Simulizi: Mke Wangu Juliana

Simulizi: Mke Wangu Juliana

Sehemu ya 122

John alisimulia mambo mengi ambayo alikutana nayo kipindi cha nyuma kabla ya kwenda mkoani Kigoma. Deborah na wazazi wake walikuwa wakishangaa, hawakuamini kama kweli kile alichokuwa akikizungumza kilikuwa kilichotokea maishani mwake ama alikuwa amekitunga.

Alionekana kuchoka, fukara asiyekuwa na kitu, ile stori iliyozungumziwa mbele yao ilionekana kama filamu fulani hivi ambapo baada ya muda wangeambiwa imemalizika.

Juliana alikuwa kimya, alimwangalia mume wake, hakuamini yote hayo aliyokuwa ameyasikia kutoka mdomoni mwake. Kumbe John hakuwa kama alivyofikiria, alikuwa mwanaume wa kitajiri aliyekuwa na maisha mazuri mno.

Alitamani kucheka, kulia kwa pamoja, hakujua ni kitu gani hasa alitakiwa kufanya kwa wakati huo. Mzee Abraham alikuwa akiangalia chini kwa aibu, hakujua ni kitu gani alitakiwa kufanya.

Alichoka, dharau zake zilimtokea puani kipindi hicho, alipoteza kila kitu kwa kuwa tu aliidhulumu serikali lakini aliamini hayo yote yalitokea kwa kuwa alimnyanyasa huyo John, kilichokuwa kikimshangaza zaidi, kumbe kampuni ambayo ilimfukuza kijana huyo ilikuwa yake!

“Nashukuru sana Deborah kwa kuniamini siku zote,” alisema John huku akimwangalia msichana huyo.

“Najua ulinipenda sana ila bahati mbaya wazazi wako hawakutaka uwe nami. Si kosa lako, kwenye maisha kuna mambo ambayo yanatokea kwa sababu ya makusudi ya Mungu. Huwezi kujua ni kitu gani kingetokea baada ya mimi kuwa na wewe, inawezekana Mungu akawatumia wazazi wako ili nisiwe na wewe, niwe na Juliana ambaye inawezekana kutokana na uvumilivu wake Mungu alimwandalia mwanaume kama mimi,” alisema John huku akimwangalia Deborah.

“Nimeishi Kigoma kwa miaka miwili, nimepazoea sana, ni kama nyumbani ila nitatakiwa kuondoka na kwenda kuishi Dar es Salaam! Umenitendea wema sana wewe na mumeo, naomba niseme kitu kimoja, kesho nitaita kikao ofisini, nitakutangaza kuwa meneja mkuu wa kampuni yangu,” alisema John huku akimwangalia msichana huyo.
 
Sehemu ya 123

Deborah akashtuka, hakuamini alichokisikia, ni kama alikuwa akiota vile, yaani mfanyakazi yeye wa kawaida kuchukua nafasi ya kuwa meneja badala ya mzee Masako, hakika ilikuwa ndoto ambayo hakuwahi kuiota hata siku moja.

“Najua elimu yako si kubwa sana kama mzee Masako, ila utatakiwa kuwa meneja na mzee huyo nitamfukuza kazi ama kumshusha chini, huwezi kuwa na kiongozi ambaye anawasikiliza watu wengine wampangie maamuzi ya kuwafukuza watu kazi,” alisema John na kuendelea:

“Baada ya kuwa meneja, utatakiwa kusoma, nitahakikisha unakwenda nchini Sweden kusomea japo kwa mwaka mmoja, kama utakwenda peke yako ama na mume wako, hakuna tatizo, nitahakikisha nasimamia kila kitu. Kama familia mtaamua nyie wenyewe,” alisema John na kuendelea:

“Sifanyi haya kwa sababu una akili sana, au mfanyakazi mkubwa, ninafanya haya kwa sababu ya wema wako, kama ubaya hulipwa hapahapa duniani basi hata wema nao hulipwa hapahapa!” alisema na kumgeukia mzee Abraham.

“Najua ni kwa namna gani umeghafirika sana, umechanganyikiwa, umekonda kupita kawaida. Ni maisha, huwa tunapita katika matatizo mengi sana. Na katika hili ninaamini utakuwa umejifunza sana. Unadaiwa bilioni mbili na TRA, nakuahidi nitazilipa.

Ni kiasi kikubwa lakini nitajitahidi hata kulipa kidogokidogo na mwisho upate kila kitu chako kilichochukuliwa!” alisema John na kuendelea:
“Sifanyi haya kwa kuwa umestahili sana, ninafanya kwa sababu ninataka kuwaonyesha watu kwamba tunaweza kulipa ubaya kwa wema, lakini pia ninafanya hivi kwa ajili ya binti yako.

Ninahitaji kumuona akifurahia, yeye kuwa meneja huku baba yake akiwa kwenye hali mbaya, umeneja hauwezi kumpa furaha maishani mwake. Ninahitaji afurahie kila kitu na ndiyo maana nimeamua kufanya hayo yote,” alisema John.

Mzee Abraham alikuwa kimya, kile alichoambiwa hakikuaminika masikioni mwake, macho yake yakaanza kuwa mekundu na baada ya sekunde kadhaa machozi yakaanza kumtitirika.

Maneno aliyoongea John yalikuwa makubwa, yenye faraja lakini kwa msaada aliokuwa ameutoa kwake na kwa binti yake hakika hakuwa na uwezo wa kulipa wema huo hata siku moja.
 
Sehemu ya 124

Pale kochini alipokaa, akajikuta akisimama na kutaka kupiga magoti mbele ya John, haraka sana mwanaume huyo akamuwahi na kumuinua na kumuomba kutofanya hivyo.
“Ni Mungu pekee ndiye anayetakiwa kupigiwa magoti,” alisema John.

Mzee Abraham alitamani kuongea lakini kilio kilikuwa kifuani mwake, akashindwa kuufumbua mdomo wake kuzungumza kitu chochote kile.

Mke wake naye akasimama, akamsogelea John na wote kukumbatiana kwa kile alichokuwa amekifanya kwa familia hiyo.

Baada ya dakika kadhaa, John na familia yake wakaaga, wakaondoka nyumbani hapo na kuelekea walipokuwa wamepanga. Muda wote huo Juliana alikuwa na maswali mengi, alikuwa akijiuliza kuhusu mume wake, ni kwa namna gani hakuwahi kumwambia kuhusu maisha yake halisi na wakati aliona kabisa walivyokuwa wakipigwa na maisha.

Hilo akabaki nalo moyoni mwake lakini baada ya kufika nyumbani tu, kitu cha kwanza kilikuwa hicho. Kabla ya kujibu John akatoa tabasamu pana, akamsogelea mke wake na kumshika mikono.

“Nilikuwa natafura mwanamke atakayenipenda kwa jinsi nilivyo!” alijibu John.
“Lakini tayari tulioana, kwa nini hukuniambia?”

“Kuoana si tatizo! Unaweza ukaoa, baada ya mwanamke kuona anateseka, anakimbia ndoa, hutokea kwa watu wengi sana, mnakubaliana kuishi kwenye shida na raha, ila shida zikiongezeka tu, wanakimbia,” alijibu John.
“Nakupenda mume wangu!”
“Nakupenda pia!” alisema John na kukumbatiana.

Siku iliyofuata John akajiandaa na kwenda katika kampuni yake, alipofika huko, kwanza mlinzi akataka kumzuia lakini kwa jinsi mwanaume huyo alivyokuwa amevaa, alionekana kuwa tofauti na siku nyingine, akaamua kumuacha tu.

Alikwenda mpaka mapokezi, sekretari alipomuona, alishtuka, hakuamini kumuona mwanaume huyo kwa mara nyingine tena, huku akiwa na muonekano mwingine kabisa.
“Agnes! Nahitaji kumuona bosi!” alisema John huku akimwangalia dada wa mapokezi.

“Haina shida! John! Mbona umebadilika?” aliuliza Agnes huku akimwangalia mwanaume huyo.

“Nimepata bingo!”
“Hahaha! Bingo gani tena na wewe?” aliuliza.
 
Sehemu ya 125

John hakujibu zaidi ya kutoa tabasamu tu. Agnes akachukua simu yake na kupiga mpaka kwa sekretari wa meneja wake na kumwambia kulikuwa na mgeni alifika mahali hapo kwa lengo la kuonana na mzee Masako.

