Sehemu ya 91
“Unaweza kuona huumwi kama watu wengine, mambo yako yanafanikiwa, kumbe bila kujua, Mungu anakulinda kwa sababu tu unatenda wema kwa watu wenye matatizo,” alisema John huku akianza kulengwa na machozi.
“Leo kuna watu wametusaidia bila kutujua! Wamesikia tuna matatizo, wametusaidia tu. Mtu anayekusaidia si lazima awe anakufahamu, na usitake kila unayemsaidia lazima umfahamu, hapana!
“Unapoguswa kumsaidia mtu fulani, saidia, usiangalie dini, kabila ama cheo cha mtu, kuna masikini wengi wana mahitaji, wasaidie, wengine wana nguo nyingi kabatini, wanajisifu kuwa na nguo lukuki, ni ajabu wanapopita mitaani wanawaona watu wana nguo zilizochakaa na bado hawawasaidii.
“Inawezekana kuna wengine mambo yenu hayafanikiwi kwa sababu hamsaidii watu, umesoma, una vyeti vimekaa tu ndani lakini hupati kazi, yote ni kwa sababu kwa kidogo ulichonacho hutaki kuwasaidia wasivyonavyo.
“Huu ndio moyo niliotaka sana kuuona kwa kipindi kirefu, nilihitaji kujua ulimwengu wa pili watu walikuwa wakiishi vipi.
Unapokuwa kwenye ulimwengu huu, watu wanakuchukuliaje! Sikuwahi kuishi maisha haya niliyokuwa nikiishi kwa miaka miwili, nilikuwa nayasikia tu kwa sababu nilizaliwa kwenye familia ya kitajiri, baba yangu ni bilionea.
“Kwenye maisha yake aliniambia kuna siku nitatakiwa nijifunze maisha ya upande wa pili, niwe na njaa kama wengine, niteseke ili siku mtu akija na kuhitaji msaada, basi nijue aliteseka kwa kiasi gani,” alisema John na kuwafanya watu kuwa makini kanisani hapo, si hao tu bali hata mke wake.
“Nilipokwenda India kwa ajili ya watoto wangu, baba na mama yangu walikuja kutoka nchini Australia wanapoishi na kufanya biashara zao.
Waliponiona, wakanisogelea na kunipongeza, waliniangalia machoni, sikuwa John yule wa kipindi cha nyuma, nilichakaa mno, nilikonda, hilo ndilo jambo ambalo walikuwa wakilitaka sana, kunifundisha mtoto wao maisha ya upande wa pili, jinsi masikini wanavyo...” alisema John, hakumalizia sentensi yake, akanyamaza na kuanza kulia.