mwanaume huyo akipata mateso, alikuwa radhi kumsaidia kwa lolote lile.

Hasira yake ilikuwa kwa baba yake, alimchukia, hakuamini kama kweli mzee huyo alishindwa hataka kutoa milioni moja kumsaidia John, alikuwa na pesa nyingi lakini hakupenda kuambiwa lolote kuhusu mwanaume huyo.

Akarudi hospitalini, akaonana na John ambaye alimpa taarifa kuhusu michango ya wananchi ilivyokuwa ikiingia kwenye simu yake mfululizo.

Watu waliguswa na matatizo aliyokuwa akipitia, hilo lilimtia uchungu mno Deborah, kama watu ambao hawakumjua John, walimchangia ili watoto wake wasafirishwe na kupelekwa nchini India, ilikuwaje kwa baba yake ambaye aliwahi kuonana na mwanaume huyo na kuongea naye?
 
Sehemu ya 80

“Chuki dhidi ya baba yangu imeongezeka maradufu,” alisema Deborah.
Muda haukuwa rafiki, haraka sana akaondoka na kuelekea Kigoma kwa ndege, njia nzima alikuwa na majonzi tele, alijiuliza maswali juu ya hali aliyokuwanayo John lakini alishindwa kupata majibu.

Hakujua Mungu alikuwa na mpango gani kwake, alipitia matatizo makubwa mno, hakuwahi kupata furaha hata kidogo, kila alipokuwa akijiuliza kuhusu mwanaume huyo, moyo wake uliendelea kuwa na uchungu kupita kawaida.

Alipofika Kigoma, akaonana na wazazi wake, aliwaambia kuhusu roho mbaya waliyokuwanayo lakini hawakuonekana kujali kitu chochote kile kana kwamba huyo John aliwahi kuwafanyia jambo baya kupita watu wote.

“Mungu atawalipia kwa mabaya mnayofanya,” aliwaambia na kuondoka zake huku akiwa na hasira tele.

Mpango uliokuwepo ulikuwa ni kuuza kiwanja chake lakini asingeweza kufanya hivyo bila kumshirikisha mume wake. Usiku wa siku hiyo akamuita na kuongea naye, alihitaji ushauri juu ya kile alichohitaji kukifanya.

Jericho alimsikiliza mkewe, alivyokuwa akiongea alionekana kuguswa kwa kile kilichokuwa kimetokea. Alimwangalia Deborah, ni kweli alionyesha kuguswa na hali ya John na alihitaji kumsaidia kwa moyo mmoja.
 
Sehemu ya 81

“Pole sana! Kama tuna nafasi ya kusaidia! Tumsaidie,” alisema Jericho bila wivu wowote ule.

Wakati akizungumza hayo, simu ya Deborah ikaanza kuita, haraka sana akaichukua na kuipokea, ilitoka kwa Bwana Kinyora ambaye alihitaji kuzungumza naye.

“Mungu ni wa ajabu sana,” alisema mzee huyo kwenye simu, Deborah akawa na hamu ya kusikia ni kitu gani alitakiwa kuambiwa.
“Kwa sababu gani?”

“Nilizungumza na wafanyakazi, wamekubali kumsaidia John kwa pesa zao wenyewe, wakatwe kwenye mishahara yao,” alisema mzee huyo.

“Unasemaje?” aliuliza Deborah huku akiwa haamini alichokuwa akikisikia.
“Wamekubali! Wamesema watachanga kiasi cha shilingi milioni sitini kwa ajili ya John!” alisema mzee huyo.

“Un...as..ema..j..e..” Aliuliza Deborah, hakuamini alichokisikia, akaanza kulia hapohapo.

“Mungu ni mkuu Deborah! Kiwanja chako umeshakiuza?” aliuliza, Deborah hakujibu, alikuwa akilia kwa uchungu, hakuamini kile alichokuwa amekisikia.

Alibaki kwenye hali hiyo kwa dakika nzima ndipo akamwambia kwamba hakukiuza ila alizungumza na mumewe, wote wakakubaliana wauze kiwanja kwa lengo la kupata pesa hizo.
“Mumeo akakubali?”

“Bila kinyongo! Ndiyo nilikuwa nazungumza naye, wewe ukapiga simu!” alisema Deborah.
“Mungu ambariki sana. Ninakuhakikishia wiki hii ataanza kazi hapohapo Kigoma,” alisema mzee huyo, hapohapo akakata simu.
|
|

Je, nini kitaendelea?
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom