Simulizi: Hujuma, Sehemu ya Kwanza (1) Bahari ya Hindi

kapingili

Senior Member
Jul 4, 2012
155
192
IMEANDIKWA NA: RICHARD MWAMBE
Simulizi: Hujuma
Sehemu Ya Kwanza (1)
Bahari ya hindi

MANOWARI ya kijeshi kubwa kabisa ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania kikosi cha wanamaji cha Kigamboni ilikuwa ikikata maji kwa kasi, ikitokea Tanzania kuelekea Urusi. Ilikuwa ni safari ya kusafirisha makombora kumi na mbili ya kisasa, makubwa yenye nguvu, makombora ya kisasa ambayo Urusi na Tanzania zilishirikiana kuyaunda ndani ya ardhi ya Tanzania. Kiwanda kikubwa kilikuwa kimejengwa maeneo ya pwani ya Mtwara eneo la Msanga mkuu, maalum kwa kazi hiyo.

Baada ya uchunguzi wa muda mrefu uliochukua takribani miaka kumi na tano hatimaye wataalamu wa milipuko wa jeshi la Urusi na wale wa Tanzania walikuwa wamekamilisha kuunda makombora hayo yenye nguvu aina ya R-36 ambayo teknolojia yake ni ya kule Urusi tangu miaka mingi ‘Intercontinental ballistic missile’, yenye urefu wa mita 32.2 (futi 106) na kipenyo cha mita 3.05 (futi 10), linaloweza kusafiri kwa kasi ya kilomita isiyopungua 7.9 kwa sekunde. Ni makombora yanayokwenda kasi ya ajabu na yenye mlipuko usio wa kawaida. Baada ya kuundwa katika kituo hicho maalum huko Msanga mkuu, Mtwara, sasa yalikuwa yakipelekwa kwa majaribio katika jangwa kubwa la Ryn lililoko Kusini Mashariki mwa Urusi, Maghalibi mwa Khazakistan, Kaskazini mwa bahari ya Caspian. Manowari kubwa ya Tanzania Kirov Class yanye urefu wa futi 827 iliyotengenezwa kati ya miaka ya 1970 na 1990 huko Urusi na kuiuza kwa serikali ya Tanzania ndiyo ilifanya kazi hiyo ya kubeba makombora hayo makubwa kumi na mbili kuyapeleka huko bahari ya Caspian kwa majaribio.

Wanamaji waliokuwa ndani ya meli hiyo walikuwa wakiendelea kula raha kwa kucheza michezo mbalimbali kama bao, karata, draft na mingineyo mingi huku manaodha nao wakiwa kwenye kebini yao wakabadilishana mawazo. Wengi wa wanamaji hao walikuwa kutoka Tanzania na wacahache walikuwa kutoka Urusi, jumla yao ilikuwa ni kama ishirini na tano hivi. Ilikuwa ni wakati wa pekee wa wapiganaji hawa kubadilishana uzoefu wa kazi yao, ukiachilia wanamaji hao pia kati yao kulikuwa na wataalam wa milipuko nao walikuwamo. Siku hizo kulikuwa na wimbi kubwa la utekeji meli za mizigo, mafuta na nyinginezo katika bahari ya Indi hasa eneo la Somalia.

Usiku wa manane kila mtu akiwa kasinzia katika lile saa la shetani yaani saa nane kwenda saa tisa, kila mmoja alijibwaga ndani ya kitanda chake akiwa kabebwa na usingizi wa ajabu, kwa kuwa chombo hicho kilikuwa kikijiongoza kwa mitambo maalumu ya kompyuta hakikuwapa tabu waongozaji kujipumzisha japo kwenye viti vyao.
Mara ghafla kioo kikubwa katika chumba cha nahodha kilipasuka na kumwagika sakafuni, nahodha mmoja alishtuka kwa kelele za kioo hicho na upepo mkali ulikuwa ukiingia ndani ukipeperusha karatasi huku na kule, wasaidizi wa nahodha huyo nao wakaamka lakini kabla hawajakaa sawa, mmoja alibamizwa ukutani alikuwa amerushwa kwa risasi nzito ya mdunguaji, damu ikaanza kumwagika, kabla nahodha hajaminya ile nobu ya kengele ya hatari, naye alijikuta chali kifua chote kikiwa fumu kwa risasi nyingine ya mdunguaji.

Msaidizi mmoja aliyebaki akaona isiwe tabu akaamua kutimua mbio kutoka chumba cha nahodha ili kuwahi mlango wa kuingia ndani ambako wengine walikuwa wamelala, alipotoka tu kwenye deki akajikuta akimulikwa na mwanga mkali sana uliomfanya ajizibe macho asiweze kuuona. Helkopta kubwa ya kijeshi ilikuwa angani si mbali sana na uwanja wa meli hiyo ambao uliweza kuruhusu helkopta kama hiyo kutua juu yake, alipotaka kukimbia tena la haikuwezekana, alitunguliwa risasi ya mgongo na kujibwaga chini kwa kiwewe kilichomshika akakimbia na kujitumbukiza baharini, lile helkopta likashuka taratibu na kukanyaga sehemu ya juu ya manowari hiyo.

Giza nene likaivamia meli hiyo ghafla, kila mtu akashtuka ndani ya meli hiyo na kukurupuka kujiweka sawa kujua kulikoni, wamechelewa. Kila kona kulikuwa kumetanda watu walioficha nyuso zao wakiwa na silaha nzito za kisasa za kivita, walikuwa ni wengi maana mara tu baada ya ile helkopta kutua zilifuata boti nyingi ziendazo kasi zikaizunguka manowari ile, Maharamia. Kiongozi wa wale maharamia akatoa amri ya kuikagua ile manowari, na kuhakikisha kila binadamu mwenye uhai anateremshwa.

Wale wapiganaji wote wakatolewa nje na kuwekwa mstari mmoja huku wakimulikwa na taa kubwa la ile helkopta.
“Karibuni sana Somalia, hii ndiyo Pwani ya Shetani, asikwambie mtu, hapa kila goti litapigwa,” yule Kiongozi alikuwa akiongea kwa kujigamba huku mkononi mwake amekamata bunduki kubwa yenye kilo nyingi, usoni akiwa kijifunika na soksi jeusi ili hasionekane uso wake, akatoa amri myingine na wale wafuasi wake wakawafunga kamba wale wapiganaji na kuwavisha kila mmoja soksi usoni baada ya kuwavua makombati waliovaa juu. Kishapo wakawapakia kwenye boti zao na kuondoka nao eneo lile. Maharamia wanaojua kuongoza vyombo kama hivyo waka shika usukani wa Manowari hiyo kubwa kabisa na kuigeuza kuipeleka pwani ya Somalia, Mogadishu.

MOGADISHU
Maharamia waliwafikisha mateka wao katika pwani ya Mogadishu na kuwashusha wakiwaswaga mpaka kwenye malori yaliyokwisha andaliwa kisha wakaondoka nao kuelekea kusikojulikana.
Alkadhalika, ile manowari nayo ilifikishwa Mogadishu na mara moja usiku ule ule ilianza kazi ya kupakuwa yale makombora na kuyaficha kwenye ghala kubwa lililojengwa chini ya maji karibu kabisa na bandari kuu ya Mogadishu, yalifichwa hivyo ili kama wakija kuwakomboa wenzao basi waikute meli tupu kisha wale maharamia nao wakaondoka eneo lile.

Jamhuuriyadda Federaalka Soomaaliya, ‘Jamhuri ya Shirikisho la Somalia’, ni nchi iliyoko katika pembe ya Afrika, sehemu kubwa upande wa Mashariki ni bahari ya Indi. Somalia ni nchi iliyokuwa katika mapigano ya wenyewe kwa wenyewe kwa kipindi kirefu na vikundi mbalimbali vya kigaidi kama Al-Shabab walitokea ndani ya nchi hiyo kutokana na tofauti za kisiasa.

Wimbi la utekaji vyombo vya majini liliibuka katika pwani ya nchi hiyo na kulaaniwa na kila taifa, kila serikali, kila taasisi ya kibinadamu duniani zikitoa wito kwa mataifa makubwa kukomesha uharamia huo.
Ilikuwa ni vigumu sana kutimiza lengo hilo la kukomesha wimbi la utekaji vyombo vya majini, haikujulikana sababu ni nini hasa ya kushindikana kwa juhudi hizo. Ilikuwa ni kitendawili kisicho na mteguaji. Hali kwa ujumla ilikuwa ni ya kuogofya katika eneo hilo, maharamia wa Somalia walikuwa hawaogopi hata sheria za maji makubwa, wao walichojua ni kuteka meli ilimradi wapate pesa, ukiwaona maharamia hao wanavovaa utasema ni masikini wakutupwa, lakini majumba hayo wanayomiliki ndani ya mji wa Mogadishu na viunga vyake ni kufuru kwa nchi hiyo isiyo na serikali kwa kipindi kirefu, kila mtu akiwa anajiamulia madaraka yake mkononi.


Jazeera Palace Hotel
Saa 2:10 asubuhi

Pembezoni kabisa mwa barabara ya Uwanja wa ndege ‘Airport road’,gari aina ya Jaguar nyeusi ilikuwa ikikunja kona kuingia katika hoteli ya Jazeera Palace asubuhi hiyo, moja kwa moja ikaingia katika maegesho na kuegeshwa sawasawa kabisa. Bwana mmoja wa makamo akateremka kutoka katika katika gari hiyo ya kifahari na kuuendea mgahawa wa hotel hiyo akachagua siti moja na kuketi. Haikupita hata dakika tano akaja mtu mwingine mnene kiasi mwenye upara unaong’aa ulioonekana wazi baada ya kuvua ile balaghashia yake na kuiweka mezani.
“Nipe habari,” yule bwana mwenye upara akamwambia Yule mwingine.

“Kila kitu tayari mzigo tunao, kilichobaki ni kuhesabiana tu, sisi wenyewe tunajua jinsi ya kuifikisha mahali husika,” alijibu bwana Shalabah, kiongozi wa maharamia. Ilikuwa ni biashara kubwa ya pesa nyingi za kigeni, nah ii ndio hasa waliokuwa wakiifanya maharamia hawa, safari hii walikuwa wamefanya biashara kubwa ya makombora hayo mazito.
“Ok, hatuna muda wa kupoteza, pesa iko tayari lini?” bwana Shalabah alimuuliza Yule mwenye upara.
“Pesa, pesa kitu gani? Kama wewe tayri una mzigo basi pesa utapata,” Yule mwenye upara alijibu.
“Kuna makombora 12, yenye uzito wa hali ya juu, ukipiga New York mpaka Ontario watatetemeka kwa hofu,” bwana Shalabah alimweleza Yule mwenye upara umadhubuti wa makombora hayo.

“Umenishtua sana, usijali nitwasiliana na washika dau ili tuyachukue yote 12 tuyapeleke huko maskani, sasa yako wapi japo niyaone,” Yule mwenye upara akamwambia Shalabah. ”Huwezi kuyaona, na wala hutakiwi kujua yako wapi, unachotakiwa kufanya wewe ni kuwasiliana na watu wako ili tufanye biashara, basi, hakuna kingine,” Shalabah alimueleza. Kisha akavuta mkoba wake na kufungua, akatoka kijitabu Fulani wakaandikiana mawasiliano yao na kisha wakaagana, kila mtu akachukua hamsini zake.

Shalabah akaikunja miguu yake na kuiweka kwa mtindo wa nne na kuagiza kinywaji kikali, alipoletewa alikuwa akinywa taratibu akisubiri miadi mingine, mara hii ya watu wake. Haikupita hata saa moja vijana watatu warefu, wembamba wakaingia na land cruiser pick up, wakateremka na kuungana naye katika kinywaji hicho.
“Mmekuja?” akawauliza wakati akiwaona.
“Ndio, mkuu, tumeitika wito,” wakajibu
“Sasa, nimeona kazi mliofanya, hongereni sana, lakini kama kuna jambo nataka kuwaambia ni kuimarisha ulinzi pale gahalani, silaha za safari hii hawa jamaa hawatakubali zipotee hivihivi lazima watakuja, hivyo muweke ulinzi wa kutosha kwa maana jamaa wako tayari na wanataka kuchukua mzigo wote kwa pesa iliyotakata sana. Mimi jioni ya leo nitakwenda kuonana na Top ili tuone mgao wenu mpaka hapa mlipofanikisha unakuwaje,” Shalabah alikuwa akiwaeleza wale vijana mpango ulivyo kwa ujumla.
Maharamia hawa walikuwa tayari kufanya biashara ya makombora hayo na kikundi kimoja kinachoendesha mapigano yasiyokoma huko katika jangwa la Pakistan mpaka Afghanistan, kutokana na kuishiwa na silaha nzito waliingia mkataba na maharamia hawa ili wawatafutie silaha nzito na zenye nguvu ili kuwaadabisha mahasimu wao, safari hii wakazipata. Pesa waliokubaliana kuyanunua ilikuwa ni pesa ambayo inaweza kulisha Tanzania nzima kwa miezi kumi na moja kwa milo mitano ya mlo kamili kwa kila mwananchi bila kujali mtoto au mtu mzima. Ilikuwa ni biashara haramu kuliko haramu yenyewe.

Mr SHALABAH aliendelea kuketi pale alipoketi mara baada ya kuiachana na wale vijana wake, akiwa katika kuburudika na kinywaji chake mara akajikuta hayupo peke yake katika meza hiyo, mbele yake kulikuwa na kijana mkakamavu aliyevalia suruali ya jeans na shati jepesi, usoni akiyaficha macho yake kwa miwani nyeusi iliyomkaa sawia.
“Biashara imeenda?”Shalabah akauliza.
“Kama kawaida, hakuna kinachoharibika hapa,” Yule kijana akajibu.
“Ok, mzigo uko kamili?” Shalabah akarusha swali lingine.
“Mzigo hauna shaka, uko sawa, mmetusaidia sana na mapinduzi yanaendelea,” Yule kijana akajibu. Akaisukuma briefcase ilikuwa chini kwa mguu wake wa kushoto, ikamgusa Shalabah, Shalabah akaitazama na kuiinua akaiweka mezani, akaifungua na kuchungulia kidogo, manoti ya dola za kimarekani yalikuwa yamejipanga kwa mtindo wa kupendeza, akatabasamu na kutikisa kichwa. Akaingiza mkono katika mkoba wake mdogo na kutoa kamashine kadogo, akabofya hapa na pale akatoa kijikaratasi Fulani na kukiweka saini kisha akampa Yule kijana na kuagana naye. Alipohakikisha amepotelea nje, akanyanyuka na kuibeba ile briefcase naye akaielekea gari yake aina ya Jaguar aliyoiacha kwenye maegesho na kuondoka kwa kasi katika hoteli hiyo.

Ndani ya mji wa Mogadishu. Jumba hilo ambalo nyuma yake lilikuwa limepakana na bahari ya Indi lilikuwa limejitenga na majumba mengine, lilikuwa mbali kabisa na makazi. Shalabah alikunja kona na kulifikia geti kubwa la jumba hilo, na mara lile geti likafunguka lenyewe na kuruhusu Shalabah aingie, akakanyaga mafuta kuifuata barabara inayoelekea katika jumba hilo ambalo lilijengwa umbali wa kilomita moja kutoka getini, aliegesha gari yake katika eneo maalumu, akashuka na ile briefcase mkononi na kuelekea mlango mkubwa wa jumba hilo. Vijana wawili wenye bunduki kubwa zenye nguvu walikuwa wamesimama katika mlango huo, mmoja huku na mwingine kule, walimkagua Shalabah na kuhakikisha hana silaha yoyote mwilini mwake, wakamruhusu kuingia ndani ya jumba hilo.

Jumba lote lilikuwa kimya kabisa, ni viatu vya Shalabah tu vilivyokuwa vikisikika wakati huo, akapanda ngazi kuelekea juu mpaka ghorofa ya kwanza, akapita tena katika korido ndefu iliyopambwa kwa sakafu na kuta za mbao safi ambazo polishi iliyopakwa na kung’aa sawia ilikufanya mpitaji ujione pande zote nne. Baada ya milango kama sita hivi, Shalabah alifika katika mlango wa saba akageuka na kuutazama, kulikuwa na kidubwasha chenye tarakimu tisa, akabofya tarakimu hizo kwa mtindo anaoujua yeye na mara ule mlango ukafunguka, Shalabah akaingia ndani ya kijichumba hicho kidogo na ule mlango ukajifunga, kisha kile chumba kikaanza kuteremka chini, kikaiacha ile mandhari ya mbao na kubaki kioo tupu, Shalabah aliweza kuona samaki aina mbalimbali na mandhari nzuri ya chini ya bahari, mara kile chombo kikaingia tena katika mandhari nyingine ya mbao zenye kung’aa kama zile za mwanzo, mara ikasikika sauti Fulani ikabip, ule mlango ukafunguka na Shalabah akateremka na kuifuata njia nyingiine ndefu mbele kulikuwa na mlango mwingine, ukafunguka kabla hata ya kuugusa, akaingia na kujikuta kwenye sebule pana yenye vitu vya thamani sana.

“Karibu Mr Shalabah,” sauti ilimkaribisha. Shalabah akaketi katika moja ya viti vilivyomo katika sebule hiyo. Mbele yake katika ukuta kukajitokeza luninga kubwa ‘flat’ na hapo aliweza kumuona Yule anayeongea naye.
“Ndiyo Mr. Shalabah, nipe ripoti kwa ujumla,” Yule mtu kwenye ile screen alimwambia Shalabah. Shalabah alitoa taarifa kamili ya mchakato mzima wa utekaji wa manowari ya kijeshi iliyotoka Tanzania, pia akamweleza kuhusu pesa aliyolipwa na Yule kijana kwa biashara nyingine waliyokuwa wameifanya siku chache za nyuma. “Vizuri sana,” Yule bwana kwenye ile luninga akajibu, kisha akaendelea, “Sasa kuna mpango gani kuhusu hizi silaha za sasa?” akuliza.

“Kwanza wale jamaa walitaka makombora lakini hawakusema idadi, sisi tumepata makombora makubwa kumi na mbili na silaha nyingine nyingi za kufaa,” Shalabah alieleza. “Ok, hakikisha kila kitu kinakwenda sawa, imarisha ulinzi ijapokuwa naamini hakuna wa kutuumiza kichwa kwani kwa taarifa ambazo ninazo mpelelezi mkorofi wa Tanzania hayupo kazini kwa kipindi kirefu na nafasi yake imechukuliwa na mwingine, hakikisha kila mtu anayekuja kuhusiana nah ii shughuli unamuua, hakuna kumpa mtu nafasi hata ya robo sekunde, weka watu kila mahali, kila sehemu nyeti hakikisha umeweka kinasa sauti kilicho hai na Yule mdunguaji niliyekwambia umkodi ulimpata?” Yule bwana kwenye luninga alijaribu kupanga na kuuliza.

“Bila shaka mzee, nimempata na leo jioni nitaingia naye mkataba,” Shalabah akajibu. “Sasa umwambie mkataba wetu utakwisha pale tu jamaa hawa watakapochukua mzigo wao, na hao mateka hakikisha tunawauza kwa vikundi vya ugaidi kwani nao ni silaha nzuri sana,” yule mtu kwenye luninga alimaliza na kisha ile luninga ikadidimia chini, pale ilipokuwapo pakatoakea picha kubwa ya mwanamke aliyelala uchi. Mlio wa bip ukasikika, Shalabah akainuka na kuiacha ile briefcase palepale akatoka na kuingia katika kijichumba kile alichotokea mwanzo, kikampandisha na kumleta juu kabisa, akashuka na kuondoka zake huku akiliacha lile jumba nyuma yake likifanya mandhari safi inayolipamba jiji la Mogadishu.

Shalabah alikanyaga mafuta mpaka eneo linguine kabisa la mji, hapo palikuwa na jengo kama shule kubwa, Shalabaha akaingia na kupita moja kwa moja kwenye jengo linguine lililokuwa limejengwa ndani yake. “Karibu sana bwana mkubwa, tukusaidie nini?” mlinzi wa eneo hilo aliuliza kwa sauti ya majigambo huku akimtunishia kifua Shalabah.
“Nahitaji kumuona bosi wako,” Shalabah akajibu.
“Unaitwa nani na umetoka wapi?” Yule mlinzi akauliza.
“Shalabah, kutoka Uranus,” akajibu. Yule mlinzi akainua simu na kupiga sehemu fulani, kisha akaongea maneno machache na alipoirudisha simu hiyo mahala pake, akamruhusu Yule bwana kuingia ndani. Shalabah alijikuta kwenye uwa mkubwa uliokuwa na watoto wengi waliokuwa katika mafunzo makali ya karate na kungfu, mkufunzi wao aliyekuwa mbele kabisa alionekana kuwa stadi sana kwa minyumbuliko aliyokuwa akifanya akiwaelekeza jinsi ya kukunja mikono na jinsi ya kusimama kimapambano.

Shalabah alipitishwa kwenye ujia mrefu mpaka katika mlango mmojawapo kati ya mingi, akaingizwa ndani na kuketi katika sebule kubwa lenye nakshi za kuvutia, zuria la gharama liliificha sakafu safi ya terrazzo, Shalabah alikuwa akiitalii sebule hiyo kubwa ya kuvutia iliyokosa kitu kimoja tu, muziki, muziki mororo ambao ungemfanya aliyeketi katika moja ya matandiko hayo ama achezeshe mguu au kichwa kufuatisha midundo ya muziki huo. Shalabah akiwa katika mawazo hayo mara akasikia mlango ukifungwa nyuma yake, akageuka lakini hakumuona mtu, aliporudisha uso wake mbele alikutana na mtu aliyekwishaketi tayari katika tandiko moja wapo mbele yake. Mtu aliyevalia juba la kibuluu lililoficha mwili wote na kuaacha macho mawili tu yaliyokuwa yakionekana kwa taabu kidogo. Shalabah hakujua kama mtu huyo ni mwanamke ama mwanaume kutokana na vile alivyovaa vazi lake hilo.

“Mr Kalabah, karibu sana katika himaya yangu,” Yule mtu alimkaribisha, Kalabah alimtambua kuwa ni mwanamke kutokana na sauti yake.
“Nimekwishakaribia, shukrani,” kalabah alishukuru.
“Tusipoteze muda, niambie shida yako,” Yule mwanamke alimweleza.
“Bimekuja kutoka Uranus, nina shida ya kikazi kama ofisi ilivyonituma,” Shalabah akiwa aneleza lililomleta, akaktishwa na sauti ya nhuyo mwanamke.
“Kazi au biashara?” akauliza.
“Si biashara kwa kuwa hakuna tunachotaka kukuuzia, ila kazi kwa kuwa tunataka ututekelezee jambo Fulani,” Shalabah akaeleza.

“Ok, linahusu damu ya mwanadamu?” Yule mwanamke akauliza.
“Ndiyo, litahusisha,” Shalabah akajibu.
“Sikila Mr. Shalabah, kwa hilo unalotaka tuongee hapa si mahali pake, nitakuelekeza wapi tuonane, hatuwezi kufanya biashara ya damu katika kasri hili tukufu, kasri la marehemu baba yangu alilotumia kuabudu, wewe nenda na mimi nitakujulisha wapi tuonane,” Yule mwanamke akamaliza kuzungumza na kuinuka kutoka pale alipokuwa ameketi akatokomea katika mlango mmoja wapo. Shalabah akainuka tayari kutoka ndani ya jumba lile, msichana mrembo wa uso alikuwa tayari kumwongoza kumtoa nje ya kasri hilo.

Shalabah alitolewa nje ya jengo lile kwa kupitia njia ileile lakini mara hii ali[pofika kwenye ule uwa akasimama na kushangaa anachokiona, mara ya kwanza alikuta watoto wakifanya mafunzo ya kungfu na karate, lakini mara hii alikuta uwa wote umeota nyasi na wanyama kama mbuzi walikuwa wakiburudika, alishindwa kuuliza akaamua kupitiliza mpaka nje ambako aliagana na Yule msichana akalielekea gari lake. Alipoketi nyuma ya usukani ndipo alipoiona kadi ndogo nyeupe ikining’inia katika swichi ya kuwashia vifuta maji (wipers) vya gari hiyo, akainyakuwa na kuisoma.
‘…Dar es salaam Club, saa 3:00 usiku…’

Makao makuu ya JWTZ
Lugalo – dar es salaam


TAARIFA za kupotea kwa manowari ya jeshi la Tanzania na wapiganaji wake zilifika katika makao makuu ya jeshi hilo pale Lugalo mnamo majira ya saa tatu ausbuhi muda ambao manowari ile ilitakiwa kuwa imefika katika moja ya vituo vyake kabla ya kuwasili katika bahari ya Caspian siku mbili zinazofuata. Jeshi la Urusi lilipowasiliana na lile la Tanzania ilionekana wzi kuwa manowari hiyo imepotelea katika bahari ya Indi usiku uliotangulia, kwani kila walipojaribu kuitafuta kwa vifaa vya kisasa walishinda kabisa kuiona ilipo lakini waliweza kuona ilipoishia safari yake. Wakipiga picha ya eneo hilo wanakuta ilikuwa sehemu za Somalia ijapokuwa ilikuwa katika maji makubwa, maji ya kimataifa.

Mkuu wa majeshi, brigedia jenerali Kamsumi alikuwa ameketi na viongozi wake wa ngazi ya juu kabisa jeshini wakijaribu kujadili juu ya upotevu wa manowari hiyo. Ulikuwa ni mkutano mzito ambao kila mshiriki alionekana kushikwa na jazba au hasira.

“Hao ni maharamia tu, si wengine, siku hizi wamekuwa wakiteka meli nyingi bila kujali sheria za kimataifa kuwa meli hizo ziko katika maji ya kimataifa, kwa nini tunawadekeza?” alilalama mmoja wa washiriki aliyekuwa katika jopo hilo.
“Meli sio tatizo, lakini vipi kuhusu makombora hayo ambayo gharama tu ya kuyatengeneza ilikuwa ni kubwa ijapokuwa tumepata ufadhili wa asilimia Fulani ya Warusi, tukiyaacha hawa jamaa si watatugeuka wenyewe?” Mjumbe mwingine alieleza.

“Hivyo vyote havina maana, wapiganaji wetu, watoto wetu wametekwa au kupotea pamoja na manowari hiyo kwa nini tuvumilie? Tuna makomandoo hapa tutume japo wawili tu wakaitafute hiyo meli kisha tuikomboe,” mjumbe wa tatu alikuwa akiongea mpaka anatoa machozi. Baada ya majadiliano marefu na yaliyokuwa hayana mwisho, muada ulifika wa kufanya video conference na amiri jeshi mkuu. Luninga iliyokuwa ukutani ikachukua uhai na moja kwa moja mbele yao akainekana mheshimiwa Rais. Mkuu wa majeshi akaeleza kwa kifupi waliyojadiliana wajumbe katika kikao kile.

“Sikilizeni, hatuwezi kuvumilia wala kuwapa nafasi, ile ni pesa ya kodi za Watanzania, kwa nini ipotee hivihivi? Isitoshe kuna watoto wetu, vijana wetu na wapiganaji wetu, lazima waokolewe kwa gharama yeyote,” amiri jeshi mkuu aliongea kwa ukali sana, “Ninyi mna kitengo cha upelelezi ndani ya JW, haya mara moja chagueni mtu au watu wakafanye kazi hiyo, nitahitaji ripoti haraka,” mwisho wa maneno hayo ile luninga ikazimika. Kila mshiriki alishusha pumzi ndefu. Ilikuwa ni sentensi ndefu kidogo iliyowatetemesha wakuu hao wa jeshi waliokuwa wakibishana bila kupata muafaka katika lipi la kufanya. Kutokana na kauli ya aamiri jeshi mkuu, hakukuwa na mjadala mwingine kilichoangaliwa kilikuwa ni nani apewe kazi hiyo.

“Lakini jamani ee, tuiangalie hii kazi kwa ugumu na upana wake,” kiongozi mmoja alisema.
“Yeah ni kweli kuliko kudharau na kupeleka mtu ambaye atafika na kushindwa kufanya lolote. Nani tumtume akafanye kazi hiyo, kazi yan hatari kuliko hatari mwenyewe. Chekecha chekecha ikapita, Jamil Semindu, komandoo aliyemeliza mafunzo yake siku si nyingi nchini Cuba, jina lake lilipitishwa tayari kwa kazi hiyo. Mchana wa siku hiyo kijana huyo aliitwa makao makuu ya jeshi kutoka kambi ya Lugalo kule Mwenge. Naye hakukataa wito bali aliamini msemo wa wahenga, ;usikatae wito kataa neno’.

Majira ya saa nane mchana, Jamil Semindu alikuwa amesimama wima kiukakamavu mbele ya mkuu wa majeshi. Hakuwa peke yake, pembeni yake kulikuwa na mtu mwingine wa makamo, aliyavalia nguo nadhifu ya kijeshi.
“Jamil Semindu, Gwamaka Mwakajinga, tunatambua umuhimu na mchango wa kazi yenu katika jeshi letu tukufu la wananchi wa Tanzania. Nimekuiteni hapa kuwapa kazi maalum ambayo inatakiwa kuanzwa mara moja, kama mnavyojua au milivyosikia, manowari yetu ya jeshi la Tanzania, Kirov Class, ndani yake ikiwa na wapiganaji ishirini na tano pamoja na makombora kumi na mbili ya R-36 imepotea katika maji ya kimataifa huko Somalia, inahisiwa kuwa huenda ikawa imetekwa na maharamia kama iloivyotokea kwa meli zingine za mizigo. Tunawatuma muende mkafanye kazi, kwanza mkawaokoe wapiganaji wetu, pili mkaokoe makaombora yetu, tatu mkailete na meli yenyewe, mambo yote yamekwisha andaliwa mkitoka hapa tu mtaelezwa cha kufanya,” alimaliza mkuu jeshi. Wale wanajeshi wawili wakapiga salute na kisha kutoka nje ya ofisi hiyo.

Gwamaka Mwakajinga alikuwa mpelelezi wa kijeshi aliyeaminika sana hasa kwa kuzisoma nyanyo za adui, na kujua wapi alipo. Kijana huyu ndiye aliyewaongoza wenzake katika vita ya ukombozi huko visiwa vya Komoro, vita ya kumng’oa madarakani aliyekuwa rais wan chi hiyo. Alishiriki pia kupeleleza vizuri sana makazi ya waasi wa M23 pamoja na kujua maisha yao ya kila siku, mwisho wa siku aliwapa ramani yote majeshi ya Umoja wa Mataifa yakiongozwa na Tanzania na kuwafutilia mbali waasi hao. Jopo lililokaa kuchagua wawili hao liliangalia mambo mengi na tofautitofauti.

Gwamaka na Jamil wakapeana mikono na kusalimiana wakati wakiwa nje ya jengo hilo, kisha wote wawili wakaelekea katika jengo linguine kama walivyoongozwa.
“Unaonaje Meja, hawa vijana watawaweza wale maharamia wanaokunywa damu?” Luteni kanali Gogo alimuuliza mwenzake aliyekuwa naye, kapteni Kamazima.
“Wataweza tu, tuweke imani,” Meja Kamazima alimjibu.
“Maana wale maharamia kuwapata ni kazi, nao pia wamejikamilisha kwa silaha na upiganaji wa silaha,” Luteni Kanali Gogo alionesha waziwazi wasiwasi wake katika hili.
“Wataweza tu usihofu,” Meje Kamazima alimjibu na kumtia moyo mwenzake.
Taratibu zote zilikamilishwa za safari za hao jamaa, na siku iliyofuata kwa kutumia ndege ya shirika la ndege la Ethiopia waliondoka Tanzania kuelekea Somalia kupitia Addis Ababa.
“Sijacheza michezo hii siku nyingia sana,” Jamil alimwambia Gwamaka.
“Michezo midogo sana hii, nilikuwa Kivu juzijuzi tu kuwasaka M23 hivyo bado damu ya moto,” akazungumza Gwamaka. Walibadilishana mawazo wakiwa katika ndege hiyo safarini kuelekea Mogadishu.
“Sasa sikia Jamil, unajua hawa jamaa ni wajanja sana, kwa vyovyote lazima wanajua kama tunakwenda, tukifika naomba tushuke kila mtu kivyake na tusijuane isipokuwa tuwasiliane kwa simu tu kila mtu atakapofikia,” Gwamaka alijaribu kupanga mpango.
“No, tufikie hotel moja lakini tutofautishe vyumba kwa umbali mrefu kama kuna ghorofa basi mmoja ya juu mwingine ya chini,” Jamil naye akatoa pemdekezo ambalo lilikubaliwa na wote.
“Tutafanyaje operesheni yetu?” Jamil akauliza.
“Kutokana na kazi zetu, mi nitakuwa nafanya uchunguzi nakupa information na wewe unakwenda kumaliza kazi maana we ni jeshi la mtu mmoja,” wote wakacheka na kugonga viganja vyao.

RAMADA PLAZA HOTEL
Ramada plaza hoteli, ni hotel tulivu iliyo jirani na bahari katika jiji la Mogadishu, ikitazamana na bandari ya zamani ya jiji hilo. Mandhari safi, chakula na mazingira ya kuvutia viliwafanya wapiganaji hawa kuvutiwa na mahali hapo.
Alikuwa Gwamaka wa kwanza kuingia katika hotel hiyo, akapanga chumba ghorofa ya tatu juu. Baadae jamil nae akafika na kuchukua ghorofa ya chini kabisa, wakiwa tayari kikazi na wamekamilika.
Kutoka ghorofa ya tatu Gwamaka aliweza kutumia darubini yake kuangalia upande wa baharini kila baada ya nusu saa na kuandika kwenye kidaftari chake mambo anayoyajua mwenyewe. Jioni ya siku hiyo wakiwa chakulani walibadilishana mawazo hili na lile na kupanga nini cha kufanya.

DAR ES SALAAM CLUB
SHALABAH aliegesha gari yake katika maegesho ya club hiyo ya usiku, akateremka na kuufunga mlango nyuma yake. Kisha kwa hatua za taratibu aliuendea mlango mkubwa. Kwa upande wa nje zaidi ya walinzi walioonekana kuangalia usalama wa mali za wateja, hakukuwa na vurugu wala hakukusikika kelele yoyote ya kitu chochote, mtaa ulikuwa kimya kabisa. ni wale tu waliokuwa hawafuati sawasawa misingi ya dini yao ndiyo waliokusanyika katika klabu hiyo pamoja na wageni kutoka Katika nchi za pembezoni na zile za mbali.
Shalabah alizipanda ngazi na alipofika katika mlango wa kuingilia alisimamishwa na akatakiwa kusalimisha kama ana aina yoyote ya silaha, alikuwa na bastola moja na kisu cha kukunja, akaviacha na kuandikisha, akapewa namba na kuingia ndani.

Tofauti na nje, ndani ya klabu hiyo kulikua na kila aina ya starehe, muziki laini ulikuwepo na wale waliopenda disco walitakiwa kuteremka chini kabisa. watu walikula na kunywa wakifurahia maisha. Shalabah alijipenyeza taratibu katika makundi ya watu mpaka akaifikia kaunta kubwa.

“Nikusaidie nini?” akauliza mtu aliyekuwa kaunta. Shalabah hakujibu isipokuwa alitoa sigara na kumuonesha, kisha yule jamaa akatoa kiberiti na kukiwasha lakini hakuiwasha ile sigara. Sekunde chache tu mwanadada mrembo aliyekuwa na nywele mpaka kiunoni alimjia Shalabah na kumshika begani. Shalabah akamfuata. Wakapenya penya katika makundi ya watu, wakapita nyuma ya jukwaa la wacheza uchi wakaingia kwenye pazia la kumetameta, ndani ya mlango mkubwa na mzito wa kioo, hakukuwa na kelele yoyote, palikuwa kama nyumbani, huko kulikuwa na vyumba vingi sana.
809, yule mwanadada akasimama na kubofya kitufe Fulani, mlango ukafunguka, wakaingia. Ndani ya chumba hicho kulikuwa na chumba kimoja kidogo na mwanadada mrefu aliyekuwa na upara kichwani mwake huku akivuta mtemba kinywani mwake alikuwa amekunja nne kwenye sofa moja pana na kuiachia nguo yake yenye mpasuo mrefu kumwagika kwa chini na kuruhusu mapaja yake laini kuonekana kwa ukamilifu.
“Karibu Kijana,” yule mwanamke akamkaribisha.
“Asante sana,” Shalabah akajibu.
“Haya tuna dakika tano tu za kuzungumza, nipe mzigo, nikupe kipimo,” yule mwanamke mwenye upara akamwambia Shalabah.

“Nafikiri unatufahamu, sasa tuna biashara nzito sana ya kufanya, ijapokuwa hatuna hofu na usalama kutokana na biashara zetu zilizopita, ila hii tumetahadharishwa sana, kuna watu tunatakiwa kuwaondoa haraka iwezekanavyo lakini pia tunahitaji usaidizi wa kiteknolojia katia kuyatambu makombora kumi na mbili tuliyoyateka,” Shalabah alieleza.
“Ha ha ha ha nyie watu mna biashara za hatari sana, kwa kuwa tuliingia mkataba huo tangu mwanzo na tajiri wenu hamna tabu, haya kazi ya kwanza itafanyika, nipe picha za hao watu na wapi wamefikia, kuwatungua si tatizo, kisha tutaliona la pili,” yule mwanamke mwenye upara akaeleza. Shalabah akatoa Ipad yake na kuparazaparaza vidole vyake kwenye kioo cha chombo hicho, kisha akamkabidhi yule mwanamke. Akachukua na kutazama, naye akaparaza hapa na pale na zile picha zikahamia kwenye simu yake ya kisasa kwa njia ya Bluetooth.

“Ok Mr. kila kichwa dola 1000 za kimarekani, nimemaliza, fanya mchakato kama tunavyofanya kila wakati,” yule mwanamke akanyanyuka na vazi lake likamfunika vyema, akafungua mlango wa nyuma yake na kutokomea. Shalabah alitoka ndani ya chumba kile na kutembea taratibu kurudi ukumbini, kisha akatoka nje ya klabu ile.

Ndani ya bahari ya Indi katika bandari ya zamani ya Mogadishu, maharamia wateka meli walikuwa katika ulinzi wa aina yake. Walionekana ni watu masikini kimavazi lakini ukiwatazama silaha walizobeba mikononi mwao utakubali tu. Wapo waliokuwa juu muda wote wakitazama usalama kwa kujifanya wana shughuli mbalimbali. Na daima walikuwa wakifuatilia sana nyendo za wageni wanaoingia Somalia hasa wale kutoka nchi za maghalibi kwa maana walikwishateka meli kadhaa za mataifa hayo na kuwaweka mateka wanajeshi wao.

Hata zile nchi zilipojaribu kutaka kuwapata watu hao ilikuwa ngumu kutokana na nchi ya Somalia kutokuwa na serikali ambayo unaweza ukafanya mazungumzo nao. Wapiga mbizi kadhaa walikuwa ndani ya maji wakikagua makombora hayo, upande wa wale wanaouza ambao ni hao maharamia na wale wanaouziwa wapiganaji waasi kutoka huko Pakistani na Afghanistani, walikuja na wataalamu wao na wakati huo maharamia hao nao walikuwa na mtaalamu wao wa silaha, mwanamke yule mwenye upara. Ukaguzi ulifanyika chini ya maji kwa muda takribani wa dakika thelethini, kisha wapiga mbizi hao wakatokea ndani kwa ndani na kuingia katika chumba kilichojaa maji ambacho kuna ngazi unapanda na kutokea chumba cha juu kisicho na maji. Hapo wakavua mitambo yao walioibeba migongoni na kubaki katika nguo zao za kawaida. Kisha wakafuatana kutoka na kuingia katika gari iliyoandaliwa wakaelekea mjini.

Kepteni Gwamaka Mwakajinga akashusa darubini yake kutoka katika uso wake akaichia ining’inie kifuani.
“Wametoka,” Gwamaka akawasiliana na Jamil aliyekuwa kwenye gari nyingine.
“Wasindikize, unambie wanapoishia,” Jamil akamwambia Gwamaka. Kwa mwendo wa taratibu Gwamaka akaingiza gari barabarani na kuendessha kuelekea kule ambako gari ile ilikwenda. Alihakikisha haipotezi kabisa gari hiyo katika macho yake.

Aliendelea kuwafuata akiwa peke yake ndani ya gari. “Gwamaka, kuna gari imenipita kasi sana hapa hebu iwekee tahadhari,” Jamil aliwasiliana na Gwamaka wakati gari hyo aliyoisema ikiwa mbele yake kama mita kumi tu. Walipoiacha barabara ya Corso Somalia na kuupita mzunguko kisha kuikamata barabara ya Jidka Jannaral Daud ndipo komandoo Jamil alipoona hila ya watu hao, akajua wazi kuwa wako matatani na hana budi kumsaidia mwenzake aliyekuwa mbele.
“Nimeiona,” akajibu.

“Kaa tayari, jamaa wameandaa silaha nahisi wanataka kufanya shambulizi la ghafla,” Komandoo Jamil alimwambia Gwamaka. “Natafuta mbinu ya kufanya,” Gwamaka akamwambia Jamil. Haikupita sekunde thelathini, wakati wanakaribia kabisa shule ya sekondari ya Jan Daud, ile gari nyuma ya Gwamaka ikaovateki ghafla na kukaa upande wake wa kushoto, Gwamaka akawa tayari amekwishaiona, akaipa sekunde mbili ilipokuwa tayari inakaribia nusu ya gari yake kuovateki, nae akaitoa gari yake kushoto, na kusababisha dereva wa wale jamaa kuyumba, ile gari ikagonga nguzo ya umeme, cheche zikawaka na transifoma la jirani likalipuka.

“Usisimame, wafuate,” Komandoo Jamil akamwambia Gwamaka kwa simu yake ya upepo yeye akiwa katika gari iliyokuwa nyuma yao umbali wa mita kama hamsini hivi, aliishuhudia ile gari ikigonga nguzo na ule moto wa umeme uliolipuka ukafanya gari ile kushika moto. Jamil alishuhudia watu wale walivyokuwa wakijaribu kutokea madirishani.
“Safi sana Gwamaka!!!!” Komandoo Jamil aliikubali mbinu iliyofanywa na Gwamaka, akaongeza mwendo na kuzipita gari mbili zilizo katikati yake. Akapunguza mwendo na kushuhudia wawili wakiungua vibaya kwa kushindwa kutoka ndani ya gari, na mmoja akiwa ndiye anajinasua dirishani. Komandoo Jamil, akaegesha gari pembeni na kuteremka kwa minajiri ya kutoa msaada, akamuendea yule wa dirishani na kumnasua katika kioo, akambeba na kumtia kwenye gari yake.

“Wapi Hospitali?” akawauliza watu waliokuwa eneo lile kwa lugha ya kiarabu ambapo walielewana vizuri, hilo halikumfanya yeyote kutia mashaka juu ya Jamil, akaondoka kwa kasi mapaka njia panda ya Siinay akakunja kushoto na kuendesha gari hiyo kwa kasi ya ajabu, mpaka akauacha mji na kufika maeneo yaiyo na watu, jangwa lilianza kumkabili, akaegesha gari pembeni, akamshusha yule jamaa.

“Hapa ndo hospitali?” yule majeruhi aliuliza kwa tabu kidogo. “Aliyekwambia mi mwezi mwekundu nani hata nikupeleke wewe hoapitali?” Jamila akajibu na kumvuta akambwaga kwenye mchanga ulioshika joto kali la jua. Akamkanyaga pajani ambapo palikuwa na donda kubwa la moto.
“Nani mwajiri wako?” akamwuliza. Yule jamaa hakujibu isipokuwa akamtolea macho Jamil. “Nakuuliza nani unamfanyia kazi? Aliyewatuma kuifuatilia ile gari,” akaongeza swali linguine, yule jamaa akawa mgumu kujibu, Jamila akamuinamia na kuchomoa kisu, akachoma mchomo mmoja kwenye paja. Yuele jamaa akatoa yowe la uchungu sana.
“Nitakwambia, nitakwambi, nitakwambia,” akapiga kelele.
“Haya nambie,” Jamil akamsikiliza.
“Sharon, Sharon, kamanda Sharon,” akajibu.
“Ndiyo nani?” akauliza tena Jamil.
“Kiongozi wetu, aliwaona mkitufuatilia, akatutuma tumuue yule mwingine, wewe hakukuona,” yule bwana akajibu huku akilia kwa uchungu.

“Anaishi wapi huyo Sharon?” Jamil akahoji. Yule bwana akawa jeuri kujibu, kila alipolazimishwa hakujibu. Jamil akashika kile kisu kilichodinda katika nyama ya paja la yule jama na kukizungusha, yowe kali lilimtoka tena yule bwana akalia mpaka akawa akipigapiga ngumi kwenye mshanga. “Jidka Dabaqayn,” akajibu huku akilia. Jamil akamuacha na kuchomoa kile kisu. Kitendo cha ghafla yule jamaa kutoka pale chini akajinyanyua na kutaka kumvamia Jamil, Jamil akaliona hilo haraka, akaachia makonde mawili makali yaliyomrudisha chini na kumtoa roho. Akamuendea na kumsukasuka kwa mguu wake, ameshakufa. Akampekua mifukoni hakuna cha maana alichokipata zaidi ya picha moja ya msichana mbichi aliyepiga akiwa uchi wa nyama, akaichukua na simu yake pia na akaondoka navyo. Jamil akaliendea gari lake na kuondoka akiuacha mwili wa yule jamaa palepale jangwani yeye akarudi mjini.

Gwamaka aliendelea kuifuata ile gari mpaka pembezoni mwa mji, ikaingia katika jengo moja kubwa lililoonekana kama kiwanda Fulani, yeye akapitiliza na kwenda kuegesha gari mbele kidogo. Akateremka na kurudi polepole mpaka kwenye mgahawa uliokuwa ukitazamana na jengo lile. Akaketi upenuni mwa mgahawa huo na kuagiza kinywaji huku macho yake yakitazama mara kwa mara jengo lile.

Moqdisho textile, ni maandishi yaliyolipamba godown lile kwa upande wa juu, Gwamaka akachukua kijidafutari chake na kuandika jina hilo, jina la barabara na namba ya kiwanja, akahifadhi mfukoni mwake. Akaendelea taratibu kupata kinywaji chake. Akiwa bado anaendelea mwanadada mmoja alitoka ndani ya mgahawa huo na kuketi katika kiti cha mbele yake, wakasalimiana, ijapokuwa Gwamaka alikuwa akibabaisha kusalimiana kwa lugha yao. Akabadilisha lugha na kuanza kuongea kiingereza.

“Inaonekana ni mgeni wewe hapa?” yule mwanamke akamwuliza Gwamaka. “Ndiyo, ni mgeni hapa, nimesimama kidogo nipate kinywaji, si waona jua lilivyo kali,” Gwamaka akamweleza. “Aa yah ni kweli, wewe watokea wapi?” yule mwanamke akamwuliza. “Mimi ninatokea Kenya naitwa Charles Musungu,” Gwamaka akajitambulisha kwa jina la bandia. “Oh, jina zuri, mi naitwa Fatma, huu mgahawa hapa ni wa familia,” Fatma akaendelea kuzungumza, baada ya hapo mazungumzo mengi yakaendelea kati ya wawili hao, Gwamaka akachukua kadi ya kibiashara ya Fatma na kuihifadhi. Wakati wakiendelea kuzungumza, aliiona ile gari aliokuwa akiiangalia akaiona ikitoka na kuondoka.
“Fatma, maadam nina namba yako, basi nitakupigia jioni, vipi unaweza kuungana nami jioni ya leo?” Gwamaka akamwambia Fatma huku akiwa amenyanyuka tayari kuondoka.

“Bila shaka Charles,” Fatma akaitika huku akimshuhudia Gwamaka akaiziacha ngazi za mgahawa huo na kuingia mtaani, aliichuku gari yake na kuondoka kwa kasi kuifukuza ile gari, si mwendo mrefu aliikuta, akaipa nafasi gari ile na kuifuata taratibu.
“Braza,” sauti ikaita katika earphone yake.
“Hey Jamil,” Gwamaka akajibu.
“Uelekeo,” Jamil akauliza.
“Bado nawinda, nitakucheki,” Gwamaka akajibu.
“Copy,” Jamil akaitikia.
Msafara wa ile gari ukaelekea uwanja wa ndege moja kwa moja. Gwamaka akaendele kuwatazama watu wale wakiagana, akachukua kamera yake na kupiga picha kadhaa. Aliporidhika na zoezi hilo akaingia kwenye gari yake na kurudi mjini.

Gwamaka alikuwa akiendesha gari taratibu huku akipiga mruzi, mbele yake akaona kibao kilichoandikwa SHELL, alipotazama mshale wa mafuta ulimuonesha tanki lake liko mbioni kumalizika, akawasha indiketa ya kulia na kuingia katika kituo hicho cha kujazia mafuta. Moja kwa moja akaegesha katika moja ya pampu sita zilizofungwa hapo.
“Full tank tafadhali,” akamwambia kijana aliyekuwa akihudumia pampu hiyo, na kijana yule akafanya kazi yake kama ilivyotakiwa. Gwamaka akalipa na kuondoka eneo lile kurudi hotelini kwake.

Akaingia kwenye maegesho ya magari na kuliweka gari lake vizuri, akatulia kwanza kabla ya kushuka, baada ya dakika kama kumi hivi akateremka na kuvuta hatua ndefundefu huku mikono ikiwa mfukoni na, akazipanda ngazi za hotel hiyo mpaka katika chumba chake, alipofika mlangoni akatulia kidogo akatzama mitego yake akagundua ama kuna mtu aliingia au ameingia, akachomoa bastola yake na kuishika barabara kwa mkono wake wa kulia kisha taratibu akanyonga kitasa na kuufungua mlango huo, akaingia ndani na kutazama huku na kule, akaangalia kila kona ambayo anajua kama imeguswa au la, kwa jinsi alivyokiacha chumba chake alijua tu kuna mtu aliyepekuwa kitaalamu sana kiasi kwamba kwa amtu ambaye ni wa kawaid hatoligundua hilo lakini haikuwa kwa Gwamaka. Alipojiridhisha kuwa usalama upo akaketi kitandani na kuvua fulana aliyokuwa ameivaa.

Akaliendelea dirisha ambalo alikuwa amefunga darubini yake ya jicho moja, akachungulia kuona nini kinaendelea upande wa bandari ya zamani ya Mogadishu ambako inasemekana huko ndiko maharamia wale wanakoficha nyara zao. Hakuna jipya zaidi ya kuona walinzi walewale wakivuta bangi na kuendelea kulinda maeneo yao. ‘Nchi isiyo na serikali ni shida tupu’ akajisemea wakati akitoka pale dirishani.

Mwanamke mwenye upara akashusha darubini yake iliyokuwa ikimwangali Gwamaka alipofika chumbani kwake, akaiacha ining’inie kifuani mwake.
“Amerudi,” Fasendy akawaambia vijana wake machachari. Wakanyanyuka mara moja, “hakikishenu mnamleta mzima, tunataka tumtoe sadaka kesho ijumaa,” akaongezea maneno hayo kisha akavuta kiti akaketi na kuwasha sigara akaipachika kinywani. Wale vijana walifanya kama walivyoagizwa, wakafika Ramada hotel na kukamata kila mtu kona yake kisha wawili kati yao wakaingia ndani na kupanda ghorofani kukifuata chumba cha Gwamaka. Hawakugonga hodi wala kuuliza, wakapiga teke mlango nao ukafunguka, wakajitoma ndani kwa ustadi ikiwa na kutanguliza mtutu wa bunduki, hakuna mtu. Wakaingia mpaka ndani na kutazama kila mahali lakini bado hawakuona mtu, uvunguni kwenye makabati kote Gwamaka hayupo. Wale jamaa wakashusha pumzi ndefu kung’uta mashuka yote inua kitanda, hakuna Gwamaka.

“Aisee, huyu mtu ameondoka hayupo hapa,” mmoja wao akasema kumwambia mwenzake, kisha wakatoa taarifa kwa redio na kutoka nje ya chumba kile.
Gwamaka aliibuka kutoka katika beseni kubwa la kuogea lililojengewa pembeni kabisa mwa bafu hilo, wakati jamaa hao walipokuwa wakipekua kumtafuta, yeye tayari alikwishajizamisha kwenye beseni hilo lililojaa maji ya sabuni ambayo haiukuwa rahisi mtu kuona kilichopo ndani yake.

Alitoka na kusimama pembeni huku nguo zake zikimwagika maji, akatulia kimya akisubiri kuona kama watu hao wamekwishatoka au la. Alipoona ukimya umetawala akampa taarifa Jamil aliyekuwa bado hajafika mahala pale.
Plaza hotel iliwekwa chini ya nuangalizi wa siri na wapiganaji maharamia wakiwahofia watu hao kutoka Afrika Mashariki, walidhamiria kuwamaliza vijana hao, kwa maana walishaona hatari itakayosababishwa nao. Waliizingira hotel ile kwa siri, wengine wakijifanya kuja kula, wengine wakifanya jambo hili au lile ilimradi tu ni kutaka kujua kama watu hao wapo au hawapo ili watekeleze azma yao.

“Usitoke ndani, jamaa inaonekana bado wapo,” Jamil alimwambia kwa simu ya upepo. Gwamaka akaendelea kutulia chumbani mwake, akisubiria asikie nini ataambiwa na Jamil ambaye alikuwa nje ya hotel hiyo.
Jamil alikuwa akiegesha gari yake nje ya hotel hiyo alipojikuta akiwekewa mtutu wa Short Machine Gun sikioni mwake.
“Sihitaji kukuuliza wala kuniuliza, shuka kwenye gari,” Jamil aliamrishwa na mtu mmoja mwenye bunduki hiyo aliyeishika madhubuti mkononi mwake, ikiwa imefungwa kwa mkanda uliomzunguka nyuma ya bega lake. Jamil hakuwa na ujanja kwani aliona wazi kuwa jamaa huyo hana masihara hata kidogo, alikuwa ni mwembamba mrefu mwenye macho mekundu, kinywani mwake alikuwa akitafuna mirungi. Jamil akateremka kutoka katika gari lake, lakini kabla hajatoka kabisa alidondosha vikolokolo vyote alivyochukua kutoka kwa yule mateka wake aliyemuua jangwani, kisha akatoka nje.

“Weka mikono kichwani,” aliamuriwa, akafanya hivyo na kuswagwa mpaka kwenye jeep moja iliyokuwa upande wa pili wa barabara, Jamil alipokuwa akipanda kwenye hile jeep akafanya hila ambayo hawakuigundua, akabofya kitufe cha redio yake ambayo iliunganishwa kwa ndani ya shati lake juu karibu na mdomo, wakati huo alikuwa amevua zile earphone zake, hivyo moja kwa moja ikaunganisha kwa Gwamaka. Gwamaka akaanza kusikia lugha ya kisomali ikiongelewa na watu waliokuwa wakibadilishana mawazo.

“Hatari nimetekwa,” Jamil alinong’ona na sauti ile ilisafiri moja kwa moja mpaka kwa Gwamaka.
“Unaongea na nani?” akauliza mtu mmoja aliyekuwa na rifle mkononi mwake, akaiinua na kumpiga kwa kitako cha bunduki hiyo, jamili akaenda chini ndani ya bodi ndogo ya gari ile.
“Shiiit,” Gwamaka akang’aka, akachukua bastola zake mbili, na kuziweka magazine na nyingine akajaza mifukoni katika jeans, akatoka mlangoni, bila hadhari yoyote akitaka kuwahi kujua jamil anapelekwa wapi. Lilikuwa ni kosa kubwa sana alilolifanya, hakuna kingine alichokihisi zaidi ya maumivu makali kichwani mwake, kizunguzungu kikafuatia, akadondoka chini.

Mwanamke mwenya upara alisimama pembeni yake. “Mlivyosema hayupo na huyu ni nani?” akawauliza wafuasi wake. Hakuna aliyejibu, wakamnyanyua Gwamaka na kutoka naye kupitia mlango wa nyuma, wakampakia kwenye gari yao na kuondoka naye.

SHALABAH alitulia kitini akinywa taratibu kahawa yake. Gari moja nyeusi aina ya Toyota Nadia ilisimama mita chache kutoka pale alipokuwa ameketi. Mwanamke mrefu akateremka, aliyevaa kininja, akavuta hatua ndefundefu mpaka pale alipoketi, akavuta kiti na kukaa. “Sina maneno mengi, ila unajua kuwa nimekwsihamaliza kazi uliyotaka nifanye, nimefata hundi yangu,” Fasendy akamwambia Shalabah.

“Usijali, niliketi hapa kukusubiri wewe, ili kukukamilishia malipo yako lakini pia kuna kazi nyingine ya kufanya,” Shalaba akamwambia Fasendy huku akimpatia bahasha nyeupe ambayo ndani yake kulikuwa na hundi hiyo. Akaifungua na kutazama akaiona ni sawa, akaifutika ndani ya nguo yake. “haya, ongea linguine,” Fasendy akamwambia Shalabah.

“Nifuate,” Shalabah akamwambia Fasendy kisha akanyanyuka na kuingia ndani ya jengo hilo lililoonekana kama gofu, lililotelekezwa kwa muda mrefu sana, wakapita koridoni mpaka kwenye moja ya chumba, wakaingia na kukatiza milango kama mitatu hivi, mlango wan ne ulikuwa mlango wa kioo safi uliozungukwa na kamera za cctv ili kulinda usalama wa eneo hilo. Shalabah akabonya kitufe na mara mlango ule ukafunguka, wakaingia ndani.

Kilikuwa ni chumba kidogo lakini chenya kila kitu kinachohitajika katika ofisi yoyote duniani. Shalabah akamkaribisha Fasendy na wote wawili wakaketi katika viti vyenye vono safi. Katika meza iliyokuwa mbele yao kulikaliwa na mtu mmoja mnene mwenye mwili mkubwa aliyejaa katika suti kali nyeusi, kichwa chake kilionekana kuungana na kiwiliwili, hakuonekana shingo yake kama ilikuwepo au ilimezwa na unene huo.

“Karibu sana mwanamke,” akamkaribisha Fasendy, akajikohoza na kuendelea, “ kwanza nikupongeze kwa kazi ngumu nay a hatari uliyoifanya ya kutuletea wale watu wawili wanaojifanya kufuatilia nyayo za samba. Nafikiri malipo yako umeshayapata, lililobaki huku mbeleni tuachie sisi tunajua cha kuwafanya, lakini nina jambo moja, hawa Watanzania wakishaona wenzao hawapatikani kwa mawasiliano kwa vyovyote watatuma mtu mwingine au watu wengine kuja kuwatafuta, sasa nataka nikupe kazi nyingine ya mkataba wa miezi mitatu, ya kuhakikisha kila anayeingia hapa ni kumpoteza moja kwa moja kama tulivyofanya kwa wale Waamerika waliojifanya waandishi wa habari, upo tayari?” yule mtu akauliza.

“Wewe unajuaje kama watatuma watu wengine?” Fasendy akauliza.
“Mimi najua, ninalokwambia ndilo hilo, kumbuka tuna wanajeshi wao ishirini na tano, na hawa wawili, unafikiri watavumilia? Tunataka kuhakikisha biashara yetu inakwenda safi kabisa,” yule Bwana akamaliza.
Fasendy, akatulia kimya akiitafakari uzito wa kazi hiyo.
“Sawa, hamna tabu,” akajibu Fasendy. Yule mtu mnene akasimama na kumpoa mkono Fasendy kisha akamruhusu aende. Shalabah akamsindikiza hadi nje na kuagana naye.
“Sharon,” yule mtu mnene akaita. Sharon akajitokeza kutoka katika mlango Fulani pembenzoni mwa chumba kile, akasimama akisikiliza, “Boss ansema uhakikishe wale mateka wawili wanajutia walichokifanya na upeleke onyo kali kwa waliowatuma, kisha simamia biashara nzima, wateja wetu wamesema watakuja baada ya siku tatu kuangali makombora yaliyobaki, kama kuna shida yoyote wasiliana na Shalabah, yeye ndiye mwenye uwezo wa kuwasiliana na mimi na Mr Lonely kwa utatuzi wa mwisho,” yule Bwana akamaliza na kuagana na watu wake, kisha akabaki yeye na Shalabah tu.

MOQDISHO TEXTILE
Jamil alikuwa amefungwa kamba na kuning’inizwa kichwa chini miguu juu, hakuweza kufanya lolote kwani pembeni yake alikuwa akilindwa na vijana wawili wadogo waliokuwa na silaha za maana zilizodungwa mkanda mrefu wa risasi, hawakuona taabu kummiminia yeyote atakayeleta shida katika himaya hiyo. Walikuwa ni vijana wawili wenye kukadiriwa umri wa miaka kumi na tano na kumi nane. Vinywani mwao waote walikuwa wanakula mirungi. Jamil aliwatazama kwa zamu ili aone kama kuna jinsi ya kujiokoa lakini hali ilikuwa siyo, kwa kuwa mlango wa chumba hicho ulikuwa ni wa chuma madhubuti kabisa. Jamil alitulia palepale huku akiwaza ni wapi Gwamaka atakuwapo kwani alimuacha hotelini.
Mara mlango ukafunguliwa, Sharon akaingia ndani na vijana wengine wawili waliovaa kiraia lakini wakiwa na silaha nzito. Jamil aliona wazi hawa jamaa hawajui matumizi ya silaha kwamba silaha hii nitumia vitani na sio kutembea nayo nah ii nitumie wapi, ilikuwa haishangazi kumkuta mjini au sokoni begani mwake amejitwika RPG huku akitalii akitazama hili na lile.

“Mfungue, umtoe hapa,” Sharon aliamuru, kijana mmoja akaja na kisu na kukata kamba iliyofunga miguu ya Jamila, akaanguka na kutanguliza kichwa, akajipiga kwenye sakafu na kubwagika chini kama mzigo. Jamil akatoa mguno hafifu wa maumivu, kisha akatulia kimya. Wakamfungua kamba za miguu na kumuinua, akasimama wima lakini akiegemea ukuta maana alikuwa akisikia kizunguzungu cha hali ya juu.
Sharon akamsogelea Jamil.

“Komandoo, koamndoo utakuwa wewe? Hiyo serikali yenu bora iombe msaada niwape hawa watoto wawili tu ni sawa na vikosi vyenu kumi vya kijeshi, na sasa utajuta, kukamatwa na sisi, sisi hatuna serikali kwa taarifa yako, na sasa utaenda kushuhudia ndugu yako anavyouawa na hiyo ndiyo salamu kwa serikali yako, mataifa ya magahribi yameshindwa itakuwa ninyi, ninyi ni nani hata mjifanye mna uchungu?” Sharon alimwambia Jamil, alipomaliza tu kusema akageuka na kuwaamuru watu wake kumuongoza Jamil upande wa pili wa jengo. Wakamto ilhali akiwa na kamba mkononi mwake.
Ulikuwa ni ua mkubwa sana wenye malori kadhaa yaliyokuwa yameegeshwa. Watu wenye silaha walikuwa wengi, vijana, watu wazima, walikuwa na silaha nzito nzito.

“Simama hapa” Jamila aliambiwa na wale waliokuwa wakimlinda, akasimama pamoja na watu wengine wawili, wazungu walioonekana kuchoka sana. Mara akachukuliwa mmoja wao na kupelekwa katikati ya ule uwanja, kelele zikaanza kusikika, kelele za mashangilio, huku wakipiga risasi hewani, yule aliyempeleka pale akachomoa jambia na kumkata shingo, akamchinja na kutenganisha kabisa kichwa na kiwiliwili. Kwa kitendo hicho wenzake wakashangilia sana, ilikuwa ni kama tafrija kwao. Jamil alishindwa kutazama kitendo hicho, aliinama na kufumba macho.
“Watu makatili sana hawa, sidhani kama ni binadamu wa kawaida,” Jamil aliongea kwa sauti ya chini. Kisha yule jamaa aliyemchinja yule mtu akaja kwa Jamil na yule mwingine, akasimama mbele yao.

“Burudani yetu ni kuwachinja watu kama ninyi, siku yenu bado,” akamaliza na kuondoka. Jamil na yule mwenzake wakachukuliwa na kufungiwa ndani ya chumba kisicho hata na dirisha isipokuwa tundu dogo kama shimo la panya lililoweza kuingiza hewa kwa tabu na mwanga kidogo sana. Kufungiwa ndani ya chumba hicho kwa Jamil haikuwa mateso, bali kukaa bila kujua Gwamaka yuko wapi hilo ndilo lilikua teso kubwa kuliko yote, alibaki hivyo akitafakari bila jibu, hakuwa na jinsi ilimpasa kutulia. JUA kali la saa saba lilikuwa likichoma kwelikweli, mji wa Dar es salaam uligubikwa na joto kali, kila umuonaye kama hana kitambaa mkononi cha kufuta jasho basi alikuwa kifua nusu wazi ilimradi apate kaupepo hako kadogo. Lakini wote waliokuwa wakiteseka na joto hilo ni wale watu wa KCC yaani Kima Cha Chini, lakini kwa mwenye nazo daima jiji la Dar es salaam ni jiji lenye baridi sana kiasi kwamba kila muda anatembea na suti ya vipande vitatu.

Jiji linalosifika kwa uzuri na linalovutia watalii kwa historia yake ya utulivu na amani. Kila kijana wa Tanzania anaamini kuwa katikan jiji hilo ndiko maisha yanakoanzi hivyo huwafanya wengi kukimbilia huko ili kuanza maisha mapya wakiamini watatajirika. Lakini hali huwa tofauti sana wakifika katika jiji hilo, mwisho wake ndio vibaka, wabwia unga, makahaba kuongezeka katikati ya jiji na kwenye viunga vyake. Ijapokuwa kila mara wanasomba na polisi na kuwekwa mahabusu lakini wakitolewa tub ado huendelea na shughuli zao hizo hizo wanaacha kwenda vijijini wakawekeze katika kilimo na ufugaji, lakini siwalaumu wao, ila nailaumu serikali inayoshindwa kuwawekea mafunzo thabiti ya ujasiriamali tangu wakiwa shule ya msingi, hata somo la sayansi kilimo lililokuwapo shuleni siku hizi hata haliko katika mitaala, basi waache vijana wajikimbilie mjini na taifa kuwa taifa la vibaka.

Katika ofisi ya wizara ya ulinzi na jeshi lakujenga taifa, Mwenge, Mlalakuwa hali ya utulivu ilikuwa imetawala, ni bendera tu ya Taifa iliyokuwa ikipepea huku na huko kadiri ya upepo ulivokuwa ukiitaka. Geti lilifunguliwa taratibu na mwanajeshi aliyekuwa lindoni siku hiyo.
“Kuna mzigo wenu hapa,” kijana mmoja aliyekuwa juu ya pikipiki aina ya Yamaha alikuwa akiwaambia walinzi hao.
“Ok, nenda mlango ule pale kuna mwanadada pale mkabidhi,” yule MP akampa maelekezo baada ya kusoma anwani na kukuta imeelekezwa katika ofisi ya waziri mwenyewe.
Katibu muhtasi wa wizara, Miranda, alisaini kitabu cha dispatch cha kijana huyo kamba ameupokea mzigo huo katika hali ya usalama. Kisha wakaagana.

Kilikuwa ni kikasha cha mbao, kilicho tengenezwa vizuri na kupigwa vanish safi, pembeni anwani yake ilikuwa imeandikwa kwa maandishi ya chuma yaliyokuwa yaking’aa sana, na kwa sababu kilikuwa na anwani ya ofisi haikuwa tabu kwa Miranda kukifungua kujua ndani kuna nini kwa kuwa ni mzigo wa kiofisi, akachukua kijinyundo kidogo na kubabazua mfuniko wa kikasha hicho nao ukafunguka, ndani yake akakuta kitu kama box hivi, alipoligusa lilikuwa la baridi kama lina barafu ndani yake, akaondoa gundi iliyofunga box hilo na kulifungua ndani, huko akakuta kasha maalum sililoruhusu barafu kuyeyuka akaondoa mfuniko wake.
“Aaaaaaaaaaaaaaaiiiiiiiiiggghhhhhhhhh!!!!!!!” ilikuwa ni kelele moja kali kutoka kwa Miranda, mara ikakatika ghafla na kishindo cha kikasikika, Miranda akaanguka na kupoteza fahamu.

Mp aliyekuwa getini alisikia kelele ile na ukinya uliofuata akamwachia mwenzake lindo akakimbia kutazama kuna nini, alipoingi alimkuta Miranda chini hana fahamau, akaomba msaada haraka na wengine wakatoka maofisini kuja kumsaidia kwa huduma ya kwanza, hakuna aliyejua ni nini kimeamfanya aanguke. Ni pale mwanajeshi mmoja aliposogelea lile box akabaki kaduwaa, kinywa wazi. Hakutaka kuyaamini macho yake kwa kile yanachokiona. Kichwa cha binadamu, kichwa cha Gwamaka kilikuwa kimetulia ndani ya box lile, hakuongea kitu alitoka nje na kulia sana. Kila aliyeingia ndani ya ofisi hiyo alitoka akilia kwa uchungu.

Brigedia jenerali Kyambassa alikuwa hatulii ofisini, alitoka kona hii ya ofisi na kwenda ile kule, akishika hiki na kuacha kile, kama umemzoea ungeweza kumjua wazi jinsi alivyoshikwa na hasira kwa ndita zilizojipanga katika paji la uso wake, na kufanya kama matuta ya kuwalazimisha madereva kupunguza mwendo barabarani. Hakuwa na amani mwilini wala moyoni, kijasho kililowesha suti yake ya kijeshi yenye rangi ya kijani kibichi, kama haikutosha hata viatu alivyovaa vilionekana kumbana ghafla, akavilegeza gidamu zake na kuendelea kuizungukan ofisi hiyo bila kuchoka, hakuweza kukaa kwani alihisi kiti ni cha moto.

“Hii ni dharau, dharau iliyopita kipimo,” Kyambassa aliongea kwa ukali kuwaambia watu wachache waliokuwamo katika ofisi hiyo. Kwa ujumla hakuna aliyeongea kila mtu kama si kutiririkwa na machozi basi alibaki katumbua macho akitazama lile kasha la mbao safi lililotumwa kwao likiwa na zawadi ya kichwa.
"Afande, kiukweli ni swala linaloumiza sana, sasa kama huyu wamemfanya hivi ni vipi kuhusu Jamil, komandoo wetu, kwa maana tunajua thamani ya komandoo mmoja, sisemi Marehemu Gwamaka hakuwa na thamani ila yeye tayari tumeshampoteza hatuwe zi kuimjadili, lakini vipi huyu aliyebaki ambaye hatuna mawasiliano naye na wala hatujui yuko wapi, pia na vipi wale wanamaji wetu ishirini pamoja na wale Warussia watano?” aliongea kwa uchungu Kanali Hosea Mlawa. Ukimya ukatawala tena.

“Hapa tutajadili lakinin jibu halitapatikana, mi nafikiri sisi kama wapiganaji ambao usalama wa watoto wetu uko mikononi mwetu tuamue jambo moja, tuiongie kijeshi Somalia, tukawatwange hao wanaojiita maharamia tuwachukue ndugu zetu,” aliongea kwa jazba mwanamama pekee aliyekuwa katika jopo hilo la watu wa juu kabisa wa JW.
Brigedia Jenarali Kyambasa, alionekana kujifuta machozi kila wakati, mara hii alikuwa ameketi katika kiti chake cha kazi ambacho mbele yake kilizungukwa na na viti kadhaa vyote vikiwa vimekaliwa na watu waliofura mpaka mashavu yao yakavimba, hakika kama angetokea Msomali hapo angegombaniwa kama mpira wa kona.
“Ukiona mtu mzima analia waziwazi mbele za watu, ujue kuna jambo, mimi ndugu zangu, nimehuzunishwa sana na kitendo hiki, nimekerekwa tangu ndani, ningekuwa na uwezo ningeshusha kombora moja na kuipoteza hiyo nchi katika uso wa dunia,” Kyambassa alizungumza.

Ukimya bado ulikuwa ukichukua nafasi kila wakati kati ya jopo lile kwa maana simanzi ilitawala kuliko maamuzi.
Mjadala uliochukua takribani masaa mawili haukuzaa matunda, ilibidi uhairishwe kwanza ili kila mjumbe akatafakari kuhusu hilo, lakini kwa wakati huo iliazimiwa kichwa cha Gwamaka kikahifadhiwe katika hospitali ya jeshi ya Lugalo na shughuli za mazishi zisiwepo mpaka ufumbuzi utakapopatikana ili mpiganaji huyo mahiri azikwe kishujaa. Swala lilibaki ni kumuokoa Jamil kama bado yuko hai na wengine ishirini na watano waliokuwa wakisafiri na meli hiyo.
Ilibidi Brigedia Jeneral Kyambassa akaonane na mkuu wa majeshi ili kuona wao wawili tu wafanyeje. Bado hata walipokutana mjadala kati ya wawili hao haukuwa na muafaka na ikaonekana wazi kuwa shauri hilo la kuingia katika nchi nyingine kwa nguvu linaweza kuleta shida katika uhusiano wa kimataifa kwani aliyewatenda hayo ni kikundi tu Fulani na maamuzi ya mwisho kikatiba kutangaza swala hilo au kulisaoni ni Rais tu mwenye mamlaka.

“Hapana Kyambassa, najua nia yako lakini tusifike huko, tunahitaji amani na majirani zetu, ni kweli usemavyo kuwa hatuwezi kufanikisha hili kidiplomasia kwa sababu nchi yenyewe haina serikali, kila mtu anaamua anavyotaka, lakini tutumie mbinu nyingine, mi nadhani peleka makomandoo wengine wawili wakamalize hiyo kazi,” alimaliza kuzungumza Jenerali Mubah aliyekuwa mkuu wa majeshi mwaka huo, yeye hakukubaliana na uamuzi wa kuingia kijeshi ila akatoa mbinu mbadala ya kufanya.

Brigedia Jenerali Kyambassa akakubaliana na mkuu wake wa kazi, akampigia saluti na kuondoka ofisini hapoi kurudi ofisini kwake ili kuongea na wale aliowaacha ambao walikuwa wanasubiri jibu kutoka kwa mkuu.
Jopo lilirudi tena mezani chini ya Kyambassa, wakapewa mrejesho wa kikao chake na mkuu, kila mmoja alionekana wazi kutoridhiswha na uamuzi huo lakini waliombwa subira ichukue nafasi, swali likawa gumu, nani aende akashike kazi hiyo katika nchi ya Somalia. Jopo likamteua Komandoo mchanga kabisa Daudi wa Daudi akisaidiana na mwingine Sebeki.
Daudi alikuwa ndiyo kwanza anamalizia mafunzo yake huko Cuba na Sebeki alikuwa tayari nchini akiendelea na majukumu mengine ya kitaifa.

Daudi alipokea barua kutoka kwa mkuu wake wa kikosi akitakiwa kufika Somalia moja kwa moja ili kuifanya kazi hiyo, barua ilimpa maelekezo ya nini kilichotokea na nini anachotakiwa kufanya. Kwa kuwa tayari alikwishakuwa mwana wa jeshi hakuwa na la kukatata bali jibu kwa mkuu wake wa mafunzo hapo Havanna, Cuba lilikuwa ni “Yes, Sir!” na siku iliyofuata aliagwa rasmi na kuondoka Havanna kuelekea Mogadishu kuokoa jahazi.

BANDARI YA ZAMANI-MOGADISHU
“Mimi watu wabishi nawapenda sana, hivi wao hawakuwahi jiuliza kuwa kwa nini wenzao wenye nguvu huko Maghalibi wametelekeza meli zao?” Sharon alikuwa akizungumza katika kikao kidogo na vijana wake ndani nya kijichumba kimoja katika bandari ya zamani ya Mogadishu huko Somalia. Tayari walikwishajua kuwa kuna makomandoo wawili kutoka Tanzania wameingia nchini mwao kwa minajili ya kuokoa wenzao.
“Hii ni vita Sharon,” Shalabah alimwambia Sharon kutoka pale alipokuwa ameketi.
“Kama ni vita basi tutapigana mpaka mwisho, wanamkanyaga nyoka mkia, wanafikiri walivyompiga Idd kule Uganda mpaka leo wana uwezo ule? Wameumia, hapa ndipo watakapofia na kuzikwa,” Sharon alikuwa akiongea huku akishikashika kisu chake kikali alichokichomoa kutoka alani mwake.

“Kwa hiyo mkuu unatuambiaje?” kijana mmoja mwembamba mrefu kana kwamba anakula saruji alisimama na kumuuliza Sharon, mgongoni mwake alikuwa na bunduki kubwa AK 47 na kujizungushia mkanda mrefu wa risasi.
“Hakuna linguine, haina haja ya kuwaacha hai, muwasake mkiwapata muwaue hapohapo wala msiniletete mimi,” Sharon alimaliza na kuwataka vijana hao kutawanyika.


Fasendy alishusha sigara yake kutoka kinywani mwake ilimokuwako kama dakika mbili mfululizo, aliitazama kama imesiha lakini ilikuwa bado inafaa kuendelea kuvutwa, akapiga pafu moja na kuteremsha mkono, akaweka kishungi hicho ndani ya kibompoli maalum kwa kazi hiyo. Akashusha pumzi ndefu na kisha akajimininia glasi moja kubwa iliyojaa maji. Akaendelea kutega windo lake palepale, maana alijua wazi kuwa windo hilo litapita tu tena muda si mrefu sana. Pembeni akiwa na bunduki kubwa ya masafa marefu maalum kwa kudunguli lenye kuingia risasi moja tu, aliendelea kusubiri akiwa juu kabisa ya jengo la ghorofa lilikuwa likitazamana na hoteli ya Somali Hotel, katikati ya mji wa Mogadishu. Fasendy alikuwa akimfuatilia komandoo Sebeki tangu siku aliyoingia pale uwanja wa ndege bila ya yeye kujua.

Sebeki hakujua kama Daudi kafika na wapi yupo alkadhalika kwa Daudi nako ilikuwa hivyohivyo, Fasendy alijua ujio wa Sebeki lakini hakuujua wa Daudi, hivyo alimweka kwenye uangalizi wake kwanza ili ajue mtu huyo atafikia wapi na uwezo alionao katika shughuli hiyo.
Sebeki ye akiwa hana hili wala lile, aliendesha maisha kama raia wa kawaida, akifuatili chinichini kujua ni wapi yalipo maficho ya maharamia hao ili asababishe vurugu ambayo itawaachia historia. Kwa ujumla aliwapania sana. Hii ilikuwa ni mbinu yake anapotaka kuvamia sehemu, kujichanganya na wakaazi na kufanya kila kitu pamoja nao lakini akiwa na wazo moja tu kichwani mwake, kulipa kisasi kabla hawajamuwahi kwa maana hapo alijua wazi kuwa ni lazima mmoja amuwahi mwenzake ili shughuli inoge.
Wakati maharamia wameamua kuwa wakimuona basi ni kumuua tu nay eye alijiseme atakayejipendekeza nayeye atahakikisha anatenganisha mwili na roho. Alikuwa akitembea taratibu kwenye vijia vya hotel hiyo. Muda wote Sebeki alikuwamo katika pembe za hotel hiyo akipata chakula cha mchana pa si na wazo lolote. Alipokwishamaliza, aliondoka na kuelekea katika chumba chake, wageni walikuwa ni wengi sana katika hotel hiyo hivyo kulikuwa na nyendo nyingi za hapa na pale.

Fasendy katika angalia angali zake alimuona Sebeki, kama alivyoelekezwa akaweka sawa bunduki yake akaitazamisha kule kunako lengo lake na kutumbukisa jicho lake katika kiona mbali kilichofungwa juu kidogo ya bunduki hiyo, akajaribu kutafuta shabaha lakini ilikuwa ngumu kwa Sebeki alikuwa akipishana na watu mbalimbali. Dole la shahada la mkono wa kulia la Fasendy lilikuwa tayari katika kifyatulio, likiminya kidogo na kuachia mara kadhaa.
“Shiit!” aling’aka pale alipomuona Sebeki akiingia kwenye mlango Fulani na kupotelea humo. Akaiachia ile bunduki yake na kutoka pale alipolala, akachukua sigala yake nyingine na kuiwasha kabla ya kuanza kuivuta kwa fujo.
“Idara ya usalama Tanzania imeishiwa, mpaka inawatuma hawa, mi ilitegemea kumuona Kamanda Amata hapa, na angekuja yule nakwambieni kweli Mogadishu pangekuwa padogo kama kidonge cha pirton,” Fasendy akamwambia kijana mwingine aliyekuwa nae hapo.
“Kwa nini unasema hivo?” yule kijana akauliza.
“Eh, we acha tu, yule shetani, ana mbinu za kijasusi ni hatari, na sijui kapatwa na nini mpaka simuoni kwenye mkasa mkubwa kama huu,”

MOSCOW - URUSI

Maofisa wa jeshi walikuwa wamekusanyika katika makaburi, wakiwa kwenye ibada maalumu ya mazishi ya kiongozi wa juu wa jeshi hilo ijapokuwa alikuwa amestahafu lakini bado alikuwa na heshima yake kubwa katika jeshi la nchi ya Urusi.
Akiwa katika kumalizia ibada hiyo, mkuu wa jeshi la Urusi Bwana Vladimir Kalachinikov alipenyezewa kijibahasha mahali alipokaa, alipokichuku na kusoma juu kilikuwa kimeandikwa kwa lugha ya kiingereza, Confidencial.

Akiwa anvuta hatua fupifupi akitoka katika eneo hilo la makaburi, Vladimir alikuwa akiifungua bahasha ile huku akihakikisha haionekani na mtu mwingine. Akaanza kuisoma taratibu huku akiendelea na mwendo wake, mlinzi wake alikuwa nyuma kidogo. Colonel Vladmir akasimama ghafla, akatzama saa yake, akashusha mkono chini, akatikisa kichwa kama kuna kitu kilikuwa kinamsumbua kwa ghafla, akaiweka ile bahasha katika mfuko wa koti lake.
Baridi ilikuwa kali sana, theruji iliganda kila mahali, miti, maua, magari, nyumba vyote vilikuwa vyrupe vikipendezesha na hali hiyo hadimu kwa nchi zetu zenye uoto wa kisavanna, hiyo yote ilihashiria kuwa Krismasi imekaribia. Akafika mahali akasimama huku amejishika kiuno, palepale alipo gari yake ikasogea na kusimama mbele yake, akaingia pamoja na mlinzi wake na kumwamuru dereva amfikishe kwa waziri wa ulinzi mara moja.

Mazungumzo yake na mkubwa wake wa kazi ambaye ni waziri wa ulinzi wan chi ya Urusi yalikuwa ni yale yale jinsi ya kuwakomboa wanajeshi wao watano waliokuwa pamoja na wengine wa Tanzania.
“Unajua, Colonel Vladimir, wale jamaa sio wa kuwaongia ovyo kama unavyofikiri, ni wanyama wabaya kuliko wanyama wenyewe,” alizungumza waziri wa Ulinzi akimweleza Colonel Vladimir Kalachinikov.
“Sasa tunafanyaje kiongozi, na unajua hali halisi iliyopo kule ni karibu wiki sasa, watu wetu wanateseka,” alilalamika Vladimir.

“Ok, fanya hivi, chagua mtu mahiri anayeweza kuifanya kazi hii kwa umakini, umtume, mwambie afanye kazi hiyo kwa siri maana akijulikana tu, wale jamaa watafanya kweli,” Waziri wa ulinzi akamaliza hapo. Colonel Vladimir Kalachinikov akasalute na kutoka ofisini hapo.

KAMBI YA JESHI YA SARATOV-URUSI
COLONEL Vladimir Kalachinikov, alikuwa ameketi kitini katika ofisi ndogo anayopenda kuitumia mara kwa mara kama anakuwa na mambo magumu ya kuamua juu ya idara hiyo ya ulinzi. Siku alikuja hapa na ujio wake ulikuwa ghafla hata kwa viongozi wa kambi hiyo ya mambo ya anga na milipuko mikubwa ya jeshi la Urusi inayojulikana kama ‘Eagle Air Force Base au Eagles – 2’.

Alikuwa ameketi kimya akiwa hajui la kufanya, alishika hapa na pale lakini yote hayo yalikuwa ni bure. Baada ya dakika kama kumi hivi, mlango ukafunguliwa na wanajeshi wengie sita wenye vyeo vya juu waliwasili ofisini hapo, wakatoa salute zao na kila mmoja kuchukua kiti chake, wote waliweka kofia zao juu ya meza kwa mtindo wa kupendeza.
“Karibuni sana makamanda, najua mtashangaa sana leo nimewaita mje Saratov badala ya Moscow tuliyoizoea, kuna jambo moja la kuamua kwa pamoja, na hili si jipya ni lile ambalo mnalijua, juu ya ile Manowari ya Tanzania iliyotekwa kule Somalia ikiwa na makobora kumi na mbili ambayo yalikuwa yakija hapa bahari ya Caspian kwa majaribio, ukiachana na hilo, tuna wanajeshi watano wako pale wanashikiliwa na hao Maharamia, sasa kwa sauti yetu moja, tunafanyaje kwenda kuwakomboa watu wetu?” colonel Vladimir alimaliza kuzungumza. Wajumbe wakabaki kimya kwa muda, wakitafakari jambo au mambo Fulani.

“Colonel, mi nafikiri hili swala tulishalizungumza, na tukaona kwa kuwa Tanzania imechukua hatua, basin a tuangalie wanafikia wapi vinginevyo kama watahitaji msaada wetu, ila kwa idara ya usalama Tanzania nawaaamini asilimia 95, wanaweza kazi, labda tungepata ripoti kwanza,” akazungumza mkuu wa jeshi kutoka Tupolev.
“Makamanda, kule hali ni tete sana, komandoo mmoja wa Tanzania amechinjwa, na mwingine hajulikani alipo, ijapokuwa wizara ya ulinzi ya Tanzania imeamua kupeleka wengine wawili, lakini kule ni kule tu,” Colonel Vladimir alitoa majibu kwa kifupi. Baada ya mabishano makali, akasimama mkuu wa kikosi cha wanaanga wa Saratov.

“Mimi sioni haja ya kucheka na hawa watu, watatusumbua mpaka lini? Nchi nying za maghalibi meli zao zimetekwa mpaka sasa wamekaa kimya hakuna jitihada wanazofanya, haya bora wao ni meli za mizigo, sasa hii ya sasa ni ya kijeshi, ina uhusiano mkubwa sana na sisi, hatuna haja ya kucheka nao, tufanye uchunguzi, tuone walipo mi ntatuma ‘tai’wawili tu wanatosha kufagia hao mende wote,” kila mtu katika mkutano huo akacheka baada ya kauli hiyo iliyotoka kwa bwana Makubaliano yakapitishwa, mchunguzi apelekwe akafanye uchunguzi wa eneo zima, wapi hao jamaa wanajificha na wapi wanafanyia shughuli zao, awape maelekezo kwa vipimo vya ardhini, na baadae wakafanye kazi ya kuwakomboa wenzao. Hilo likapita kwa wajumbe wote. Kikao kikavunjwa na colonel Vladimir akapeleka mapendekezo wizara ya ulinzi ili kuanza mara moja, ijapokuwa hakuwa na uhakika kama litakubaliwa kwani kutuma ndege vita kwenye nchi ya mwenzako kwa sheria za kimataifa ni uvamizi.

MOGADISHU

SEBEKI alikuwa akitoka kuoga, mara tu alipofika katika chumba chake cha kulala akasikia hodi, mlango ukigongwa mara kwa mara, akajiweka tayari, akachukua bastola yake na kuikamata sawia, akauendea mlango na kuufungua, kabla hajamkaribisha aliyegonga akaingia ndani.
“Vipi, mbona unavamia vyumba vya watu?” Sebeki akauliza huku bastola lake likiwa limemtazama mwanadada huyu.
“Usiniue, nina kitu cha kukwambia,” akasema yule msichana.
“Sema haraka, kabla sijabadili mawazo,” Sebeki akamwambia yule dada.
“Ndugu yako, ndugu yako amekamatwa na maharamia, nenda kamsaidie watamuua vibaya,” yule msichana aliongea huku akikatakata maneno.

“Wewe, kama ni maigizo sisi Watanzania ndio tuna chuo cha sanaa hiyo, mi kwetu sina ndugu, na nani aliyekutuma?” Sebeki akamuuliza, akamkamata kwa kono lake moja la kushoto na kumsokomeza bastola mdomoni, “Nafumua ubongo wako, sijaja kucheza huku!” akamalizi kusema na kuitoa ile bastola kinywani mwa yule msichana, akamwacha akitetemeka pale chini. Sebeki aligeuka na kuliendea kabati, yule msichana alitumia nafasi hiyo, alichomoa bastola yake iliyopachikwa juu kabisa mapajani kwa ndani ya nguo, kwa haraka alimlinga Sebeki. Sebeki aliposikia mliowa kiondoa usalama akajua tayari, kumbe alifanya hivyo kwa makusudi mazima, alijirusha upande wa pili wa kitand na ile risasi ikamkosa. Akanyanyuka kama umeme akatuliza guu lake kichwani mwa yule msichana na kumbamizia ukutani, akamnyanyua mzima mzima kwa mikono yake miwili, kifua chake kilichokuwa wazi kilituna na misuri ilidinda kwenye mikono yake, akamrusha yule msichana katika dirisha la kioo na kudondokea nje.

Kelele za alam za magari zilisikika baada ya ule msichana yule kudondoka juu ya gari zilizokuwa maegeshoni. Sebeki akakung’uta mikono yake, na kufungua kabati, akavaa nguo zake haraka haraka na kuchuku bastola zake mbili, akajiandaa kuteremka chini ili aone nini kinaendelea. Akashuka chini na kuzunguka upande wa pili wa ile hotel, akatazama watu waliokuwa pale wakimsaidia yule msichana aliyedondoka kutoka ghorofa ya tatu, akachukuliwa na kupakiwa kwenye gari moja iliyochoka sana, na wale waliompakia walionekana wazi si wema sana. Sebeki akili ikamcheza, ‘lazima niwafuatilie’ akajisemea, akachomoka pale alipo na kuikimbilia gari yake.

“Nooooooooooo!!!!!!!!!!!!” sauti kali ya mtu ilisikika nyumaya Sebeki umbali kama wa mita mia moja, Sebeki hakuifuatilia kwani hapo palikuwa na mkanganyiko wa watu. Akaingia na kujifungia mlango, mara akasikia kioo cha gari yake kikipigwa kwa ngumi, hakumjua mtu huyo. Sebeki akawasha gari, lo, kumbe maharamia wale walikuwa wametega bomu kwenye injini ya gari ile, na vitendo vyote hivyo Daud aliviona kwani aliwafuatilia toka mbali. Mlipuko mkubwa ukatokea, anga yote ikawa nyekundu na moshi mzito, ile gari ilinyanyuliwa juu na kugeuzwageuzwa kama kiberiti, ikaanguka na kutua juu ya gari nyingine nazo zikadaka moto, kizaazaa. Kwa kishindo kile, Daudi aliwahi kulala chini, lakini msukumo wa mlipuko ule ukamsukuma na kumbamiza kwenye gari ya jirani, Daud, akajiviringa na kutumbukia kwenye mtaro wa maua na kushuhudia ule moto ukiwaka hewani.

“Kazi imekwisha! Nimeshaingiza pesa,” Fasendy alizungumza na kugeuka akiuacha mlipuko ule ukiendela nyuma yake, akatembea taratibu kuelekea gari iliyoandaliwa kumchukua, akiwa anavuka barabara ndipo akamuona Daud akiwa hajiwezi, anahangaika ndani ya ule mtaro.
“Usipofanya jitihada za kuondoka ndani ya masaa manne nakuua,” Fasendy akamwambia Daud kisha akaingia kwenye gari na kuondoka zake.

Tarumbeta maalum ya maazishi ilimaliza kupulizwa, amri ya kijeshi ikatolewan risasi kadhaa zikapigwa hewani huku wanajeshi wengine wakiwa wamepiga salute kama heshima yao ya mwisho kwa wapiganaji hao Sebeki na Gwamaka ambao walikuwa wakizikwa rasmi katika makaburi ya Kinondoni. Ilikuwa siku ya huzuni sana kwa familia zao, na wapiganaji wote kwa ujumla, hasira na uchungu zilitawala miongoni mwa wale wenye dhamana. Manyunyu ya mvua yalinyurunyuta na kufanya hali ya hewa ya jiji la Dar es salaam kuwa tulivu kama wakazi wenyewe ambao walikuwa wakifiuatilia habari hiyo ama kwenye Tv au redioni, kila mtu alishikwa na hasira.
Siku hiyo gumzo kwenye vyombo vya habari lilikuwa hilo, wahariri wakaandika kwenye tahariri zao,vipiondi vya kuruhusu watu wapige simu navyo vikawa ni shida, kila aliyepiga alilaumu, na alipendekeza hata kama jeshi basi lipelekwe likafanye kazi hiyo kwa mapana yake.

Brigedia Jenerali Kyambassa alifuta machozi, na kuiangalia jopo lake lote, hakuna aliyekuwa na furaha.
“Tumepoteza askari 1600 na 1600 wengine hatujui walipo, nafikiri mmenielewa kwa lugha hiyo, kwa maana komandoo wetu mmoja ni sawa na battalion moja, yaani askari 800, hawa jamaa yumkini kama si mashetani basi wana mbinu za ajabu sana kwenye mashambulizi yao,” Kyambassa aliongea kwa ukali.
Akiwa katika kikao hicho, mara katibu wake akaingia na moja kwa moja akamwendea, akamnpng’oneza kitu.
“Naombeni mnisamehe kidogo makamanda,” Kyambassa akatoka na yule katibu wake wakaingia ofisi ya pili. Kyambassa akakutana na Miranda, katibu muhtasi wa wizara ya ulinzi.
“Karibu Miranda,” akamkaribisha. Miranda akatoa bahasha moja ya serikali na kumkabidhi. Kyambassa alitetemeka akajua hapo tayari hana kazi na hakuna kitu kingine, akaipokea na kuanza kuifungua taratibu huku mikono yake ikitetemeka.

Kyambassa akashusha pumzi ndefu, akamtazama Miranda usoni, Miranda nae alikuwa kakaza macho kwa mzee huyo aliyechafuka kwa vyeo vya kijeshi.
“Ok, Nimeelewa,” akamwambia Miranda kisha akainuka na kurudi kikaoni. Akawakuta wajumbe wakiwa wanabadilishana mawazo, alipoingia wote wakarejesha ukimya. Kyambassa akaenda palepale alipokuwa kwanza, akajiweka sawa na kuwatazama wajumbe wa kikao. “Ndugu wajumbe, nimepata taarifa sasa hivi ya kiofisi, kusitisha mara moja operesheni yoyote inayohusiana na utagutwaji au uokozi wa watu wetu huko Somalia, hivyo sina budi kusema kikao hiki hakina haja kuwepo mpaka tutakapopata taarifa nyingine, mission aborted,” Brigedia Jenerali Kyambassa akawaambia wajumbe wake. Kikao kikavunjika na kila mtu akarudi kuendelea na majukumu yake ya kulijenga taifa.

GINA binti Komba Zinga Zinga alikuwa ametulia tuli katika ofisi ya AGI investment, ndani ya jengo la JM Mall, ghorofa ya tano. Akiwa anaangalia televisheni, ni kipindi kirefu sana alikuwa ndani ya ofisi hiyo bila boss wake kamanda Amata ambaye mara tu alipoachishwa kazi miezi sita iliyopita alijikita kwenye kilimo huko kwao Lindi. Ni mara chache sana alikuwa akija kutembelea ofisi hiyo, hata yeye Gina alikuwa akija mara chache sana, mara nyingi alikuwa akifanya kazi zake za kiofisi katika kituo cha polisi cha kati kwa kuwa yeye alikuwa ni muajiriwa wa jeshi la polisi.
Simu ya ofisini hapo iliunguruma kwa fujo, Gina akaitazama simu hiyo ambayo ni siku nyingi hakuwahi kuitumia, aliitazama na kuinyakuwa pa si kuotea ni wapi intoka, kaiweka sikioni na kusikiliza.
“Hello, Gina!” iliita sauti ya upande wa pili mara tu Gina alipoiweka simu ile sikioni. Ilikuwa ni sauti ngeni hakuwahi kuisikia kabla.

“Ndio mimi, unasemaje?” Gina akajibu.
“Unaongea na idara ya usalama wa taifa kitengo maalumu kisicho na mipaka, TSA,” ile sauti ilimwambia.
“Nakusikiliza,” Gina akajibu.
“Unatakiwa kufika katika ofisi hii kesho saa mbili asubuhi, asante sana,” ile sauti ikatoa agizo na kukata simu bila kusubiri jib u la ndio au hapana. Gina akatahayari kwani alijiuliza ni vipi watu hao wamejua kuwa yuko ofisini hapo mpaka watumie simu ya ofisi kuweza kumpata. Akaitua simu na kuiweka kwenye kikalio chake kisha akaketi kitini, akaitazama ofisi hiyo ambayo ilikuwa bado haijapata mtu wa kukaa kama boss baada ya Amata kutoka. Ilikuwa ni ofisi maalumu ya kitengo cha usalama lakini ikionesha kuwa inafanya kazi za kijamii kumbe ndani yake kuna kikubwa kinachoendelea.
Ni Kamanda Amata aliyempendekeza Gina kuwa kama katibui muhtasi ndani ya ofisi hiyo miaka kadhaa nyuma pindi tu kilipoanzishwa kitengo hicho. Gina alikuwa ni polisi (WP), ambaye kwa kipindi cha miaka mitatu alikuwa akisomea sheria katika chuo kikuu cha Dar es salaam.

Gina alishtushwa na wito huo, ‘Kwa nini asipige Madam S au mtu mwingine ninayemfahamu?’ akajiuliza. Kichwani mwake alihisi kuchanganyikiwa, hakujua kama ni wito wa kweli au ni mtego kwake, maana ni siku nyingia hakuingia kwenye kashkash za namna hiyo. Akachukua simu yake ya mkononi na kuimpigia Madam S.
“Yes madam, shikamoo!” alimsabahi.
“Marhaba Gina, mbona kimya sana mwanangu, upo?” madam aliuliza katika simu.
“Nipo mama niende wapi?” Gina alisema, akatulia kidogo na kupisha mazungumzo ya hapa na pale na Madam S huku moyoni akiwa na shaka kumuuliza juu ya ile simu lakini mwishowe akaamua kuuliza.
“Aaaa Gina, we fanya kama simu hiyo ilivyokuelekeza, usiwe na wasiwasi,” Madam alimtoa hofu binti huyo na simu ikakatika. Gina akpigwa na butwaa, ‘kuna nini?’ alijiuliza.

SIKU ILIYOFUATA saa 2 asubuhi
OFISI YA T.S.A
MADAM S, au H.O.T (Head Of TSA) alikuwa na shughuli maalumu siku hiyo katika ofisi ya TSA, akiwa nadhifu katika suti yake ya rangi ya udongo, nywele alizotengeneza katika saluni kubwa ya kisasa, alikuwa amesimama mbela ya meza yake kubwa kabisa ya ofisi, mezani hapo kukiwa na kikasha kimoja cheusi kimetulia. Pembeni ya Madam S kulikuwako Chiba, Dr Jasmine, Scoba na Gina. Dr Jasmin alikuwa amesimama akitazamana na Madam S. ukimya ulitawala kati ya wote.

“Dr Jasmine, baada ya kufanya kazi kwa kipindi kirefu na ofisi ya TSA, leo hii ofisi hii, kwa mamlaka iliyopewa na ofisi ya Rais, inakuteua kuwa mmoja wa wanaunda idara hii nyeti, ukiwa kama daktari bila kupoteza taaluma yako, sasa utatambulika kwa utambulisho maalum, TSA 3, utasaidia ofisi hii kwa kila jambo linalohusisha utabibu,” Madam S aliongea maneno hayo huku akimtazama Dr Jasmine aliyekuwa kasimama mbele yake kiukakamavu. Madam S Litoa baeji maalum ya rangi ya dhahabu, yenye nembo ya serikali na chini yake ikipambwa kwa maandishi yenye nakshi ya kuvutia, Tanzania Secrety Agency 04. Madam S hakuishia hapo, alikinyanyua kile kikasha cheusi pale juu ya meza na kukifungua.

“Na hizi ndio zana zako za kazi tangu leo, hutakiwi kuiacha nyuma, unatakiwa uibebe kila uendapo, kwa utii na uangalifu ili itumike pale tu inapobidi,” madam S akamkabidhi kile kikasha, ndani yake kulikuwa na bastola moja ya kisasa na risasi nane, pembeni yake kulikuwa na kiwambo cha sauti kwa ajili ya bastola hiyo. Dr Jasmin akakipokea kikasha hicho na kurudi alipokuwa mwanzo. Dr Jasmine kabla ya kuwa daktari alikuwa ni muajiriwa kati jeshi la kujenga taifa, baada ya kuacha kazi hiyo akajikita katika udaktari zaidi chini ya wizara ya afya akiwa ni muajiriwa, Kamanda Amata alipenda sana kumtumia daktari huyu katika mambo yake hasa yakihitaji taaluma ya kiganga, alimuamini kwa kuwa alikuwa msiri, jasiri na asiye na woga, Madam S alipopewa pendekezo la kumtumia mwanadada huyo hakuwa na kipingamizi na Kamanda, alimruhusu aendelee kumtumia.

“Gina binti Komba Zinga Zinga, baada ya kufanya kazi kwa kipindi kirefu na ofisi ya TSA, leo hii ofisi hii, kwa mamlaka iliyopewa na ofisi ya Rais, inakuteua kuwa mmoja wa wanaounda idara hii nyeti, ukiwa ni muajiriwa wa jeshi la polisi na ofisi hii inalitambua na kuliheshimu hilo, sasa utatambulika kwa utambulisho maalum, TSA 5, utasaidia ofisi hii kwa kila jambo utakalotakiwa kufanya, kuanzia sasa nafasi yako katika jeshi la polisi haitakuwepo tena kwa mujibu wa sheria iliyowekwa juu ya kuunda na kuteua wadau wa ofisi hii,” Madam S vilevile, kama alivyofanya kwa Jasmine alimkabidhi beji maalum Gina iliyoandikwa Tanzania Secret Agency 05. Kisha akamkabidhi vifaa vile vile kama alivyofanya kwa Dr Jasmine.

Baada ya shughuli hiyo walipiga picha ya pamoja, Madam S, Chiba TSA 02 idara ya teknohama, Scoba TSA 03 idara ya usafirishaji na uokoaji, Dr Jasmin TSA 04 idara ya afya, Gina TSA 05 asiye na idara maalum. Timu ilikuwa imekamilika, lakini bado ofisi hiyo ilikuwa haijapata mtu wa kushika beji ya TSA 01 ambayo mwanzoni ilikuwa na Kamanda Amata.
Tafrija fupi ndani ya idara hiyo nyeti ilikuwa ikiendelea, mara mlio wa chombo cha mawasiliano ukasikika, Madam S akabofya kitufe Fulani na screen maalum iliyo katika ukuta wa ofisi hiyo ikapata uhai, picha iliyoonekana hapo haikuwa nyingine ni ya waziri wa ulinzi.

“Ndiyo mheshimiwa,” Madam S aliitika.
“Nakuhitaji ofisini kwangu mara moja, bila kuchekewa,” Waziri wa ulinzi alimwambia Madam S kupitia chombo kile.

“Madam S, nimekuita mara moja kuna dharula ambayo tunahitaji ofisi yako iweze kutusaidia,” Waziri wa ulinzi alikuwa akimwambia maneno hayo Madam S aliyekuwa ameketi kitini, akisikiliza neno moja baada ya jingine. Mheshimiwa waziri akaendelea, “Manowari yetu kubwa Kirov Class, imetekwa Somalia na maharamia, leo ni wiki ya tatu, tumepelea makomandoo lakini wawili wameuawa kikatili na wawili hatujui walipoa, ndani ya manowari hiyo kulikuwa na wanajeshi 25 Watanzania isihirini na Warusi watano pamoja na makombora makubwa kumi na mawili, tunahitaji ufumbuzi wa jambo hili, haraka iwezekanavyo”.
Madam S aliendelea kumtazama waziri wa Ulinzi hata baada ya kumaliza kuongea, alitamani kumuuliza jambo lakini aliamua kuacha.

“Sawa nimekusikia, lakini unajua wazi kuwa ofisi yangu imepungukiwa tena imepungukiwa nguvu kubwa sana, unafikiri nitawezaje kulifanya hili kwa sasa? Kama mmetuma makomandoo na wawili wameuawa, we unaionaje hiyo kazi?” madam S akauliza.

“Ni kazi ngumu inayohitaji umakini sana,” akajibu waziri.
“Na unafikiri mtu makini ni nani wa kuweza kuikamilisha kazi hiyo?” Madam akauliza. Waziri wa ulinzi akamkazia macho Madam, akamtazama kwa hasira, maana alielewa kile anachokizungumza, kabla hajaongea kitu Madam S alikuwa amekwishanyanyuka na kutoka kwenye ofisi ile. Kichwa kilizunguka, hakujua nini cha kufanya, ugumu wa kazi aliyopewa na serikali aliuona ukimwelemea waziwazi, akitazama kwenye jopo lake hakuna amtu wa makabiliano ya ana kwa ana na mwenye wepesi na akili za haraka kama Kamanda Amata ambaye sasa hayupo kazini.
Alirudi ofisini akawakuta vijana wake bado wanagalipo wakiendelea na viburudisho vilivyo hapo. Akawaita wote mbele ya meza yake na kuwaketisha.

Kabla hajaongea kitu alijiinamia kwanza kwa dakika kadhaa akifikiria jambo.
“Tuna kazi ya kufanya Somalia, kuirudisha manowari iliyotekwa na wanajeshi waliopotea,” madam aliwaambia, wote wakatazamana, na minong’ono ya hapa na pale ikatawala.
“Samahani Madam, hapa katika hili tusifanye masihara hata kidogo, hii kazi ni ngumu sana na kiukweli bila Kamanda Amata tumefeli,” Gina alieleza na kuungwa mkono na wote waliopo katika kikao hicho.

“Kumbukeni Kamanda hayupo kazini, hivyo tunapoteza muda sana kumzungumzia kuliko kujipanga,” Madam S aliwaeleza na kuwaacha hapo yeye akatoka nje ya ofisi.
“….Siwezi kufanya kazi bila Kamanda Amata, we mwenyewe unajua uzito wa kazi,” ilikuwa sauti ya Madam S alipokuwa akiongea kwa simu, hakuna aliyejua ni nani anayebishana nae humo simuni.
Baada ya kama dakika kumi na tano hivi, Madam S alirudi ofisini akiwa katika hali tofauti na mwanzo, akaketi kitini. Akavuta simu yake na kuipiga namba Fulani kisha, akatulia kusikiliza.

“Scoba, chukua helkopta, sasa hivi kamlete Kamanda Amata, Gina atakuongoza anajua ni wapi alipo, nawasubiri hapa,” Madam alimaliza. Scoba na Gina wakachomoka, na kuingia garini, safari ilikuwa ni katika kituo cha polisi Oyserbay ambapo helkopta yao ya ofisi ilikuwa anaegeshwa hapo, baada ya kusainiana na ofisa anayehusika, Scoba na Gina walioondoka.


ITAENDELEA
1.jpeg
 
Ngoja niingize gari getini kwanza hii ndefu sana naweza jikuta nalala nje kwenye gari
 
Simulizi: Hujuma

Sehemu Ya Pili (2)

4… nangumbu – Lindi Vijijini

WATOTO wa shule ya msingi walisikika wakipiga kelele za woga, wakikimbilia madarasani na wengine porini. Waalimu wao walitoka nje kuangalia watoto hao wanakimbilia nini. Helkopta kubwa lilikuwa likitua katika uwanja wa shule hiyo.
Nyumba kubwa iliyozungukwa na maua mengi ya kupendeza, ilikuwa mbele yao, gina aliielekea mpaka mlngoni na kugonga kengele. Kamanda Amata akaibuka mlangoni na kuwatazama wawili hao.
“Karibuni sana,” akawakaribisha.

“Kamanda sisi sio wa kukaa,” Scoba akamwambia.
“Hata kama sio wa kukaa, lakini Gina hapa ni nyumbani kwake hawezi kuingia na kutoka,” Kamanda akawaambia huku akitoa miwani yake usoni, shati lake lilionesha wazi kuwa alikua ni mtu katoka shambani muda si mrefu.
“Kamanda Amata, hali ya mama yako ni mbaya sana, unatakiwa kuja nyumbani kumsaidia,” Gina alimwambia Kamanda kama alivyoagizwa na Madam S. “Najua, na nanjua kuwa hali yake mbaya lakini kwa sasa mwacheni afe, sina msaada,” Kamanda Amata alijibu huku akiipachika tena miwani yake usoni.
“Kamanda, hebu fikiri mara mbili juu ya hili, mpaka kukufuata na usafiri maana yake ni kuwa tuondoke sasa hivi,” Scoba alikazia.

“Haitatokea, nimebanwa sana na shughuli za kilimo, mahindi yangu yananihitaji, mikorosho nayo ndiyo hiyo hapo, vyote hivyo vinanisubiri, mifugo yangu hata sina mtu wa kuniangalizia nikitoka,” Kamanda akawaambia. Mazungumzo yalikuwa magumu sana kati yao na Kamanda Amata, haikuwa rahisi kwa Kamanda kukubali wito huo.
“Ninyi nani aliyewatuma, mpaka mnapoteza mafuta ya hilo chopa, kulileta huku porini kwetu?” Amata akauliza.
“Tumetumwa na ofisi, bibi kachanganyikiwa anakuhitaji nyumbani,” Scoba akasisitiza. Gina wakati huo alikuwa ameingia ndani na kuwaacha wawili hao wakiwa bado na mvutano. “Sikiliza Scoba, nenda kamwambie Bibi, siwezi kuja hata kwa mkinivuta kwa bulldoza,” kamanda Amata akamaliza mazungumzo yake akanyanyuka na kuondoka zake. Akamtazama Scoba palepale alipomuacha yeye akapanda pawatila yake na kuingia kazini.

Madam S, aliinama mezani, alionekana wazi kuchanganyikiwa kwa jibu alilolipata kutoka kwa Gina na Scoba.
“Amekataa kabisa amesema hawezi kuja kwa lolote,” Gina akamaliza. “Hata wewe Gina umeshindwa kumbembeleza Kamanda aje, unaniangusha Gina, umeingia kitengo cha ujasusi lazima ujue sometime kutumia body language,” Madam S alimwambia Gina. Ukimya ukatawala kati yao, Madam S hakuwa na la kusema, akanyanyuka na kutoka nje ya ofisi, akachukua gari yake na kuondoka.

Breki yake ya kwanza ilikuwa mbele ya ofisi ya wizara ya ulinzi, moja kwa moja akaingia katikia ofisi yam zee huyo anyependa kuitwa mheshimiwa pa si kuwajibika sawasawa kwa Watanzania.“Ndiyo Madam, najua umerudi na jibu zuri kinywani mwako,” mheshimiwa waziri akasema. “Hapana, hapa nimekuja kukwambia kuwa ofisi yangu haiwezi kiufanya kazi uliyonipa kwani uwezo tulionao ni mdogo sana kiutendaji mpaka tujipange nah ii itachukua miaka mingine sita,” Madam S akamwambia waziri wa ulinzi. Alipomtazama usoni waziri huyo alionekana kuvimba sura kwa hasira.
“Madam S, wizara ikishakupa kazi imekupa, utajipanga vipi utajua wewe, sasa habari za kunambia kuwa hauko tayari mimi sizielewi, unajua kabisa kuwa hili tayari limeshaiweka ofisi yangu katika hali ya sintofahamu, Mheshimiwa Rais atanielewaje wakati nimemhakikishia kuwa kila kitu kitakuwa sawa?” Waziri wa ulinzi akaongea kwa ukali, huku akiwa amesimama, kauma meno yake na kupigapiga ngumi mezani kwake.

Madam S naye alipoona hayo akawa amesimama akimtazama baba huyo aliyekuwa akipiga kelele bila mpangilio.
“Sikia, mheshimiwa, ulimpomfukuza kazi Kamanda Amata ulitegemea nini?” Madam S akamwuliza waziri. Kimya kifupi kikatawala kati yao. “Kwa hiyo unasemaje?” waziri akamwuliza Madam S.
“Nasema kazi haiwezekani, nenda kamwambie na mheshimiwa Rais hivyohivyo kuwa TSA haiwezo kufanya kazi hii mpaka miaka sita ijayo, watakapomtengeneza TSA 1 mwingine,” Madam S akamaliza na kugeuka kuondoka zake.
“Madam,” waziri akaita, Madam S akasimama akageuka kumtazama, “Kibarua chako kipo mashakani,” akamwambia, huku akiwa ameuma meno kwa hasira. Madam S akatoka na kubamiza mlango nyumba yake.

Hali ilikuwa tete kwa waziri wa ulinzi, aligundua kosa kubwa sana alilofanya miezi sita nyuma katika mkasa ambao uliandikwa kama riwaya na kupewa jina la Julai 7. Aliwaza na kuwazua hakuna jibu alilolipata juu ya hilo, alihisi uzee ukimjia kwa kasi, hasira zilimtawala, akatoka ofisini kwake mara moja na kuondoka zake.

Kikao cha baraza la usalama la taifa kiliitishwa kwa dharula katika ofisi maalumu ndani ya Ikulu ya Dar es salaam, kikihudhuriwa na wadau wa juu kabisa wa usalama. Katika ofisi hiyo ndogo inyojulikana kama Mraba wa Kilimanjaro, hoja ilikuwa nzito juu ya hatima ya wapiganaji wa Tanzania waliokuwa huko Somalia, hakukuwa na habari kabisa juu ya wapi walipohifadhiwa, au kufichwa, wazima au wameuawa, hali ilikuwa tete katika ya wadau hao wa juu kabisa wa usalama ambao hatima ya usalama wa Watanzania ipo juu yao. Mwanamke pekee katika jopo hilo Madam S alikuwa akiwasikiliza kwa makini na akipinga kabisa swala la idara yake kuingizwa katika sakata hilo hali hana nguvu ya kutosha, mwanamke alitunisha misuli ndani ya ofisi hiyo mpaka kila mmoja akabaki kimya. Baada ya mazungumzo hayo lawama zote zikarudi kwa Waziri wa ulinzi kwa kuwa yeye ndiye aliyeng’ang’ania Kamanda Amata aachishwe kazi kwa kile kilichodaiwa utovu wa nidhamu.

“Hatuwezi kufanya kazi hii bila ya Kamanda Amata,” akasema makamu wa Rais aliyekuwa akiongoza jopo hilo.
“Hapo mheshimiwa nakuunga mkono, hatukufanya jambo la busara kabisa kumtoa kazini Kamanda Amata, na kwa sababu hiyo ndiyo maana hata sasa tunakutana hapa ambapo si kawaida yetu, kwa nini Kamanda Amata asirudishwe kazini?” Mkuu wa majeshi aliliambia jopo na kuungwa mkono na jopo zima. Waziri wa ulinzi alikuwa kimya, hakuongea kabisa alikuwa akiwasikiliza wajumbe hao.

“Mimi nahitaji Kamanda arudi kazini, hapo ndiyo nitaifanya kazi hii kwa ufanisi wa hali ya juu,” Madam S akalieleza jopo. Uamuzi ukapitishwa wa kamanda Amata kurudishwa kazini, ikaandikwa barua na kusainiwa na jopo zima kama ilivyokuwa mwanzo, akakabidhiwa waziri wa ulinzi ahakikishe Kamanda Amata anarudi kazini.
“Mheshimiwa waziri wa ulinzi, lazima tu ukubali kuwa umekata tawi ulilokalia,” Madam S alitamka maneno hayo na kumuudhi sana waziri wa ulinzi

“Hapo mheshimiwa nakuunga mkono, hatukufanya jambo la busara kabisa kumtoa kazini Kamanda Amata, na kwa sababu hiyo ndiyo maana hata sasa tunakutana hapa ambapo si kawaida yetu, kwa nini Kamanda Amata asirudishwe kazini?” Mkuu wa majeshi aliliambia jopo na kuungwa mkono na jopo zima. Waziri wa ulinzi alikuwa kimya, hakuongea kabisa alikuwa akiwasikiliza wajumbe hao.

“Mimi nahitaji Kamanda arudi kazini, hapo ndiyo nitaifanya kazi hii kwa ufanisi wa hali ya juu,” Madam S akalieleza jopo. Uamuzi ukapitishwa wa kamanda Amata kurudishwa kazini, ikaandikwa barua na kusainiwa na jopo zima kama ilivyokuwa mwanzo, akakabidhiwa waziri wa ulinzi ahakikishe Kamanda Amata anarudi kazini.
“Mheshimiwa waziri wa ulinzi, lazima tu ukubali kuwa umekata tawi ulilokalia,” Madam S alitamka maneno hayo na kumuudhi sana waziri wa ulinzi.

Ugeni mpya ulifika nyumbani kwa Kamanda Amata siku ya pili baada ya Gina na Scoba, waziri wa ulinzi akifuatana na ujumbe wa watu watatu. Kamanda Amata alikuwa akiendelea na shughuli zake za shamba.
“Salama Kamanda?” sauti hiyo ikamshtua Amata kutoka katika kazi iliyoiteka akili yake, akaacha na kugeuka nyuma, akakutana uso kwa uso na waziri wa ulinzi aliyekuwa na bahasha mkononi mwake. Mheshimiwa waziri akavuta hatua mpaka aliposimama Kamanda Amata.

“Samahani sana Kamanda kwa yaliyotokea, yaliyopita si ndwele tugange yajayo,” waziri wa ulinzi akamwambia Amata huku akiwa amekwishamfikia pale alipo, akamkabidhi ile bahasha. Kamanda akaipokea na kuifungua bila kusema chochote, akaisoma, barua ya kumtaka kurudi kazini. Alipokwishakumaliza kusoma, akainuan uso wake na kumtazama mzee huyo.

“Asante, nitawajibu kwa maandishi,” kamanda akajibu na kuitia mfukoni ile karatasi kisha akapanda pawatila na kupotelea shambani. Waziri wa ulinzi na wapambe wake wakabaki wakitazamana, hakuna jipya, waliamua kuondoaka zao.

“Taifa linautambua sana mchango wako katika mambo mbalimbali, umepigania haki, uliyaweka hatarini maisha yako kwa ajili ya Watanzania. Kumbuka ubinaadamu upo, hivyo serikali inakuomba kurudi kazini na kusaidia tena taifa lako ulipendalo, Watanzania wanahitaji akili, nguvu, umakini na utayari wako…”
Ilikuwa sehemu ya barua aliyoandikiwa kutoka baraza la usalama la taifa, akaikunja tena ile karatasi na kuirudisha mfukoni. Akajaribu kufikiria mateso ya wapiganaji wa Tanzania ambao wapo huko Somalia kama wanayapata yatakuwa makali kiasi gani, moyo wake ukamuuma sana, akamfikiria madam S jinsi atakavyokuwa anahangaika katika hilo, Kamanda akaangusha chozi, akakata kauli na kurudi nyumbani kwake.

“Nasafiri mara moja, naomba muangalie shamba na mambo mengine, nitarudi labda baada ya wiki moja au mbili,” Kamanda akawaambia watu anaoishi nao wakiwemo wafanyakazi wake wa mazingira, akamshika mkono binti yake Jenny.
“Jenny, nitakuona nikirudi, sawa mrembo wangu?” Kamanda akaagana na binti yake. Jenny akaitikia kwa kutikisa kichwa.
Baada ya kuweka sawa zana zake chache muhimu katika begi lake, Kamanda Amata akaingia ndani ya Land Rover Defender, gari ya kazi na kuelekea mjini.

Ilikuwa ni siku nzito sana, Madam S alikuwa na uchovu wa ajabu, aliegesha gari yake katika maegesho ya nyumba yake huko Masaki na kuingia ndani kupumzika, kabla hajawasha taa akiwa anaelekeza mkono wake katika switch, taa ya sebuleni ikawaka yenyewe, akashtuka na kutazama huku na huko kwa hadhari kubwa.
“We unafanya nini hapa?” akatamka baada ya kumuona Kamanda Amata akiwa ameketi kochini na mbele yake kwenye kijimeza kulikuwa na pombe kali aliyokuwa akiigida kwa madaha.

“Nimekuja kwa mama yangu,” Kamanda akamjibu Madam S. madam S akamtazama kijana huyu, kisha akavuta hatua chache na kujitupa kwenye kiti. Hakushangaa kwa kamanda Amata kuwa ndani ya nyum,ba hiyo kwani anamju wazi utundu wake wa kucheza na vitasa vya kila aina na kuingia bila uharibifu.
“Karibu konyagi,” Kamanda akamkaribisha Madam S, akamsogezea glass iliyojaa nusu.
“Asante Kamanda,” Madam alijibu huku akiinyanyua glass na kupiga funda moja la nguvu.
“Kamanda, hali ni tete hapa, mi nafurahi umekuja, na nilijua utakuja, ila umenyanyasa sana yule mzee. Kwa ujumla tumeshapoteza makomandoo wawili na wawili haijulikani walipo, ukiachana na wanajeshi wa maji ishirini wa Tanzania na watano wa Urusi pamoja na meli yetu kubwa ya kivita ililiyokuwa na makombora ya masafa marefu na uzito wa hali ya juu kumi na mbili, Mama amechanganyikiwa kupoteza mali zote hizo,” Madam S alimweleza Kamanda Amata.
“Hujuma?” Kamanda akatupa swali.
“Sijajua,” Madam S akajibu.

“Hujuma, hiyo ni hujuma, ina maana hao maharamia na washirika wao wanajuaje serikali inapotaka kutuma watu kwenda kule? Mpaka wawaue kirahisi namna hiyo? Hujuma, Madam kubali kataa hiyo ni hujuma,” Kamanda alisisitiza juu ya hilo.
“Kamanda, sikuwahi kufikiria hilo, sasa unaanza kunipa mwanga, ila mheshimiwa umemnyanyasa sana, au ni yeye?” Madam aliuliza.
“Sijui labda ni wewe Madam, maana ukiwapa siri wale wanakupa pesa ya maana sana kuliko unavyofikiria,” Kamanda akajibu, akainua glass yake na kupiga funda moja.
“Mi nimekuja kwa heshima yako, na kwa familia za wale wa liotekwa, lakini sio kwa sababu ya waziri wa ulinzi wala nani ni hayo mawili tu,” Kamanda akajibu, na kunyanyuka, “Mi naondoka tutaonana kesho,” akasema huku akivuta hatua kuuendea mlango.

“Kamanda subiri TSA 5 atakuja kukuchukua, huwezi kwenda peke yak oleo,” Madam S akamwambia. Kamanda akageuka na kurudi kama hatua mbili akajishika kiuno na kumtazama Madam.
“TSA 5?!” akauliza kwa mshangao.
“Ndiyo, TSA 5, tuko namba tano sasa ila moja bado ilibaki wazi mpaka sasa, imeniwia ngumu sana kuteua namba hizo ukizingatia nilikuwa na Chiba tu,” Madam akamwambia.
“Ok, 3 ni nani? 4 ni nani na 5 ni nani?” kauliza Amata.
“Scoba TSA 03 idara ya usafirishaji na uokoaji, Dr Jasmin TSA 04 idara ya afya, Gina TSA 05 asiye na idara maalum,” akajibu Madam S, “nimewatawadha leo kwa mujibu wa sheria iliyowekwa ya kuunda na kuteua juu ya idara hii ya ujasusi,” akaongeza.

Kamanda Amata akampongeza Madam kwa kumpa mkono, “Hata kama ungenishirikisha hao ndio ningekupendekezea kwa sasa, timu imetimia,” Akasema Kamanda.

Shalabah, alikuwa ametulia tuli juu ya kiti na kutazama kwa makini skrini iliyojitokeza mbele yake, Mr Lonely alikuwa akiongea na kijana huyo wa juu kabisa katika timu yake, akimpa hili na lile. Mr Lonely, alikuwa ni mtu asiyebishiwa, ila unaruhusuwa kumwuliza, na kauliu yake ni ya mwisho, akisema Fulani auawe basi auawe hakuna linguine. Yeye alikuwa akiishi ndani ya jumba lake la fahari sana lililojengwa baharini, chini, sio kila mtu alikuwa anaweza kuongea na huyo bwana, na hakun a aliyejua kama bwana huyo ana mke na watoto au hana kwani utaambia amesafiri lakini hukuwahi kumuona akitooka na gari ndani ya jumba hilo lakini amesafiri, kwa hiyo hakuna aliyeamini kama bwana huyo ni mtu wa kweli au wa kufikirika, lakini sauti yake ilisikika na picha yake ilionekana uingiapo sebuleni hapo kuzuingumza naye.

“Hakikisha, yeyote anayekuja kufuatilia habari hii anauawa mara moja, mmefanya vizuri kuwauwa wale wawili, na hao wengine hakikisheni wanapata mateso mpaka wanakufa, pia watupatie na siri nyingine, kwani biashara ya safari hii ina tija sana na najua hawatakubali kuacha hivi hivi lakini we endelea kupanga vijana kwani mauzo ya bidhaa hii ni siku kumi zijazo na hao watu wao tutawazika wazimawazima,” maneno mazito ya Mr Lonely yalipenya katika ngoma za masikio ya Shalabah.

“Sawa, Lonely,” akajibu Shalabah.
“Hakikisha macho yote kuanzia uwanja wa ndege mpaka mahotelini yanafanya kazi sawasawa, jicho letu lililoko Tanzania linafanya vizuri, lazima tuitazame dunia kama tunavytokitazama kiganja cha mkono, kwa heri,” Lonely alamaliza kuongea, kabla Shalabah hajajibu chochote, ile skrini pale ukutani ikarudi taratibu chini mahali inapojihifadhi na kopo lenye maua ya kunukia likachukua nafasi yake.
Shalabah alipoliacha jumba hilo, moja kwa moja alifika katika ofisi yao nyingine, ofisi ya siri ambapo alimkuta Sharoni na vijana wengine, akawapa maagizo yote yaliyotolewa na Mr Lonely na kumpa kazi Sharon ya kuimarisha ulinzi mpaka biashara ile itakapofanyika.

“Kwani we una wasiwasi kuwa watatuma tena mtu? Hiyo sahau, tumeshaua wawili na tunao mkononi ishirini na saba, haji mtu hapa, serekali isiyo na akili itafanya hilo,” Sharon akamwambia Shalabah, wote wakacheka na kisha wakatoka eneo hilo kuelekea bandari ya zamani ambako kwa ujumla mambo yote yalikuwa hapo.

5..Dar es salaam
“Hebu nambieni kwanza juu ya hali ya usalama wa vijana wetu huko Somalia,” Mkuu wan chi ambaye dhamana ya taifa lote na watu wake lipo mkononi mwake alimuuliza waziri wa ulinzi aliyekuwa mbele yake, ukimya ukachukua nafasi, waziri hakujibu lolote, “Unajua kupoteza makomandoo wawili ni hasara sana kwa jeshi letu, wakati mnajua kuwa wapo na zipo idara nyeti za kuifanya kazi hiyo na siyo wanajeshi kwa kuwa wao wako kwa ajili ya kazi kubwa zaidi,” akaongeza. Waziri wa ulinzi alikuwa akiona muda hauendi kabisa kwa maswali aliyokuwa akibanwa na mkuu huyo.
“Ah… eh…. Mh…. Unajua mheshimiwa, tulighafirika kidogo na kuwapeleka wale watu tukijua kuwa wataifanya kazi hiyo vizuri kutokana nja kwamba adui tuliyekuwa tukimkabili alikuwa kivita zaidi,” akajibu waziri.
“Ni uzembe, lazima ukubali ni uzembe na hao mlioshirikiana juu ya hilo wote ni wazembe na mtawajibika kwa hili, naomba uende, sasa nitaamua mimi la kufanya juu ya hilo inaonekana wewe umeshindwa kama waziri,” akamaliza kuongea Mkuu wa nchi, amiri jeshi mkuu.

“Kwa nini mpaka sasa, wapiganaji wetu wanapoteza maisha na we upo hapa unatazama?” swali kutoka kwa mkuu wan chi lilitua katika ngoma ya sikio ya Madam S.
“Sikuwa na nguvu ya kutosha kukabiliana na swala hilo mkuu,” Madam S alijibu.
“Sijakuelewa, hukuwa na nguvu kivipi na wakati mwingine ulikuwa na nguvu kivipi?” akaulizwa tena.
“Mheshimiwa, wewe unajua kitengo chetu ndio kimeanza miaka mitano hii na mpaka sasa nilikuwa na watu wawili tu yaani TSA 1 na 2, kutokana na sakata la Julai 7 la kupambana na magaidi lilipokamilika TSA 1 aliachishwa kazi kwa ajili ya utovu wa nidhamu, nikabaki na TSA 2, ndio nikakuandikia barua ya kuomba kuongeza nguvu kikosini kwangu, ukanikubalia, nimeongeza juzi watu wa watatu, lakini bado sina TSA 1, nitafanyeje?” Madam S akajibu kinagaubaga na kumuona wazi mkuu wa nchui akikodoa macho kumshangaa.

“Nani anayeweza kumuondoa kazini mtu wa kitengo cha ujasusi? Kile kitengo kiko chini yaofisi yangu ni mimi tu ninayeweza kumuondoa mtu au kumuingiza mtu na si mtu awaye yote, sasa popote alipo TSA 1 arudi kazini kwa amri yangu, na mara moja akabidhiwe hiyo kazi aende akaokoe jahazi,” Mkuu wan chi aliongea kwa hasira.
“Sawa mkuu, TSA 1 amekwisharejea kazini,” Madam S akajibu.
“Sawa, umefanya vyema, na nitafurahi zaidi ukinambia kuwa usiku wa leo atakuwa tayari ameondoka, kama hakuna ndege basi ya serikali itampeleka, asante, nasubiri jibu lako,” Mkuu wan chi akamaliza kuongea na kuagana na Madam S.

Madam S akaiacha ofisi hiyo na kupita kwenye korido ndefu iliyomtolea kwenye sebule ya kupumzikia wageni, akapita mlango mkubwa na kuziteremka ngazi harakaharaka, akaingia kwenye gari yake na kuondoka katika viwanja vya Ikulu.

Gina alikuwa ameketi ndani ya ofisi aliyoizoea, macho yote yakiwa kwenye luninga akitazama habari za kimataifa kupitia channel ya Al-Jazeera. Akiwa hana hili wala lile, mlango wa ofisi ukafunguliwa bila hodi, mtu asiyemtegemea akaingia ndani.

“Kamanda!” akajikuta akitamka.
“Ndiyo mimi hakuna mwingine,” Kamanda Amata akajibu na kuvuta kiti chake, akaketi. Gina
“Afadhali umekuja, maana bibi yako alikuwa amechanganyikiwa, na ofisi nzima pia,” Gina akajibu.
“Najua, nimekuja kwa sababu ya Watanzania na si kitu kingine, naomba niaandalie safari ya kuelekea Somalia leo hii,” kamanda akaagiza.
“Bila shaka, sasa nina furaha, kwa kuwa umekuja, unaonaje tukienda pamoja?” Gina akamwambia Amata.
“Hapana, kwa sasa huwezi kutoka nje ya nchi au hata mkoa bila ruhusa ya bosi wako, Madam S, wewe umeshaingia katika kitengo nyeti cha kijasusi tayari jina lako litakuwa kati ya majina yanayosakwa na watu wabaya katika mitandao ya kimataifa, ikibidi utakuja lakini hatuwezi kuondoka wote ndivyo oda ilivyo,” kamanda Amata akamwelewesha Gina. Gina akabakio kasimama akimwangalia kijana huyu ambaye hakuwa naye kwa muda mrefu sasa kikazi.
“Ok, nimeelewa,” Gina akajibu na kutoka kwenda katika kiti chake, akawasha kompyuta na kuanza kutembelea mashirika ya ndege ya ndani na nje kuangalia kama kuna lolote ambalo linapitia upande huo.
Dubai airline, ilikuwa ni ndege inayoondoka kutoka uwanja wa Jomo Kenyatta, Nairobi usiku wa siku hiyo kuelekea Dubai kupitia Mogadishu. Kutoka Tanzania hakukuwa na kampuni yoyote ya ndege inayokwenda upande huo. Kamanda Amata alikubaliana na Gina kutumia uwanja wa Jomo Kenyatta kuingia Somalia, hiyo kwake aliona itakuwa mbinu nzuri ya kuwapoteza malengo kama kuna mtu anyevujisha taarifa. Kutoka Dar es salaam kwenda Nairobi alipata ndege ya shirika la Ethiopia.

“Sasa fanya malipo yote, usimwambie mtu kama natumia Dubai airline, ila kila mtu ajue naingia Somalia kwa shirika la ndege la Ethiopia, hata madam S asijue,” kamanda Amata almwambia Gina wakati akimpa taarifa ya ndege hizo.

Baada ya kukamilisha itifaki zote, Gina na Kamanda Amata wakatoka kuelekea ofisi ya Madam S, pale waliwakuta wengine ambao wote walikuwa wakiwasubiri wawili hao. Moja kwa moja alikutana na Madam S aliyekuwa mbele ya meza yake kubwa ya ofisi.

“Kamanda Amata, kwa mujibu wa sheria iliyoruhusu kuunda na kuteua idara ya Kijasusi ya TSA, nakurudishi cheo chako cha TSA 1 kuanzia sasa,” Madam S akamwambia maneno machache na wakati huo wote wengine walikuwa wima kwa heshima, akamrudishia beji yake pamoja na kitambulisho na kikasha chenye bastola kama kitendea kazi.
Baada ya hayo wote wane wakampa salute Kamanda Amata wakati yeye akimpa salute Madam S.
Madam S akampa Kamanda Amata bahasha ya khaki mikononi mwake huu yake ilikuwa imeandikwa kwa maandishi mazito, HUJUMA? Akaitazama na kuifungua ndani, maelezo yote akayakuta yakiwa yameandikwa kwa ufasaha kabisa, picha za Sebeki na Gwamaka, pia wapiganaji wote ishirini na tano picha zao zilikuwapo na majina na vyeo vyao, picha ya Daud na Jamil pia zilikuwapo na picha ya Manowari kubwa ya kijeshi.
Kamanda Amata alishusha pumzi ndefu, akaitazama ile bahasha na kuiweka mezani kisha akachukua kalamu ya wino mzito na kuondoa alama ya kiulizo katika katika andishi HUJUMA? Likabaki kuwa HUJUMA.
OFISI NYETI TSA (SHAMBA)

“Ok, Kamanda, kaa tayari tunakuwekea GPS micro chip,” Chiba akamwambia Kamanda Amata wakati, Dr Jasmine akiwa tayari na sindano maalum ya kumchoma kwenye msuli wa mkono ili kupachika hiyo chip, akakunja shati lake na zoezi hilo likafanyika chini ya Chiba na Dr Jasmin.
“Ok, Kamanda nakuona sasa kupitia satellite,” Chiba akamwambia Kamanda Amata ambaye wakati huo alikuwa akishikilia pamba iliyokuwa na dawa maalum ya kukausha damu na kuua bacteria.
“Hii ni bastola mpya ya kisasa, inayoweza kupiga mpaka mita mia tano kwa nguvu ileile, bastola hii hawezi kutumia mtu yeyote mwingine ni wewe peke yako, ishike vizuri, niiunganishe,” Kamanda Amata akaikamata vyema na mkono wake ulioshika bastola ukapitishwa kwenye kifaa maalumu cha kielektroniki.

Baada ya zoezi hiulo Chiba akaendelea, “ Hii bastola Kamanda ni teknolojia mpya kabisa iliyotengenezwa hapahapa nchini kwenye baada ya utafiti wa kina wa wataalamu wetu wa JW kule Mzinga, Morogoro.” Kamanda Amata akaigeuza geuza na kutikisa kichwa kuonesha ameikubali maana ilionekana ya kisasa hasa. Akakabidhiwa na vikorokoro vingine kwa ajili ya kazi zake zikiwemo silaha za siri za kijasusi, saa ya kisasa inayoweza kubeba risasi tatu zenye kipenyo cha milimita 3 na urefu wa sentimita moja.

“Utatumia gari aina ya Kilimanjaro, hii ni gari mpya kabisa tuliyoiunda maalumu kwa kazi ngumu kama hizi, ina mwendo kasi wa kilomita 350 kwa saa, uwe mwangalifu sana kwani ni gari ya hatari katika kasi, kiti chake kina parachute na paa lake linafunguka kwa switch moja tu, ukibonyeza parachute na paa lake linafunguka wakati huohuo hivyo inaweza kukuokoa katika hatari yoyote, Kamanda Amata ni wewe mtu wa kwanza kutumia aina ya gari hii iliyotengenezwa hapa nchini, utaikuta pale uwanja wa ndege Mogadishu,” Chiba akamkabidhi funguo Kamanda Amata, na kumtakia heri na baraka kwa maana wote walijuwa uzito na ugumu wa kazi hiyo ndiyo maana wakamkabidhi vifaa vya kisasa kwa teknolojia mpya na ya kwanza kutoka Tanzania.

“Kamanda vidonge hivi vitakufanya usisikie njaa, kwa masaa sabini na mbili, na hivi ni vya sumu na vingine vya kulevya kama utahitaji kuvitumia,” Dr Jasmin akampatia aina tatu ya vidonge.
Madam S alikuwa akifuatilia kila jambo linalofanyika, akaridhika na mipangilio ya vijana wake.
“Safi, Kamanda nakutakia kazi njema sana, sasa unatakiwa kufika katika kambi ya wanamaji pale Kigamboni uonane na mkuu wa kikosi, kanali Shemweta

KAMBI YA JESHI LA WANAMAJI
KIGAMBONI

KAMANDA Amata alikuwa ndani ya chumba maalum, yeyeb pamoja na Madam S na maofisa wengine wa jeshi la wanamaji, pamoja nao waziri wa ulinzi alikuwapo. “Kamanda, unaona huu mchoro, meli yetu, imepotelea hapa, tulikuwa tukiifuatilia kila hatua kwa kutumia lada, lakini kufika hapa hatukuweza kuiopna tena, tuna uhakika kwa asilimia mia moja imetekwa na maharamia wa Somalia, kwa kuwa mele nyingi sana zinapotelea hapa,” alizungumza mwanajeshi mmoja aliyekuwa na nyota tatu mabegani mwake, akimuonesha Kamanda Amata ramani iliyopigwa kwa satellite kuonesha njia iliyokuwa ikipita meli hiyo kubwa ya kivita. Kamanda Amata akatazama kwa makini sana, daima alikuwa akitikisa kichwa kuonesha kuwa anaelewa anachoambiwa.

“Kadiri ya taarifa za awali zilizotumwa na wapiganaji wetu ambao wamekwishatangulizwa mbele ya haki, meli hii haionekani kabisa majini hata pale Mogadishu, hivyo hawakuweza kujua kama ipo au imeondolewa,” Yule mwanajeshi akaendelea. “Lingine Kamanda, hawa jamaa ni hatari sana, uwe muangalifu tusije kukupoteza, Watanzania tunakupenda sana na tunaithamini kazi yako,” Waziri wa ulinzi aliendeleza hoja. Kamanda Amata akapiga saluti, akiwa ndani ya suti safi ya kijeshi. Kisha wote wakatoka, na Madam S akiwa na Kamanda Amata pamoja na waziri wa ulinzi wakaondoka na helkopta maalum kurudi mjini.

JNIA – saa 2:00 usiku
MADAM S alimpa mkono Kamanda Amata alipokuwa uwanja wa ndege wa kimataifa Dar es salaam tayari kwa safari.
“Kila la kheri Kamanda, nakuaminia sana,” Madam alimwambia. Kamanda Amata akasaluti kisha akamuendea Gina na kumbusu.
“Nahitaji urudi Kamanda, urudi na pua yako,” Gina alimwambia Kamanda.
“Usijali, nitarudi na kila kitu changu,” Kamanda akaagana na wote pale uwanja wa ndege kisha akaingia katika chumba cha wasafiri tayari kwa safari.
“Habari ya jioni,” mtu mmoja alimsalimu Kamanda Amata walipokuwa ndani ya chumba cha wasafiri.
“Salama kabisa,” Kamanda akajibu na kuendelea kusoma gazeti lililo mkononi mwake.

“Unaelekea wapi?” yule mtu akamwuliza Kamanda Amata. Kamanda Amata akamtazama kuanzi kiatu alichovaa mpaka nywele, ndipo alipomgundua mtu huyo kwa mbali ana asili ya watu kama Wamburu.
“Naenda Arusha, wewe je?” Kamanda akamwuliza.
“Naenda Moqdishu,” yule mtu akajibu, akajikohoza na kuendelea, “Sasa unaenda Arusha kwa Ethiopia Airline!” akaongeza.
“Hilo halikuhusu, nina uwezo wa kwenda Morogoro kwa British Airways,” kamanda alipomaliza kuongea hayo, tayari mlango ulikuwa wazi na abiria wakaanza kuingia ndegeni.

Yule mtu aliyekuwa akiongea na Amata pale uwanja wa ndege alikuwa mara kwa mara akienda maliwato ndani ya ndege hiyo. Kamanda Amata alikuwa ameketi siti za mbele ilihali yule bwana alikuwa siti za nyuma, kamanda Amata aliweza kumuona vizuri kwa kupitia miwani yake ambayo iliweza kumuonesha vinavyotokea nyuma yake.
Baada ya kumtazama kama mara nne akienda maliwato, mara hii Kamanda Amata akainuka kutoka katika kiti chake na kuelekea upande wa nyuma wa ndege hiyo. Moja kwa moja akaenda mpaka katika mlango wa maliwato, akasimama kusikiliza kama mtu huyo anaongea chochote, akasikia lakini kwa sauti ya chini sana kutokana na mlango huo jinsi ulivyotengenezwa, kamanda Amata akachomoa kifaa kidogo chenye mfano wa koni akakiegesha hapo mlango na kusikiliza kila kinachoongelewa, alipoona kuwa mtu huyo anakaribia kumaliza mazungumzo Amata akashika kitasa cha mlango huo na kukifungua kwa nguvu kwa kukivunja, akausukuma mlango ndani na kuingia kisha akaufunga nyuma yake.

Ndani ya choo hicho akakutana na yule bwana, Kamanda Amata akamtazama kwa jicho baya.
“Nani ulikuwa unampa habari zangu?” akamwuliza.
“Hapana, mimi nilikuwa naongea na ndugu zangu,” akajibu huku akitetemeka.
“Ndugu zako ndio unawatajia jina langu?” Kamanda Amata akauliza, kisha akatazama kifaa alichokuwa anatumia kuwasiliana na jamaa hao, kilikuwa ni kifaa cha ajabu sana kidogo kwa mfano wa kiberiti, alikiunganisha kwa ufundi sana kupitia nyaya ndogo zinazosafirisha mawasiliano ndani ya ndege hiyo. Kamanda Amata akakitazama na kuzing’oa zile nyaya zake pale alipoziunganisha na zile zilizo kwenye mfumo wa ndege hiyo.

Alipohakikisha anacho kile kidubwasha mkononi mwake, akamwamuru yule jamaa kutoka ndani ya choo kile.
“Sasa utakwenda kukaa pale nilipokaa mimi na mimi nitakaa hapa ulipokaa wewe,” Kamanda alimwambia yule jamaa.
“Ah, siwezi kukaa kule kwani mi sti yangu ni hii hii,” yule bwana alilalama. Kamanda Amata hakujibu, alimtandika kofi moja kali sana, mpaka yule bwana akakaa chini. Wahudumu wa ndege wakamfuata Kamanda kumwambia kuwa analolifanya haliruhusiwi ndani ya usafiri huo, wakamwomba akae kwenye siti yake. Kamanda Amata akawaonesha kitambulisho chake halisi. Hapo wakamwacha afanye atakalo, kwa kuwa huyo ni mtu wa kuaminika. Yule mtu akaketi kwenye siti ya Amata na Amata akakaa kwenye siti yake, sasa alikuwa akimwangalia kwa mbele.
Baada ya kutua Nairobi, yule bwana aligeuka nyuma kwa woga kumtazama Amata, hakumwona.
Kamanda Amata alishuka katika uwanja wa ndege wa Jommo Kenyatta bila yule bwana kujua. Baada ya kufanyiwa itifaki za kiusalama, hakuchukua muda mrefu alikwea ndege shirika la Dubai Airline na kuelekea Mogadishu, tayari kabisa kuanza kibarua alichotumwa.

MOGADISHU – SOMALIA
Uwanja wa ndege wa ADEN ADDE
SHALABAH alikunja sura baada ya kupata taarifa kuwa Kamanda Amata hayupo katika ndege waliyoitarajia. Alionekana wazi kupumua kwa nguvu, akiwaza jambo.
“Shalabah, vipi?” Sharon akamuuliza.
“Huyo wanaemwita Kamanda Amata hayupo katika ndege tangu watoke Nairobi,” Shalabah akamwambia Sharon. Sharona naye akaonekana wazi kupigwa butwaa.
“Atakuwa kaamua kukatisha safari?” Sharon akauliza.
“Hapana, huyu anataka kutuchezea mchezo, nina uhakika yuko humohumo, kajificha sehemu, hebu ongea na watu wetu upande wa cargo kuwa wanaangalia vizuri, bado saa moja ndege itatua,” Shalabah akatoa maelekezo na Sharon akawapanga upya watu wake.

“Vipi?” Fasendy akamwuliza Sharon, pindi alipotoka pembeni kuvuta sigara.
Fasendy alikodiwa katika mpango huo ili kummaliza Kamnda Amata palepale uwanja wa ndege kwa kumdungua, alikuwa tayari kajipanga kwa hilo, alichoambiwa yeye ni kuwa atapewa maelekezo tu ya jinsi mtu huyo alivyo.

NDEGE ya Dubai Airline ilikanyaga ardhi ya Mogadishu ikiitangulia ile ya Ethiopia ambayo maharamia hao walikuwa wakiisubiri kwani walishaambiwa kuwa Kamnda yuko humo, na walitahadharishwa kuhakikisha haingii mjini kwani ni mtu hatari sana. Mpaka dakika hiyo walikwishakubaliana na hilo kuwa mara hii wanapambana na mtu makini mwenye akili za ziada kwa mchezo tu aliowachezea kwenye ndege hiyo.

Kamanda Amata alikiacha kiti chake, akaweka kijibegi chake mgongoni na taratibu kuziteremka ngazi za ndege hiyo na kwa mara ya kwanza aliweka unyanyo wake katika ardhi ya Mogadishu, uwanja wa ndege wa Aden Adde. Akiwa na miwani yake usoni aliweza kuona vyema kabisa katika mianga ya taa kali za umeme iliyokuwa ikimulika eneo hilo, akavuta hatua ndefundefu na kuelekea katika eneo la kukagulia mizigo. Kamanda Amata aliinyakua mizigo yake na kuibwaga mezani kwa mwanadada mrembo wa Kisomali, mwanadada yule alikagua vizuri kabisa mizigo ya kamanda lakini hakuona hata kitu kimoja cha hatari wakati ndani yake kulikuwa na silaha nyingi za kijasusi.

Alipomaliza akatoka katika mlango mkubwa, huku akisindikizwa na kijana mmoja aliyekuwa akisukuma kile kitorori cha mizigo. Macho ya Kamanda Amata yalikuwa yakicheza huku na kule kuwaangalia wote waliopo katika uwanja huo ili aone kama adui yoyote. Kutokana na kazi zake za kijasusi aliweza kuitambua ni ya mtu kwa kumwangalia tu usoni mara moja. Akingiza mkono mfukoni na kutoa kidubwasa kidogo ukubwa wa kidole gumba akaminya sehemu ya katikati ambayo ilikuwa na kitufe chekundu. Gari moja iliyokuwa katikati ya nyingine ikawasha taa zake na kujiwasha injini, ikabaki inaunguruma.

“Asante sana kijana nimekwishampata mwenyeji wangu,” alimshukuru yule kijana na kumpa dola za kimarekani hamsini. Yule kijana hakuamini, aliigeuza huku na huku ile noti hakuamini, akabaki kukenua huku akimwangalia kamanda Amata.
“Unaitwa nani?” kamanda akamwuliza.
“Naitwa Ahab,” yule kijana akajibu.
“Una simu?” Kamanda akamwuliza.
“Ndiyo, ndiyo ninayo,” akajibu na kuitoa simu ya kizamani kidogo iliyokuwa imeshikizwa kwa mipira.
Akamnda Amata akatikisa kichwa na kumtazama kijana huyo aliyeonekana mjanja machoni na matendo yake pia. Kamanda Akachukua namba ya kijana huyo akamwahidi kumtafuta usiku wa siku inayofuata. Yule kijana akafurahi sana na kuondoka eneo hilo. Kamanda Amata akaisogelea ile gari ambayo hata hakujua ni nani aliyeiweka mahala hapo. Akafungua mlango na kuketi baada ya mizigo yake kuitupia kwenye buti ya gari hiyo. Akaketi kwenye kiti cha dereva na kujiweka sawa, ile gari ikamkumbusha kufunga mkanda.
‘Tanzania tumeendelea sana kiteknolojia,’ akajiwazia wakati gari hiyo ikimpa maelekezo mafupi juu ya matumizi, aliporidhika akaitoa mahali pale taratibu na kuiingiza katika barabara kubwa ya kutokea nje ya uwanja huo.

JAZEERA PALACE HOTEL
KAMANDA Amata aliegesha gari katika maegesho ya hotel hiyo, akashuka na kutoa mizigo tayari kuelekea ndani.
“Karibu sana Jazeera palace Hotel,” sauti tamu ya kike ikamkaribisha Kamanda alipokuwa pale mbele ya kaunta.
“Asante sana, nimekaribia, natumaini kupata huduma safi na bora kuliko mahala popote nilipowahi kwenda,” kamanda akajibu karibisho hilo.
“Usijali, kila huduma inapatikana,” yule msichana akamwambia.
Baada ya kuandikisha na kumaliza kila kilichohitajiwa pale kaunta, Kamanda Amata akaingia kwenye lifti na kupanda ghorofa ya tatu.

305, ilikuwa namba ya chumba iliyomtazama mbele yake, akaingia ndani na kuufunga mlango nyuma yake, kabla ya lolote, akachukua kifaa chake maalumu kwa kazi ya ukaguzi kama kuna kitu chochote cha hatari, alipohakikisha usalama upo aliweka vizuri mambo yake, akatazama simu yake ilikuwa saa saba za usiku, akajua bado dakika kumi na tano tu ile ndege ya Ethiopia itakuwa hapo Mogadishu, Kamanda Amata alitaka kuwa pale ili aone kinachoendelea; hasa kumuona yule mtu aliyemgundua akitoa maelezo fulani kwa ndugu zake, akabadili nguo na kuvaa mavazi ya kazi: suruari nyeusi, koti la suti jeusi lililotanguliwa na kabashingo nyeusi, shingoni akaninginiza mkufu mzito wa dhahabu, akaichukua bastola yake mpya kabisa aliyokabidhiwa na Chiba, akaiweka tayari na kuificha ndani ya koti hilo, akakusanya silaha zake za siri na kuzipachika katika sehemu mbalimbali za suruali yake, akajitazama kwenye kioo, akajiona kamili. Akaufunga mlango na kuteremka kwa ngazi mpaka chini, akatoka nje na kuingia kwenye gari yake aina ya Kilimanjaro, akaondoka kuelekea uwanja wa ndege. ‘Hakuna kulala…’

Uwanja wa ndege wa ADEN ADDE saa 7.15 usiku.
Kamanda Amata aliegesha gari yake na kuteremka kuelekea eneo ambalo wageni hufikia kusubiri mizigo yao. Usoni akiwa amevalia miwani yake yenye uwezo wa kupiga picha na kuona upande wa nyuma. Akavuta hatua chache na kusimama karibu na mti wa mtende ulio pembezoni tu mwa barabara inayotenganisha upande wa maegesho na upande wa jengo kuu la uwanja huo. Akijifanya kuwa hajui lolote au hana la maana mahala hapo, Kamanda Amata alitulia kwa kujiegemeza katika mti huo, akitazama wanaoingi na kutoka. Ilikuwa ni muda huohuo ndege ya Ethiopia ilitua katika uwanja huo.

Punde si punde, lile alilolitarajia lilitukia; kutoka katika mlango mkubwa wa jengo lile alimuona yule bwana akitoka huku akisukuma kitoroli cha mizigo, mara kidogo akalakiwa na watu watatu, wanaume, akajaribu kuzinasa picha zao kwa kutumia miwani yake, akabahatika japo kwa shida kidogo. Baada ya tukio hilo aliwafuatilia kwa macho akitazama walikokuwa wakielekea, kutoka mbali aliwaona kana kwamba walikuwa wakilaumu jambo kutoka kwa huyo mwenzao waliyekuja kumpokea. Kamanda Amata kwa haraka kidogo akarudi katika gari yake na kuketi kitini, nyuma ya usukani, akiendelea kuwatazama huku miwani yake ikimuonesha kwa uzuri zaidi. Baada ya kusimama kidogo mahala fulani, ikaonekana wamekubaliana jambo, wakaingia garini wote wanne. Kamanda Amata akaitazama ile gari ilipokuwa ikitoka kwenye maegesho hayo na kuingia barabara kubwa, akaitazama namba zake za usajili na kuzikariri akilini mwake, kisha akaiacha kidogo itoke, na ye taratibu akawa anatoka kuelekea barabara kubwa, lakini kabla hajaingia barabarani gari nygine pick up, ilimpita mbele yake kwa kasi nay eye ikabidi asimame ghafla, baada ya hapo akaendelea kuifuata kwa mbali.

“Yaani wewe imekuwaje ukampoiteza yule wakati wote mpo ndege moja?” akauliza Sharon akiwa kageuza nusu ya mwili wake nyuma kwa yule mgeni.
“Yaani Sharon, mi hata sielewi yule Bwana kanipotea vipi,” akajibu yule mgeni huku akibabaika. Kisha ukimya ukatawala kati yao.
“Sasa mmeangalia vizuri kwenye mizigo?” Shalabah nae akauliza.
“Ndiyo mkuu, tumetazama na hayupo, sasa sijui itakuwaje.”
Baada ya mazungumzo marefu kati yao, ile gari iliegeshwa kwenye moja ya hoteli kubwa pale mjini, Jabir Hotel. Kamanda akamshuhudia yule bwana akishuka na kuwaacha wenyeji wake wakiendelea na safari nay eye akachukua uelekeo wa mlango mkubwa wa hotel hiyo huku akisaidiwa mizigo yake na mhudumu wa hapo, ile gari iliyomleta ikaondoka zake. Kamanda Amata akasukuti kwa nukta kadhaa, akaona kuwa hiyo ni nafasi pekee ya kuanzia kazi yake. Akaondoa gari yake na kuiacha ile hotel kuwaelekea wale jamaa wengine. Lakini haikuwa nia yake, alipofika mbele kidogo eneo lililokuwa na maghorofa mengi aliegesha gari yake katika supamaketi moja kisha yeye akashuka na kuingia ndani yake akiwa kama mteja, lakini lengo kubwa ilikuwa ni kuangalia kama kuna anayemfuata nyuma yake. Alipohakikisha kuwa hakuna, alitokea upande wa pili na kuchukua taxi

“Jabir Hotel tafadhali,” alimwambia dereva huku akiketi sawia katika kiti cha nyuma. Dakika kumi na tano hivi alikuwa tayari amekwishafika alipopakusudia, akamlipa dereva taxi na yeye kuuendea mlango wa hoteli hiyo. Jambo la kwanza alilofanya ni kuona kama anaweza kumpata yule kijana aliyemsaidi mizigo yule mgeni. Haikuwa tabu kumpata, alimwendea na kumwita kama mtu mwingine yeyote mwenye shida.
“Samahani, kuna mgeni tumemleta hapa kama dakika thelethini zilizopita,” alijaribu kiumwuliza yule mhudumu naye kwa kuwa anapokea wageni wengi haikuwa rahisi kujua ni yupi, lakini baada ya kumuelekeza vizuri alimkumbuka japo hakuwa na uhakika.

“Kama ni huyo yupo chumba namba 243,” akajibu yule mhudumu.
Kamanda Amata akashukuru na kushika njia, akapanda ghorofa ya pili kwa kutumia ngazi na isha kutokea kwenye korido ndefu ambayo ilikuwa imetanganisha vyumba vingi upandee mmoja na mwingine. Akatazama milangoni huku na huku na kujikuta mbele ya chumba hicho, namba 243 ilisomeka mlangoni bila kificho, akatulia kusikiliza kama kuna lolote ndani humo. Ukimya ulikuwa sehemu kubwa ya chumba hicho, Kamanda Amata hakuwa na uhakika kama ni sahihi mtu huyo yuko humo ndani, alipotaka kukata tama alisikia kwa mbali maji yakimwagika, hapo akawa na uhakika kuwa mlengwa wake yupo. Akachukua funguo yake na kuitumbukiza tunduni, lakini akajikuta anakabiliwa na upinzani kwani ndani ya mlango huo kulikuiwa na funguo ambayo iliikwamisha ile yak wake kufanikisha zoezi hilo. Akaitazama ilivyokaa akaiona kuwa imekaa sawia, akaisukuma ikaangukia ndani kisha akaipachika ya kwake.

Kitendo cha ile funguo kuanguka kilimshtua mtu wa ndani, Kamanda Amata alisikia nyayo za mtu aliyekuwa akitembea kuelekea mlangoni huku akipiga mruzi, akakinyonga kitasa wakati funguo yake tayari ilikwisharudi mfukoni, yule bwana alipokuwa akiipachika ile funguo kwa upande wa ndani, Kamanda Amata akaufungua mlango kwa ghafla na kumpiga usoni yule mtu.

Sekunde tano tu, Kamanda Amata alikuwa kajaa ndani kuufunga mlango nyuma yake, huku bastola uyake ikiwa mkononi. Yule bwana alikuwa chini kwa kusukumwa na ule mlango.
“We n… na….. nani? Aliuliza kwa kukatisha maneno.
“Hunijui”?
Yule bwana alionekana kuchanganyikiwa na kile kitendo, akawa anasota kwa makalio kurudi nyuma, akagota ukutani, hakuna njia.

“Niambie ulikuwa unatoka Tanzania kwa nani?” Kamanda akamuuliza.
“We mambo yangu unayatakia nini?” yule bwana akajibu kijeuri.
“Sikiliza wewe bwege, sijaja kupoteza muda na mtu, nitakuuwa sasa hivi,” Kamanda alimtahadharisha yule bwana aliyeonekana kutokuogopa chochote. Akiwa katulia kamtumbulia macho Amata, kwa mara ya kwanza, Kamanda Amata aliiamuru bastola ile ndogo ifanye kazi yake, risasi moja ikavunja mguu wa yule bwana, akalia kwa uchungu, kisha Kamanda Amata akamwendea pale na kumkanyaga kwenye jeraha lake.
“Aaaaaiiigggghhhh, unaniumiza!” alipiga yowe, akiongea kwa lugha ya Kiswahili, “Nitakwambia kaka, nitakwambia.”
“Sema.”

Kamanda Amata akalegeza mguu wake kutoka pale kwenye jeraha, akamtazama yule bwana pale chini, damu zikitiririka mguuni mwake. Mara ghafla yule bwana aliufyatua mkono wake uliokuwa na kisu mkononi kuulenga mguu wa Amata. Kamanda Amata aliuona mchezo huo kwa kuchelewa, akaruka nyuma lakini kile kisu kilipita kwenye suruali yake na kuchana kipande karibu na ugoko ila hakikufika kwenye ngozi. Kitendo kile kiliiamsha akili ya Kamanda Amata, kabla yul;e bwana hajafanya jambo linguine, teke kali lilitua mkononi mwake na kukiondoa kile kisu, teke la upande mwingine lilitua shavuni na kumrudisha chini. Yule bwana ijapokuwa alikuwa na jeraha mguuni mwake hakujali, alichomoa bastola kutoka kwenye kiuno chake lakini kabla hajafyatua tayari risasi ya Amata iliyotoka kimyakimya ilipenya kwenye paji la uso wake na kumlaza palepale chini; chali.

Kamanda Amata akasonya kwa kukosa maelezo yoyote toka kwa huyo mtu. Akamwendea na kumpekua mifukoni, hakuwa na kitu chochote zaidi ya kiburungutu cha pesa za kisomali. Alipotazama kitandani aliona baadhi ya vikolokolo, akaviendea, na kuichukua hati ya kusafiria ya mtu huyo, baadhi ya kadi za kibiashara na kijitabu kidogo, akakiacha chumba hicho na kuondoka zake.
Akiwa ndani ya gari yake, aliiangalia ile hati ya kusafiria na kuisoma hapa na pale, akamtambua kijana huyo kwa jina lake la Shaib, mwenye umri wa miaka thelathini na sita. Akaitupa pembeni na kupekuwa vitu vingine.
…Dar es salaam Club, saa 6.30 mchana…

Ilikuwa ni moja ya miadi aliyokuwa akitakiwa kufanya na mtu fulani hapo katika hiyo club. Kamanda Amata akawasha gari yake kuondoka kutoka katika eneo hilo, moja kwa moja akarudi hotelini kwake.
SIKU ILIYOFUATA saa 2.00 asubuhi
Kamanda Amata alikuwa akifuatilia habari katika televisheni ndogo iliyowekwa ndani ya chumba chake, kati ya habari zilizokuwa zikirushwa asubuhi hiyo ni pamoja na ile ya kukutwa marehemu ndani Jabir Hotel. Aliisikiliza kwa tabu kidogo kutokana na kuwa alikuwa haelewi lugha iliyokuwa ikitumika, alijaribu kuangali nyuso za watu waliokuwa eneo lile lakini hakuna aliyemhisi kwa lolote.

Asubuhi hiyo aliiacha hoteli aliyofikia na kufunga safari kuelekea Ramada Plaza Hoteli, iliyopo pembezoni kabisa mwa bahari ya Hindi karibu na bandari ya Mogadishu, kwa maelezo aliyokuwa ameyasoma katika taarifa aliyopewa kuwa katika hoteli hiyo ndipo Gwamaka na Jamil walikuwa wamepanga. Kamanda Amata alikuwa na miadi feki aina mbili, mmoja katika hoteli hiyo na mwingine ni Dar es salaam Club.


Kamanda Amata aliegesha gari yake mbele ya hoteli hiyo kubwa, akashuka na kuufunga mlango wa gari hiyo ya kisasa, akasimama na kuangalia kwa makini lango kuu la hoteli hiyo, akavuta hatua mbili tatu mbele, akasimama na kuangalia vizuri, akajifanya anafunga kamba za viatu kisha akaendelea na safari yake mpaka mapokezi. Akakutana na mhudumu wa ofisi hiyo, msichana mrembo, mweupe wa haja, Kamanda Amata akamtazama kwa jicho la husuda.
“Habari mrembo,” alimsalimu.
“Nzuri, sijui nikusaidie nini?” yule mhudumu akajibu na kuuliza.
“Ok, naitwa Jaffar kutoka Tanzania, nimekuja hapa nina shida kidogo, siku za nyuma kuna kaka zangu walikuja kikazi wakafikia hapa lakini mpaka sasa hatujapata habari za wapi, nimekuja kufuatilia habari zao,” kamanda alimueleza yule mhudumu.

“Ok, naomba uingie ofisi namba tano kuna mtu atakuhudumia,” akajibiwa. Kamanda Amata bila hofu akaenda na kuingia katika ofisi hiyo, pale akamkuta bwana mmoja aliyevali nadhifu kabisa. akamsabahi na kumueleza shida yake.
Yule bwana akamkazia macho Kamanda Amata.
“Unasema unaitwa Jaffar?” akauliza.
“Ndiyo,” akajibu Kamanda.

Yule mtu akainua simu yake na kupiga namba Fulani, mara kijana mmoja akaingia na mabegi manne makubwa.
“Hizi ni mali za kaka zako, ila taarifa nyingine ya kujua wapi walipo ndugu zako kiukweli hatujui, na hatuna msaada mwingine zaidi ya huu tuliokupa sasa,” yule bwana akajibu. Kamanda Amata akayatazama yale masanduku na kuwaamuru wale wahudumu wayafungue nao wakafanya hivyo; akatazama vitu vilivyomo katika masanduku hayo kwa harakaharaka aliporidhika akamshukuru yule bwana. Kwa kusaidiwa na wale wahudumu akatoka nay ale masanduku lakini muda huo tayari alikuwa amekwishayasoma mazingira ya hoteli hiyo.

Saa 6.00 Mchana- Dar es salaam Club
Akiwa ameketi kwenye moja ya viti vilivyojaa katika ukumbi wa club hiyo, Kamanda Amata alikuwa aking’aza macho huku na kule kumwangalia mgeni asiyemjua. Moyo wake ulijaa hasira sana na watu hao wanaojiita maharamia. Aliendelea kutulia pale huku akitazama wanaoingia na wanaotoka.
Akiwa katika hali hiyo, mara waliingia watu watatu, wanaume walioongozwa na kijana mmoja aliyeonekana machachari. Walipita kona mbili tatu na kuelekea upande wa nyuma ambao ulikuwa na vyumba vya V.I.P, vyumba vilivyotumika kwa kazi au mazungumzo maalum. Akiwa katika kushangaa watu hao mara alihisi kitu kama bilauri ikitua juu ya meza yake, akageuka na kukutana macho na msichana aliyekuwa ameketi mbele yake bila kukaribishwa.
“Usishtuke kaka Jaffar,” yule mwanadada akamwambia. Kamanda Amata akashtuka kusikia jina lake likitamkwa sawia na binti huyo, “Naitwa Farheen, nafanya kazi hoteli ya Ramada Plaza,” akajieleza. Kamanda akamtazama bila kummaliza.

“Nikusaidie nini?” akamuuliza.
“Sikia Jaffar, najua huko hapa kwa minajiri gani, lakini ninachokwambia usifanye hicho unachotaka kufanya, utajiweka hatarini, tukiachana hapa, hakikisha unauacha salama mji wa Mogadishu, tayari wanajua lile ulilolifanya leo pale Jabir Hotel, sina zaidi,” yule mwanadada akamaliza na kunywa kinywaji chake kisha akaondoka kutoka pale mezani na kuingia upande ule wenye vyumba vya V.I.P.
Kamanda Amata alimtazama yule mwanamke na kisha akamfuata alikokwenda, alipouaona mlango alioingia naye akaelekea huko, hakuogopa, aliingia moja kwa moja ndani ya chumba hicho na akajikuta yeye na mwanadada yule tu wakitazamana.

“Unanifuata?” akauliza, “Watakuua,” akaongeza huku akionesha ishara ya kukata shingo kwa mkono wake.
“Bila shaka unajua mengi sana juu ya kaka zangu, nataka unieleze, nani aliyewaua?” kamanda akauliza.
Yule mwanadada akatoa cheko la dharau, na alipotulia akamtazama kamanda huku akiweka vizuri gauni lake refu lililomfunika mpaka miguuni, “Wauaji, wamewaua kaka zako,” akatoa jibu tata. Kamanda Amata akageuka na kutoka ndani ya chumba kile akimuacaha yule mwanamke peke yake, kabla hajavuta hatua nne au tano akakutana na watu wengine wawili wakamzuia. Kamanda akasimama katikati ya watu hao na yule mwanamke, lakini yule mwanamke akatoa ishara ya kuwa wamuache aondoke, akaondoka zake.

“Inaonekana sasa Tanzania wamemleta mtu makini, maana hata kuzifuata nyayo zake lazima hujipange, ama atakupotea au atakupoteza,” aliongea mmoja wa watu wale walioingia katika chumba cha V.I.P pale Dar es salaam Club.
“Ndiyo, maana jinsi alivyoingia tu hapa Mogadishu imetosha kutuonesha kuwa ni mtu hatari, inabidi juu chini ashughulikiwe mara moja,” mwingine akadakia.
“Aaaaa sio kazi kubwa kumtia mkononi yule mende, ni kumuotea tu chumbani kwake basi,” mtu wa tatu aliongeza.
“Tutamuoteaje?” yule mjumbe wa kwanza akauliza kwa shauku huku akijivuta kwa mbele kusikiliza hoja hiyo.
“Tunamtegea mtu chumbani kwake amsubiri, akiingia tu asimpe nafasi, ammalize,” wazo likatolewa, wote wakalipitisha. Baada ya hapo wakazungumza machache kati yao na kuagana wakiwa na mikakati kabambe ya kumnasa kamanda Amata.

Kamanda Amata kwa hatua za taratibu alijivuta na kuingia ndani ya gari yake, akaketi kimya akitazama nyendo za hapa na pale, dakika arobaini na tano baadae aliwaona wale watu wakitoka ndani ya club ile na kuziendea gari zilizokuwa hapo, kila mmoja akaingia katika gari yake na kuondoka. Kamanda Amata akaichagua moja kati ya gari hizo tatu na kuifuatailia mpaka inapoishia.

Kwa mwendo wa wastani alikuwa nyuma ya gari kama tatu hivi huku ile anayoifuata ikiwa mbele sana lakini alihakikisha kuwa haimpotei katika macho yake. Baada ya mwendo kama wa dakika ishirini na sita hivi, ile gari ikaingia katika jumba Fulani la kifahari ambalo lilizungukwa na ukuta mkubwa sana ulioziba eneo kubwa na kufanya jumba hilo lionekane kwa tabu. Kamanda akapita na kutupia jicho jumba hilo, mbele kidogo akaegesha gari yake na kutulia akisubiri ni wakati gani yule bwana atatoka. Akiwa ametulia ndani ya gari yake alijikuta akipitiwa na usingizi mtamu wenye ndoto mbalimbali, haloi hiyo ilikuwa ikimsumbua sana, wakati akigombana na hali hiyo aliiona ile gari ikitoka langoni na kurudi kwa barabara ileile iliyojia.

Amata naye akaigeuza gari yake na kuifuata kwa mwendo wa wastani akihakikisha kuwa yule mtu asijue kabisa kama anafuatwa. Baada ya kupita mitaa kadhaa ile gari ilitokea upande wa baharini na kufuata barabara kandokando yake. Akiendelea kupishana na magari kadhaa makubwa kwa madogo, Kamanda Amata aliendelea kuifuata ile gari, sasa aliiona ikiongeza kasi kuliko mwanzo, akilini mwake akajua kwa vyovyote mtu huyo amejua kama anafuatiliwa. Amata naye akabadilisha gia na gari yake aina ya Kilimanjaro ikaanza kuinyanyasa barabara kwa mwendo kasi, akiwa katika kasi hiyo akiifukluza ile gari nyingine, alisikia sauti ya honi ya garimoshi, alipotazama vizuri kulikuwa na reli inakatisha eneo lile. Kizuizi cha barabar kilikuwa kikiteremka taratibu kuzuia magari yasivuke katika reli hiyo, lakini aliishuhudia ile gari anayoifuata ikivuka kwa kasi na kuvunja kile kizuizi ambacho tayari kilikuwa kimefika chini. Kamanda Amata alisonya kwa hasira kwani alielewa jambo alilofanya mtu yule, hakuwa na jinsi ilibisi kusubiri mpaka ile treni ilipomalizika, hakuweza tena kuiona ile gari, naye kwa kuonesha kuwa ni mwelevu akageuza gari na kurudi alikotoka hakuifuata ile njia.

Breki ya kwanza ilikuwa ni katika hoteli ya Ramada Plazza, akaegesha gari yake na kuingia tena ndani ya hoteli hiyo. Mara hii alipita mapokezi na kuzunguka upande wa maofisi, akasimama katika mlango ulioandikwa ‘Security Room,’ akagonga, mlango ukafunguliwa, akaingia ndani na kukuta watu wawili.

“Samahani hairuhusiwi mtu kuingia humu ndani,” mmoja wao akamwambia Kamanda Amata lakini kabla hajajibiwa alikuta akipewa kipigo cha dharula na kupoteza fahamu, vivyo hivyo kwa yule mwingine. Kamanda Amata akavuta droo na kupekua pekua huku akisoma tarehe za disc hizo ndogo zilizohifadhi kumbukumbu za matukio ya kila siku. Alipoona katika saraka hiyo hakuna anachokitaka akapekuwa saraka nyingine na kuiona ile aliyoihitaji, alipojiridhisha kuwa ndiyo hiyo akaipachika katika chombo maalum kwa kazi hiyo na kuanza kurudisha nyuma kuangali matukio ua siku hiyo.
Aliirudisha nrudisha nyuma picha hiyo ya video iliyopigwa kwa kamera za usalama, ikionesha Jamil alivyokamatwa, akiamriwa kuweka mikono kichwani. Kamanda Amata alitazama kwa makini sana, akajaribu kuangalia sura za watu wale waliokuwa na silaha nzito za kivita, alitazama jinsi walivyompakia Jamil kwenye jeep na kuondoka nae. Kamanda Amata akaichukua disc hiyo na kuitia mfukoni kisha akatoka nje ya ofisi hiyo na kuondoka zake.

Moja kwa moja akaenda kufuata taarifa za Sebeki baada ya kujua kuwa naye alikufa kwa mlipuko wa bomu mbele tu ya hoteli aliyofikia, nako alipata disc kama ile iliyohifadhi picha za video zikionesha mlipuko ule, Kamanda Amata alitazama kwa makini sana, mara hii aliona taswira ya mwanamke, alijaribu kurudisharudisha mara kwa mara kumwangalia mwanamke huyo lakini hakuweza kumtambua, aliichukua disc hiyo na kupotea zake.
Dakika kumi na tano baadae alifika kwenye hoteli aliyofikia, hoteli ya Jazeera Palace, kabla hajashuka garini, alifungua kompyuta ndogo ndani ya gari yake, akapachika zile disc moja baada ya nyingine na kuzituma picha hizo katika idara ya usalama Tanzania ili zifanyiwe kazi. Alipohakikisha kazi imekamilika akateremka na kuvuta hatua kuingia ndani ya hoteli hiyo.

“Ujumbe wowote!” akamwambia mhudumu wa mapokezi, yule mhuidumu akainama na kutoa bahasha moja ya kaki akampatia. Amata akainyakua na kuondoka zake kuelekea ghorofa ya juu. Alifika mlangoni mwa chumba chake, kabla hajashika kitasa alisimama kwa sekunde kadhaa, akagundua kuwa ndani ya chumba chake kuna mgeni, alitazama alama ndogo aliyoiacha kwenye kitaza cha mlango ambayo haikuwepo tena. Akachomoa bastola yake na kuiweka sawa, kisha akafungua mlango na kuuacha wazi bila yeye kuingia, ukimya ukatawala. Amata hakuingia ndani na wala aliyekuwa ndani hakutoka nje, waliwindana. kamanda Amata akaamua kuingia kwa kasi huku akijirusha kwa ustadi wa hali ya juu sana na kutua upande wa pili wa chumba, kwa haraka alimuona mtu aliyemtarajia nyuma ya mlango, yule jamaa alifyatua risasi iliyomkosa padogo Kamanda na kuchimba ukuta, Kamanda Amata akavingirika na kupita chini ya kitanda, risasi ya pili nayo ikamkosa padogo vilevile, wakati huo Kamnda Amata akawa tayari ametokea upande wa pili, kwa kasi ya ajabu alifyatua risasi iliyopiga sawia bega la mtu huyo.

“Aaaaaaaaiiiihhhhgggghhhh!!!!” yowe la maumivu likamtoka yule mtu huku akiidondosha bastola yak echini. Ksbls hsjsfiks chini sakafuni risasi ya pili ilifumua kifua cha mtu huyo na kumbwaga chini. Kamanda Amata akawahi pale alipoanguka kabla hajakata roho.
“Nani kakutuma?” akamwuliza, lakini yule mtu alikuwa akipumua na kuangusha mabonge ya damu kutoka kinywani mwake. Akamtazama Amata, lakini hakujua ajibu nini, “Wapi mmemweka Jamil?” akauliza tena.
“Gha…la….ni…” akajibu kwa tabu.
“Ghalani wapi?” Kamanda akauliza tena.
“Ki…wa…nda… cha ngu…. Nguuuoo” baada ya kujibu hilo yule mtu akanyamaza kimya, roho ikauacha mwili.


Amata akairudisha bastola yake katika mahali husika, akaugeuza mwili wa yule mtu na kupekuwa mifukoni, akatoa simu moja, zaidi ya hapo hakukuwa na kitu chochote kingine. Kamanda Amata aliitazama ile simu kwa makini sana, ilikuwa ni simu ya kisasa sana iliyofungwa mtambo wa GPS ambao unaweza kukuonesha mahali ulipo au mahali unapaotaka kwenda. Kamanda Amata akachana bahasha aliyopewa na ndani yake kukadondoka kijikadi kigumu kimoja, akakiokota na kukisoma.
‘Mujabba Club 2030’
Akairudisha ndani ya bahasha ile na kuitia katika begi. Kisha akainua mkono wa simu na kubofya namba za chumba cha usalama cha hoteli hiyo.
“Haraka sana mfike chumba namba 305 kuna shida,” akakata simu baada ya kutoa taarifa hiyo. Nukta chache tu mlango wa chumba chake ukagongwa, akawaruhusu kufungua. Vijana wawili waliokuwa na askari mmoja mwenye silaha waliingia na kulakiwa na dimbwi la damu, wakapigwa na butwaa.

“Huyu ni nani na ameingiaje chumbani mwangu?” Kamanda akawauliza.
“Hata sisi mzee hatujui, na ndo maana tunashangaa,” akajibu mmoja wa vijana wale.
“Haya ondoeni mzoga wenu,” Kamanda akawaamuru, nao mara moja wakapiga simu na gari ya wagonjwa ikafika pamoja na polisi kadhaa. Kamanda Amata akatoa maelezo kwa maandishi, misatari miwili tu ilitosha na kuwarudisia faili lao. Yule askari aliposoma akamtazama kamanda usoni.
“Ni hivi tu?” akauliza.
“Ndiyo ni hivyohivyo tu,” akajibu Kamanda.

Shalabah alionekana kuchanganyikiwa, alikuwa akizunguka huku na kule akiwa kama mtu aliyesahau kitu, viajana wake walikuwa wameketi kwa utulivu kabisa.
“Sharon,” akaita, na Sharoni akainua uso kumtazama, “Tuna kazi kubwa.”
“Huyu ni chui sijui au tumwiteje, maana hatabiriki,” Sharon alijibu.
“Mpaka sasa amekwishatuondolea watu takriban watatu, tunamfanyeje mtu huyu?” Shalabah akauliza.
“Leo ni kumfanyia uvamizi wa maana na kummaliza,” Sharon, ambaye ndiye kiongozi wa kikosi hicho hatari alitoa uamuzi.

“Yule ni zaidi ya jeshi kaka, tutumie mbinu nyingine tu, lakini swala la kumvamia tusithubutu kulifanya,” Shalabah alitoa rai. Mara mlango wa chumba hicho ukafunguliwa, Fasendy akaingia kati ya wanaume hao.
“Nimekuja,” Fasendy akasema.
“Karibu sana, bila kuchelewa nataka uongoze kikosi hiki ukisaidiana na Sharon kumkabili mtu huyu, muilete roho ama ndani ya mfuko au mikononi mwenu, malipo makubwa umeahidiwa kutoka kwa Mr. Lonely,” Shalabah alimwambia Fasendy na kuitupa picha ndogo mezani, fasendy akaiokota na kuitazama.
“Mbona umeshtuka?” Shalabah akauliza.
Fasendy akatikisa kichwa juu chini, “Sasa Mogadishu imekuwa ndogo.”
“Kwa nini unasema hivyo?” Sharon akauliza.

“Huyu jamaa ni hatari sana, usije kujidanganya kumkabili ana kwa ana, huu ni ama mzimu au roboti ana akili ya ajabu ana mbinu za utatanishi,” Fasendy alieleza.
Shalabah na Sharon wakatazamana, kisha wakarudisha macho yao kwa Fasendy.
“Kwa hiyo unasemaje?” Shalabah akauliza.
“Kufa atakufa tu lakini si kwa ngumi wala teke, huyu labda tumwekee sumu,” Fasendy akajibu.
“Fasendy, mbona sikuelewi?” Sharon akauliza.
“Utanielewa tu Sharon siku ukikutana naye, ninamaanisha huyu jamaa tujipange upya ili kumkabili,” Fasendy akaeleza.
“Yuko Jazeera Palace chumba namba 305, fanya unaloweza, niletee majibu ya kuridhisha,” Shalabah alimpa maagizo Fasendy kisha yeye kuwaacha hapo na kuingia mlango mwingine.

CLUB MUJABBA saa 2.30 usiku
KATIKA kona moja ya ukumbi mdogo wa club hiyo, Kamanda Amata alitulia kimya akiwa na juisi baridi huku akisubiri huyo aliyemuachia ujumbe kule hotelini. Hakuwa na hofu kwa kuwa alikwishzoea kukutana na watu asiyowajua.
Haikumchukua muda mrefu, mbele yake alimuona mzee wa makamo aliyeonekana kuishiwa nguvu tayari akiwa anatembea kwa msaada wa mkongojo, alitembea kwa taabu mpaka pale kwenye meza ya Kamanda Amata, akavuta kiti na kuketi kwa mtindo wa kutazamana. Kamanda Amata alimtazama shaibu huyo mwenye nywele nyeupe zilizojaa mvi, miwani ya macho, suti iliyomkaa vizuri na mkononi mwake alikuwa na saa kubwa ya gharama sana ikitanguliwa na pete ya dhahabu.

“Kamanda Amata,” akaita kwa tabu huku akisindikiza maneno yake na kikohozi kikavu.
“Yeah ndo mimi, wewe, wewe ni nani?” kamanda akauliza kwa uoga kidogo.
“Haunijui, lakini utanijua mimi ni nani,” akasema yule mzee na kuanza kukohoa, akakohoa sana mpaka Kamanda akamwonea huruma.
“Babu, nikupeleke hospitali,” kamanda akamwambia.
Yule babu akamwangalia Kamanda usoni, “Ngoja kidogo,” akamwambia.
Akakohoa tena mara mbili kwa nguvu, mkononi mwake kikadondoka kitu cheusi, akakipekuwa kwenye kohozi la njano, Kamanda Amata, alishikwa na kichefuchefu lakini alivumilia.

“Kamanda Amata, kazi hii uliyopewa ni wewe tu unayeweza kuifanya kwa kuwa nakufahamu tangu ujana wako, nakufahamu tangu ukiwa C.C.P kabla hujatolewa kuja idara ya usalama,” yule mzsee akamwambia, akakohoa lakini sasa kikohozi kilikuwa cha kawaida, akaendelea, “Umeiona hiyo chip? (Kamanda akatikisa kichwa huku akiifuta kwa kitambaa) ndani yake kuna kila kitu juu ya sakata hili, Kamanda hii ni hujuma kubwa sana, mimi mwenyewe nimeijua wakati niko pale Msanga Mkuu, Mtwara, najua, najua sana,” akajishika mikono yake usoni na kuvua sura la bandia alilokuwa amelivaa usoni mwake, lililotoka na nywele zile nyeupe, akabaki na sura yake halisi.
Mshtuko mkubwa ukampata Kamanda Amata, akabaki mdomo wazi, hakuamini anachokiona mbele yake, mzimu.
“Usiogope, sio mzimu ni mimi,” Yule mzee akaongea kwa upole.
“Mwalimu?” Kamanda akauliza.

“Ndiyo ni mimi, sikufa kama unavyojua au niseme mnavyojua, ile ilikuwa ni mbinu yangu ya kutoroka na kwenda katika upeo wa macho na akili zenu, niko hai,” yule mzee alijieleza.
“Ni ngumu kuamini, ni ngumu sana kuamini,” kamanda alisema huku akiwa kajishika kichwa chake.
“Kamanda Amata, ninakuamini sana ndiyo maana nimejidhihirisha kwako, na ninajua kuwa hautamwambia mtu yeyote kuwa umekutana na mimi, lazima uchanganyikiwe, lazima Kamanda na ninajua kwa nini, lakini mimi kufa mbele ya macho yenu ilikuwa ni kuondoka kwa sababu nilishaijua hujuma inayokuja na ambayo ningehusishwa kwa namna moja au nyingine, sikuwa tayari kwa hilo, nikajiondoa kwa njia ile, sasa habari iko hivi,”
Miaka kumi na nne iliyopita

Wizara ya nishati na madini
ILIKUWA ni ajenda ndefu iliyojadiliwa kwa siku kadhaa ndani ya ofisi hiyo nyeti katika serikali ya Tanzania. Yote hiyo ilitokana na ugunduzi uliofanywa na wanasayansi wa Tanzania wakisaidiwa na wale wa Urusi waliokaa katika pwani na bahari ya Hindi huko Mtwara. Madini ya Urani na mengineyo hatari kabisa kwa maisha ya binadamu na viumbe vingine yaligunduliwa kutoka katika kina kirefu cha bahari eneo la Msanaga Mkuu. Baada ya kugundulika na kuwa na uhakika kuwa ndiyo yenyewe serikali ya Urusi ilitaka kuingia mkaba na serikali ya Tanzania ili kuchimba na kurutubisha madini hayo hapahapa nchini. Baada ya kusainiwa kwa mikataba pale wizara ya madini; serikali hizo mbili zilikubaliana kugawana kwa asilimia, ile ya Tanzania 60% na ile ya Urusi 40%. Kwa mkataba huu ilikuwa Tanzania ifaidike sana. Kubaliano linguine lilikuwa ni lile la kuunganisha nguvu za kijeshi kwani nchi hizo mbili zilitaka kurutubisha madini hayo na kutengeneza silaha kali za na nzito za kivita.

Katia ya watu waliokuwa wakifuatilia kila hatua ya mkataba na makubaliano hayo tangu kuanza kwa uchunguzi huo alikuwa ni mwanausalama mashuhuri sana katika idara ya usalama Tanzania ambaye mara kadhaa aliwahi kufanya kazi na mashirika makubwa kama NSA, CIA, MOSSAD na mengine mengi kwa kutoa ushauri au mafunzo fulani ya mbinu za kijasusi; hata alipostahafu bado serikali ya Tanzania ilimchukua kwa kazi maalum ikiwa ni pamoja na kuanzisha idara ya kijasusi, idara nyeti ya kushughulikia matatizo ya kimataifa katika Nyanja ya kiusalama. Mzee huyo waliyempa jina la ‘The Chamelleon’ lakini kwa jina lake halisi ni Mzee Mwambe, kachero aloyewahi kuwekwa kwenye jeneza mara kadhaa ikidhaniwa amekufa lakini alikuwa akifanya danganya toto. Mzee Mwambe alijichanganya katika kundi la watafiti wa Tanzania na kuangalia kila kinachofanyika, kwa kuwa serikali ilimuweka kwa malengo maalum alikuwa akipewa nafasi za juu makusudi ili akutane na watu mbalimbali na ajue nini kinazungumziwa katika mradi huo.

‘The Chamelleon’, aliushtukia mchezo mchafu unaotaka kufanywa na baadhi ya watu katika mradi huo. Tajiri mmoja mkubwa kutoka nchi za Magharibi, tajiri asiyeonekana kwa macho ya binadamu alikuwa akiyataka madini hayo ama yawe yamerutubishwa au yawe ghafi. Alitoa pesa nyingi sana kuhonga huku na kule na wale wenye uchu wakazipokea pesa hizo na kuzifanyia watakayo. Mmoja wa wanasayansi wakubwa wa Urusi alijiingiza kwenye sakata hilo na kuwa akitoa siri kwa tajiri huyo ya kuwa nini kinaendelea katika mradi huo. The Chamelleon aliyekuwa akiujua mchezo mzima huo, alikuwa akitoa taarifa zake katika idara ya usalama ya serikali ya Tanzania kuwa wakae macho na hujuma hiyo inayotaka kufanywa na baadhi ya wenye uchu wa pesa chafu. Kila aliyekuwa akihusika kwa namna moja au nyingine, serikali ya Tanzania ilikuwa makini kuwawajibisha na kuwatimua kazi wote wanaohusika, hakukuwa na mchezo hata kidogo.

Baada ya miaka kadhaa ikajulikana kuwa ni nani anayetoa taarifa hizo serikalini, walijaribu kila mbinu ya kumshawishi The Chamelleon, kwa rushwa za aina mbalimbali lakini aliwakatalia katakata.
Mkutano wake wa mwisho kabla ya kufa kwake aliufanya na Rais wa nchi pale katika Ikulu ndogo ya Chamwino, Dodoma, kilikuwa kikao cha siri sana.

CHAMWINO – DODOMA

ULIKUWA ni mkutano wa siri lakini uliochukua muda mrefu wa kutosha ndani ya Ikulu hiyo ndogo pale Chamwino. Mzee Mwambe, kachero aliyekuwa kazini kwa shughuli maalum alikuwa akikutana na Rais, mkuu wan chi kujadiliana mambo kadhaa. Tayari aliiona hatari kubwa mbele yake, mpango kabambe wa kumuondoa duniani ili wapenda pesa wafanye kile watakacho.

Alipogundua hilo alifanya haraka kumshawishi Rais kuanzisha kitengo hicho cha kijasusi katika Tanzania, TSA, wazo ambalo halikupingwa na mpango ulianza mara moja.
“Sasa unajua kama ulivyosema kuwa ni muhimu kuwa na kitengo hicho, sawa, lakini unafikiri ni nani anaweza kukiongoza, muaminifu?” Mheshimiwa Rais alihoji.
Mzee Mwambe alitoa maelekezo yote mpaka jinsi ya kukiweka kitengo hicho. Baada ya mazungumzo hayo ndipo alipompa taarifa mpya juu ya maendeleo ya kazi za ujenzi wa kituo cha kurutubisha Urani huko Mtwara, lakini alionesha wazi hofu yake ya kupangiwa njama ya kuuawa na wabaya wake ambao walikuwa wakifanya juu chini kuhujumu mkakati huo.

“Nilifikiri kukukabidhi wewe kitengo hiki,” Mheshimiwa alimwambia Mzee huyo.
“Hapana, mpe Madam S, yeye ni mtu wangu wa karibu na ni jasiri sana, msiri aliyebobea kwenye kazi hizi,” Mzee Mwambe akajibu kwa kutoa maelekezo.
“Na upande wa vijana je?”
“Nimemwandaa vyema Amata Ric, yeye atakuwa Kamanda wa kikosi, baadaye tutaona jinsi ya kuwapata vijana wengine wenye hari na uzalendo wa taifa lao, kama unavyojua nimempa kazi nyingi ngumu za kimataifa, amezifanya kwa ustadi wa hali ya juu sana, yeye amefuzu katika kila Nyanja ya mapambano, sasa yuko huko Sierra Leone, kuna kazi nyingine nimempa,” Mzee yule alieleza.

Mheshimiwa Rais aliinamisha kichwa mezani, kisha akainua uso wake na kumtazama Mzee huyo.
“Ok, mi nafikiri kazi uliyoifanya mpaka hapa imetosha, nikuondoa kwenye nafasi yako nisije kukupoteza kama walivyopanga wabaya hao,” Mheshimiwa Rais alionesha wasiwasi wake wa wazi wa kumpoteza Kachero wake wa juu kabisa ingawazje alikuwa amestahafu. Mzee Mwambe alikuwa kimya akimsikiliza, akakohoa kidogo na kusema, “Sawa, ni wazo zuri lakini huna budi kumchagua mtu makini kukaa pale”.
Ilichukua masaa takribani matano kuhitimisha kikao hicho ambacho kilimuacha Rais na maswali mkubwa, shaka nzito na hofu ya kutosha, ‘wananisaliti?’ alijiuliza.

Ilikuwa ni baada ya kuagana na Rais pale Chamwino, Mzee Mwambe alikuwa akitoka na gari yake akiiacha barabara ya kuingilia Chamwino, sasa alikuwa alkiingia barabara kubwa ya Dodoma-Morogoro alipokutana na lori kubwa la mizigo lililoigonga gari yake kwa kishindo, ngao kubwa la chuma la lori lile liliifinya vibaya gari ya Mzee Mwambe na matairi makubwa kuibonda, kisha ile lori haikusimama, iliendelea na safari kama kilomita tano na dereva akaitelekeza na kuondoka.

Hali ilikuwa tete, Mzee Mwambe alitolewa kwenye gari ile kwa shida na kukimbizwa hospitali ya Dodoma kwa matibabu, lakini wakiwa pale Dodoma ilionekana wazi kuwa hawezi kupata matibabu stahiki kwa jinsi alivyokuwa ameumia hasa kwa ndani, hivyo alipewa rufaa na usiku huohuo aliondoshwa na ndege ya serikali mpaka hospitali ya Taifa ya Muhimbili. Pale napo hali ilikuwa hivyohivyo, Mzee Mwambe aliondoshwa na kupelekwa nje ya nchi kwa matibabu, alikuwa huko kwa siku kadhaa ndipo taarifa mbaya ilipokuja Tanzania kuwa Mzee huyo, Kachero wa siku nyingi, The Chamelleon, amefariki dunia katika hospitali kubwa ya Appolo.
Ilikuwa ni taarifa iliyotikisa idara nzima ya usalama katika serikalai ya Tanzania, wakati upande huu unasikitika basi upande mwingine ulikuwa unafurahia, tafrija kubwa iliangushwa katika hoteli ya Embassy pale Dar es salaam, tafrija ya kushangilia ushindi, ‘Tumekata mzizi wa fitna.’ilikuwa kama kauli mbiu.

6…rejea, MOGADISHU CLUB ya MUJABBA
“Kamanda Amata, mimi sikufa, ile ilikuwa ni mbinu niliyoipanga nikiwa hospitali mara tu baada ya kuipata nafuu na kuhakikishiwa uzima,” Mzee Mwambe alimwambia Kamanda Amata. Mshangao wa wazi ulionekana usoni mwa Kamanda Amata.
“Usishangae Kamanda, inapobidi unafanya hivyo ili kujiondoa machoni mwa watu, na wapo wengi waliofanya hivyo hasa majasusi wan je kwa nini isiwe mimi.
“Sasa unaishi wapi Mzee?” kamanda akauliza.

“Naishi Tanzania, Lindi kwetu, mi nilirudi Tanzania mwaka mmoja baadae, na moja kwa moja nikaenda kuishi kwetu Lindi, lakini harakati zangu hazikukomea hapo, Kamanda, ukiwa mzalendo ni mzalendo tu na ukiwa fisadi ni fisadi mpaka vizazi vyako. Nilirudi na kuishi maisha duni sana hiyo ilikuwa ni mbinu yangu, nikapata kazi ya ulinzi palepale Msanga Mkuu kwenye duka moja kubwa la Prakesh, ambalo kutoka lilipo, kufika kwenye kile kinu hapakuwa mbali, hivyo niliendelea kufuatilia nyendo zote za ule mchezo bila wao kujua, nilikuwa nina uwezo wa kuingia mle ndani ya jengo lao kwa njia zangu mpaka nilipojua kilichopo, nilipotega vifaa vyangu vya kunasa sauti ndani ya ofisi ya mkurugenzi ambaye alikuwa na asili ya Uarabu ndipo nilipopata siri hii (akamwonesha ile memory card), nikajua kuwa ile meli lazima itekwe pale Somalia kwani huyu mkurugenzi alikuwa na mawasiliano na Maharamia, na ni mchezo uliochezwa, watu wanajua. Siku manowari ile ilipopakia yale makombora kwa ajili ya majaribio, nilikuwa naona kila kitu, kabla haijaondoka mimi niliondoka na kuja Somalia,” akakohoa kidogo kisha akaendelea na simulizi yake ambayo ilimuwacha Amata katika hali ya bumbuwazi,

“Unasikia, Kamanda Amata, hawa jamaa wamejipanga, sasa kila unaporudi hotelini kwako hakikisha unapita kaunta utakuta ujumbe wako, ukiona siku hakuna ujumbe wowote ujue nimepatwa na hatari kubwa, naomba tuagane,” Mzee Mwambe akamaliza na kuiweka vizuri sura yake, kisha akainuka na kutoka ndani ya club ile. Kamanda Amata alikuwa akimwangalia mzee huyo mpaka alipopotea, moyoni mwake hakuwa anaamini wala hakuwa haamini, alifikicha macho mara kadhaa kuona kama yuko usingizini lakini sivyo.

Saa saba usiku, Kamanda Amata aliegesha gari yake kando kando ya hoteli moja iliyo pembezoni mwa bahari ya Hindi, hapo aliweza kuona mandhari nzuri ya usiku katika bandari ya zamani ya Mogadishu. Kutokana na maelekezo aliyoyapata katika ile memory card aliyopewa na yule mzee ‘The Chamelleon’ alihakikisha hakosei maelekezo hayo. Alijiweka sawa na kuteremka garini akiwa na nguo nyeusi tupu, mkononi akiwa na begi alilolishikilia. Kwa mwendo wa hadhari wa kukimbia na kutembea, aliambaa na ukuta mpaka kwenye kingo za gati la zamani kabisa la bandari hiyo, akatulia na kutazama huku na kule, aliona walinzi waliokuwa wakirandaranda, alipohakikisha hawajageukia upande wake, alivuka eneo hilo na kufikia kwenye miti mingi ya mikoko iliyoota sambamba na miisho ya ukuta huo, akatulia akisikiliza lolote lisilomhusu, alipoona hali ni shwari alifungua begi lake na kutoa vifaa kadhaa vya uogeleaji, akavaa tayari tayari kisha taratibu akaingia majini bila kumgutusha mtu yeyote.

Kamanda alipiga mbizi na kujivuta mpaka kwenye kilindi cha bahari, Kamanda Amata akiwa anasaidiwa na mitungi ya hewa ya oksijeni mgongoni mwake kwa mbali aliona kitu kama ukuta uliojengwa ndani ya maji, aliuendea na kuufuata ulikokwenda, mbele kabisa alikutana na mlango mkubwa uliofungwa kwa mnyororo wenye kutu na kufuli lake lilikuwa kwa ndani, hakujali, alichomoa kijimtungi kidogo alichokipachika juu ya tumbo lake, akakimata mkononi, na kukibonyeza kwa juu kisha kikaanza kutoa moto wa gesi ambao haukuweza kuathiliwa na maji.

Taratibu akakata ule mnyororo na kuugawanya huku na huku, akakirudisha kile kijimtungi mahala pake na kuutikisa ule mlango, bado ulikuwa ngangari, ukiszingatia ulikuwa umekandamizwa na msukumo mkubwa wa maji, akatoka na kutazama kama kumahala pengine penye mlango hakuona. Akiwa katika kurudi katika ule mlango, akaona kitu cha kustahajabisha kidogo. Kitu kama donge la hewa likipita mbele yake kutokea chini, likielekea juu. Hii kwa Kamnda ilikuwa na maana, akajibinua na kuelekea upande wa chini kule lilikotokea donge lile, akakutana na ukuta mwingine lakini hapa palikuwa na tundu kubwa ambalo angeweza kupeita bila shida, akachomoa tochi yake na kuingia taratibu huku akitazama huku na huko.

Lilikuwa ni tundu refu sana, lakini alifanikiwa kufika mwisho wake, kote kulikuwa ni maji tupu. Alipofungua kijimlango kidogo kilichokuwa na chekeche la kuzuia takataka akafanikiwa kuingia ndani. Lilikuwa ni jengo kubwa, huku ardhini tungeliita ‘godown’, ndani yake Kamanda aliona mabaki na magofui mengi ya meli za zamani zilizotelekezwa. ‘Kwa nini jengo hili liwe huku?’ alijiuliza, kisha akaendelea kuogelea akipita huku na huko, akiwa anaelekea karibu kabisa na lile lango aliloshindwa kulifungua ndipo alipoiona meli kubwa iliyojikita chini na kufungwa na minyoronyoro mikubwa mikubwa.

Kerov Class-JWTZ 26-90, yalikuwa ni maandishi yaliyoandikwa katika upande mmoja wa meli hiyo juu kidogo ya tundu kubwa la kutolea nanga. Kamanda akatikisa kichwa kuashiri amegundua kitu, akaingia ndani ya meli hiyo na moja kwa moja akaingia chumba cha kuhifadhi makombora, alifika bila kupotea kutokana na ramani aliyoikuta katika memory card aliyopewa na yule mzee.

Katika vishikio vya makombora hayo, ni vishikio viwili tu ambavyo havikuwa na makombora, ikiwa na maana mawili kati ya kumi na mbili yalikuwa yamekwishaondolewa, akayazunguka na kulifikia moja, akatulia pale, akalitazama mbele ya kichwa cha kombola hilo na kuona skurubu kadhaa zilizoshikilia sehemu hiyo ya mbele. Alikwishasoma muundo wa makombora hayo aina ya R-26 IBM, akatoa kifaa cha kufungulia skurubu hicho kinachotumia umeme wa betri ndogo ukubwa wa AAA, akafungua skurubu ya kwanza mpaka ya mwisho, kwa tahadhari kubwa akachomoa kichwa cha lile kombora, akakigeuzauza na kuona jinsi kiloivyotengenezwa kitaalamu, ni alama ya mlipuko ilichorwa kwa ndani, ikiwa na maana kuwa katika kichwa hicho ndipo penye mlipuko mbaya kabisa, yaani ndio bomu lenyewe, alipojiridhisha na hilo, akalegeza taratibu ile chemba yenye madini hatari ya Urani, akakichomoa kutoka kwenye kile kichwa kisha akakifunga vizuri katika jaketi lake.

Alipomaliza kurudishia kile kifuniko kama kilivyokuwa mwanzo, akaitazama saa yake, ilikuwa inatimu saa nane usiku, akavuta mpira wenye hewa ya oksijeni na kutazama kipimo cha hewa aliyobakia nayo, ilikuwa haitoshi kustahimili zaidi ya dakika arobaini na tano. Akaamua kutoka eneo lile na kufikiri kurudi usiku unaofuata. Akapita njia ileile aliyoingia nayo na kutoka nje ya meli ile. Alipokuwa anatafuta lile tundu la kutokea ndipo alipohisi kitu kama mshale kikipenywa kati ya mgongo wake na mtungi wa gesi na kukata mikanda iliyoshikilia mtungi huo, ukafunguka. Kamanda akajua, tayari, ameonekana, akauacha mtungi ule ukidondoka taratibu, akachomoa bunduki yake aliyokuwa ameipachika mgongoni, bunduki kubwa yenye nguvu.

Mbele yake aliwaona wapiga mbizi wawili wakija upande wakiwa na mihsale ya kuwindia Papa, Kamanda akaliweka vizuri bunduki lake na kufyatua, risari ya kwanza ilipiga kichwa cha mmoja wao. Wakati Kamanda anajiandaa kupachika risasi nyingine, mshale wa yule mwingine ukamchoma katika nyama ya mkono sehemu ya kati ya bega na kiwiko, maumivu makali yakampata Amata, kabla hajafanya lolote yule jamaa alimfikia, Kamanda akakabwa koo. Hakuna aliyeweza kuongea chochote. Kamanda alikukuruka lakini ilikuwa ni ngumu kutokana na maumivu makali ya ule mshale. Akanyosha mikono yake na kuifyatua mipira ya hewa kutoka katika mtungi wa yule mtu, akakosa hewa na kumuachia Kamanda. Amata akatumia nafasi hiyo, akajivuta mguu na kuchomoa kisu, akamchoma tumboni na kumuona yule mtyu akilegea taratibu.

Akachomoa kitu kama tyubu ya dawa ya meno na kuifungua kicha akakipachika mdomoni, kidubwasha hicho kilihifadhi hewa ya oksijeni inayoweza kutumika ndani ya dakika kumi tu. Akajitahidi na kutoka nje ya ghala lile, Kamanda Amata akajivuta taratibu mpaka kwenye ile mikoko alipokuwa ameacha begi lake, hakulikuta, akajua kwa vyovyote wamemgundua, kengele za hatari kichwani mwake zikagonga, akajiweka kwenye hali ya tahadhari, akavua yale mavazi yake na kuyafunga pamoja kisha akaanza kutembea taratibu, mbele kidogo inapoishia ile mikoko na kuanza ule ukuta wan je kulikuwa na kijana mmoja mwenye bunduki kubwa akishika doria.

Kamanda Amata akatazama pande zote hakumuona mtu zaidi ya huyo tu, akajitokeza na kumwita, yule bwana alipogeuka, Kamnda akamrushia kile kifurushi cha zile nguo, yule mlinzi akababaika nacho, sekunde hiyohiyo, Amata aliruka kiufundi na kutua kwa miguu kifuani mwa yule mlinzi na kumpeleka chini, akamkandamiza pale chini mpaka alipohakikisha amelegea kabisa, akamuachia na kuondoka taratibu akiambaa na ule ukuta mpaka kwenye gari yake, akiwa mbali kabla ya kuifikia akabonyeza swichi yake ya mkono na kuiwasha gari hiyo kisha akatulia kuangalia kama kuna mtu atakayeisogelea au la, kwa hatua za taratibu akaifikia na kufungu milango kisha akajiweka kwenye kiti cha dereva, akafungu droo ya chini ya dashboard, akatoa kikasha cha huduma ya kwanza na kujiganga jeraha lake la mkononi.

Alipohakikisha yuko sawa, aliitoa gari yake taratibu na kuondoka eneo lile kurudi hotelini kwake.
“Ujumbe wowote,” alimwambia mhudumu wa mapokezi, yule mwanadada akainama chini na kutoa bahasha, Kamanda akaipokea na kuifungua hatua chache kabla hajaondoka, akasoma ujumbe uliopo, ulikuwa ujumbe mfupi sana, akaondoka na kuzikwea ngazi taratibu kuelekea chumbani mwake.

SEHEMU YA XIV
Kamanda Amata hakutamani kukaa chini au kufanya starehe yoyote maana alijua wazi akipoteza dakika au sekunde basi maisha yake yako hatarini, alishaonywa uhatari wa hao watu hivyo kila nukta alikuwa katika kujilinda kwa nguvu zote.

Ulikuwa ni wakati mgumu sana kwa Maharamia wa Mogadishu kumtega Kamanda Amata, kila walipojaribu waliambulia hasara tu. Mara kwa mara walikuwa wakiitana chemba na kujipanga upya mpaka upya ukaisha.
Sasa hoja ya kumdhibiti Amata ikafika kwa mtu wa juu kabisa, Mr. Lonely.

“Mi nashindwa kukuelewa Shalabah, huyo mtu ni mtu wa aina gani asiyewezekana kudhibitia, huyo ni Kunguni tu, nataka kichwa chake hapa ndani ya masaa sita tu” Mr. Lonely alitoa amri akiwa amewaka hasira.
“Tumejaribu kila namna ya kumnasa lakini tumeshimdwa, zaidi watu wetu wanapungua kila kukicha mzee,” Shalabah aliongea na luninga iliyobeba taswira ya mtu huyo asiyeonekana, ila katika taswira hiyo alionekana jinsi alivyofura kwa hasira.

“Mpaka mtu anaingia godown maana yake ameshajua kila kitu, hakuna mpelelezi yoyote ulimwengu huu amewahi kufika ‘kuzimu’ akarudi duniani, sasa huyu imekuwaje?” Mr. Lonely aling’aka kwa hasira zilizomfanya Shalabah kutulia kitini kwa upole, “Sasa nataka mfanye kazi niliyokupa mkiniaharibia biashara tu nakata shingo wote ninyi,” akamaliza na na ile luninga ikazama ardhini taratibu.
Shalabah akaliacha jumba hilo na kuondoka na gari yake aina ya Jaguar kurudi katika kambi ya muda ili kuwapanga vijana wake.

Juu ya jengo moja refu lililokuwa mkabala na hoteli ya Jazeera Palace, bunduki kubwa aina ya M107.50 Calliber Long range lilikuwa limesimama kwa miguu yake miwili huku kwenye kitako kukiwa na mwanamke aliyevalia suruali aina ya cardet, akiwa kaweka jicho lake la kulia kwenye kiona mbali kilichofungwa juu ya bunduki hilo. Akiwa kalala chini kwa utulivu huku pembeni yake kukiwa na kijana mwingine aliyebeba bunduki ya AK 47, usoni mwake akiwa kapachika darubini ambayo ilimsaidia kutazama kule anakitazama mwanamke yule.
“Umemuona?” yule kijana akamuliza Fasendy.

“Nimemuona,” Fasendy akajibu, huku bado jicho lake likiwa kwenye kiona mbali na akimwangalia kijana huyu kwa makini akiwa na mawzo chungu mbovu kichwani mwake. ‘Kwa nini nimuue? Mbona yeye aliniachia uhai wangu kule Uganda?’ alijiuliza huku akitembeza mtutu wa bunduki yake taratibu akifuatilia mwendo wa Kamanda Amata aliyekuwa akitoka kuifuata gari yake.

ITAENDELEA

Huu uzi utaletwa wote hatutoishia njiani wakuu

1.jpeg
 
HUJUMA - 3

Simulizi : Hujuma

Mkononi mwa Kamanda Amata kulikuwa na bahasha iliyowekwa kitu fulani ndani yake.
“Hapo hapo Fasendy, shoot... shoot Fasendy,” yule kijana alimwambia Fasendy, alipomgeukia alikutana na jicho kali la Fasendy.
“Kwani mi sijui kazi yangu?” Fasendy akamuuliza, kisha akarudisha jicho kwenye kile chombo na kupachika dole la shahada la mkono wa kulia katika kifyatulio, akavuta taratibu na kumwacha Kamanda Amata asogee pasipo na watu.
Kamanda Amata aliteremka ngazi na kutembea kwa hadhari pale upenuni kwenye maegesho ya hotele akiiendea gari yake, lakini ghafla alisikia mlio wa risasi nzito na bahasha aliyoishika mkononi mwake ikipigwa na kutoka mkononi mwake.

“Shabash,” alitamka, huku akiruka kiustadi kuliacha eneo lile na kufikia kwenye maua ambayo yalimkinga asionekane.
Kutoka juu ya ghorofa lile, Fasendy alitazama kwa mashine yake lakini hakumuona Amata zaidi ya watu wachache waliokuwa wametawanyika eneo lile.
“Uemuona alivyokuwa mwepesi?” Fasendy akamuuliza yule kijana ambaye alibaki katoa macho na darubini yake ikiwa inaning’inia kifuani mwake.
“Sasa kwa nini hukumuua, hivi unafikiri Sharon na Shalabah watatuelewa!” alilalamika yule kijana.
Fasendy hakujibu neno, alimtazama na kisha akainuka na kunyanyua bunduki yake, akasimama na kumtazama yule kijana, “Muda bado.”

JIDKA SODONKA
Kamanda Amata aliegesha gari kwenye moja ya majengo makubwa katika barabara hiyo kubwa, Jidka Sodonka. Moja kwa moja akaingia ndani ya jengo hilo na kukuta watu waliokuwa wakifanya usafi na katika vijia vya jengo hilo kulikuwa na makasha ya takataka mengi. Akaliendea mojawapo na akatumbukiza kitu kilicho kwenye mfuko wa plastiki kwenye moja ya kasha hizo, yeye mwenyewe akapita moja kwa moja na kuingia katika moja ya duka la nguo, aksimama katika mlingoti mmoja ulioning’inizwa nguo za kike, lakini jicho lake likawa makini kutazama katika kasha lile. Sekunde chache alimuona mzee wa makamo akipita karibu na lile kasha akiwa kavalia mavazi kama ya wale wanaofanya usafi, akachukua lile kasha na kuondoka nalo kuelekea mahali wanakomwaga taka hizo. Kamanda Amata akatoka mle dukani mara baada ya kuona lile kasha limerudishwa pale, alipolipita lilikuwa tupu, akaelekea nje ya jumba hilo lenye maduka mengi ndani yake. Akiwa ameketi katika gari yake, simu yake ikaingia ujumbe, akaitazama, akausoma na alipomaliza akawasha gari na kuondoka.

Kituo cha basi cha W Sheikh Abaadir, kilicho nje kidogo ya mji wa Mogadishu kilikuwa na watu wengi wakisubiri usafiri wakwenda sehemu mbalimbali. Kamanda Amata aliweka gari yake mbali kidogo na kituo hicho na kusogea kwa mwendo wa miguu. Katikati ya wasafiri kulikuwa na benchi lililokaliwa na watu kadhaa huku wengine wakiwa wamesimama kutokana na ufinyu wa eneo hilo. Alipokuwa akiliendea benchi hilo alitoa sigara mfukoni na kuiweka kinywani kisha akaibana sawia na midomo yake, akaanza kujipapasa kutafuta kiberiti asikione. Kati ya watu waliokaa katika benchi lile mmoja akawasaha kiberiti cha gesi na kunyanyuka, Kamanda Amata akamfuata mtu huyo mpaka katika moja ya gari nyingi zilizoegeshwa kituoni hapo

“Kamanda Amata,” yule mtu akaita kwa sauti tulivu.
“The Chamelleone,” Kamanda naye akajibu, kisha ile gari ikaondoka, na kutoka nje ya mji kabisa ikipita katikati ya jangwa nene lenye jua kali na vumbi.
Baada ya mwendo wa takribani saa moja ile gari iliegeshwa kwenye nyumba kuukuu iliyozungukwa na miti michache. Kamanda akatelemka na kuongozwa na yule mtu mpaka ndani ya sebule kubwa, hapo alimkuta mtu anayemfahamu fika, The Chamelleone alikuwa ameketi katika sura ileile aliyokuwa ameizoea tangu zamanai.
“Karibu Kamanda,” akamkaribisha.

“Asante sana, kila linalopita kwangu ni kama ndoto za alinacha,” Kamanda akasema.
“Inabidi iwe hivyo, maana leo hii asubuhi ulikuwa unauawa, na usingekikwepa kifo hicho, lakini umepona, una bahati,” Chamelleone akamwambia Amata. Kamanda Amata akamweleza juu ya tukio la asubuhi la kupigwa risasi bahasha iliyokuwa mkononi mwake. “Kamanda Amata, hawa jamaa hawatanii kabisa katika kuua, na sasa wamecharuka maana wamegundua ulilolifanya hivyo pale hotelini kwako sio salama tena na ningekushauri uhamie huku shamba,” Chamelleone alimwambia Amata. “Nakubaliana na hilo, lakini huku ni mbali sana, na mi nataka nikamilishe kazi hii mapema iwezekanavyo,” Kamanda akajibu.

“Usijali, kwanza kabla ya kuendelea kufanya kazi hii unatakiwa ufanye kazi moj ya ziada, umpate Jamir, kutoka kwake utapata jinsi ya kuimaliza hii kazi ndani ya dakika chache,” Chamelleon akamwambia Amata.
“Jamir! Bado yupo hai?” Kamanda akauliza.

“Jamir yupo hai, nitakuelekeza alipofichwa, ukiweza ukamtoe ili pamoja au vyovyote vile umalize sakata hili, nitafurahi sana kama utaimaliza hujuma hii na wahujumu wajulikane,” Chamelleone akamweleza Amata.
Kabla ya kuanza mazungumzo yale na Amata kwanza akawataka wale watu wake kutoka mle ndani ili abaki yeye na kijana wake tu. Hali ilipotulia alimtazama Kamanda usoni kisha akashusha uso wake mahala pake.
“Unahitaji kupumzika, macho yako yanaonesha wazi umechoka na una usingizi,” The Chamelleone akamwambia Amata, “…Utakapoamka ndipo utaianza kazi hii kwa umakini zaidi kwa sasa kutokana na uchovu wako hutokuwa makini, watakukamata,” almalizia.

Kamanda Amata akaitikia kwa kichwa na kutulia kochini, “Umepata mzigo?” akamwuliza.
“Ndiyo, nimeupata na baadaye nitauchunguza kuona kama ni sahihi au kuna mchezo mwingine uliochezwa katika hili, nakusubiri uamke ili tuone pamoja, (akamtazama Kamanda kwa makini) naona bado una maswali uliza tu,” Chamlleone alimwambia.
“Hapana sina swali, nahitaji kupumzika,”
“Ok, Kamanda.”
Yule mzee mtu mzima akanyanyuka kitini na kuiendea simu iliyopachikwa ukutani, akaipachua na kuminya tarakimu Fulani kisha akaiweka sikioni; akaongea maneno machache kwa lugha ya kiarabu na kisha kurejea kitini. Haikupita sekunde kumi mwanadada mrembo alitokea katika mlango mmoja kati ya mingi ya jumba lile, akiwa amevalia siketi ndefu iliyonyima nafasi japo vidole vya mguu kuonekana, kuyoka kiunoni kwenda juu alivalia sidiri inayowakawaka kwa vingaro vyake vya kupendeza huku akiwa na kiblauzi cha mtindo huohuo kisicho na vifungo mbele na nikifupi kiasi kwamba hakijafika kiunoni, kwa jinsi hiyo tumbo lake mwororo lilikuwa wazi na kuruhusu kitovu mbonyeo kuonekana wazi.

Moja kwa moja alikuja kwa Kamanda Amata na kumsalimu kwa adabu.
“Mfuate,” ilikuwa sauti nzito ya Chamelleone ikimwambia Kamanda, naye akanyanyuka na kumfuata yule mrembo aliyekuwa akitembea mwendo wa ki-paka ulioyafanya makalio yake madogo kuyumba huku na kule, bila shaka alikuwa miss, Kamanda alijiwazia kichwani mwake huku macho yake yakiburudika kwalo.

Chumba kikubwa kilimlaki Kamanda Amata, kitanda kikubwa chenye miguu mirefu, kitanda cha kisultani, aliendelea kuwaza.“Utapumzika hapa na kwa shida yoyote utapiga simu, namba zote zipo hapo, asante,” yule mrembo alimwambia Kamanda Amata.“We unaenda wapi, mi nilijua unabaki na mimi,” Kamanda akaanza uchokozi. Yule mwanadada akacheka na kutoka nje, lakini kabla hajaufunga mlango alimtazama Amata, “Namba za simu hizo hapo…” akamwambia kisha akaufunga mlango nyuma yake. Kamanda Amata akakitazama kile chumba kwa haraka haraka, akabonyeza itufe Fulani kwenye saa yake na kuigeuzia huku na kule aone kama kuna chochote kilichotegeshwa ndani humo hasa vinaa sauti na vitu vyenye madini ya milipuko. Usalama ulikuwa kwa 100%, akaufunga mlango na ufunguo kisha akajiandaa kujiswafi kabla ya mapumziko.

“Fasendy, umefanya nini? Tangu nimeanza kukupa kazi leo umenivuruga akili yangu,” aliongea kwa wahka bwana Shabalah, huku akimtazama mwanamke huyo aliyesimama kando kidogo ya mlango wa kijiofisi hicho ambacho daima hupenda kukutania kwa mipango yao. “Shalabah, sikufanya makusudi, wakati mimi nimemuweka kwenye shabaha mtu wangu, huyu Jeslaim akanigonga begani kuniambi kitu hivyo bunduki ikacheza nyuzi chache sana lakini kutokana na umbali wa mlengwa tayari ilikuwa ni Off-Target,” akajitetea. Jeslaim aliyekuwa pembeni kidogo akisikiliza juu ya matokeo ya umbea aliouleta, sasa alipambana na jicho kali la Shalabah, macho yakamtoka pima kwa woga, akajua wazi kuwa amekwishaingia matatizoni kwa swala ambalo si la kweli. “Msilete mchezo katika hi…” kabla hajamaliza kutoa onyo lake simu yake ya kiganjani ikaita kwa fujo, akainyakua na kuweka sikioni.
“Hello…” akaita na kuisubiri sauti ua uapnde wa pili kujibu.

“…aonekani pande zote za jiji? (…) ok, sasa hakikisheni mpo karibu na hiyo gari kwa maana lazima atarudi tu hata kama ni wiki ijayo.”
Shalabah akakata simu na kuipachika kwenye kibweta chake. Akawatazama wale watu wawili, mmoja baada ya mwingine. Kisha hakuwa na la kusema aliwataka kuondoka mara moja. Na dakika ileile Sharon aliingia mle ndani na kulete habari nyingine kwa Shalabah.

“Sikia, weka watu wawili chumbani mwake, kule kwenye gari weka kama wane hivi kisha wengine wawe tayari-tayari kwa amri yoyote ile, mkiona tu jicho lake mulitungue, Fasendy atasubiri tayari kwa amri utakayompa, mi naandaa kikao cha biashara kesho, jamaa wanakuja kununua yale makombora kesho na wataingia na meli yao hapa usiku wa manane wa kesho hiyohiyo, hakikisha pia ulinzi unaimarishwa baharini, weka doria kali yule majinuni asituharibie,” Shalabah akamaliza na kuketi kitini huku akifungua kile kitambaa cha kichwani na kukiweka juu ya meza, akashusha pumzi ndefu na kubaki akitazama ukuta usiyo na picha wala pambo lolote kama zezeta.

Dar es salaam
Gina binti Komba Zingazinga aliishusha miwani yake myeusi, bado alikuwa ameegemea gari yake upande wa mbele wa boneti, akihakikisha hampotezi mtu huyo ambaye ni windo analolifuatilia siku ya pili sasa. Alimtazama akiwa ametoka katika hoteli ya Kilimanjaro na kuingia kwenye gari maalumu la kupelekea wageni uwanja wa ndege. Naye bila ajizi akajitoma ndani ya gari yake na kuiwasha kisha akaitoa kuifuata ile gari ya hoteli iliyombeba yule bwana.
Kama kawaida ya jiji la Dar es salaam, jumapili hiyo barabara zilikuwa nyeupe kabisa, gari zilikuwa ni chache sana, hivyo haikuwapa taabu kuufikia uwanja wa ndege wa Julius Kambarage Nyerere kule pande za Ukonga. Kati ya gari yake na ile ya hoteli kulikuwa na kama gari nne katikati lakini walipofika pale kwenye kona ya kuingia uwanjani ni yeye alikuwa wa kwanza kuitoa kushoto kidogo gari yake na kuwasha indiketa, hivyo hivyo sekunde chache baadaye na ile gari ya hoteli ikafanya hivyo na kuanza kukunja kona kuingia uwanja wa ndege.

Alishuka na kuufunga mlango wa gari yake, akaipachika tena ile miwani usoni pake na kuvuata hatua za madaha, hatua za mwanamke mrembo kuelekea katika jengo kubwa la uwanja ule, hakuonesha dalili za kumfuatilia mtu wala lolote lile, alionekana kuwa kivyake, moja kwa moja akaufuata mlango wa kuingilia abiria, mlango ambao yule bwana alipita pale muda si mrefu, Gina akasimama mbele ya mwanadada mmoja mrembo aliyejipaka rangi yam domo kama kachinja njiwa kwa meno. Akamsalimi na kumtupia swal, “Umemuona yule bwana mwenye suti ya kijivu?” akamwuliza yule mhudumu. Yule mhudumu akajibu kwa kutikisa kichwa, “Niambie anakwenda wapi sasa hivi?”

“Kwa nini unauliza, mi sio kazi yangu kutoa habari za wasafiri nenda paleeeee ofisi ya Maelezo,” yule mhudumu alijibu huku akimuonesha kwa kidole ofisi ndogo ilioandikwa kwa Kimombo na Kiswahili, Information/Maelezo.
“Sikiliza mrembo,” Gina alianza lugha ya ulaghai, “Nisaidie mwanamke mwenzio, yule mzee ni m’me wangu, kaniaga anaenda Nairobi kikazi sasa mi nataka nijue maana kila wakati ananidanganya”. Gina alisema hayo huku mezani kwa mhudumu huyo kukiwa na noti ya shilingi elfu kumi, yule mhudumu alimtazama na kucheka, ndoa zina mambo, ndo maana sitaki kuolewa, yule mhudumu alijisemea kwa sauti ya kujisikia mwenyewe.
“Anakwenda Mtwara na ndege ya saa 4.30 asubuhi hii,” akajibiwa. Gina akatikisa kichwa juu-chini kuashiri kaelewa.
“Na kurudi lini?” akaongeza swali.

“Leo hii hii jioni, ndege ya saa 12.00,” akajibiwa Gina akafurah9i moyoni, akaaga na kutoka nje, moja kwa moja akaenda na kusimama mbele ya luninga kubwa iliyokuwa ikionesha ratiba ya ndege zinazoondoka. Air Tanzania - TC 206 saa 4.30 as- Dar – Mtr, aliisoma ile ratiba na kuitazama saa yake ilikuwa imebaki dakika sabini na tano hivi ile ndege iondoke, akasogea mahali ambapo hakuna watu akaiinua saa yake ya mkononi na kubofya kitufe fulani, “Mission Mtwara,” akatamka maneno hayo huku akitazama ile saa.

Sekunde chache baadaye saa yake ikamfinya kwa upande wa chini, akaitazama ilikuwa ikiwaka-waka kijimwanga cha kijani, aliitazama na kubofya mahala fulani, ile saa ikatoa kijimkanda chenye maandishi katika moja upande wake, Gina akakavuta na kukasoma. Bon Voyage aliyasoma maneno hayo ya Kifaransa yaliyomtakia safari njema, tayari alielewa kuwa anatakiwa aende Mtwara muda huo bila kuchelewa. Kwa hatua za haraka, alikimbilia kwenye ofisi moja ya Air Tanzania na kuingia ndani. “Samahani dada, ninahitaji tiketi ya sasa hivi nakwenda Mtwara,” Gina alieleza.
“Ndege imejaa,” akajibiwa.

“Hata kama, ni bora abaki rubani mimi niondoke,” Giana akasisitiza. Yule mwanadada aliyevalia nguo nadhifu, sketi nyeusi na blauzi ya rangi ya machungwa ilipachikwa na kitambaa shingoni mwake kikining’inia kwa nyuma, aliinua uso wake wa duara na kumtazama Gina, Mtazame vile, ka’ katumwa, alijiwazia na kisha akasimama mbele ya Gina kati yao wakitengwa na meza kubwa yenye fomeka safi juu yake, akamsogezea sura yake Gina kama anamshushua kitu, “Ndege imejaa mdada, umeelewa?”

“Hata kama imejaa, lazima niende, uwe na lugha ya kistaarabu kwa wateja,” Gina alaing’aka na kufungua pochi yake, akatoa kikadi maalum na kumpa, yule mwanadada alikipokea na kukigeuza-geuza, hakuamini. Ilikuwa kadi maalumu inayomtaka ampa usafiri wakati wowote bila gaharama ya yoyote bila swali lolote, usafiri wa kwenda popote ndani ya ardhi ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Yule dada akagwaya, akajirudisha kitini kama aliyesukumwa na mtu, akabonya kompyuta yake na kuingiza tarakimu Fulani ndani yake, kisha akampa ile kadi Gina.
“Na ya kurudi mrembo, ndege ya saa kumi na mbili jioni,” Gina akaongezea kumwambia kwa nyodo ilhali akijua wazi kuwa anamkera mwanadada huyo. Dakika mbili alikuwa na tiketi mkononi, akaondoka zake.

UWANJA WA NDEGE – MTWARA
SAA 5.15 asubuhi walishuka katika uwanja wa ndege wa Mwara, jua lilikuwa likiwaka kwelikweli, joto la mvuke wa bahari lilikuwa likihisika bila kificho. gina alimtazama yule bwana ambaye alitoka na mkoba wake na kuiendea meza ya ukaguzi na wakati huohuo Gina aliifikia meza hiyo. Kabla hajauliza chochote alijifanya kuinama kuweka vizuri kiatu chake na wakati huohuo akabandika kidubwasha kidogo kwenye mkoba wa bwana huyo ambao ulikuwa chini sakafuni.
“Samahani dada, naweza pata tax hapo nje?” Gina aliuliza na kupewa jibu. Akatoka nje na kutazama, kweli, tax kadhaa zilikuwa eneo lile, akaichagua moja na kuingia kiti cha nyuma.

“Wapi uelekeo dada?” akauliza dereva tax kwa lafudhi ya Kimakonde ambayo haikujificha kabisa ukijumlisha na chale alizokuwa nazo usoni mwake, hivi hawa watu bado wapo! Alishangaa peke yake, “Tulia nitakwambia,” akamjibu.
Dakika kama tano baadae yule bwana alitoka na kuingia kwenye Range Rover moja iliyokuwa ikimsubiri. Muda huohuo Gina akachomoa kidubwasha kidogo cha kupachika sikioni chenye mfano wa kile kifaa atumiacho Kiziwi katika kunasa mawimbi ya sauti (shine sikio au audiometer) na kukipachika sikioni mwake. Kila mtu aliyemuona alijua binti huyo mrembo ni kiziwi kumbe la, kutoka katika kile kifaa aliweza kusikia mazungumzo yote ya ndani ya gari alilopanda yule bwana.

“Ok, twende, nipeleke Makonde Hotel,” Gina alimwambia yule dereva na kisha wakaondoka eneo lile, “Usikimbie sana kuna ndugu zangu kwenye gari ile sasa usikae mbali nao,” alimwambia yule dereva na safari ikaendelea.

HOTELI Makonde, ni hoteli safi nay a kisasa iliyojengwa pembezoni kabisa mwa fukwe ya Shangani. Watu wengi walipenda kwenda kupumzika katika hoteli hiyo iliyokuwa ikisifiwa kwa utulivu, huduma na usafi wa hali ya juu. Hoteli hiyo iliyokuiwa ikimilikiwa na kijana wa Kimakonde kutoka Mtwara ilikuwa ni hoteli inayovuma sana katika ukanda wa pwani ya Afika Mashariki. Vigogo na matajiri mbalimbali hupenda kwenda kupumzika katika hoteli hiyo kila mwisho wa juma.

Bw. Goloko Mikidadi, mtu wa makamo aliyewahi kuwa kigogo wa serikali ya awamu ya kwanza alikuwa ameketi katika moja ya viti vya kiutamaduni vilivyokuwapo katika ukumbi mkubwa wa hoteli hiyo. Meza iliyotakiwa kuwa mbele yake ambayo kwa sasa ilikuwa kushoto kwake ilibeba chupa kubwa la John Walker na kibweta kilichojaa vibonge vya barafu. Bilauri yenye kiuno ilitulia na kinywaji hicho ndani yake kikisubiriwa kumiminiwa katika tumbo la binadamu huyo. Ni siku nyingi sana alikuwa hajafika katika mkoa ule wa Mtwara, mkoa ulio katika miisho ya nchi, upande wa Mashariki ya Kusini. Alikuwa akiingalia saa yake iliyokuwa ikimuonesha kuwa ni saa tano ikikimbilia kuwa na dakika kumi na tano hivi. Gari iliyokuwa imemleta pale ilikwishaondoka kitambo kuendelea na shughuli nyingine. Aliinua ile bilauri na kuipachika kati ya midomo yake na kuibinua kwa mkono wake wa kuume kwa madaa mazito, maisha si ndiyo haya, alijiwazia pindi akiiteremsha mezani ikiwa tupu.

Kutoka mbali, aliiona boti iliyokuwa ikija kasi sana, kwa kuwa yeye alikuwa amegeukia upande wa bahari; aliweza kuiona bila tabu boti ile iliyokuwa ikija kwenye fukwe ya Shangani. Yule bwana alikenua kidogo kisha akafunga kinywa chake, kama ungekuwa jirani naye basi ungejua kuwa ana tatizo la kiakili, lakini haikuwa hivyo bali alikuwa akimfurahia mtu aliyetakiwa kukutana naye siku hiyo. Ile boti ilifika mpaka katika gati ndogo pale Shangani ambayo hutumika na watu wa michezo ya yacht, nahodha wake akaifunga kamba na kupeana mikono ya asante na yule bwana aliyemteremsha katika boti ile. Alikuwa mnene kiasi, mwenye ngozi ya kizungu iliyopigwa jua la kutosha lililoifanya sasa ionekane kama Mhindi mwekundu, alivaa jeans aina ya Lee na raba matata sana huku kichwani akijifunika kwa pama kubwa lililopambwa na picha ya wanyama wakubwa watano wanaopatikana Tanzania. Alivuta hatua na kuvuka kwa hadhari sana ile barabara iliyokuwa ikikatisha mbele yake. Akazikwea ngazi na kufika ghorofa ya kwanza, ghorofa iliyotengenezwa kwa miti na mbao ngumu.

“Karibu Komredi, nimekuwa nikikusubiri kwa hamu sana,” Bwana Goloko Mikidadi alisimama na kumpa mkono wa karibu yule mwenyeji wake.
“Naitwa Mr. Reubellen Vinchinsk,” akajitambulisha.
“Naitwa Bwana Goloko Mikidadi,” naye akajitambulisha.
Kisha wawili hao wakaketi chini kwa mtindo wa kutazamana. Bwana Goloko akavuta mkoba wake na kuufungua kisha akatoa, akatoa kabrasha moja jembamba na kuliweka mezani. Reubellen Vinchinsk akavuta lile kabrasha na kupitisha macho kisha akaingiza mkono katika mfuko wake wa shati na kuchukua peni, akaweka saini mahala Fulani kisha akamrudishia yule bwana naye akaweka saini mahala pengine, wakagawana kila mmoja nakala yake, kisha wakapeana mikono.

Nukta hiyohiyo mhudumu alifika na kuleta vibonge vya barafu vingine pamoja na bilauri ya pili kisha akammininia kinywaji na kuondoka. Wale mabwana wawili waliinua bilauri zao na kugonga cheers, kisha wote wakajimiminia vinywaji hivyo matumboni mwao mpaka vikaisha ndipo wakashusha chini zile bilauri.
“Bwana Goloko, siamini kabisa kama huu mpango umekuwa sawa, kwa jinsi nilivyokuwa napewa taarifa za mambo mengi yaliyotukia huko nyuma juu ya hili, lakini sasa ndiyo naamini kwamba limewezekana,” Reubellen Vinchinsk alimwambia Bw. Goloko.

“Ni kweli, ni mambo mengi sana yametukia, watu wamepoteza maisha katika mkataba ishu hii, watu wameuana hapa kaka, fikiria mkakati ulianza tangu mwaka 1975, ukaleta tabu na katikati ukasimamishwa kwanza, Mwalimu Nyerere alikuwa mkali sana, kila aliyejaribu kufanya blaa blaa ama alitimuliwa kazi, alifungwa maisha na wapo walionyongwa. Kipindi kile mimi nilikuwa katibu wa wizara nyeti ya Maji Nishati na Madini, nilitimuliwa ofisini kama mbwa, ikabidi tukae chini na wadau kuona mbaya wetu ni nani, tulipomgundua, tukamfutilia mbali,” Bwana Goloko akamwambia yule Mzungu koko.

“Aisee, (akamwinamia) mlimuua?” akauliza yule mzungu
“Sasa tufanye nini komredi? Tulimuua ni muda mrefu sasa hata tumemsahau.”
“Alikuwa kitengo gani hapa au serikalini?”
“Yule bwana alikuwa idara ya uchunguzi, lakini kumbe tuligundua kuwa ni afisa wa ngazi ya juu wa usalama wa Taifa hapa Tanzania, na ndiye alikuwa akitoa taarifa Ikulu moja kwa moja, hatukuona haja ya kumuacha, tulimuua dakika chache akitoka kwenye mkutano wake na Mwalimu Nyerere pale Chamwino njia panda,” Goloko alibwabwaja.
“Mlifanya la maana sana komredi, watu kama hao ni kuwafanyia hivyohivyo tu,” yule mzungu akamwambia kisha wakaendelea kunywa.

“Ok, tuyaache hayo, sasa mkakati wa leo unakuwaje?” yule mzungu aliuliza.
“Usiku wa leo naondoka, naelekea Mogadishu, pale tutakuwa na kikao cha mauziano ya ule mzigo kisha kamisheni za kila mmoja zitafanyika baada ya kikao hicho,” Goloko alisema.
“Nategemea akaunti zitacheka soon.”
“Masaa ishirini na nne tu komredi utatajirika kwa kazi uliyoifanya…” kabla hajamaliza kusema wote wakaangua kucheka.
Bw. Goloko Mikidadi akaitazama saa yake tayari ilikuwa imetimu saa nane za mchana, akaagana na mwenyeji wake kisha kila mtu akachukua hamsini zake.

Wakati wawili hao wakiongelea juu ya ule mkakati mzito na ulipofikia, Gina alikuwa ndani ya chumba kidogo alichopanga katika lodge moja iliyokuwa mkabala na hoteli hiyo, aliweza kusikiliza mazungumzo yote huku akirekodi katika kimashine chake kidogo. Alipojiridhisha na alichokipata, alifunga vifaa vyake na kutia mkobani, hakuona haja ya kupoteza pale, alichokitaka sasa ni kumfuatilia yule mzungu ili amjue ni nani na anatoka wapi, alifunga mlango nyuma yake na kuteremka ngazi kumuwahi yule mtu. Alipofika chini alipita kwenye ujuia mdogo na kutokea nyuma ya lodge ile, eneo ambalo lilionekana kuwa ni sehemu ya kufulia nguo, aliruka ukuta mfupi na kutua kwa nje ambako moja kwa moja unaelekea baharini, akavuta hatua ndogondogo na kutokea upande wa kushoto wa lodge hiyo; akachukua ujia na kuufuata taratibu kisha akateremka na barabar ya vumbi iliyokuwa ikielekea baharini. Alipofika jirani kabisa na ile yacht club, akatulia na kumtazama yule bwana mzungu akiwa analipia ile boti yake kisha akaingia na wale viajana wake wakaliwasha na kuliingiza majini, Gina aliinua camera yake ndogo lakini yenya nguvu sana na kupiga picha boti ile. Hakuona haja ya kumfuatilia kwani alichokitaka alikwishakipata.

MADAM S alimtazama Gina pale alipoketi usiku wa siku ile, “Una uhakika?” akamwuliza.
Asilimia 100, mimi ndiye nilikwenda Mtwara, yule ni Bw. Goloko mwenyewe na mazungumzo yao ninayo kwenye mashine.
“Unasema?” Madama aliuliza kama mtu aliyeshtuliwa.
“Mazungumzo yao ninayo katika masine yangu,” Gina akajibu tena. Kisha akaufungua mkoba wake na kutoa ile mashine akampa Madam S. Madam S akasikiliza mazungumzo yote ya wawili wale, akitazama sss yake ilikuwa tayari ni saa tatu usiku.

“Kama vipi mi’ naona tu n’naona tungemkamata usiku huu,” Gina alishauri.
“Hapana, muache aende ili tumkamate na kidhibiti,” Madam S alijibu, “Asante Gina, naona sasa umeanza kukomaa taratibu, kaa tayari ukihitajika msaada huko Somalia ujue hiyo ni nafasi yako na hakuna mwingine.”
Gina aliitikia kwa kichwa alipokuwa akiinuka tayari kwa kuaga na kuondoka, kabla hajaufikia mlango alisikia Madam akiita, “Gina!” akageuka na kuitika “Yes Madam,”… “uwe muangalifu sasa.”

Kamanda Amata alifumbua macho na kurudiwa na fahamu zake, aliliendea dirisha na kuvuta pazia kando, kigiza kilikuwa tayari kimelivamia anga na kuruhusu nyota nzuri kulipamba anga lile, akameza funda la mate na kuliachia lile pazia kurudi mahala pake. Kwa hatua fupi fupi akakifikia kitanda na kujitupa juu yake, mawazo yalifudikiza fikra zake, aliwaza na kuwazua akapanga na kupangua. Akajaribu kutathmini mpaka hapo alipofikia amefikia wapi, akajisifu kwa ushujaa wake mwenyewe lakini bado aliumiza kichwa jinsi ya bkumaliza na kupata kile alichotumwa na serikali yake, akajiinua tena na kulivamia bafu, akaoga kwa muda mrefu huku akifikiri la kufanya.

Alipohakikisha kuwa yupo tayari kwa kazi usiku ule ambao kichwa chake kiliupa jina usiku wa kazi aliinua simu na kupiga namba Fulani na haikuchukua muda mlango ule ukafunguliwa na binti yuleyule akaingian na kuufunga nyuma yake. Alimkuta Kamanda Amata amekwishajiweka tayari ndani ya kadeti nyeusi, viatu vyeusi vyenye soli ya mpira isiyofanya kelele, fulana nyeusi iliyomshika mpaka kwenye koo, kaba shingo yenye mikono mirefu. Tayari alikuwa amekwishapanga kila kinachohitajika mwilini mwake kama silaha na bastola yake aliyopewa na Chiba ilikuwa tayari upande wake wa kuume wa kiuno.
“Waaaaooohhh!” yule binti alihamaki huku akimsogelea Kamanda Amata pale aliposimama, kwa kutumia vidole vyake laini alitomasatomasa kifua cha Amata kilichoonekana kujaa vizuri kimazoezi, Amata akaushika mkono wake na kuushusha chini.

“Nipeleke sebuleni,” alimwamuru yule mrembo naye akatii, akaongoza na kumtoa Amata mpaka sebuleni ambako alimkuta Chamelleone akiwa ameketi akitazama luninga kubwa iliyo mbele yake.
“Naona Kamanda wangu uko tayari,” Chamelleone alimwambia Kamanda Amata huku akijiweka vizuri kitini, “Pata kinywaji kidogo kikuchangamshe mwili, najua mpiganaji hatakiwi kulakula ovyo,” wote wakacheka. Kamanda Amata akainua glass na kugonga cheers, na mzee yule kisha akabugia pombe yote kwa funda moja tu.
“Asante sana mzee, mimi naona niingie town nina mambo ya kukamilisha na kisha nitakujuza kinachoendelea, kuhusu hilo linguine tufanye wakati mwingine,” kamanda alitoa shukrani nna wakati huo alikuwa akiuendea mlango wa mbele wa nyumba hiyo. Gari ile ile iliyomleta ilikuwa ikimsubiri nje, akaingia na kurudi mjini.
CHANZO : Deusdedit Mahunda

Vijana watatu waliokuwa jirani kabisa na gari ya Amata pale katika kituo cha mabasi cha W Sheikh Abaadir walikuwa wameanza kukata tama ya kumnasa mmiliki wa gari hilo. Walikuwa wakibadilisha aina za mikao au misimamo wakingoja na kungoja tangu mchana wa siku hiyo.
Kule hotelini nako vijana waliowekwa kuizingira hoteli ile, walingoja bila mafanikio, kila walipojaribu kufanya mawasiliano huku na kule mtu nhuyo hakuonekana kabisa katika viunga vya jiji la Mogadishu, iliwasumbua akili, walihaha.
“Sasa atakuwa kajificha wapi hayawani huyu?” Sharon alijiuliza kwa sauti ya chini huku akiyupa nje ya gari kichungi cha sigara iliyokwisha, akasonya kwa hasira. Fasendy mwanamke pekee aliyekuwa juu ya landcruiser hiyo yenye mtutu mkubwa wenye nguvu alitulia palepale akicheza gemu katika simu yake. Mpaka giza lilipokuwa likiingia hawakumuona Kamanda Amata wanayemsubiri wala kivuli chake, kila mmoja akakata tamaa. Mara redio iliyokuwa mkononi mwa Sharon ikakoroma kuashiria kuna taarifa mpya inayotaka kuingia muda huo.
“Sharon, usiku wa leo tuna wageni wengi uwanja wa ndege, naomba uchague vijana watano wazuri katika usalama uwaweke pale, wakiongozwa na wewe mwenyewe, msako wa huyo Hayawani muachie Fasendy, na vijana wengine wanakuja kushika nafasi za hao watano,” ilimaliza sauti ya Shalaba.

Baada ya kuliacha gari alilokuwa amepanda kama mita mia tano hivi mtaa wa pili nyuma ya kile kituo cha mabasi, Amata alipita kwenye vibaraza vya maduka na kutokea nkwenye barabara kubwa inayoelekea katika kituo kile. Alisimama mbele ya duka kubwa la vyombo akitazama huku na kule, alijua kwa vyovyote vile lazima wamuwekee mtego katika gari lake, hivyuo aliamua kuwacheza shere, alikodi tax na moja kwa moja akaelekea hotelini kwake.
Mbele ya hoteli ile alijaribu kusoma sura za watu na akagundua kuwa kuna sura ambazo hawezi kuziamini hata kidogo, aliamua kuwabadilishia mchezo. Ilikuwa lzima afike katika chumba chake kwani kuna dokumenti alizokuwa akizihitaji kwa usiku huo. Akazunguka nyuma ya hoteli na kuichunguza akagundua kuna mlango wa kutokea upande huo wa nyuma, akajaribu kuutikisa akakuta umefungwa, akatulia kimya kufikiri mara mbili la kufanya. Nukta hiyohiyo akasikia sauti za watu wanaoongea wakija upande wa nyuma wa hoteli ile, akajibana katikati ya mabomba mawili ya uchafu, yanayotiririsha majitaka toka juu kuleta chini. Walikuwa ni walinzi wa hoteli hiyo, walipompita aliamua kukwea kupitia yale mabomba. Chumba chake hakikuwa juu sana ilikuwa ni ghorofa ya tatu tu, hivyo haikumchukua muda kwa mtu kama yeye kufika usawa wa chumba chake, pale kulikuwa na kaukuta kalikojitokeza ambako kalikuwa kamebeba ndoo kadhaa za maua, akakanyaga kwa uangalifu kabisa asije kudondosha hata moja, alipohakikisha kuwa yuko usawa wa dirisha la chumba chake akalitikisa kidogo na lenyewe likatii amri, taratibu akaingia kupitia dirisha hilo kubwa lililoundwa kwa aluminiam safi, akatua ndani ya chumba hicho kwa madaha bila kufanya kelele yoyote kwani alijua kuwa lazima wapo wengine walio ndani.

Akakiendea kitanda chake na kukibonyezabonyeza, kilikuwa kimetulia kama kilivyo. Kamanda Amata akalisogelea kabati kubwa la nguo. Akashika kitasa cha mlango huo tayari kuuvuta lakini kengele za hatari kichwani mwake ziligonga, akajiandaa, kisha akavuta kwa nguvu ule mlango. Hakuwa tofauti na hisia zake, alipofuangua mlango tu, mtu mmoja aliyekuwa amejificha ndani ya kabati hilo alijitokeza kwa minajiri ya kumpamia Kamanda Amata, lo, Kamanda alipoufungua ule mlango tayari alikuwa kajiweka kando hivyo yule mtu akapitiliza peke yake na kumpita Amata ambaye alinyanyua mguu na kumpiga ngwala maridadi iliyomfanya mtu yule atue kwa uso katika sakafu na kuvunja mwamba wa pua. Kabla hajajigeuza, mguu mzito ulitua nyuma ya shingo yake na kumfanya mtu huyo kugugumia kwa maumivu. Amata akamwinamia palepale alipo na kumtazama mtu yule ambaye alikuwa chini, damu zikimvuja puani huku akilia kwa uchungu, lakini hakuweza hata kujigeuza kutokana na uzito wa guu la Amata.
“Wenzako wako wapi?” Kamanda alimuuliza.

“Niko pe-pe-ke ya-ngu,” alijibu kwa shida huku akijaribu kujiinua, lakini hakuweza kufanya hivyo.
“Unanitania sio?” Kamanda aliuliza na kumkanyaga kwa nguvu, yule mjinga pale chini alianza kutupatupa miguu na mikono kwa kutafuta pumzi.
“Ni-niiii-takwa-mbi-i-a,” alijibu. Kamanda Amata akalegeza mguu kidogo.
“Haya sema,”
“Wa-po nje,” akajibu.
“Wangapi?” Kamanada akahoji.
“Si- si… unaniumiza bwana,” yule mtu akashindwa kutoa jibu na badala yake akamtamkia maneno hayo Kamanda.
“Niambie, yule komandoo na wale wengine mmewaweka wapi?” akauliza tena.
“Si si – sijui mi-mi,” akajibu.

Muda huohuo saa ya Kamanda Amatav ikaanza kumfinya kwa fujo kuashiria kuna ujumbe ulikuwa ukiingi. Ni nafasi hiyohiyo ambayo yule mjinga pale chini aliitumia, alijigeuza kwa nguvu na kuwa chali akitaka sasa kusimama, teke moja kali nla Amata lilikuwa likienda kupiga korodani, yule bwana akaipanga mikono yake kwa mtindo wa x na kuchanua viganja vyake chini kidogo ya kiuno chake kusha akabonyea kufanya kama anachuchumaa, teka la Amata halikuwa pata lilipokusudiwa bali lilikingwa kwa hiyo mikono kwa usatdi kabisa.

Kamanda Amata akaona akile ta mchezo hapo kazi itakuwa ngumu, wakati yule jamaa akiushusha mguu wa Amata chini mara tu baada ya kulipangua lile pigo kwa akili zote, kamanda Amata alishusha kichwa cha nguvu na katika paji ola uso la yule mjinga. Nyota zilimzunguka maana aliona kama kadondoshewa tofali, alipepesuka na kujibwaga kitandani, akajisjika pale alipopigwa kama kumepasuka lakini alishuhudia nundu lililojitokeza bila hata kushauriwa. Yule mjinga kutoka pale kitandani alijirusha kinyumenyume sarakasi inayoitwa ‘back’, akatua upande wa pili na wakati huohuo alichomoa visu viwili na kuvirusha kwa umahiri kumwelekea Amata ambaye aliviona na kujitupa chini sakafuni na kuruhusu visu vile kukutana na ukuta. Kama ni kosa yule mjinga alilifanya hapo, alirukia kitandani ili atue upande wa pili ambapo alijua Kamanda Amata yuko chini, na Kamanda Amata alikwishajua nini yule bwana atafanya baada ya yeye kujitupa chini, na ndivyo ilivyokua, yule bwana alikanyaga kitanda na kujirusha upande wa pili, kabla hajafika chini, Kamanda Amata alirusha teke kali la na kiatu chake upande wa mbele kikapiga kwenye pingili za mwisho za uti wa mgongo ‘sacrum’ karibu na nyonga, yule bwana akajikuta kama anaishiwa nguvu za miguu, alijibamiza ukutani na kujibwaga chini kiama gunia, marehemu.

Kamanda Amata akasonya na kuiweka saa yake vizuri, kisha katika lile kabati akachukua kijitabu kidogo kutoka katika vitu vya Marehemu Gwamaka, akatia mfukoni, akajiongezea na vikolokolo vichache katika mifuko yake ya akiba, kisha akatoka kwa jinsi ileile aliyoingilia. Walinzi waliowekwa doria upande wa chini, walikuwa bado wakizungukazunguka kutafuta wapi windo lao litatokea, labda hapa au pale lakini walikuta usiku unazidi kuwa mwingi na hakuna dalili za windo hilo kurudi.

Kiongozi wa kundi lile lililokuwa likiweka doria chini ya hoteli hiyo aliinua simu yake ya upepo na kupiga kwa mtu ambaye alimuweka ndani ya chumba cha hoteli ili kutoa taarifa pindi tu windo lao litakapofika. Simu iliita na kuita lakini hakuna jibu lolote.

“Hamsud, huyu jamaa mbona hapokei simu, hebu panda juu umwangalie,” akatoa maagizo kwa kijana mwingine. Yule aliyeagizwa akaweka pembeni bunduki yake na kutwaa bastola moja na kuipachika kiunoni, akashuka garini na kuzijongea ngazi za jengo hilo. Sekunde chache tu aliufikia mlango wa chumba kile, akagonga na kugonga lakini hakuna jibu lolote. Akatoa funguo Malaya, akajaribu kuufungua ule mlango, ukafunguka, lo, hakuamini alichokiona, alitazama mwili wa swahibaye uliokuwa umelala bila uhai.

“Shiiiiiiittttt!!!!” akang’aka kwa hasira, akarudisha mlango na kuufunga kama ulivyokuwa. Kisha kwa hatua fupifupi kama za mtu aliyelewa, Hamsud alijivuta na kuteremka chini.
“Vipi?” yule kiongozi alimuuliza.
“Hakuna mtu, amekufa,” Hamsud akajibu.

“What?” yule kiongozi alijishika kichwa kwa mshangao, akawa anazungukazunguka huku na kule. Akampiga kijikofi Hamsud na kuelekea naye ndani, walifika katika chumba na kutazama maafa waliyoyakuta. Yule kiongozi akaugeuza ule mwili wa yule marehemu. Akatikisa kichwa, na mikono yake akaiweka kiunoni mwake. Ametuzidi kete mwanaharamu huyu, yule kiongozi alijiwazia. Wakapekua makabati na kukuta peupe, Kamanda Amata aliondoka na kila kitu chake mle chumbani, kwa ujumla alihama, lakini hakuna aliye Shabalah alishusha simu masikioni mwake akiwa amefura kwa hasira, alitamani amuone huyo mtu anyeitwa Amata ili amtafune kama ikibidi. Kama kuna kitu kilichomuuzi sana ni kitendo cha mtu wake kuuawa ndani ya hoteli pasina muuaji kuonekana. Shalabah alichanganyikiwa, akainua simu yake na kuwapa taarifa wengine wote ili kukomaza doria usiku huo, wakiwa wamepewa amri ya kuhakikisha Amata anapatikana ama mfu au hai.

Kituo cha mabasi cha W Sheikh Abaadir
KAMANDA Amata akatulia kwenye kona moja ya jengo lililokuwa na watu wengi, kila akitazama saa yake alikuwa akiona muda unamkimbia na wakati huo alikuwa akilitaka gari lake, alijua wazi kuwa kwa vyovyote wapo wanaomtega katika eneo hilo. Kamanda Amata aliamua la kuamua, akajivuta taratibu mpaka kwenye gari yake akainua mkono na kuitazama saa yake, akaizungusha kwa namna ya pekee kidogo, lengo ilikuwa ni kutazama kama kuna kitu chochote cha hatari ambacho kimetegwa katika gari hilo, alipoona kuna usalama, akafungua buti ili kuweka mabegi yake, lo, alijikuta akitazamana na mtutu wa shot gun, uso kwa uso, Kamanda Amata akamtazama mtu huyo aliyekuwa amelala ndani ya buti lile.

“Tumekukamata sasa, mshenzi wewe, umeshatuulia wenzetu wengi tu lakini leo hii ni zamu yako,” sauti ilitoka nyuma yake, alipogeuka tu alijikuta akikutana na konde zito lililotua shavuni mwake, hakuyumba, alisimama kidete akimtazama huyo aliyepiga konde hilo, Amata akajifuta pale lilipotua konde hilo. Wale waliofuatana na mtu huyo wakacheka kwa kitendo kile, Amata alichukizwa sana kwa hilo aliona kama anazihakiwa.
“Mpekue…” amri ilitoka.

Kamanda akapekuliwa na wakatoa bastola yake iliyokuwa kwenye kikoba maalumu.
“Yuko safi,” akajibu yule aliyekuwa akimpekua huku akimkabidhi yule kiongozi wao ile bastola. Kisha Kamanda Amata akafungwa pingu na kuingizwa kwenye land cruiser iliyofika wakati huo, kisha mmoja wale maharamia akatakiwa kuiendesha ile gari ya Amata. Kamanda Amata akawapatia rimoti kwa ajili ya kuendeshea gari ile, gari iliyokuwa ikitumia rimoti tu.

“Lala chini, unaangalia nini?” mtu mwingine alimuamuru Amata huku akimpiga na teke moja kali la usoni ambalo lilimpeleka chini, kisha wale jamaa wakasimama juu yake. Ile land cruiser ikawashwa.
Mbala mwezi ilizidi kung’aa katika anga la Mogadishu, wakati ile land cruiser ikiondoka na kutimua vumbi ikiwaacha yule kiongozi wa kikosi na yule jamaa aliyetakiwa kuiendesha ile gari ya Kamnda Amata. Wakiwa njiani kuelea chimbo, simu ya upepo ya mmoja wa askari aliyekuwa katika ile landcruiser iliita, akaichomoa na kubofya kitu Fulani kisha akajiruhusu kuongea.

“Sierra 1, Sierra 1,” aliitikia ile simu.
“Geuza gari mrudi hapa mara moja,” ilikuwa sauti ya kiongozi wa kikosi aliyebaki kwenye gari ya Kamanda. Ile Cruiser ilipiga norinda na kurudi ilikotoka.
Kamanda Amata akiwa ndani ya ile cruiser huku watu watatu wamesimama kwa kumnyaga mgongoni, alijua wazi kuwa tayari gari imewashinda kuwasha, alipiga akili kujua nini anatakiwa afanye ili aweze kutoroka katika mikono ya hao maharamia.

“We mbwa! Usitufanye sisi mabwege unasikia wewe!” alikoroma kwa hasira yule kiongozi, “Haya utuambie hii rimoti yako unaitumiaje?” akauliza. Kamanda Amata alimwangalia tu hakumjibu, akatema mate chini yaliyochanganyika na damu, akajiinua kwa tabu kutoka pale alipolala na kukaa kitako, akawapa ishara ya kuomba apewe ile rimoti. Yule kiongozi alikataa na kumtaka amwelekeze kutoka pale alipo, Kamanda Amata kakohoa kidogo.
“Nobu nyekundu mara mbili kisha ya kijani mara tu, tofauti ya mbonyezo ni sekunde mbili kwa kila kibonyezo,” akatoa maelekezo na kutulia akiangalia kitakachoendelea.

“N-n-nobu nyekundu,” akawa akibonyeza huku akirudia maneno ya Kamanda jinsi ya kuitumia rimoti ile, alipofika kwenye nobu ya kijani na kukibonya kisha akasubiri sekunde mbili ili akamilishe muamala.Na hapo ndipo alipoikuwa akisubiri Kamanda Amata. Mara tu alipobonyeza, sauti kali za bunduki kubwa, nzito ilisikika katika mtindo wa burst, zile kelele zikawafanya wale jamaa wachanganyikiwe wakijua wazi kuwa wamevamiwa.

Wakiwa katika kushangaa kwa taharuki wengine wakilala chini kujikinga na adha hiyo, kamnada Amata aliinuka kutoka pale alipokuwa amelala ndani ya ile gari. Mjinga mmoja akamuona na kumrushia teke kali akimuamuru kulala chini, Kamanda Amata akiwa tayari kajigeuza na kuwa chali alidaka kanayagio la mtu yule na kuzungusha kwa nguvu ule mguu, yule jamaa akapiga kelele za uchungu kisha Kamanda Amata akamsukumia nje na kumbwaga. Alijinyanyua kwa ustadi kabisa bila kugusa popote pale, akasimama wima na kukutana na mtu mwingine aliyekuwa bado juu ya ile gari.
“Simama!!!” yule mtu alibwata, kabla hajajiweka sawa na bunduki yake, alijikuta akipata kichwa kikali cha nguvu kilichopmpeleka nyuma, Kamanda Amata alimuwahi na kuichomoa bastola kiunoni mwa yule jamaa, kwa mikono yake miwili iliyofungwa kwa pingu, alfyatua risasi na kumpiga kifuani yule mjinga akambwaga nje ya gari. Aligeuka na kumkuta yule kiongozi wao badoa hajajiweka sawa.

“Anatorok…” zilikuwa ni kelele za mtu mwingine aliyekuwa kalala chini barabarani lakini kabla hajamaliza kauli yake alizimishwa kwa risasi ya kichwa. Kamanda Amata aliruka na kutua ardhini, kisha akajitupa kwa sarakasi maridadi kabisa. akiwa kapiga goti moja chini, alimtwanga risasi mtu mwingine na alipotaka kumgeukia yule kiongozi wao alijikuta kila akifyatua risasi zinagoma, chemba imeishiwa, akaitupa pembeni ile bastola. Wakati huo huo yule kiongozi wa wale jamaa akawa anakuja akikimbia pale alipo Amata huku akitoa matusi ya ajabu, Amata hakumsubiri amfikie, alisimama kwa haraka na kuruka kwa akilina kumchapa teke moja la shavu lililompeleka chini huku bunduki yake ikilalama kwa uchungu na kutawanya risasi huku na kule, kizaazaa. Kamanda Amata alikimbia akawahi kwenye gari yake, akafungua na kuketi kitini huku nje bado kukiwa na kile kizaazaa, bado mikono yake ilikuwa na pingu, akawasha gari kwa kutumia swichi maalum, akaliseti liwe katika automatiki, kisha akaliruhusu liondoke huku akiwa kakamata usukani kwa mikono yote miwili.

Aliizungusha ile gari kwa ustadi wa hali ya juu, wale maharamia waliobaki walifyatua yisasi kupiga matairi na wengine wenye vioo lakini gari ya Kamanda iliyotengenezwa na wanasayansi wa Kitanzania haikupata dhara lolote, iliingia barabarni na kuondoka kwa kasi. Wale jamaa nao wakaamka na kuingia kwenye ile landcruiser na kumkimbiza Kamanda.

“Tulikwishamkamata lakini ametutoroka, ova,” ilikuwa sauti ya yule kiongozi akiwasiliana na kamanda wao, Sharon.
“Hakikisha hamumpotezi tunakuja na nguvu kubwa zaidi, ova,” Sharoni alimjibu.
“copy,” alimaliza kwa kujibu namna hiyo akaiweka ile redio kitini kisha wakaingia barabarani na kuanza kufuata uelekeo wa kule alikokwenda Amata.

Kupitia kamera maalumu iliyokuwa nyuma ya gari ya Amata aliweza kuwaona wale jamaa wakija na ile cruiser yao kwa kasi ya hatari, akatazama vizuri na kuona kuna jamaa tayari juu ya lile bunduki kubwa la kudungulia akijaribu kulenga shabaha. Kamanda Amata akakunja kona kwa ustadi mkubwa na ufundi wa hali ya juu, ile gari ikasota na kuzunguka barabarani ikatazama ilikotoka, nukta hiyohiyo mikono yake miwili yenye pingu lakini liikamata bastola yake kwa umakini wa hali ya juu sana alifinywa jicho moja huku akiwa kauacha usukani peke yake, alifyatua risasi iliyopiga na kuchana sehemu ya mkono wa mtu yule aliye juu ya gari.

Yule bwana akapiga yowe na kuachia lile bunduki huku akivuja damu katika kiganja cha mkono.
Kamanda Amata akajaribu kulenga tena lakini mara hii alijikuta anashindwa, akakamata usukani na kuiweka gari sawa na kukanyaga mwendo. Mfukuzano uliendelea kwa kasi ya hatari, huku wale jamaa wakimwaga njugu lakini bado walishin dwa kuidhibiti gari ya Amata iliyopewa jina la Kilimanjaro kutokana na uzuri wake ilivyo na matata yake yaliyowekwa kwenye mfumo huo. Kamanda Amata alijitahidi kuendesha huku akifungua pingu kwa kutumia kipini maalumu kwa kazi hiyo kilichokuwa katika saa yake, alikichomoa kwa vidole viwili na kukibana kwa meno; punde si punde ile pingu ilifyatuka mkono mmoja. Kamanda Amata alikuw akishusha mteremko mrefu, tayari alikuwa ameyaacha makazi ya watu na kulifikia jangwa, mara nyuma yake juu kukatokea chopa kubwa. Mvumo wa mapangaboi yake ukamfanya Kamanda Amata ajue kuwa sasa kazi imeamka.

Washenzi wamenipania, aliwaza huku akiendelea kukanyaga mafuta na kuongeza kasi ya ile gari. Sasa alikuwa akifukuzwa juu na chini. Hakujua la kufanya, hakujua jinsi ya kujiokoa katika domo la mamba. Kamera katika gari yake zikawa zinafanya kazi sawasawa, nyuma aliiona ile cruiser na juu aliiona ile chopa. Alipotazama vizuri alimuona yule aliyekuwa kwenye chopa mlango akilifutia bunduki lake kubwa lenye risasi za kulipuka upande mmoja. Akajiweka tayari, akafunga mkanda wa kiti sawasawa. Akafungua kijikasha kilicho karibu kabisa na mkono wa gia, akapapasa vinobu kadhaa. Alipogeuka tena kutazama ile kamera yake aliona kitu kama moto kikitokezea pale kwenye domo la ile bunduki, mara moja akajua amedunguliwa. Alam katika gari ikaanza kupiga kelele, Kamanda bila kuchelewa alibinya vitufe Fulani kwenye kile kiboksi mara paa la gari likafunuka na kile kiti cha dereva kikafyatuliwa kwa nguvu na kurushwa juu kama mita 150 hivi. Lile bomu lililopigwa likaifumua gari ya Kamnda nukta ileile na kuichakaza vibaya.

“Iiiiiiiiiiihaaaaaaaaaaa,” ilikuwa ni kelele ya shangilio la yule jamaa kwenye ile chopa akishangilia shabaha yake. Kila mtu alikuwa akishangilia mpaka wale wapio katika ile cruiser. Ile chopa ikageuka na kwenda kutua mbele kidogo, na ile gari nayo ikasimama. “Bora tumemuua, mshenzi huyu,” aliongea Sharon huku akikimbia kuwahi kule inakoungua ile gari akifuataiwa na wenzake kutoka katika gari na ile chopa kila mmoja akiwa na furaha.“Tumemlipua nina uhakika hapa haponyoki,” Sharon alikuwa akionmgea kwa simu ya upepo. “Oh, hongereni sana, kumuua huyo jamaa ni sawa na kufanikisha mipango yetu yote,” Shalabah alijibu huku akionesha tabasamu lake bila kuficha, akiwa anaelekea uwanja wa ndege kwa ajili ya kupokea wageni wanaoingia usiku huo kwa minajiri ya kumaliza biashara yao.

Sharon na wale maharamia wengine walilisogelea gari la Amata lililokuwa likiteketea kwa moto mkali wa ule mlipuko, hakuna aliyesogea kariobu, wote waisimama mbali kidogo wakilitazama likiisha.

DAR ES SALAAM – TANZANIA

CHIBA alishtuka kukuta kompyuta iliyokuwa imeunganishwa na gari ya Amata kwa mtambo wa satellite ikiwa inaonesha mchelemchele kwamba hakuna mawasiliano. Alihamaki kaidogo hakuelewa nini kimetokea, kwa tokeo hilo alijuwa wazi kuwa lazima Kamanda Amata amepatwa na shida kubwa au gari peke yake imepatwa na shida, hakujua kipi ni sahihi. Aliinua simu na kumwita Madam S aliyekuwa kwenye mazungumzo na Dr. Jasmin pamoja na Gina, wote watatu wakakimbilia kwenye chumba cha mawasiliano.

“Vipi Chiba?” akauliza.
Akamuonesha ile kompyuta, Madam S akakodoa macho, “What?”
“Mawili, ama Kamanda na gari lake au gari peke yake imelipuka,” Ciba alijibu.
“Lo, hebu mtafute kwa mawasiliano yake binafsi,” Madam S alitoa amri. Gina na Dr. Jasmin walibaki midomo wazi hawajui kipi ni kipi.
“Hapatikani!” Chiba alishusha simu chini.
Madam S akashusha pumzi ndefu, akajishika kiuno, “No; yuko salama, hawezi kufa kikuku hivyo, we jaribu kumtafuta.”
“Kama alikumbuka kuminya nobu ya dharula, bila shaka atakuwa hai,” alijibu Chiba.
“Nobu ya dharula?” Gina na Jasmin wakauliza pamoja kisha wakatazamana.
“Yeah, kweye ile gari kuna nobu ya dharula ukiibonyeza, inakutoa nje wewe dereva pamoja na kiti chako na kama ni ajali basi gari hupata peke yake,” Chiba akawaelewesha.
“Lakini si ulimuonesha?” Gina akahoji.
“Yap, nilimuonesha.”

“Basi, kabonyeza, hajafa huyo, tusubiri taarifa nyingine,” Madam S akajiaminisha.
Chiba aliendelea kufanya kila analoweza kumtafuta Kamanda Amata, kila simu aliyopiga haikupatikana, alijaribu huku na huku wapi, alipoona kila kitu kimeshindikana, akanyanyuka na kwenda kupata kikombe cha kahawa.
PUUUU! Kamanda Amata alidondoka na kiti chake umbali wa takribani mita 200 kutoka pale kwenye tukio, akaguna kwa mtuo huo, kisha akafungua mkanda wa kiti hicho na kufyatua ule mwamvuli uliomteremsha hapo, akajitoa eneo lile na kutulia kimya nyuma ya kichaka cha mmea wa mkakati, mmea unaostawi jangwani. Alitazama kule barabarni na kuona ile chopa ikiwa chini na ule moto sasa ulikuwa ukipungua taratibu.

Hapa sasa ni kurudi mjini, alijiwazia huku akijipekuwa kuona kama ana kila kitu, bastola hakuna, akakumbuka kuwa amechukua yule kiongozi wa lile kundi, alibakiwa na silaha za baridi tu, kama visu vidogodogo na vikolokolo vingine. Kwa kuwa eneo lile lilikuwa jangwa, na hakukuwa na mbala mwezi alitulia kusubiri watu wale waondoke. Haikupita muda aliona wakiingia kwenye gari na ile chopa kisha kuondoka na kuliacha lile eneo pweke kama awali. Kamanda Amata akavuta hatua kuelekea barabarani.

Alijishika kiuno kulitazama gari lile ambalo sasa lilikuwa haliwaki tena, ila lilikuwa limebaki gofu tu.
Akainua mkono wake na kutazama saa, ilikuwa ikikaribia saa sita tano nne za usiku. Akaliendea jiwe kubwa lililokuwa mahala pale na kuketi.

Haukupita muda, aliona mwanga wa gari ikitokea mbali kidogo, akasogea barabarani na kusubiri, macho hayakumdanganya, alipunga mkono kuashiria gari hiyo kusimama, na ile gari ikampita kidogo kisha ikasimama mbele kama umbali wa kutupa jiwe. Kamanda Amata akaiendea, ilikuwa ikiendeshwa na mwanamke aliyekuwa na watoto wawili ndani ya gari. Kamanda Amata akaomba msaada wa usafiri mpaka mwanzo wa mji tu, yule mama alikuwa ni mtyu wa dini sana, akamwambia aingie huku akimpa pole kwa kuunguliwa na gari yake.
“Kwa hiyo ulikuwa unatoka uwanja wa ndege?” akauliza.

“Ndiyo, nimeingia hapa Mogadishu kama masaa manne yalopita,” Kamanda akajibu kwa kuongopa.
“Sasa utafanyaje usiku huu na ulikuwa waelekea wapi wewe?” akauliza yule mama.
“Nilikuwa naenda Kismayu, lakini sasa itabidi kubadili ratiba, kwani sina chochote.”
“Yaani uko kama ulivyo hivyo? Tena umechafuka vumbi la jangwa kwelikweli, basi hata ufike nyumbani uoge,” yule mama alionesha ukarimu wa hali ya juu sana.

“Hapana asante sana,” Kamanda alishukuru huku akijua kuwa akijilegeza kwa huyo mama ataharibu kazi.
“Hapana bwana usiogope, mimi sina mume, mume wangu aliuawa kitambo yeye alikuwa mwanajeshi,” yule mama akaeleza.
“Usijali mama, nitakuja, lakini ngoja kwanza nifike uwanja wa ndege nikapate kibali kingine japo cha muda wa kuwa hapa,” Kamanda aliomba.

Baada ya mvutano mkubwa na mwanamama yule, mwisho Kamanda alishinda, yule mama akampa kadi ya kibiashara na kumwambia akimaliza kazi yake tu huko uwanja wandege basi amtaarifu ili amkaribishe kwake kabla ya kuendelea na hiyo safari yake ya Kism

Wanawake bwana! Akajiwazia na kutikisa kichwa wakati akivuka barabara na kuelekea upande wa kituo cha tax, akajificha sehemu na kujikung’uta vumbi kisha akachukua tax moja wapo. “Uwanja wa ndege tafadhali,” akamwambia dereva wa tax.

Kamanda Amata ilimbidi abadili ratiba ya kazi usiku huo, kwani kwanza alipanga kwenda kule kuliko na ghala la hao jamaa lakini kutokana na vitu vyake vyote kuungua katika ile gari hivyo hakuwa na kumbukumbu nyingine ya kumuongoza kwenda kule, maadam alisiki katika mawasiliano ya watu wale kuwa kuna wageni wanaokuja uwanja wandege basi aliamua kwenda kuona kwanza ni nani na nani wanakuja usiku huo.
“Tayari boss,” yule dereva tax alimshtua Amata aliyekuwa kapitiwa na usingizi, akaamka na kumpa noti ya dola ya kimarekani kisha yeye akavuka barabara moja na kuwasili katika maegesho ya magari. Akachomoa simu yake na kubonyeza namba fulani.

Akaweka simu sikioni na kusubiri majibu ya upendo wa pili.
“Yeah, Ahab!” akaita.
“Ndiyo, unaongea na Ahab hapa, nani mwenzangu?” Ahab akauliza.
“Mimi ni rafiki yako tulikutana siku chache zilizopita hapo Uwanja wa ndege nikakuahidi kukupigia pindi tu nikitulia,” kamanda alimkumbusha.
“Yeaaaaah, uuuuuu n’mekukumbuka asee,” akajibu.
“Niko hapa Uwanja wa ndege, ninahitaji msaada wako wa haraka,” akamwambia.
“Bila shaka braza, uko wapi?” Ahab akauliza.
“Niko nje hapa, njoo nyuma ya hili jengo la matangazo,” akamwambia.
“Sawa, sawa niko njiani.”

Kamanda Amata akarudisha simu mahala pake na kuendelea kujibana pale pale alipo, kila alipokuwa akiangaza macho hakumuona yeyote aliyekuwa akimuhitaji. Mara akamuona Ahab, yule kijana anayefanya kazi za kubebea wasafiri mizigo yao akiwa anashangaa shangaa.
“Ahab,” akaita, na yule kijana akashtuka kutazama pale mahali akamuona Kamanda akiwa pale.
“Eee braza! Sema,” Ahab akamuendea.

“Sikia nahitaji msaada wako rafiki, naweza kupata vazi la wafanyakazi wa hapa uwanja wa ndege?” akamwambia. Ahab akashtuka kidogo na kumtazama Kamanda, alikuwa kama hajasikia vizuri kile alichomwambia. Akatahayari kwa ombi hilo na baadae akawa kama mtu aliyekurupuka, “Sawa, sawa inawezekana, nilikuwa nafikiri jinsi ya kupata.”
“Nahitaji sasa hivi, nikimalizia kazi tu nitakupa urudishe, ila usimwambie mtu,” Kamanda akamuasa.
“Ok, nifuate,” sauti ya Ahab ilitoka kinywani mwake huku akiliacha eneo lile na Kamanda Amata akamfuata nyuma. Ahab akamwongoza Kamanda mpaka pembezni mwa jengo lile la uwanja wandege sehemu ambayo haruhusiwi mtu kupita kirahisi, akaingia nae kwenye kijimlango kidogo na wakatokea kwenye chumba kilichojaa maboksi tupu mengi sana yaliyovurugwa vurugwa.

“Subiri hapa, ila braza ni hatari wakinikamata,” Ahab alisema kwa woga, Kamanda Amata akampa ishara ya kutokuwa na wasiwasi akimtaka aendelee mbele.
Dakika mbili baadae, alirudi pale akiwa na mfuko wa plastiki, akamtupia Amata. Ndani ya mfuko huo kulikuwa na nguo ndefu iliyounganishwa kutoka juu hadi chini. Akalivaa haraka haraka na sasa kuonekana kama mmoja wa wafanyakazi wa hapo. Akamwambia Ahab wataonana punde tu akimaliza kazi yake. Akamsisitizia kutosema au kutamka lolote juu ya hilo.

Kamanda Amata akatokea kwenye kile kimlango na kuzunguka mbele ya uwanja ule ambako watu huingia na kutoka, magari hushusha na kupakia, akaenda moja kwa moja hadi sehemu iliyoonekana kuna vikokoteni vingi vimezagaa na wachache wa wafanyakazi waikuwa wakivikusanya kurudisha ndani, naye alijiunga nao akapata nafasi ya kuingia ndani ya uwanja huo. Bado alikumbuka kuwa ndege zinazosubiriwa ni moja ya Ethiopia ambayo wageni hao wote watashuka pamoja pasina wao kujuana. Aliitazama saa yake, ilimuonesha saa saa saba za usiku, bado ilibaki muda kidogo tu ndege hiyo ifikie. Kamanda Amata alifanya kila analoweza kujaribu kuona sura zilizopo eneo lile ndani na nje ili kubaini kati ya maharamia waliopo hapo basi ni nani yupo, lakini hakuweza, lakini alimini kuwa ama walikuwa nje au kuna sehemu ambayo walikuwa wamejibana, wanaogopa nini sasa? Akajiuliza.

Bw. Goloko alifyatua kitufe cha mkanda na kushusha pumzi ndefu, kisha akatazama abiria waliokuwa wakiteremka kwenye ndege hiyo. Alizitazama tiketi zake na kisha akazihifadhi vizuri, akasimama mara baada ya wale watatu waliokuwa pembeni yake kufanya hivyo. Alikuwa ni mzee wa makamo, kichwa chake kilikuwa na mvi za kuhesabika, shati lake la kitenge cha Urafiki lilikuwa limemka sawia. Weusi wake ulikuwa tofauti na abiri wengine waliokuwamo ndegeni ambao waling’aa kidogo ama kwa asili yao au kwa kutakata kwa wema. Kwa hatua za uhakika alishusha mguu mmoja baada ya mwingine huku macho yake yakitazama vizuri ngazi ile labda miguu isije kukosea na kufanya ajali isiyo lazima.

Aliwahi kuwa katibu wa wizara nyeti ya Maji, Nishati na Madini, kigogo katika serikali ya sera za ujamaa na kujitegemea, serikali iliyopambana vikali na wahujumu uchumi, iliyowasaka mpaka mapangoni na mashimoni baada ya kuifanya nchi kupitia katika kipindi kigumu kiuchumi, serikali ya Mwl. Nyerere. Mzee huyu aliyefukuzwa kazi katika wizara hiyo mara tu alipobainika kupokea hela ndefu kutoka kwa tajiri mmoja mkubwa huko duniani ambaye wengi hawakuwahi kumuona kwa macho, alifukuzwa kazi kama mbwa na serikali ya awamu hiyo, na hiyo ilikuwa ni bahati kwani wengine walifungwa kabisa.

Hata akiwa nje ya kifungo bado aliweza kufanya kazi hiyo ya kuhakikisha hujuma hiyo inawezekana, na hakika iliwezekana, na usiku huu alikuwa akija kukamilisha mazungumzo na wadau wengine ili kufanya malipo ya mabilioni ya pesa na kuwagawia washikaji zake. Nyuma yake kulikuwa na watu wengine wawili waliojaa katika suti kali za bei mbaya ambazo hapa zingeweza kuvaliwa na kiongozi wa juu wa serikali. Nao walikuwa wkishuka ngazi hizo kwa madaha kabisa wakijitabiria utajiri unaowafikia dakika chache zijazo.

Kamanda Amata kutoka pale alipokuwapo moyo wake ulipiga chogo chemba kumuona mzee yule, hakukosea, ni yeye, aliyewahi kuitwa Mheshimiwa, alimtazama kwa makini sana huku akiendelea kujifanya anasafisha kwa mashine katika sakafu hiyo ng’avu.

Alipomuona tu mzee huyo na kuhisi jambo, aliirudisha ile mashine mahala pake na kujongea karibu na eneo la wageni hao kusubiri mizigo yao, akapita mpaka kwenye tundu ambako mizigo hiyo hutokea, na kuikodolea macho akijifanya kuiweka vizuri pindi inapotaka kudondoka, lakini jicho lake lilikuwa likitazama nyendo za yule mzee.

Akamuona akipokelewa kwa bashasha na wenyeji wake, akatzama sura za wenyeji wake hakuna aliyemtambuwa, inaonekana hawa ndio matop wao, alijiwazia kisha akatazama mizigo mingi inayochukuliwa, akabaini watui hao wana wageni zaidi ya mmoja na kweli alishuhudia wageni wane waliokusanywa nao na kisha kupakiwa mizigo yao katika kitoroli, Amata akawahi kuwasaidia nao wakaridhia bila kumjua kutokana na vazi alilovaa na kofia aliyojitwika kichwani, miwani aliyoichukua kwa Ahab iliupoateza kabisa uso wa kijana huyo, akakokota kile kitoroli mpaka sehemu inayotakiwa.
Cadillac Escalade/ESV, gari ya bei mbaya ya kutisha, ilisimama miguuni mwa Amata na mlango wa nyuma ukafunguka wenyewe bila kuguswa na mtu. Akapakia mizigo yote ndani ya gari hiyo huku akikariri sura za wageni hao, akilini mwake alijuwa wazi kuwa watachukuliwa na gari yenye buti la kufunika ili atumbukiemo, lakini walileta gari hiyo ya gharama yenye umbo asilolitarajia.

Akapakia mizigo na kuliona gari hilo likiondoka taratibu. Akaikariri namba ya gari hiyo ya kifahari SOM kisha ikafuatiwa na maandishi ya kikwao na chini ikamalizia AC528B, akachomoa peni kutoka mfuko wake wa siri na kuiandika pembeni, akaitazama ile gari ikiondoka taratibu na kuacha eneo lile na nyuma yake ikafuatia nyingine iliyokuwa wazi juu na aliona wazi kuwa waliokaa mle ndani walikuwa na bunduki kubwa walizozifutika kwenye miguu yao ila mitutu yake ilionekana wazi. Aliinua simu yake na kubofya namba Fulani kisha akatega sikioni.

Kelele ya simu ilimshtua Chiba aliyekuwa bado akifanya kazi ya kumtafuta Amata, akainyakuwa na kuiweka sikioni.
“Hello!” akaita.
“TSA 1,” akajibu upande wa pili. Chiba akarukwa na furaha, akamuunganisha Madam S kutoka chumbani kwake.
“Ndiyo Amata, vipi wewe maswahibu gani yamekukuta huko?” Madam aliuliza kwa sauti ya usingizi.
“Niko poa, ila gari yangu imelipuliwa vibaya sina usafiri kwa sasa na vifaa vyangu vingi vimeharibika, lakini hilo si tatizo, niko uwanja wa ndege nimemuona mzee Goloko kafika usiku huu, mna taarifa yoyote juu yake?”
“Yeah, ndio maana tulikuwa tukikutafuta sana kukupa taarifa hiyo kuwa umfuatilie amekuja nkufanya nini huko? Leo TSA 4 alifuatilia nyayo zake na kupata mengi, kwa vyovyote anahusika na hujuma hii, tumeshamkabrasha pamoja na raia mmoja wa Kirusi ambaye yupo kule Mtwala ‘kisimani’ anaitwa Mr. Reubellen Vinchinsk, naye tunamuangaza pia, tutawapata tu mmoja mmoja, pole kwa matatizo, sasa unasemaje?” Madam S alimweleza kwa kifupi.

“Nimeng’amua samaki alipo, mayai yake kumi na mbili yamebaki kumi tu, na yai moja nimelinyofoa kiini ninacho, sasa natafuta wadogo zangu nikishajua walipo ndiyo niliamshe rasmi hapa jangwani,” Kamanda aliongea kwa lugha ya mafumbo ambayo walielewa wao wenyewe tu. Walipomaliza, kamanda akakata simu na kuiweka mahala pake, akavua lile gwanda alilovaa na kulikunja vizuri, akampigia rafiki yake Ahab na kumpatia pamoja na hela kidogo. Ahab akashukuru sana na kumwambia Amata kama ana shida yoyote amtafute muda wowote. Swala gumu lililofuatia hapo ni jinsi ya kurudi mjini, akili yake ilizunguka sasa akaanzie wapi, mara simu yake nyingine ikaita akaichomoa na kuitazama, lo, ni yule mwanamama wa kiarabu aliyempa lift akaipokea, simu ilitaka kujua ni wapi alipo kwa wakati ule, Kamanda akagwaya.

“Ni usiku sasa, nikuchukue upumzike nyumbani na kesho utaendelea na shughuli yako,” Kamanda aliisikiliza sauti hiyo akashindwa ajibu nini, aliitafakari mara mbilimbili. Huwezi kujua labda ananiepusha na balaa kubwa zaidi, lakini pi itakuwaje kama ni mtego? Akabanwa na maswali hayo mazwili yasiyo na majibu.
“Nipo Uwanja wa ndege,” akajibu Kamanda.

Ndani ya jumba kubwa la kifahari, jopo la watu sita liliketi katika meza ndefu iliyokaa kwa umbo la ovali, mbele yao kulikuwa na luninga kubwa iliyoonesha taswira ya mtu, Mr. Lonely.
“Nawakaribisha sana wageni wangu kwa moyo mkunjufu,” Mr Lonely alikaribisha, sauti yake ilisikika kutoka katika luninga ile kubwa. Na kila mjumbe aliketi sawia kwenye kiti chake, huku vinywaji mbalimbali vikipitishwa na akina dada warembo kabisa waliokuwapo hapo kwa idadi ya wageni, ikiwa na maana kuwa kila mgeni alikuwa na mahudumu wake kwa kila kitu. Baada ya kula na kunywa na kutambulishana, kufahamiana vyema, ilipangwa siku ya pili asubuhi ndipo biashara hiyo ifanyike rasmi. Usiku huo kila mmoja alipewa mahala pa kulala katika jumba hilo kubwa na pweke, wakisubiri siku jua la siku inayofuata ili wakamilishe.

Asubuhi iliyofuata
Kila mmoja akiwa ndani ya suti nadhifu, baada ya kupata kifungua kinywa na huduma zingine za kibinaadamu ndani ya jumba hilo la kifahari walikutana tena kwenye sebule ileile na kuketi katika meza ileile kwa mtindo uleule. Kati ya watu hao alikuwepo Bwana Shalabah pamoja na yule bwana mnene asiye na shingo ila kiwiliwili kilichoungana na kichwa tu, alijulikana kama kwa jina moja tu la Hussein.

“Ndugu wadau natumaini hakuna la kutuchelewesha, leo ni siku tuliyoingoje kwa muda mrefu sana ili kukamilisha zoezi letu la kuuziana zile silaha za maangamizi,” Bwana Hussein akaanzisha mazungumzo. Kila mtu akaitikia kwa kichwa kuashiria ni sawa, kisha akaendelea kusema, “Na ninapenda kumshukuru sana komredi Goloko Mikidadi kwa kazi ngumu ambayo ilitaka hata kuyagharimu maisha yake, lakini Mungu mkubwa leo tuko naye hapa, bila huyu jambo hili lisingefanikiwa kani tangu miaka kumi iliyopita alikuwa akihakikisha mambo yanakwenda na leo msemo wa kwao Tanzania umetimia Mvumilivu hula mbivu,” akajikohoza kidogo kisha akavuta faili lake lililofingwa kwa tepe za dhahabu, “Kama mnavyojua, kazi hii haikua ndogo mpaka hapa tulipoifikisha…”

Baada ya mazungumzo marefu kati yao, na kukubaliana namna ya kununua silaha hizo za maangamizi, kwanza ikabidi wakaangalie ghalani aina yenyewe ya silaha na wakati huo zilitakiwa kupakiwa na kuondoka katika eneo hilo. Wajumbe waliafiki na kuanza kujipanga kutoka kuelekea huko ziliko.

Shalabha aliwaongoza mpaka katika mlango Fulani akabonyeza kitufe na mlango ule ukafunguka kisha wote wakaingia na kujifungia ndani. Ilikuwa ni lifti iliyowateremsha chini kabisa kama mita hamsini hivi, ikasimama wote wakatoka na kufuata ujia mrefu mpaka kwenye sehemu kama kijisebule hivi, Shalabah akabonya sehemu na sekunde chache tu kilikuja chombo kama gari kilichokuwa kikipita kwenye mkondo wa maji, kikasimama mbele yao na wote wakaingia na chombo kile kikaondoka.

Mwali wa jua la asubuhi ulipenya kati ya vioo vya dirisha lililopendezeshwa kwa mapazia mazuri ya kupendeza, akavuta moja kulisogeza pembeni na kupepesa jicho, anga samawati lisilokuwa na wingu lilimlaki, akainua mkono na kutazama saa yake, ilikuwa ikikimbilia saa tatu asubuhi, lo, nimelala kama mtoto mdogo, alijiwazia na kuamka, akaketi ukingoni mwa kitanda, kilikuwa chumba kikubwa kizuri chenye kila kitu kilionekana wazi hakikutumika kwa muda mrefu, lakini harufu nzuri ya ‘air freshner’ ilikifanya kionekane kizuri maradufu.

Kamanda Amata aliingia maliwato kujiweka sawa, hakuwa na nguo za kubadilisha baada ya mizigo yake kuungua pamoja na gari usiku uliotangulia. Lakini ulikuwa ni ukarimu wa ajabu kwani pembeni yake kulikuwa na suti maridadi iliyoning’inizwa, suti mchanganyiko, suruali nyeusi na juu koti la kijivu, shati safi la bluu bahari lililowekwa tai ndefu mpya kabisa ikiwa hata haijafungwa bado. Amejuaje? Akijuliza huku akijifuta maji kwa taulo safi jeupe, mara mlango ukagongwa, akatulia kidogo, ukagongwa tena. Kamanda Amata akajifunga taulo na kuuendea, akaufungua kidogo na kukutana uso kwa uso na yule mama.

“Habari za asubuhi,” akamsalimu.
“Salama, umemakaje wewe?” yule mama akauliza.
“Nimeamka salama, asante kwa ukarimu wako, wewe ni mwanamke wa pekee sana,” Amata alimshukuru. Yule mama alimtazama Amata usoni kwa jicho lililoongea, akarudisha macho yake kifuani mwa kijana huyo, kifua kilichojaa kimazoezi.

“Pole sana,” akamwambia Amata. Pole hiyo ilimshtua kidogo akamkazia macho na kumtupia swali, “Pole ya nini?”
Badala ya kujibu, alipitisha kiganja cha mkono wake kwenye ubavu wa Kamnda Amata na kuumgusa kwa mguso laini uliomfanya Amata kutulia kwa nukta kadhaa.
“Umeumia sana hapa,” alimwambia.

“Ni kweli nilipata ajali mbaya sana,” Kamanda akajibu huku kiganja cha mkono wake kikiwa kimekifumbata kile cha yule mwanamama bado kikiwa kimeugusa ubavu wa Amata, yule mama akaingia ndani ya chumba kutoka pale mlangoni alipokuwapo, na kuurudisha mlango kwa kuugonga na makalio yake.

Hakuwa mtu mzima sana, alikuwa wa wastani labda miaka thelathini na mitano au arobaini, alikuwa mfupi kiasi mwenye mwili ulioshiba. Kamanda Amata hakuamini alipomtazama kwa ukaribu, alivaa jeans iliyombana sawia na kufanya shepu yake ilitengenezeka vyema kwa unene ule kuonekana sawia, wakatazamana kwa nukta kadhaa mara pepo likafanya kazi yake, ndimi za wawili hao zikabadilishana mawazo vinywani mwao, wakapapasana hapa na pale na taulo la Kamnda Amata likadondoka chini baada ya kuondolewa kiufundi na mwanamama huyo. Alionekana kuwa na moto wa hali ya juu wa kuibanjua amri ya sita kwa jinsi alivyokuwa akimng’ang’ania mwili wa Amata.

Kamanda Amata akameza mate pindi alipouona mwili ule mwororo ukiondolewa mavazi ya juu, alikuwa kajitunza, matiti mawili hayakuanguka abadani, yalisimama kama msichana asiyevunja ungo.

Fasendy alishindwa kuiamini taarifa aliyopewa usiku uliopita kuwa yumkini Kamnada Amata atakuwa amekufa kwenye ule mlipuko. Alikuwa akiwasikiliza vijana watatu waliokuwa wakiongea wakati wakiwa katika lindo la nje karibu kabisa na bandari ya zamanai ya Mogandishu, wakiongea na kucheka sana huku wakiendelea kula mirungi na kuwa kama mbuzi.
Fasendy alitikisa kichwa kwa dharau na kuwaona kama watu wasiojua wasemalo kwa kuwa hawakuwa wakimjua Kamanda Amata na mambo yake. Mara redio aliyokuwa ameishika mkononi mwake ikaanza kukoroma kuashirian kuwa kuna mwito utakaoingia muda si mrefu.

“Sierra 5, Sierra 5,” ile sauti ikaita. Yule kijana mmoja kati ya wale waliokuiwa wakiongea akiinua ile redio na kujibu, “Sierra 1 umesomeka,” alipomalisa aliminya kidubwasha Fulani.
“Sierra 5 hali usalama ikoje?”
“Sierra 1 usalama huku upo sawa hakuna tabu yoyote,” akajibu.
“Sierra 5 hakikisha umakini wako unakuwa makini muda wote, tuna hakika yule shetani anaweza kuibuka muda wowote,” ile sauti ikajibu.

“Read and clear!”
Baada ya kuongea na watu wa upande wa pili, yule bwana akamgeukia mwenzake, “Habib, unajua mi simuelewi huyu mwanamke sasa hivi.”
“Kwa nini?” akahoji Habib
“Jana asubuhi badala ya kumlenga yule shetani, kafanya off target,” Habib akaeleza. Kisha wote wawili wakageuka kumtazama Fasendy aliyekuwa kasimama mbali na wao akiendelea kuvuta sigara yake, akipanga na kupangua.
“Oya, mi nawaacha kidogo narudi baadae,” Fasendy aliwaaga wale jamaa wawili kisha akaondoka eneo lile.
Wale jamaa wakatazamana, “Unaona?” akamuuliza Habib.
“Si amesema atarudi!” Habib akajibu, yule bwana akainua redio yake na kubofya tufe moja wapo, akaiweka tayari.
“Sierra Sierra,”

“Unasikiwa Sierra,” akajibiwa.
“Sierra 5, lindo limepungua, mwanmke kaondoka,” akatoa taarifa.
“Sierra 1, ujumbe umefika unafanyiwa kazi,” ile sauti ikamjibu na mawasiliano yakakatika.

Fasendy alivuta hatu mpaka barabarni akasimamisha tax iliyokuwa ikikatiza hapo, akingia na kujitupa katika kiti cha nyuma.
“Jazeera Palace,” alimwambia yule dereva.
Alipofika akamlipa yule dereva na yeye moja kwa moja akakatisha kwenye maegesho ya magari na kuingia mpaka mapokezi, akamsalimu mwanadada aliyemkuta hapo na kumpa bahasha moja ndogo iliyoandikwa juu jina la mlengwa. Mara hiyo hiyo simu yake ya mkononi ikaanza kufurukuta kwa fujo kutoka katika nguo yake, akaito na kuiweka sikioni.
“Fasendy, kwa nini umeondoka kwenye point yako na unajua tunaihitaji shabaha yako,” sauti ya Sharon ilisikika.
“Sijaondoka, nipo katika kutekeleza majukumu yangu kama tulivyokubaliana,” akajibu huku akiwa anatoka katika hoteli ile kurudi barabarani. Akapita kwenye maegesho na kuakatiza kijibustani cha maua marefu mpaka barabarni kwenye maegesho ya tax, akaingia katika noja wapo na kuagiza kurudishwa kule alikotoka. Kichwani mwake gadhabu ilimshika hasa alipopata ile simu kwani alijua kwa vyovyote ni walewale waliotoa taarifa.

“Aaaaa usiende Amata,” mwanamke wa Kiarabu alilalama kitandani wakati Kamnda Amata akikiacha kitanda na kuoliendea bafu kwa mara ya pili.
Akiwa mbele ya kioo kikubwa alijiweka sawa tai yake na kutazama kama koti lile limemkaa sawa au la.
“Unaenda Kismayu?” yule mwanamama aliuliza.
“Hapana, naenda mjini kuna kazi ya kufanya,” akajibu.
“Twende wote,” yule mwanamama akaasisitiza hiloo kwa Amata.
“No. we baki hapa na watoto, nitarudi, lakini kama hutojali uniazime gari,” akamwambia. Yule mwanamama aliyejulikana kwa jina la Hassna alitoka kitandani na kuliendea bafu, dakika mbili tatu tu akatoka na kujitupi mavazi yake akionesha wazi kutoridhika na jibu la Amata. Akatoka na kumpa ishara ya kumfuata, moja kwa moja mpaka sebuleni.
“Pata kifuangua kinywa kwanza kisha utaenda,” akamwambia Amata huku dada wa kazi akiandaa hiki na kile. Kamanda Amata akatazama saa yake, ilikuwa inakimbilia saa nne za asubuhi, penzi kitovu cha uzembe alisema Ngoswe, Kamanada akawa akijiwazia.

Wakiwa ghorofa ya chini, Hassna alimwongoza Amata mpaka banda la uani, “Hii hapa utatumia,” akamwambia huku akivuta tambala kubwa lililojaa vumbi, akalifunua gari lililofichwa katika tambala hilo. Kila mtu alibana pua kwa kuogopa vumbi hilo. Gari moja matata, iliyoweka ufito wa alluminium juu ya bonet lake, “Sawa, ina mafuta?” akauliza Amata.
Yule mwanadada akawa akining’iniza funguo za gari hiyo, akamrushia Kamanda naye akazidaka kwa umahiri, “Mafuta?” akarusha swali kwa yule Hassna.

“Jamani mafuta si umeshatia au unataka kutia tena?” Hassna aliuliza huku anacheka kwa utani. Kamanda Amata akabana jicho moja na kuzama ndani ya gari hiyo, 504. Akaitekenya kwa funguo ile nayo ikawaka, Kamanda Amata akaitoa ile gari kwa kasi na kuingia barabarani. Nimechelewa sana kuanza kazi, alijisemea huku kauma meno, akikunja kona moja baada ya nyingine, akaegesha gari hiyo mbele ya benki moja kubwa mara tu alipoona ibao cha ATM. Akashuka na kuilekea mashine hiyo, akatoa kiasi cha pesa anachokihitaji na kurudi ndani ya gari. Kwanza nahitaji silaha, aliongea na nafsi yake huku akiingia barabarani.

MOQDISHU ARM MARKET ni maandishi yaliyokuwa yakisomeka juu ya mlango mkubwa wa duka hilo, halikuwa na watu wengi bali ni wachache sana, zaidi zaidi palionekana pamefungwa muda wote.
“Tukusaidie nini?” akauliza mlinzi mlangoni.
“Nahitaji huduma,”nakajibu Kamanda.

Yule mlinzi akamchukua na kumuingiza ndani ya duka hilo kubwa, ndani yake hamkuwa na bidhaa nyingine zaidi ya silaha za kila aina. Kamanda Amata alifikishwa kaunta na kuonana na mhusika.
“Ee nahitaji bastola mbili zenye nguvu na risasi zake,” kamanda aliagiza.
“Ok, bahati mbaya zile zenye nguvu kabisa zimekwisha nab ado hatujapata mzigo, ila nitapendekeza kwako, Smith and Wesson double barell na Nagnum 22 au ukipenda kuna hii Revovler,” mzee wa makamo alimwambia Amata naye akaitika kwa kichwa. Dakika kadhaa tu.zile zana zilikuwa tayari mezani, “Huu hapa mzigo kaka,” yule babu alimgutusha Kamanda aliyezama katika mawazo, akachukua Magnum 22 na kuijaribu kidogo kwa kuitekenya hapa na pale, alipojiridhisha akaiweka mezani, kisha akajaribu na nyingine zote.

Alipohakikisha zinamfaa, akazilipia na kuchukua risasi za kutosha.
“Sasa kijana kuna utaratibu wa kiserikali wa kumiliki silaha huwezi kununua kama machungwa,” yule babu akawa mkali kidogo, alipoinua macho akakutana na macho makali yasiyo na masihara, macho ya mpiganaji, Amata Ric au Kamanda Amata.

“Sikujua kama hata Somalia mnahitaji vibali kumiliki silaha,” Kamanda Amata alimwambia, akatoa noti ya dola hamsini na kumuwekea mezani, “ Nenda ukanijazie fomu zote, mi sina muda,” yule mzee akakenua kwa fuaraha, chezea noti wewe. Kamanda akarudi katika gari yake.

JAZEERA PALACE
Peugeot 504 iliingia maegeshoni taratibu na kuwekwa mahala salama. Kamanda Amata akashuka akiwa na balaghashia kichwani na moja kwa moja akaenda kaunta ya hoteli hiyo.
“Oh, karibu, umenishtua sana,” alisema mhudumu wa mapokezi huku akimpa kijibahasha kidogo, na wakati huohuo akampa ishara ya kuzunguka upande wa pili, Kamanda Amata alifanya hivyo, akamfuata yule mhudumu wa kike katika kiujia kilichotenganisha ofisi mbalimbali.

“Jaffer, nakwambia hili kwa kuwa nakupenda,” yule mhudumu alianza namna hiyo na Amata akahisi kama hajasikia vizuri, akamkazia macho, “Unatafutwa na polisi kwa kuwa wana mashaka na wewe kwa nini chumba chako kinatokea mauaji mara kwa mara, nakuomba uondoke hapa haraka usirudi,” yuele mhudumu alikuwa akiongea huku akitazama huku na huku kama anayehofia jambo Fulani, akaingiza mkono katika nguo yake na kutoa kadi ya kibiashara akampatia, “Kama unataka kujua lolote nipigie.”

Kamanda Amata akaitazama ile kadi, “Ok, nitahitaji maelezo juu ya chochote kinachoendelea sawa? Nitakuta baadaye.”
“Haya, nenda, pita huku nyuma haraka,” mhudumu akamwonesha njia Amata na ye akaifuata. Akazunguka nyuma ya jengo la hotel hiyo na kuruka uzio mdogo wa michongoma kisha akatokea katika maegesho ya magari, akatazama usalama huku na kule kama kuna anayemhofia, usalama ulikuwepo, akavuta hatua na kuingia katika ile gari, akatoka taratibu eneo hilo na kuchukua barabara kuu inayoelekea nje ya mji lakini inapita mbele ya bandari ya Mogadishu ikianzi ile mpya na kumalizia ile ya zamani. Akiwa anakaribia kuiacha ile barabara kuu ili kuchuku barabara ndogo, alikuta kuna foleni kubwa, hakujua mbele kuna nini, hakuona haja ya kupoteza muda kwani alijua wazi jinsi anavyowindwa, akaigeuza gari na kurudi alikotoka, mara akasikia ving’ora vya polisi nyuma yake, “Polisi, weka gari pembeni,” akaamriwa.
“Shiiit,” akang’aka na kupiga ngumi usukani huku akiitoa ile gari na kuiweka sehemu salama nje ya barabara. Afisa wa polisi akasogea mpaka pale dirishani, akamwamurtu kuteremka.
“Lete vitambulisho!”

Kamanda Amata akawapa hati ya kusaifiria ya serikali ya Congo iliyomtambulisha kwa jina la Zubi Mathuren.
“We ni raia wa Congo?” akaulizwa lakini hakujibu, “Mpekue!”
Askari mmoja alimpekua na kumkuta akiwa na bastola hizo tatu mwilini mwake, “Nyie ndiyo tunaowatafuta, mnatoka kwenu mnakuja kupoteza amanai hapa halafu jumuia ya Kimataifa inasema Somalia hakuna amani, tia pingu huyo,” yule afisa wa polisi akatoa amri.

Kamanda Amata akatiwa pingu, kisha gari yake ikapekuliwa na walipofungua buti la gari hiyo, wale polisi wakabaki midomo wazi, hawakuamini wanachokiona. “Nini hiki kwenye buti?” yule afisa aliyekuwa akipekua aliuliza. Kamanda Amata alibaki kumtazama kwa kuwa alikuwa hajui ni nini ,kipo ndani yake. Yule polisi mwingine akamshika kwenye kiwiko na kumvuta upande wa nyuma wa gari hiyo.

Hakuamini anachokiona, mwili wa binadamu ulikuwa ndani ya buti la gari, ukivuja damu mbichi. Kamanda Amata akautazama mwili ule kwa makini moyo wake ukapiga tik – tak, Hassna, mwanamke aliyelala nyumbani kwake, na kufanya naye mapenzi asubuhi tu ya siku hiyo, aliyempa gari hiyo atumie. Amewekwa saa ngapi humu na mi nilimuacha nyumbani? Akili ya Kamanda Amata ilifanya kazi haraka haraka, akamuinamia yule marehemu, kwa mikono yake iliyofungwa pingu mbele akakamata nguo ya Hassna, akamuinua, chozi likamdondoka. Amewakosea nini mwanamke huyu, mbina watu ni wakatili hivi?. Kamanda Amata akaurudisha chini ule mwili wa Hassna na kuulaza tena katika buti lile.

“Wewe ni muuaji, jamb…!” aliongea kwa kelele yule askari, kabla hajamaliza kusema hayo, taa ya kimulimuli kwenye gari ya polisi ilitawanyika vipande vipande, kioo cha mbele cha gari ya Kamanda kikamwagika na kuwa kama chumvi barabarani, jicho la Amata lilishuhudi land cruiser pick up juu yake ikiwa na watu kama watano wenye silaha.
“Ambusssshhhhh!!!!” polisi mwingine alipiga kelele wakati huohu Kamnda Amata alijitupa chini na kumshuhudia yule polisi aliyepiga kelele kutoka nyuma yake akipaishwa juu na kutupwa kando akiwa marehemu.

Amata alijibiringisha uvungu wa gari na kutokea upande wa pili, pingu alizovalishwa zilimnyima uhuru wa kufanya makeke yake. Hali ya pale mahala ikavurugika, kelele la marushiano ya risasi na harufu ya baruti zilitawala. Kutoka uvungu wa gari ile aliona tairi za ile land cruiser zikisugua lami na kufanya kelele nyingi, alitazama hapa na pale hakuna pa kutorokea. Akajua wqazi kuwa akijitokeza tu atakuwa chakula cha risasi hizo zenye hasira. Kando mwa barabara, kulikuwa na mtaro mkubwa sana uliounganishwa na bomba kubwa la maji machafu linaloelekea baharini, akazungusha akili haraka haraka akajibiringisha kwa haraka na kujidondosha mtaroni, kutokana na wingi wa maji yanayopita katika mtaro huo, nay eye hali kafungwa mikono, hakuweza kupingana nayo yalimbeba.

Wale jamaa walishuka kwenye gari yao na silaha kali mkononi, wakiwa wamekwisha wacharaza askari wote risasi na wote kuwa marehemu.
“Katoroka?” mmoja aliuliza.
“Yule sio binadamu asee, alikuwa hapa chini ya gari,” mwingine alijibu huku akiwa ameshika silaha yake ikiangalia juu kwa usalama zaidi.
“Tawanyika mumtafute!” yule kiongozi alitoa amri; wale jamaa waliotafuna mirungi walizagaa kama vichaa wakipiga makelele ya kuonesha munkari wa hali ya juu, “Angalieni kwenye mtaro,” alitoa amri nyingine na wawili kati yao walijitosa kwenye mtaro kumsaka Amata.

Mkondo wa maji ulikuwa ni wa kasi sana ndani ya bomba kubwa la maji machafu, harufu mbaya ilitawala ndani humo, Kamanda Amata aliwaona wale watu waliokuwa wakija kumtafuta wakiwa na silaha mikononi mwao, Amata alijificha kwenye maungio ya bomba akajibana akisubiri.

“Songa mbele!” ilikuwa sauti ya yule wa nyuma ikimuamuru wa mbele, huku wakipiga risasi ili mradi walikuwa wamerukwa akili. Mmoja alipofika pale kwenye maungio tu, Kamanda Amata alimkamata kwa mikono yake miwili na kumvuta kwake, akampa ndosi moja matata yule bwana akapepesuka na nguvu ya yale maji ikaanza kumshinda, Amata alimpachika mikono yake shingoni na kumbana kabala ya nguvu mpaka alipohakikisha yule bwana kalegea akamuachia akajibwaga chini.

“Yuko hukuuuuu!” yule wa pili akapiga kelele ya kuona mwili wa mwenzake ukijibwaga majini na kubebwa na maji hayo. Mara Amata akasikile ukelele wa maumivu alipotokeza kichwa kuangalia kulikoni alimshuhudia yule jamaa akijibamiza katika moja ya kingo za bomba lile ambalo liliungana na mtaro mkubwa, akajibwaga na kutulia. Akiwa katika kutaharuki nani aliyefanya shambulizi hilo, akashikwa mkono na kuvutwa upande wa pili, akikimbizwa kupita ndani ya maji mpaka eneo Fulani.

Yule mtu akamuachia na kunyanyua mikono yake akafungua mfuniko mkubwa wa chuma kwa mikono yake, mwanga wa jua ukaingia ndani ya bomba hilo yule mtu akapanda kwa ufundi wa ajabu sana kiasi kwamba Kamanda Amata alijua wazi kuwa kama mtu huyo si mwanajeshi basi ni mtu aliyepitia jeshi, yule mtu aliyekuwa kava sox mpaka usoni na kuonekana macho tu alimpa ishara Kamanda Amata kupita pale kwenye tundu; naye bila kusita akajirusha kwa namna ileile na kupenya wote wakatokea juu ya bomba lile, yule mtu akalivuta lile funiko na kulirudisha mahala pake kisha akaanza kutimua mbio na Kamanda Amata akiwa anamfuata.

Walikuwa mbani na ile barabara, walikimbia kufuata fukwe ya bahari iliyopo eneo hilo kwa mwendo kama wa dakika tano, kisha yule mtu akasimama, akaingiza mkono mfukoni na kutoa kitu kama funguo ndogo akaipachua ile pingu nayo ikafunguka, akaitupa mbali na kuendelea na safari na Kamnda Amata bila kuongea, walipita katika majumba jirani na eneo hilo. Na mbele ya eneo hilo walisimama, yule mtu akatoka ile sox yake usoni, Kamanda Amata hakuamini anyemuona mbele yake.
“Umeokoa maisha yangu?” akamwuliza kwa mshangao mkuu.

KATIKA ghala kubwa lililojengwa chini ya maji, wale wafanya biashara waliokuja kufanya biashara ile haramu waliketi kwenye moja meza kubwa kwa mtindo wa nusu duara, wakiwa wamefungua mnakabrasha Fulani mezani hapo, pembeni yao kulikuwa na vijana wasiocheka, walioweka ‘uso wa mbuzi’ waliojazia kimazoezi, mmoja upande huu na mwingine upande ule, wakifuatilia kila hatua ya mazungumzo ya wanene hao.

Ilionekana kuna kitu kama kutokukubaliana katika biashara hiyo, kwani ubishani kati ya watu wale ulikuwa mkubwa sana.
Yule mtu mnenen ambaye alikuwa na Shalabah wakifanya mazungumzo hayo kwa niaba ya Mr. Lonely aliinuka na kuelekea ukutani, kisha ile meza ikazunguka na kumtazama yeye, pale ukutani likashuka pande la kitambaa na mara nuru kutoka kwenye chombo maalumu ikang’aza kitambaa kile.

“Wote tutazame hapa,” alisema yule mtu huku akiwa ameshika kijifimbo kirefu akinyooshea kule kwenye ule mwanga, “Hii ndiyo aina ya makombora yaliyopo kama mlivyoomba, nawahakikishieni mtaadabisha ile serikali mnayotaka kuiangusha na washirika wake wote, makombora haya yanaitwa R-36 au unaweza kuyaita kitaalamu Intercontinental Ballistic Missile (ICBM) wengine huliita Shetani, ni kombora ambalo liligunduliwa na watu wa Russia miaka ya nyuma lakini likarekebishwa na kuongezwa madoido na nguvu na wanasayansi wa kijeshi kutoka Tanzania kule Mtwara na kuliweka tena kombola hili kama silaha tishio au silaha ya maangamizi.

Lina urefu wa mita 32.2 yaani ni sawa na futi 106, kipenyo chake ni mita 3.5 au futi 10. Limeiwa pia Shetani kwa sababu lina uwezo wa kwenda kasi ya mita 7.9 na mlipuko wake linapofika lilipokusudiwa ni mkubwa na wa kutisha,” kisha akawaonesha jinsi lilivyoundwa na, akawaonesha na mfano wa mlipuo wake kwa kutumia video ya kutengenezwa kwa kompyuta, ukumbi wote ulibaki kimya wakati kile kitambaa kikirudi juu mahala kilipotoka. Kila mtu alishusha pumzi ndefu na kujiweka sawia kitini kwake. Hakuna aliyekuwa na shaka katika hilo.
Yule bwana naye akarudika katika siti yake na mazungumzoy akirndelea, mwisho waliafikiana jinsi ya kusafirisha kwa ujumla.
“Sawa?” akauliza yule mtu.
“Sawa”
Haya anza kuhamisha pesa. Mmoja kati ya wale wageni aliyeonekana kuwa ndyiye mkubwa wa lile jopo lote akachukua kompyuta na kuwasha kisha akaingiza vijinamba Fulani na kusubiri, ilipofunguka akaunganisha na mtandao moja huko Ulaya wa benki na kushuhudia muamala unafanyika katika nia ya kielektroniki kutuma mabilioni ya pesa katika namba za akauti kama ilivyoelekezwa.

Bwana Goloko Mikidadi alikuwa ameketi kwa utulivu juu ya kiti chake, mawazo yalikuwa yamegubika akili yake, alitazama kwa makini malekezo yaliyotolewa na yule bwana pale katika kile kitambaa na hapo ndipo alipogundua ni nini alikuwa amefanya na wenzi wake, mauaji ya kikatili, mauaji yasiyo na huruma kwa kila aliye karibu ama ana hatia au hana, silaha haina macho.

Aliwatazama wenzake wote waliokuwa katika kikao na kuwaona jinsi nyuso zao zilivyo na furaha lakini ni yeye tu aliyeonekana hana furaha. Alitamani ajitoe katika biashara hiyo lakini alijikuta hawezi kwani yeye ndiye kinara na alichofuata hapa ni mgao wake na washirika wake wengine walio Tanzania ambao walikuwa wakisubiri kwa hamu wauage umasikini kwa biashara hiyo. Nafsi yake ilimsuta, roho yake ikamzomea, akakosa amani.
“Kijana, naweza kuonana na Mr. Lonely?” alimuuliza Shalabah.
“Mr. Lonely!” akatulia kidogo, “Ni mtu ambaye huwezi kumuona kwa macho, na ukimuona, hakika utakufa,” Shalabah akajibu kwa nyodo.

“Nahitaji kumuona,” alisisitiza Bwana Goloko.
“Mzee, huwezi kumuona, kama una ujumbe nipe nitamfikishia,” Shalabah akajibu. Ulikuwa ni mvutano mkubwa kati ya Shalabah na Goloko katika swala la kumuona Mr. Lonely. Bwana Goloko alikuwa ameamua kumuona Mr Lonely kwa minajiri ya kujitoa katika biashara hiyo aliyoiona kwa wakai ule kuwa ni haramu, akiwa amesahau tangu huko walikotoka wakiwa wanatengeneza zengwe la kuitia mkononi ile hela chafu kutoka katika mikono ya vikundi vya waasi huko Pakistani, Khazakistani na Huzbekhstani. Mr. Lonely ambaye daima alikuwa akifadhili na kuwauzia silaha kalikali waasi karibu wengi duniani, sasa alimua kufanya kufuru hiyo kwa kuwauzia makombora hayo hatari kabisa yenye uzito mkubwa katika malipuzi. Ilikuwa ni pesa ndefu ambayo ingeyajaza mabenki ya wenye uchu hao kupita kawaida. Kwao methali isemayo subira huvuta heri ilichukua maana yake halisi, walionyongwa wangekula watoto wao, waliofungwa wangezikuta wakitoka, waliopon uraiani kama akina Goloko wangeszifaidi kwa nafasi yao, kwa kula kuku kwa mrija.

“Rafiki yangu Bwana Goloko, tumekuwa tukiwasiliana sana kwa njia ya wajumbe tu, miaka mingi sana sasa, leo tumeonana uso kwa uso, una bahati ya pekee kati ya viumbe vya ulimwengu,” Mr Lonely aliongea kwa tuo, aliongea kwa madaha sana. Bwana Goloko alikuwa akitumbua macho tu alipojikuta amekal;ia kiti chenye kingo za ndhahabu, alikanyaga sakafu ya kioo ambayo chini yake aliweza kuona viumbe vya baharini vikitalii na kuvinjari.
“Mr. Lonely, kweli kabisa nimeona nilichofanya si sahihi, nilikuwa na ombi moja tu kwako, kunitoa katika mchakato huu, katika orodha ya wale washirika wako wa kibiashara, sihitaji pesa zako,” Goloko alisema.

“Goloko Mikidadi, umekuwa swahiba wangu wa kalamu kwaa muda mrefu sana, ukaongea na mjumbe wangu ukijua ni mimi kwa miaka yote, nikakupa pesa nyingi ili ufanikishe wewe na wenzako kuhujumu nchi yenu na kunipa siri hii nzito, sasa tumemaliza, nukta ya mwisho unasema hutaki kuwepo? Magari ya kifahari, watoto wako wanasoma Ulaya, jumba la ghorofa, hoteli kubwa unayomiliki, je utanirudishia vyote hiyo na we urudi kwenu Mafia, kisiwani ukavue samaki kwa ngalawa ya miti?

Kumbuka huna nyumba wewe, nilikukuta katika nyumba ya serikali, nyumba ya Nyerere, lakini sasa upo kwenye ghorofa kubwa unadai unataka kujitoa, hainiiingii akilini ukizingatia tayari tumefika mwisho,” Mr Lonely aliongea kwa utaratibu sana. Bwana Goloko alijikuta akikumbuka kweli hakuwahi kujenga hata nyumba katika utumishi wake wa umma katika serikali ya awamu ya kwanza, alipokuwa katika mchakato wa kuhujumu taifa lake, utajiri wake ulikuwa ukiongezeka kwan kasi pasina kujua ni ni wapi ilikuwa ikitoka, kazin yake ilikuwa ni kutoa siri tu na mipango kwa mtu asiye mjua, kusaini mikataba na makabrasha yaliyo na tija kwake na wenzake. Alijikuta hana jibu, hana la kufanya. Utajiri ule wote auche arudi kwao Kilindoni kuvua samaki.

“Nimeamua,” aliropoka.
“Ok, nimekuelewa, sasa wewe nenda na mi nitakutoa kwenye orodha yangu, sipendi watu vigeugeu, lakini shukrani yangu kwako ni hii,” akaita kwa ishara ya mkono wake, mwanadada mrembo kama malaika aliingia katika kasri ile pweke akiwa na kijibegi kidogo mikononi mwake, akampa Goloko. “Safari njema sana, wasalimie uendako, hakikisha humwambii mtu yeyote juu yah ii biashara, sawa?” Mr Lonely akampa onyo. Goloko akaondoka kwenye lile kasri la ajabu, akaingizwa kwenye chombo maalumu cha kumtoa mle ndani. Alipofungiwa milango alitabasamu, akafungua kile kibegi, kulikuwa na pesa maburungutu kadhaa, akaona hayo yangemtosha na si yale ya udhalimu.

“Hakuna mtu aliye muaminifu duniani,” Mr. Lonely akasema kwa sauti ya chini na kubofya kitufe Fulani kwenye meza yake. Vyuma vikali vikachomoka kwenye kila chombo alichopanda Goloko, vilikuwa vyuma kama kumi hivi vikamchoma huku na huku, mbele na nyuma, hakukuna na muda wa kupiga kelele wala muda was ala ya mwisho, alibaki kutumbua macho tu, roho ikamwacha kwa taabu.

1.jpeg

ITAENDELEA
 
Mkuu kapingili nimejaribu kufuatilia hii story iko poa sana hebu weka tag kwangu kila unapoongeza part nyingine.

Jamaa yangu flani mzee wa un_ended story 4G LTE fuatilia hii story unipe mrejesho.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom