Sehemu ya 81
“Pole sana! Kama tuna nafasi ya kusaidia! Tumsaidie,” alisema Jericho bila wivu wowote ule.
Wakati akizungumza hayo, simu ya Deborah ikaanza kuita, haraka sana akaichukua na kuipokea, ilitoka kwa Bwana Kinyora ambaye alihitaji kuzungumza naye.
“Mungu ni wa ajabu sana,” alisema mzee huyo kwenye simu, Deborah akawa na hamu ya kusikia ni kitu gani alitakiwa kuambiwa.
“Kwa sababu gani?”
“Nilizungumza na wafanyakazi, wamekubali kumsaidia John kwa pesa zao wenyewe, wakatwe kwenye mishahara yao,” alisema mzee huyo.
“Unasemaje?” aliuliza Deborah huku akiwa haamini alichokuwa akikisikia.
“Wamekubali! Wamesema watachanga kiasi cha shilingi milioni sitini kwa ajili ya John!” alisema mzee huyo.
“Un...as..ema..j..e..” Aliuliza Deborah, hakuamini alichokisikia, akaanza kulia hapohapo.
“Mungu ni mkuu Deborah! Kiwanja chako umeshakiuza?” aliuliza, Deborah hakujibu, alikuwa akilia kwa uchungu, hakuamini kile alichokuwa amekisikia.
Alibaki kwenye hali hiyo kwa dakika nzima ndipo akamwambia kwamba hakukiuza ila alizungumza na mumewe, wote wakakubaliana wauze kiwanja kwa lengo la kupata pesa hizo.
“Mumeo akakubali?”
“Bila kinyongo! Ndiyo nilikuwa nazungumza naye, wewe ukapiga simu!” alisema Deborah.
“Mungu ambariki sana. Ninakuhakikishia wiki hii ataanza kazi hapohapo Kigoma,” alisema mzee huyo, hapohapo akakata simu.
|
|
Je, nini kitaendelea?