Hakumwambia alikuwa mgeni gani ila akakubaliana naye na kwenda huko. Alipofika, naye sekratari akashangaa, hakuamini kumuona mfagia ofisi akiwa amerudi tena ofisini hapo akiwa na muonekano mwingine kabisa.

“John! Ni wewe ama naota?” aliuliza msichana huyo.
“Ni mimi Upendo! Mzima lakini?” alijibu John na kumjulia hali.
“Wa afya tele!”

“Ofisi yenu haikunitaka tena kisa demu!” alisema John huku akicheka.
“Hahaha! Eti kisa demu! Halafu si unajua Deborah aliolewa?” “Ndiyo! Na mbaya zaidi hata hamkunialika nije kula ubwabwa! Mna roho mbaya sana nyie,” alisema John na wote kuanza kucheka.

Walipiga stori kwa dakika chache na kumwambia kilichompeleka mahali pale. Alihitaji kuonana na mzee Masako, kwanza msichana huyo alisita kumruhusu kwa kuwa alimfahamu mzee huyo, alikuwa mtu wa lawama, hakupenda kuona akifanyiwa kitu ambacho hakupenda kufanyiwa.

“Usiwe na hofu Upendo!” alisema John baada ya kumuona msichana huyo akionekana kuwa na hofu.
“Basi subiri!” alisema.

Akachukua mkonga wa simu na kumpigia mzee huyo, aliposikia John ndiye aliyefika mahali hapo, haraka sana akatoka ndani na kumfuata hapohapo mapokezi, hakutaka hata kuingia ofisini kwake.
“John! Umefuata nini?” aliuliza mzee huyo bila hata salamu.

“Kukusalimia tu mzee wangu! Shikamoo!” alisema John, alisimama na kumpa mkono huku akitoa tabasamu.

“Marahaba! Nikusaidie nini? Au umekuja kunitambia kwamba maisha yako yamekuwa mazuri?” aliuliza mzee huyo huku akimwangalia John kuanzia juu mpaka chini.

“Hapana mzee! Tunaweza kuingia ofisini tukaongea mara moja?” aliuliza John huku akimwangaliaangalia Upendo kumaanisha kitu alichotaka kuzungumza hapo msichana huyo hakutakiwa kusikia.

“Hapana! Tuongee hapahapa! Nipo bize kidogo!”
“Bosi! Naomba tu tuongee kidogo ndani!” alisema John.
“Kuna ishu gani hasa?”
 
Sehemu ya 126

“Ya muhimu sana! Nikuombe msamaha pia, ikiwezekana unirudishe kazini! Nilikwenda kusoma, nadhani sasa naweza kupata ngazi ya juu kidogo!” alisema John huku akitabasamu.
“Kupata kazi hapa?”
“Ndiyo!”

“Cha kwanza hilo haliwezekani! Cha pili zungumza hayo mengine!”
“Mzee Masako......”
“Zungumza hapahapa!” alisema kwa hasira kidogo.

“Utakuwa huru?”
“Haina shida! Wewe zungumza!”
Wakakaa kwenye kochi, mzee Masako alikuwa akimwangalia John, hakujua alibadilikaje kipindi hicho, alimshangaza kupita kawaida.

John akaanza kuzungumza naye, kitu cha kwanza kilikuwa ni kumpa tahadhali juu ya maamuzi aliyokuwa akiyafanya, kumfukuza mtu kazi kwa sababu tu aliambiwa na mtu fulani kufanya hivyo.

“Kwa hiyo umekuja kuninanga na kunifundisha kazi?” aliuliza mzee huyo kwa ukali kidogo.
“Hapana! Nimekuja kukupa taarifa moja tu!” alisema John.

“Taarifa gani?”
“Subiri!” alisema.
John akatoa simu yake na kumpigia Deborah na kumuhitaji kufika mahali hapo. Ni ndani ya dakika moja, msichana huyo alifika hapo, kitu cha kwanza alichokitamka baada ya kumuona John ni neno ‘Bosi’.

Mzee Masako alibaki akishangaa, hakujua kilichokuwa kikiendelea. John hakutaka kuzungumza lolote lile, alimwambia Deborah amwambie kila kitu kilichokuwa kikiendelea, na mwisho wa siku amwambie zaidi kuhusu mpango wa mkurugenzi juu ya mzee huyo, alipomaliza, akaondoka zake.

Deborah akabaki kimya kidogo, alimwangalia mzee huyo, alionekana kuwa na hofu lakini hakuwa na jinsi, akaanza kumwambia yote kuhusu huyo John, mwanaume ambaye alimfukuza kazi kwa kuwa aliambiwa na baba yake kufanya hivyo.

Mzee Masako alitulia akimsikiliza Deborah, kulikuwa na kiyoyozi lakini kwa maneno aliyokuwa akiambiwa, akaanza kuweweseka na kijasho chembamba kuanza kumtoka, alichoambiwa kilikuwa kama ndoto.
“John ndiye mwenye kampuni hii?” aliuliza mzee Masako.

“Ndiyo!”
“Mzee huyo hakutaka kukubali, haraka sana akarudi ofisini kwake na kuangalia management nzima ya kampuni hiyo, alichoambiwa alihisi ni sahihi kwani mkurugenzi wa kampuni hiyo alijulikana kwa jina la Josephat Malecela.

“Deborah! Njoo mara moja,” alisema mzee huyo, haraka sana Deborah akafika ndani ya ofisi hiyo.
“Huyu anaitwa John nani?”
 
Sehemu ya 127

“John Malecela!”
“Mungu wangu!” alisema mzee huyo na kukaa kwenye kiti.

Aliona dunia yote ikiwa imemgeuka, hakuamini alichokuwa akikiona, aliuona mwisho wa maisha yake ukiwa umefika, kwa kile alichokuwa amemfanyia John aliamini kabisa angechukua uamuzi wa kumfukuza kazi.

Alijuta, alitulia kwenye kiti chake, alihisi kabisa presha ikianza kupanda mpaka Deborah kuanza kuogopa. Ilipofika majira ya saa saba mchana muda wa chakula kukawa na kikao cha wafanyakazi wote.

Wakaitwa na mtu ambaye aliyehitaji kuzungumza nao alikuwa John. Wote walishtuka na baada ya kujitambulisha wakashangaa, hawakuamini kama mwanaume huyo ndiye alikuwa mkurugenzi wa kampuni hiyo.

Alianza kuongea nao, aliwashukuru kwa yote yaliyokuwa yakiendelea ndani ya kampuni hiyo, jinsi wafanyakazi walivyokuwa wakijitoa kufanya kazi usiku na mchana. Alimshukuru kila mmoja ambaye alijitahidi kuiendeleza kampuni hiyo mbele zaidi.

Baada ya kuongea mengi, akawaahidi kitu kimoja kwamba ni lazima aboreshe mishahara yao zaidi, kwenye mambo mengi aliyoongea, hilo likawafanya watu wote wapige makofi na kushangilia.

“Nitazungumza nanyi zaidi. Ila ofisi inafikiria kuwashusha baadhi ya wafanyakazi na kuwapandisha vyeo baadhi ya wafanyakazi. Naomba tuvumiliane kwa mabadiliko yoyote yatakayotokea,” alisema John na kufunga kikao, wafanyakazi wakatakiwa kwenda kuendelea na kazi zao.

**** John na familia yake hawakukaa mkoani Kigoma, walichokifanya baada ya siku kadhaa ni kurudi jijini Dar es Salaam na kuanza maisha yao upya,

Siku ambayo walifika nyumbani hapo Juliana alibaki akishangaa tu, hakuamini kama yeye ndiye ambaye aliolewa na mwanaume aliyekuwa akimiliki jumba kubwa na la kifahari kama lile alilokuwa akiliona mbele yake.

Alibaki akiliangalia tu, hakuamini, kwa mwendo wa taratibu akamsogelea mume wake na kumkumbatia, hatimaye masikini yeye, mwanamke aliyekuwa kwenye maisha ya kimasikini kama yeye alikuwa akitarajiwa kuishi katika jumba hilo la kifahari.

John alimwangalia Juliana, alimpenda, kwake alijivunia kuwa na mwanamke mzuri kama alivyokuwa mwanamke huyo.

Alibaki akitabasamu na mara zote alitamani kumwambia ni kwa namna gani alimpenda, alimthamini kuliko mwanamke yeyote katika dunia hii.
 
Sehemu ya 128

Kwenye eneo la maegesho ndani ya nyumba hiyo kulipaki magari ya kifahari, ya gharama kubwa ambayo yalimfanya mwanamke huyo kupigwa na mshangao kupita kawaida.

John akamchukua na kumpeleka ndani. Mwanamke huyo alipoingia, alizidi kuchanganyikiwa, kwenye kila kitu alichokuwa akikiona ndani ya nyumba hiyo kilimfanya kutokuamini kwamba hatimaye alikuwa akitarajia kuishi humo.

Maisha yalianza ndani ya nyumba hiyo, waliamua kusahau kila kitu kilichokuwa kimetokea. John hakuridhika, alitamani kuwa na utajiri mkubwa, alifungua biashara nyingine nyingi zilizomuingizia kiasi kikubwa cha pesa.

Alikuwa kijana mdogo lakini mwenye mafanikio makubwa. Alihitaji mwanamke ambaye angempenda kwenye maisha yake ya shida aliyokuwanayo, akampata huyo Juliana ambaye alimuahidi angeishi naye mpaka siku wanaingia kaburini.

Watoto wao wazuri waliendelea kukua bila matatizo kabisa. John akawa na daktari wa familia ambaye kila siku alikuwa na jukumu la kufika nyumbani hapo na kuwaangalia watoto hao wadogo.

Kwa upande wa Deborah, aliendelea na maisha yake, kuna wakati mwingine alikuwa akiwalaumu wazazi wake moyoni kwa kuwafanya kutokuwa na John lakini pia kuna wakati mwingine alimshukuru Mungu kwa kuamini kila kitu kilichokuwa kimetokea kilikuwa katika mipango yake.

Yeye na mume wake waliishi kwa furaha na upendo, walipendana mno. Maisha ya Deborah yalibadilika na hata siku ambayo alitakiwa kuanza kazi kama meneja wa kampuni hiyo, hakuamini, alikikalia kiti, akayafumba macho yake na kuanza kumshukuru Mungu.

Ili kuonyesha hakuwa na tatizo lolote wala kisasi, John akamuhamisha mzee Masako na kwenda kusimamia kampuni yake iliyokuwa jijini Mwanza, akamlipa mshahara mzuri ila kitu ambacho alimtahadharisha ni kuwachukia watu wengine kwa sababu ya cheo chake.

“Kuna watu wenye sifa nyingi kama zako, ni kitendo cha kuwaita tu, wakaja na kufanya kazi, ila ninaamini bado wewe ni binadamu na unaweza kubadilika,” alisem John, alikuwa akizungumza na mzee Masako aliyekuwa upande mwingine wa simu.

“Nashukuru kwa nafasi nyingine bosi!”
“Usijali!” alisema John na kukata simu.
 
Sehemu ya 129

Stori ya maisha yake ikawa gumzo Kigoma nzima, hapakuwa na watu waliokuwa wakiamini kwamba yule kijana aliyekuwa akiishi kwenye maisha ya kimasikini, John alikuwa tajiri kama alivyokuwa.

Wapo waliokuwa wakibisha ambao walichukuliwa na kupelekwa mtaani kwake ambapo huko watu waliwajibu kwamba ni kweli kile walichokuwa wakikisikia ndicho kilikuwa ukweli wenyewe.

Wengi walibadilika, waliokuwa na dharau dhidi ya watu masikini wakaanza kuwaheshimu watu hao kwani waliamini kama mzee Masako ilimtokea yale yaliyomtokea basi kulikuwa na uwezekano hata wa kuwatokea wao.

Maisha yake yaliwabadilisha watu wengi. Vijana wengi wakajifunza, mabosi wakabadilika, masikini wakaheshimiwa. Kuanzia mwaka 2017 ambapo John alianza kuishi mkoani Kigoma, mpaka leo hii historia ya maisha yake ilibaki kuwa vichwani mwa watu wengi.

MWISHO.

Asanteni kwa kuwa nami toka mwanzo mpaka mwisho wa story hii na kuvumiliana na arosto za apa na pale

Mwisho wa story hii ndio mwanzo wa story nyingine nyemo chilongani na shunie tunawapenda sana

Tuendelee kumuunga kijana mkono kwa kununua vitabu vyake no ya simu hii 0718 069269 piga mda wowote
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom